Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 5/1 kur. 199-203
  • Jinsi Wakaripiaji Wenye Hekima Wanavyosaidia Wenye Kukosa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi Wakaripiaji Wenye Hekima Wanavyosaidia Wenye Kukosa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JINSI “KARIPIO” NA “KEMEO” YANAVYOTOFAUTIANA
  • KUSUDI LA KARIPIO LA KIKRISTO
  • KUKARIPIWA NA MIOYO YETU WENYEWE AU KUPITIA KWA WENGINE
  • Karipio
    Ufahamu wa Kina wa Maandiko
  • Kukaripia “Mbele ya Watazamaji Wote”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • ‘Makaripio Ndiyo Njia ya Uzima’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Kukaripia Watu Wanaozoea Dhambi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 5/1 kur. 199-203

Jinsi Wakaripiaji Wenye Hekima Wanavyosaidia Wenye Kukosa

“Kipuli cha dhahabu . . . ni mkaripiaji mwenye hekima juu ya sikio lenye kusikia.”​—Mit. 25:12, NW.

1, 2. Ni nini matokeo ya kuitikia au kushindwa kuitikia karipio la Mungu, na wazee wapaswa kufanya nini ili wawe wakaripiaji wenye hekima?

ZAMANI za kale mwanamume mwaminifu Elihu alisema juu ya Yehova Mungu hivi: “Yeye huyafunua masikio yao, wasikie maonyo, na kuwaagiza warudi kuuacha uovu. Kama wakisikia na kumtumikia, watapisha siku zao katika kufanikiwa, na miaka yao katika furaha. Lakini wasiposikia, wataangamia kwa upanga, nao watakufa pasipo maarifa. Lakini hao wasiomcha Mungu mioyoni hujiwekea hasira; hawalilii msaada hapo awafungapo.”​—Ayubu 36:10-13.

2 Kwa kufaa wazee Wakristo wanaonyesha wao ni wakaripiaji wenye hekima ili ‘kurudisha wenye kukosa waache uovu.’ Ni wazi kwamba wanatakiwa kufahamu maana ya “karipio” katika Biblia.

JINSI “KARIPIO” NA “KEMEO” YANAVYOTOFAUTIANA

3. Kemeo ni nini, na kwa kawaida kusudi lake ni nini?

3 Katika Biblia, katika lugha zake za asili, twaona maneno fulani yakitumiwa kueleza wazo la kukaripia na mengine kueleza wazo la kukemea. Tofauti ni nini? “Kukemea” maana yake ni kulaumu vikali au kutolea mtu sauti ya ukali, “kugombeza.” Huenda “kemeo” likawa kukataa jambo kwa ukali na mara nyingi kusudi lake ni kusimamisha mtu aache tendo fulani au usemi fulani unaoudhi au usiopendeza. (Linganisha Mwanzo 37:10; Ayubu 11:3.) Kwa mfano, wakati wanafunzi wa Yesu walipokuwa wakimshangilia akielekea Yerusalemu, Mafarisayo walimwambia, “Mwalimu, ukemee wanafunzi wako,” kumaanisha, ‘Waambie waache kusema mambo hayo.’ Yesu alijibu kwamba “hawa wakikaa wamenyamaza, mawe yatapaza sauti.”​—Luka 19:39, 40, NW.

4. Je! ulinganisho wa Mathayo 18:15 na Luka 17:3 waonyesha kwamba “kemeo” na “karipio” yaweza kutumiwa kwa njia ile ile?

4 Hapa mwandikaji wa Injili aliyeongozwa na Mungu alitumia neno la Kigiriki e·pi·ti·maʹo linalomaanisha ‘kemeo.’ Neno la Kigiriki linalolingana na ‘karipio’ ni e·lengʹkho. Katika Mathayo 18:15 (NW) neno hilo linaonekana wakati Yesu asemapo kwamba “ikiwa ndugu yako amefanya dhambi, nenda ukafunue kosa lake [Kigiriki, e·lengʹkho; Kingdom Interlinear, “ukaripie”] kati yako wewe na yeye peke yenu.” (Linganisha Mambo ya Walawi 19:17.) Katika kifungu kinacholingana na hicho katika Luka 17:3 (NW) Yesu atajwa akisema, “Ndugu yako akifanya dhambi mkemee [Kigiriki, e·pi·ti·maʹo], na akitubu msamehe.” Je! hiyo yaonyesha ‘kemeo’ na ‘karipio’ ni maneno yanayotumiwa kwa njia ile ile, yakiwa na maana moja? Isingekuwa hekima kuamua hivyo kwa kutegemea mfano huo mmoja. Matumizi ya Maandiko ya maneno hayo mawili yaonyesha wazi yanatofautiana.

5, 6. Ni mifano gani inayoonyesha kwamba maneno haya mawili yanatofautiana maana, na hiyo yaonyesha nini kuhusu matumizi yake katika maandiko mawili yaliyotangulia kutajwa?

5 Kwa mfano, katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, Yesu ‘anakemea’ (e·pi·ti·maʹo) mashetani, akiwaambia ‘wafumbe kinywa, na ‘kutoka’ ndani ya watu. (Mt. 17:18; Marko 1:25; 9:25; Luka 4:35, 41; 9:42) Hakuna po pote ambapo waandikaji wa Biblia wanataja mashetani wakikaripiwa (e·lengʹkho) na Yesu. Vilevile ‘aliikemea’ homa aliyokuwa nayo mama-mkwe wa Petro, ikamwacha; na katika Bahari ya Galilaya, ‘alizikemea’ pepo zenye nguvu nyingi na bahari yenye mawimbi makali, akazikomesha zisipindue mashua alimokuwa yeye na wanafunzi wake.​—Luka 4:39; Mt. 8:26; Marko 4:39; Luka 8:24.

6 Isingefaa kujaribu kutumia neno jingine badala ya “kukaripia” (e·lengʹkho) katika mifano iliyotangulia. Mtu aweza kukemea hata mnyama. (Zab. 68:30) Lakini, kama tutakavyoona, wanadamu peke yao, ambao ndio wenye uwezo wa kufikiri na wana sifa za moyoni na dhamiri, ndio wanaoweza kukaripiwa. Kwa hiyo inaonekana kwamba matumizi ya neno ‘kemeo’ katika andiko la Luka 17:3, lililotajwa mapema, yaonyesha tu kwamba karipio laweza kufuatana na kemeo.

7. Ni nini iliyokuwa maana ya neno la Kigiriki la “kukaripia” walilotumia waandikaji wa Biblia wenye kuongozwa na Mungu, kulingana na vile neno hilo lilivyotumiwa na watu wa siku zao?

7 Basi, neno la Kigiriki e·lengʹkho (kukaripia) lamaanisha nini? Ni kweli kwamba wakati mmoja neno hilo lilitumiwa wakati mmoja katika Kigiriki cha zamani kumaanisha “kutweza” au “kuaibisha.” Lakini kamusi za Kigiriki zaonyesha kwamba kwa kawaida neno hilo halikutumiwa katika maana hiyo.a Tena zinaonyesha kwamba katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo hilo silo wazo kuu la neno hilo. Angalia ufafanuzi unaofuata wa neno e·lengʹkho (kukaripia) unaotolewa na kamusi ya Liddell na Scott iitwayo Greek-English Lexicon:

“Kuhoji-hoji, kuuliza mtu maswali, . . . kushtakia mtu jambo fulani, . . . kusadikishwa kwamba umefanya kosa. . . . 2. kujaribu, kuchunguza. . . . 3. kuthibitisha . . . kuleta uhakikisho wenye kusadikisha. . . . 4. kukanusha, . . . b. kusawazisha, kusahihisha. . . . 5. kushinda mtu. . . .6. kufunua wazi ubaya wa mtu,”

8. Hiyo yaonyesha nini juu ya sababu kuu iliyofanya karipio lihitajiwe?

8 Ufafanuzi huo unategemea hasa jinsi maandiko ya Kigiriki yasiyohusiana na Biblia yanavyolitumia neno hilo. Lakini jambo moja li wazi kabisa kutokana na ufafanuzi huo. Wote unaonyesha kwamba mtu anayelazimika kukaripiwa anaonyesha nia ya kutokubali kosa au kadiri fulani anashindwa kutambua hali ya kosa lenyewe na uhitaji wa kulitubia, au anakana kabisa kwamba hakufanya kosa. Mtu wa namna hiyo aonyesha ahitaji “kusadikishwa” amefanya kosa. Tutaona sababu gani jambo hilo ni la maana kukumbukwa.

9, 10. Biblia yaonyeshaje pia kwamba kushindwa kutambua na kutubia kosa ndiko hufanya iwe lazima karipio litolewe?

9 Ufafanuzi huu unahakikishwa na matumizi ya Biblia ya neno la Kigiriki. Kwa mfano, angalia andiko lililotajwa mapema katika Mathayo 18:15 (NW) ambapo Yesu asema kwamba “ikiwa ndugu yako amefanya dhambi, nenda ukafunue kosa lake [e·lengʹkho; “ukaripie (yeye),” Kingdom Interlinear] kati yako wewe na yeye peke yenu.” Linalofanya iwe lazima mwenye kukosewa akaripie mkosaji kwa kufunua kosa lake ni kwamba, mkosaji hatambui au hakubali dhambi yake na kuitubia.

10 Maandiko mengine ambapo neno hili (e·lengʹkho) linatumiwa yanaeleza pia kukaripiwa kwa wale ambao kufikia wakati huo hawakuwa wamekubali sahihisho, wakaonyesha hivyo kwa kuendelea kufanya kosa lao.​—Linganisha Luka 3:19; Yohana 3:20; Waefeso 5:6, 7, 11-14; 2 Timotheo 4:2-4; Tito 1:9-13, NW; 2 Petro 2:15, 16.

11, 12. (a) Kwa hiyo njia inayolingana na Maandiko ya kukaripia wakosaji inatia ndani jambo gani la lazima, nalo kusudi lake ni nini? (b) Tofauti kati ya “kemeo” na “karipio” yaweza kuonyeshwaje katika jinsi wazazi wanavyotia adabu watoto?

11 Basi, ni kwa njia gani watu wanakaripiwa? Kukaripia si kufanyia mtu shtaka tu au kumlaumu kwa jambo ambalo amefanya (kama vile katika kemeo). Wala hakumaanishi kusoma tangazo tu kwamba mtu fulani ameingia katika mwenendo mbaya. Biblia yaonyesha kwamba karipio lahitaji kutoa ushuhuda au sababu. (Linganisha Waebrania 11:1, (NW), ambapo jina e·lengʹkhos limetafsiriwa “onyesho dhahiri” la mambo ya hakika.) Kwa hiyo, anapokazia tofauti kati ya maneno ya Biblia ya ‘kukemea’ na ‘kukaripia,’ kitabu cha mwanafunzi Mgiriki Trench kinachoitwa Synonyms of the New Testament chasema:

“Mtu aweza ‘kukemea’ mwenzake bila kumsadikisha kosa lake; na aweza kufanya hivyo kwa sababu kulikuwa hakuna kosa, kwa hiyo kemeo hilo halikuhitajiwa au halikuwa la haki (linganisha Mathayo 13:22; 19:13; 20:31); au kwa sababu, ingawa kosa lilikuwako, kemeo halikuhakikisha mkosaji alilifanya; nao uwezekano huu wa ‘kukemea’ mtu kwa sababu ya dhambi, bila ya ‘kumsadikisha’ ameitenda, ndio unaoonyesha tofauti ya maneno hayo mawili. . . . eʹleng·khos [karipio] halimaanishi shtaka lenyewe tu, bali pia ukweli wa shtaka lenyewe, na uwazi wa ukweli wa shtaka lenyewe; si hivyo tu; bali mara nyingi sana lamaanisha kutambua ukweli wake kwa ndani, ikiwa si nje, kwa upande wa mshtakiwa. . . . ”

12 Tofauti hiyo yaweza kulinganishwa na mzazi mmoja anayetosheka kwa kugombeza mtoto aache kufanya jambo fulani na mzazi mwingine mwenye nia ya kutumia wakati akisaidia mtoto aone sababu tendo lenyewe ni baya hasa na sababu gani yampasa atake kuliepuka. Ingawa makemeo yanastahili nyakati zinazofaa, mara nyingi karipio ndilo lahitajiwa zaidi.

13. Ushuhuda unaotolewa katika karipio unatimiza makusudi gani mawili?

13 Kwa hiyo kutoa ushuhuda wakati wa kukaripia huenda kukatimiza makusudi mawili: Huenda kusudi likawa kuhakikisha kwamba mtu huyo alifanya kweli tendo au matendo anayoshtakiwa, kumwonyesha mtu huyo jinsi mwenendo wake ulivyokuwa mbaya. Katika Yohana 16:8, 9 Yesu alisema kwamba roho takatifu ya Mungu ‘itauhakikisha ulimwengu [e·lengʹkho; “karipio,” Int] kwa habari ya dhambi, kwa sababu hawaniamini mimi.’ Lakini kwa habari yake mwenyewe Yesu alijua kwamba ingawa huenda wapinzani wake wakamkemea isivyo haki, wasingeweza kutoa “ushuhuda wenye kusadikisha” kwamba alifanya dhambi yo yote, kwa hiyo aliwaambia hivi: “Ni nani miongoni mwenu anishuhudiaye [e·lengʹkho; “anayekaripia,” Int] ya kuwa nina dhambi?”​—Yohana 8:46.

KUSUDI LA KARIPIO LA KIKRISTO

14, 15. Lakini, lengo la mwisho la karipio la Kikristo ni nini na ushuhuda wake wenye kusadikisha?

14 Lakini si hayo tu. Kwa watumishi wa Mungu, karipio si kuonyesha na kuhakikisha tu kwamba kosa limefanywa (kama neno hilo linavyomaanisha mara nyingi katika maandiko ya kilimwengu ya Kigiriki). Matumizi ya Biblia ya neno hilo yanatofautiana na linavyotumiwa katika ulimwengu. Kwa njia gani? Kwa sababu “karipio” katika Maandiko halikusudiwi kusadikisha watu tu kwamba wamefanya makosa wala kuwahukumu kwa haki tu. Ikieleza kusudi, kamusi Theological Dictionary of the New Testament (Vol. II) yasema (sisi ndisi tumelaza maneno):

“Matumizi ya e·lengʹkho katika A[gano] J[ipya] yana mipaka. . . . Maana, yake ni ‘kuonyesha mtu dhambi yake na kumwagiza atubu.’ Huenda hilo likawa jambo la faragha kati ya watu wawili, kama vile katika Mt. 18:15; Efe. 5:11. Lakini huenda pia likawa jambo linalohusu kundi likisimamiwa na kiongozi wake, kama vile katika Barua zinazozungumza juu ya Uchungaji wa Makanisa: 1 Tm. 5:20; 2 Tm. 4:2; Tt. 1:9, 13; 2:15. . . . Neno hilo halimaanishi ‘kulaumu’ au ‘kukaripia’ tu, wala ‘kusadikisha’ katika maana ya kutoa uhakikisho, wala ‘kufunua wazi’ au ‘kuonyesha wazi ubaya,’ bali pia ‘kusawazisha,’ yaani, ‘kuelekeza mtu atoke katika dhambi atubu.’”

15 Basi, kusudi la karipio si kuaibisha mtu tu au kuonyesha tendo lake baya lakataliwa, kama vile kemeo linavyokuwa. Badala ya kujaribu kumwachisha mtu tendo baya tu, kusudi la karipio linakuwa jema, yaani, kufikia moyo wa mtu na kumfanya alichukie kosa hilo. Kwa hiyo kusudi la ‘kufunua’ vyo vyote kosa la mtu si kuonyesha wazi ubaya wake mbele ya wengine bali ni kumpata kama ndugu na kujaribu kumzuia asipotee aliache kundi kwa sababu ya kuingia zaidi katika dhambi.​—Mt. 18:15, 16.

KUKARIPIWA NA MIOYO YETU WENYEWE AU KUPITIA KWA WENGINE

16, 17. Katika kujibu ulizo juu ya uhitaji wa kukaripia mtu ambaye amekwisha acha kosa, ni mambo gani yanayopaswa kukumbukwa?

16 Basi, namna gani Mkristo akifanya kosa fulani mara moja au zaidi, lakini baadaye dhamiri yake imwongoze kutubu kisha aache kosa lake? Je! bado ahitaji mtu wa kumkaripia?

17 Hapa yatupasa kukumbuka maana ya neno “kukaripia” (e·lengʹkho). Tumeona kwamba laweza kuwa na maana ya kushtaki na pengine kuuliza mtu maulizo au kumhoji-hoji, kuchunguza kosa lake ili alione, au kukanusha maoni yake mabaya juu ya tendo alilokubali amelitenda kwa kumpa sababu yenye kumsadikisha katika akili na moyo wake mwenyewe. Nalo kusudi la kufanya hivyo ni kumfanya atubu, ili aache lile jambo baya asilirudie tena.

18. Je! mtu anaweza kukaripiwa na moyo wake mwenyewe, na ikiwa ndivyo, ni jinsi gani?

18 Lakini, katika hali iliyotajwa mapema juu ya mtu anayetubia dhambi yake na kuiacha, je! mtu huyo hakujikaripia mwenyewe tayari? Ndiyo, dhamiri yake mwenyewe inamshtaki nalo Neno la Mungu na roho yake inamsadikisha, kisha moyo wake unamwongoza atubu na kuliacha kosa. Hahitaji mtu mwingine wa ‘kufunua kosa lake’ ili kumfanya akubali mwendo wake mbaya na kuusahihisha.​—⁠Linganisha Zaburi 16:7; Yeremia 2:19.

19. Twapata mfano gani wa hilo katika matendo ya Petro?

19 Bila shaka ndivyo ilivyokuwa kwa mtume Petro. Yesu alikuwa amemwonya Petro kwamba angemkana Bwana wake mara tatu. Hali zenye magumu za kukamatwa kwa Yesu na kujaribiwa kwake zilipofika, Petro alionyesha udhaifu akamkana Yesu mara tatu. Hata hivyo, kwa kutupiwa jicho tu na Yesu, moyo wa Petro uliguswa akatoka nje akalia kilio kichungu akitubia alilofanya. Moyo wake mwenyewe na kumbukumbu la maneno aliyokuwa ameambiwa na Yesu ulimkaripia. Mwendo aliofuata Petro tangu hapo wahakikisha alikuwa amekaza nia asirudie kosa kubwa kama hilo. Juma chache baadaye Yesu aliona imefaa kumtumia Petro kama mojawapo la ‘mawe ya msingi’ kulijenga kundi la Kikristo.​—Luka 22:54-62.

20, 21. (a) Ingawa mtu amekaza nia asirudie kosa, ni mpango gani anaoweza kutumia kwa hekima? (b) Kwa sababu gani Daudi alihitaji karipio, naye Nathani alimpaje?

20 Hiyo haimaanishi mtu hahitaji kusaidiwa inapokuwa hivyo. Ingawa huenda akawa amekaza nia asirudie kosa fulani, aweza kuhitaji kutiwa nguvu na wengine katika nia hiyo. Yehova Mungu ametokeza ndugu wa kutusaidia kwa njia hiyo.​—Mit. 17:17; Luka 22:31, 32; Gal. 6:2.

21 Tofauti na ilivyokuwa kwa habari ya Petro, Mfalme Daudi alihitaji mtu wa kumkaripia. Alitenda makosa mazito sana, yakaumiza sana wengine. Tena hakuwa amekubali kosa lake, bali alitafuta njia za kulifunika. Kwa hiyo Mungu alimtuma nabii Nathani akamkaripie Daudi. Nathani alifanya hivyo kwa kutumia mfano hodari wenye kumwonyesha wazi hali iliyolingana kabisa na kosa lake. Daudi alikasirishwa sana na uchoyo wa mtu aliyetajwa katika mfano wa Nathani, akamlaumu vikali mtu huyo kwa ukatili wake. Ndipo Nathani alipomshtua Daudi kwa kusema, “Wewe ndiwe mtu huyo.” Alipoona matendo yake yalivyokuwa mapotovu Daudi alitubu. Kama asingalitubu angalistahili kufa, kama yeye mwenyewe alivyokubali.​—2 Sam. 12:1-13.

22. Daudi aonyeshaje nia nzuri ambayo mtu apaswa kuwa nayo akaripiwapo, na vilevile faida kuu zinazoletwa na toba?

22 Katika mojawapo ya zaburi zake, Daudi alionyesha nia inayofaa kuwa nayo mtu anapokaripiwa, kwa kusema: “Mwenye haki angenipiga, zingekuwa fadhili za upendo; naye angenikaripia, ingekuwa mafuta juu ya kichwa changu, ambayo kichwa changu kisingetaka kukataa.” (Zab. 141:5, NW) Tena, katika Zaburi 32:1-6, Daudi alieleza mateso makali sana yaliyompata kwa kukosa kumwomba Yehova amsamehe dhambi zake na kupata faraja kwa kumtubia Mungu na kumwungamia.

23. Wakaripiaji wenye hekima watatambua nini, nayo maandiko yaliyoonyeshwa katika fungu hili yaonyeshaje hilo?

23 Ili wachungaji wa kundi wawe wakaripiaji wenye hekima, wanapaswa kukumbuka pia kwamba, karipio laweza kuwa na ukali unaotofautiana, kama vile kosa linavyoweza kuwa na uzito unaotofautiana. (Linganisha Wagalatia 6:1; 2 Timotheo 2:24-26 na Tito 1:13, NW.) Hata wale wanaofanya matendo mema wakiwa watumishi wa Mungu huenda nyakati nyingine wakahitaji kukaripiwa kwa kuwa na maoni mabaya, usemi au tendo baya.

24, 25. Je! Inawezekana watumishi waaminifu wa Mungu wahitaji pia karipio, nao wanapata faida gani kutokana nalo?

24 Ndivyo ilivyokuwa kwa Petro baadaye. Wagalatia 2:11-14 yasimulia kwamba alipokwenda Antiokia katika Shamu alichangamana na Mataifa wasiotahiriwa, akala vyakula pamoja nao. Lakini watu fulani wa kundi la Yerusalemu (watu ambao yaelekea bado walishikilia maoni ya Kiyahudi ya kujitenga na Mataifa) walipokuja Antiokia, Petro aliacha kushirikiana na Wakristo wa Mataifa. Mtume Paulo alipoona mwendo huo mbaya na matokeo mabaya uliyoleta juu ya waamini Wayahudi wengine, alilazimika kumkaripia Petro. Kwa kumpa Petro sababu kamili, alimwonyesha ubaya wa mwendo wake, akafanya hivyo wote waliokuwapo wakisikia. Hakuna shaka kwamba Petro alikubali karipio hilo na baadaye amtaja Paulo kwa kumthamini sana.​—2 Pet. 3:15, 16.

25 Naam, kama vile Mithali 9:8, 9 isemavyo: “Mkaripie mwenye hekima, naye atakupenda. Mwelimishe mwenye hekima, naye atazidi kuwa na hekima.” Kama ilivyokuwa kwa habari ya Petro, ‘mwenye ufahamu apaswa kukaripiwa, ili apate kufahamu maarifa.’ Basi, sikuzote na tufungue masikio yetu tupokee ‘makaripio ya adabu’ yenye hekima ambayo ndiyo “njia ya uzima” kwa wale wote wanaompenda Mungu, na haki yake.​—Mit. 19:25; 6:23; 25:12.

[Maelezo ya Chini]

a Kamusi Lexicon of the New Testament ya Robinson yasema juu ya neno e·lengʹkho hivi: “kuaibisha, kutweza, katika Homer tu [mtunga mashari Mgiriki aliyeishi kabla ya nyakati za Ukristo]. . . . Kwa kawaida na katika A[gano] J[ipya] kusadikisha, . . . kukanusha, kuhakikishia mtu ana kosa.”

Kitabu Word Studies in the New Testament cha Vincent chasema: ‘‘Katika Kigiriki cha asili lamaanisha kutweza au kuaibisha . . . Halafu [baadaye], kuhoji-hoji au kuuliza maulizo, kwa kusudi la kusadikisha, kusadikisha mtu kwamba ana kosa au kukanusha. . . . Kuhusu mabishano, kujaribu; hakikisha; hakikisha kwa mfululizo wa sababu.”‏ (Sisi ndisi tumelaza maneno)

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki