Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w74 11/1 kur. 499-502
  • Je! Ungetaka Uweko?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Ungetaka Uweko?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • DUNIA YENYE HAKI
  • HUKUMU YA MIAKA ELFU
  • NAMNA GANI WALE WASIOTII?
  • Siku ya Hukumu Ni Nini?
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Siku ya Hukumu na Baada ya Hapo
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Siku ya Hukumu ya Mungu—Matokeo Yayo Yenye Shangwe!
    Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
  • Kutoka Katika Taabu ya Ulimwengu Kuingia Katika “Nchi Mpya” Yenye Amani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
w74 11/1 kur. 499-502

Je! Ungetaka Uweko?

Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi

1-6. Ni hali gani unazoziomba unapoirudia sala ya Bwana ya kielelezo, nawe watazamia kuzifurahia wapi?

JE! WEWE ungependa kuishi mahali ambapo si lazima utatizwe na ulimwengu wa biashara ili kujipatia riziki? Mahali ambapo ungekuwa bila wasiwasi juu ya bei zinazopanda, upungufu, kukosa kazi au mapato?

2 Je! ungependa kujiepusha na upotovu wa serikali, tofauti za haki na nafasi na ukosefu katika usimamizi wa haki?

3 Je! unatamani kwamba ingaliwezekana ungeishi mahali pasipokuwa na wanasheria, madaktari, mahospitali au makaburi?

4 Huenda ukajibu, ‘Wasema juu ya mbinguni.’

5 Sivyo. Twasema juu ya dunia. Inaelekea wewe umeitamani hali ii hii. Je! umepata kusali hivi: “Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni”? Sala hii si ombi la kwenda mbinguni. Inaziomba hali zenye haki na zifaazo za mbingu za Mungu ziletwe duniani.​—Mt. 6:10.

6 Je! hali hiyo yaweza kuwapo? Inaweza na itakuwapo. Wakati gani? Kwa njia gani?

7, 8. (a) Ni wakati gani na kwa njia gani hali hizo zitaletwa? (b) “Mbingu” na “nchi” ya sasa zinafanyizwa na nini?

7 Wakati ujao unaokaribia, kwa kuletwa na Mungu mwenyewe. Kwa kweli waona kwamba hii taratibu inayoendeshwa na wanadamu imechakaa. Walakini, kuna ushuhuda wa kwamba ziko nguvu zisizoonekana zenye uvutano mwingi sana. Biblia inazionyesha nguvu hizi kama mashetani, viumbe vibaya vya kiroho vinavyoongozwa na shetani mkubwa, Shetani Ibilisi. Kwa kutokuonekana, yeye ‘anaudanganya ulimwengu wote.’​—Ufu. 12:9; 2 Kor. 4:4.

8 Kwa hiyo, kunao utawala mwovu usioonekana, unaoitwa na Biblia “mbingu,” na jamii ya kibinadamu inayoonekana inayoitwa “nchi.” Juu ya hivi, Biblia yasema hivi kwa unabii: “Nchi na mbingu zikakimbia uso wake, na mahali pao hapakuonekana.” (Ufu. 20:11) Hii inatabiri kwamba Mungu ataiondoa taratibu hii ya upotovu iliyowatia wanadamu katika hofu nyingi sana, upotovu, vita, magonjwa na mauti.​—2 Pet. 3:7, 13.

DUNIA YENYE HAKI

9. “Mbingu mpya” na “nchi mpya” zinafanyizwa na nini?

9 “Mbingu mpya” za Yesu Kristo na wafalme wake na makuhani washirika 144,000 ndipo zitakapotawala bila kuonekana. (Ufu. 21:1; 14:1; 20:4-6) Mnara wa Mlinzi umezizungumza sifa zao kama watawala na mahakimu katika matoleo yaliyotangulia. Lakini namna gani jamii ya kibinadamu itakayokuwa chini yazo? Itafanyiza “nchi mpya.” Ili kufanya uamuzi wa busara​—kutaka kuwako​—imempasa mtu aelewe itakavyofanya kazi.

10. Zaburi ya 45 inatuambia nini juu ya usimamizi wa mambo ya “nchi mpya”?

10 Ni nani watakaokuwa wasimamizi waonekanao wa haki katika “nchi mpya?” Zaburi ya 45 inatuambia. Inaelekezwa kwa unabii kwa mrithi wa kifalme wa Daudi, Bwana Yesu Kristo. Baada ya kuisimulia “arusi” ya kimbinguni ya Yesu Kristo na kundi lake la “bibi-arusi,” zaburi hii yasema hivi: “Badala ya baba zako watakuwapo watoto wako, utawafanya kuwa wakuu katika nchi zote.”​—Mst. 16.

11. (a) Babu za Yesu watakuwaje wanawe? (b) Ni nani mbali na babu za kimwili wa Yesu watakaowekwa kama “wakuu” duniani?

11 Ni nani “wakuu” watakaosaidia kufikiliza haki katika “nchi mpya”? Wengine wao watachaguliwa kati ya babu za Yesu. Wajapokuwa babu za Yesu kwa njia ya kimwili, watamtegemea yeye kwa uzima. Wanaume hawa watafufuliwa kutoka kwa wafu, Yesu akiwa “Baba” yao, nao wakiwa “watoto” wake. Wengine watatumikia pia kama “wakuu” kati ya waokokaji wa uharibifu wa taratibu hii na kati ya wanaume waaminifu wa kale wasiokuwamo katika ukoo wa Yesu.

12-14. “Wakuu” watakuwa wanaume wa namna gani, nao watawafanyia watu nini katika “nchi mpya”?

12 Jambo kubwa linalowastahilisha hawa kuwa wakuu ni ukamilifu. Yesu Kristo atafuata kanuni ya Mungu mwenyewe katika kuwachagua wanaume hawa, kama inavyotajwa katika Kutoka 18:21: Utachagua “watu walio na uwezo, wenye kumcha Mungu, watu wa kweli, wenye kuchukia mapato ya udhalimu.” Wakuu hawa hawatakuwa wenye kupotoka, kama walivyo watawala leo. Watakuwa mashujaa na watunzaji wa yaliyo haki, kama vile wakuu wanaosimuliwa katika Isaya 32:1, 2:

13 “Tazama, mfalme atamiliki kwa haki, na wakuu watatawala kwa hukumu. Na mwanadamu atakuwa kama mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba; kama mito ya maji mahali pakavu, kama kivuli cha mwamba mkubwa katika nchi yenye uchovu.” Wote, bila ya kujali kabila, rangi au taifa la zamani, watapokea haki. Hakutakuwa na haja ya wanasheria kutetea haki za raia. Haki haitafikilizwa kwa msingi wa hali yo yote ya uchumi, ya kijamii au ya kikabila.

14 Chini ya usimamizi huo wenye haki wa kimbinguni na wa kidunia, choyo inayozuia ukuzi wa chakula na ugawaji uliosawazika kwa wote itaondolewa. Ahadi ya Mungu yenye upendo itakuwa uhakika wa wazi na wenye kufurahika: “Katika mlima [ufalme] huu [Yehova] wa majeshi atawafanyia mataifa yote karamu . . . ya vinono vilivyojaa mafuta, karamu ya divai iliyokaa juu ya urojorojo wake, iliyochujwa sana. . . . Amemeza mauti hata milele.”​—Isa. 25:6-8.

HUKUMU YA MIAKA ELFU

15, 16. Isimulie njozi ya mtume Yohana ya siku ya hukumu ya miaka elfu.

15 Chini ya Yesu Kristo na mahakimu wake washirika wa kimbinguni 144,000 wakuu watafanya kazi. Watakuwa na miaka elfu ya kulisaidia taifa la kibinadamu lijifunze kutii sheria za Mungu na kupata uzima. Uzima ukiwa mwangavu na wenye kutia nguvu, hakutakuwako magonjwa yakihitaji madaktari na mahospitali, yaliyo ya lazima sasa kupunguza kwa kadiri fulani mateso ya kuogofya yanayoletwa nayo. Mungu alimpa mtume Yohana njozi inayotoa mfano mwema wa hii siku ya hukumu. Yohana anaandika hivi:

16 “Nikawaona wafu, wakubwa kwa wadogo, wamesimama mbele ya hicho kiti cha enzi; na vitabu vikafunguliwa; na kitabu kingine kikafunguliwa, ambacho ni cha uzima; na hao wafu wakahukumiwa katika mambo hayo yaliyoandikwa katika vile vitabu, sawasawa na matendo yao.”​—Ufu. 20:12, 13.

17, 18. Ni nani watakaofufuliwa, na ni nani watakaouhitaji msaada wa mahakimu wakati wa hiyo miaka elfu?

17 Njozi hii inaonyesha waziwazi ufufuo wa wafu, kutoka katika kaburi la kidunia au la majimaji​—wote waliokombolewa, ambao kwa ajili yao Mungu anaikubali dhabihu ya upatanisho ya Kristo. Hawa watakuwa wingi wa wanadamu waliopata kuishi.

18 Kuongezea kwa watakaofufuliwa watakuwako waokokaji wa ‘dhiki kubwa’ itakayoiharibu hii taratibu mbovu ya mambo ya kidunia. (Mt. 24:21; Ufu. 7:9-17) Hawa watauhitaji msaada wa mahakimu wa kimbinguni na makuhani ili wakamilishwe, ijapokuwa huenda wengine wakatumikia kama “wakuu.” Vivyo hivyo, wanaume watakaofufuliwa watakaowekwa kama “wakuu” watauhitaji msaada huo wa kimbinguni.

19, 20. Msingi wa hukumu ya watu ni nini, wakati wa miaka elfu?

19 Wote hawa lazima wasimame mbele za kiti cha enzi cha hukumu cha Yehova. Mungu amemtolea Yesu Kristo mamlaka ya kuhukumu wakati wa miaka elfu. (Yohana 5:22) Je! msingi wa hukumu ni matendo ya zamani ya wale watakaohukumiwa? Sivyo. Msingi wa hukumu si kama majina yao yamo katika kitabu cha uzima wanapokuja mbele za kiti cha enzi au sivyo. Njozi yaonyesha kwamba vitabu vingine vya kukunja vilifunguliwa na kwamba “wafu wakahukumiwa katika mambo hayo yaliyoandikwa katika vile vitabu, sawasawa na matendo yao.” Hivyo, uamuzi unafanywa juu ya kama wanaipata nafasi ya kuandikwa majina yao katika kitabu cha uzima au sivyo.

20 Vitabu hivyo vya kukunja vinaonyesha sheria za Yehova za kuishilia na kufanya kazi katika “nchi mpya.” Watu hawatahukumiwa wote pamoja, bali “kila mtu kulingana na matendo yao (NW)” ya utii au ya kutokuzitii sheria hizi zilizoamriwa na mahakimu wa kimbinguni. Wakuu wa kidunia watawasaidia watu wajifunze hizi na kuzitii.

21. Kwa sababu gani si jambo la akili kudhani kwamba wingi wa idadi ya watu wa dunia watageuka wawe waovu na wasiotii wakati wa Siku ya Hukumu?

21 Chini ya hali hizi, je! twaweza kutazamia kwamba wingi wa idadi ya watu wa dunia wakati huo watageuka wawe waovu, wasiotii? Halielekei kuwa jambo la akili kufikiri hivyo. Kwa sasa hali nyingi zinafanya watu wasitii sheria. Mojawapo ya hizi ni njia ya polepole ya kufikiliza haki katika mahakma za siku hizi, na pia kuhonga na kupendelea kunakotokeza udhalimu. Hali katika ulimwengu huu imetia moyo uvunjaji wa sheria. Imetukia kama vile Biblia isemavyo: “Kwa sababu hukumu juu ya tendo baya haitekelezwi upesi, mioyo ya wanadamu huthibitishwa ndani yao ili kutenda mabaya.”​—Mhu. 8:11.

22, 23. Hali itakuwaje bora, nao wenye mioyo ya haki watakuwa na hali gani?

22 Hakuna hali kama hiyo itakayokuwako wakati wa utawala wa miaka elfu wa Kristo. Wakati huu wote udongo wa kibinadamu wa “nchi mpya” utaitikia na kuzaa sawasawa kwa sababu ya kumwagika na kutiririka kwa haki kutoka “mbingu mpya.” Biblia inasema hivi kwa njia nzuri sana: “Dondokeni, enyi mbingu, toka juu, mawingu na yamwage haki; nchi na ifunuke, ili kutoa wokovu, nayo itoe haki ikamee pamoja; mimi, [Yehova], nimeiumba.”​—Isa. 45:8.

23 Kwa hiyo, njia ya mtu mwenye moyo wa haki haitakuwa mbaya kama ilivyo sasa, bali italainishwa. Nabii wa Mungu Isaya aliandika hivi: “Njia yake mwenye haki ni unyofu; wewe uliye mnyofu wainyosha njia ya mwenye haki. Naam, katika njia ya hukumu zako sisi tumekungoja, Ee [Yehova]. . . . maana hukumu zako zikiwapo duniani, watu wakaao duniani hujifunza haki.”​—Isa. 26:7-9.

24. Tofautisha hali iliyopo sasa na itakayokuwako wakati wa utawala wa miaka elfu wa Kristo.

24 Hali zitakuwa tofauti na ambavyo zimekuwa chini ya “mungu wa dunia hii” aliye wa kishetani pamoja na utawala mpotovu wa kisiasa na uvutano wa dini ya uongo ili kutiisha watu. Watafundishwa “vitabu” vya maagizo ya Mungu ya kushughulikia mambo ya dunia bila ya kuzuiwa na mawazo ya uongo na filosofia za kufuatia vitu vya kimwili za watu wenye choyo. Biashara yenye pupa haitaongoza maisha za watu tena kutumia mali za dunia kwa faida yao wenyewe hata kusababisha bei zinazopanda, kupungua kwa thamani ya fedha, hasara na kutaabika kunakofuata, pamoja na uchungu, huzuni na wasiwasi. Yaliyo haki na mema yatatukuzwa, na haitatokea tena kwamba “hukumu juu ya tendo baya haitekelezwi upesi.”

NAMNA GANI WALE WASIOTII?

25-27. Wasiotii watatendewaje?

25 Bila shaka, watakuwako wengine wasioyatii “mambo hayo yaliyoandikwa katika vile vitabu” ya kuongoza wanadamu katika njia ya Mungu. Nabii Isaya anaendelea kusema hivi: “Mtu mbaya ajapofadhiliwa, hata hivyo hatajifunza haki; katika nchi ya unyofu atatenda udhalimu, wala hatauona utukufu wa [Yehova].”​—Isa. 26:10.

26 “Nchi ya unyofu” ya miaka elfu, ya kushughulika kwa unyofu na watu na kati ya watu, itakuwa mahali ambapo upendeleo mwingi unaonyeshwa kwa wanadamu wote wakiwa na kutokamilika kwao kwa kibinadamu kulikorithiwa. Lakini washiriki wengine wa jamaa ya kibinadamu wameingia sana katika upotovu wa dhambi kuliko wengine nao wamezoelea utu usio wa haki. Maelekeo yao ni kwenye udhalimu, ijapokuwa mahali pote kuwazunguka pana unyofu. Wao hawatataka kuukubali ukuu wa Yehova kama Mpaji wa sheria afaaye wala hawataukubali unyofu wa kanuni zake za kuishilia.

27 Watu watakaopokea ‘fadhili’ ya Mungu bure katika “nchi ya unyofu,” wakilikosa kusudi lake la upendo, na wanaoonekana kutoweza kugeuka, hawana haja ya kuachiliwa mpaka mwisho wa miaka elfu kabla hawajauawa kama wasiostahili uzima wa milele katika Paradiso iliyorudishwa duniani. Bila ya udhalimu wo wote kufanywa kwa hao wanaoonekana kutosahihika, wanaweza kuuawa na yeye ambaye Mungu amemweka aihukumu dunia inayokaliwa na watu kwa haki. (Ufu. 20:14, 15; Matendo 17:31) Kwa hiyo, ni jambo la hekima na busara kama nini kuwa watiifu sasa kwa “injili ya Mungu” na kusitawisha upendo wa haki kwa sababu ya hiyo Siku ya Hukumu ijayo!​—1 Pet. 4:17, 18.

28. Je! kuna lo lote liwezalo kufanywa sasa na wale wanaotaka kuwa katika hiyo “nchi mpya”?

28 Je! wewe ungependa uwe katika ulimwengu kama huu? Je! ungekuwa mwenye furaha zaidi kuliko sasa kama ungekuwa na afya kamili na kuweza kuwakaribisha wapendwa na rafiki zako wakifufuliwa? Hali hii ya furaha itakuwa papa hapa duniani. Ikiwa wataka kweli kweli uishi katika ulimwengu huo, moyo wako na dhamiri yako vitakuongoza uzidi kulichunguza Neno la Mungu Biblia. Sababu ya Mungu hasa kukiandikisha kitabu hiki ilikuwa kututolea maagizo wakati huu. Kinatuonyesha namna ya kujiongoza wenyewe kusudi tuifuate njia ya kwenye uzima katika hiyo “nchi mpya.”​—Rum. 15:4.

​—Kutoka Kitabu God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki