Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 8/1 kur. 352-356
  • Sifa Zinazofaa Zinahitajiwa Kuhukumu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sifa Zinazofaa Zinahitajiwa Kuhukumu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUTUMIA SIFA ZA KIMUNGU KATIKA HUKUMU
  • KUSHUGHULIKA NA MATATIZO MAZITO ZAIDI
  • KUFAIDIKA SASA NA WAKATI UJAO
  • Wazee Wanaosimamia Vema
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Wazee, Hukumuni kwa Uadilifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Toba Inayorudisha Mtu Kwa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Jinsi Ambavyo Kutaniko Limepangwa
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 8/1 kur. 352-356

Sifa Zinazofaa Zinahitajiwa Kuhukumu

“Sikizeni ninyi maneno kati ya ndugu zenu, mkaamue kwa haki kati ya mtu na nduguye, na mgeni aliye pamoja naye.”​—Kum. 1:16.

1. Ni jambo gani linaloonekana wazi katika matakwa ya kuhukumu ambayo Musa alitaja katika Kumbukumbu la Torati 1:16, 17?

NI DARAKA zito kuamua mambo yanayohusu maisha na uhusiano wa watu. Yawapasa wazee hasa katika kundi la Kikristo wachunguze waone jinsi wanavyotimiza daraka hilo. Kutoa maoni wakati wa kushauri au kufanya maamuzi si sawa na kuhukumu kwa haki. Ili wazee washike kanuni ya Mungu ya kuhukumu, yawapasa wakumbuke maagizo ambayo Musa aliwapa waamuzi katika siku zake: “Sikizeni ninyi maneno kati ya ndugu zenu, mkaamue kwa haki kati ya mtu na nduguye, na mgeni aliye pamoja naye. Msitazame nafsi za watu katika hukumu; mwasikize wadogo na wakubwa sawasawa; msiche uso wa mtu awaye yote; kwa kuwa hukumu ni ya Mungu.” (Kum. 1:16, 17) Hata ikiwa jambo lenyewe lahusu mtu anayeelekea kuwa mkubwa kwa sababu ya mali zake za kimwili, elimu yake au mambo makubwa aliyotimiza yakampa sifa, au ikiwa yanahusu mtu ‘mdogo’ katika mambo hayo, wazee wasipendelee. Lengo lao liwe kufanya yaliyo haki, si machoni pao wenyewe, bali kulingana na maoni ya Mungu. (Mit. 21:2, 3) Kwa njia hiyo hukumu kweli itakuwa ya Yehova, kama inavyoonyeshwa kupitia kwa Neno lake na tengenezo lake la kidunia.

2. Kwa sababu gani ni lazima kutumia hekima wakati wa kuhukumu, na matokeo ya kufanya hivyo ni nini?

2 Wazee hawawezi kuamua mambo vizuri bila kujua mambo mengi yanayohusika. Yawapasa wajue mambo yote yanayohusika wanaposikia jambo fulani. Lazima wazee waulize maulizo ya busara yanayohusiana na habari, ili wajue mambo hatua kwa hatua na kuona jinsi tatizo lilivyoanza. Wanaohusika katika kesi wanapaswa kushirikiana nao kwa kuwaeleza mambo yote badala ya kueleza nusunusu. Hiyo inawezesha wazee watumie sheria za Biblia zinazohusu masuala yaliyotokezwa au mashtaka yanayofikiriwa. Sulemani aliomba hekima ili kutimiza daraka alilopewa. (1 Fal. 3:9, 12) Wazee pia wanahitaji hekima ya kimbinguni watumie vizuri mambo yanayosemwa na Neno la Mungu kuhusu hali wanazolazimika kushughulika nazo. Hiyo inatokeza matunda yenye haki ndani ya kundi.​—Yak. 3:17, 18.

3, 4. (a) Ni kwa njia gani yawapasa wazee wamwige Mungu kuonyesha rehema? (b) Zaidi ya wakosaji, ni akina nani wengine wanaopaswa kurehemiwa kwa kusudi jema?

3 Sifa nyingine ambayo lazima wazee watumie katika hukumu ni rehema. (Yak. 2:13) Yawapasa wamwige Yehova, ambaye mtunga zaburi aliandika habari zake kwa kusema: “Kama vile baba awahurumiavyo watoto wake, ndivyo [Yehova] anavyowahurumia wamchao.” (Zab. 103:13) Israeli walipokwenda kombo, Yehova alitendaje walipotafuta upendeleo wake wakiwa na nia inayofaa ya moyoni? Aliwahurumia, si kwa kupunguza hukumu yake bila kutaka, bali kwa kufunika makosa yao akiwa na kusudi jema. Ghadhabu yake ilikuwa ya muda ikilinganishwa na rehema alizowaonyesha daima. (Isa. 54:7, 8) Kwa habari ya wale waliokuwa katika shida, mwandikaji aliyeongozwa na Mungu amsifu Yehova kwa kusema kwamba “huwahifadhi wageni; huwategemeza yatima na mjane.”​—Zab. 146:9.

4 Vivyo hivyo, yawapasa wazee wafariji wote walio na shida, si wakosaji wanaotubu peke yao. Kati yetu tuna wagonjwa, wenye vizuizi vya kimwili, wenye uzee, wenye kuogopa watu na wenye umaskini. (Yak. 1:27) Kwa hiyo yawapasa wazee wazoee kuonyesha rehema, si kwa kujizuia katika hukumu tu toba inapoonyeshwa, bali pia kwa kufadhili na kuhurumia walio na shida kwa sababu ya kutumbukia katika kosa, kwa sababu ya udhaifu wa kiroho au kwa sababu ya shida za kimwili.

KUTUMIA SIFA ZA KIMUNGU KATIKA HUKUMU

5. (a) Kunakuwa na matokeo gani wakati watu wanaposifiwa wanavyostahili? (b) Wazee wanawezaje kushughulika na maelekeo yasiyofaa, na kwa sababu gani yatupasa tujitahidi kuwa na kiasi katika mambo yote?

5 Wazee wanaposhughulika na akina ndugu katika mambo ya kila siku yawapasa waangalie mambo mazuri wanayofanya, waangalie maendeleo yao na kuwa tayari kuwasifu. Hiyo yatia akina ndugu moyo wa kufanya maendeleo zaidi. Wasijaribu kuagiza wengine wafuate maoni yao katika mambo ya kibinafsi. Ikiwa kanuni za Biblia hazikudharauliwa yawapasa wajue kwamba ndugu wana uhuru wa kuchagua mambo mbalimbali wanayopenda na wasiyopenda. Ndivyo ilivyo katika tafrija, katika mazoea yetu ya kula na kunywa na katika desturi za kuvaa na kujipamba. Badala ya kuweka sheria kali ili kupinga maelekeo fulani ambayo wameona, wazee wenye busara wanapaswa kuwa wenye kujenga, kutia ndugu moyo wafuate yanayopendeza. Bila shaka, wengine wakipita kiasi au kuanza kuvunja Neno la Mungu, wanapaswa waambiwe au wasaidiwe.​—Rum. 14:19-23; Tito 2:2-5.

6. (a) Ili kufanya maamuzi yanayofaa kuhusu mavazi na kujipamba, yatupasa tufikirie kanuni gani za Maandiko? (b) Tunapokumbuka mambo yaliyotajwa katika Mithali zilizoongozwa na Mungu, yatupasa tutafute upendeleo machoni pa nani, na twawezaje kufanya hivyo?

6 Kwa mfano, fikiria kujipamba. Ingawa Mnara wa Mlinzi umetoa maelezo mara kwa mara juu ya jambo hilo, wengine wanaona ni vigumu kujifanyia uamuzi kwa kufikiria kanuni za Maandiko zinazohusika. Au, wanajaribu kuzipinda, kuzipanua kupita kiasi kuhusu hali fulani. Kwa kuzungumza nao maulizo makuu na kuwapa sababu, mawazo yao yanaweza kurekebishwa. Je! mavazi yenyewe ni nadhifu na safi? Je! ni ya adabu na kiasi, na yanawafaa wale wanaomwogopa Mungu? Je! mvaaji anataka kuwa na utulivu na upole au sura ya kupita kiasi? (1 Tim. 2:9, 10; 1 Pet. 3:3-5) Je! wengine wataudhiwa na vazi la mtu? Je! linaharibu heshima ya wakati huo, hasa ikiwa ni mahali pa ibada? (2 Kor. 6:3, 4) Daraka la baba au mume anayetumia ukichwa wa jamaa ni nini? (Kol. 3:18-21) Ikiwa vazi latokeza mashaka au laletea kundi sifa mbaya, Biblia yapendekeza jambo gani lifanywe? (1 Kor. 10:31-33) Je! una unyenyekevu wa kutosha kukuwezesha ujinyime mapendezi yako mwenyewe usije ukaudhi wenye dhamiri dhaifu? (Rum. 14:21) Kwa kufikiria maulizo hayo na kanuni zinazohusika, wazee wanaweza kukazia Neno la Mungu badala ya kuwekea watu sheria. Watawatia moyo wafuate yaliyo haki machoni pa Mungu na kusaidia watu mmoja mmoja wafanye uamuzi unaotegemea Biblia badala ya kutegemea ufahamu wao wenyewe au kujiacha waende kombo kwa kuchukuliwa na fikira tu.​—Mit. 3:5-7; 12:15; 16:2.

7. (a) Mtu akitenda makosa madogo, aweza kufanya nini? (b) Maandiko yanasema ni njia gani ya pekee ya kupata msamaha?

7 Nyakati nyingine watu hufanya makosa madogo. Si lazima kuendea wazee kuwaeleza kila kosa dogo ili kuwa tena na uhusiano mzuri na Mungu. Kwa mfano, itakuwaje ikiwa mtu alitumia usemi wa kudharau mwenzake? Au, labda mtu alihamaki wakati fulani. Au labda mtu aligombana kidogo na nduguye, na baadaye akasikitikia jambo hilo. Mtu aweza kutajia mzee visa kama hivyo, akitaka. Lakini, kumbuka kwamba wazee si ‘mababa wa kuungamia’ kila kikosa kidogo tunachofanya. Mzee akifikiwa kuelezwa mambo kama hayo atajaribu kusaidia. Lakini msamaha hautokani na kupewa mashauri tu na mzee. Mtu hupata msamaha kwa kumwendea Yehova mwenyewe katika sala, kuungama kosa lake, kutubu kisha kuliacha.​—1 Yohana 1:9; Ebr. 4:14-16.

8. Mtu akilaumiwa na moyo wake kwa sababu ya kutenda dhambi, wanaume wazee wanaweza kumsaidiaje akiwaendea?

8 Kwa upande mwingine, ndugu ambao wamefadhaika kiroho kwa sababu ya tatizo wanapaswa kujiona huru kuendea wazee. Ikiwa wametenda dhambi nzito hiyo yaonyesha wana udhaifu fulani upaswao kuondolewa. Huenda mtu akafikia hatua ambayo sala zake zinaelekea kuzuiwa au kutokuwa na maana yo yote; huenda moyo wake ukamlaumu, kisha akose matumaini na uhuru wa kusema. (1 Yohana 5:14; 4:17, 18) Inapokuwa hivyo anahimizwa aendee wanaume wazee, aungame dhambi zake, na kufaidika kutokana na mashauri na sala zao.​—Yak. 5:14-16.

9. Wazee wanaweza kushughulikaje na watu wanaoudhi wenzao, kulingana na Maandiko?

9 Wazee wanatakiwa wawe wastahimilivu na kujizuia katika visa fulani. Kutokamilika kumeiingia sana jamaa ya kibinadamu. Hilo laweza kuonekana wazi zaidi katika matendo ya wengine wanaosema au kufanya mambo yenye kuudhi. Mtu aweza kutaabisha wazee bila kujua, kwa kuwaendea mara nyingi kuwaeleza habari za kikosa kidogo anachodhani alifanyiwa. Huenda wengine wakalaumu wazee kupita kiasi juu ya jinsi wanavyofanya mambo. Mzee akilaumiwa aoneje? Aweza kufuata shauri la Paulo katika 2 Timotheo 2:24, 25, “kuwa mwanana kwa watu wote, awezaye kufundisha, mvumilivu; akiwaonya kwa upole wao washindanao naye” anaposhughulika na mambo ya watu na kuwasahihisha.

10. Ikiwa mtu ametenda kosa kwa sababu ya kutojua au ameghafilika akiwa dhaifu, wazee wanaweza kuonyeshaje hekima na rehema?

10 Si hekima kufanya haraka ya kusema kwamba watu wanafanya mambo wakiwa na makusudi mabaya. Watu hufanya makosa fulani bila kujua. Mtu aliyefanya kosa bila kujua atafurahi sana akirehemiwa. Paulo, aliyetenda makosa bila kujua kabla hajaongolewa, alishukuru sana kwa ajili ya rehema aliyoonyeshwa. (1 Tim. 1:12-15) Baada ya watu kujiweka wakf wawe watumishi wa Mungu, itakuwaje wakichukua hatua mbaya kabla hawajaijua? Inapokuwa hivyo wazee wanakuwa na daraka la kuwashauri na kujitahidi kutengeneza wakosaji hao kwa rehema.​—Gal. 6:1.

KUSHUGHULIKA NA MATATIZO MAZITO ZAIDI

11. Ni baadhi ya makosa gani mazito ambayo huenda yakapaswa kusikilizwa na halmashauri ya hukumu, na kwa kawaida wazee huyajuaje?

11 Makosa mazito yanapofanywa wazee wanatakiwa kujua hatua ya kuchukua ili ndugu wote waendelee kuwa na afya ya kiroho. Makosa hayo yatia ndani dhambi ambazo mtume Paulo ataja katika 1 Wakorintho 6:9, 10 na Wagalatia 5:19-21, dhambi ambazo mtu alitenda baada ya kubatizwa. Huenda mtu ambaye ametenda kosa zito lenye kuvunja sheria ya Mungu akajipeleka kuungama dhambi yake. Au huenda mshiriki fulani wa kundi akashtakiwa kosa zito. Inapokuwa hivyo, wazee wanaotumikia katika halmashauri ya hukumu wanapaswa kuchunguza mambo kwa uangalifu, wakijua kwamba huenda mambo fulani yakatofautisha hali na hali. Badala ya kuongozwa na sheria kali-kali, yawapasa wafikirie kanuni zinazohusika na kuhukumu kila mtu kama anavyostahili.

12. Halmashauri ya hukumu itafanya mambo gani inapoamua jambo kwa haki?

12 Kwa kuwa halmashauri ya hukumu inajua maagizo ya kanuni zenye haki za Mungu, lazima ichunguze mambo yote ya hakika kabla ya kutoa uamuzi. (Mit. 18:13) Mkosaji au aliyeshtakiwa asipoungama wazi kosa zito, lazima mashahidi wasikilizwe ili iweze kufahamika kama jambo ni la kweli au si la kweli. (Kum. 19:15; 1 Tim. 5:19) Wazee wanachunguza pia hali zinazohusu kisa. Je! mtu huyo alidharau mashauri aliyopewa zamani? Je! ushuhuda waonyesha kwamba alifanya tendo hilo makusudi au kwamba anazoea dhambi? Mambo hayo yataamua jinsi jambo litakavyoshughulikiwa. Wazee wakifikiria mambo na hali zote kwa kusali na kuangalia sana sheria ya Mungu, kwa kawaida wanaweza kufanya uamuzi thabiti.

13. (a) Yaipasa halmashauri ya hukumu iwe na lengo la kufanya nini, nayo Mathayo 18:17 yaonyeshaje kwamba matokeo yategemea jinsi mkosaji atakavyoitikia? (b) Kwa sababu gani nyakati nyingine inakuwa lazima watu watengwe na ushirika?

13 Ingawa mkosaji ana hatia ya kosa zito, wazee wanajua kwamba lengo lao ni kumsaidia huyo ambaye ametumbukia katika kosa, wakati wo wote iwezekanapo. Akiwasikiliza,’ kuonyesha toba ya kweli, huenda ‘akapatikana,’ hivyo asitengwe na ushirika. (Mt. 18:15-17) Asipowasikiliza, hawawezi kuendelea kumrehemu, kwa maana wangeonyesha wanadharau kanuni ya Mungu yenye haki na utakatifu. Mkosaji huyo asiyetubu ataharibu roho ya kundi akiruhusiwa abaki kati ya watu wa Mungu. (1 Kor. 5:3-6) Akitengwa na ushirika kundi la Kikristo litaondolewa suto na kuwekwa katika hali ya usafi nyakati zote.

14. Kwa sababu gani nyakati nyingine ni hekima kuomba wazee wengine wanaostahili maoni yao, kama inavyoonyesha Mithali 13:10?

14 Lakini, huenda zikawako nyakati ambazo mambo fulani yanayohusu kesi yanahitaji kuelezwa wazi. Badala ya kufanya uamuzi haraka haraka, inaweza kuhakikishwaje kwamba uamuzi wa haki umetolewa? Linaweza kuwa jambo lenye msaada kuomba maoni ya wazee wengine wa kundi wanaostahili, hasa ikiwa wazee wanaoshughulika na tatizo hilo hawana ujuzi mwingi kama hao wengine. (Mit. 13:10) Jambo likizidi kutatiza, wazee wengine wenye ujuzi wa eneo hilo wanaweza kuitwa wasaidie kwa maoni yao, au mwangalizi anayesafiri, ikiwa huo ndio wakati anapozuru. Huenda wakawa wamekwisha shughulika na tatizo la namna hiyo na wanaweza kutoa mashauri yenye msaada mkubwa.

15. Kwa sababu gani watu fulani waliokuwa wametengwa na ushirika sasa wameingia tena katika msimamo mwema na watu wa Yehova, kupatana na maandiko yaliyoonyeshwa katika fungu hili?

15 Wengi kati ya wale ambao wakati fulani walitengwa na ushirika sasa wameingia tena katika msimamo mwema pamoja na watu wa Yehova. Walionyeshwa rehema kwa sababu ya kutubu, wakanyosha maisha zao na kumrudia Yehova. (Isa. 55:7) Ni wazi kwamba Mungu amebariki wale waliokubali hatua Yake kwa unyenyekevu wa moyo. Huenda wengine ambao sasa wametengwa na ushirika wa kundi wakawa wamerudiwa na akili, na wanataka sana kumrudia Yehova.​—Luka 15:17, 18.

16. Halmashauri ya hukumu huchunguza ione nini wakati watu waliotengwa na ushirika wanapotaka warudishwe, nayo huwa ikikumbuka maulizo gani?

16 Yawapasa wazee wawe na kiasi wanaposikiliza maombi ya watu ya kurudishwa kundini. Haiwapasi kurudisha mtu vivi hivi tu ati kwa sababu ameomba arudishwe. Lazima kuwe na msingi wa Maandiko wa kumrudisha mtu huyo aliyekuwa amekwenda kombo akaletea jina la Yehova na kundi suto. Kwa hiyo kabla ya kufanya uamuzi wo wote lazima wazee waamue kama kweli mkosaji ametubu. Je! ameonyesha matendo ya kutubu? (Matendo 26:20) Hatakiwi kutubu kwa maneno tu. Lazima matendo yaonekane. Amekuwa akienendaje? Kwa muda gani? Nia yake ya moyoni yaonyesha nini? Je! amekuwa akijifunza Neno la Mungu kwa bidii na kujitahidi kulitumia arekebishe njia yake ya maisha? (Yer. 10:23, 24) Je! kweli anafahamu kwamba alimtenda Yehova kosa hilo? Je! amefanya mabadiliko halisi, kuonyesha kwamba ameongozwa na huzuni ya kimungu wala hasikitiki kwa sababu amepatikana tu? Hayo ni maulizo ambayo wazee wanafikiria wanapozungumza na mtu. Halafu wanakuwa katika hali bora ya kuweza kuamua kama kuna sababu za kumrudisha wakati huo au hakuna.

17. (a) Wazee wanaweza kufanya nini ili wahukumu watu kwa haki, hekima na rehema? (b) Wanaweza kujifaidije kwa kufanya hivyo?

17 Wakati mtu aliposhtakiwa mambo fulani mara ya kwanza, labda wenye kutoa ushuhuda walisema mambo yenye kupingana. Wazee watajiangalia wasipite kiasi kwa kumkaza-kaza mtu akubali dhambi ambazo hazikuhakikishwa waziwazi. Fikirieni hali zote kwa ujumla, kama mtu huyo ametubia kosa ambalo kweli alitenda na kumekuwa na ushuhuda wa wazi. Ikiwa yaliyohusika ni mambo ya kibiashara au deni hazijalipwa bado, huenda isiwe lazima nyakati zote kusisitiza zilipwe kwanza kabla mtu hajarudishwa, kwa mfano ikiwa udanganyifu ulihusika. Wazee wote wakikubaliana, wanaweza kusaidia kuamua jambo linalofaa kufanywa ili kutatua tatizo hilo. Lazima hukumu nzuri na haki isawazishwe na rehema. (Yak. 2:13) Hivyo, wazee wanaweza kutazamia kurehemiwa wakihukumiwa wakati ujao.

KUFAIDIKA SASA NA WAKATI UJAO

18. Sote twaweza kushikaje kanuni ya haki ya Mungu, nayo itatufaidije sasa na wakati ujao?

18 Sote tuna sababu kamili za kushukuru kwa ajili ya mpango ambao Yehova amerudishia watu wake katika siku hizi za mwisho. Wazee, wakiwa kama waamuzi na washauri, wamegawiwa daraka la kutusaidia tujipatanishe na kanuni ya kimungu ya haki. Sisi nasi tuna wajibu wa kuwaheshimu wale wanaohukumu kwa sifa za kimungu. Ni njia gani bora ya kufanya hivyo? Ni kuitikia upesi mashauri ya Maandiko na kuwa na nia ya kunyenyekea mpango wa kitheokrasi. (Ebr. 13:17) Hiyo inatuletea ulinzi na hali njema ya kiroho sasa, katikati ya ulimwengu wenye kuasi sheria. Inaonyesha pia kwamba tunataka sana kutimiza matakwa ya Mungu huku tukitafuta kibali Yake na kujitayarisha kuishi katika Taratibu Mpya.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki