Ndoa Ni Mpango Unaoheshimiwa Katika Neno la Mungu
“Ndoa na iheshimiwe na watu wote.”—Ebr. 13:4.
1. Adamu alijisikiaje alipomwona mwenzi wake wa ndoa mara ya kwanza, na kwa sababu gani ndoa yao ingaliweza kuwa na furaha daima?
NDOA ya mwanamume na mwanamke yapaswa iwe wakati wenye kufurahisha sana. Ndivyo ilivyokuwa kwa wanadamu wawili wa kwanza. Baada ya Adamu kungojea muda fulani, alipomwona mwanamke ambaye angekuwa mwenzi wake wa ndoa, alipaza sauti kwa usemi wa mashairi akasema: “Sasa huyu ni mfupa katika mifupa yangu, na nyama katika nyama yangu.” (Mwa. 2:23) Maisha yao yote ya ndoa yangaliweza kuwa yenye furaha isiyokwisha, kwa maana Muumba wao alikuwa amewafanyia mipango yote waliyohitaji ili kuwa na maisha ya namna hiyo.
2. (a) Je! ndoa inaweza kuleta furaha katika hali za kutokamilika? (Mit. 5:18) (b) Yeremia 7:34 na Isaya 62:1, 5 yaonyesha ndoa kuwa yenye hali gani?
2 Jitihada nyingi zikifanywa kutumia kanuni za Biblia, hata sasa ndoa yaweza kufurahisha sana katika hali za kutokamilika zilizotokea wanadamu wawili wa kwanza walipokataa utawala mkuu wa Mungu. Maandiko ya Kiebrania na ya Kigiriki yanataja mara nyingi kwamba arusi zilifurahisha watumishi wa Mungu. (Mwa. 24:67; Wimbo Ulio Bora 3:11; Yohana 3:29) Alipokuwa akitabiri uharibifu uliokaribia kuupata Yerusalemu usio mwaminifu, Yehova alisema: “Ndipo katika miji ya Yuda, na katika njia kuu za Yerusalemu, nitaikomesha sauti ya kicheko na sauti ya furaha, sauti ya bwana arusi na sauti ya bibi arusi; kwa maana nchi hiyo itakuwa ukiwa.” (Yer. 7:34) Naam, kutokuwapo kwa arusi kungekuwa mfano wa kutokuwa na furaha na shangwe kwa sababu ya ukiwa. Lakini, wakati nabii wa Yehova alipokuwa akitaja habari za kurudishwa kwa Waisraeli kutoka uhamishoni, alisema juu ya Yerusalemu kwamba, “kama vile bwana arusi amfurahiavyo bibi arusi, ndivyo Mungu wako atakavyokufurahia wewe.”—Isa. 62:1, 5.
MPANGO UNAOPASWA KUHESHIMIWA SANA
3. (a) Kwa sababu gani malazi ya ndoa yapaswa kuwekwa katika hali safi? (b) Maandiko yanaruhusu talaka kwa sababu gani ya pekee?
3 Kwa sababu mpango huo ulianzwa na Mungu na kubarikiwa naye, ni vyepesi kufahamu sababu gani mtume aliyeongozwa na Mungu aliwatia Waebrania moyo akisema: “Ndoa na iheshimiwe na watu wote, na malazi yawe safi; kwa maana waasherati na wazinzi Mungu atawahukumia adabu.” (Ebr. 13:4) Kuna sababu thabiti ya kutochafua malazi. Baada ya Yesu kueleza kwamba mwanamume na mwanamke waliumbwa na Mungu, alitaja kwamba Mungu alisema: “Kwa sababu hiyo, mtu atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; na hao wawili watakuwa mwili mmoja.” Hivyo alionyesha kwamba maneno yaliyoandikwa katika Mwanzo 2:24 hayakusemwa ‘ na Adamu, bali na Yehova Mungu. Yesu aliendelea kusema kwamba, kwa sababu ya umoja huo, “aliowaunganisha Mungu mwanadamu asiwatenganishe.” Alisema kwamba sababu ya pekee ambayo Mungu anaruhusu talaka ni “uasherati” (Kigiriki, por·neiʹa, maana yake mwenendo mpotovu unaohusu viungo vya uzazi unaofanywa pamoja na mtu mwingine au hata mnyama).—Mt. 19:3-9.
4. Yehova Mungu awaonaje watu wasioona ubora wa kudumisha ndoa?
4 Kwa hiyo, Yehova Mungu anachukua kwa uzito hali inayoonyeshwa na viumbe vyake juu ya mpango huo wa kimungu wa ndoa. Wapaswa kuwa mwungano wenye kudumu, wa maisha yote, wenye kuvunjwa na kifo tu cha mmoja wa wenzi. (Rum. 7:2, 3) Mungu alipokuwa akionya watumishi wake katika Israeli wasiudharau mwungano huo, alisema: “[Yehova] amekuwa shahidi kati ya wewe na mke wa ujana wako, uliyemtenda mambo ya hiana. angawa yeye ni mwenzako, na mke wa agano lako. . . . Jihadharini roho zenu; mtu awaye yote asimtende mke wa ujana wake mambo ya hiana. Maana mimi nakuchukia kuachana, asema [Yehova], Mungu wa Israeli.” (Mal. 2:14-16) Naam, “waasherati na wazinzi Mungu atawahukumia adhabu,” hata wale wanaokimbilia talaka zisizo haki watimize makusudi ya kichoyo. Kwa hiyo wenye kuoana wanapaswa kujua wanachukua daraka zito sana. Muumba wa ndoa atazamia watumishi wake waiheshimu na kusaidia wengine waiheshimu pia.
5. (a) Yampasa mume Mkristo amtendeeje mkewe? (b) Mume anakuwa na uhusiano wa namna gani na Yehova Mungu anapokosa kumtendea mke wake vizuri?
5 Yehova Mungu aeleza kwamba mke wa mwanamume ni ‘mwenzake’ katika agano la ndoa. Waume Wakristo hawawezi kuheshimu mpango wa ndoa bila kuheshimu wenzi wao wa ndoa. Kama vile mtume Petro anavyoshauri, yawapasa ‘kuwapa heshima, kama chombo kisicho na nguvu; na kama warithi pamoja wa neema ya uzima, kusudi kuomba kwao kusizuiliwe.’ (1 Pet. 3:7) Mume Mkristo hataheshimu mkewe kwa kumfanyia mambo ya huruma tu, bali atamheshimu hasa kwa kulinda mwungano wao wa ndoa. Sikuzote yampasa ajaribu kuuchukua kama daraka takatifu. Ikiwa kushindwa kuonyesha mkewe upole na huruma inayomstahili kwaweza kuzuia sala zake, zitazuiwa zaidi sana akikosa kushikamana naye, akipendezwa na mtu fulani aliye nje ya mwungano wa ndoa. (Mit. 5:15-21) Kutomheshimu mke wake ni kutoheshimu mpango wa ndoa pamoja na Yeye aliyeuanzisha. Lakini mume mwenye kuheshimu mpango huo atampenda mkewe kama mwili wake mwenyewe, akiwa mwenye nia hata ya kumfia.—Efe. 5:25, 28-33.
6. (a) Neno la Mungu lamtaka mke Mkristo afanye nini? (b) Mke anayefuata mashauri ya Biblia anapata baraka gani?
6 Hivyo ndivyo mke Mkristo atakavyofanya pia. Aonyesha amtii mumewe, aliye kichwa chake, kwa njia ile ile ambayo kundi la Kikristo ‘lamtii Kristo.’ Hampi mumewe heshima ya kijuu-juu tu, bali ‘anamstahi.’ (Efe. 5:22-24, 33) Ikiwa staha hiyo inamzuia asinenee mumewe kwa dharau, yampasa zaidi sana aepuke kupendezwa na mtu mwingine asiye katika mwungano wa ndoa, asicheze-cheze na wanaume wengine kwa njia ya ubembelezi. Hawezi kumheshimu Mungu kwa kumdharau mumewe au uhusiano wao wa ndoa. (Mit. 2:16, 17) Lakini ‘akipenda mumewe na watoto wake, akiwa safi na kufanya kazi nyumbani,’ kuonyesha “roho ya upole na utulivu,” atakuwa kama madini yenye thamani nyingi, na kumletea Yehova Mungu sifa. Hataacha kupendwa na mumewe, tena atamfanya aheshimiwe sana na wanaume wenzake.—Mit. 31:10-12, 23, 26-31; Tito 2:4, 5; 1 Pet. 3:1-4.
KUHALALISHA NDOA NYAKATI ZA BIBLIA
7. Maandiko yaonyesha ilihakikishwaje kwamba watu walikuwa wameoana?
7 Nyakati za Biblia, ilihakikishwaje kwamba watu walikuwa wameoana? Ndoa ilishughulikiwa na jamaa au kabila. Serikali za kilimwengu hazikujiingiza katika mpango huo, wala hazikuhalalisha ndoa. Lakini, yalikuwako masharti fulani. Kwa kawaida mapatano ya ndoa yalifanywa na vichwa vya jamaa. (Mwa. 34:4, 6, 8-10) Ilikuwa lazima mchumbiaji apate kibali ya baba ya msichana, kama Yakobo alivyofanya alipopendana na Raheli. (Mwa. 29:18-20) Msichana angeweza kuulizwa kama alitaka kuolewa, kama wakati Rebeka alipoombwa awe mke wa Isaka. (Mwa. 24:8, 58) Desturi ilikuwa kumlipa baba mahari, ambaye sasa angeacha kutumikiwa na binti yake.—Mwa. 34:11, 12; Kut. 22:16, 17.
8. Hapo kale, hadhara ya watu ilijulishwaje kwamba mwanamume na mwanamke walikuwa wakiingia katika agano la ndoa?
8 Kama ilivyokuwa Edeni, wakati wa arusi hakukuwa na sherehe ya pekee wala mahubiri ya kuitukuza, lakini bwana arusi alikuwa akienda nyumbani kwa bibi arusi na kumsindikiza barabarani mpaka nyumbani kwake. Kwa kufanya hivyo alitangazia hadhara ya watu kwamba alikuwa akimchukua awe mkewe. (Mat. 2:20, 24) Inaelekea bibi arusi alijitayarisha kwa njia ya pekee, akaoga na kutumia mafuta yenye manukato, na labda akajifunga matiti na kuvaa vazi refu jeupe na mapambo fulani au johari. (Zab. 45:13-15; Isa. 49:18; 61:10; Yer. 2:32) Mara nyingi watu wenye kutaka kuona waliooana karibuni walijipanga kando kando ya barabara, hasa wanawali wenye kupendezwa na arusi na kuifurahia. (Yer. 7:34; Mt. 25:1-6) Baada ya bwana arusi kufika nyumbani kwake kungeweza kuwa na karamu yenye wageni wengi wenye kufurahia arusi, nao pia walivaa mavazi ya pekee kwa ajili ya wakati huo.—Mwa. 29:22; Mt. 22:2, 3, 11; 25:10.
9. Sababu kubwa zaidi ya kuwa waaminifu kwa agano la ndoa ni nini, na kwa nini?
9 Kwa njia hizo bwana arusi na bibi arusi walijulisha watu waziwazi kwamba walikuwa wameingia katika agano la ndoa wakakubali kuchukua daraka lililotokana na ndoa hiyo. Baadaye inaelekea kwamba kumbukumbu za ndoa ziliandikwa na kuwekwa. Lakini jambo la maana zaidi kuliko kuwa na wanadamu wengine wa kushuhudia mwungano wao ni kwamba, wenye kuoana walijua kwamba Yehova Mungu alifahamu walikubaliana wakaungana. Jambo hilo hasa ndilo lapaswa kuwaongoza waendelee kushikamana. Lapaswa liwafanye wajitahidi kuzuia ndoa yao isiwe na unajisi, na vilevile waheshimu sana ndoa za watu wengine wote.—Linganisha Mwanzo 20:1-7; 39:7-9; Ayubu 31:9-12; Mithali 6:23-35.
NDOA YATUMIWA KWA HESHIMA KUFANANISHA MIPANGO YA KIMUNGU
10, 11. Maposo na ndoa nyakati za kale’ yafananishaje uhusiano wa Yesu Kristo na washirika wenzake katika Ufalme?
10 Mambo yote hayo ya ndoa yanatumiwa vizuri katika Neno la Mungu kufananisha mwungano ulioanzwa kati ya Mwana wa Mungu na wale wanaokuwa washirika wenzake katika Ufalme. (Ufu. 21:2, 9, 10) Biblia yaonyesha kwamba Baba, Yehova Mungu, ndiye anayechagulia Mwanawe jamii hiyo ya “bibi arusi,” inayofanyizwa na wafuasi wa Yesu waliotiwa mafuta, na kwamba wananunuliwa kwa bei kubwa sana, yaani, uhai wa Mwana huyo huyo anayekuwa mume wao wa kiroho, ambaye aliwapenda sana hata akawafia. (Yohana 13:1; Efe. 5:25-27) Wanaonyesha wana nia ya ‘kumfuata Mwana-Kondoo kila aendako,’ kama Rebeka alivyokubali alipoulizwa kama alitaka kuolewa. (Ufu. 14:1, 4) Wanapokuwa duniani wanajichukua kuwa wameposwa na kujitahidi kujiweka katika hali ya “bikira safi,” wasitiwe madoa na ulimwengu wala wasishikamane na mtu mwingine. (2Kor. 11:2) Wanaendelea kushikamana na Kristo Yesu hata wanapopatwa na majaribu yaliyo makali zaidi na vishawishi vikubwa zaidi. Wanajivika utu mpya unaoonyesha wameiga sifa nzuri za Bwana arusi wao wa mbinguni, tena, kwa kuwa na matendo yenye haki wanaendelea kuwa na kitambulisho safi, kilicho kama vazi jeupe safi.—Kol. 3:9, 10, 12-14; Ufu. 19:7, 8.
11 Katika wakati wake, bwana arusi ambaye sasa ni Mfalme mbinguni, atakuja kuwachukua awapeleke mbinguni, kuwe na karamu yenye shangwe. (Yohana 14:2, 3; Ufu. 19:9) Kwa kuanza Ukumbusho wa kifo chake, ni kama kwamba ameambia jamii ya bibi arusi wake hivi: ‘Msinisahau kamwe wala msiache kunipenda. Kumbukeni kwamba, mimi niliwafia.’ (1 Kor. 11:25, 26) Watakapoungana na Mwana wa Mungu mwishowe, watafurahi kuwa wenzi wake, washiriki kwa utii katika pendeleo la kutawala na kufaidi wanadamu watakaokuwa watoto wa Mfalme.—Ufu. 5:9, 10; 20:4, 5; linganisha Isaya 9:6, 7.
12. Kwa sababu gani uhusiano wa Yesu Kristo na wafuasi wake waliotiwa mafuta wapaswa uchochee sana wanadamu waendelee kuwa na ndoa zenye kuheshimika?
12 Hivyo Mungu ameona inafaa afananishe mambo yaliyo ya maana sana kwetu na mipango hiyo ya ndoa. Hiyo ni sababu nyingine kubwa inayotupasisha kuheshimu ndoa. Kushindwa kufanya hivyo kunavunja heshima ya uhusiano wa Kristo Yesu na wafuasi wake waliotiwa mafuta, na vile-vile ya baraka ambazo mwungano wao wenye faida utaletea wanadamu wote kwa ujumla.
HATUTIWI MOYO TUTALIKIANE
13. (a) Je! wakati wo wote sheria za Yehova zinatia watu moyo watalikiane? (b) Twaweza kujifunza nini juu ya ndoa kutokana na matendo ya Yehova na Waisraeli wa kale?
13 Ni kweli kwamba sheria za Yehova zaruhusu watu wawe na talaka. Lakini, Mungu aonyesha kwamba hakuna mahali anapotutia moyo tuchukue hatua hiyo, bali anatuhimiza tujitahidi sana kudumisha ndoa. Yehova alitumia ndoa kwa njia ya mfano tena kuonyesha alikuwa amelioa taifa la Israeli kupitia kwa agano lake nao. (Yer. 31:31, 32) Aliwakomboa utumwani Misri. (Kum. 9:26) Yehova alishikamana sikuzote na uhusiano wake na Israeli, wala hakuanza kupenda mataifa mengine wala hakuhusiana nao. Hata Israeli mke wake alipokuwa mwasi, Yehova hakufanya haraka ya kumtupilia mbali. Alionyesha uvumilivu na ustahimilivu wa ajabu kwa sababu ya upendo. Yehova alilitaliki taifa hilo lililokuwa limekuwa kama mke mzinzi baada ya kujitahidi karne nyingi kuhifadhi mwungano wao.—Isa. 50:1; Yer. 3:8.
14. Waliooana wapaswa kufanya nini wakiongozwa na mfano wa Yehova wa kushughulika na Waisraeli?
14 Kwa hiyo, hakuna anayeweza kusema kwamba Mungu atuagiza tufanye jambo ambalo yeye mwenyewe hana nia ya kulifanya anapotutia moyo tujitahidi tuwezavyo tuendelee kuheshimu ndoa na kuhifadhi mwungano wa ndoa. Hakika mtu ye yote anayetafuta talaka akiwa na sababu za kichoyo hawezi kumpendeza Yeye. Kwa sababu ya kumheshimu Yehova, kumthamini na kumpenda, yatupasa tuepuke kitu cho chote kinachoweza kuharibu sifa ya ndoa zetu au ya mtu mwingineyo. Kwa njia hiyo hatutamletea Mungu sifa mbaya kwa vile anavyotumia ndoa kufananisha matendo yake mwenyewe na utimizo wa makusudi yake.
KUTOCHAFUA MALAZI YA NDOA
15. Maandiko yana maoni gani juu ya haki za ndoa?
15 Kusudi kuu la ndoa ni kuwa na jamaa. (Mwa. 1:27, 28) Hata hivyo, Neno la Mungu laonyesha kwamba si lazima watumishi wake wafanye ngono wanapojaribu kupata watoto tu. Ngono zinaweza kuwafurahisha moyo na mwili mara kwa mara. (1 Kor. 7:1-5) Maandiko mbalimbali yaonyesha kwamba mahaba yanayofanywa kabla ya ngono ni yenye kuheshimika. (Mit. 5:18, 19; Mwa. 26:8, 9) Lakini, yawapasa waliooana waangalie uhusiano wao wa ndoa usichafuke. Kutozuia nyege kwaweza kuchafua uhusiano huo. Jinsi gani?
16. Ni mwenendo gani katika ngono unaopaswa kuepukwa ili ndoa iendelee kuheshimika?
16 Watu wengine waliooana wamefuata mazoea mapotovu yanayofanywa na mahanithi (waume wenye kulala waume wenzao) wasiokuwa na ngono za asili, wakitafuta “raha” nyingi zaidi, yaani, kwa kuingiza mboo ndani ya mdomo au mkundu wa mwenzi wa ndoa. Alipokuwa akiandika juu ya hali za siku zake, mtume Paulo aliyeongozwa na Mungu alisema kwamba mahanithi ‘walivunjiana heshima miili yao kwa kufuata tamaa za aibu, wakabadili matumizi ya asili kwa matumizi yasiyo ya asili; wakayatenda yasiyopasa, wakapata nafsini mwao malipo ya upotevu wao.’ (Rum. 1:24-27) Watu waliooana wanapoanza kufuata mitindo ya mahanithi hakika hawaheshimu ndoa, bali wanaishusha na kutukuza nyege zao wenyewe, kisha malazi ya ndoa yanachafuka.a
17. Ni jambo gani lapaswa kuongoza waliooana katika ngono zao?
17 Mbali na matendo ambayo yanaonekana waziwazi kuwa mabaya na machafu, kama mazoea ambayo yametangulia kutajwa, lazima Mkristo aongozwe na dhamiri yake aamue mambo anayoweza kufanya anapokuwa na mahaba kabla ya ngono. Hata hivyo, ni hekima kutokaribia kufanya mazoea machafu yaliyotangulia kutajwa kwa sababu ya kushindwa kujizuia.—Yak. 1:14, 15.
18. Ni faida gani zinazotokana na kuendesha mambo ya ndoa kupatana na Neno la Mungu?
18 Kufuata kanuni bora za Neno la Mungu hakuzuii mtu hata kidogo asipate furaha za ndoa. Bali, kufuata kanuni hizo kunaongeza furaha, kunaleta uradhi mwingi zaidi huku waliooana wakizidi kupendana kikweli, kuonyeshana huruma na kutumikiana bila choyo. Naam, “Maagizo ya [Yehova] ni ya adili, huufurahisha moyo. Amri ya [Yehova] ni safi, huyatia macho nuru. . . . Ni za kutamanika kuliko dhahabu, . . . nazo ni tamu kuliko asali, kuliko sega la asali.”—Zab. 19:8, 10.
[Maelezo ya Chini]
a Tazama pia toleo la Mnara wa Mlinzi la Februari 15, 1975, kurasa 94-96: Watchtower, Julai 15, 1974, ukurasa 424; Watchtower, Januari 15, 1975, ukurasa 48.