Shauri Lililokatwa Lisitokee Tena Kamwe
Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi
1-3. Ni maulizo gani yasiyoweza kujibiwa hata na Wakristo wakati huu juu ya ukamilifu wa mtu mwenyewe?
JE! WAWEZA kuwa na hakika juu ya namna nia zako na uaminifu utakavyokuwa wakati ujao? Kwa sasa huenda ukawa mwaminifu sana kama unavyoamini. Lakini je! waweza kuwa na hakika sana juu ya hali yako mwenyewe hata useme, “Mimi najua nitakuwa ivi hivi nilivyo miaka kumi au ishirini ijayo”?
2 Watu waliomtumikia Mungu sikuzote walitambua kutokamilika kwao na kutokutegemeka kwa mioyo yao. Nabii Yeremia alisema hivi: “Moyo huwa mdanganyifu kuliko vitu vyote, una ugonjwa wa kufisha; nani awezaye kuujua?” (Yer. 17:9) Mtume Paulo alisema kwamba ilimlazimu apigane daima na maelekeo yake mwenyewe yasiyokamilika aweze kuendelea kuwa mwenye hali thabiti na ya uaminifu mbele za Mungu.—1 Kor. 9:27; Rum. 7:15, 16.
3 Lakini je! mtu hawezi kufikia hali ya kujua kwamba ataendelea kuwa mwaminifu milele bila ya kuondoka katika uaminifu kwa Mungu? Je! aweza kujua kwamba haitakuwa lazima Mungu apate sababu ya kuutumia uwezo Wake amfishe?
4. Watu waishio duniani watapata kuwa na uhakikisho wakati wo wote wa kwamba hawatatenda dhambi kamwe?
4 Yehova Mungu anakusudia kutoa uhakikisho huo kwa wale wampendao. Anaweza kupanga kuwe na jaribu lililo kamilifu kama vile kazi zake za uumbaji zilivyo kamilifu. Wale watakaolishinda jaribu hilo kwa kufaulu wataonyesha kwa njia hiyo kwamba uaminifu wao ni wa kudumu milele. Walakini, jaribu hilo halitawajia watu wasiokamilika na wenye dhambi, ‘ambao mawazo ya mioyo yao ni mabaya tangu ujana wao.’ (Mwa. 8:21; Yak. 4:5) Bali, jaribu litawajia watu waliotoka katika dhambi—watu waliokamilishwa katika dunia yenye haki.
5, 6. Hali duniani zitakuwa nini mwishoni mwa utawala wa miaka elfu wa Kristo?
5 Katika matoleo ya karibuni ya gazeti hili tumeuzungumza uharibifu wa taratibu mbovu ya mambo iliyopo na utawala wa miaka elfu wa Kristo utakaofuata. Wakati wa kipindi hicho cha miaka elfu waokokaji na mamilioni mengi ya wanadamu waliofufuliwa watakuwa na nafasi kamili ya kuachishwa na dhambi ambayo Adamu alililetea taifa la kibinadamu, ikileta kutokamilika na mauti.
6 Hali duniani zitakuwa nini mwishoni mwa utawala wa miaka elfu wa Kristo? Jamaa ya kibinadamu itasimama mbele ya Yesu Kristo ikiwa kamilifu. Wale waliokuwa waasi wakati wa miaka elfu watakuwa wamekwisha haribiwa. (Ufu. 20:12, 15) Walio watiifu, ambao hapo kwanza walikuwa na nyutu “za kinyama,” watakuwa wamekwisha geuza nyutu zao nao watapatana kabisa na sheria na hali za hiyo taratibu ya mambo yenye haki. (Efe. 4:23, 24) Wanyama watatiishwa kabisa kwa mara nyingine. Wanyama wote watamwogopa na kumheshimu mwanadamu kama ilivyokuwa mwanzoni. (Mwa. 1:28; Hos. 2:18) Kama ilivyokuwa mwanzoni katika Edeni, hata wanyama-mwitu hawatamdhuru mwanadamu wala mali zake. (Isa. 11:6-9) Amani itatawala kati ya vyote vilivyo hai.—Zaburi 148.
7. Ni kwa njia gani mauti ‘itakavyobatilishwa’?
7 Mauti iliyorithiwa na wanadamu kutoka kwa Adamu mwenye dhambi itakuwa imekwisha ‘batilishwa.’ (1 Kor. 15:26) Hivyo, hakuna atakayekufa tena kwa sababu ya mauti ya Adamu. Itakuwa imekwisha haribiwa, kama ionyeshwavyo kwa njia nyingine katika kitabu cha Ufunuo. Humo mauti inaonyeshwa kama ikitupwa katika “ziwa la moto,” kwenye “mauti” yake yenyewe, uharibifu wake.—Ufu. 20:14, 15; linganisha Ufunuo 21:1-4.
8. Ni kwa njia gani “hao wafu waliosalia hawakuwa hai, hata itimie ile miaka elfu”?
8 Kwa msaada wa mambo haya ya hakika twaweza kuyaelewa maneno ya Ufunuo 20:5: “Hao wafu waliosalia hawakuwa hai, hata itimie ile miaka elfu.” Huduma za Kristo na wafalme na makuhani washirika wake 144,000, walioshiriki katika “ufufuo wa kwanza,” zimewaleta “hao wafu waliosalia,” kwenye ukamili wa uzima ulio kweli kweli wakati huu.
UFALME WA MOJA KWA MOJA WA YEHOVA WAFUATA
9, 10. (a) Ni ulizo gani linalobakia kwa wale watakaopata ukamilifu mwishoni mwa miaka elfu? (b) Mtume Paulo anayasimuliaje yanayofuata?
9 Kwa kuwa wanadamu ndipo watakaposimama mbele ya Kristo watakuwa katika hali inayolingana na ile ya Adamu na Hawa katika Bustani ya Edeni. Watakuwa na uzima mkamilifu. Lakini ulizo labaki: Ni nani watakaostahili kupewa amana, uhakikisho wa uzima wa milele katika dunia ya paradiso? Wakiwa na uwezo kamili wa kuziongoza akili zao zote, je! wo wote kati yao watafanya lo lote watakalojichagulia, kwa makusudi, ili wastahili kufa kwa kuhukumiwa na Yehova? Mtume Paulo anasimulia yanayofuata kutukia:
10 “Hapo ndipo mwisho, [Kristo] atakapompa Mungu Baba ufalme wake; atakapobatilisha utawala wote, na mamlaka yote, na nguvu. Maana sharti amiliki yeye, hata awaweke maadui wake wote chini ya miguu yake. Adui wa mwisho atakayebatilishwa ni mauti. Kwa kuwa, Alivitiisha vitu vyote vikiisha kutiishwa chini yake, ndipo Mwana mwenyewe naye atatiishwa chini yake yeye aliyemtiishia vitu vyote, ili kwamba Mungu awe yote katika wote.”—1 Kor. 15:24-28.
11. Kuna badiliko gani katika serikali wakati huu, nalo lamaanisha nini kwa wale walioko duniani?
11 Kufikia wakati huu Yesu Kristo amekuwa akihukumu wanadamu. Ufalme wake wa Kimasihi umekuwa ukitenda kama ufalme wa kuusaidia ufalme wa Mungu, kwa maana enzi ya Mungu ndiyo kuu kupita zote sikuzote. Lakini sasa haubakii ufalme wo wote wa kusaidia katikati ya Yehova na wanadamu. Wanadamu watauitikiaje Ufalme wa moja kwa moja wa Mungu? Wanasimama mbele za Mungu kabisa, bila ya kuhani ye yote kuwamo katikati. Je! majina yao yataandikwa daima katika “kitabu cha uzima”? Ni Mungu peke yake awezaye kuamua hilo. Ni Mungu peke yake awezaye kusema aliye na haki kuishi katika ulimwengu wake wote milele. Waaminifu hao wataonyeshwa wazi kwa njia ya jaribu la ukamilifu wa moyoni na utii. Jaribu hili litamwezesha Mungu na viumbe vyake vyote vyenye akili pia, kutia na majeshi ya kimalaika, kuwajua sana, katika kila upande. Yeye atahakikisha kuwa uaminifu wao hauvunjiki.
12. Ni mfano gani unaoonyesha kwamba Yehova anaweza kuwatumaini kabisa wale anaopata ‘kuwajua’ sana sana kwa njia ya jaribu la mwisho?
12 Kwamba Yehova aweza kuwatumaini kabisa wale ‘awajuao’ kwa njia hii yaonyeshwa katika habari ya Yesu Kristo. Huyu Mwana wa Mungu alikuwa ameishi miaka mingi sana pamoja na Baba yake mbinguni kabla hajaja duniani. (Yohana 1:1; 8:58) Upendo wake na utii ulikuwa mwingi sana hata Mungu angeweza kutabiri bila shaka, kwamba Mwana huyu wake mzaliwa wa pekee ataendelea kuwa mwaminifu katika majaribu makali kupita yote ya ukamilifu.—Ufu. 20:12, 15; Isa. 53:10-12; Rum. 8:33.
13, 14. Kitabu cha Ufunuo kinalisimuliaje jaribu la mwisho?
13 Jaribu la uzima wa milele linaendeshwaje? Ufunuo 20:7-10 unalisimulia:
14 “Na hiyo miaka elfu itakapokwisha, Shetani atafunguliwa, atoke kifungoni mwake; naye atatoka kuwadanganya mataifa walio katika pembe nne za nchi, Gogu na Magogu, kuwakusanya kwa vita, ambao hesabu yao ni kama mchanga wa bahari. Wakapanda juu ya upana wa nchi, wakaizingira kambi ya watakatifu, na mji huo uliopendwa. Moto ukashuka kutoka mbinguni, ukawala. Na yule Ibilisi, mwenye kuwadanganya, akatupwa katika ziwa la moto na kiberiti, alimo yule mnyama na yule nabii wa uongo. Nao watateswa mchana na usiku hata milele na milele.”
15. Hali ya Shetani na mashetani zake imekuwa nini wakati wa utawala wa miaka elfu?
15 Shetani Ibilisi na mashetani zake washirika wamekuwa wasiotenda kwa hiyo miaka elfu, wasiweze kuzuia uadilifu na haki visitolewe wakati wa kipindi hicho. Watu wa dunia wamekuwa hawasumbuliwi hivyo na Ibilisi ambaye kwa kutumia njia zake zenye nguvu nyingi angeweza kuwaweka wanadamu wote ‘katika hali ya utumwa maisha yao yote kwa hofu ya mauti.’ (Ebr. 2:14, 15) Sasa, Shetani atafunguliwa “muda mchache” kwa makusudi ya jaribu.—Ufu. 20:1-3.
WENGINE WATAISHAMBULIA ENZI YA MUNGU
16-18. (a) Ni ulizo gani litakalotokezwa tena? (b) Watakaopotoshwa ni “kama mchanga wa bahari” kwa njia gani? (c) Kwa sababu gani wanaitwa “mataifa”?
16 Ulizo atakalolitokeza Shetani ndilo lile lile alilolitokeza katika Bustani ya Edeni, yaani, unyofu wa enzi ya Yehova, inayohitaji utii kamili wa viumbe vya kibinadamu kwa sheria na makatazo ya Mungu.
17 Ni akina nani watakaopotoshwa na Ibilisi? Ni watu walio kati ya wanadamu waliokamilishwa watakaokuwa waasi. Wao ni “kama mchanga wa bahari,” yaani wanaelekea kutohesabika. Hii haimaanishi kwamba wingi wa wanadamu wataasi pamoja na Ibilisi. Biblia inautumia usemi huu kuhusu hesabu isiyojulikana lakini iliyo kubwa vya kutosha kuweza kumaanisha kundi kubwa.—Linganisha Yoshua 11:4; Waamuzi 7:12.
18 Wenye kupotoshwa wanaitwa “mataifa,” si katika maana ya kwamba kungali kutakuwako migawanyiko ya kitaifa au ya kikabila kati ya watu wa dunia waliokamilishwa. Bali, inaonyesha kwamba waasi hawa wanajitenga na waaminifu walio wengi, wakikataa kuikubali enzi ya Yehova na kujaribu kusimamisha enzi yao wenyewe ya kidunia, kama enzi ya kitaifa. Huenda hata wakawa hawana umoja kati yao wenyewe, kama ilivyo kwa kawaida kwa watu wachoyo wenye kung’ang’ania mamlaka. Kwa hiyo huenda wakawa na enzi mbalimbali vikundi vikundi. Walakini, wana umoja katika jambo moja; yaani, katika kuipinga enzi ya Yehova, kama vile ambavyo mataifa yalikuwa yamefanya miaka elfu moja mapema katika vita ya Har–Magedoni iliyoiharibu taratibu ya mambo ya kale.—Ufu. 17:13, 14.
19. “Mataifa” hayo yakoje katika “pembe nne za nchi” kwa njia ya mfano?
19 “Mataifa” haya yanasemekana kuwa katika “pembe nne za nchi” kwa maana wako mbali sana na enzi ya Mungu. Katika maana ya kiroho wako mbali sana na walio waaminifu kwa Mungu. Kwa habari yao Mungu hawi “yote katika wote.”
20. Watu waliopotoshwa wanasemwa kama “Gogu na Magogu” kwa sababu gani?
20 Kuitwa kwao “Gogu na Magogu” ni kuisimulia roho waliyo nayo na hatua wanayoichukua, kama ile ya “Gogu wa nchi ya Magogu.” Karne nyingi mapema, nabii Ezekieli alikuwa ameonyesha kwamba Gogu (Ibilisi), akitumia kundi la watu wenye kufanyiza majeshi ya kisiasa ya mataifa, angeshambulia watu wa Yehova. Hii ilitukia wakati watu wa Yehova walipokuwa wamekwisha rudishwa kwenye hali ya kiroho nao walikuwa wakikaa kwa amani, bila kuta za halisi, bali wakimtumainia Mungu kama ulinzi wao. Sasa ni miaka elfu tangu kundi hilo lilipoharibiwa penye Har–Magedoni. Lakini sasa jaribio linalolingana na hilo linafanywa. Kwa hiyo si kwa kufufuliwa kwa watu wenye mfano wa Gogu na Magogu kwamba vita inafanywa juu ya enzi ya Mungu. Bali, roho ile ile iliyoonyeshwa wazi na kundi la Gogu na Magogu miaka elfu iliyotangulia inatokea tena katika wengine wa wanadamu waliokamilishwa.
WANAVYOFANYA SHAMBULIO LAO NA SABABU YAKE
21. Kusudi la Ibilisi katika kuushambulia “mji ule mtakatifu” ni nini?
21 “Mataifa” haya yenye mfano wa Gogu na Magogu yanashambulia nini? Hawawezi kumfikia Mungu mbinguni waishambulie enzi yake. Sivyo, wanaushambulia “mji ule mtakatifu.” Huu ndio Yerusalemu Mpya. Walakini, “mji” huu pia ni wa kimbinguni, kwa hiyo hawawezi kuushambulia kwa njia halisi. Lakini “mji” huu umetimiza mambo fulani mema, yenye haki duniani wakati wa miaka elfu. “Mataifa” yaliyokusanywa na Ibilisi yanataka kuyaharibu mambo haya na kwa njia hiyo waifutilie mbali enzi ya Mungu kutoka duniani, wakifanya wanadamu wote waipinge.
22. “Kambi ya watakatifu” inashambuliwaje?
22 Unabii wasema kwamba “mataifa” haya maasi wataizingira “kambi ya watakatifu, na mji huo uliopendwa.” Mungu aupenda Yerusalemu Mpya, mji wa kimbinguni, ambao jina lake limeandikwa juu ya warithi na wafalme washirika wa Kristo 144,000. Wako pia “watakatifu” duniani waupendao huu “mji,” yaani, wale walio kati ya wanadamu walioponywa wanaodumisha ukamilifu wao kupita jaribu hili la kukata maneno. Hawa hawamo katika “mji” ulioko mbinguni, bali wako duniani, katika “kambi,” kama vile katika kambi ya vita nje ya mji ulioshambuliwa na mashujaa-maadui. Kikao cha kidunia cha serikali kinachouwakilisha “mji” wa kimbinguni kati ya “watakatifu” wakati wa miaka elfu kimekuwa chenye “wakuu.” Hawa wamekuwa ndio mawakili waonekanao wa baraza inayoongoza ya kimbinguni.—Zab. 45:16; Isa. 32:1, 2.
23. Je! “vita” hii itakuwa vita halisi yenye silaha za kimwili za kuharibu, au namna gani?
23 “Mataifa” yanakusanyika pamoja kwa “vita” juu ya watakatifu na mji uliopendwa. Je! hii ni vita ya kutumia silaha za atomiki au njia nyingine za kuharibu zisizo za asili? Sivyo, kwa maana wakaaji wa dunia hawatakuwa wamelundika silaha hizo wala hawatakuwa wamejifunza vita hiyo tena. (Isa. 2:2-4) Itakuwa vita ya udanganyifu, porojo zenye kupotosha, vishawishi vya kuwa wachoyo kwa kutokuaminika kwa Mwenye Enzi wa Ulimwengu Wote.
24, 25. (a) Yawezekanaje kwamba Ibilisi aweza kufaulu kupata wafuasi, kwa maana wote ni wakamilifu? (b) Huenda wakafuata kuwaza gani kwenye makosa?
24 Jambo kama hilo lifauluje kupata wafuasi kati ya watu waliokuwa wameishi wakiwa chini ya serikali ya Ufalme ya Kimasihi wakati wa miaka elfu na waliokuwa wamefanya maendeleo kwa utii hata kufikia ukamilifu? Ni kama vile jitihada ya Shetani ilivyowafanyia Adamu na Hawa wakamilifu. Wajapokuwa wakamilifu, waliutumia uhuru wao wa hiari kufanya uamuzi mbaya. Hawakudumisha uaminifu kwa enzi ya Mungu bali walijiachilia wakubali tamaa mbaya, iliyozaa tunda la dhambi na mauti.—Yak. 1:13-15.
25 Wale wanaochagua kujipanga waipinge enzi ya Mungu Shetani anapofunguliwa walikuwa wamekwisha jua walipokuwa wangali chini ya serikali ya Kimasihi, kwamba walizihitaji faida za ukuhani wa Kristo na matumizi ya dhabihu ya upatanisho ili kuiondoa dhambi na kutokamilika kulikokuwa ndani yao. Kama wasingalikuwa wamekuwa wenye nia na watiifu kabisa, wakiwa wanyofu kweli, Mfalme, Kuhani na Hakimu Yesu Kristo angalisitasita asiwaruhusu wafikie jaribu la mwisho. Kwa hiyo wao ni wakamilifu. Lakini, kama vile ambavyo Hawa alionyeshwa, ndivyo Ibilisi atakavyofanya ionekane kwamba kuna nafasi ya kufuata njia yao wenyewe, kujichagulia yaliyo haki na mabaya. Watashawishiwa wajione kwamba imewapasa waruhusiwe kujiongoza kama watakavyo, kwa kuwa ni wakamilifu na serikali ya Ufalme ya Kimasihi haiwatawali tena. Watajitokeza, kama vile Adamu na Hawa walivyofanya, wajitegemee.
26. Ni nani atakayepigana na “mataifa” yanayoushambulia ‘‘mji ule mtakatifu” na ‘‘kambi ya watakatifu”?
26 Wakati ambapo “watakatifu” wanasimama imara kuitetea enzi ya Yehova, wakiitaka iendelee kuwatawala milele, Mungu atawachukulia waasi hao hatua kupitia kwa Kristo. Moto utashuka kutoka mbinguni na kuwala.
27. Ni hali gani yenye furaha itakayokuwa ya wale watakaolishinda jaribu hili kwa uaminifu kwa enzi ya Mungu?
27 Walio waaminifu watathawabishwa haki bora ya kulindwa na kurefushiwa maisha zao kwenye umilele wote katika furaha, kwa sababu ya kulishinda jaribu kali la ukamilifu wao wa nafsi yote kwa Mungu. Watajua kwamba Mungu ‘awajua’ wao sana, kama vile alivyomjua Mwanawe aliye mzaliwa wa pekee duniani—kwamba wao ni watu wenye imani na uaminifu usiobadilika wala usiovunjika milele. Wanaweza kuwa na hakika ya kwamba wataendelea kufuata njia ya uaminifu wakimpendeza Mungu na kuiunga mkono enzi yake mamilioni yote ya miaka katika wakati ujao usiokoma kamwe.—Rum. 8:21.
28. Ni nini habari itakayozungumzwa katika toleo lifuatalo la Mnara wa Mlinzi?
28 Namna gani juu ya mashetani wenye kupigana na Mungu? Unabii wa Ufunuo waonyesha kwamba Shetani na mashetani zake watatupwa katika “ziwa la moto.” Maana ya hili itazungumzwa katika toleo lifuatalo la Mnara wa Mlinzi.
—Kutoka Kitabu God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached.