Kuja kwa Siku ya Bwana Mungu ni Hakika
(Funzo la kitabu)
1, 2. Ni nini kitakachowagundulia (kuwapata ghafula) watu ambao, wajapomhesabia Mungu ukawivu, wao wenyewe wanakawia kuchukua hatua ya wokovu?
WATU wanaodhani kutumia kwa Mungu ustahimilivu na uvumilivu kuwa ukawivu upande Wake na wanaokawia kuchukua hatua ya wokovu watagunduliwa na uharibifu kutoka kwa Mungu. Mtume Petro alionya juu ya mwendo huo wa kudhania, wa uzembe na usio wa hekima kwa kusema: “Hata hivyo siku ya Yehova [he·meʹra Ky·rıʹou, Kigiriki; siku ya Bwana]a itakuja kama mwivi, ambayo katika hiyo mbingu zitatoweka kwa sauti yenye kelele, lakini vitu vya asili kwa kupata moto sana vitayeyuka, nayo dunia na kazi zilizomo zitavumbuliwa.”—2 Pet. 3:10, NW, maandishi ya pembeni.
2 Ile siku ya mwisho wa “mbingu zilizo sasa, na dunia” itakuja bila shaka, kwa maana ni sehemu ya kusudi la Mungu lililotangazwa. Wakati wake wa kufika kwa siku hiyo umewekwa katika mpango wake mwenyewe wa wakati. Makasisi wa Jumuiya ya Wakristo wanaoendelea kutumia dini kama njia ya kunyonyea watu wasio na akili wataona kwamba ndio wanaosinzia na kulala usingizi wasijue yanayotukia, na si Mungu mwenyewe. “Na katika kutamani watajipatia faida kwenu kwa maneno yaliyotungwa; ambao hukumu yao tangu zamani haikawii, wala uvunjifu wao hausinzii.”—-2 Pet. 2:3.
3. Mtume Paulo na Yesu Kristo walisema siku ya kufikiliza hukumu ya kimungu ingekuja kama nini?
3 Kuja kwa siku ya Yehova kama mwivi usiku kunaelezwa pia na mtume Paulo, anapowaandikia Wakristo katika Thesalonike, Makedonia hivi: “Lakini, ndugu, kwa habari ya nyakati na majira, hamna haja niwaandikie. Maana ninyi wenyewe mnajua yakini ya kuwa siku ya Bwana yaja kama vile mwivi ajavyo usiku. Wakati wasemapo, Kuna amani na salama, ndipo uharibifu uwajiapo kwa ghafula, kama vile utungu umjiavyo mwenye mimba, wala hakika hawataokolewa.” (1 The. 5:1-3) Kwa kuwa Yesu Kristo mwenyewe atatumiwa na Yehova Mungu kama mfishaji katika siku ya Yehova, alionya wanafunzi wake juu ya kukaribia kwa siku hiyo kama mwivi ili kuanza kufikiliza hukumu, akisema: “Lakini fahamuni neno hili; kama mwenye nyumba angaliijua ile zamu mwivi atakayokuja, angalikesha, wala asingaliacha nyumba yake kuvunjwa. Kwa sababu hiyo ninyi nanyi jiwekeni tayari; kwa kuwa katika saa msiyodhani Mwana wa Adamu yuaja.”—Mt. 24:43, 44; Luka 12:39, 40.
4. Kama inavyotajwa katika 2 Petro 3:10, ni “mbingu” gani zitakazotoweka?
4 Katika siku ya Yehova wanadamu watajikuta wamefunikwa na hali yenye moto ya taratibu hii ya mambo isiyomwogopa Mungu. Zile “mbingu,” “vitu vya asili,” na “dunia” ambayo wanadamu wamejua kwa maelfu ya miaka vitaharibiwa. Zile “mbingu” zitakazotoweka ni serikali za kisiasa ambazo zimetumikia kama “mamlaka iliyo kuu” kwa ruhusa ya Mungu na ambazo zimeendelea kutenda ijapokuwa mwisho wa Majira ya Mataifa katika mwaka wa 1914 W.K. Zimeinuka juu kama milima katika mambo ya dunia na kufunika mambo ya jamii ya kibinadamu. Makasisi, manabii na mapadre wa dini wamejiingiza katika serikali na wamejaribu kujitia kama sehemu kamili ya serikali, wakifanyiza mwungano wa Serikali na Kanisa katika nchi nyingi. Katika miungano ya Kanisa na Serikali ambayo ingali inaendelea katika huu “wakati wa mwisho,” ile sehemu ya kidini ndiyo ndogo, yenye kutii na inavumiliwa tu, haipendelewi kwa shauku sana.
5. Ni nini linaloonyeshwa na uhakika wa kwamba “mbingu” zitatoweka kwa “sauti yenye kelele”?
5 “Mbingu” hizo za kiserikali zitatoweka “kwa sauti yenye kelele,” kama mlio wenye kuendelea wa herufi “s.” Hii ingeweza kumaanisha sauti yenye mlio, kama ile inayofanyizwa na kitu kinachokwenda kwa kasi sana hewani, kama wakati tai anaposhukia mawindo yake kwa nguvu sana. Kwa hiyo, sauti hii yenye kelele ingeonyesha kutoweka kwa haraka kwa “mbingu” hizi za kiserikali. Kutoweka huku kwa mbingu za kiserikali hakutatokea kwa tendo la vyama vyenye mageuzi, vyenye mapinduzi miongoni mwa wanadamu, kwa maana wao wenyewe wangeweka serikali yao wenyewe badala ya ile inayopinduliwa. Badala yake, kule kutoweka kwa “mbingu” za kisiasa kutakuwa kwa tendo la Yehova Mungu. Kwa kuwa zimeishi kuzidi yale “majira ya Mataifa,” ingezifaa ziondolewe kwa haraka kama vile kwa tendo ambalo limekawia sana. Bila kujali itafanyiza mlio gani, ile “sauti yenye kelele” itasikiwa na wakaaji wa dunia.
6. Eleza “vitu vya asili” ni nini vitakavyoyeyuka, kulingana na 2 Petro 3:10.
6 Vile “vitu vya asili” (elements) ‘vitakavyopata moto sana’ kisha ‘viyeyuke’ si vile vinavyoitwa “four elements,” yaani, moto, maji, udongo na hewa. “Vitu vya asili” vinamaanisha sehemu za msingi zenye kufanyiza kitu fulani. “Vitu vya asili” vingeweza kuonyesha vitu fulani vilivyotengenezwa pamoja katika utaratibu fulani, kama herufi za alfabeti ya lugha. Vile “vitu vya asili” vinatajwa vikiwa tofauti na “mbingu” na “dunia,” vikiwa si sehemu za msingi za hivyo. Kati ya mbingu na dunia yetu halisi kuna hewa wanamoishi wanadamu, wakiivuta wapate kuendeleza uhai. Hewa hii ni yenye mchanganyiko wa mivuke na hivyo inazo sehemu za asili. Vilevile, kuna roho inayoenea makao ya kidunia ya wanadamu ambayo wanadamu wanavuta na inayowahuisha, ikiwaendesha kama kwa nguvu isiyoonekana ili watende, wafikiri, waseme na kupanga njia yao. Hii ndiyo roho ya ulimwengu. Haihusiani na roho ya Mungu lakini ina uadui naye. Kwa sababu hiyo, Mungu anapinga roho hiyo ya kilimwengu katika sehemu zake zote za asili. Yampasa aiyeyushe wakati wa siku Yake, yampasa aiharibu katika joto la hasira yake. Mafundisho yote, mipango na mashauri yanayoonyesha roho hii ya kilimwengu na kutokana nayo yapaswa yavunjwe, yabatilishwe, pamoja nayo.
7. (a) “Dunia” inayotajwa hapa maana yake nini? (b) Usemi huu “kazi zilizomo” wamaanisha nini?
7 Si “mbingu” na “vitu vya asili” peke yake vinavyoangaliwa na Mungu, bali pia “dunia na kazi zilizomo.” Hizi “zitavumbuliwa.” (2 Pet. 3:10, NW) Zitaonwa. Katika habari hii “dunia” yafananisha jamii ya kibinadamu iliyotengwa na tofauti na mabaki waliotiwa mafuta wa Waisraeli wa kiroho na “mkutano mkubwa” walio katika paradiso ya kiroho na wanaomwabudu Yehova katika hekalu lake la kiroho. (Ufu. 7:15) Usemi huu “kazi zilizomo” haumaanishi matendo ya mwenendo ya jamii ya kidunia ya kibinadamu, bali kazi zao za ujenzi, vitu ambavyo jamii ya kibinadamu inajenga na kufanyiza kwa namna ya majengo. “Kazi” hizo zaonyesha maoni ya kimwili, maelekeo ya kidunia, ya jamii hii ya kibinadamu, “dunia” hii ya mfano.
8, 9. (a) Ni katika maana gani dunia na kazi zilizomo ‘zinavumbuliwa,’ kama inavyosemwa katika 2 Petro 3:10, NW? (b) Wazo hilo lalingana namna gani na lile linalosemwa katika 1 Wakorintho 3:13-15?
8 Ni kwa sababu gani inasemekana kwamba “dunia na kazi zilizomo zitavumbuliwa [kwa halisi, zitaonwa]”? Kwa sababu gani “zitavumbuliwa,” “zitaonwa,” badala ya “zitateketea,” kama inavyosomwa katika tafsiri ya kale ya King James Authorized Version na Union Version ya Kiswahili katika 2 Petro 3:10? ‘Kuvumbuliwa’ au ‘kuonwa’ kwa kazi hizo hakumaanishi kwamba katika siku ya Yehova zitafunuliwa wazi zitazamwe tu na kuachwa hali zimefunuliwa hivyo. Katika 2 Petro 3:7, ZSB inasemekana kwamba, mbingu zilizo sasa, na dunia, zimewekwa akiba kwa moto kwa neno” la Mungu. Kwa hiyo, “dunia na kazi zilizomo” hazitaokoka ule “moto” wa uharibifu kama vile “mbingu” na “vitu vya asili” hazitaokoka. ‘Zitavumbuliwa’ au ‘kuonwa’ kwa njia ya moto. Ule moto utaiteketeza “dunia na kazi zilizomo” pia. ‘Zitavumbuliwa’ au ‘kuonwa’ kuwa zenye kuweza kuteketezwa kwa moto, kama vile “mbingu” za mfano na “vitu vya asili” vya mfano ni vitu vinavyoweza kuteketezwa kwa moto. Ule “moto” wenye kuharibu wa siku ya Yehova utajaribu hivyo. Basi maana ya kuvumbua au kuona ni kama ile katika 1 Wakorintho 3:13-15, ambamo mtume Paulo anaandika hivi:
9 “Siku ile itaidhihirisha, kwa kuwa yafunuliwa katika moto; na ule moto wenyewe utaijaribu kazi ya kila mtu, ni ya namna gani. Kazi ya mtu aliyoijenga juu yake ikikaa, atapata thawabu. Kazi ya mtu ikiteketea, atapata hasara. . . . ”
10. Basi ni kitu gani kinachotazamiwa kupata “dunia na kazi zilizomo” za mfano, na hili laonyeshwaje zaidi na maneno ya unabii ya Sefania?
10 ‘Siku ya Yehova ya hukumu na uharibifu wao wasioogopa Mungu’ itakuja kama mwivi juu ya “dunia [ya mfano] na kazi zilizomo,” na “moto” wa siku ile ya kufikilizwa hukumu ya kimungu utazijaribu zionekane kuwa zenye kuteketea na kuungua. Zitawaka moto. Hazitastahimili, kuiokoka ile siku yenye moto ya Bwana Mungu Yehova. Maneno ya unabii ya Sefania 1:14-18 yana maana kubwa kwa wakati wetu. “Hiyo siku ya [Yehova] iliyo kuu i karibu; i karibu, nayo inafanya haraka sana; naam, sauti ya siku ya [Yehova]; shujaa hulia. . . . Fedha yao wala dhahabu yao havitaweza kuwaokoa katika siku ile ya ghadhabu ya [Yehova]; bali nchi yote pia itateketezwa kwa moto wa wa wivu wake; maana atawakomesha watu wote wakaao katika nchi hii, naam, ukomo wa kutisha.”
‘KUHIMIZA KUWAPO KWA SIKU YA MUNGU’
11. Ni kutia moyo gani kwa mtume Petro kwa habari ya matazamio na mwenendo kunakotuhusu sisi leo kwa nguvu ya pekee?
11 Tofauti na wenye dhihaka waliotabiriwa kutokea wakati wetu, sisi tunajionyesha kuwa watu wa namna gani tunapokutana na uharibifu unaokaribia sana wa taratibu hii ya mambo isiyomwogopa Mungu? Kutia moyo kwa mtume Petro alikowapa Wakristo wa karne ya kwanza kunatuhusu sisi leo kwa nguvu kubwa zaidi: “Basi, kwa kuwa vitu hivi vyote [mbingu za mfano, vitu vya asili, dunia na kazi zilizomo] vitafumuliwa hivyo, imewapasa ninyi kuwa watu wa tabia gani katika mwenendo mtakatifu na utauwa, mkitazamia hata ije siku ile ya Mungu, na kuihimiza; ambayo katika hiyo mbingu zitafumuliwa zikiungua, na viumbe vya asili vitateketea na kuyeyuka? Lakini, kama ilivyo ahadi yake, tunatazamia mbingu mpya na nchi mpya, ambayo haki yakaa ndani yake.”—2 Pet. 3:11-13.
12. (a) Ikiwa kweli twaamini Neno la Mungu linavyosema, imetupasa tuishi namna gani? (b) Ni kutia moyo gani mtume Petro anatolea wale walioitwa kwenye uzima wa kimbinguni?
12 Inawapasa waamini wa kweli wa utimizo fulani wa neno la Mungu la unabii waishi kulingana na matazamio yao. Hawataishi kichoyo kwa ajili ya taratibu hii ya mambo, yaani, kwa ajili ya “mbingu” na “vitu vya asili” na “dunia” vitakavyoyeyushwa, kuharibiwa, kwa namna Neno la Mungu linavyosimulia. Sababu gani kuishi kwa ajili ya vitu ambavyo karibuni vitaharibika? Na kuharibiwa pamoja navyo? Hasa Wakristo walio wakf na kubatizwa, wameipata “imani moja na [mtume Petro], yenye thamani, katika haki ya Mungu wetu, na Mwokozi Yesu Kristo.” (2 Pet. 1:1) Mtume Petro anaendelea kuwaambia Wakristo hao walio na mwito wa ufalme wa kimbinguni: “Jitahidini zaidi kufanya imara kuitwa kwenu na uteule wenu; maana mkitenda hayo hamtajikwaa kamwe. Maana hivi mtaruzukiwa kwa ukarimu kuingia katika ufalme wa milele wa Bwana wetu, Mwokozi wetu Yesu Kristo.” (2 Pet. 1:10, 11) Mtume Petro anasema kwamba wao ni “wapitaji na wasafiri,” na, kwa sababu hiyo, wao si sehemu ya “mbingu,” “vitu vya asili,” na “dunia” za mfano ‘zitakazofumuliwa hivyo.’—1 Pet. 2:11.
13. (a) Kupatana na kutia moyo kwa Petro, Wakristo wa kweli wanaepuka kuwa watu wa namna gani na matendo gani? (b) Ili kuendelea kukaa katika paradiso ya kiroho, ni jambo gani la lazima?
13 Kwa hiyo, wale wanaotii kutia moyo kwa Petro hawana sehemu na wale “waalimu wa uongo” ‘wanaoingiza kwa werevu uzushi wa kupoteza’ na “wakimkana hata Bwana aliyewanunua, wakijiletea uharibifu usiokawia.” Wakristo wanaofuata sana unabii wa kweli hawafuati waalimu hawa wa uongo. Wakristo hao waaminifu hawamo miongoni mwa wengi ambao “watafuata ufisadi wao” na kwa sababu ya hao “njia ya kweli itatukanwa.” (2 Pet. 2:1, 2) Ili waepuke kufanya wenye kudhihaki na walimwengu wengine waitukane njia ya kweli ya Biblia, Wakristo wanaotii maneno ya Petro wanaangalia daima namna inavyowapasa wawe “katika mwenendo mtakatifu na utauwa.” Kwa mwendo huu wataepuka ‘kujiletea uharibifu usiokawia’ pamoja na “mbingu zilizo sasa, na dunia” na ambazo “zimewekwa akiba kwa moto.” (2 Pet. 3:7, ZSB) Mashahidi wa Kikristo wa Yehova leo wanakaa katika paradiso yao ya kiroho kwa “mwenendo mtakatifu na utauwa.”
14. (a) Je! kuna lo lote tuwezalo kufanya ili tuiharakishe “siku ya Yehova”? (b) Twawezaje kuonyesha kwamba ‘tunaikaribisha akilini’?
14 Hawajiruhusu wapatwe na dhihaka yo yote ya wale wanaokawiza katika akili zao kuja kwa siku ya Yehova ya hukumu kama mwivi. Wameingojea muda mrefu na, mpaka ifike, wataendelea kungojea “kuwapo kwa siku ya Yehova.” (NW) Bila kuwa kama wenye kudhihaki, wao ‘wanaihimiza’ siku ya Yehova. Hawaiondoi katika akili zao. Wanaikumbuka daima kama tukio lililo karibu sana. Kwa kadiri waishivyo duniani, ndivyo inavyokaribia zaidi. Hawawezi kuiharakisha, kuihimiza au kuikimbiza katika njia halisi, kwa maana wanajua kwamba Yehova ameweka mwenyewe tarehe ya kufika kwayo. Lakini wanaendelea kukesha ili, bila kujali kama itakuja upesi au kwa ghafula, wastahili kuingia ndani yake wakiwa katika hali inayokubaliwa na Yehova Mungu. Basi kuendelea kwao katika “mwenendo mtakatifu na utauwa” kwapatana na “kuihimiza” siku ya Yehova. Wanajua kuwapo kwa siku hiyo kunavyomaanisha. Nini?
KUZITOLEA “MBINGU MPYA NA NCHI MPYA” NAFASI
15. “Mbingu” zitakapoyeyuka, itakuwa na maana gani kwazo?
15 “Kuwapo kwa siku ya Yehova” ndiyo njia “ambayo katika hiyo mbingu kwa kuteketea zitayeyuka na vitu vya asili kwa kupata moto sana vitayeyuka!” (2 Pet. 3:12, NW) Zile “mbingu” za kiserikali, ambazo viongozi wa kidini wa ulimwengu wameshikamana nazo wapate msaada na ulinzi, zitateketezwa na Yehova Mungu. “Maana,” yasema Waebrania 12:29, “Mungu wetu ni moto ulao.” (Kum. 4:24) Huku kutamaanisha kuvunjwa, kuharibiwa, kwa “mbingu” hizo za kiserikali. Mtume Petro haelezi namna hili litakavyotukia kwa njia ya moto. Walakini, “yale maneno yaliyonenwa zamani na manabii watakatifu” yanasimulia namna hili litakavyokuwa.—2 Pet. 3:2; 1:21.
16. Ni kupitia kwa nabii gani aliyeongozwa na Mungu yalipewa maelezo juu ya namna “mbingu” hizo za mfano zitakavyoharibiwa kama kwa moto?
16 Katika ndoto ya unabii ya Nebukadreza, mfalme wa Babeli wakati wa siku za nabii Danieli, ulitolewa mfano wa “mbingu” hizo za mfano tangu tarehe ya mwaka wa 607 K.W.K., wakati Nebukadreza alipoharibu Yerusalemu na hekalu lake, mpaka wakati wa “kuwapo kwa siku ya Yehova.” Ile ndoto ya unabii ilitumwa na Yehova Mungu kwa mfalme wa Babeli, kwa maana mfalme aliisahau njozi ikawa nabii wa Yehova Danieli peke yake ndiye aliyeweza kumkumbusha mfalme ndoto hiyo kisha akamweleza.—Dan. 2:1-30.
17. Mfalme wa Babeli aliona nini katika ndoto yake, na kilifananisha nini?
17 Katika ndoto yake mfalme wa Babeli aliona mfano wa mfulizo (mfuatano) wa serikali za kisiasa za ulimwengu, tangu Serikali ya Ulimwengu ya Kibabeli ya nasaba ya kifalme ya Nebukadreza mpaka na kutia Serikali ya Ulimwengu ya Saba inayosemwa katika Biblia, yaani, Mamlaka ya Ulimwengu ya Waingereza na Waamerika ya karne yetu ya 20. Kwa hiyo, ile sanamu ya ndoto, iliyotumiwa kufananisha mfululizo wa mamlaka za ulimwengu za kiserikali, ilikuwa yenye mchanganyiko wa vitu vya asili. Kichwa kilikuwa cha dhahabu, kifua na mikono vilikuwa vya fedha, tumbo na viuno ni vya shaba, miguu ya chuma na nyayo na vidole vyake ni vya mchanganyiko wa chuma na udongo.—Dan. 2:31-33.
18. Eleza maana ya sehemu mbalimbali za ile sanamu ya ndoto.
18 “Hii ndiyo ile ndoto,” Danieli akamwambia Nebukadreza, “nasi tutaihubiri tafsiri yake mbele ya mfalme. Wewe, Ee mfalme, u mfalme wa wafalme [na kwa sababu hiyo ni mwenye milki juu ya mamlaka ya ulimwengu], na Mungu wa mbinguni amekupa ufalme, .. . naye amekumilikisha juu ya hao wote; wewe u kichwa kile cha dhahabu.” (Dan. 2:36-38) Kwa hiyo, kile kichwa cha dhahabu kilifananisha Mamlaka ya Ulimwengu ya Kibabeli katika nasaba ya kifalme ya Nebukadreza. Kifua na mikono vilifananisha Umedi na Uajemi, Mamlaka ya Ulimwengu iliyofuata. Lile tumbo la shaba na viuno vilifananisha Mamlaka ya Ulimwengu ya Ugiriki, Makedonia. Miguu ya chuma ilifananisha Mamlaka ya Ulimwengu ya Kirumi na chipukizi lake, Mamlaka ya Ulimwengu ya Mwungano wa Waingereza na Waamerika. Nyayo zikiwa nusu chuma na nusu udongo zilifananisha mamlaka za kiserikali za sasa au za mwisho ambazo nusu zimekuwa zenye mageuzi (za kisoshalisti; za kikomunisti) au nusu milki (za ubepari). Wakati wa zaidi ya kame 25 tangu Majira ya Mataifa yalipoanza wakati wa uharibifu wa Yerusalemu katika mwaka wa 607 K.W.K., serikali nyingine za kisiasa duniani zimetawalwa na mfuatano huo wa mamlaka za ulimwengu.—Dan. 2:39-43.
19, 20. Sanamu hiyo ya mamlaka za ulimwengu inaendelea kusimama mpaka kipindi gani cha historia, na inapatwa na nini wakati huo?
19 Kulingana na ndoto ya unabii ya mfalme, “sanamu” hiyo ya mamlaka ya ulimwengu yaendelea kusimama, katika utimizo wayo wa kihistoria, katika “mwisho wa taratibu ya mambo,” tunamoishi sisi. (Mt. 24:3; 28:20; 13:39, 49, NW) Huo “mwisho wa taratibu ya mambo” unafikishwa kwenye ukomo wake mkubwa na “kuwapo kwa siku ya Yehova,” ambayo katika hiyo zile “mbingu,” “vitu vya asili,” na “dunia na kazi zilizomo” za mfano zinaharibiwa kama kwa moto. Hiyo ndiyo “siku ya hukumu na uharibifu wao wasioogopa Mungu.” (2 Pet. 3:7-12, ZSB) Kwa hiyo, yenye kuogofya sana ni ile sehemu ya ndoto ya mfalme inayoonyesha mwendo na tendo na ambayo Danieli alimkumbusha mfalme kwa kusema:
20 “Nawe ukatazama hata jiwe likachongwa bila kazi ya mikono, nalo jiwe hilo likaipiga sanamu miguu yake, iliyokuwa ya chuma na udongo, likaivunja vipande vipande. Ndipo kile chuma, na ule udongo, na ile shaba, na ile fedha, na ile dhahabu, vilivunjwa vipande vipande pamoja, vikawa kama makapi ya viwanja vya kupepetea wakati wa hari; upepo ukavipeperusha, hata pasionekane mahali pake; na lile jiwe lililoipiga hiyo sanamu likawa [mlima] mkubwa, likaijaza dunia yote.”—Dan. 2:34, 35.
21. Hilo lamaanisha nini kwa tawala zote za kibinadamu?
21 Utimizo wa sehemu hii ya maana ya ndoto ya unabii uko wakati ujao ulio karibu sana. Kulingana na haya, kila salio au alama ya mamlaka za ulimwengu za kisiasa za historia ya kibinadamu, kutia na Mamlaka ya Ulimwengu ya Nane, yaani, Umoja wa Mataifa, lazima ziharibiwe kwa nguvu hata zisiweze kuundwa tena. Falme na tawala zote ndogo za kibinadamu lazima zifutiliwe mbali duniani vilevile.
22, 23. Ni kupitia kwa njia gani Yehova analeta uharibifu huo wa ulimwenguni pote?
22 Hilo ni neno la Mungu, si la mwanadamu. Si kazi ya mabaki ya Waisraeli wa kiroho waliotiwa mafuta, wala si kazi ya “mkutano mkubwa” wa waabudu wenzao wa Yehova. Njia ambayo Yehova Mungu Mwenye Nguvu Zote atatumia ili alete uharibifu huo wa ulimwenguni pote ilifananishwa katika ndoto ya Nebukadreza kama “jiwe” lililochongwa katika mlima bila msaada wa mikono ya kibinadamu. Kwa sababu hiyo, lile “jiwe” bila shaka lafananisha jambo fulani linalofanyizwa na Muumba, Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu. Yeye alimwongoza Danieli aeleze kilichofananishwa na lile “jiwe,” akisema:
23 “Na katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine [kama warithi] hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele. Na kama vile ulivyoona ya kuwa jiwe lilichongwa mlimani bila kazi ya mikono, na ya kuwa lilivunja-vunja kile chuma, na ile shaba, na ule udongo, na ile fedha, na ile dhahabu.”—Dan. 2:44, 45.
24, 25. (a) ‘Mlima’ ambao kutoka huo “jiwe” linachongwa bila mikono ya kibinadamu ni nini? (b) Lile “jiwe” lenyewe lafananisha nini, na ni nini linalotukia kwa habari zake sasa?
24 Kwa kuwa lile “jiwe” lafananisha ufalme ambao Mungu wa mbinguni anasimamisha, ule ‘mlima’ bila shaka wafananisha chanzo cha uwezo na mamlaka ya ufalme, yaani, Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote ya Mfalme wa Umilele, Yehova Mungu. Kwa njia hiyo ule mfalme ulio kama jiwe unakuwa sehemu na njia ndogo ya enzi kuu Yake ya ulimwengu wote. Ni ufalme wake wa Kimasihi kupitia kwa Mwana wake mzaliwa wa pekee, ambaye akawa Bwana Yesu Kristo. (Dan. 7:13, 14) Huu ndio ule ufalme ambao Yesu Kristo alisema habari zake katika unabii wake juu ya “mwisho wa taratibu ya mambo”: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mt. 24:14, NW) Katika unabii ule ule Yesu Kristo alitangulia kujiona mwenyewe akiwa katika ufalme huo, aliposema:
25 “Hapo atakapokuja Mwana wa Adamu katika utukufu wake, na malaika watakatifu wote pamoja naye, ndipo atakapoketi katika kiti cha utukufu wake; na mataifa yote watakusanyika mbele zake.”—Mt. 25:31, 32.
26. Ufalme huo wa Kimasihi umegawiwa na Yehova kufanya nini?
26 Nyote ushangilieni ufalme wa Kimasihi wa Mwana wa Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu! Ni serikali ya kimbinguni iliyopewa mamlaka ya kuziondoa “mbingu zilizo sasa, na dunia” na kuzileta “mbingu mpya na nchi mpya” kwa utukufu wa Mungu na kwa kubariki milele wanadamu wote wenye kutii.—Kutoka Kitabu Man’s Salvation Out of World Distress at Hand!, sura ya 16.
[Maelezo ya Chini]
a “Maneno haya yaeleza uhakika wa kuja kwa siku ya hukumu, na hos Kle’ptes [kama mwivi] na ghafula yake isiyotazamiwa; . . . tes tou Theou hemeras [ya siku ya Mungu], mst. wa 12 waonyesha kwamba kyriou [Bwana] hapa [mstari wa 10] pia ni sawa na Theou [ya Mungu], (si na Khristou [ya Kristo]; . . . ”—Mistari ya 3-6, fungu la 1, ukurasa wa 428, ya Critical and Exegetical Handbook to the General Epistles of James, Peter, John, and Jude, cha J. E. Huther (1887).