Utii Una Ubora Gani?
MCHEZAJI wa namna fulani ya mpira alikuwa mwenye ujuzi mwingi sana. Angeweza kutumia kijiti chake cha kupigia mpira kama alivyopenda, isipokuwa akionyeshwa afanye vingine na msimamizi wake. Lakini yeye aliona huo ulikuwa mchezo wa maana sana, tena alikuwa na hakika kwamba angeweza kufanya uamuzi bora kuliko msimamizi wake. Kwa hiyo, ingawa aliagizwa asukume mpira polepole tu, yeye aliinua kijiti chake akaupiga mpira kwa nguvu nyingi, upande wao ukashinda mchezo huo. Wapenda-mchezo walimshangilia kwamba yeye ni bingwa, lakini akatozwa faini ya dola 100 (kama shilingi 816 au 50Z) kwa sababu ya kutomtii msimamizi wake. Alijifunza kwamba utii ni bora kuliko kushinda mchezo.
Jambo hilo lilitukia miaka mingi iliyopita, na tangu wakati huo wachezaji wengine wametozwa faini kwa sababu izo hizo. Lakini huenda mtu akauliza, Ilikuwa haki kuadhibu mchezaji kwa sababu ya kushinda mchezo? Hapana, yeye hakuadhibiwa kwa sababu ya kushinda mchezo bali kwa sababu ya kutenda kinyume cha maagizo. Mchezo huo wa mpira ungekuwaje kila mchezaji akifanya apendavyo? Mapatano yangetoka wapi? Tena, ingawa katika kisa hicho kimoja uamuzi wa mtu huyo aliyepiga mpira unaweza kuwa ulikuwa bora, je! ndivyo inavyokuwa nyakati zote? Zaidi ya hilo, nani ajuaye kama wasingalishinda mchezo kama mchezaji huyo angalitii? Watu wengine wanaandikwa kazi na kulipwa kwa sababu ya kutoa maagizo, maana hiyo ndiyo kazi wanayojua zaidi; wengine wanalipwa kwa sababu ya kukubaliana nao. Kwa kawaida mtu anapokubaliana na mwenzake anamtii, lakini mchezaji huyo wa mpira hakutii.
Watu wengi wanachukia kusikia neno “-tii” likitajwa. Mabibi-arusi wengine wa kisasa wanakataa neno “-tii” lisitumiwe katika nadhiri zao za ndoa. Watu wengi sana wanataka uhuru wa kufanya wapendavyo. Lakini bila utii hatuwezi kuanza kuishi wala kuendelea kuishi. Kwa sababu gani? Kwa sababu ili kuendelea kuishi lazima sote tutii sheria za uumbaji, kama nguvu za uvutano, sheria inayosema kila tokeo lina chanzo, inayohusu mabadiliko ya chakula katika miili yetu, na kadhalika.
Hatufaidiki kwa kutii sheria za uumbaji tu, bali pia sheria ambazo wanadamu wametunga ili watu wawe na utaratibu mzuri. Watu wanaopenda fujo wangependa kuondolea mbali sheria zote; lakini jambo hilo lingeleta mvurugo na hatari nyingi! Chukua mfano mdogo wa taa zinazoongoza magari katika barabara zinazopitana. Taa hizo zisipokuwako, nao waendesha magari wasipozitii, magari huenda yakavurugika sana yafikapo hapo na huenda watu wengi wakafa. Bila shaka kuna ubora wa kutii sheria za barabarani!
Au wafikirie watu walio katika tarabu. Huenda kiongozi akawa ni hodari sana, lakini ujuzi wake ungekuwa na faida gani watu wake wasipomtii? Wanamuziki wanajua sana ubora wa kutii, kwa maana kazi zao zinategemea kabisa kumtii kiongozi, maandishi ya muziki na mwanamuziki wa kwanza katika upande wao! Je utii una ubora kwao? Bila shaka!
Tunaweza kutoa mifano zaidi, lakini iliyotolewa inatosha kukazia ubora wa utii katika mambo ya maisha ya kila siku. Basi, ni vizuri kwamba Mungu anakazia ubora wa utii katika mambo ya kiroho katika Neno lake, Biblia Takatifu, alilotupa liwe ‘taa ya miguu yetu, na mwanga wa njia yetu.’ (Zab. 119:105) Neno “tii” linapatikana katika Biblia zaidi ya mara 160 likiwa katika namna zake mbalimbali, na mara nyingi sana tunaona amri za Yehova Mungu, sheria zake, maagizo yake, hukumu zake na kanuni zake zikitajwa, na hizo zote zinapaswa kutiiwa na wanaompenda. Sura za mwanzo kabisa za kitabu cha kwanza cha Biblia zinatuambia kwamba taabu zote zilizomo ulimwenguni zilianza kwa sababu wazazi wetu wa kwanza hawakumtii Mungu.—Mwa. 2:17; 3:11-19.
Ili kuwe na utaratibu mzuri, mapatano na kutimiza mambo, lazima watu wakubaliane, nao utii wa kadiri fulani unahitajiwa ili kukubaliana. Lakini ni nani anayepaswa kuamua atakayetoa amri na atakayetii? Kwa kuwa Mungu ndiye aliyeiumba dunia na mwanadamu aliye juu yake, na vyote ni mali yake, je’ hana haki ya kudai mwanadamu amtii? Kwa kuwa ndivyo ilivyo, yeye ana haki ya kuwapa watu fulani haki ya kutoa amri na kuwahitaji wengine wawatii. Naye Mungu anafanya hayo kwa hekima na upendo, si kwa kushikilia sana sheria.
Neno la Mungu linaamuru hivi: “Ninyi watoto, watiini wazazi wenu katika mambo yote; maana jambo hili lapendeza katika Bwana.” (Kol. 3:20) Je! hiyo ni amri yenye upendo na hekima? Ndiyo, kwa maana, zaidi ya wazazi kuwa na madaraka kwa sababu ndio walioleta watoto ulimwenguni, wana ujuzi mwingi zaidi na wajibu wa kuwapa watoto wao chakula, mavazi, mahali pa kukaa, elimu, mazoezi, mafundisho ya kidini na tafrija. Wanawezaje kutimiza wajibu huo vizuri watoto wao wasipokubaliana nao kwa kuwatii? Hata kiongozi hawezi kutokeza muziki mzuri watu wake wasipokubaliana naye kwa kumtii!
Ziko pande nyingine za mambo ya kibinadamu ambazo Mungu anataka watu wamtii. Kwa mfano, utii unahitajiwa katika uhusiano wa ndoa ili kuwe na amani, mapatano na furaha katika jamaa (Efe. 5:21-23), kati ya uhusiano wa raia na serikali zao ili kuwe na haki (Rum. 13:1-7), kati ya watumishi au wafanya kazi na matajiri wao ili kazi ifanywe (Efe. 6:5-8), na unahitajiwa kati ya washiriki mmoja mmoja wa kundi na waangalizi au wazee wao ili wafaidiane. (Ebr. 13:17) Bila shaka, utii wote huo ni wa kiasi, yaani unaoonyeshwa maadamu haupingi amri za Mungu.—Matendo 5:29.
Kuna kisa kimoja katika Biblia kinachoonyesha kwamba ni jambo la maana sana watu wa Mungu walio wakf wamtii. Mtawala wa kwanza wa Israeli, Mfalme Sauli, alikuwa ameamriwa na Yehova Mungu aliadhibu taifa la Waamaleki kwa sababu waliwashambulia Waisraeli sababu waliwashambulia Waisraeli walipokuwa jangwani. Sauli hakutii maagizo ya Mungu, hakumharibu mfalme wa Waamaleki wala mifugo yao, akatoa kisababu kwamba aliiachilia mifugo kwa kusudi la kuitoa kama dhabihu. Lakini nabii Samweli alimwambia: “Kutii ni bora kuliko dhabihu, na kusikia kuliko mafuta ya beberu. . . . Kwa kuwa umelikataa neno la [Yehova], yeye naye amekukataa wewe usiwe mfalme.”—1 Sam. 15:22, 23.
Utii una ubora gani? Una ubora mwingi sana, sana!
[Picha katika ukurasa wa 521]
Nabii Samweli alimwambia Mfalme Sauli asiyetii, “Kutii ni bora kuliko dhabihu”