Tumekuwa Wazazi Miaka Ishirini
Imesimuliwa na Norman C. Pearcy
WAUME na wake wengi vijana wanatazamia kwa shauku kuzaliwa kwa mtoto wao wa kwanza. Wengine wanakutazamia wakiwa na mashaka, kwa maana kitoto kichanga kitabadili sana maisha zao.
Sisi tulikuwa kama watu hao wenye mashaka, kwa maana mtoto wetu wa kwanza alibadili sana maisha zetu. Tulikuwa tukifanya kazi ambayo tusingeweza kuendelea nayo huku tukitumia wakati na pesa za kutunza jamaa.
Tangu mwanzo tulijua kwamba ni upumbavu kumwacha mtoto aongozwe na kitu cho chote kitakachomwongoza. Miaka mingi iliyopita tulisoma kitu kilichotuonyesha kwamba kiasi utakachompenda mtoto wako kitaamuliwa na jinsi utakavyojitahidi kuepuka shughuli nyingine uwe na wakati wa kuwa pamoja na mtoto wako anayekua. Wakati mke wangu nami tunapotazama nyuma, tunaweza kusema kwamba nyakati nyingine mambo yanakuwa makavu sana. Lakini kwa kuwa sasa tumekuwa wazazi miaka 20, yaani watoto wetu wana miaka kumi na tisa na 20, tunaweza kusema kwamba matokeo mazuri yanayopatikana yanafanya iwe vizuri kujitahidi.
Lakini, kwanza acha nikueleze kifupi jinsi tulivyooana tukaanza kuwa wazazi miaka 20.
NDOA NA JAMAA
Mwaka 1948 nikawa “painia,” kama vile Mashahidi wa Yehova wanavyowaita waalimu wa wakati wote wa habari njema za ufalme wa Mungu. Miaka miwili baadaye nilijiunga na jamaa ya makao makuu ya Mashahidi katika Brooklyn, New York, nisaidie kutokeza vitabu vyenye habari za Biblia.
Mwaka uliofuata, yaani 1951, nilikwenda kwenye mazoezi ya kuhitimu ya Gilead School, ambako wamisionari wa Mashahidi wa Yehova wanazoezwa. Mmoja wa wanafunzi, Marianne Berner, alibaki mjini New York juma kadha kabla ya kuondoka kwenda kwenye mgawo wake, basi tukafahamiana. Baada ya kukaa zaidi ya miaka mitatu katika Yokohama, Japan, alirudi mwaka 1955 ahudhurie kusanyiko la mataifa yote mjini New York. Nikamchumbia, naye Marianne akawa mke wangu na mwenzi wangu wa maisha.
Tulipewa nafasi ya kutumikia katika kazi ya mzunguko, kutembelea na kusaidia makundi ya Mashahidi wa Yehova katika kusini ya Illinois. Makundi hayo yalitufurahisha sana, nasi tulitaka kutumia maisha zetu katika utumishi wa wakati wote. Mwishowe tulitumainia kurudi tukatumikie pamoja na jamaa ya makao makuu katika Brooklyn. Lakini, baada ya muda mfupi tukajua kwamba tutakuwa wazazi, tukahuzunika kidogo kwa sababu jambo hilo lingebadili sana mipango yetu.
Wakati wa hotuba ya mwisho katika kusanyiko letu la mzunguko lililofuata, nilichekesha watu kwa kuwaambia kwamba mke wangu aliisikia hotuba yangu inayosema “Kusonga Mbele ili Kukomaa,” akadhani nilisema, “Kusonga Mbele Ili Kuwa Mama.” Tulianza kuishi California tukamzalia huko binti yetu Cynthia. Ndipo alipofuata mwana wetu, Gregory.
MAZOEZI YENYE KUSUDI
Watoto wetu walitufurahisha sana, nasi tukakaza nia tuwalee vizuri kama tuwezavyo. Lakini tungewaongoza na kuwaadibisha namna gani miaka 20 iliyokuwa ikija? Tuliukumbuka mfano wa baba ya kijana Samsoni, aliyemwomba Yehova uongozi wa kulea kivulana wake.—Amu. 13:8.
Kila juma tulionyesha tulitaka kuongozwa na Mungu kwa kujifunza Biblia na watoto wetu, tangu walipokuwa vitoto vichanga. Tuliona kwamba ni vyepesi kuacha kujifunza na watoto wako maana ni vigumu kujifunza nao kuliko kujifunza na watu wengine. Vilevile, mazoea yetu ya kila siku yalikuwa kuzungumza nao andiko la Biblia wakati wa chakula.
Tena, wakati wa chakula tulifundisha watoto wetu alfabeti, kwa njia hiyo tukawatayarisha kwenda shuleni. Katika darasa la kwanza Greg alitatizwa kusoma. Kila siku tulitumia saa moja tukiwa naye, kumsaidia afanye maendeleo. Tulionana na waalimu mara nyingi wakaona kwamba tulitaka sana kuona watoto wetu wakifanya maendeleo.
Tangu Cynthia na Gregory walipozaliwa, tulikwenda nao kwenye mikutano yote ya kundi na makusanyikoni, tukijua kwamba wangepata maongozi bora huko. (2 Tim. 3:15) Walipoendelea kukua, tuliwasaidia kutayarisha maelezo ya kutoa mikutanoni. Mara za kwanza walisema maneno machache tu, lakini tulihakikisha kwamba walilielewa funga walilokuwa wakijibu. Tulipokuwa tukirudi nyumbani baada ya kusikiliza hotuba za Biblia za watu wote, tulikuwa tukiwauliza waeleze mambo waliyokumbuka.
Jitihada zetu za kuwafundisha zilikuwa na matokeo mazuri, kwa maana mambo tuliyowafundisha yalidumu katika akili zao changa. Kwa mfano: Wakati Greg alipokuwa na miaka minne tu tulikuwa tukijifunza habari za Ibrahimu, na jinsi alivyojaribiwa imani yake kwa kuagizwa amtoe mwanawe pekee, Isaka, kama dhabihu. Tukamweleza kwamba Ibrahimu na mwanawe pia walikuwa na nia ya kumtii Yehova. Halafu nikatoa mfano nikasema: “Basi waona, Greg, ni kama kwamba Yehova aliniambia nikupeleke nje uani nikutoe kama dhabihu.” Halafu nikamwuliza, “Kama ingekuwa hivyo, ningefanya nini?” Greg alijibu moja kwa moja akasema inanipasa kumtii Yehova.
Baadaye tukamsikia Greg akitoa sala zake. Alifunga macho, akainama kichwa, akasema: “Yehova, ukimwambia Baba anipeleke nje uani anitoe kama dhabihu, hiyo ni SAWA kwangu.”
Si ajabu kwamba Yesu alisema wale watakaoingia katika Ufalme wa mbinguni wanatakiwa wawe na sifa kama za mtoto. Tuliona kwamba kweli za Biblia zilikuwa zikiifikia mioyo ya watoto wetu, nao walijisikia wakitaka kutii.
Wakati Cindy alipokuwa na umri wa miaka saba tulimsaidia kutolea watu milangoni kwao magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Kila siku, wakati aliporudi nyumbani kutoka shuleni, alikuwa akigonga mlango wa nyuma na kutoa mahubiri yake. Ndipo siku yenyewe ilipofika, akaenda nyumbani kwa mtu asiyemjua. Alipingwa, akaanza kulia. Tuliporudi garini, mke wangu alimweleza kwamba hata Yesu na mitume wake hawakukubaliwa na watu, na kwamba haitupasi sisi kukata tamaa, maana wao hawakukata. Basi Cindy hajakata tamaa.
Mwaka 1966 mke wangu alijiandikisha tena akawa painia, akapanga kutumia saa mia moja kwa mwezi akifundisha watu Biblia nyumbani kwao. Tuliona kwamba ili watoto wakue wakiwa na tamaa ya kuingia katika kazi hiyo ya maana sana, walipaswa kutuona sisi pia tukiiheshimu sana. Kiangazi hicho nilikaribishwa nitumikie tena kama mwangalizi wa mzunguko kwa muda katika eneo letu, halafu jamaa yetu yote ikaweza kushiriki.
Jumamosi nilimsikia Greg mwenye miaka minane akifanya mipango na watoto wengine wa rika lake wafanye kazi ya kuhubiri mlango kwa mlango. Alikuwa akifuata sana mfano alioniona nikimwekea muda mfupi tu kabla ya hapo. Jambo hilo likanionyesha sana ubora wa kuweka mfano unaofaa.
KUSHUGHULIKA NA HALI MBALIMBALI
Watoto walipoendelea kukua, maulizo yalitokea juu ya mambo kama kujipamba, mitindo ya mavazi, matembezi ya wavulana na wasichana na vikaramu. Tulijaribu kuwafundisha maamuzi mazuri, tukawapa maongozi.
Wakati Cindy alipokuwa na umri wapata miaka kumi na mitano, alitaka kuwa na suruali fulani yenye kubana viuno ambayo wasichana walivaa wakienda shuleni. Mke wangu alinyamaza akaanza kuchunguza ni wasichana wa namna gani waliovaa suruali hizo. Aliomba vijana wengine kundini maoni yao juu ya vijana waliovaa hivyo, bila kuwaeleza kusudi lake la kuwauliza. Wakasema wasichana wenye tabia mbaya hasa ndio waliovaa suruali hizo.
Marianne alimweleza Cindy uchunguzi wake, akamweleza sababu hapaswi kufanana na wasichana hao. Cindy alipewa nafasi ya kutoa maoni yake mwenyewe aonyeshe kama alikubaliana na uamuzi wetu au sivyo. Linalotufurahisha ni kwamba, maneno yaliishia hapo. Alijifunza pia kwamba mavazi yetu yanaonyesha watu jinsi tulivyo.
Wakati Greg alipokuwa na umri wapata miaka kumi na minne, alianza kuchukia kuwa “kivulana,” akataka sana kutambuliwa kuwa “kijana mwanamume.” Alifanya urafiki mwingi na Shahidi kijana aliyekuwa na umri wa miaka kumi na tisa. Lakini, ushirika wao ulimfanya Greg atake kuwa na uhuru mwingi kama kijana mwenzake. Alianza kujitegemea mwenyewe. Tukaanza kumzuia asishirikiane na kijana huyo, basi Greg akauliza: “Sababu? Mnadhani yeye ni rafiki mbaya?”
Tulimweleza kwamba urafiki wenyewe haukuwa mbaya, lakini labda usingemfaidi. Nilimpa nafasi ya kutoa maoni yake mwenyewe. Nikamwambia: “Ikiwa hukubaliani nami, au ikiwa unadhani tunakosea, au tuna maoni mabaya, tafadhali tuambie.”
Baada ya kunyamaza kidogo, Greg akasema: “Nakubaliana nanyi. Mimi nilitaka kujua sababu tu.”
Wakati mmoja tulipokuwa tukisafiri garini Cindy alimtabasamia (akamwonyesha uso wa furaha) kivulana mmoja aliyekuwa akipita, ingawa hakuwa na kusudi baya. Kivulana huyo alitufuata nyumbani bila ya sisi kujua, halafu akaongea na watu fulani wakamweleza jina la Cindy. Wakaanza kufahamiana bila ya sisi kujua. Tulitumia wakati mwingi kumwonyesha kwamba kivulana huyo hakupendezwa naye kwa sababu ya kutaka kumwona akiwa katika hali njema, bali alipendezwa na mwili wake tu.
Sisi tumethamini sana makala nzuri za Mnara wa Mlinzi zinazoeleza matatizo yanayowapata vijana. Tulisoma baadhi yazo mara nyingi pamoja na watoto wetu, tukazungumza mema na mabaya ya matendo fulani. Halafu sisi wazazi tukafanya maamuzi imara, tukawekea watoto wetu mfano wa kumheshimu Yehova na Neno lake lililoandikwa.
KUWAFUNDISHA UFUNDI
Nilikuwa na kazi ndogo ya kutengenezea watu vitu vilivyoharibika, kwa hiyo Greg alipokuwa na umri wa miaka kumi na mitatu alianza kufanya kazi nami kabla ya kwenda shuleni, tangu saa 11:00 ya asubuhi mpaka saa 2:00 asubuhi. Cindy alipokuwa na umri wa miaka kumi na mitano alianza kujifunza hesabu za kibiashara, akiongozwa na rafiki yetu Shahidi. Tulitia mkazo pia ajifunze kupika, kushona kwa kutumia cherehani na kujifunza ufundi mwingine. Greg pia alijifunza kupika, nikamfundisha kazi ya kutandika mikeka sakafuni.
Mambo hayo yote yalitupa kazi nyingi, basi tukaamua watoto wamalize masomo yao kwa njia ya posta. Kufanya hivyo kuliwapa wakati wa kujifunza kazi ya kuwachumia pesa, na vilevile kupata elimu ya kilimwengu waliyohitaji. Ili kumchangamsha Greg apate elimu aliyohitaji, tulimzuia asipate leseni ya uendeshaji mpaka atakapomaliza shule. Alimaliza masomo ya juu yanayofanywa miaka minne shuleni kwa muda wa miaka miwili, kisha akajiunga na Marianne, Cindy na mimi katika upainia wa wakati wote.
MAZOEZI YA MAANA
Wakati Greg alipokuwa na umri wa miaka kumi na minne, naye Cindy akawa na kumi na mitano, tuliona ilifaa kutimiza miradi ambayo jamaa yetu ilikuwa imekuwa nayo muda mrefu kwa kuwapeleka wakaone makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova, mjini New York. Makao hayo yalikuwa maili 3,000 (kilomita 4,800) kutoka kwetu, nasi hatukuwa na pesa nyingi. Jamaa nzima tulizungumza jambo hilo tukakaza nia twende, hata kama jambo hilo lingetulazimu tuweke nyumba yetu iwe rehani. Lakini tena, tukaona kwamba mkono wa Yehova si mfupi. Rafiki alikuja akasema alitaka kutufanyia jambo fulani. Akatupa kadi yake ya kampuni ya kukopa petroli (essence) tuitumie katika safari yetu.
Watoto wetu walishangazwa sana na Betheli, vilevile na watu wa huko wenye upendo, wanaojitolea kutumia wakati wao kutupatia vitabu vyenye maagizo ya kiroho. Mke wangu nami tulifurahi sana kuonana tena na wengi wa watu hao waaminifu ambao wametia bidii nyingi katika utumishi wa Yehova miaka mingi.
PENDELEO KUBWA
Ingawa kwanza tulikuwa hatuna shauku tulipotazamia kupata mtoto, tunaweza kusema kikweli kwamba hilo limekuwa pendeleo tunalopaswa kutolea shukrani. Ni kweli kwamba si vyepesi kulea watoto, katika ulimwengu huu, uliojawa na mazoea mengi sana yasiyo ya Kikristo. Baadhi ya sikukuu zake za upagani zinaweza kuvuta vijana. Lakini tumekuwa waangalifu tukasaidia watoto wetu hivi kwamba, hawakujisikia wakiwa na ukosefu wa kitu cho chote chema.
Kwa hiyo wakati watu wengine walipokuwa wakisherehekea Krismasi, sisi tulitumia siku ambazo watoto hawawi shuleni kukaa katika kijumba milimani na kuifurahia theluji. Nilikuwa nikimpeleka Greg kuvua samaki mara kwa mara. Tena tulihudhuria makusanyiko makubwa ya Kikristo na kujitolea pamoja tufanye kazi za kutayarisha makusanyiko. Jambo hilo liliwezesha watoto wetu kupata rafiki wengi wazuri. Wao hawajawa na ukosefu wa kitu cho chote, isipokuwa kisonono na kaswende, mimba zinazopatikana kabla ya kuolewa, utoaji wa mimba, kuzoea matumizi ya dawa za kulevya na mambo mengine kama hayo yanayofanywa sana na vijana ambao hawakupewa uongozi ufaao na wazazi wao katika Neno la Mungu.
Watoto wetu wana moyo uliotulia vizuri, nami nadhani sababu moja ni kwamba sisi tunafanya mambo mengi pamoja nao. Kwa mfano, kila mwaka tunakuwa na karamu kubwa ya ukumbusho wa siku ya arusi yetu, kisha sote wanne tunajipatia zawadi. Tunaziweka juu ya piano siku nyingi mapema, tena tunakula chakula cha pekee pamoja. Hiyo si karamu yetu peke yetu, kwa maana watoto walitokea kwa sababu ya arusi yetu.
Watoto wetu wamefurahia kazi nyingi zisizofurahiwa na wengine, kama kuhubiri na kutoa hotuba za Biblia. Wakati Cindy alipokuwa na umri wapata miaka kumi alitoa hotuba ya mwanafunzi mbele ya watu wengi katika kusanyiko letu la mzunguko. Mke wangu alimtengenezea vazi la kizamani, naye Cindy akaitoa habari kama kwamba ni kisichana cha karne ya kwanza chenye kueleza kisichana kingine habari ya Biblia. Tena, watoto wote wawili wamechangamka kwa kushiriki katika programu za makusanyiko makubwa zaidi ya wilaya.
Sisi tunajisikia kwamba tumefurahia sana maisha. Tumewatazama watoto wetu wakikua, tukafurahi kuwaona wakiendelea kuwa waalimu hodari wa kweli za Biblia tunazothamini sana. Sasa, kwa kuwa tuna watu wazima wawili zaidi wanaomtumikia Yehova katika jamaa yetu, tunatazamia furaha na mapendeleo zaidi katika utumishi wa Mungu wetu.
[Picha katika ukurasa wa 499]
Nilimfundisha Greg kutandika mikeka sakafuni
[Picha katika ukurasa wa 499]
Mke wangu alimfundisha Cindy kushona