Kukumbuka Kifo cha Kristo
Jinsi Gani? Wakati Gani? Namna Gani? Akina Nani? Wapi?
KISA kilichotukia Ibrahimu alipokaribia kumtoa Isaka mwanawe awe dhabihu ni kimojawapo visa vingi vyenye maana fulani na vyenye kupendeza watu katika Maandiko ya Kiebrania.
Ibrahimu alipatwa na jaribu kubwa kweli kweli alipoambiwa na Mungu hivi: “Umchukue mwanao, mwana wako wa pekee, umpendaye, Isaka, . . . ukamtoe sadaka ya kuteketezwa huko juu ya mlima mmojawapo nitakaokuambia.” (Mwa. 22:2, 3) Ibrahimu alishinda jaribu hilo kwa sababu ya imani nyingi, akiwa na uhakika kwamba Mungu angeweza kumfufua Isaka ili kutimiza ahadi ya kumpa uzao. (Mwa. 12:2, 3; 21:12; Ebr. 11:17-19) Kwa njia hiyo Ibrahimu alikuwa mfano mwema wa jinsi Yehova Mungu angemtoa Mwanawe mzaliwa pekee, Yesu Kristo, aliyempenda sana kama vile Ibrahimu alivyompenda Isaka.—Yohana 3:16; Gal. 3:16.
Lakini, je! ulijua kwamba Isaka pia alishinda jaribu kubwa wakati huo? Wakati huo inaonekana kwamba alikuwa kijana mwenye nguvu. Kama angalitaka, angaliweza kumzuia baba yake au kukimbia bila ugumu wo wote. Lakini yeye alimtii baba yake. Kwa kufanya hivyo, Isaka alikuwa mfano mwema wa jinsi Yesu Kristo angefanya mapenzi ya Baba yake wa mbinguni mpaka wakati ambao angefia mtini, akisema: “Si kama nitakavyo mimi, bali kama utakavyo wewe.”—Mt. 26:39; Flp. 2:5-8.
Mambo mengi sana yalitimizwa Yesu alipotii mapenzi ya Baba yake wa mbinguni! Ayubu sura ya 1 na ya 2 inaonyesha kwamba Shetani Ibilisi alimlaumu Yehova Mungu akisema kwamba Mungu asingeweza kuweka duniani wanadamu ambao wangeendelea kumwonyesha ukamilifu. Watu waaminifu, kama Ayubu, walimhakikisha Ibilisi kuwa mwongo. Lakini, je! mwanadamu mwingine aliye mkamilifu kama vile Adamu alivyokuwa mkamilifu Edeni angeweza kuendeleza ukamilifu bila kutenda kosa, na hali Adamu alishindwa kufanya hivyo? Ni kosa la nani lililomfanya Adamu ashindwe? La Mungu au lake? Kwa sababu Yesu aliendeleza ukamilifu kabisa akiwa mwanadamu mkamilifu, alihakikisha kwamba Yehova Mungu alitenda haki kwa kufanya Adamu asiweze kupata uzima wa milele bila ya kumtii Yeye kabisa. Yesu alihakikisha kwamba Adamu alitenda dhambi kwa kupenda kwake mwenyewe, si kupenda kwa Mungu. Kwa njia hiyo Yesu alimtetea Baba yake wa mbinguni akaonyesha kwamba ndiye anayestahili kuwa Mwenye Enzi Kuu. Alimfanyia Baba yake mambo hayo kwa kuendeleza ukamilifu mpaka alipokufa.
Yesu alitimizia wanadamu jambo gani? Alipokufa alitoa dhabihu ya upatanisho inayoondoa dhambi ya ulimwengu na kuleta msingi wa kurudishia wanadamu ukamilifu. (1 Yohana 2:2) Wanadamu watarudishiwa ukamilifu huo na ufalme wa Mungu, katika paradiso itakayokuwa duniani. (Mt. 6:10; 20:28) Vilevile, Yesu alitujulisha mapenzi ya Baba yake kwa kuwa Mwalimu mkuu, na mfano mmoja mzuri wa kuonyesha hivyo ni Mahubiri aliyotoa juu ya Mlima. (Mt. 5:1—7:28) Tena, aliwekea wafuasi wake kielelezo kizuri kabisa: “Kristo naye aliteswa kwa ajili yenu, akawaachia kielelezo mfuate nyayo zake.”—1 Pet. 2:21.
Ukumbusho Ufanywe kwa Sababu Gani?
Hakika Yesu alitaabika sana. Kwa sababu hiyo, wakati mmoja alisema hivi: “Nina ubatizo unipasao kubatiziwa, nami nina dhiki kama nini hata utimizwe!” Wakati mmoja hata alimtolea Mungu sala kwa “kulia sana na machozi.” (Luka 12:50; Ebr. 5:7) Looo! Yesu alipatwa na mzigo mzito kama nini usiku huo uliokuwa wake wa mwisho kuwa mwanadamu! Alijua mambo ambayo Baba yake wa mbinguni alikusudia yampate, lakini alijua pia kwamba alipaswa kuwa mwaminifu ajaribiwapo. Angaliweza kushindwa. Kama angalishindwa, Baba yake angalipatwa na aibu nyingi namna gani, na loo! wanadamu wangalipata hasara kubwa kama nini! Lakini yeye aliendelea kuwa mkamilifu kabisa. Inafaa sana kifo chake kikumbukwe kwa sababu ya mambo yote aliyotimizia Yehova Mungu na wanadamu.
Mara Ngapi? Wakati Gani?
Madhehebu fulani katika Jumuiya ya Wakristo zinasherehekea kifo cha Kristo kila siku, nyingine kila juma, na nyingine baada ya kila miezi mitatu. Lakini je! si jambo la kawaida kukumbuka matukio makubwa na ya maana mara moja kwa mwaka? Ndivyo ilivyokuwa kuhusu sikukuu ya kupitwa iliyokumbukwa kuonyesha jinsi Waisraeli walivyokombolewa utumwani Misri. Ilisherehekewa mara moja kwa mwaka katika tarehe ile ile ambayo jambo hilo lilitukia, yaani, siku ya kumi na nne ya mwezi unaoitwa na Biblia Nisani. Nisani 14, mwaka 33 W.K., ndipo Yesu alipoanzisha ukumbusho wa kifo chake, halafu akafa baadaye siku iyo hiyo. Kwa hiyo inafaa sana kifo chake kikumbukwe mara moja kwa mwaka, katika tarehe hiyo. Mwaka huu, Nisani 14 itakuwa Alhamisi, Machi 23, baada ya jua kushuka. Kwa sababu gani itakuwa baada ya jua kushuka? Kwa sababu nyakati za kale, wakati Biblia ilipokuwa ikiendelea kuandikwa, siku zilikuwa zikianza kuhesabiwa tangu jua liliposhuka (machweoni) mpaka liliposhuka tena siku iliyofuata. Kwa hiyo, mkate na divai za Ukumbusho zinapaswa zipitishwe baada ya jua kushuka, hata ikiwa katika nchi fulani za kaskazini jua litashuka likiwa limechelewa.
Kinasherehekewaje?
Alipoanzisha ukumbusho wa kifo chake, Yesu alichukua mkate (mkubwa mwembamba), kisha akaumega akisema: “Chukueni, mle. Huu maana yake ni mwili wangu. (Mt. 26:26, NW) Yesu alikuwa akitaja mwili gani? Alikuwa akitaja mwili wake mwenyewe wa nyama na damu, kwa maana huo ndio mwili aliotoa ili ulimwengu upate uzima. Kutokuwamo kwa chachu katika mkate kulionyesha kwamba Yesu hangekuwa na dhambi. Kwa hiyo, mkate unaotumiwa katika Ukumbusho usiwe na chachu, usiwe na kikolezo wala kitu cho chote isipokuwa unga na maji.—Yohana 6:51; 1 Kor. 5:7, 8; 1 Pet. 2:22.
Halafu, Yesu alikichukua kikombe chenye divai, na baada ya kushukuru akawapa wanafunzi wake, akisema: “Nyweni katika hicho, ninyi nyote; kwa maana hiki maana yake ni ‘damu ya agano’ yangu, ambayo itamwagwa kwa ajili ya msamaha wa dhambi za wengi.” (Mt. 26:27, 28, NW) Maneno hayo yanatufahamisha kwamba damu ya Yesu iliyomwagwa inatimiza makusudi mawili. Kwanza, inasafisha dhambi za wanadamu. (1 Yohana 1:7) Pili, inaendesha au inafanya agano jipya liwe halali kati ya Mungu na kundi la Kikristo, kama vile agano la kale la Torati lilivyofanywa halali kati ya Mungu na taifa la Israeli wakati Musa aliponyunyiza damu ya wanyama. (Ebr. 9:19, 20) Kwa kuwa Yesu alitumia divai nyekundu iliyotiwa chachu, lakini isiyochanganywa na vitu vingine, divai inayotumiwa leo katika Ukumbusho inapasa iwe nyekundu, isiyoongezwa kitu cho chote cha kuitia nguvu, utamu au ladha.
Ni Nani Wanaokula na Kunywa?
Ni nani anayefaa kula au kunywa mifano hiyo? Yesu alianzisha Ukumbusho mbele ya mitume waaminifu kumi na mmoja tu. Baada ya hapo angekwenda kuwatayarishia mahali mbinguni. (Yohana 14:1-3) Vilevile aliwaambia kwamba alifanya nao agano la kuwa katika ufalme. (Luka 22:28-30) Kwa wale wanaotazamia kushiriki na Yesu katika Ufalme wake wa mbinguni, walio pia katika agano jipya, ndio peke yao wanaopaswa kula na kunywa katika Chakula cha Bwana cha Jioni, kama kinavyoitwa kwa jina jingine.—Luka 12:32; Ebr. 8:10-13; 1 Kor. 11:20.
Tunaendelea kusoma yafuatayo juu ya wale wanaokula na kunywa: “Roho yenyewe hushuhudia pamoja na roho yetu kwamba sisi tu watoto wa Mungu. Basi, ikiwa sisi tu watoto, sisi tu warithi pia: warithi kweli wa Mungu, lakini warithi washirika pamoja na Kristo, tukiteswa pamoja ili tupate kutukuzwa pamoja pia.” (Rum. 8:16,17, NW) Paulo aliandikia Wakristo wa namna hiyo akawapa maagizo juu ya jinsi inavyofaa kuadhimisha Ukumbusho. Alisema kwamba wakati wa kufufuliwa wangevikwa hali ya kutoharibika na kutokufa. (1 Kor. 11:20-34; 15:50-54) Kwa hiyo inaonekana kwamba wenye tumaini hilo la kwenda mbinguni ndio peke yao wanaopaswa kula mkate na kunywa divai ya Ukumbusho.
Ni Nani Wengine Wanaofaidika?
Wafuasi mbalimbali wa Yesu watakuwa mahali pawili mbalimbali. Jambo hilo linaonekana kwa vile Maandiko yanavyotaja utukufu wa mbinguni na hali nzuri za kiparadiso zitakazofurahiwa duniani na watu wa Mungu. (Ufu. 20:4, 6; 21:3, 4) Yesu alizitaja jamii hizo mbili kama makundi mawili yanayokuja kuwa kundi moja mwishowe. (Yohana 10:16) Vilevile tunasoma kwamba viumbe vya kibinadamu vinatazamia sana kufunuliwa kwa “wana wa Mungu” wa kiroho. (Rum. 8:19-21) Wana hao wanatajwa pia kuwa “malimbuko kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo,” kuonyesha kwamba wako wengine wanaovunwa baadaye. (Ufu. 14:1, 4) Jambo hilo linaonekana tena katika maneno yaliyoongozwa na Mungu, yanayosema kwamba Yesu Kristo “ndiye kipatanisho kwa dhambi zetu; wala si kwa dhambi zetu tu, bali na kwa dhambi za ulimwengu wote.” (1 Yohana 2:2) Tofauti ya jamii hizo mbili inaonekana pia kwa sababu warithi wa Ufalme wanafananishwa na uzao wa Ibrahimu utakaozibariki jamaa zote za dunia.—Mwa. 22:17,18; Gal. 3:29.
Kwa hiyo ni wazi kwamba wale walio na matumaini ya kuishi duniani, yaani, “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine” wasio katika agano jipya, hawapaswi kula mkate wala kunywa divai katika Ukumbusho. Basi, je! wanapata faida yo yote kwa kuhudhuria? Kabisa! Tunaweza kulinganisha kipindi hicho na sherehe ya kukumbuka siku ya arusi. Wanaohusika hasa ni wale waliooana siku hiyo, lakini wanaweza kukaribisha watu wengine, rafiki na watu wa ukoo wao, waje kushiriki furaha yao. (Linganisha Ufunuo 19:6, 7.) Wale walio na matumaini ya kuishi duniani wanapendezwa sana na mambo yanayowahusu wale walio na matumaini ya kuishi mbinguni; wanafurahi kuheshimu kipindi hicho kwa kuhudhuria.
Wote wanaweza kufaidika sana kwa kuhudhuria, hata wawe wataishi wapi. Nyakati zote kipindi hicho kinatumiwa kuikumbuka sifa bora ya upendo ambao Yehova Mungu alionyesha kwa kumtoa Mwanawe awe mkombozi wetu. Kinakazia pia upendo mwingi sana ambao Yesu alionyesha kwa kutufia, na vilevile mfano mwema aliowekea wafuasi wake. (Yohana 15:12, 13; 1 Kor. 15:3) Maandiko yanaendelea kuonyesha kwamba Chakula cha Bwana cha Jioni ni kipindi cha wahudhuriaji wote kujichunguza. Inawapasa hasa wajichunguze waone kama wanapendana, kwa maana wakati huo Yesu alisema: “Amri mpya nawapa, Mpendane. Kama vile nilivyowapenda ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo. Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” Inawapasa Wakristo wote waweze kutambuliwa kwa kuonyesha upendo huo mwingi ulioonyeshwa na Yehova Mungu na Yesu Kristo, hata wawe wana tumaini la kuishi wapi.—Yohana 13:34, 35.
Utahudhuria Wapi?
Wakati wa kukumbuka kifo cha Kristo ni wa kufurahi. Sababu ya kufurahi ni kwamba, wakati Yesu alipokuwa pamoja na mitume wake katika chakula hicho cha jioni kinachopasa kukumbukwa, aliwaambia: “Mimi nimeushinda ulimwengu.” (Yohana 16:33) Kwa kuendeleza ukamilifu, Yesu alileta furaha kwa kumhakikisha Ibilisi kuwa mwongo na Mungu kuwa wa kweli. Hivi karibuni, Mashahidi wa Yehova watafurahi kukikumbuka kifo cha Yesu katika makundi zaidi ya 40,000 duniani pote. Je! wewe unaona ubora wa mambo ambayo Yehova Mungu na Yesu Kristo wamekufanyia? Basi unakaribishwa ufike kwenye mojawapo Majumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova baada ya jua kushuka Alhamisi, Machi 23,1978, kisha ujiunge na wengine kukikumbuka kifo cha Kristo kwa kusudi la kumsifu Yehova Mungu na kujipatia hali nzuri ya kiroho.