Toba ya Kweli—Inatambuliwaje?
“Moyo uliovunjika na kupondeka, Ee Mungu, hutaudharau.”—Zab. 51:17.
1. (a) Ili kupata msamaha, ni nani anayepaswa kuungamiwa dhambi, na kwa sababu gani? (b) Kwa sababu gani dhambi juu ya Yehova Mungu inaweza kuwa dhambi juu ya kundi pia?
WAZEE si mapadre ambao wamepewa mamlaka ya kusamehe washiriki wa kundi dhambi zote ambazo huenda wakafanya. Yehova Mungu ndiye anayesamehe watu dhambi zao wanapotubu, naye anafanya hivyo kwa kutegemea dhabihu ya Mwanawe yenye kulipia dhambi. Kwa hiyo, mtu hasamehewi na Yehova kwa sababu ya kuungamia wazee dhambi zake. (1 Yohana 1:8, 9; 2:1, 2) Lakini, anaweza pia kulitenda kundi dhambi kwa kufanya kosa kubwa. Ndivyo ilivyo kwa sababu kosa kubwa linaweza kuleta suto kubwa na matata mengi juu ya kundi ambalo mwenye kupotoka anashirikiana nalo. Kwa hiyo, wazee wanaowakilisha kundi wahakikishe kwamba mtu ametubu kikweli kabla ya kumsamehe kuhusu sifa mbaya ambayo ameletea kundi.
2. (a) Tunajifunza nini katika 2 Wakorintho 2:7 juu ya kama kundi linaweza kusamehe watu dhambi? (b) Kundi lilimsamehe nini hasa Mkorintho huyo mwenye kutubu?
2 Kwa kuangalia maneno ambayo mtume Paulo aliwaambia Wakorintho ili wakubali kumrudisha mtu mwenye kutubu aliyekuwa ametengwa na ushirika, inaonekana wazi kwamba kundi linaweza kusamehe watu au kukataa kuwasamehe nyakati fulani. Aliandika hivi: “Mmsamehe na kumfariji.” (2 Kor. 2:7) Mtume alipendekeza mtu huyo asamehewe kwa sababu ‘kemeo alilopewa na walio wengi’ lilikuwa limetimiza kusudi lake la kumsaidia atubu. (2 Kor. 2:6, NW) Ilifaa kundi limrudishe kwa sababu alikuwa ametubu kwa moyo mweupe na kunyosha maisha yake yakapatana na matakwa ya haki ya Yehova. Yeye alikuwa amemwomba Yehova amsamehe dhambi yake, kisha kundi nalo likamsamehe, lakini si katika maana ya kumwondolea hatia ya dhambi yake, bali kumsamehe kuhusu matata, suto na huzuni ambayo kosa lake lililietea kundi.
3. Watu ambao wamefanya dhambi nzito wakidai kwamba walijikaripia wenyewe, inawapasa wazee wafanye nini?
3 Nyakati fulani huenda ikaja kujulikana kwamba mtu amekuwa akitenda dhambi zenye kuleta aibu nyingi sana. Kwa muda wa miezi mingi au hata miaka mingi huenda akawa ameenenda kwa njia ambayo hata ulimwengu unaiona kuwa yenye dhambi. Baadaye, huenda akawajia wazee na kuwaambia kwamba juzijuzi aliacha makosa yake akamwomba Mungu amsamehe. Huenda akajisikia kwamba amejikaripia mwenyewe. Au, baada ya kupewa ushuhuda wa kuonyesha kwamba amekuwa na mwenendo wenye kuleta aibu, huenda akawaambia wazee kwamba alijikaripia mwenyewe, kwa hiyo hakuona uhitaji wa kuwaendea awapashe habari za mwenendo wake. Wazee wafanye nini? Inawapasa waangalie waone mtu huyo anahitaji msaada gani wa kiroho na kuona kama ametubu kikweli. Huenda wakahitaji kuzungumza naye zaidi ya mara moja ili kujua vizuri maoni yake, makusudi yake na mahitaji yake hasa. Mtu mwenye kutubu kikweli atakubali kwa unyenyekevu asaidiwe na wazee kwa njia hiyo ya upendo.
HUZUNI YA KILIMWENGU AU TOBA YA KWELI —JAMBO JIPI?
4. Je! nyakati zote huzuni nyingi ndiyo inayokuwa ushuhuda wa toba ya kweli? Eleza.
4 Bila shaka, inampasa mtenda kosa aone huzuni, masikitiko mengi na majuto juu ya dhambi yake. Huenda akatokwa au asitokwe na machozi, ikitegemea jinsi hali yake ya asili ilivyo. Lakini, wazee wakumbuke kwamba si nyakati zote mtu anapohakikisha ametubu kikweli kwa kuhuzunika, kusikitika sana au kujuta. Paulo mtume Mkristo aliandika hivi: “Huzuni iliyo kwa jinsi ya Mungu hufanya toba liletalo wokovu lisilo na majuto; bali huzuni ya dunia hufanya mauti.” (2 Kor. 7:10) Kwa hiyo, wazee watapaswa kutumia busara waone sababu inayomfanya mtenda kosa aone huzuni.
5. Ni jambo gani linaloongoza mtu awe na huzuni ya kilimwengu, na kwa sababu gani hiyo si toba ya kweli?
5 Huenda mtu akawa na huzuni ya kilimwengu kwa sababu tu anajisikia amekosa na kukata tamaa, au kwa sababu ya kuwa na wasiwasi wa kupoteza heshima au mapendeleo fulani, au kwa sababu ya kutarajia kupata adhabu au aibu. Anaona huzuni hiyo kwa sababu kosa lake lina matokeo yasiyopendeza na linaleta maumivu, au kwa sababu limejulikana. Ingawa ni jambo la kawaida kujisikia hivyo, ikiwa mtu anaona huzuni kwa sababu hiyo tu, huyo hajuti kikweli kwa sababu ya kutenda dhambi hiyo bali anasumbuka kwa sababu amejulikana. Huyo hasikitiki kikweli juu ya suto ambalo kosa lake limemletea Mungu.
6. Ni nini linaloonyesha kwamba Esau hakutubu kikweli ingawa alipiga mayowe wakati Isaka alipombariki Yakobo?
6 Mfano mzuri wa jambo hilo ni Esau. Yeye alimwuzia Yakobo haki yake ya uzaliwa kwa chakula kimoja. Miaka mingi baadaye, wakati Yakobo alipopokea baraka iliyokuwa haki ya mzaliwa wa kwanza, Esau alipiga mayowe kwa huzuni. “Akalia kilio kikubwa cha uchungu sana,” akitaka kumsihi Isaka baba yake abadili nia na kuiondoa baraka juu ya Yakobo. Esau hakujuta kwa sababu ya nia isiyo ya kiroho iliyomfanya ‘aidharau haki yake ya mzaliwa wa kwanza.’ Sivyo, yeye alijuta kwa sababu tendo lake lilimkosesha mapendeleo,—Mwa. 25:29-34; 27:34; Ebr. 12:16, 17.
7, 8. Ni jambo gani linaloonyesha kwamba Mfalme Sauli hakutubu kikweli ingawa alikubali kwamba alitenda dhambi?
7 Mfano mwingine ni Mfalme Sauli. Alipoambiwa na nabii Samweli kwamba aliidharau amri ya Mungu yenye kusema awaharibu Waamaleki, Sauli alijaribu kujitetea, akasisitiza kwamba alifanya kama Yehova alivyomwagiza. Ndipo Samweli alipomwonyesha mfalme huyo kosa lake kwa njia ya waziwazi, kisha akamwambia: “Kwa kuwa umelikataa neno la [Yehova], yeye naye amekukataa wewe usiwe mfalme.” Kusikia hivyo, Sauli akakubali kwamba: “Nimefanya dhambi; maana nimeihalifu amri ya [Yehova], pia na maneno yako; kwa sababu naliwaogopa wale watu, nikaitii sauti yao. Basi sasa, nakuomba, unisamehe dhambi yangu; rudi pamoja nami, nipate kumwabudu [Yehova].” (1 Sam. 15:17-25) Lakini kukubali dhambi yake kwa njia hiyo hakukuwa toba ya kweli. Kwa sababu gani?
8 Sauli alikuwa bado akipunguza uzito wa dhambi yake, akijaribu kutoa kisababu kwamba watu ndio waliomfanya aogope. Hakukubali kwa moyo kwamba alimtenda Yehova dhambi. Ni wazi kwamba alisema aliyosema kwa sababu ya kuogopa asikataliwe kuwa mfalme na kuaibishwa mbele ya watu. Jinsi gani? Kusudi la Sauli halikuwa kwamba Samweli arudi akamwombee asamehewe tu, hapana. Wakati Samweli aliposisitiza kwamba anakwenda zake, Sauli alimsihi sana akisema: “Uniheshimu sasa, nakuomba, mbele ya wazee wa watu wangu, na mbele ya Israeli; rudi pamoja nami.” (1 Sam. 15:30) Kwa hiyo Sauli alisikitika kwa sababu watu wangemchukua vingine. Alitaka Samweli awe pamoja naye ili watu wamheshimu, asije akapata aibu Samweli asipokuwapo. Basi alikubali dhambi yake kwa mdomo tu. Hakuwa na “huzuni iliyo kwa jinsi ya Mungu” kwa sababu ya kumkosea Yehova.
9. Tunajifunza nini juu ya toba kutokana na mambo yanayosemwa na Maandiko juu ya Esau na Sauli?
9 Kutokana na habari za Biblia juu ya Esau na Mfalme Sauli, tunaweza kupata mambo ya maana sana yanayoweza kusaidia wazee wawe na busara ya kujua kama mtenda kosa ametubu. Huenda mtu akaonyesha huzuni ya kweli kwa kutokwa na machozi. Hata hivyo, mfano wa Esau wa kutokwa na machozi unaonyesha kwamba mtu anaposumbuka moyoni, hiyo tu haihakikishi ametubu. Vivyo hivyo, mtu asipotokwa na machozi, hiyo tu haionyeshi kwamba hakutubu. Jambo la maana ni kwamba mtu huyo ajute (asikitike) sana kwamba amefanya kosa, akubali kwamba amemtenda Yehova dhambi. Akiendelea kutetea matendo yake atafanya kuwe na mashaka kama kweli ametubu. Inampasa auchukie sana mwendo wake mbaya. Ingawa ni jambo la kawaida kuona aibu fulani kwa sababu ya kuwa na hatia ya dhambi nzito, asisikitike kwa sababu hasa ya matokeo yasiyopendeza yaliyoletwa na kosa lake, bali asikitike kwa sababu ameleta suto juu ya Yehova Mungu na kundi la watu wake. Inampasa ajute kwa moyo mweupe kwa sababu ameharibu uhusiano wake na Aliye Juu Zaidi.
NI MAMBO GANI YANAYOHUSIKA KATIKA TOBA YA KWELI?
10. Kwa sababu gani mtu anapoonyesha huzuni kwa sababu ya kumletea Yehova suto anapaswa pia kusikitika sana kwa sababu ya kuumiza ndugu zake na wanadamu wenzake?
10 Mtu akihuzunika kwa sababu ya kumletea Yehova suto, kwa kawaida ataonyesha amesikitika sana kwa sababu ya kuumiza ndugu zake na wanadamu wenzake pia. Mtume Yohana anaonyesha kwamba kuwapenda ndugu zetu kunaonyesha tunampenda Mungu pia, kwa maana mambo hayo mawili hayawezi kutenganishwa. (1 Yohana 3:11, 17; 4:7, 8, 11, 12, 20, 21) Nyakati zote kosa linaleta madhara. Tukiingia katika kosa fulani kubwa wakati wo wote, inafaa tutafakari mambo kama haya:
11. Tukiingia katika kosa kubwa wakati wo wote, ni baadhi ya mambo gani inatupasa tufikirie bila mchezo?
11 Baada ya kutenda kosa hilo, je! tunajisikia tukiumia moyoni tujuapo kwamba tumeacha kuwa kama Mungu tunayemtumikia, mwenye upendo na unyofu, tukatenda kwa choyo na pupa, bila kufikiria faida za wengine? (1 The. 4:3-6) Je! kweli ingefaa tudhani kwamba kosa kama uasherati linaweza kuwapa wengine furaha halisi? Ni kwa kadiri gani tumeonyesha tunataka wawe na tumaini la kupata faida za milele na uzima wakiwa katika upendeleo wa Mungu? Matendo yetu yanaweza kuwa hayakuwagusa wengine moja kwa moja, lakini bado wanaweza kuumizwa na mfano tunaoweka na mambo tunayofanya. (Rum. 14:7) Basi, je! tunajifikiria sana hata tujipendeze wenyewe ingawa tunajua tunaweka mfano mbaya, tukitenda mambo yanayoweza kulegeza wengine kiroho? (Tofautisha Warumi 15:2, 3.) Kulingana na maneno ya Yesu Kristo, njia ya uzima ‘ni nyembamba na imesonga, nao waionao ni wachache.’ (Mt. 7:14) Sisi wenyewe tunajua bila shaka kwamba bidii nyingi sana inatakiwa ili kuweza kubaki katika njia ya haki. Basi, je! tunataka kuwa watu wa kutembea katika njia hiyo nyembamba tukiangusha-angusha miamba inayoweza kukwaza wengine au kuwalemea zaidi ingawa tayari wanatatizwa kusonga mbele? Looo! tungekuwa tofauti namna gani na Baba yetu wa mbinguni! (Isa. 40:11) Kama vile mtume Paulo anavyosema, hakika ‘sivyo tulivyojifunza Kristo.’ (Efe. 4:19-24) Ikiwa kweli tunampenda Mungu na Mwanawe na kuwaonea fahari kwa sababu ya sifa zao bora, je! hatuoni aibu na huzuni nyingi kutenda tofauti sana na wao, kuwafanya waache kututumaini? Naam, mtu anatakiwa afikirie mambo kama hayo ili kuonyesha toba ya kweli.
12. Tunaweza kujifunza nini juu ya toba kutokana na mwendo ambao Mfalme Manase alifuata baada ya kusamehewa na Mungu?
12 Sehemu nyingine inayohitajiwa sana katika toba inaonyeshwa katika mfano wa Mfalme Manase wa Yuda. Biblia inatueleza habari hizi juu ya dhambi yake: “Akafanya mabaya mengi machoni pa [Yehova], hata kumkasirisha.” (2 Fal. 21:6) Mwishowe, Manase alichukuliwa mateka akapelekwa Babeli, kuonyesha kwamba Yehova alimhukumu. Alitubia huko. Maandiko yanasema: “Akamsihi [Yehova], Mungu wake, akajinyenyekeza sana mbele za Mungu wa baba zake. Akamwomba; naye akamtakabali, akayasikia maombi yake; akamrudisha tena Yerusalemu katika ufalme wake.” (2 Nya. 33:12, 13) Baada ya hapo Manase alijitahidi kama alivyoweza arekebishe makosa yake, akafutilia mbali ibada ya sanamu katika ufalme wake, akamtolea Yehova dhabihu na kutia watu moyo wamtumikie Aliye Juu Zaidi. (2 Nya. 33:15, 16) Hiyo inaonyesha kwamba toba ya kweli inahusu kuuacha mwendo mbaya na kujikaza sana pia kufanya yaliyo haki.
13. Ni mambo gani yanayoweza kuwa kati ya “matunda yapasayo toba,” na kwa sababu gani?
13 Basi, mtu mwenye kutubu kikweli anapaswa aweze kuonyesha “matunda yapasayo toba.” (Mt. 3:8) Hiyo inatia ndani kujitahidi arekebishe mambo kama awezavyo katika hali zake za sasa. Kwa mfano, kusema kwamba ametubu kusingekuwa na maana sana ikiwa hataki kurudisha kitu alichoiba. Vilevile kungekuwa na mashaka makubwa kama kweli ametubu asipokaza nia kufuata mwendo wenye haki.
14. Ni jambo gani linalopasa kuamua kama mtu atatengwa au hatatengwa na ushirika ikiwa dhambi yake ni kubwa sana na imeeneza sana sifa mbaya?
14 Lakini itakuwa namna gani ikiwa dhambi ya mtu ni kubwa sana na imeeneza sana sifa mbaya? Hapo tena, kutubu au kutotubu kikweli ndiko kutakakoamua kama mtenda kosa ataondolewa au hataondolewa kundini.
15. Ni wakati gani inapofaa wazee watenge mtu na ushirika, na kwa sababu gani?
15 Wakati wo wote kusipokuwa na ushuhuda wa kuonyesha kwamba mtu ametubu kwa moyo mweupe, wazee wanahitaji kujiangalia wasifanye mambo kwa ghafula tu bila kufikiri. Hawapaswi kuachilia makosa wakidhani si kitu sana hata ikiwa uvunjaji sheria wa mtu asiyetubu umeletea kundi suto na matata. Wakifanya hivyo, kundi lote kwa ujumla linaweza kuharibika. Huenda washiriki fulani wa kundi wakapata ujasiri wa kufanya mambo yasiyofaa na kutojali shauri hili lililoongozwa na Mungu: “Mwe kama watu walio huru, lakini mwushike uhuru wenu, si kama kitu cha kuwapofusha msione ubaya, bali kama watumwa wa Mungu.” (1 Pet. 2:16, NW) Tena, huenda mtenda kosa mwenyewe akadhani si jambo la maana sana kujiepusha na dhambi, akose kujizuia sana wakati ujao na kuingiza wengine katika uvunjaji sheria. Mfalme Sulemani mwenye hekima alisema hivi: “Kwa sababu hukumu juu ya tendo baya haitekelezwi upesi, mioyo ya wanadamu huthibitishwa ndani yao ili kutenda mabaya.” (Mhu. 8:11) Kwa hiyo, kukiwa na mashaka makubwa kama mtenda kosa ametubu kikweli, kisha kuwe na ushuhuda wa wazi kuonyesha kwamba ataelekea kuchafua wengine, wazee wasisite-site kutii onyo hili la upole: “Mwondoeni yule mbaya miongoni mwenu.”—1 Kor. 5:13.
MAKOSA YA WAZEE NA WATUMISHI WA HUDUMA
16. Mzee akiwa na hatia ya kosa zito, inampasa afanye nini, na kwa sababu gani?
16 Kwa kuwa wazee wana daraka zito sana katika kundi la Kikristo, wawekee wengine mfano mwema kwa mwenendo wao. Kwa hiyo, mzee akitenda kosa zito, ana wajibu wa kuipasha baraza ya wazee habari hizo, hata ikiwa amekwisha tubia kosa lake. Kwa sababu gani? Kwa sababu sasa amekuwa na lawama na kwa hiyo hastahili kuendelea kutumikia kama mwangalizi. (1 Tim. 3:2) Lisingekuwa jambo lenye kupatana na kanuni ya Mungu ya utakatifu wanaume wenye mawaa mazito ya kiroho wakitumikia kama wazee.—1 Pet. 1:15, 16; linganisha sheria iliyo katika Mambo ya Walawi 21:17-23, iliyokataza wanaume wa nyumba ya Haruni wasifanye kazi za kikuhani ikiwa walikuwa na walakini katika mwili.
17. Ni jambo gani linapasa kufanywa ikiwa mzee anajisikia kwamba sasa amekuwa na lawama?
17 Bila shaka, wazee wanapungukiwa mara kwa mara kuiga mfano wa Yehova kwa ukamili, sawa na washiriki wengine wote wa kundi. Huenda mzee akapata kujisikia kwamba hatimizi tena matakwa ya Maandiko kwa sababu ya kukosa-kosa mara nyingi, na huenda akawapasha wazee wale wengine habari hizo. Walakini, wakiisha chunguza jambo hilo na kufikiria dhamiri ya kundi lote kwa ujumla, wazee hao huenda wakakata maneno kwamba namna ya makosa yaliyofanywa na mwanamume huyo hayaleti mashaka juu ya sifa zake za kutumikia kama mwangalizi. (Angalia Wagalatia 2:11-14, ambapo tunaelezwa kwamba Petro alikaripiwa; kosa hilo halikumfanya asistahili kuendelea kutumikia kama mzee.) Hata hivyo, dhamiri ya mzee huyo ikiendelea kuona kwa-mba sasa amekuwa na lawama, wazee wale wengine waheshimu maoni yake na kumwondolea madaraka yake.
18. wazee wana wajibu wa Kumfanyia nini mzee mwenzao anayekuwa na hatia ya dhambi nzito?
18 Kwa upande mwingine, kukiwa na shtaka la haki juu ya mzee, au yeye akiungama dhambi nzito, wazee wale wengine wanapaswa kabisa kumwondolea uzee wake na kumkaripia kulingana na uhitaji, kisha wamwekee vizuizi vyo vyote vinavyoonekana kufaa. Au, wanapaswa kumtenga na ushirika ikiwa hataki kutubu.
19. Mtumishi wa huduma afanye nini akifanya dhambi nzito, na kwa sababu gani?
19 Kama ilivyo kwa habari ya wazee, kadhalika watumishi wa huduma wakiwa na hatia ya makosa makubwa wana wajibu wa kupasha wazee habari hizo. Wanaume ‘wasio na shtaka’ peke yao ndio wanaostahili kutumikia katika cheo hicho. (1 Tim. 3:10, NW) Kwa hiyo, makosa ya watumishi wa huduma yanashughulikiwa kama ya wazee.
20. Kuwekea wengine mfano mwema wa toba ya kweli kunaweza kuleta faida gani?
20 Ikiwa Mungu anamtaka kila mshiriki wa kundi la Kikristo awe na uangalifu mwingi wa kumpendeza na kuendelea kuwa safi kwa ajili ya utumishi wake, hakika inawapasa wazee na watumishi wa huduma pia waangalie sana mwenendo wao. Kwa kawaida wao wanakuwa na ujuzi mwingi zaidi katika maisha ya Kikristo naye Mungu anatazamia mengi zaidi kwao, kwa maana wao ni mifano kwa wengine. (Linganisha Luka 12:48; 1 Petro 5:2, 3.) Hata wakifanya kosa zito, wanawekea wengine mfano mwema wakitubu kwa moyo mweupe na kuonyesha hivyo wazi kwa kuliacha kosa lao na kuipasha baraza ya wazee habari za kosa hilo. Mfano huo unaweza kusaidia wengine wanaotumbukia katika dhambi nzito wafuate mwendo kama huo wa kutubu. Juhudi hiyo ya kujiweka katika hali nzuri mbele za Mungu kwa kuchukizwa na makosa yao wenyewe na kuyarekebisha italetea wote wokovu. Zaidi ya hilo, itadumisha amani kundini—amani pamoja na Mungu na kati ya mtu na mwenzake.—2 Kor. 7:11.
21. Toba inaweza kutuletea mambo gani yanayofaa?
21 Lo! jinsi toba ya kweli ilivyo ya maana sana! Hakika, kila siku tunashindwa kwa njia fulani kuiga mfano wa Yehova Mungu kwa ukamilifu, kwa sababu sisi si wakamilifu. Inafaa tujute (tusikitike) tuonapo tumepungukiwa hivyo. Lakini tusijitese sana kwa sababu ya kila kikosa tufanyacho. Hata hivyo, kujua kwamba tunakosa mara nyingi kwa maneno na matendo kunapasa kutunyenyekeze na kutusaidia turehemu wengine wanapotutenda dhambi. Halafu, tusalipo Mungu atusamehe makosa yetu, tunaweza kuwa na hakika kwamba atapendezwa na sala zetu. (Mt. 6:12, 14, 15) Hivyo, tutafurahia kuwa na dhamiri safi tunapoendelea kujitahidi kufanya mapenzi yake. Naam, tutakuwa wenye furaha kweli kweli, tukijua kwamba Yehova ametusamehe dhambi zetu na anatuona kuwa watumishi wake safi wenye taraja la kupata uzima wa milele.—Zab. 32:1, 2; 103:10-13. —Kutoka The Watchtower, Nov. 15, 1977,
[Picha katika ukurasa wa 16]
Ingawa Mfalme Manase alikuwa ametenda dhambi nyingi, alihakikisha ametubu kikweli kwa kuyaondolea mbali “maashera” (nguzo takatifu) kwa juhudi