KARIPIO
Tendo linalokusudiwa kuwasadikisha watu kwamba wamekosea, ili kuwachochea kutambua makosa yao na kuyarekebisha. Tofauti na karipio, kemeo linaweza kuwa himizo lisilotia ndani kufunuliwa kwa kosa kupitia ushahidi. (Ona KEMEO.) Kitenzi cha Kiebrania ya·khachʹ (karipia) ni neno la kisheria linalofafanuliwa ‘kumfanya mtu awajibike’ (Isa 37:4) na “kunyoosha mambo” (Isa 1:18; 2:4). Neno la Kigiriki linalofanana na hilo ni e·legʹkho. Mara nyingi maneno hayo hutokeza wazo la kumpata mtu na hatia na kumtaka atubu. Kuhusiana na neno e·legʹkho linapotumika kwenye Septuajinti ya Kigiriki kutafsiri neno ya·khachʹ linalopatikana mara nyingi, kamusi ya Theological Dictionary of the New Testament inasema hivi: “Linahusisha Mungu kumtia nidhamu na kumwelimisha mwanadamu kama matokeo ya matendo Yake ya hukumu. Hilo linatia ndani nyanja zote za elimu kuanzia kumsadikisha mtenda dhambi mpaka kumpa adhabu, kuanzia kumwelekeza mwadilifu kupitia majaribu makali mpaka kumpa mwongozo kupitia mafundisho na himizo.”—Iliyohaririwa na G. Kittel, 1964, Buku la II, uku. 473.
Wakati Linapohitajika. Katika sheria ya Mungu kwa Waisraeli, watu waliotendewa makosa walihimizwa hivi: “Usimchukie ndugu yako moyoni mwako. Lazima umkaripie mwenzako, usije ukashiriki dhambi yake.” (Law 19:17) Hisia za kinyongo kumwelekea ndugu aliyekosea hazikupaswa kuruhusiwa kusitawi moyoni. Alipaswa kukaripiwa kukiwa na tumaini la kumsaidia aache dhambi zake. Kushindwa kutimiza wajibu huo kungemfanya aendelee kutenda dhambi, na yeyote ambaye angekataa kumkaripia ndugu yake angekuwa akishiriki katika dhambi za mtu huyo.—Linganisha Mt 18:15.
Nyakati nyingine, wazee wanaowakilisha kutaniko wanapaswa kumkaripia mtu aliyetenda dhambi nzito, na hata kufanya hivyo mbele ya watu wengine wanaojua kuhusu dhambi iliyotendwa. Karipio kama hilo si kwa ajili tu ya wale walio tayari kusikiliza. Wazee wanaambiwa ‘wawakaripie wale ambao hupinga’ na “kuwakaripia kwa ukali” wale ambao ni “waasi” na “wanaoongea maneno yasiyo na faida.”—1Ti 5:20; Tit 1:9, 10, 13.
Ingawa karipio linaweza kuwasaidia wale wanaolipokea, jitihada za anayetoa karipio hazithaminiwi nyakati zote. Ndio sababu Methali 9:7, 8 inatoa onyo hili: “Anayemrekebisha mtu mwenye dhihaka hualika aibu, na yeyote anayemkaripia mtu mwovu ataumia. Usimkaripie mtu mwenye dhihaka, kwa maana atakuchukia. Mkaripie mwenye hekima, naye atakupenda.”
Mtazamo Unaofaa. Kwa kuwa Maandiko yameongozwa na roho ya Mungu, ni wazi kwamba karipio lolote linalotegemea Maandiko linatoka kwa Mungu. (2Ti 3:16) Karipio kutoka kwa Yehova ni wonyesho wa upendo, na halipaswi kuchukiwa au kukataliwa. (Met 3:11, 12) Akiwa kichwa cha kutaniko la Kikristo na akiongozwa na upendo kuelekea wale waliofanyiza kutaniko, Yesu Kristo, anaona kwamba inafaa karipio litolewe kupitia wanaume wanaostahili kiroho. (Ufu 3:14, 19) Watu wenye hekima wanatambua kwamba “makaripio ya nidhamu ndiyo njia ya uzima.”—Met 6:23.
Mwelekeo wa mwanadamu mwenye dhambi ni kuchukia karipio na kumchukia anayetoa karipio. Lakini mtu mwenye mwelekeo huo ni sawa tu na mnyama asiyeweza kutofautisha mema na mabaya; kama methali iliyoongozwa kwa roho inavyoeleza: “Anayechukia karipio hana akili.” (Met 12:1) Tofauti na hilo, mtunga zaburi Daudi, aliyekaripiwa mara kadhaa, aliandika hivi: “Mwadilifu akinipiga, hilo litakuwa tendo la upendo mshikamanifu; akinikaripia, hilo litakuwa kama mafuta kwenye kichwa changu, ambayo kichwa changu hakiwezi kamwe kukataa.”—Zb 141:5.