Toba Inayorudisha Mtu Kwa Mungu
“Wema [sifa yenye fadhili, NW] wa Mungu wakuvuta upate kutubu.”—Rum. 2:4.
1, 2. Inatupasa tufahamu nini juu ya dhambi na maoni ya Mungu?
KILA mmoja wetu anaweza kutiwa moyo na maneno ya Daudi mtunga zaburi:
“Yehova ni mwenye rehema na neema,
Si mwepesi wa hasira na ni mwenye wingi wa fadhili za upendo.
Yeye hakutufanyia sisi kulingana na dhambi zetu;
Wala kulingana na makosa yetu hakutuletea sisi yale tunayoyastahili.
Kama vile baba huwaonyesha wana wake rehema,
Yehova ameonyesha rehema wale wanaomwogopa yeye.
Kwa kuwa yeye mwenyewe ajua vizuri umbo letu,
Akikumbuka kwamba sisi tu mavumbi.”—Zab. 103:8, 10, 13, 14, NW.
2 Ingawa Mungu anajua kwamba sisi sote ni watenda dhambi, yeye anataka kutusaidia na anapenda kusamehe. (Zab. 32:1, 2) Ingawa hivyo, ufahamu wetu juu ya Mungu usingekuwa sahihi kama tusingeyakubali maoni yake yote juu ya dhambi. Ijapokuwa Zaburi ya 103 inatuhakikishia kwamba Yehova “anasamehe kosa [letu] lote,” inaonyesha pia wajibu mbalimbali tunaopaswa kutimiza, ikisema: “Fadhili za upendo wa Yehova ni za kutoka wakati usiojulikana mpaka wakati usiojulikana kuelekea wale wanaomwogopa yeye, . . . kuelekea wale wanaokumbuka maagizo yake ili wapate kuyatimiza.”—Zab. 103:3, 17, 18, NW.
3. Kwa nini toba inahitajiwa kabisa?
3 Ikiwa mtu ametenda dhambi nzito, naye hatubu wala hatafuti rehema ya Mungu iliyo kama ya baba-mzazi, bali yeye anaendelea kufuatia dhambi, sasa iweje? Kutoka 34:6, 7 (NW) inatupa maelezo juu ya alivyo Yehova. Baada ya kukazia rehema yake, kutokuwa kwake na wepesi wa hasira na kupenda kwake kusamehe kosa, inaongeza kusema hivi: “Lakini kwa vyo vyote yeye hatatoa ruhusa ya kuepuka kupata adhabu.” (Linganisha Hesabu 25:1-5; Ezekieli 33:12, 13.) Kwa hiyo, tusiichezee rehema yake kwa kuichukua kama jambo linalotolewa vyo vyote tu. Basi, mwabudu wa kweli afanye nini akitumbukia katika dhambi?
KUCHUKUA HATUA ZA KUMRUDIA MUNGU
4. Tunaweza kupataje msamaha? (2 Nya. 7:13, 14)
4 Mkristo ambaye ametenda dhambi juu ya sheria ya Mungu anahitaji msamaha. Ni nani anayeweza kutoa msamaha huo? Kusema kweli, ni Mungu tu. Mtume Yohana aliandika hivi: “Tukiziungama dhambi zetu [kwa Mungu], Yeye ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote.”—1 Yohana 1:9; 2:1.
5, 6. Yakobo 5:14-16 inashauri nini, na kwa nini ni jambo la akili nzuri mkosaji alifuate shauri hilo?
5 Katika kisa cha dhambi nzito, kwa hekima Mungu anashauri kwamba Mkristo mwenye ‘kuziungama dhambi zake’ anapaswa achukue hatua nyingine. Katika habari zenye kuhusiana na jambo hili linalozungumzwa, ambazo ni wazi zinamaanisha ugonjwa wa kiroho unaozihusu “dhambi,” mwanafunzi Yakobo aliandika: “Mtu wa kwenu amekuwa hawezi [mgonjwa]? na awaite wazee wa kanisa; nao wamwombee, . . . Na kule kuomba kwa imani kutamwokoa mgonjwa yule, na Bwana atamwinua; hata ikiwa amefanya dhambi, atasamehewa.”—Yak. 5:14-16.
6 Kuchukua hatua hiyo ni jambo la akili nzuri, kwa maana Mkristo ambaye amejiacha ashindwe na dhambi nzito anaonyesha ana kadiri fulani ya udhaifu wa kiroho na kwamba anahitaji msaada. Yeye anaweza kufaidika na sala za imani za ‘wazee wa kundi.’ Wao wamo pia katika cheo cha kuweza kumpa mashauri ya Biblia na kumsaidia ili aweze kupata tena nguvu za kiroho. Zaidi ya hilo, makosa mengine yanafikia kipimo cha kuwa dhambi halisi juu ya kundi la Kikristo, kwa maana yanaleta suto (heshima mbaya) na huzuni juu ya watu wa Mungu. Jambo hilo linafanya ifae hata zaidi mtenda dhambi huyo atafute msaada wa wazee.—2 Kor. 2:10.
7. Wazee wanapashwaje habari za kosa lililofanywa ili waweze kusaidia? (Mit. 28:23; 29:24)
7 Mkristo mwenye hatia ya kutenda dhambi yenye kusikitisha sana anaonyesha ana hekima na unyenyekevu akiwaendea wazee yeye mwenyewe, bila kuambiwa na wengine awaendee. “Afichaye dhambi zake hatafanikiwa; bali yeye aziungamaye na kuziacha atapata rehema.” (Mit. 28:13) Nyakati nyingine, kwa sababu ya aibu, kujisikia ni mwenye hatia au kukosa huzuni ya moyoni mtenda dhambi hawaendei wazee, kama Yakobo anavyoshauri. Mkristo ye yote anayejua habari za dhambi hiyo anapaswa amtie mkosaji moyo aache kosa lake na kutafuta msaada wa kiroho anaouhitaji. Ikiwa bado mkosaji hataki kuwaendea wazee, Mkristo huyo mwingine atawapasha habari hizo ili waweze kutoa msaada unaohitajiwa. Wakristo wote wanapaswa wawe na nia ya ‘kumrejeza mwenye dhambi hata atoke katika njia ya upotevu’ na hivyo ‘waokoe nafsi yake na mauti.’—Yak. 5:19, 20.
KUKARIPIA KWA KULITUMIA NENO LA MUNGU
8. Wazee wanaendeshaje mkutano wa halmashauri?
8 Wakati halmashauri ya hukumu inapofanya mkutano wa kushughulikia kosa, inatafuta uongozi wa Yehova kwa sala. Wazee hao wanazungumza na mtu anaye-husika kwa subira juu ya linaloelekea kuwa ndilo tatizo au kosa, kwa njia inayowafaa wachungaji wenye upendo. (Efe. 5:1, 2; 1 Pet. 5:2, 3) Hata kukiwa kuna mashahidi wanaothibitisha kwamba kosa limefanywa, halmashauri ya hukumu inamtia mtu huyo moyo aeleze waziwazi si lile kosa tu bali pia jambo lililomwongoza alifanye na maoni yake juu ya kosa hilo. (Kum. 19:15; Yohana 8:17) Kwa sababu gani kufanya hivyo kunahitajiwa kabisa?
9, 10. Kwenye kisa cha halmashauri cha kusikia habari za kosa lililofanywa, wazee wanajitahidi kufanya nini? (Zab. 51:13)
9 Ingawa wazee wenye kusikia habari za kisa wanathibitisha kama mtu ana hatia au wanamsadikisha juu ya kosa lake, jambo wanalopendezwa nalo hasa ni kumsaidia ndugu yao wa Kikristo ambaye ameiacha njia. Wao wanataka kumvuta atubu ili ‘burudisho limjie kutoka kwa Yehova.’ (Matendo 3:19) Ikiwa mtu huyo hakubali kosa lake, hatambui kwamba ni lenye kusikitisha sana wala haoni uhitaji wa kutubu, huenda ikawalazimu kumtolea ‘ushuhuda wenye kusadikisha kuhusu dhambi yake na kuhusu haki.’ (Linganisha Yohana 16:8, NW.) Lakini katika kutoa karipio hilo la kimungu wasiwe na moyo wa kulipa kisasi wala wasiwe wakatili. Biblia inahimiza hivi: “Karipia, kemea rasmi, shauri kwa bidii nyingi, kwa ustahimilivu wote na ustadi wa kufundisha.” (2 Tim. 4:1, 2, NW) Kwa kutoa karipio lenye uthabiti, fadhili na subira huenda wakaweza kuufikia moyo wa mtenda dhambi, wakimsaidia alichukie kosa lake na kumgeukia Mungu.—Yer. 3:12, ! 13.
10 Tunaweza kujifunza kutokana na mfano wa Ezra. Yeye aliwaonyesha Wayahudi waziwazi kosa lao. Kusudi hasa halikuwa kuwaaibisha bali kuwafanya waliache, kuugusa moyo wao, kuwavuta walichukie kosa na kutubu. Wao walihitaji kumwungamia Yehova na kutenda kulingana na ungamo lao kwa kufanya kadiri walivyoweza wauondoe ubaya ulioletwa na kosa lao. (Ezra 10:7-14) Vivyo hivyo, halmashauri yenye kushughulikia kisa cha dhambi nzito inataka kumsaidia mkosaji auone uzito wa kosa lake na kumfanya ajisikie moyoni akiwa na uhitaji wa kutubu.—Isa. 1:18.
“KARIPIA MBELE YA WATAZAMAJI WOTE”
11. Ni kina nani walio na uhitaji wa kupewa karipio la Maandiko?
11 Kuhusiana na mikutano ya hukumu wanayofanya pamoja na wakosaji, wazee wanatumia maneno ambayo mtume Paulo alimwandikia Timotheo: “Karipia mbele ya watazamaji wote [kwa uhalisi, “katika mahali pa kuonekana na wote”] watu wazoeao dhambi, kwamba wale wengine wote wawe na woga.” (1 Tim. 5:20, NW) Wakosaji hao ni watu ambao ‘wamejikaza katika dhambi’ (Revised Standard Version) au “wanaoendelea katika dhambi” (New American Standard Bible) mpaka wakati ambao karipio linatolewa hasa.
12. Halmashauri ya hukumu inatumia shauri lililo katika 1 Timotheo 5:20 kwa njia gani?
12 Katika karne ya kwanza, Timotheo, akiwa mjumbe aliyeamrishwa aliyepewa mamlaka)wa mtume Paulo, angeweza akiwa peke yake kulitimiza agizo hilo aliloandikiwa ‘katika mahali pa kuonekana na wote’ wale waliohusika, yule mkosaji akiwapo. Siku hizi kwa kawaida karipio hilo linatolewa na halmashauri fulani ya wazee iliyotajwa wazi badala ya kutolewa na mtu mmoja tu. Si lazima karipio hilo lifanywe mbele ya kundi zima. Kuelekea mwisho wa mkutano wa halmashauri ya hukumu, wazee wanatoa karipio la Maandiko juu ya kosa lenyewe baada ya mtu kuthibitishwa kuwa mwenye hatia. Hapo wanakuwa na mashahidi wale waliotoa ushuhuda wa dhambi iliyofanywa, na watu hao wanaozijua habari zenyewe wanakaribishwa wasikie karipio la Biblia likitolewa. Kwa njia hiyo linatolewa “mbele ya watazamaji wote” au ‘katika mahali pa kuonekana na wote.’ Watu hao, ambao ndio “wale wengine wote” wanaotajwa katika 1 Timotheo 5:20, NW, huenda wakasaidiwa kwa njia hiyo wawe na woga unaofaa kuhusu dhambi, wauone uhitaji wa kuepuka dhambi na hali zinazoweza kuwaongoza kwenye dhambi hiyo.
JE! YEYE ANATUBU?
13. Ni utatizi gani unaowakabili wazee katika kushughulika na dhambi yenye kusikitisha sana?
13 Mmoja wa utatizi mwingi kwa wazee wenye kushughulikia visa vya kutenda makosa ni kuamua kama mtenda dhambi anaonyesha toba ya kweli. Haiwapasi kamwe kuamua kwa kutazama mambo kinje-nje tu. Kwa hiyo, kwa sababu wao hawana uwezo wa kusoma mioyo, wanahitaji kutumia ufahamu mwingi sana, usawa na hekima katika kulichanganua kosa, kuona linahusiana namna gani na sheria ya Mungu na kuangalia yale anayosema na kufanya mtenda dhambi.
14, 15. Kwa nini inawapasa wazee wawe waangalifu katika kuamua kama mtu ametubu?
14 Wazee hawapaswi kufanya haraka-haraka ya kuamua kwamba mtu ametubu. Kwa nini? Kwa sababu wakikosea kwa kuamua kwamba mtenda dhambi ametubu na kumbe sivyo, jambo hilo linaweza kuletea kundi madhara. Lakini tafadhali angalia mfano wa Biblia ulio tofauti unaohusu mkosaji katika kundi la Korintho. Baada ya yeye kuwa amefukuzwa kwa muda fulani, alirudishwa kwa sababu ya kutubu kikweli. Basi sasa kina ndugu wangeshughulika naye kwa njia gani? Wakorintho hao, kwa kuutumaini uamuzi wa kwamba mtu huyo alitubu, walitiwa moyo watumie fadhili ‘wasamehe na kumfariji,’ ‘kumthibitishia upendo wao.’ (2 Kor. 2:6-8) Ndivyo na siku hizi wakati halmashauri inapofikia uamuzi wa kwamba mtenda kosa ametubu. Lakini kama uamuzi wao wa jambo hilo ungekuwa Usiofaa kisha wamrudishe kundini mkosaji ambaye hakutubu kikweli, wangekuwa wakiutia hatarini utakato (usafi) wa adili na wa kiroho wa wote walio kundini.—1 Kor. 5:6.
15 Ni jambo gani ambalo halmashauri inaweza kuangalia ili kuamua kama mkosaji anatubu kikweli? Mtu anayetubu hajaribu kupunguza ukubwa wa mwendo wake mbaya wala hautetei. Yeye anatambua akilini mwake ubaya wa jambo alilotenda na kujisikia moyoni akiwa na majuto ya ndani sana kwa sababu ya kumtenda Mungu dhambi. (Yer. 3:25; Matendo 3:19) Hivyo lazima wazee wanaoshughulikia kisa wahakikishe kwamba mtu ana majuto au huzuni ya namna hiyo.
16, 17. (a) Kuna tofauti gani kati ya “huzuni ya ulimwengu” na ‘huzuni ya kimungu’? (Ebr. 12:16, 17) (b) Machozi au mawonyesho ya kusisimuka moyoni yatahusuje uamuzi wa wazee?
16 Huenda wazee wakalazimika kutofautisha kati ya “huzuni ya ulimwengu” na “huzuni katika njia ya kimungu [ambayo] yatokeza nafasi ya toba inayoongoza kwenye wokovu.” (2 Kor. 7:10, NW) Huenda mtu mwenye hatia ya kufanya kosa akajisikia akiwa na huzuni ya ukosefu wa jambo fulani la kibinafsi, akapata aibu kwa sababu kosa lake litajulikana wazi au akawa na masikitiko makubwa kwa sababu kuna uwezekano wa kutiwa adabu. Lakini hiyo “huzuni ya ulimwengu” haimaanishi kwamba huyo anahuzunikia jambo la’ kwamba amemtenda Mungu dhambi au ameleta suto juu ya Mungu na watu Wake, hivyo vikiwa ndivyo viishara vinavyoonyesha ‘huzuni ya kimungu.’ Ingawa Esau alichururisha machozi kwa sababu ya kuipoteza haki ya uzaliwa, Yehova alijua kwamba Esau hakuwa ametubu kikweli kwa moyo. Kwa hiyo, mtu mwenye hatia ya dhambi nzito akitiririsha machozi, lazima wazee waamue kama anafanya hivyo kwa sababu ana ‘huzuni ya kimungu’ au hana. Huenda akawa anayo. Siku za Ezra watu ‘walilia sana’ baada ya kuisikia sala yake yenye bidii nyingi kuhusu dhambi yao, naye Petro alilia kwa uchungu mwingi kwa sababu alimkana Yesu.—Mwa. 25:29-34, 27:34; Ezra 10:1; Luka 22:59-62.
17 Mifano hii ya Maandiko inakazia sababu kwa nini wazee hawawezi kufanya uamuzi kwa kuangalia tu vile mtu anavyoonyesha misisimuko (mahangaiko) ya moyoni. Umbo la watu na uwezo wao wa kuzuia misisimuko ya moyoni linatofautiana. Kwa hiyo kama mtu anatoa machozi au hatoi, jambo la maana ni kwamba mkosaji huyo aguswe moyoni, awe na roho ya kusumbuka sana au ajisikie kwa ndani sana akiwa na majuto kwa sababu amemkosea Yehova na kuharibu uhusiano wake pamoja na Mungu. (Zab. 51:1-4) Kwa hiyo, inaelekea wazee watamwuliza mkosaji kama amemwungamia Yehova kosa lake kwa sala, akiutafuta msamaha wa Mungu, kama Daudi alivyofanya.—Zab. 32:3-5; 41:4; Yer. 31:19.
18. Ungamo linahusika namna gani?
18 Ikiwa mkosaji aliungama mbele ya ‘wazee wa kundi’ kwa kupenda kwake mwenyewe, huenda hicho kikawa ni kiishara chenye kuwasaidia wajue hali yake ya moyoni iko namna gani. (Yak. 5:14, 16) Namna gani kama yeye hakuungama kwa kupenda kwake mwenyewe, ikawa lazima jambo hilo lithibitishwe kwa kumwonyesha ushuhuda wa kwamba alitenda kosa au ikawa lazima akabiliwe na mashahidi wenye kushuhudia jambo hilo? Bado (hapo kwenye mkutano huo) huenda akafikiwa, aikubali dhambi yake. (Uangalie mfano wa toba ya Daudi juu ya dhambi iliyofanya na Bath-sheba, kwenye 2 Samweli 12:1-13.) Lakini, wakati inapokuwa lazima mkosaji apewe karipio la muda mrefu kabla hajaanza kuonyesha dalili za toba, hapo ndipo hasa inaipasa halmashauri itumie uangalifu. Lazima wasadikishwe (waaminishwe) kwamba mkosaji amebadili hali ya moyo wake na kwamba yeye ana juhudi ya kulirekebisha kosa na kwamba amejikaza kabisa kabisa aliepuke kosa hilo wakati ujao.—2 Kor. 7:10, 11; Ufu. 3:19.
19. Mkosaji mwenye kutubu anapaswa awe na maoni gani juu ya kundi?
19 Inampasa mkosaji awe na masikitiko kwa sababu ya vile alivyovunja heshima ya kundi la Kikristo. Wakati Daudi alipotenda dhambi kwa kuhesabu idadi ya watu kisha akatambua alilokuwa ametenda, yeye alikubali wazi alifanya jambo la kipumbavu. Halafu alipoyaona matokeo mabaya sana yakilipata taifa zima, moyo wake uligusika akasema: “Tazama, ni mimi niliyekosa, ni mimi niliyepotoka; lakini kondoo hawa, wamefanya nini?” (2 Sam. 24:10, 17) Basi, je! mkosaji anayehusika anaonyesha masikitiko ya kweli yenye uchungu mwingi kwa sababu ya suto, matatizo na huzuni anayoweza kuwa ameliletea kundi?
“MATENDO YANAYOPATANA NA KUTUBU”
20-22. (a) Ni “matendo” au “matunda” gani ambayo wazee watachunguza waone kama yanapatikana? (b) Toa mfano wa kuonyesha jinsi mtu mwenye kutubu anavyoweza kuzaa “matunda” hayo.
20 Mtume Paulo alishauri watu kwa bidii nyingi “watubu na kumwelekea Mungu, wakiyatenda matendo yanayopatana na kutubu kwao.” (Matendo 26:20) Wakati Wayahudi wa siku za Nehemia walipotubu kwa sababu walikuwa wamekuwa na wake wa kigeni, walichukua hatua yenye kuonekana wazi ikaonyesha walitubu. (Neh. 9:1, 2; linganisha Yona 3:5-10.) Kwa hiyo, wakati wazee wanaposhughulika na kisa cha dhambi nzito, watataka kujua kama mkosaji ‘amezaa matunda yapasayo toba.’—Mt. 3:8.
21 Ikiwa yeye alimtenda dhambi mtu mmoja, je! ameungama dhambi yake mbele ya mtu huyo na kumwomba msamaha?” Kwa mfano, katika kisa cha uzinzi, je! yeye ameungama mbele ya mwenzi wake asiye na hatia na kumwomba msamaha? Au ikiwa mkosaji ana hatia ya kupunja (kuiba kwa kutumia udanganyifu), je! amechukua hatua zo zote za kurudisha kitu alichokuwa amechukua? Katika hali nyingine huenda asiweze kurekebisha mambo yote aliyoharibu, lakini je! anaonyesha ushuhuda wa kwamba atachukua hatua za kadiri inayofaa amlipe mwenzake kwa sababu ya hasara aliyopata? (Luka 19:8) Jambo la maana ni kwamba, ni kwa kadiri gani mtu huyo mwenye hatia amezaa “matunda yapasayo toba”?
22 Labda dhambi yenyewe ilitokana na kupuza mashauri ya Maandiko. Kwa mfano, labda yeye alikuwa amekuwa na kawaida ya kushiriki katika tafrija pamoja na wafanya kazi wenzake wa kiulimwengu, halafu ushirika mbaya huo ukamwongoza kwenye uasherati. Kwa hiyo je, mtu huyo mwenye kukosa ameuacha ushirika huo? (Mit. 13:20; 1 Pet. 4:3, 4) Vilevile, je! yeye ametia jitihada akutane kwa ukawaida pamoja na watu wa Mungu, na je! ameonyesha tamaa ya moyoni ya kumsifu Mungu akiwa mwabudu safi? Kati ya “matunda” hayo hakuna moja peke yalo linaloweza kutumiwa kama kanuni ya kuamua mtenda dhambi ametubu au hakutubu. Wazee watataka kuona kwamba yeye ana ushirika unaofaa, anahudhuria mikutano ya Kikristo na kuwa mwenye juhudi katika utumishi wa shambani, kwa maana wao wanayakubali maoni ya Mungu yanayosema kunapasa kuwe na “matendo yanayopatana na kutubu.”
23. Halmashauri inahitaji kuangalia nini ikiwa dhambi imerudiwa-rudiwa?
23 Halmashauri ya hukumu ihangaikie sana kuliweka kundi katika hali ya usafi na kutumia uangalifu mwingi sana ikiwa mkosaji amekuwa akiendesha kwa siri dhambi nzito kwa kipindi kirefu. Ingekuwa ivyo hivyo wakishughulika na mtu aliyekuwa ameanzisha kawaida ya kutenda dhambi halafu ikaonekana kijuu-juu kama kwamba ametubu. Huenda akawa amefanya kosa nyakati kadha lakini kwa sababu ilionekana ni kama ametubu yeye alikaripiwa kila wakati na kuruhusiwa abaki kundini. Sasa ametenda dhambi tena. Inapokuwa hivyo, kwa kuifikiria hali njema ya kundi zima lazima wazee waangalie kama maisha yake yanaonyesha ushuhuda wa kweli kwamba anazaa “matunda yapasayo toba.” Je! kwani kwa njia yake ya maisha hakuonyesha kwamba kuna mashaka mengi juu ya kama anafaa kuwa katika kundi la Mungu?—Zab. 119:104; Rum. 12:9.
24. Ni jambo gani linaloamua kama mikutano zaidi inaweza kufanywa pamoja na mkosaji? (Hos. 5:4; Mt. 21:30)
24 Nyakati nyingine mtenda dhambi anakuwa mgumu au anataka vita, asionyeshe toba yo yote ya kweli wazee wajapofanya jitihada za unyofu wa moyo na kutumia subira. (Mhu. 8:11) Si lazima wazidi-zidi kufanya mkutano pamoja na mkosaji huyo kama kwamba wanambembeleza au kumwomba-omba atubu kwa hisani yake. Lakini katika visa fulani huenda wakauona uhitaji wa kukutana tena na mtenda dhambi, ikiwa ushuhuda unaohusu maoni yake, makusudi na toba yake haujafahamika waziwazi sana. Akiisha kuwa na wakati wa kusali na kuyafikiria mazungumzo ya Maandiko yaliyotangulia kufanywa, sasa huenda ikawa wazi kama ametubu au hakutubu.
25. Kwa nini wazee wana daraka zito kuhusiana na makosa?
25 Daraka la wazee katika kuamua toba ya kweli ni zito. Inawapasa wawarehemu na kuwasaidia wakosaji wanaotubu kikweli. Hata hivyo wanahitaji pia kujihadhari wasitumie huruma inayoweza kufanya “chachu” hatari ibaki kundini.—Gal. 5:9.
KULISAIDIA KUNDI
26. Visa fulani vinaweza kushughulikiwa kwa njia gani ikiwa ni watu wachache wanaolijua kosa lililofanywa?
26 Katika visa fulani dhambi yenye kusikitisha sana haiwi imejulikana na watu wengi, na inaelekea haitajulikana na wengi hata baadaye. Labda watu wachache tu, kama jamaa ya mtu au wale mashahidi wachache, ndio wanaoijua dhambi hiyo. (Ingawa hawa ni “watazamaji” tu, wanapaswa wajulishwe kwamba halitakuwa jambo la upendo kupiga-piga domo [porojo] juu ya jambo hilo.) Kwa hiyo, halmashauri ya hukumu ikiisha kuhakikisha kwamba mkosaji ametubu, hakuna uhitaji wa kufanya jambo hilo lijulikane na watu wengine zaidi, kwa maana “watazamaji” wote wamesikia karipio la Maandiko likitolewa juu ya jambo hilo, naye mtenda dhambi ametubu.
27, 28. Ni wakati gani inapoweza kufaa kundi lijulishwe kwamba mtu fulani amekwisha kukaripiwa?
27 Katika visa vingine huenda wengi kundini na/au mtaani wakawa wanajua habari za dhambi fulani. Au huenda dhambi ikawa ya namna ambayo bila shaka itajulikana na wengi baadaye. Kisa kama hicho kinahitaji kushughulikiwa kwa njia tofauti. Inahitajiwa kwamba kundi zima litulizwe moyo lijue kama jambo hilo limeshughulikiwa ifaavyo. Vilevile, linaweza kufaidika na mashauri ya Maandiko yanayoweza kulisaidia liwe na woga unaofaa juu ya kutenda dhambi.
28 Au huenda kukawa na wakati ambao wazee wanaona kwamba lazima watumie uangalifu wa kadiri fulani. Kwa mfano, ingawa sasa mkosaji anatubu kikweli, huenda wakati uliopita akawa alionyesha udhaifu wa namna namna wa kutokujikaza aiepuke njia yenye kumwelekeza dhambini. Kwa hiyo kwa sababu ya kuhangaikia kundi lisiletewe hatari ya kuchafuliwa na mtu fulani aliye katikati yalo, halmashauri ya wazee inaweza kuazimia kwamba hotuba ya Maandiko yenye kuarifu inahitaji kutolewa.
29, 30. (a) Wazee watalipasha kundi habari kwa njia gani? (b) Kushughulikia visa fulani kwa njia hii kunaweza kuleta faida gani?
29 Katika yo yote ya hali hizi, wazee wa kundi wanaweza kupanga kulishughulikia jambo lenyewe kwenye mkutano wa utumishi wa kila juma, wala si kwenye mikutano mingine. Kwenye mkutano wa utumishi ingeweza kutangazwa kwamba yule aliyekuwa mkosaji amekwisha kukaripiwa na halmashauri ya hukumu na ameonyesha toba. Vilevile, huenda halmashauri ya hukumu ikaona kuna uhitaji kabisa wa kuwekea mtu vizuizi fulani. Vizuizi hivyo vinaweza kutia ndani kutokushiriki katika sehemu za mikutano, kutokuwakilisha kundi katika sala au, labda, kutokusoma maandiko au kutokutoa maelezo mikutanoni. Ikiwa halmashauri imeanzisha vizuizi fulani, inaweza kuwaeleza wazee kama inaona kwamba jambo hilo linapasa kutangaziwa kundi. Vizuizi hivyo vinaweza kuondolewa-ondolewa polepole wakati ujao.
30 Jioni iyo hiyo (au alasiri iyo hiyo), lakini baadaye kidogo katika programu ya mkutano wa utumishi, mzee aliyegawiwa anaweza kutoa hotuba ya Maandiko yenye uthabiti. Asitaje jina la mkosaji wala asifunue waziwazi yale mambo ya siri yaliyojulikana wazi katika mkutano wa halmashauri ya hukumu. Lakini anaweza kuzungumza mambo yanayosemwa na Neno la Mungu juu ya namna ya kosa au dhambi inayohusika katika kisa hiki, hatari ya dhambi hiyo na jinsi ya kuiepuka. Kundi lote linaweza kufaidika na onyo hilo la upole la Maandiko.—2 Tim. 4:1, 2.
31. Imetupasa tuyaone namna gani maoni ya Mungu juu ya toba?
31 Inatupasa sisi sote tuithamini sana (tushukuru) nia ya Yehova ya kupenda kukubali toba ya kweli. Kwa uhakika haitupasi ‘tuzikubali fadhili zisizostahilika za Mungu kisha tulikose kusudi lazo.’ (2 Kor. 6:1, NW) Mtu asipozithamini, kisha ajiachilie ashindwe na dhambi na kukosa kutubu, Mungu analiagiza kundi limchukulie hatua kali zaidi. Hatua hizo zitazungumzwa katika toleo letu linalofuata. —Kutoka The Watchtower, September 1, 1981.
[Sanduku katika ukurasa wa 18]
WEWE UMEJIFUNZA NINI JUU YA TOBA?
Tukitenda dhambi nzito, tunahitaji kumwungamia Mungu na pia inatupasa tulitumie shauri lililo katika Neno lake lenye kusema tutafute msaada wa “wazee.”
Kwenye mkutano wa halmashauri ya hukumu, wazee wanajaribu kuthibitisha mtu ana hatia na kujitahidi kumsaidia mkosaji huyo atubu.
Kwenye mkutano huu, ‘kukaripia mbele ya watazamaji wote’ kunawahusu wale waliopo kama mashahidi au wanaojua habari za dhambi iliyofanywa.
Mtu ambaye ametubu kikweli anakuwa amegusika moyoni kwa sababu ya kumtenda Mungu na watu Wake dhambi na kuwaletea suto (kuwavunjia heshima).
Wazee watatafuta ushuhuda wenye kuonyesha “matendo yanayopatana na kutubu.”
Ingawa halmashauri inapendezwa na kumsaidia mkosaji, inahangaikia pia kulilinda kundi lisichafuliwe.