Imani Inayoongoza Kwenye Wokovu
“Mtafuteni [Yehova], enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, ninyi mliozitenda hukumu zake; itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya [Yehova].”—Sef. 2:3.
1-3. (a) Ni kwa msingi gani kutakuwa na waokokaji wa taabu ya dunia yote inayokuja? (b) Ni baadhi ya mifano gani ya Maandiko inayoonyesha kwamba ndivyo ilivyo?
IJAPOKUWA uharibifu unaokuja utakuwa mkubwa mno, Biblia yatupa tumaini kwamba watakuwako waokokaji. Wataokoka kwa sababu gani? Kwa sababu ya kumwamini Mungu, kama ilivyoonyeshwa mara nyingi wakati Yehova Mungu alipoleta uharibifu juu ya wanadamu zamani. Wale waliokuwa na imani, si kuamini tu kwamba kuna Mungu, bali pia kuzitumaini ahadi zake na kuonyesha kwa matendo kwamba walizisadiki, ndio waliookoka. Mfano wa zamani zaidi ni Nuhu na jamaa yake. Walikuwa na imani wakaokoka. (Ebr. 11:7) Vilevile jambo lenye kujulikana sana ni kuokoka kwa Lutu na binti zake wawili wakati Sodoma na Gomora ilipoharibiwa. Huruma ya Lutu juu ya wale waliotazamiwa kuwa wakwe zake ilimfanya awaonye. Aliendelea kusema: “Ondokeni mtoke katika mahali hapa kwa sababu [Yehova] atauharibu mji huu. Lakini akawa kama achezaye machoni pa wakweze.” Ikawa kuchelewa mno walipopata kujua kwamba Lutu hakuwa akicheza.—Mwa. 19:14.
2 Katika karne ya tisa kabla ya Wakati wetu wa Kawaida Yehova Mungu alimpeleka Yona akawaonye watu wa Ninawi, ule mji mkuu wa Ashuru. Alikuwa ameamuru waangamizwe kwa sababu ya uovu wao mkuu. Walakini, watu hao wakatii onyo: “Basi watu wa Ninawi wakamsadiki Mungu.” Halafu ikawaje? “Mungu akaona matendo yao, ya kuwa wameiacha njia yao mbaya. Basi Mungu akalighairi neno lile baya, ambalo alisema atawatenda; asilitende.” (Yona 3:5, 10) Kizazi hicho cha Waninawi wenye kutubu kikaokoka hatari.
3 Karne zilizofuata baadaye, nabii Yeremia na Ebedmeleki, mtumwa Mwethiopia, aliyesaidia sana kuokoa uhai wa Yeremia, waliokoka uharibifu wa Yerusalemu kwa sababu ya imani yao. (Yer. 39:16-18) Habari ya historia yaonyesha jinsi Wakristo wa karne ya kwanza walivyookoka uharibifu wa pili wa Yerusalemu kwa sababu waliyaamini maonyo ya Yesu waukimbie mji walipouona umezungukwa na majeshi.—Luka 21:20, 21.
4. Ni amri gani za unabii zinazotuhakikishia kwamba kutakuwa na waokokaji?
4 Akitoa tumaini la kuokoka katika wakati wetu, Yehova Mungu alimwagiza nabii wake Sefania aandike hivi: “Mtafuteni [Yehova], enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, . . . itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya [Yehova].” (Sef. 2:3) Na kama Yehova alivyowaambia watu wa Yuda katika Isaya 26:20, 21, ndivyo atakavyowaambia watumishi wake waaminifu: “Njoni, watu wangu, ingia wewe ndani ya vyumba vyako, ukafunge mlango nyuma yako ujifiche kitambo kidogo, mpaka ghadhabu hii itakapopita. Kwa maana, tazama, [Yehova] anakuja kutoka mahali pake, ili kuwaadhibu wakaao duniani, kwa sababu ya uovu wao.”
HALI NJEMA YA MOYO NI YA LAZIMA
5-7. Kwa sababu gani inaweza kusemwa kwamba hali zinazowezesha mtu ajipatie imani ya kweli ni (a) uaminifu? (b) unyenyekevu? (c) kuwa na njaa ya kiroho?
5 Kama vile ilivyo lazima kuijua kweli ili kujipatia imani, vivyo hivyo hali njema ya moyo ni ya lazima ili kujipatia maarifa hayo. (Rum. 10:13-15) Kwa hiyo, imesemwa kwa kufaa kwamba ili mtu asitawishe imani isiyotikisika na tumaini hakika katika Mungu, ni lazima awe mnyofu, mnyenyekevu tena aitamani kweli. Viongozi wa kidini wa siku za Yesu hawakuweza kumwamini Yesu, kwa sababu hawakuwa wanyofu ila walikuwa wanafiki. (Mt. 23:13-33; Yohana 8:46) Walakini, watu wanyonge na wasio na cheo walimsikiliza kwa furaha.—Marko 12:37.
6 Wala wenye kiburi hawaelekei kuamini na kutumaini yale ambayo Mungu amesema. Kwa sababu gani? Kwa sababu ili kufanya hivyo, yampasa mtu awe mnyenyekevu, awe na nia ya kujifunza, nao wenye kiburi hawataki kufundishwa. Zaidi ya hayo, tunaambiwa kwamba imani ni zawadi kutoka kwa Mungu. Kwa kuwa Mungu huwapinga wenye kiburi, hawezi kuwapa zawadi hiyo.—Zab. 25:9; Efe. 2:8; Yak. 4:6.
7 Vilevile, kuona njaa ya kiroho ni sharti la kwanza la kupata maarifa ya makundi ya Mungu. Mtu mwenye kinaya, asiyejali na mwenye ubaridi juu ya dhambi zake mwenyewe na hali za ulimwengu si mwenye njaa ya kiroho. Mtu anayeona njaa ya kiroho anafahamu uhitaji wake wa kiroho. Ndiyo sababu Yesu aliweza kusema katika Mahubiri yake ya Mlimani hivi: “Heri walio maskini wa roho . . . Heri wenye njaa na kiu ya haki.” (Mt. 5:3, 6) Yesu alitoa pia mwito huu: “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.” (Mt. 11:28-30) Karne zilizotangulia, Yehova alimwagiza nabii Isaya aseme wazo linalofanana na hilo hivi: “Haya, kila aonaye kiu, . . . naye asiye na fedha; njoni, nunueni mle; naam, njoni, nunueni divai na maziwa, bila fedha na bila thamani. . . . Nisikilizeni kwa bidii. . . Sikieni, na nafsi zenu zitaishi.”—Isa. 55:1-3.
KUJIPATIA IMANI YENYE NGUVU
8. Ni sababu gani moja inayofanya watu wasiweze kumwamini Yehova Mungu na Neno lake?
8 Ni wazi kulingana na hayo yaliyotangulia kwamba ni hapo tu mtu anapokuwa na hali njema ya moyo ndipo moyo wake unapoweza kuitikia vizuri kweli ya Neno la Mungu. Ni lazima iweko nia ya kusadiki yaliyo kweli. Mtu anayepinga ushuhuda wa msingi wa imani kwa kiburi na kwa unafiki, na mwenye moyo wa mashaka, hawezi kusadikishwa, kwa sababu yeye hataki kuamini. Ni kama anaona uhitaji wa kulaumu mno makosa madogo, na ni mwenye mashaka.
9. Ni baadhi ya maandiko gani yanayoonyesha kwamba kuna imani ya kadiri mbalimbali?
9 Kwa wazi, kuna imani ya kadiri mbalimbali. Kwa mfano, Biblia inataja kuwa “dhaifu wa imani,” naye Yesu aliwakaripia wanafunzi wake kwa sababu ya kuwa “wa imani haba.” (Rum. 4:19; Mt. 8:26) Kwa upande mwingine, Neno la Mungu lasema pia juu ya “uthabiti wa imani,” juu ya “imani kubwa namna hii” na juu ya imani iliyo mashuhuri sana hata “inahubiriwa katika dunia nzima.”—Kol. 2:5; Mt. 8:10; Rum. 1:8.
10, 11. (a) Ili kuwa na nguvu katika imani, lazima mtu afanye nini kwa bidii? (b) Lazima mtu atii shauri gani la Maandiko ili kutimiza kusudi hilo?
10 Bila maarifa haiwezi kuwako imani. Kwa hiyo, ili mtu awe na nguvu katika imani, yampasa afanye bidii kuyatwaa maarifa. Maana yake ni kulitii shauri lililoongozwa na Mungu “mwache kufanyizwa kulingana na mtindo wa taratibu hii ya mambo, bali mgeuzwe kwa kubadili akili zetu, mpate kujithibitishia wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” Ni kwa kujifunza tu Neno la Mungu ndipo unapoweza kubadili nia yako, ukikumbuka maneno ya Yesu aliyosema hivi: “Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.”—Rum. 12:2, tafsiri ya Kiingereza ya New World; Mt. 4:4.
11 Mtu anatakiwa ajitahidi sana katika siku hizi zenye shughuli nyingi, ili aone wakati wa kutimiza mahitaji yake ya kiroho kwa kujifunza Neno la Mungu. Kwa sababu kupenda mali kumeenea mno na kuna mikazo ya kutafuta raha, shauri walilopewa wale Wakristo wa karne ya kwanza kwa sababu ya mazingira yao ya kipagani linafaa sana leo. “Basi mwangalie sana namna munavyotembea, si kama watu wasio na hekima, lakini kama watu wenye hekima; mukikomboa wakati kwa sababu siku hizi ni za uovu. Kwa hivi musiwe wajinga, lakini wenye kufahamu mapenzi ya Bwana.” Bila shaka mtu anatakiwa ajifunze Neno la Mungu ili kuweza kufanya hivyo, kwa maana ndilo peke yake linaloweza kutuambia yaliyo mapenzi ya Mungu.—Efe. 5:15-17, tafsiri ya Kiswahili ya Zaire.
12. Maana yake nini ‘kuukomboa wakati’?
12 Maana yake nini ‘kujikombolea wakati’ leo? Kunamaanisha tuache kutumia wakati wetu kwa shughuli zisizo na maana na kuukomboa utumiwe katika njia yenye maana. Zaidi ya hayo, kunaweza kuwa na maana ya kwamba inatupasa tuchukue wakati kutokana na mambo mengine ambayo si yenye maana sana, kutokana na mambo ambayo ni yenye kupendeza tu, yenye kufurahisha na labda hata yenye kuelimisha. Kunaweza kuwa na maana ya kutokutumia wakati mwingi tukitazama televisheni, kutotumia wakati mwingi tukisoma magazeti au vitabu vya ulimwengu. Kunaweza kuwa na maana pia ya kutokutumia wakati mwingi kwa shughuli za tafrija zenye kupoteza wakati bure. Kufanya hivi ni kutanguliza mambo ya Biblia. Yaangalie kwanza, ndipo wakati unaobaki uutumie kwa shughuli zisizo na maana sana. Bila kufanya hivyo, unaweza kuona kwamba mambo haya mengine yanavuta fikira sana hata yanasonga mambo ya kiroho yanayoweza kuitia imani yako nguvu. Ndiyo maana Yesu alishauri hivi: “Utafuteni kwanza ufalme [wa Mungu], na haki yake.”—Mt. 6:33.
13-15. (a) Kwa sababu gani ni lazima mtu awe na maarifa sahihi ili kuwa na imani yenye nguvu? (b) Tunahitaji nini ili kupata maarifa sahihi, na tunaweza kuyapata wapi? (c) Ni jambo gani jingine ambalo ni la maana ili kutia imani yetu nguvu?
13 Lakini kusoma Biblia peke yake hakutaifanya imani yako iwe yenye nguvu. Yakupasa ufahamu na kuthamini maana ya yale unayosoma. Ni lazima uwe na maarifa sahihi. Wayahudi wengi katika nyakati za mitume walikuwa na maarifa ya kadiri fulani juu ya Maandiko ya Kiebrania, lakini kwa kuwa hawakuwa na maarifa sahihi, bidii yao ilikuwa ya bure. (Rum. 10:1-4) Unahitaji msaada ujipatie maarifa sahihi, pamoja na ufahamu. Kwa mfano, baada ya kufufuka kwa Yesu, aliwatia, moyo wanafunzi wake wenye huzuni kwa kuwaeleza yaliyosemwa na Neno la Mungu juu ya lazima ya kuteswa na kufa kwake. (Luka 24:15-47) Hali kadhalika, ilikuwa lazima Filipo, mhubiri wa injili, amsaidie mkuu wa baraza, Mwethiopia, apate ufahamu, maana alikuwa akisoma Isaya sura ya 53 lakini asifahamu maana yake.—Matendo 8:27-39.
14 Kwa sababu hii hii Wakristo wanatiwa moyo hivi: “Na tuangaliane kwa njia ya kusukumana katika mapendo na kazi nzuri; tusiache kukusanyika pamoja, kama ilivyo desturi ya wengine; lakini tukionyana, zaidi sana mnavyoona siku ile inakaribia.” Unaweza kupata msaada katika mikutano ya kujifunza Biblia ya mashahidi Wakristo wa Yehova kutoka kwa wale wanaotumikia kama ‘wainjilisti, wachungaji, waalimu, waangalizi, wazee’ wanaoliona kuwa pendeleo kusaidia wengine wapate maarifa sahihi ya kweli ya Mungu.—Ebr. 10:24, 25, tafsiri ya Kiswahili ya Zaire; Efe. 4:11-13; 1 Tim. 3:1-7; 1 Pet. 5:1-3.
15 Wala usisahau ubora wa sala ya kutia imani yako nguvu. Yesu aliwaambia wafuasi wake waombe roho takatifu ya Mungu, nayo imani ni mojawapo matunda ya roho hiyo. (Luka 11:13; Gal. 5:22, 23) Pia alitutumainisha kwamba tukiomba katika imani na kudumu katika sala, Mungu atajibu sala zetu. (Mt. 7:7; 17:20) Lakini tusisahau kwamba yatupasa tutimize sehemu yetu. Yatupasa tujitahidi tutende kupatana na kile tunachoomba. Kama vile mkulima asivyolima, kupanda na kupalilia tu, bali yampasa pia amtegemee Mungu atoe mwangaza wa jua na mvua, hivyo ndivyo ilivyo na kujipatia imani yenye nguvu. Tukitimiza sehemu yetu, Mungu naye atatimiza sehemu yake.—Mt. 5:45.
“PIGA VITA VILE VIZURI VYA IMANI”
16. Kuna uhusiano gani kati ya imani na matendo?
16 Maana ya kuonyesha imani inayoongoza kwenye wokovu si kuepuka mambo yaliyo magumu na kufuata yale ambayo tunaona ni mepesi kufuata. Si jambo jepesi kuonyesha imani, wala si gumu mno. Imani inaonekana kwa matendo, kwa maana bila matendo imani ni kama mzoga, maiti. Imani isiyo na matendo ni ya bure; haitaongoza mtu kwenye wokovu. (Yak. 2:14-26) Ili kuokoka lazima ufanye vita, kama vile mtume Paulo alivyomkumbusha rafiki yake Timotheo: “Piga vita vile vizuri vya imani; shika uzima ule wa milele.”—1 Tim. 6:12.
17-19. (a) Ni mifano gani inayokazia ubora wa imani? (b) Imani inatoa ulinzi gani? (c) Ni jambo gani jingine linalohusika katika kufanya vita vile vizuri vya imani?
17 Kwa kupiga vita vile vizuri vya imani ‘hutatupwa huku na huku, na kuchukuliwa na kila upepo wa elimu, kwa hila ya watu.’ Bali, kwa kutumia “ngao ya imani” ‘utaweza kuizima mishale yote yenye moto ya yule mwovu.’ (Efe. 4:14; 6:16) Imani inakuwa kama dirii pia ya kukinga moyo usiambukiwe na uchoyo wote uliomo ulimwenguni leo. (1 The. 5:8; 1 Yohana 2:16) Ukiwa na ulinzi huo utaweza ‘kuhesabu kuwa ni furaha tupu, ukiangukia katika majaribu mbalimbali; ukifahamu ya kuwa kujaribiwa kwa imani yako huleta saburi.’ Yeremia alikuwa na imani hiyo akaweza kuwapa ushuhuda kwa ushujaa watu waasi, zaidi ya miaka 40.—Yak. 1:2, 3.
18 Kama ilivyokuwa wakati wa Yesu, leo ulimwengu unapinga vikali Wakristo wanaoishi kupatana na kanuni za haki. Maneno ya Yesu yanayosema wafuasi wake si sehemu ya ulimwengu, na kwamba watachukiwa, yangali ya kweli. Alisema: “Ulimwenguni mnayo dhiki; lakini jipeni moyo; mimi nimeushinda ulimwengu.” Aliushindaje? Kwa imani yake, kwa maana twasoma: “Huku ndiko kushinda kuushindako ulimwengu, hiyo imani yetu.” (Yohana 16:33; 1 Yohana 5:4) Imani ya namna hiyo itakuzuia usiyaache mafundisho ya Biblia, ikufanye uepuke vishawishi vya maarifa ya uongo na hekima ya ulimwengu. Itakulinda pia na utafutaji wa mali za ulimwengu huu, kupenda pesa. (1 Tim. 6:10, 20, 21) Itakuwezesha utii amri ya kimungu inayosema ujitenge na ‘Babeli Mkuu/ milki ya ulimwengu ya dini ya uongo: “Tokeni kwake, enyi watu wangu, msishiriki dhambi zake, wala msipokee mapigo yake.”—Ufu. 18:4.
19 Kufanya vita vile vizuri vya imani kwahusu pia kueleza watu mambo ambayo umejifunza juu ya msingi wa imani na taraja la kuokoka. Ni kama vile mtume Paulo alivyoeleza kwa uzuri mwingi: “Kwa kuwa tuna roho ile ile ya imani; kama ilivyoandikwa, Naliamini, na kwa sababu hiyo nalinena; sisi nasi twaamini, na kwa sababu hiyo twanena.”—2 Kor. 4:13.
KUOKOKA KUINGIA KATIKA NINI?
20. (a) Ni kutii amri gani ya unabii kutakakowezesha watu kuokoka? (b) Kwa sababu gani Sefania anasema “huenda,” na hilo linatuhusuje leo?
20 Kwa kujipatia imani yenye nguvu na ‘kuvipiga vita vizuri vya imani,’ utaweza kulitii shauri ambalo ni la muhimu zaidi leo kuliko zamani, yaani: “Mtafuteni [Yehova], enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, . . . itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya [Yehova].” Kwa nini inasemwa, “Huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya [Yehova]”? Ni kwa sababu kwanza maneno hayo yalihusu taifa la Israeli kabla halijaharibiwa katika mwaka wa 607 K.W.K., tena wokovu ulitegemea rehema ya Mungu juu ya wale ambao wangetii peke yao? Maneno hayo ni kumbukumbu kwetu kwamba hatuwezi kudhani kwamba Mungu ataturehemu hata tusipotii.—Sef. 2:3.
21. Watakaookoka taabu ya dunia yote wataweza kutazamia nini?
21 Ukiisha kuuokoka mwisho wa taratibu hii ya kale ya mambo, waweza kutazamia nini? Taratibu mpya yenye amani, haki na shibe; kuja kuiona dunia ikifanywa kuwa paradiso, kama lilivyokuwa kusudi la kwanza la Yehova kwa dunia na wanadamu. (Mwa. 1:28; 2:16) Ndipo Mungu “atapangusa kila chozi katika macho yao; wala mauti haitakuwa tena; wala maombolezo, wala kilio, wala uchungu hautakuwa tena; kwa maana maneno ya kwanza [yatakuwa] yamekwisha kupita” wakati huo. (Ufu. 21:4, tafsiri ya Kiswahili ya Zaire) Tena maneno ya nabii Isaya katika sura ya 25:6, 8 yatatimizwa: “Na katika mulima huu [Yehova] wa majeshi atafanyia mataifa yote karamu ya vitu vya kunona, karamu ya mvinyo ya vipande vya chini, ya vitu vya kunona vilivyojaa mafuta, ya mvinyo ya vipande vya chini iliyochujwa sana. . . . Atameza kufa kusiwe tena milele. Na Bwana MUNGU [Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu] atapangusa machozi toka nyuso zote; na haya ya watu wake ataiondosha toka dunia yote: maana [Yehova] amesema maneno haya.” (Tafsiri ya Kiswahili ya Zaire, na tafsiri ya Kiingereza ya New World) Lo! jinsi lilivyo tumaini tukufu kwa wote watakaoiokoka “dhiki kubwa” kwa sababu ya imani yao!
—Kutoka The Watchtower, April 15, 1977.
[Picha katika ukurasa wa 471]
Katika siku hizi zenye shughuli yatupasa tutafute wakati wa kujifunza Neno la Mungu na kuyaacha mambo yasiyo na maana sana, hata yanayofurahisha, ikiwa tunataka imani yenye nguvu
[Picha katika ukurasa wa 472]
Ili kuwa wenye nguvu katika imani yatupasa tukutane kwa kawaida pia pamoja na Wakristo wenzetu