Kukaripia “Mbele ya Watazamaji Wote”
“Yakupasa umpige mwenye dhihaka, ili mjinga apate kuwa mwenye busara; na mwenye ufahamu apaswa kukaripiwa, ili apate kufahamu maarifa.”—Mit. 19:25, NW.
1. Kulingana na 1 Timotheo 5:20, wanaodumu katika dhambi wanapaswa kukaripiwa mbele ya nani, na kwa sababu gani?
BASI, namna gani maagizo ambayo Paulo alimpa Timotheo kukaripia “mbele ya watazamaji wote [kwa halisi, katika Kigiriki, “machoni pa wote”]” wale wadumuo katika dhambi? Kusudi la kukaripia hivyo liko wazi, yaani, ili “wale wengine wote waogope pia,” yaani, waogope kuingia katika mwendo uo huo wa kutenda dhambi. (1 Tim. 5:20, NW) Basi, ni hali gani zinazofanya mtu astahili kukaripiwa hivyo, na awezaje kukaripiwa “machoni pa wote”?
2-4. Ni nini linaloweza kusemwa juu ya matumizi ya maneno “mbele ya watazamaji wote,” na ni mifano gani ya Biblia inayoonyesha hivyo?
2 Maneno “mbele ya watazamaji wote” au “machoni pa wote” hayaonyeshi waziwazi yanavyotumika. Yanaweza kumaanisha kwamba karipio linatolewa mbele ya kundi zima au linatolewa mbele ya wote wale wanaohusika kwa njia fulani au wanaojua jambo hilo, kutia na mashahidi wa kosa lenyewe, wanaokuwapo wakati mtenda kosa anapokaripiwa. Vyo vyote iwavyo, ni wazi kwamba karipio lilipaswa kuwa mbele ya watu wengi badala ya kuwa la faraghani tu.a
3 Maneno ayo hayo ya Kigiriki yanayopatikana katika 1Timotheo 5:20 yanatumiwa pia katika Luka 8:45 juu ya mwanamke aliyeponywa kutiririka damu na Yesu. Masimulizi yasema kwamba ‘alimweleza mbele ya watu wote [Kigiriki, “machoni pa wote”] sababu yake ya kumgusa.’ Ni wazi kwamba hiyo haimaanishi mwanamke huyo alimweleza mbele ya watu wote wa mji (ambao pengine ulikuwa Kapernaumu) bali mbele ya watu waliokuwa katika kundi hilo wakamsikia Yesu akiuliza hivi: “Ni nani aliyenigusa?”—Luka 8:43-47.
4 Habari nyingine zinazofanana kidogo na hilo ni zile anazosema mtume Paulo juu ya alivyokaripia Petro katika Antiokia: “Walakini, nilipoona ya kuwa njia yao haiendi sawasawa na ile kweli ya Injili, nalimwambia Kefa [Petro] mbele ya wote [hao, NW] . . .” Ingawa “mbele ya wote” hapa yaweza kumaanisha mbele ya kundi zima lililokusanyika, kijina “hao” chaweza kumaanisha pia wale ambao Paulo alikuwa ametaja wakati uo huo, ‘wale ambao njia yao haikuwa ikienda sawasawa na ile kweli ya Injili.’ Chaweza kumaanisha alitoa karipio lake katika kusanyiko lililokuwa tofauti na mkutano wa kundi, pengine chakulani, ambapo waamini Wayahudi walikuwa, wakiwa wamejitenga na wengine, kama Petro.—Gal. 2:11-14.
5. Kusipokuwa na kanuni ya wazi ya Maandiko, tutaongozwa na nini katika matumizi haya?
5 Kwa kuwa hatuwezi kushikilia kauli yetu juu ya vile maneno “mbele ya watazamaji wote” yanavyopaswa kutumiwa hasa, inaelekea kwamba uhitaji uliopo ndio unaopaswa kuongoza matumizi yake. Ikiwa kundi lote lapaswa kujulishwa habari za karipio, basi na iwe hivyo. Ikiwa halipaswi, karipio litolewe mbele ya wote wanaohusika katika jambo hilo au wale ambao kwa sababu fulani wanahitaji karipio ili wafaidike nalo.
UPENDO WA KIMUNGU WAONGOZA
6. Kulingana na Maandiko, upendo una maongozi gani katika mambo haya?
6 Ziko kanuni za Maandiko zinazokataza kutangaza makosa na dhambi za wengine bila sababu. Biblia kwa ujumla yaonyesha kwamba upendo kwa kawaida wapaswa kuongoza mtu afunike dhambi za ndugu yake badala ya kuwaeleza wengine kwa makusudi. (Linganisha Mithali 10:12; 11:12, 13; 16:27; 17:9; 1 Pet. 4:8.) Yehova ataja habari za kukaripia mtu ambaye, licha ya kutenda makosa mengine, amefunua au akaeleza wengine kosa la ndugu yake mwenyewe isivyompasa. (Zab. 50:20, 21) Mwana wa Mungu alitoa kanuni ya kimungu inayotumika katika visa vyote: “Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo.” (Mt. 7:12) Hakuna ye yote kati yetu angetaka makosa yake yatangazwe hadharani ikiwa hakuna uhitaji halisi wa kufanya hivyo. Kwa upande mwingine, ikiwa ndugu zetu wanahitaji kusikia jambo fulani kwa faida yao wenyewe, lazima tufikirie vile ambavyo tungalijisikia kama tungalikuwa katika hali yao, na kutambua kwamba sisi wenyewe tusingetaka tufichwe habari tunazopaswa kuzijua.
7, 8. Toa mfano wa vile kutangaza bila sababu kosa la mtu mwingine kunavyoweza kuleta madhara ya bure.
7 Ikiwa hakuna uhitaji halisi wa kutangaza makosa ya wengine, kuyatangaza kwaweza kuleta madhara ya bure. Kwa mfano, fikiria msichana mrembo ambaye alifanya kosa fulani mara kadha akiwa katika kazi yake ya kusafiri. Tuseme wazee wamepata habari hizo kwa mtu mwingine, na kwa sababu msichana huyo ameshindwa kuwaendea kwa hiari yake mwenyewe, baadaye wanaamua kutangazia kundi kwamba wamemkaripia, na kutaja jina lake, baada ya kuzungumza naye na kuamua kwamba ripoti hiyo ni ya kweli. Kundi lingedhani namna gani? Ingekuwaje kama wengine wangedhani kosa alilofanya ni uasherati, na kumbe haikuwa hivyo. Katika safari hii msichana alikwenda karibu na nyumbani kwao akatembelea watu wa jamaa yake ambao si Mashahidi. Mazoea yao ya kuvuta sigara yakamdhoofisha hata yeye akavuta mara kadha. Basi, kundi likitangaziwa tu jina lake na kuelezwa kwamba amekaripiwa, huenda wengi wakaanza kumdhania isivyo.
8 Hali nyingine kama hiyo huenda ikahusu mume anayekunywa vileo kwa kawaida kiasi cha kulewa akiwa nyumbani, akifanya hivyo mara kadha. Tena, kundi likitangaziwa amekaripiwa, huenda wengine wa wasikilizaji wakamdhania mume huyo alikuwa mzinzi au alifanya dhambi nyingine nzito, na kumbe sivyo. Tangazo hilo lingeletea watu hao na kundi faida gani, na je! lingeondoa madhara yaliyotokezwa?
9, 10. (a) Njia iliyotumiwa kushughulika na kesi za makosa katika Israeli yaonyesha nini juu ya kutangaza makosa ya mtu? (b) Hatua kali ambayo ingechukuliwa hata Waisraeli wasikie na kuogopa ilihusu dhambi za namna gani?
9 Kanuni ya kutotangaza kosa la mtu isivyohitajiwa ingeelekea pia kuungwa mkono na utaratibu wa kawaida, uliofuatwa katika Israeli wa asili chini ya agano la Torati. Kanuni za Biblia na masimulizi yake yaonyesha kwamba visa vya kutenda makosa vilipelekwa mbele ya wazee wa mji katika malango, hasa mabishano yalipotokea, kama wakati mkosaji alipokataa kuwa hakumkosea mwenzake, na vilevile wakati mtaa mzima ulipoumizwa vibaya au ukahatirishwa na kosa.—Tazama Aid to Bible Understanding, kur. 384, 385, 1053, 1054.
10 Maneno yaliyotumiwa na mtume katika 1 Timotheo 5:20, NW “ili wale wengine wote waogope pia,” yatukumbusha mitajo katika agano la Torati juu ya hatua kali iliyochukuliwa juu ya wakosaji fulani, nayo maneno yanayotumiwa hapo ni “Israeli wote watasikia na kuogopa, wasifanye tena uovu mfano wa huo katikati yako.” Lakini inastahili kuangaliwa kwamba dhambi zilizohusika ama zilikuwa zile ambazo zingeweza kuleta hatari kubwa mtaani na kufanya mtu astahili kifo, kama kuchochea watu waasi imani, ama zilikuwa dhambi ambazo zilikuwa zimekwisha julikana hadharani, kama kutoa ushuhuda wa uongo katika baraza ya hukumu ya hadhara.—Kum. 13:6-11; 17:8-13; 19:15-20.
11, 12. Ni nia gani ambayo Yesu anatia watu moyo wafuate katika Mathayo 18:15-17 juu ya dhambi nzito alizotoa mashauri kuzihusu?
11 Maagizo ya Yesu katika Mathayo 18:15-17 pia yaonyesha matatizo ya kipekee yasitangazwe ikiwezekana. Kifungu kinachohusiana na hicho katika Luka 17:3, 4 chaonyesha kwamba shauri hili lahusu dhambi zilizotendwa na mtu mmoja juu ya mwingine. Yesu alisema kwamba mwenye kutendwa dhambi hapaswi kutangaza jambo lenyewe, bali amwendee mkosaji na kulinyosha faraghani. Hiyo yaweza kumwonyesha mkosaji huruma aliyofanyiwa kwa kutotangaza jambo hilo, kumfanya aitikie zaidi karipio. Hata ikiwa mtu hakufaulu alipomwendea mkosaji faraghani, hakupaswa bado kulieneza jambo hilo, bali ilimpasa kuendea mtu mmoja zaidi au wawili wajaribu tena. Baada ya kikundi hicho kidogo kushindwa, ndipo jambo lenyewe lingeletewa “kundi” (yaani, washiriki wenye kuliwakilisha, wazee; linganisha Hesabu 35:12, 24, 25 na Kumbukumbu la Torati 19:12; Yoshua 20:4).
12 Yapaswa iangaliwe kwamba dhambi zinazofikiriwa katika shauri la Yesu zilikuwa dhambi nzito, kwa sababu alisema kutokuitikia karipio la kundi kungefanya mtu atengwe na ushirika. (Mt. 18:17) Hata hivyo, ijapokuwa zilikuwa nzito, dhambi hizo hazikupaswa kutangazwa ikiwa hali hazikuhitaji zitangazwe. Tena, ingawa shauri hili lahusu waziwazi dhambi ambazo mtu alitenda mwenzake, inaelekea kwamba kanuni ambayo Mwana wa Mungu alitoa juu ya kuepuka utangazaji usio na sababu inatumika katika visa vyote, hata kosa liwe la namna gani.
13. Kwa kurudia, ni wakati gani mtu apaswa kukaripiwa mbele ya kundi lote kwa sababu ya kutenda dhambi, na ni wakati gani hilo lapaswa kufanywa “kwa ukali”?
13 Kutokana na ushuhuda wote wa Maandiko ingeelekea kwamba nyakati ambazo mtu aliyetenda dhambi ahitaji kukaripiwa mbele ya kundi lote zingekuwa nyakati chache ambazo makosa mazito yalifanywa, ambayo bila shaka yatajulikana na watu wote au yamekwisha julikana, au nyakati mtu amesaidiwa kwa jitihada nyingi atubu na kuacha kosa lakini matokeo yakawa yenye kuleta wasiwasi na kuonekana kwamba hatari yaweza kutokea kundini, hatari ambayo yawapasa waonywe ili wajilinde.b Ikiwa kosa linafanya matata yaenee kundini, karipio lapaswa litolewe “kwa ukali” na kuendelea kutolewa mpaka makosa yasafishwe kabisa.—Tito 1:13.
KUKARIPIA HADHARANI
14. Kwa sababu gani tangazo peke yake kwamba mtu amekaripiwa halitimizi hasa agizo la ‘kukaripia mbele ya watazamaji wote’? Ni nini kinachohitajiwa?
14 Karipio lenye matokeo mazuri juu ya mtu anayedumu katika kosa lahitaji ushuhuda wenye kusadikisha utumiwe kutoka Neno la Mungu. Kufanya tangazo mbele ya kikundi cha watu kwamba mtu “amekaripiwa” hakuwezi peke yake kuwa kisa cha ‘kumkaripia mbele ya watazamaji wote.’ Tangazo lasema kwamba “amekaripiwa,” kuonyesha kwamba alikaripiwa zamani—si mbele ya wenye kusikia tangazo, ama sivyo wasingehitaji kusikia tangazo la namna hiyo. Tangazo hilo lingeweza kuitwa ‘kemeo mbele ya watazamaji wote’ lakini likiwa peke yake halitoshi kuwa karipio. Ni kweli kwamba kemeo hilo linashtaki au linafunua wazi ubaya wa mtu mbele ya wengine, lakini halina ushuhuda wenye kusadikisha unaoonyesha maana ya karipio. Ili kutoa karipio la kweli mbele ya kundi, Neno la Mungu lazima likaziwe sana juu ya jinsi linavyohusu namna fulani ya dhambi inayohusika. Hilo ni jambo la lazima ili kutia wasikiaji woga wa kuingia katika kosa hilo.—2 Tim. 4:2.
15, 16. Je! kutaja jina la mtu ni kwa lazima ili kumkaripia “mbele ya watazamaji wote,” nayo 1 Wakorintho 14:23-25 yaonyeshaje hilo?
15 Je! linalohitajiwa ili kukaripia mtu aliyekosa “mbele ya watazamaji wote” ni kutaja jina lake? Kwa kuwa Maandiko yenyewe hayaonyeshi jina lapaswa kutajwa, ingeelekea kuwa kwamba jambo hilo pia lingetegemea uhitaji uliopo. Lakini ni wazi kwamba karipio hilo laweza kutolewa katika kusanyiko la watu wote bila kutaja jina au majina ya wenye kukaripiwa.
16 Kwa mfano, katika barua yake ya kwanza aliyowaandikia Wakorintho, mtume Paulo aeleza juu ya kuingia kwa mtu wa nje katika mkutano wa Kikristo. Hapo zamani huenda mgeni huyu akawa hakutambua ubaya wa matendo na maisha yake ya zamani. Hakuona haja ya kutubu. Lakini mtume asema kwamba, baada ya kuwasikia waliopo mkutanoni wakisema kweli ya Mungu, mtu huyu “akaripiwa [asadikishwa dhambi yake, An American Translation] na wote hao, anachunguzwa sana na wote; siri za moyo wake zinakuwa dhahiri.” Hiyo haimaanishi wote waliopo wanataja jina lake kwa sauti kubwa, kwa maana yeye ni mgeni kwao. Lakini kweli thabiti wanazonena zinamwonyesha kwa njia mpya jinsi alivyo na kumchochea moyo wake atubu.—1 Kor. 14:23-25, NW.
17. Kwa sababu gani wengine Krete walihitaji karipio kali, naye Tito angewezaje ‘kuendelea kuwakaripia’?
17 Alipomwandikia Tito katika kisiwa cha Krete, Paulo alimwonya kwa upole ‘aendelee kukaripia watu fulani kwa ukali, ili wapate kuwa na afya katika imani.’ Sababu ya kuhitaji karipio kali ni kwamba wao walikuwa wafanya matata kundini. Walikuwa ‘wakipinga, wakikaidi, wakinena mambo yasiyo na faida na kudanganya akili, wakipindua jamaa nzima kwa kuzifundisha mambo wasiyopaswa’; wengine walikuwa na kawaida ya kusema uongo na kuwa wavivu. Ili ‘kuendelea’ au kudumu katika kuwakaripia, haielekei kwamba Tito alirudia-rudia kusoma majina fulani na kutoa matangazo mara kwa mara kwamba walikuwa wakifuata mwenendo mbaya. Bali, katika mikutano ya faragha na ya watu wote, alikaza daima fikira zao juu ya Neno la Mungu na amri zake juu ya mabaya hayo. Kwa njia hiyo kundi lingeweza kutambua watu wo wote walioyafanya na kujilinda nao ili wasiwaongoze vibaya. Mashauri makali ya Maandiko yangesaidia kundi zima liwe na woga mzuri wa kutoshiriki katika mazoea hayo.—Tito 1:9-13; linganisha 2 Timotheo 4:2-4; 2 Wathesalonike 3:6-15.c
18. Ni hali gani hasa zingehitaji mtu akaripiwe kwa kosa katika mikutano ya kundi?
18 Bila shaka mara nyingi washiriki wa kundi wanapoingia katika kosa wanaweza kushughulikiwa faraghani na wachungaji wa kundi. Lakini ikiwa wachungaji wana sababu ya kuamini kwamba wengine huenda wakashawishwa kuingia katika dhambi iyo hiyo, yawapasa watumie wakati katika mikutano yao kutoa karipio juu ya kosa la namna hiyo. Ikiwa jambo limejulikana na hadhara au linahusu kashifa, yawapasa kabisa wafanye hivyo.
19. Ni chini ya hali gani wazee wanaweza kuona inafaa kutoa tangazo fupi na kutaja jina la mkosaji?
19 Wanaweza hata kutaja jina la mtu na kusema wamemkaripia (ingawa watafanya hivyo bila kutoa hotuba yo yote juu ya habari hiyo), wakiona hali zinafanya iwe lazima. Ikiwa kashifa inahusika, hiyo itawezesha washiriki wa kundi kulitetea kundi likishtakiwa na watu kwamba laachilia ubaya. Na hata ikiwa kosa halijulikani na watu wengi, au limefanywa kwa siri, huenda wazee wakaona ni lazima kufanya hivyo. Kwa mfano, huenda kijana akawa alifuata mwenendo fulani usio wa adabu (si lazima uwe uasherati) pamoja na wasichana kadha, akitoka kwa huyu na kwenda kwa yule. Baada ya kukaripiwa, huenda akatubu. Hata hivyo huenda wazee bado wakaona wana haki ya kumchukulia hatua. Pengine zamani alishauriwa na hivyo aonyesha hajitahidi sana kuepuka makosa. Huenda wazee wakaona ni lazima kundi lipewe taarifa fulani kuamsha wote, hasa dada vijana, kwamba wanapaswa kujihadhari kushirikiana na kijana huyo. Wanaweza kutangaza kwamba wamemkaripia, na kutaja jina lake.
20. Ikiwa tangazo fupi tu ndilo limetolewa; ni nini pia kinachohitajiwa ili kundi ‘liogope’ kuingia katika kosa la namna hiyo?
20 Bila shaka, ikiwa taarifa fupi imetolewa kwa njia hiyo, ikiwa kosa lenyewe lilifanywa kwa siri, walio wengi katika kundi hawatajua ni kosa la namna gani wanalopaswa kujihadhari nalo. Wasingeweza kutazamiwa, ‘kuogopa’ kufanya jambo bila kujua ni jambo gani. Kwa hiyo katika mkutano mwingine mzee anaweza kutoa habari za Maandiko zinazohusu namna ya kosa linalohusika, akionyesha jinsi watu wanavyoingia katika kosa hilo na sababu gani linakatazwa sana na ni lenye madhara, na vilevile kutoa mashauri juu ya njia za kujiimarisha tusitumbukie katika mtego huo. Lakini, atoapo hotuba hiyo hatataja majina yo yote.
21. Hata ikiwa jina halikutajwa, washiriki wa kundi wanaweza kulindwaje na wakosaji au kujulishwa kwamba wale ambao dhambi yao imeleta matokeo mabaya yenye kuonekana wazi, wamekaripiwa mbele ya watu wote?
21 Kwa kweli, huenda wazee wakaona hotuba hiyo tu ndiyo inayohitajiwa, kwa maana ingawa hakuna jina limetangazwa katika mkutano wa mapema, huenda hotuba hiyo ikatosha kuwapa washiriki wa kundi habari zote wanazohitaji ili kujikinga mtu huyo akiwaendea na kutumia tena njia zake za ujanja kama zilizoelezwa katika hotuba. Au, fikiria kisa ambapo uasherati umefanya mtu achukue mimba isiyo ya mwenzi wa ndoa au ukafanya atalikiwe kwa sababu ya uzinzi. Hotuba yenye kuonyesha jinsi mtu anavyoweza kuingia katika matendo ya uasherati yaweza kutia ndani onyo la kwamba ‘haitupasi kujisikia hilo haliwezi kutupata sisi, kwa maana limetukia katika kundi letu nasi twasikitika kwamba sasa linatokeza mambo haya yenye kuhuzunisha.’ Ingawa jina lo lote halikutajwa kabla ya hotuba, wakati ilipokuwa ikiendelea au baadaye, kundi lingejua kwa kuona mimba au talaka kwamba karipio limetolewa kweli.
22. (a) Wazee wana daraka gani la Maandiko kuhusu makosa na wenye kuyafanya? (b) Ingawa rehema yaonyeshwa, kwa sababu gani mwenye kutenda dhambi sikuzote hulipa kwa alilotenda?
22 Kama wachungaji, wazee wa kundi wanaweza kuponya, kukaripia kukemea (2 Timotheo 4:2, Kingdom Interlinear Translation), wanaweza kutengeneza mtu upya na kumtia adabu kwa kutumia Neno la Mungu. (Gal. 6:1; 2 Tim. 3:16; Yak. 5:14-16) Wanaweza ‘kukemea’ pia kwa kutenga na ushirika wasiotubu. (1 Kor 5:1-13; 2 Kor. 2:6-8) Kundi laweza kuonyesha rehema, lakini hiyo haionyeshi watenda dhambi wanaweza kuponyoka wasijulikane wakati wo wote. Kwa maana ingawa mtu akitubu aweza kupata rehema ya Yehova, dhambi italeta matokeo yasiyoepukika. Kwa kawaida dhambi huleta madhara sikuzote kwa mtenda kosa—madogo au makubwa—katika akili, mawazo ya moyoni au hata mwilini na kumharibia mali zake. Lakini yeye peke yake ndiye wa kujilaumu kwa madhara hayo. Anavuna kile ambacho amepanda.—Gal. 6:7, 8.
23. Ni mwendo gani unaofaa sote tuufuate kwa matumaini hakika na uvumilivu?
23 Basi, kwa hekima acheni sote tujitahidi kuwa ‘tukipandia,’ si mwili wenye dhambi na maelekeo yake mapotovu, bali roho, tukijua kwamba twaweza ‘kuvuna uzima wa milele katika roho.’ Naam, “tusichoke katika kutenda mema; maana tutavuna kwa wakati wake, tusipozimia roho” ya kufuatia haki inayotuhakikishia kwamba tutapata upendeleo wa Mungu na baraka zake nyingi.—Gal. 6:8, 9.
—Kutoka The Watchtower, Dec. 1, 1976.
[Maelezo ya Chini]
a Tafsiri kadha zinatumia neno “hadhara” au “kwa hadhara” zinapotafsiri 1 Timotheo 5:20. Lakini, baadhi yazo zaonyesha ‘watenda dhambi’ wanaotajwa ni miongoni mwa wazee tu waliotajwa katika mstari uliotangulia (mstari wa 19). Kwa mfano, tafsiri ya Knox inayosema, “Toeni kemeo la hadhara kwa wale wanaoishi isivyowapasa,” ina maelezo ya chini yanayosema hivi: “Kwa hao,’ labda ikimaanisha ‘kwa hao wazee’; nalo agizo la kwamba wanapaswa kukemewa hadharani laeleweka zaidi kumaanisha ‘Mbele ya wazee wale wengine.’” Kwa habari ya kama maneno “mbele ya wote” yanatumika ama kwa ‘wazee wote’ au kwa ‘wote kundini,’ kitabu cha maelezo cha Schaff-Lange chasema: “Kulingana na sarufi, maana zote mbili zaweza kwenda.” Twaonyesha mambo haya kuonyesha tu kwamba matumizi ya maneno katika 1 Timotheo 5:20 “mbele ya watazamaji wote” (au, “machoni pa wote”) yaweza kutumiwa kwa njia zaidi ya moja kulingana na sarufi: kwa kikundi kikubwa, kama kundi lililokusanyika, au kwa kikundi kidogo, kama baraza ya wazee.
b Vitabu vingi vya maelezo ya Biblia, vinapozungumza 1 Timotheo 5:20, vinatoa maelezo kupatana na jambo hilo. Kile cha Albert Barnes chasema: “. . . maana hapa inahusiana na vile mkosaji ambaye amehakikishwa kuwa ana hatia anavyopaswa kutendewa, na ikiwa jambo lile limejulikana na hadhara ya watu. Halafu inapaswa ionyeshwe hadharani kwamba jambo hilo limelaumiwa.” Kitabu cha maelezo cha Schaff-Lange kinasema: “Namna ya kisa chenyewe yahitaji kwamba neno ha·mar·taʹnon·tas lifahamike hasa kutumiwa juu ya uhalifu mbaya zaidi; ule unaoleta kashifa.” Henry’s Bible Commentary yasema: “Watenda dhambi wa hadhara, wenye kukashifu lazima wakemewe hadharani; kwa maana dhambi yao wameitenda hadharani, mbele ya watu wengi, au habari zake zikasikiwa na wote, kwa hiyo lazima karipio lao liwe hadharani, na mbele ya wote.”
c Ingawa watu fulani wametajwa kwa njia mbaya katika maandiko ya Paulo na Yohana, na iangaliwe kwamba hilo lilifanywa katika barua walizoandikiwa watu mmoja mmoja kwa kusudi la kuwaonya na waasi imani au watu waliopinga sana kazi ya mitume. (1 Tim. 1:19, 20; 2 Tim 1:15; 4:10, 14, 15; 3 Yohana 9) Lakini, barua nyingi zilioandikwa na waandikaji wenye kuongozwa na Mungu zina makaripio mengi yaliyohitajiwa kabisa lakini wakosaji hawatajwi majina.—Linganisha Warumi 2:1-4, 17-24; 1 Wakorintho 1:11-13; 3:1-4; 15:12; Yakobo 2:19.