Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 8/1 kur. 356-360
  • Wazee wa Kundi—‘Simamieni Vizuri’!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wazee wa Kundi—‘Simamieni Vizuri’!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • NIA YA KUSIMAMIA MIKUTANO
  • KUSIMAMIA KWA UNYENYEKEVU
  • UNYENYEKEVU HUSAIDIA KUTATUA MATATIZO KATI YA WATU
  • Wazee Wanaosimamia Vema
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • “Mwatilie Maanani Wale Wanaofanya Kazi kwa Bidii Kati Yenu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • “Mwendelee Kuwachukua Watu wa Namna Hiyo Kuwa Wapendwa Wanaothaminika”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Uangalizi Wenye Upendo Hujenga
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 8/1 kur. 356-360

Wazee wa Kundi​—‘Simamieni Vizuri’!

“Acheni wanaume wazee wanaosimamia vizuri wahesabiwe kuwa wanastahili heshima maradufu.”​—1 Tim. 5:17, NW.

1. Kulingana na Mithali 11:14, kuna ubora gani wa kuwa na wazee wa kusimamia watu wa Mungu?

KWA kawaida watu husimamiwa na mtu fulani wanapoungana kutimiza kusudi au kazi fulani bora. Wanaposimamiwa vizuri, wanaweza kupewa uongozi unaofaa, kisha kuwe na maendeleo na mambo yatimizwe. Wasipopewa, watatatanishwa na kuanguka. Mithali 11:14 yasema hivi: “Pasipo mashauri taifa huanguka; bali kwa wingi wa washauri huja wokovu.” Mashahidi wa Yehova ni watu wenye mipango, wenye kusudi la kufanya mapenzi ya Mungu na kazi yake, nao wanashukuru kupokea uongozi na mashauri ya wazee waaminifu wanaowasimamia.

2. Ni maulizo gani yanayotokea juu ya anayesimamia kundi, nayo 1 Timotheo 5:17 yaelezaje jambo hilo wazi?

2 Sasa kuna makundi zaidi ya 40,000 ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Ingawa kila kundi lina “mwangalizi-msimamizi” aliyewekwa, je! yeye peke yake ndiye mwenye haki ya kusimamia? Namna gani wazee wengine wanaofanyiza baraza ya wanaume wazee? Wote wanapaswa kutambua agizo wanalopewa na Neno la Mungu katika 1 Timotheo 5:17, NW: “Acheni wanaume wazee wanaosimamia vizuri wahesabiwe kuwa wanastahili heshima maradufu, hasa wale wanaotia bidii katika kusema na kufundisha.” Ikiwa kundi lina wazee kadha waliowekwa, kila mmoja ana fungu la kusimamia utendaji mbalimbali wa kundi.

3. Mzee anayesimamia kundi anatofautianaje na baba anayesimamia jamaa yake?

3 Hata hivyo, ni katika maana gani wazee ‘wanasimamia vizuri’? Si kwa kutumia mamlaka ile ile ambayo mababa hutumia kusimamia jamaa zao. Nyakati nyingine vichwa vya jamaa hupaswa kukata maneno juu ya mambo mbalimbali yanayoongoza wake na watoto wao. Lakini, wazee mmoja mmoja hawana mamlaka hiyo. Yesu Kristo ndiye kichwa cha kundi. (Kol. 1:18) Anatajwa katika 1 Wakorintho 11:3 pia kama “kichwa cha kila mwanamume,” hali “kichwa cha mwanamke ni mwanamume.” Kwa hiyo pana tofauti ya kusimamia kundi la watu wa Mungu na kusimamia jamaa.

4. Kwa sababu ya madaraka ambayo wazee wamepewa na Maandiko, kwa nini inafaa ‘wasimamie’ kundi?

4 Neno la Kigiriki “simamia” halimaanishi kuwa mwenyekiti tu. Maana halisi ya ‘kusimamia’ ni “kusimama mbele ya,” kwa hiyo lamaanisha kuongoza, kuelekeza, kuagiza kuangalia wengine. Maelezo hayo yanafaa sana wazee ambao tunawaona ‘wakituongoza’ kwa kusimamia mikutano, kutufundisha na kutuagiza katika utumishi wetu (Ebr. 13:7, 17); kuchunga au kuangalia hali yetu ya kiroho (1 Pet. 5:2, 3); na kutulinda na cho chote kinachoweza kuhatirisha uhusiano wetu na kundi na Yehova Mungu hasa! (Yohana 10:11-15) Wanapofanya yote hayo wanajitahidi kufuata mashauri na mfano wa “Mchungaji mwema,” Yesu Kristo.

NIA YA KUSIMAMIA MIKUTANO

5. Maneno ya Paulo yenye kutia moyo yaliyomo katika Warumi 12:8 yanahusuje nia ya mzee ya kusimamia?

5 Kila mzee apaswa kusitawisha nia gani ili kutimiza vizuri daraka lake? Katika Warumi 12:8 Paulo atutia moyo akisema: ‘Mwenye kusimamia, asimamie kwa bidii,’ ili kufundisha, kuelimisha, kutia moyo au kusaidia ndugu zake. Mzee aonyesha anawafikiria ndugu kwa vile anavyotimiza wajibu wake, na yampasa ajiulize hivi: ‘Nawezaje kusimamia vizuri, kwa bidii?’

6. (a) Ili mwangalizi wa Shule ya Kitheokrasi aonyeshe anasimamia “kwa bidii” nyingi, yampasa afanye nini? (b) Wanafunzi mmoja mmoja wanapokea faida gani?

6 ‘Kuwa na bidii’ hakumaanishi kuwa mnyofu tu, bali pia kukaza nia kufanya jambo. Kwa mfano, anayeangalia Shule ya Kitheokrasi ajua kwamba hawezi kutimiza mgawo wake kama wajibu tu, bila kupendezwa nao. Lazima apendezwe na kila mwanafunzi, kumtimizia mahitaji yake hasa. Kwa sababu gani? Kwa sababu amtaka mwanafunzi afanye maendeleo. Wapya wengi wanashiriki sasa katika Shule na wanahitaji kusaidiwa kibinafsi. Wengine ni watu wa polepole au waoga; wengine hawana elimu wala uwezo wa kusoma vizuri, au wana matatizo mengine. Mwangalizi wa Shule ya Kitheokrasi akifanya kazi yake “kwa bidii” nyingi atawaona wanafunzi wakiitikia mashauri na uongozi na kufanya maendeleo. Maendeleo yao yataonekana watoapo maelezo mikutanoni na kuwa na utumishi bora wa shambani.

7. (a) Wakati mtu anapoongoza funzo la Mnara wa Mlinzi au funzo la kitabu la kundi, kusimamia kunahusu nini? (b) Mzee aelewapo yanayosemwa na Zaburi 25:4, 5 na Mithali 16:9, anasaidika awe na makusudi gani anapofundisha?

7 Wanaosimamia kama viongozi wa Mnara wa Mlinzi na mafunzo ya kundi ya kitabu wanapaswa wakumbuke kanuni izo hizo. Wao si viongozi wa kuuliza maulizo tu na kuomba wasikilizaji majibu. Ili kusimamia kwa njia yenye manufaa wanahitajiwa wafanye funzo liwe lenye kupendeza na kuchangamsha, kukazia maandiko makuu, kuhakikisha kwamba maandiko hayo yanatumiwa vizuri na kusaidia kila mtu aone thamani ya mambo ya maana yaliyozungumzwa. Ikiwa wengine wanasitasita kushiriki, huenda ikatosha kuwaendea kibinafsi na kuwatia moyo waanze kutoa maelezo mikutanoni. Wanaosimamia wanapaswa kujitahidi kuwa waalimu bora zaidi, wakiwa na lengo la kufikia mioyo, na kuwapa akina ndugu uongozi wa Maandiko watembee katika njia za Yehova.​—Zab. 25:4, 5; Mit. 16:9.

KUSIMAMIA KWA UNYENYEKEVU

8. (a) Yatupasa sote tujitahidi kufanya nini tunapositawisha unyenyekevu? (b) Unyenyekevu na “mazungumzo ya faragha” unasaidiaje wazee?

8 Mara tu baada ya kushauri wanaume wazee walichunge kundi, mtume Petro alitaja kidogo jambo ambalo sote twapaswa kujitahidi tulifanye. “Ninyi nyote jifungeni unyenyekevu, mpate kuhudumiana. . . . Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake.” (1 Pet. 5:5, 6) Unyenyekevu husaidia wazee hasa wanapozungumza pamoja na kushughulikiana. Kila mzee apaswa achunguze aone kama yeye hutoa maelezo yaliyo ya maana kweli kweli wakati mazungumzo yanapotokea. Wanaume wanaoombana maoni wanaheshimiwa na wenzao na kundi zima. Kunakuwa na matokeo mazuri wakipashana habari na kuwa na “mazungumzo ya faragha” kuhusu faida za kundi. Wazee wasipopashana habari waone jinsi mambo yanavyoendelea kutimizwa huenda mipango waliyofanya isifaulu. Hilo lakaziwa katika Mithali 15:22, NW: “Mipango huvurugika kusipokuwa na mazungumzo ya faragha, lakini katika umati wa washauri kuna utimizo wa mambo.” Unyenyekevu unafungulia wazee njia ya kukaribiana zaidi na kuwa na uhusiano mzuri zaidi na wote kundini.

9. (a) Yampasa mwangalizi-msimamizi apasheje wazee habari zinazohusu barua? Namna gani kundi? (b) Kunakuwa na matokeo gani mwangalizi-msimamizi akitimiza vizuri daraka hilo lake?

9 Hasa mwangalizi-msimamizi anayetumikia kama mwenyekiti lazima awe na maoni ya kiasi. Yampasa ahakikishe kwamba yanayoamuliwa na baraza ya wazee yanafuatwa. Wazee wasitiwe moyo wapashane habari katika mikutano yao tu. Yawapasa wawe na nia ya kupashana habari za karibuni zaidi kuhusu mambo yanayopata akina ndugu na kuhusu kazi kwa ujumla. Hiyo yahitaji mwangalizi-msimamizi ashughulike na barua zote zinazohusiana na afisi ya tawi, halmashauri za makusanyiko, waangalizi wanaosafiri au wazee wa makundi mengine. Baada ya kuzisoma, ahakikishe amepasha baraza nzima ya wazee habari hizo karibuni iwezekanavyo. Yampasa aeleze kundi kwa ukamili habari walizoandikiwa. Hapaswi kuwa mzembe katika mambo hayo. Haiwezekani yeye mwenyewe afanye kila jambo, kwa hiyo ataomba wengine wamsaidie ili mambo ya lazima yafanywe. Kila mzee ana kazi aliyogawiwa, lakini wote wanashirikiana pamoja. Ikiwa mambo makubwa yanahusika, mwangalizi-msimamizi hachukui hatua akiwa peke yake, bali anaomba wazee wengine maoni yao nyakati za mikutano yao au nyakati nyinginezo. (Mit. 18:1) Hiyo inafanya kuwe na utaratibu mzuri, na kufanya hali ya kiroho ya akina ndugu iangaliwe vizuri pamoja na kazi ya Ufalme kwa ujumla.

10. (a) Umoja wa kundi waweza kuharibiwaje, kama Paulo alivyoonya katika Wagalatia 5:15, 25, 26? (b) Kama inavyoonyeshwa katika Warumi sura ya 12, Wafilipi sura ya 2 na Waefeso sura ya 4, yawapasa wazee wawe waangalifu kusitawisha sifa gani?

10 Mara kwa mara, huenda kukawa na mtu fulani katika baraza ya wazee atakaye kujiinua juu ya wengine. Roho ya kushindana ikitokea, hiyo yaonyesha unyenyekevu umekosekana. Huenda mzee mmoja akajisikia maoni yake mwenyewe yanafaa sana ingawa baraza ya wazee imeamua hayastahili. Akijaribu kufanya wengine waunge mkono maoni hayo, inaelekea kwamba kundi halitakuwa na umoja. (Gal. 5:15, 25, 26) Ili kuepuka lo lote la maelekeo hayo, yampasa kila mzee ajichunguze daima, ajiangalie “asinie makuu kupita ilivyompasa kunia.” (Rum. 12:3, 10)Ili kusimamia vizuri yawapasa wazee wote ‘watie bidii,’ lakini yawapasa wajiangalie wafanye hivyo wakiwa na; kusudi jema na shauku nyingi ya kusaidia kundi kwa unyenyekevu wote.​—Flp. 2:5-8, 14-18; Efe. 4:1-3.

UNYENYEKEVU HUSAIDIA KUTATUA MATATIZO KATI YA WATU

11. (a) Eleza jinsi maoni yenye kutofautiana yanavyoweza kusaidia nyakati nyingine. (b) Yawapasa wazee wajisikie namna gani juu ya kutoa maoni katika mikutano yao, lakini wataepuka nini?

11 Ziko nyakati ambazo mambo hutokea kisha maoni tofauti-tofauti yanatolewa. Watu wametoka katika hali mbalimbali na wameona mambo mbalimbali, kwa hiyo ni kawaida kwamba watafikia maamuzi tofauti. Maoni ya watu tofauti yanaweza kumpa mtu msingi wa kuchunguza maoni yake mwenyewe aone kama yanafaa. Huenda mtu akaona kwamba amesema jambo la haki, lakini, kama Mithali 18:17 inavyotukumbusha, “jirani yake huja na kumchunguza,” kwa kutumia njia nzuri zaidi na sababu ya Maandiko. Bila shaka mpango huo unatakiwa katika mazungumzo ya wazee ili kutatua ulizo fulani au tatizo linalohusu hali ya kiroho ya ndugu zetu. Kwa hiyo si ajabu kwamba wazee wanaweza kuwa na maoni yanayotofautiana bila kuwa na makusudi mabaya, ikiwa hakuna kanuni ya wazi au uongozi unaopatikana. Yawapasa wawe na hiari ya kueleza mambo katika mikutano yao, lakini wafanye hivyo bila mzozo, “hasira wala majadiliano.”​—1 Tim. 2:8.

12. (a) Tunapoangalia masimulizi yaliyo katika Matendo sura ya 15, ni baadhi ya mambo gani tunayoweza kuchunguza na kujifunza? (b) Tatizo linaloelezwa katiba Matendo 15:1, 2 lilikuwa la namna gani na ukubwa gani?

12 Twaweza kujifunza sana ubora wa unyenyekevu na mambo yanayosaidia kutatua magomvi kwa kuangalia yaliyotukia katika mkutano mmoja wa mitume na wanaume wazee karne ya kwanza. Maandishi yanayohusu habari hiyo yapatikana katika Matendo sura ya 15. Antiokia ya Shamu ndiko Paulo na Barnaba “walikoombewa neema ya Mungu kwa ile kazi waliyokwisha kuitimiza.” (Matendo 14:26) Lakini waliporudi huko wakitoka safari yao ya kwanza ya umisionari, walipata tatizo: “Wakashuka watu waliotoka Uyahudi wakawafundisha wale ndugu ya kwamba, Msipotahiriwa kama desturi ya Musa hamwezi kuokoka. Basi baada ya Paulo na Barnaba kushindana na watu hawa na kuhojiana nao sana, ndugu wakaamuru kwamba Paulo na Barnaba na wengine miongoni mwao wapande kwenda Yerusalemu kwa mitume na wazee kwa habari ya swali hilo.” (Matendo 15:1, 2) Suala hilo kubwa lililohusu mafundisho lilisumbua sana akina ndugu. Ilikuwa lazima litatuliwe.

13. Katika Matendo 15:7, tutaelewaje matumizi ya maneno ‘‘mabishano mengi”?

13 Ilikuwa vizuri wazee wenye kuhusika wakapelekewa tatizo hilo Yerusalemu. Maandishi ya Biblia yatuambia yaliyotukia. Ingawa maoni yao yalitofautiana kwanza, mwishowe ‘walipatana kwa moyo mmoja.’ (Matendo 15:25) Lakini je! Matendo 15:7 (NW) haionyeshi kulikuwa na “mabishano mengi” katika mkutano huo? Neno la Kigiriki la ‘kubishana’ lahusiana na kitendo kinachomaanisha “kutafuta” (Kingdom Interlinear Translation); hivyo linaonyesha kwamba ili kupata kweli, au njia bora kabisa ya kufanya jambo, jitihada nyingi yahitajiwa ili kuchunguza jinsi jambo lilivyo​—kuuliza maulizo, kuzungumza na kufikia uamuzi unaofaa. Tukikumbuka wazo hilo tunaweza kupendezwa tunaposoma masimulizi hayo, kuangalia jinsi mambo yalivyotukia kwa uongozi wa roho takatifu.

14, 15. (a) Kwanza Petro, kisha Paulo na Barnaba, na mwishowe Yakobo, walisaidiaje baraza kuzungumza mambo hayo ya maana? (b) Ni mambo gani yaliyowasaidia ‘kupatana kwa moyo mmoja’ wakati huo?

14 Baada ya “mabishano mengi,” Petro alisimulia jinsi alivyotumiwa na Yehova kufungulia Mataifa njia ya kuzisikia habari njema. Aliuliza kama ilifaa kutwika waamini hao Mataifa mizigo, kwa maana fadhili zisizostahilika ambazo Mungu alionyesha kupitia kwa Yesu Kristo ndizo huwezesha kuwe na wokovu. Halafu, angalia jinsi walivyonyamaa kwa heshima katika mstari wa kumi na mbili, wakati Paulo na Barnaba walipokuwa wakiongeza ushuhuda wao. Mitume hao wenye kusafiri (“waliotumwa” kutoka kundi la Antiokia) walikuwa wamepokea ushuhuda wa baraka ya Mungu kupitia kwa “ishara na maajabu” walipokuwa wakihubiri kati ya mataifa. Ushuhuda huo uliunga mkono pendekezo la Petro juu ya jambo lililopaswa kufanywa.​—Matendo 15:7-12.

15 Halafu Yakobo akaomba wamsikilize. Alitumia maneno ya manabii, kama yale yaliyo katika Amosi 9:11, 12, yakapatana na masimulizi ya Petro na kuhakikisha mambo ambayo roho ya Mungu ilikuwa imetimiza kupitia kwa Paulo na Barnaba. Hivyo uamuzi wa Yakobo uliungwa mkono na Maandiko na roho ya Mungu. Alitumia sababu hiyo thabiti kupendekeza wawaandikie waamini mataifa waliokuwa wakimgeukia Mungu, kuwaeleza wazi matakwa ya Mungu. Ilikuwa lazima mitume na wanaume wazee wafikie mapatano kwa moyo mmoja. Ubishi ulimalizwa kwa unyenyekevu kamili.​—Matendo 15:13-29.

16. Ingawa huenda mtu akabaki na maoni tofauti juu ya jambo fulani, ni roho gani inayopaswa kudumu kati ya wazee na kundi?

16 Ikiwa baraza ya wazee haiwezi ‘kupatana kwa moyo mmoja,’ mtu mwenye maoni tofauti asikatae mambo ambayo yameamuliwa kwa kuonyesha roho ya kuweka kinyongo moyoni. Itampasa aendelee ‘kutia bidii’ pamoja na baraza nzima. Hivyo kundi litazidi kuwatumaini, likijua kwamba wote wanafanya kazi kwa umoja. Wazee wakitembea “kwa unyenyekevu wote” watatia nguvu kifungo cha amani.​—Efe. 4:2, 3.

17. Yawapasa wanaume vijana na wazee wenye umri mkubwa wakumbuke shauri gani zuri kunapokuwa na mkutano wa wazee, na kwa sababu gani?

17 Wazee wakutanapo pamoja yawapasa walio vijana hasa wawasikilize kwa makini wazee wenye umri mkubwa na wenye ujuzi zaidi katika maisha ya Kikristo, wakitambua yanayosemwa na Mithali 16:31: “Kichwa chenye mvi ni taji ya utukufu, kama kikionekana katika njia ya haki.” Kwa upande mwingine, yawapasa wanaume wazee watambue kwamba kijana huenda akawa na maoni sahihi juu ya jambo fulani. Kwa hiyo kinachofanya maoni ya msemaji yastahili ni hekima nzuri inayopatikana katika anayosema, si kwa sababu ya umri wake nyakati zote. Hata hivyo, wakati vijana wanapotoa maoni yao, yawapasa waheshimu wazee, kama ambavyo Timotheo alimheshimu Paulo na mashauri yake, na kama vile Elihu alivyoungojea wakati uliomfaa kusema, kwa sababu ya kuheshimu wazee.​—1 Tim. 5:1,19; Ayubu 32:6-9.

18. Ingawa mitume waliangalia ‘mambo ya lazima,’ kama inavyoonyeshwa katika Matendo 6:1-6, ni jambo gani lililokaziwa zaidi?

18 Ingawa wazee wanaweza kutumia wakati mwingi katika mikutano fulani washughulike na matatizo yanayohusu Jumba la Ufalme au ‘mambo mengine ya lazima,’ yawapasa watangulize mambo ya maana zaidi yanayohusu hali ya kiroho ya kundi. (Matendo 6:1-6; Flp. 1:9, 10) Wakifanya hivyo watasimamia vizuri.

19. (a) Tofauti na vile watawala wa kilimwengu wanavyoshughulika na watu, mpango ulio kati yetu ukoje, kupatana na shauri la Yesu na la Paulo? (b) Kuna faida gani za kuwa na wazee wanaosimamia vizuri?

19 Tunapotazama mvurugo wenye kuhuzunisha katika ulimwengu huu, tunashukuru sana wazee wanaosimamia vizuri katika kundi la Yehova duniani pote! Wanadamu wanapapasa-papasa wakitafuta njia ya kutoka katika matatizo yao, maana watawala wao ‘wanapiga ubwana juu yao badala ya kuwaongoza kwa upendo, kuwasaidia, na kuwaburudisha. (Mt. 20:25-27) Kati yetu tuna wanaume waliokomaa kiroho wanaowekea kundi mfano mwema, nasi tunawaheshimu wanapotusimamia. (1 The. 5:12, 13) Si mtu mmoja katika kundi, mji, nchi wala sehemu ya ulimwengu anayefanya hivyo, bali wazee wote walio katika eneo walilogawiwa wana daraka la kusimamia. Kwa sababu ya msaada na uongozi wenye upendo wa umati huo wa washauri, kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi inasonga mbele ikamalizike ikiwa na matokeo mazuri. Kundi limeungana katika jitihada zake likiwa chini ya wazee wanaosimamia vizuri. Hivyo tunapatanishwa vizuri zaidi na ukichwa wa Yesu Kristo, na kumletea Yehova utukufu.

​—Kutoka The Watchtower, March 1,1977.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki