Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 5/1 kur. 203-207
  • Kukaripia Watu Wanaozoea Dhambi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kukaripia Watu Wanaozoea Dhambi
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JINSI YA KUJUA WALE ‘WANAOZOEA’ DHAMBI
  • KUTOSITA KUTAFUTA MSAADA UNAOHITAJIWA
  • KUTUMIA KIASI NA HUKUMU KUPIMA UHITAJI
  • KUKARIPIA KWA USTAHIMILIVU WOTE NA USTADI WA KUFUNDISHA
  • ‘Makaripio Ndiyo Njia ya Uzima’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Toba Inayorudisha Mtu Kwa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Kukaripia “Mbele ya Watazamaji Wote”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Toba ya Kweli—Inatambuliwaje?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 5/1 kur. 203-207

Kukaripia Watu Wanaozoea Dhambi

“Karipia mbele ya watazamaji wote watu wanaozoea dhambi, ili wale wengine wote waogope pia.”​—1 Tim. 5:20, NW.

1, 2. Paulo alimpa Timotheo maagizo gani alipokuwa Efeso, na hii inatokeza maulizo gani?

WAKATI mtume Paulo alipokuwa akishauri mfanya kazi mwenzake Timotheo juu ya jinsi ya kushughulika na matatizo katika Efeso, ambako wengine walikuwa wakitokeza mabishano ya bure tu na mafundisho yenye kupinganisha watu, alitia ndani maneno haya: “Karipia mbele ya watazamaji wote watu wanaozoea dhambi, ili wale wengine wote waogope pia.”​—1 Tim. 5:20; 1:3-7; 6:3-5, NW.

2 Mtume alimaanisha nini kwa kusema “wanaozoea dhambi”? Je! mtu akifanya kosa fulani zaidi ya mara moja, hiyo inamfanya moja kwa moja awe ‘mzoea’ dhambi?

JINSI YA KUJUA WALE ‘WANAOZOEA’ DHAMBI

3, 4. Ni nini maana ya neno la Kigiriki alilotumia Paulo hapa, kwa hiyo tafsiri nyingine zinasemaje?

3 Tukirudia lugha ambayo mtume Paulo alitumia kuandika (yaani, Kigiriki), twaona kwamba neno linalomaanisha ‘kuzoea dhambi, ni ha·mar·taʹnon·tas, ambalo katika Kigiriki ni kitendo kinachoendelea hata sasa cha “kutenda dhambi.” Hiyo yatuonyesha nini? Angalia yanayosemwa na vitabu vyenye kueleza Biblia (maneno yamelazwa ili kutia mkazo):

The Expositor’s Greek Testament chasema; “. . . matumizi ya kitendo kinachoendelea sasa yaonyesha kwamba wanaozungumzwa ni wenye desturi ya kutenda dhambi. . . . Paulo anazungumza habari ya wenye kudumu katika dhambi.”

Schaff-Lange’s Critical Doctrinal and Homiletical Commentary yasema: “Watu hao wenye dhambi wanaonyeshwa kuwa bado wanaishi katika dhambi wakati huo, hali [namna ya kitendo (verb) cha] wakati uliopo inatumiwa ambapo [namna ya] kitendo ambacho kimefanywa tayari ingetazamiwa kuwa.”

4 Kwa hiyo, Paulo alitumia neno la kitendo (au verb) linaloeleza jambo linalofanywa sasa, si zamani, tendo linaloendelea kufanywa, si tendo ambalo limeachwa. Tafsiri mbalimbali za Biblia zinatambua hivyo na kusema yafuatayo:

Young: “Wale wanaotenda dhambi . . .”

Rotherham: “Lakini hao wanaotenda dhambi wakati uliopo . . .”

Knox: “. . . wale wanaoishi isivyofaa.”

Revised Standard Version: “Kwa habari ya wale wanaodumu katika dhambi . . .”

New American Standard: “Wale wanaoendelea katika dhambi . . .”

5. (a) Matokeo ya kurudia dhambi huwa nini? (b) Hata hivyo, jambo la maana zaidi ni nini katika kuamua wanaoitwa kwa kufaa “watu wanaozoea dhambi”?

5 Hakuwezi kuwa na shaka kwamba kila mara dhambi inaporudiwa, uzito wake unaongezeka. Na mtu ye yote anayeendelea kutenda dhambi kwa muda mrefu bila shaka anaizoea. Lakini, kulingana na habari zilizotolewa mapema twaweza kuona sababu gani ikiwa mtu ametenda kosa fulani zaidi ya mara moja, pengine mara mbili au mara tatu, hiyo peke yake haimweki katika kundi moja na wale ambao Paulo awaeleza kuwa “watu wanaozoea dhambi.” Ulizo la maana ni hili, Je! mtu huyo ameliacha kosa? Au anaendelea kulifanya, akidumu katika hilo? Ikiwa anadumu, maelezo ya mtume yamhusu yeye.

6, 7. Mathayo 7:7 yaonyeshaje maana ya ‘kuzoea’ kitu?

6 Maandiko mengine yenye kutumia namna ya wakati uliopo ya vitendo vya Kigiriki yatoa mfano wa jambo hili. Kwa mfano, katika Mathayo 7:7, kitendo (au verb) cha wakati uliopo chenye kuamuru chaonekana mara tatu katika Kigiriki, nayo tafsiri New World Translation yakitafsiri hivi:

“Endeleeni kuomba, nacho kitapewa kwenu; endeleeni kutafuta, nanyi mtapata; endeleeni kubisha hodi, nanyi mtafunguliwa.”

7 Yesu kwa hakika hakumaanisha kwamba maadamu tunamwomba Mungu kitu zaidi ya mara moja​—pengine mara kadha​—​twafanya kulingana na ombi hilo. Sivyo, bali kwamba yatupasa tuendelee, tudumu katika kuomba, kutafuta na kubisha hodi.

8. Basi, ni nani wanaotajwa katika 1 Timotheo 5:20, na ni nani wasiotajwa?

8 Kwa hiyo 1 Timotheo 5:20 yataja kutenda dhambi kunakofanya mtu apaswe kukaripiwa mbele ya watazamaji wote kwa sababu anadumu katika dhambi, haiachi. Kutokana na hili inaelekea kuwa wazi kwamba mtume haelezi habari za watu ambao pengine walitenda kosa mara moja au zaidi lakini baadaye wametubu na kuliacha kikweli.

KUTOSITA KUTAFUTA MSAADA UNAOHITAJIWA

9. Ni nini kinachoonyesha kwamba mkosaji mwenye kutubu hapaswi kusita-sita kuomba msaada wa wazee Wakristo?

9 Basi, je! mshiriki ye yote wa kundi aliyetumbukia katika kosa fulani la uasherati au la mwenendo mbaya wa namna nyingine, halafu akatubu kwa unyofu, apaswa kusita-sita asitafute msaada wa wazee kumtia nguvu uamuzi wake wa kutorudia kosa hilo? Ili kupata jibu, angalia vile mwanafunzi Yakobo anavyotushauri katika Yakobo 5:14-16:

“Mtu wa kwenu amekuwa hawezi? na awaite wazee wa kanisa; nao wamwombee, na kumpaka mafuta kwa jina la Bwana. Na kule kuomba kwa imani kutamwokoa mgonjwa yule, na Bwana atamwinua; hata ikiwa amefanya dhambi [nyingi, kuonyesha kwamba pengine dhambi imefanywa zaidi ya mara moja], atasamehewa. Ungameni dhambi zenu ninyi kwa ninyi, na kuombeana, mpate kuponywa.”​—Linganisha Zaburi 41:1-4.

10, 11. (a) Kwa kujua kwamba tamaa ya wazee ni kuponya mtu, mkosaji mwenye kutubu apaswa kufanya nini? (b) Toa mfano.

10 Inatia moyo sana ‘kuungama dhambi zetu sisi kwa sisi’ ikiwa mkosaji mwenye kutubu ajua kusudi kubwa la wale anaowaungamia ni kumsaidia ‘apone’ ugonjwa wake wa kiroho. Kwa upande mwingine, mtu huyo mwenye kutubu akijisikia kwamba akiungama huenda akakemewa moja kwa moja mbele ya kundi zima kama ‘mzoea dhambi,’ huenda asiungame.

11 Kwa mfano: Mwanamume aliyekuwa akitumia vileo kupita kiasi kabla hajawa Mkristo huenda akawa peke yake nyumbani siku kadha. Wakati huo, huenda akanywa divai au pombe kupita kiasi na kulewa, pengine mara mbili muda wa siku kadha. Halafu huenda akatambua alikuwa akianza kurudia njia zake za zamani na kutaka sana asaidiwe na wazee ili wamtie nguvu uamuzi wake wa kutorudia mwenendo huo. Yeye akidhani kwamba wazee watalazimika kutangazia kundi kosa lake moja kwa moja, kwa sababu alilifanya zaidi ya mara moja, huenda akasita-sita kuwaomba wamsaidie.

12. Hakupaswi kuwe na kizuizi gani, na ni nini kitakachokizuia?

12 Nia hiyo yaweza kutokeza kizuizi kati ya wachungaji wa kundi na wale wanaohitaji sana kusaidiwa nao wasiendelee kufanya kosa. Kwa upande mwingine, mwenye kutenda dhambi akiwa na hakika kwamba wazee wataona ameliacha kosa kwa unyofu na hataki kulirudia kamwe, bila shaka atajisikia akiwa na moyo wa kuwaendea wazee, akikubali msaada wao kama vile ambavyo kondoo mgonjwa angekubali msaada wa mchungaji wake.​—Tofautisha Zaburi 23:1-5 na Ezekieli 34:4.

13. Kwa sababu gani nyakati nyingine huenda wazee wakalazimika kuchukua hatua ya kwanza kuendea mkosaji?

13 Huenda wazee wakaelezwa na mtu mwingine kwamba mtu fulani amefanya kosa zito. Kama wachungaji, kuhangaikia afya ya kiroho ya mshiriki huyo wa kundi kungewaongoza waongee naye juu ya walilosikia. Huenda wakaona kwamba athamini msaada wao lakini hakuutafuta kwa sababu ya haya au kuaibika sana kwa sababu za kipekee kama hizo. Huenda hata wakaona kwamba amekwisha tubia kosa lake akaliacha.

14. Ikiwa wazee wametosheka kwamba mkosaji amekaripiwa kweli kweli na moyo wake mwenyewe, bado watafanya nini?

14 Ikiwa wazee wametosheka kwamba mtu huyo amekaripiwa kweli kweli na moyo wake na dhamiri yake mwenyewe na kupitia kwa uwezo wa Neno la Mungu, wanaweza kujitahidi kumjenga awe na afya ya kiroho. Wangempa mashauri yanayofaa ya Maandiko ili kumtia nguvu mwenye kutubu asilirudie kosa na hiyo ingemkazia uzito wa hali yenyewe. Wangemsaidia afahamu zaidi hatari ya kujilegeza hata kwa muda, na uhitaji wa ‘kuendelea kutimiza wokovu wake mwenyewe kwa kuogopa na kutetemeka.’​—Flp. 2:12.

KUTUMIA KIASI NA HUKUMU KUPIMA UHITAJI

15. Basi, ni nini kinachoamua jambo ambalo wazee watajitahidi kufanya?

15 Lakini, wakati wo wote kosa zito linapofanywa, kama mwenye kutubu ndiye atafuta msaada wao au wao ndio wanaomwendea, wazee wa kundi watapaswa kutosheka kwamba ametubu kwa unyofu na kwamba anajitahidi sana kushikilia mwendo unaofaa. Ikiwa moyo wa mtu mwenyewe haujamkaripia na kumwongoza aliache kosa, wazee wana wajibu wa kujitahidi kumsaidia afanye mambo hayo yanayotakiwa.

16. Je! mtu anayetenda dhambi mara moja tu aweza kuwa ‘mzoea’ dhambi hiyo? Ikiwa ndivyo, kwa njia gani?

16 Hivyo, ingawa hesabu ya nyakati ambazo kosa limefanywa ni jambo zito linalopaswa kufikiriwa na kupimwa, si kila mara hesabu ya nyakati inapoamua uhitaji wa mtu wa kukaripiwa kulingana na Maandiko. Huenda mtu akawa alifanya uasherati mara moja tu. Lakini ikiwa hajatubia kosa hilo kwa unyofu yeye bado ni ‘mzoea’ uasherati. Kwa njia gani? Kwa sababu hajakataa au kuacha njia hiyo mbaya katika moyo wake. Yesu alisema kwamba mwanamume mwenye kutazama mwanamke kwa kumtamani anatenda naye uzinzi katika moyo wake. (Mt. 5:28) Kwa hiyo, ikiwa mtu bado anakumbuka dhambi aliyotenda na kuifurahia badala ya kuichukia na kusikitika sana na kujitahidi asiirudie, bado anayo dhambi hiyo moyoni mwake. Hakusafishwa dhambi kwa kusamehewa na Mungu kupitia kwa Yesu Kristo na kwa hiyo bado ni mchafu. (1 Yohana 1:9; 2:1) Inaelekea atarudia kosa hilo tena akipata nafasi na akijisikia anaweza kuponyoka asijulikane.

17. Hasa ni nani ambao wazee wamepaswa kujihadhari nao wanapodai wametubu?

17 Kwa hiyo wazee wana sababu nzuri ya kupima madai ya kutubu kwa mtu ikiwa ameonyesha ana hatia ya unafiki, ya kusema uongo na kujitahidi adanganye kwa makusudi, au ikiwa ni wazi kwamba alitenda kosa baada ya kufanya mipango, bila kujali. Hiyo ni tofauti kabisa na kutumbukia kwa sababu ya udhaifu wa kibinadamu katika mkazo usiotazamiwa wa vishawishi. Mfano mmoja ni wa Anania na mkewe Safira, waliopanga kudanganya pamoja, ‘wakakusudia tendo hilo baya katika mioyo yao.’​—Matendo 5:1-11, NW.

18. (a) Ikiwa kosa linafanywa kwa uovu, bila kujali, je! wazee wasite-site kutenga mtu na ushirika? Ni nini kinachoonyesha hilo? (b) Ikiwa mtu aliyedharau waziwazi kanuni za haki anarudishwa baadaye kwa sababu ya kutubu kwa unyofu, bado ndugu wapaswa wajiangalieje sana?

18 Hivyo, ikiwa mwanamume aliyeoa hucheza-cheza na mwanamke mwingine na kumshika-shika kwa mahaba, wakati wote huo akijifanya kuwa safi huku akikubali madaraka matakatifu ndani ya kundi, kisha amwacha mkewe na kutoroka na mwanamke huyo mwingine, je! wazee wanapaswa kusita-sita kumtenga na ushirika wa kundi? Hawapaswi. Wakati mtume Paulo alipopata habari za mwanamume aliyekuwa akiishi na mwanamke ambaye bado alikuwa mke wa baba yake, Paulo alipendekeza kundi lichukue hatua ya haraka ‘kumwondoa yule mbaya miongoni mwao. (1 Kor. 5:1-5, 12, 13) Vivyo hivyo, wazee watatumia busara nyingi wanapokubali ombi la mtu huyo la kurudishwa, kwa sababu hakuwapa msingi wa kutosha kuwafanya wamtumaini kwamba ni mnyofu na asema kweli. Baadaye, akirudishwa, yawapasa watumie busara nyingi wakati ujao juu ya kumpa daraka lo lote katika kundi.

19. Mtu ambaye hajashinda bado tatizo la kosa awezaje kuonyesha tamaa yake ya moyoni ni bora kuliko ya wale waliotangulia kuelezwa?

19 Tofauti na watu wa namna hiyo, huenda mshiriki wa kundi akaendea mzee apate msaada na kumjulisha kwamba bado anajitahidi kutatua tatizo. Ingawa hajaweza bado kulishinda tatizo kabisa, huenda akaonyesha anataka kufanya hivyo kwa unyofu, na kusipokuwa na ushuhuda mwingine wa kutilia mashaka maneno yake, wachungaji wa kundi watamsaidia. Bila shaka yeye atofautiana sana na mtu apangaye kudanganya au ajaribuye kutetea mwendo mbaya.​—Zab. 51:1-3, 10, 17.

20. Mwenye kudumu katika dhambi anajidanganyaje, na kwa sababu gani yeye ni hatari kundini?

20 Kwa kawaida mtu anayedumu katika kosa hujipa udhuru akilini mwake mwenyewe, hata kujisadikisha kwamba Mungu ataachilia analofanya. (Linganisha Zaburi 36:2; 50:17-21.) Lililo baya zaidi ni kwamba huenda akaongoza wengine kwenye mwendo huo. Mithali 10:17, NW yasema: “Yeye anayeshikamana na adhabu ni kijia cha uzima, lakini yeye anayeacha karipio anatangatangisha.” Kwa faida yake mwenyewe na ya wote, apaswa kuagizwa aeleze mambo na kunyoshwa.

KUKARIPIA KWA USTAHIMILIVU WOTE NA USTADI WA KUFUNDISHA

21. Karipio linapohitajiwa, Maandiko yanaonyesha wazee watumie njia gani?

21 Ikiwa hali zaonyesha kwamba mtu ahitaji karipio, wachungaji wa kundi watafanyaje? Ikiwa hakubali kosa lake, wazee wanalazimika kumtolea mkosaji “ushuhuda wenye kusadikisha” kwamba alifuata mwendo mbaya. Hawawezi kufanya hivyo ikiwa wamesikia uvumi tu. (Linganisha Yohana 16:8; Isaya 11:3.) Huenda wakaona ni lazima kuuliza maulizo ili kuhakikisha mambo ya lazima. Lakini, kukaripia hasa kwahitaji watumie ushuhuda na sababu za Maandiko kukanusha mawazo yo yote ya mtu huyo ya kudhani mwendo huo wenye dhambi unaweza kuachiliwa na Mungu. Yawapasa wajaribu kumsaidia aone jinsi ubaya wenyewe ulivyo mbaya hasa na sababu gani unastahili kuchukiwa. (Ebr. 1:9) Kwa njia hiyo wanamsahihisha na kumsaidia ‘anyoke.’ Kusudi lao kama wachungaji ni kumfanya atubu na kuuacha mwendo mbaya, si kwa matendo tu bali pia katika akili na moyo.​—Tito 1:9; Yak. 1:25; 2:8, 9.

22. Kusudi asili la karipio la Kikristo lapaswa kuongozaje wazee katika jitihada zao, nao wanawezaje kutimiza agizo la kukaripia “kwa ustahimilivu wote na ustadi wa kufundisha”?

22 Wakikumbuka sana kusudi la karipio, wazee hawatajichukua kuwa baraza yenye kutafuta mambo ya hakika au kuhakikishia mtu hatia yake tu. Wao hawakemei mtenda kosa na bas! (ingawa karipio lao laweza kutia ndani kemeo). Mradi wao mzuri sana na wenye upendo ni ‘kurejeza mtenda dhambi atoke katika njia ya upotevu ili kuokoa nafsi na kifo.’ (Yak. 5:19, 20) Bila shaka haiwapasi kujiona wana haraka haraka, kama kwamba wana siku moja tu ya kuzungumza na mtu huyo. Wakiona kwamba wanahitaji wakati zaidi, wanaweza kupendekeza mtu huyo afikiri na kusali juu ya mambo ambayo wamesema, kisha wanaweza kupanga kuzungumza naye tena. Huenda hiyo ikatoa nafasi ya kufanya mashauri na karipio lao liingie ndani ya akili na moyo wake. Na hata baada ya kufikia uamuzi fulani (baada ya kuzungumza naye mara moja au zaidi), watajua kwamba huenda wakahitaji kumfikiria zaidi na kumsaidia kwa kipindi fulani ili wamrudishie afya ya kiroho. Lakini watatosheka kujua kwamba, kama 2 Timotheo 4:2 (NW) isemavyo, wamekaripia na kuonya “kwa ustahimilivu wote na ustadi wa kufundisha.” Wakati na jitihada iliyotumiwa ilistahili kutumiwa.a

23. (a) Je! watu wakitubu na kuacha kosa, hiyo yaonyesha bila shaka wataendelea kufanya kazi zote za kundi walizokuwa nazo kwanza? (b) Ni mambo gani ambayo wazee watapima katika visa vyote?

23 Uhakika wa kwamba mtu amejikaripia mwenyewe katika moyo wake hauonyeshi bila shaka ataendelea kufanya kazi zote alizokuwa nazo kundini. Huenda akawa kama vile mtu ambaye ndiyo kwanza aanze kupata nafuu ya ugonjwa wa kimwili asivyoweza kuchukua vitu vizito kama wengine. Huenda wazee wakaamua inafaa kutomtumia katika madaraka kwa muda, pengine kwa kujisikia kwamba kizuizi hicho chaweza kumsaidia ‘atengenezeke upya.’ (Gal. 6:1, NW) Na kwa habari ya mtu atubuye baada ya kukaripiwa tu, yaani, baada ya kusadikishwa ana mwendo wenye dhambi, madaraka au mapendeleo aliyokuwa nayo yaweza kuondolewa ili ‘kumwadhibu katika haki.’ (2 Tim. 3:16; Ebr. 12:5, 6) Katika visa vyote, wazee watafikiria mambo kama vile uzito wa kosa, muda ambao umepita tangu kosa lilipofanywa, kama limefanywa kwa makusudi au kwa sababu ya kukataa kusikiliza onyo alilopewa mapema.

24, 25. (a) Kanuni hizi za Biblia zataka wazee watumie nini, na jinsi gani? (b) Ni nini kinachobaki sasa kufikiriwa?

24 Kwa kweli, yote hayo yahitaji kiasi na uamuzi mzuri, busara na ufahamu. Lazima wazee wapime kwa uangalifu faida za mtu huyo na za kundi lote. Kwa upande mmoja, lazima waone sana wajibu walio nao mbele za Mungu kuzuia makosa yasipenye na kuenea katika kundi. Wakati ule ule lazima waonyeshe wanafikiria sana kwamba njia yao ya kushughulika na ndugu zao inapatana sikuzote na njia za Yehova Mungu mwenyewe zenye hekima na rehema.​—Linganisha Matendo 20:28:31; Yuda 3, 4, 21-23.

25 Basi, namna gani juu ya agizo la Paulo kukaripia wale wanaodumu katika dhambi “mbele ya watazamaji wote”? Na tuchunguze jinsi agizo hilo linavyopaswa kutimizwa.

[Maelezo ya Chini]

a Katika Isaya 1:18, NW ambapo neno la Kiebrania linalolingana na e·lengʹkho limetumiwa, Yehova aambia Israeli hivi: “‘Njoni, sasa, enyi watu, na mwache tunyoshe mambo [“tusemezane,” Union Version; “mwache tuyabishanie na kuyamaliza,” New English Bible] kati yetu,’ asema Yehova. ‘Hata ikiwa dhambi zenu watu zi kama damu, zitafanywa nyeupe kama theluji.’”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki