Wewe Wapokeaje Shauri?
NI NINI kusudi la shauri ambalo mmoja humpa mtu mwingine? Ni kutoa msaada, uongozi au ufahamu juu ya namna ya kufanya jambo fulani. Yehova Mungu Muumba peke yake ndiye asiyehitaji mtu wa kumshauri, kama nabii alivyosema: “Ni nani . . . [wa] kumfundisha kwa kuwa mshauri wake? Alifanya shauri na nani, ni nani aliyemwelimisha na kumfunza njia ya hukumu, na kumfunza maarifa, na kumwonyesha njia ya fahamu?”—Isa. 40:13, 14.
Hata Yesu Kristo mwanadamu mkamilifu, akiwa na ujuzi wake wote aliokuwa nao mbinguni, alipokea na kufuata shauri kutoka kwa Mungu. Alisema hivi: “Sifanyi neno kwa nafsi yangu, ila kama Baba alivyonifundisha ndivyo ninenavyo.”—Yohana 8:28; 5:19, 30.
LAZIMA YA KUTII SHAURI
Basi, ili wafahamu njia ya haki na kutumia Neno la Mungu katika maisha zao, bila shaka wanadamu wasiokamilika wanahitaji sana shauri. Mtume Yohana alikazia hali inayofanya shauri lihitajiwe aliposema hivi: “Tukisema kwamba hatuna dhambi, twajidanganya wenyewe, wala kweli haimo mwetu.”—1 Yohana 1:8.
Ni maelekeo ya asili ya sisi sote kuchukia shauri kwa sababu ya dhambi tuliyozaliwa nayo, hasa ikiwa shauri hilo linaonyesha kosa au udhaifu. Yehova anaonya hivi: “Msiwe kama farasi wala nyumbu, walio hawana akili. Kwa matandiko ya lijamu na hatamu sharti kuwazuia hao, au hawatakukaribia.” (Zab. 32:9) Mtu anayeonyesha roho ya kuchukia, “mara nyingi akishupaza shingo,” akiwa asiyesikiliza shauri na asiyekaribiwa, atapata hatua Kali zaidi, vizuizi na, mwishowe, msiba.—Mit. 29:1.
Kwa upande mwingine, watu wanyenyekevu, wanaotamani kuendelea katika ufahamu, wanatafuta shauri. Sikuzote hawafikirii kuwa “sawa,” bali wanafikiria kufanya mambo yanayompendeza Mungu na yatakayosaidia wengine. Kwa hiyo, wanafahamu kwamba “kwa wingi wa washauri huja wokovu.” (Mit. 11:14) Wanapofanya kosa wanafurahi washauriwe, hata kama nyakati nyingine huenda isifurahishe. Wanataka waepuke kurudia kufanya kosa au jambo lisilofaa, kwa aibu yao. Wanafuata shauri la Mungu: “Inunue kweli, wala usiiuze; naam, hekima, na mafundisho, na ufahamu.”—Mit. 23:23.
ROHO NA KUSUDI LINALOFAA KATIKA KUTOA SHAURI NA KARIPIO
Huenda nyakati nyingine shauri likatia kukaripia. Neno asili la Kiebrania kwa “karipia” (reprove) lina maana ya: ‘kuamua mambo, kunyosha mambo.’ Katika maana ya Biblia, karipio ni kuthibitisha lililo jema na lililo baya katika kisa katika njia yenye fadhili na ya waziwazi. Ikitegemea hali na maoni ya mtu anayekaripiwa, huenda likafuatana au lisifuatane na kemeo (rebuke).
Mtume alifunua roho inayofaa ya yule anayetoa shauri aliposema juu ya daraka la wazee katika kundi la Kikristo: “Ndugu, hata ingawa mtu achukua hatua fulani ya uongo kabla ya yeye kuijua, ninyi mlio na sifa za kiroho jaribuni kumtengeneza upya mtu huyo katika roho ya upole, huku kila mtu akijiangalia mwenyewe, usije wewe pia ukashawishwa.”—Gal. 6:1, NW.
Kwa hiyo, mzee akiona ndugu wa Kikristo akichukua mwendo ambao huenda mwisho wake ukawa usiofaa, kwa sababu ya uamuzi usiofaa au wa upumbavu, hatamwacha ndugu yake aumie. Wala hatamkemea. Badala yake, yuko chini ya wajibu wa upendo kumwonya ndugu yake hatari, upumbavu au ubaya wa mwendo wake au wa fikira zake, na kufanya hivyo katika roho ya upole.
Kwa hiyo, kusudi la kutoa karipio ni kusaidia anayekaripiwa. Pia yule mkaripiaji anapendezwa na udumishaji wa amani na roho nzuri katika kundi. Mpokeaji wa karipio, akilikubali, anaokolewa asiingie katika taabu na kupoteza kibali machoni pa Mungu. Atabadilika, atengenezwe upya.
NAMNA GANI KAMA SHAURI LAUMIZA?
Lakini namna gani kama unaona kwamba shauri fulani unalopewa si zuri, labda ni wazo tu la mshauri? Kabla ya kulipuza shauri hilo, fikiria nia yako mwenyewe. Je! wataka kujipendeza mwenyewe, au Mungu? Labda mwendo wako si mbaya. Lakini hujali jinsi wengine waonavyo na mwendo huo? Mtume anatukumbusha hivi: “Imetupasa sisi tulio na nguvu kuuchukua udhaifu wao wasio na nguvu, wala haitupasi kujipendeza wenyewe. Kila mtu miongoni mwetu na ampendeze jirani yake, apate wema, akajengwe.”—Rum. 15:1, 2.
Ili tuongoze mwendo wetu kwa jinsi impendezayo Mungu, Paulo alisema hivi pia: “Vitu vyote ni halali; bali si vitu vyote vifaavyo. Vitu vyote ni halali; bali si vitu vyote vijengavyo.” (1 Kor. 10:23) Kulingana na sheria ya Kikristo kuna nafasi tele ya kutenda na inampasa Mkristo aamue mambo mengi kulingana na dhamiri yake ya Kikristo. Lakini yampasa afikirie pia dhamiri za wengine. Si mambo yote yamjengayo mwenyewe wala wengine. Mambo kama hayo yaweza kuachwa, hasa ikiwa yataharibu upendo na amani.
Huenda mara nyingine shauri likatolewa, si juu ya kosa, bali kwa kusudi la maendeleo. Labda unashauriwa juu ya ubora wa kusoma mbele ya watu wengi. Huenda ukashtuka, kwa vile ulidhani umesoma vizuri sana. Utafanya nini? Mbona usitafute kujua mahali ambapo hukusoma vizuri na jambo litakaloleta maendeleo? Bila shaka hakuna wo wote kati yetu ambao ni wasomaji wakamilifu—kuna nafasi ya kufanya maendeleo. Kabla ya kusoma mbele ya watu wengi, jitayarishe kwa kuangalia matamshi na maana ya maneno, angalia maana za sentensi na mkazo wa maana, na kadhalika. Bila shaka kusoma kwako kutakuwa bora, nawe utakufurahia zaidi.
Au, huenda ukashauriwa uwe mwenye urafiki zaidi na wengine. Labda unadhani moyoni mwako kwamba wewe ni mtu mwenye urafiki. Lakini kwa wazi hauonekani kwa wengine. Basi, likubali shauri kuwa lenye msingi fulani; jitahidi kupendezwa zaidi na wengine; urafiki, mwenye kusema, mwenye kuthamini. Hutaimarisha urafiki bora tu, bali pia roho yako mwenyewe itakuwa bora, nawe utakuwa mwenye furaha zaidi.
Hata ukiumizwa sana na shauri, kumbuka mfano wa Daudi. Aliadibishwa sana, lakini Mungu alikuwa akimzoeza afanye mambo makuu zaidi. Kwa yale yaliyompata, Daudi alisema hivi: “Mwache mwenye haki anipige; itakuwa fadhili: tena mwache anikaripie; yatakuwa mafuta bora, ambayo hayatapasua kichwa changu.” (Zab. 141:5, Authorized Version) Hata kama shauri la ndugu linakuwa kali usiweze kulipokea, halitakuua, ama kimwili ama kiroho, bali laweza kuwa kama mafuta yenye kulainisha, yenye kuburudisha. Ukilithamini sana, utaona utimizo wa mithali hii: “Yeye aangaliaye maonyo ataheshimiwa.”—Mit. 13:18; Ebr. 12:11.