Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 3/1 kur. 12-16
  • Mambo Ambayo Mfalme Anatufanyia

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mambo Ambayo Mfalme Anatufanyia
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JE! UKAMILIFU WA KIBINADAMU UNAWEZA KUFIKIWA?
  • SABABU YA MUNGU KURUHUSU UOVU
  • NI JAMBO GANI LITAKALOTOKEA MWISHONI MWA UTAWALA WA UFALME WA MIAKA 1,000?
  • Enzi Kuu
    Ufahamu wa Kina wa Maandiko
  • Ule Ufalme—Sababu Gani Umekawia Sana ‘Kuja’?
    “Ufalme Wako Uje”
  • Jambo Kuu Linaloelezwa Katika Habari Njema Ni Ufalme wa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Shauri Lililokatwa Lisitokee Tena Kamwe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 3/1 kur. 12-16

Mambo Ambayo Mfalme Anatufanyia

“Naye ataitwa jina lake, Mshauri wa ajabu, Mungu mwenye nguvu, Baba wa milele, Mfalme wa amani.”​—⁠Isa. 9:6.

1, 2. Watu wanakuwa na maoni gani mbalimbali wanapoona hali mbaya iliyo ulimwenguni?

NI VIGUMU wanadamu wasio wakamilifu kufahamu sababu ya Mungu kuruhusu hali zile zile za kutokamilika ziendelee kuwako zaidi ya miaka 1,900 tangu Yesu Kristo alipokuwa duniani. Wao wanasema, ‘Mbona mambo hayajawa na maendeleo ya haraka zaidi?’ Halafu, wanapouona ulimwengu ukitatanishwa, wanakuwa na kawaida ya kusema, ‘Mimi sidhani mambo yanaweza kunyoshwa kamwe.’ Tunapouchunguza mpango wa Mfalme wa serikali ya Mungu tunaweza kufahamu sababu mambo yanaonekana kama yamekawia, na hata huenda tukastaajabu kujua mambo yatakayotimizwa na serikali hiyo baada ya muda mfupi sana.

2 Katika makala iliyotangulia tumeona kwamba Yesu alihamishwa akaacha uhai wa kimbinguni na kupewa uhai wa kibinadamu ili autoe kama dhabihu, na kwa njia hiyo astahili kuwa Kuhani Mkuu wa wanadamu. Utii wake duniani ulimstahilisha kuwa Mfalme pia. Atatimizaje vyeo hivyo kwa faida ya wanadamu?

3. Kwa kutoa dhabihu yake, Yesu Kristo aliingia katika uhusiano gani na wanadamu? (1 Tim. 2:5, 6; 1 Yohana 2:1, 2)

3 Wanadamu ni mali ya Yesu Kristo kwa sababu ya dhabihu ya ukombozi aliyomlipa Yehova Mungu, Mwenye vitu vyote, naye anashughulika na kila mmoja wao kulingana na kusudi lenye haki la Mungu, mpaka mwishowe arudishe watiifu wote katika hali inayofaa, awapatanishe kabisa na Mungu. (Yohana 5:22) Huo ulikuwa mpango wa Mungu, ili wanadamu waweze kuondolewa katika dhambi na kurudishwa katika jamaa yake yenye haki. Kwa njia hiyo Mungu alidumisha haki yake kamili huku akisaidia wanadamu.​—⁠Rum. 3:23-26.

4. (a) Kristo alifanya nini baada ya ufufuo wake, naye anakuwa nini kwa watu watiifu? (b) Mwandikaji wa kitabu cha Waebrania anaonyeshaje kwamba kujaribiwa kwa Yesu kunatuhakikishia kwamba atatusaidia kwa huruma nyingi sana?

4 Kristo alipaa mbinguni baada ya kufufuliwa, akamtolee Mungu ubora wa dhabihu yake, sawasawa na vile kuhani mkuu wa Israeli alivyokuwa akinyunyiza damu ndogo ya wanyama kila mwaka Siku ya Upatanisho katika Patakatifu Zaidi pa hekalu, ambamo Mungu alikaa kwa kuwakilishwa. Kwa wale wanaotii, Kristo anakuwa “Adamu wa mwisho,” “Baba wa milele” anayeweza kuwahuisha. (1 Kor. 15:45; Isa. 9:6) Tuna hakika kwamba atatufikiria na kutusaidia sana kwa huruma kwa sababu yeye alijaribiwa alipokuwa duniani, kama ilivyoandikwa:

“Basi, iwapo tunaye kuhani mkuu aliyeingia katika mbingu, Yesu, Mwana wa Mungu, na tuyashike sana maungamo yetu. Kwa kuwa hatuna kuhani mkuu asiyeweza kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu; bali yeye alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo yote, bila kufanya dhambi. Basi na tukikaribie kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji.”​—⁠Ebr. 4:14-16.

JE! UKAMILIFU WA KIBINADAMU UNAWEZA KUFIKIWA?

5. (a) Maisha makamilifu kabisa ya Kristo, yasiyo na dhambi, yalituhakikishia nini? (b) Dhabihu na ukuhani wake unatimizia nini wenzi wake 144,000?

5 Maisha ya Kristo yenye haki yalifanya Mungu aamue kwamba alikuwa amedumisha utii kamili, akawa hana dhambi kabisa, hata wazo baya. Hiyo inahakikisha kwamba mtu ye yote anaweza kudumisha ukamilifu na kupata kibali ya Mungu kwa kusaidiwa Naye. (Rum. 5:18, 19) Mtu akiisha fikia ukamilifu, anaweza kudumisha utii uo huo kamili. Lo! ni kazi kubwa namna gani inayotimizwa na uhai wa Kristo, dhabihu yake na ukuhani wake! Anasaidia watu wengine 144,000 wawe wafalme na makuhani pamoja naye na kubariki wanadamu kwa kazi yao ya kuwapa faida za dhabihu ya Kristo ya upatanisho, wakiwa chini ya uongozi wake.

6. (a) Kifo kile ambacho ndiye adui wa mwisho atakayemalizwa ni nini? (b) Kifo kitaharibiwa kwa njia gani na wakati gani?

6 Mwishowe Ufalme utatumia ukuhani wake uondolee mbali kifo ambacho kimetaabisha sana wanadamu, walichorithi kwa sababu ya dhambi ya Adamu baba yao. (Rum. 5:12) Mwishoni mwa utawala wa Ufalme wa miaka elfu, wakati ambao watiifu wote watakuwa wamepewa uzima kamili katika ukamilifu, kifo hicho kilichotokana na Adamu kitatangazwa kwamba kimeharibiwa. Hiyo ni kwa sababu Biblia inatuambia kwamba vitu vingine vyote vinavyozuia mwanadamu asiwe na furaha, yaani, serikali mbovu, wapinzani wote wa enzi kuu ya Mungu yenye haki, naam, vitu vyote vinavyoharibu hali njema ya mwanadamu, vitaharibiwa. Halafu, “adui wa mwisho atakayebatilishwa ni mauti.”​—⁠1 Kor. 15:25, 26.

SABABU YA MUNGU KURUHUSU UOVU

7. Ahadi za Ufalme zinahakikisha jambo gani kabisa, na ni suala gani linalohitaji kujibiwa?

7 Basi, ahadi zinazohusu mambo ambayo Ufalme utatimizia wanadamu zinahakikisha kabisa kwamba Mungu haachilii dhambi, uovu, kutokamilika wala matokeo yao hatari, kwa hiyo atayafutilia mbali milele. Ulizo hilo la vile Mungu ameruhusu uovu uendelee muda mrefu limefadhaisha watu wengi waaminifu, wenye kutaka kujua sababu. Na hakika hilo ni suala kubwa mbele ya uumbaji wote. Ili kufahamu makusudi ya Mungu na kazi ya Ufalme, ni jambo la maana kabisa kulifahamu suala hilo.

8. Ni suala gani kubwa lililo mbele ya ulimwengu wote?

8 Suala hilo linahusu enzi kuu ya Mungu au utawala wake, wala halihusu habari ya kama yeye ni mwenye enzi kuu. Hilo ni jambo lisiloweza kupingwa, kwamba yeye ni mwenye enzi kuu. (Zab. 90:2; Matendo 4:24) Lakini jambo ambalo limepingwa ni kama Yehova anafaa kuwa na enzi kuu hiyo, kama anaistahili na kama ni yenye haki. Suala hilo ndilo limemfanya Mungu aruhusu uovu uwepo kwa muda mfupi.

9. Mungu aliviumba viumbe vya kwanza vya kibinadamu vikiwa na sifa gani, na je! sifa hiyo inawafanya wawe si wakamilifu?

9 Mungu ameruhusu uovu uwepo kwa sababu alifanya viumbe vya kwanza vya kibinadamu kwa mfano wake na sura yake. (Mwa. 1:26, 27) Wanadamu ni viumbe vyenye hiari ya kuchagua mambo watakayo kufanya. Wanaweza kuchagua kufanya mema au mabaya. Wao si kama mashine zilizotengenezwa mfano wa binadamu na kuongozwa zifanye mema tu. Kwa kuwa Adamu na Hawa walikuwa watu wenye akili, walikuwa wakamilifu katika uwezo wa kujiamulia mambo. Kama wangaliumbwa bila kuweza kujifanyia uchaguzi na maamuzi ya adili, wangalikuwa si watu kamili, wangalikuwa na walakini. Mungu hawezi kunyima kiumbe chenye uwezo wa kufikiri, kilichofanywa kwa mfano wake, uhuru wa kuchagua yaliyo haki na mabaya. Ndiyo sababu aliwapa dhamiri.​—⁠Rum. 2:15.

10. Adamu na Hawa walishindanaje na enzi kuu ya Mungu kwa mwendo wao?

10 Wakati Adamu na Hawa walipoamua kutotii amri ya Mungu, walikuwa wakishindana na enzi kuu yake. Hawa alitaka ‘kujijulia’ au kujiamulia mwenyewe mambo yote, ‘kuwa kama Mungu.’ Adamu alijiunga naye katika kiburi hicho cha kutaka kujitunza na kujitegemea mwenyewe. (Mwa. 3:5, 6, 22) Wote wawili walikataa kutambua kwamba waliumbwa. Hawakuonyesha upendo wala hawakuthamini mambo ambayo Mungu alikuwa amewafanyia, tena walijitakia mapendeleo yaliyokuwa ya Mungu peke yake kwa sababu ndiye Muumba na Mwenye dunia, Mwendelezaji wa uzima na Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote.

11. Ni nani hasa aliyechochea Adamu na Hawa washindane na enzi kuu ya Mungu, na jambo hilo linaonyeshwaje katika kitabu cha Ayubu?

11 Adamu na Hawa walichochewa katika kiburi hicho na mwana wa kiroho wa Mungu, malaika aliyeasi. (Mwa. 3:1-5; Yohana 8:44) Malaika huyo alilaumu utawala wa Yehova, akasema kwamba msingi wa utawala Wake na utii wa viumbe Vyake ni choyo au woga, si upendo. Baadaye, lawama hilo lilitajwa waziwazi kuhusiana na Ayubu mtumishi mwaminifu wa Mungu. Mwandikaji aliyeongozwa na Mungu (yaani, Musa) anatufahamisha jambo hili lililotukia mbinguni:

“Tena kulikuwa na siku hao wana wa Mungu walipokwenda kujihudhurisha mbele za [Yehova], Shetani naye akaenda kati yao, ili kujihudhurisha mbele za [Yehova]. . . [Yehova] akamwuliza Shetani, Je! umemwangalia huyo mtumishi wangu Ayubu? . . . Shetani akamjibu [Yehova], na kusema, Ngozi kwa ngozi, naam, yote aliyo nayo mtu atayatoa kwa ajili ya uhai wake. Lakini sasa nyosha mkono wako, uuguse mfupa wake na nyama yake, naye atakukufuru mbele za uso wako.”​—⁠Ayubu 2:1-5.

12. (a) Ni kwa njia gani ukamilifu wa mwanadamu ukawa suala jingine dogo, na kwa sababu gani Mungu akamruhusu Shetani aendeshe utendaji wake kwa muda? (b) Mwandikaji wa Waebrania anaonyesha Kristo atamtenda Shetani nini pamoja na kazi zake?

12 Kwa hiyo Shetani (maana yake “mpinzani,” “mzuiaji”) alibisha kwamba Mungu hakustahili kuwa na enzi kuu, na vilevile akaongeza suala jingine dogo juu ya ukamilifu wa mwanadamu kwa Mungu. Lakini utawala wa Mungu si wa kutumia nguvu. Basi alimruhusu Shetani aendelee kuishi kama “haramia” kwa muda mfupi ili kuwapa wanadamu na malaika nafasi ya kuonyesha uaminifu wao na kumaliza milele suala hilo katika akili zao. Wazao wa Adamu waliweza kuongozwa vibaya na mtu huyo mwovu kwa sababu ya kuwa wenye dhambi, kwa hiyo Shetani akawa “mungu wa dunia hii.” (2 Kor. 4:4) Lakini Mungu amemhukumia kifo na karibuni ataharibiwa, kazi zake zote ziharibiwe kabisa. (Mwa. 3:15) Tunasoma yafuatayo juu ya Mwenye kumharibu, Yesu Kristo:

“Basi, kwa kuwa watoto [yaani, wanafunzi wa Kristo] wameshiriki damu na mwili, yeye naye vivyo hivyo alishiriki yayo hayo, ili kwa njia ya mauti amharibu yeye aliyekuwa na nguvu za mauti, yaani, Ibilisi [maana yake “mchongezi”], awaache huru wale ambao kwamba maisha yao yote kwa hofu ya mauti walikuwa katika hali ya utumwa.”​—⁠Ebr. 2:14, 15.

Tena, inasemwa hivi: “Kwa kusudi hili Mwana wa Mungu alidhihirishwa, ili azivunje kazi za Ibilisi.”​—⁠1 Yohana 3:8.

13. Yesu alionyeshaje kwamba alilimaliza suala la ukamilifu kwa maisha aliyofuata? (Yohana 12:31)

13 Utii kamili ambao Yesu alimwonyesha Mungu ulilihakikisha suala la ukamilifu na kulimaliza milele, bila ya kuhitaji msaada wa wanadamu wengine. Kabla ya kufa, Yesu alisema hivi: “Yuaja mkuu wa ulimwengu huu, wala hana kitu kwangu.” (Yohana 14:30) Yesu ‘aliushinda ulimwengu’ unaoongozwa na Shetani mungu wake. Kabla na baada ya wakati huo, watu wengine waaminifu wameshiriki kulimaliza suala hilo, kwa kusaidiwa na Mungu na Mwanawe. Watu hao watatumiwa na Kristo kusaidia wengine wakati atakapoitawala dunia miaka 1,000.​—⁠Yohana 16:33.

14, 15. Maneno ya mtume Petro katika 2 Petro 3:9 yanaonyeshaje kwamba Mungu hakawii na kwamba anajali?

14 Huenda watu fulani wakasema Mungu anaachilia mambo mabaya yaendelee tu bila ya yeye kujali. Lakini mtume Petro anakanusha wazo hilo, akisema: “Bwana hakawii kuitimiza ahadi yake, kama wengine wanavyokudhani kukawia, bali huvumilia kwenu, maana hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikilie toba.”​—⁠2 Pet. 3:9.

15 Tunaona kutokana na maneno ya Petro kwamba Mungu anajali. Yeye anatupa sisi sote nafasi ya kuisikia kweli kwa sababu ya kuacha wakati upite. Lakini, ni kweli kwamba mamilioni ya watu wanazaliwa kila mwezi, na wengi wamekufa. Kwa hiyo maneno ya Petro yanaonyesha kwamba Mungu anajua jambo lililo bora zaidi kwa watu wote walio hai na wale watakaofufuliwa, si kwa kizazi kinachoishi sasa tu. Tena anaujua wakati barabara wa kuingilia mambo ya kibinadamu na kuimaliza taratibu hii ya mambo ili iuachie nafasi utawala wa Kristo wa miaka elfu, wakati ambao ulimwengu mzima utahukumiwa “kwa haki.” (Matendo 17:31; Ufu. 20:11-15) Hivyo watu wote wanaotaka kufanya yaliyo haki wataweza kuokolewa wapate uzima wa milele.​—⁠Ufu. 20:7-10, 15.

NI JAMBO GANI LITAKALOTOKEA MWISHONI MWA UTAWALA WA UFALME WA MIAKA 1,000?

16. Ufalme utaleta wanadamu katika hali gani? (Ufu. 21:3)

16 Wakati ambao Ufalme utatawala mambo ya dunia kwa miaka elfu utakuwa wenye furaha nyingi sana kwa wanadamu. Halafu, mwishoni mwa hiyo miaka elfu Ufalme utafikia mwisho, ukiisha timiza mapenzi ya Mungu “hapa duniani kama huko mbinguni.” (Mt. 6:10) Baada ya dhambi ya Adamu na kifo inacholeta kufutwa, ndipo wanadamu wote watakapokuwa katika hali ya ukamilifu, wasihitaji tena utumishi wa Ufalme wa kikuhani. Ndipo Mungu atakapoweza kuwakubali kabisa katika jamaa yake safi na kamilifu, wakiwa “watoto wa Mungu.”​—⁠Rum. 8:21.

17. Yesu Kristo atafanya nini mwishoni mwa miaka elfu, na kwa sababu gani?

17 Kristo, ambaye ni “yeye yule, jana na leo na hata milele” katika kumpenda Yehova Baba yake na kushikamana naye, ataikubali enzi Yake ya milele mbele ya uumbaji wote mwishoni mwa miaka elfu, kama Biblia inavyoonyesha wazi: “Hapo ndipo mwisho, atakapompa Mungu Baba ufalme wake; atakapobatilisha utawala wote, na mamlaka yote, na nguvu. . . . Vitu vyote vikiisha kutiishwa chini yake, ndipo Mwana mwenyewe naye atatiishwa chini yake yeye aliyemtiishia vitu vyote, ili kwamba Mungu awe yote katika wote.” Hapo ndipo enzi kuu ya Mungu itakaposimama ikiwa peke yake, ikiwa ndiyo kubwa zaidi, ikiwa imetetewa, na kuanza kuongoza uumbaji wake wote.​—⁠Ebr. 13:8; 1 Kor. 15:24-28.

18. Je! Yehova atakuwa na mambo mengine mazuri sana ya kumpa Kristo na wenzi wake 144,000 baada ya utawala wa miaka elfu?

18 Bila shaka, Kristo atatambuliwa na kuheshimiwa nyakati zote kwa sababu ya kazi yake kuu, naye atakuwa Mheshimiwa Kuhani Mkuu na Mfalme. Yehova, ambaye ndiye Mthawabishaji mkuu, ataendeleza uhusiano wake na Kristo na wenzi wake wa mbinguni 144,000 na kuwapa migawo kuwaonyesha kwamba anawapenda sana. (Ebr. 6:10) Biblia haifunui mambo ambayo amewawekea akibani, lakini yale ambayo amekwisha fanya yamekuwa ya ajabu.

“Mungu, kwa kuwa ni mwingi wa rehema, kwa mapenzi yake makuu aliyotupenda; hata wakati ule tulipokuwa wafu kwa sababu ya makosa yetu; alituhuisha pamoja na Kristo . . . akatufufua pamoja naye, akatuketisha pamoja naye katika ulimwengu wa roho, katika Kristo Yesu; ili katika zamani zinazokuja audhihirishe wingi wa neema yake upitao kiasi kwa wema wake kwetu sisi katika Kristo Yesu.”​—⁠Efe. 2:4-7.

19. Kwa sababu gani mtu anahitaji kuyafahamu mambo ambayo tumezungumza sasa hivi?

19 Yote hayo yanahusika katika habari njema, naye mtu anayetaka kumtumikia Mungu kwa njia anayoikubali na kutangazia wengine habari njema anahitaji kabisa kuyafahamu na kuyathamini. ​—⁠Kutoka The Watchtower, Oct. 1, 1977.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki