Kitabu Kisicho na Kifani
KUNA kitabu kilichoandikwa na watu wa nchi za Mashariki chenye kuongoza sana wanadamu kuliko kitabu kingine cho chote. Chote au sehemu yake kimetafsiriwa katika lugha zaidi ya 1,600. Kitabu hicho ndicho kimefanya watu wengi na hata mataifa mazima yajifunze kusoma! Lugha fulani ambazo hapo kwanza hazikuweza kuandikwa katika vitabu zimekwisha anza kuandikwa sasa baada ya kitabu hicho kutafsiriwa katika lugha hizo. Kitabu hicho kisicho na kifani ndicho Biblia.
Ni ajabu sana kwamba Biblia imekubaliwa na mamilioni ya watu wa kila kabila na taifa. Tunaishi katika karne ya 20, mamia mengi ya miaka baada ya kutukia kwa matukio yanayosimuliwa katika Maandiko Matakatifu. Hali zinazotajwa na Biblia juu ya nchi fulani zinaonekana na wasomaji wengine kuwa za zamani sana pia. Hata hivyo Maandiko Matakatifu yamewavuta watu mioyoni mwao kuliko maandishi mengine yo yote.
Katika kitabu Christianity’s Contributions to Civilization (Jinsi Ukristo Umesaidia Kuleta Ustaarabu), Charles D. Eldridge alitoa maoni haya: “Si kawaida vitabu vilivyoandikwa katika nchi fulani kupendwa na watu wengi wa nchi nyingine; vinakuwa kama miti inayokufa inapopandwa mahali pengine; ingawa vinapochapwa vinakubaliwa sana katika taifa moja, kwa kawaida havikubaliwi katika mataifa mengine yenye hali tofauti za kijamii, za elimu, za kisiasa na za kidini. Lakini sivyo ilivyo Biblia: hiyo imepelekwa katika nchi zote zilizo chini ya jua na bado watu wakaendelea kuipenda.”
Sababu kubwa inayofanya Biblia ivute makabila yote na mataifa yote ni kwamba inaonyesha maisha jinsi yalivyo kabisa, inaonyesha furaha na huzuni zake, mazuri yake na mabaya yake, maendeleo yake na vipingamizi vyake, mapendo yake na chuki yake. Katika utangulizi wa kitabu The Greatest Book in the Worid (Kitabu Kilicho Kikubwa Kupita Vyote Ulimwenguni), T. H. Darlow alieleza mambo hayo kwa kusema hivi: “Kuna Kitabu kimoja, tena kimoja tu, kinachozungumza mapana na marefu ya hali ya mwanadamu. Biblia inayataja mambo yale ya kawaida—kama anga na upepo na bahari, kama chakula na divai, kama mabusu ya watoto wadogo na machozi yanayotiririshwa na watu kaburini—mambo yasiyoweza kuacha kufanywa kamwe, kwa sababu ndiyo asili ya wanadamu.”
Biblia imewapa watu masomo ya ajabu na kusaidia sana vitabu vingi viandikwe. Kwa mfano, wafikirie watu karibu milioni 358 wanaosema Kiingereza. Katika kitabu A Short History of the English Peopie (Historia Fupi juu ya Waingereza), John R. Green anaandika hivi; “Vitabu vyote vya Uingereza, isipokuwa insha za Wyclif zilizosahauliwa, vimeendelea kuandikwa vizuri zaidi tangu Maandiko Matakatifu yalipotafsiriwa na Tyndale na Coverdale. Wakati agizo lilipotolewa ili Biblia ianze kutumiwa makanisani, taifa zima kwa ujumla halikuwa na vitabu vya Kiingereza vya historia, vya mahaba wala vya mashairi, isipokuwa shairi fupi la Chaucer linalojulikana.” Biblia ndiyo iliyomfanya Mwingereza William Shakespeare atake sana kuandika vitabu vyake vya michezo ya kuigiza na mashairi. Imesemekana kwamba “hakuna mwandikaji aliyetumia mawazo na maneno ya Maandiko Matakatifu kwa wingi kama Shakespeare.” Vilevile, Biblia ndicho kitabu kilichotumiwa zaidi na Shelley mtunga mashairi Mwingereza katika maktaba yake ndogo.
Miaka ya karibuni zaidi, Hall Caine, mwandikaji Mwingereza wa vitabu vya hadithi, alikubali hivi: “Hadithi inayoitwa ‘The Deemster’ (Mfikiriaji) ni hadithi ya Mwana Mpotevu, ‘The Bondman’ (Mweka Dhamana) ni hadithi ya Esau na Yakobo, ‘The Scapegoat’ (Mwenye kulaumiwa kwa sababu ya makosa yasiyo yake) ni hadithi ya Eli na wanawe, . . . na ‘The Manxman’ ni hadithi ya Daudi na Uria.” (Sisi ndisi tumeongeza maneno ya Kiswahili ili kuonyesha maana.)
Thomas L. Masson, Mwamerika ambaye ni mhariri na mcheshi, alisema haya juu ya jinsi Biblia imesaidia kufanya vitabu vingine viandikwe: “Hiyo ndiyo msingi imara wa vitabu vyetu vyote, kwa hiyo ukitaka kujua jambo lo lote, litafute katika Biblia nawe utalipata. . . . Ina mambo mengi sana yanayoweza kunakiliwa yatumiwe kwa njia nyinginezo, na inaeleza jinsi mwanadamu mwenyewe alivyo pamoja na mawazo yake yote. Hakika inaonyesha vizuri sana hali nyingi za wanadamu.”
Basi, imefaa sana kwamba chapa ya 1971 ya Encyclopædia Britannica inasema Biblia “labda ndicho kitabu chenye kuongoza sana watu kupita vitabu vyote katika historia ya kibinadamu.” Tunaendelea kusoma hivi: “Katika nchi zisemazo Kiingereza, hata watu wawe wana maoni gani juu ya Biblia, mtu akiwa na ufahamu mdogo tu juu ya vitabu vyake na historia yake, hiyo itakuwa alama ya daima kuonyesha kwamba ni mwenye elimu, kwa maana Biblia imeleta maendeleo mengi katika utamaduni wa nchi za magharibi na kufanya utamaduni wa namna nyingi utokee katika nchi za mashariki.”
Biblia imetoa uongozi mpaka vitabu vilivyo vya maana zaidi vikaandikwa katika nchi nyingi za Magharibi, pamoja na vingine vya maana sana vya lugha ya Kiingereza. Mfano mmoja ni vitabu vya Kijeremani. Heinrich Heine anayetunga mashairi ya kuimba na kuchambua vitabu, alisema hivi: “Semi zote na nahau zote zinazopatikana katika Biblia ya Luther zimeandikwa kwa Kijeremani kizuri sana. Zinamvuta mwandikaji aendelee kuzitumia bila kuacha. Na kwa kuwa hata watu walio maskini zaidi wana kitabu hicho, si lazima wawe na elimu nyingi sana ili waweze kutumia maneno ya utaalamu.” Mithali nyingi za Kijeremani zimetolewa katika Biblia, nayo tafsiri ya Luther ya Maandiko Matakatifu ndiyo iliyotegemewa hasa kuandika Kijeremani cha vitabuni.
Inafaa hasa tuangalie maelezo ya waandikaji wawili Wajeremani, Johann Wolfgang von Goethe na Heinrich Heine, kuhusu jinsi Biblia ilivyowasaidia kuandika vitabu. Goethe alisema haya juu ya kazi yake: “Kuiamini Biblia, baada ya kutafakari sana, ndiko kumeniongoza niwe na maisha mema na kuandika vitabu.—Nimeiona kuwa kama rasilmali iliyowekwa mahali salama, yenye kuzaa faida.” Akitoa maelezo yanayopatana na hayo, Heine alisema: “Elimu yangu imetokana na kusoma kitabu fulani.—Kitabu? Naam, nacho ni kitabu cha zamani kilicho cha kikawaida tu; ni kitabu kinachoonekana kuwa chenye faida na cha kikawaida tu kama jua linalotupasha joto, kama chakula kinachotutia nguvu; ni kitabu kinachotusikitikia na kutuonyesha shauku ya upendo kama nyanya mzee, ambaye anakisoma kitabu hicho yeye mwenyewe kila siku, mwenye midomo yenye upendo, yenye kutikisika, miwani yake ikiwa puani.—Nalo jina la kitabu hicho ni la kikawaida tu, yaani, Biblia.”
Watu 40 wenye kuishi katika kipindi cha karibu miaka 1,600 waliwezaje kuandika kitabu cha namna hiyo, kitabu kilichoendelea kuvuta watu muda wa karne nyingi baada ya kumalizwa kuandikwa, hata sasa? Hakuna mmoja wa waandikaji wake aliyejitakia sifa ya kukiandika. Kusudi lao lilikuwa kupitishia watu ujumbe wa Yehova Mungu, aliyewaongoza kwa roho yake, wala hawakutaka kueleza mambo yao wenyewe. Daudi mtunga zaburi alisema hivi: “Roho ya [Yehova] ilinena ndani yangu, na neno lake likawa ulimini mwangu.” (2 Sam. 23:2) Je! maneno hayo hayahakikishwi kuwa ya kweli na mtungo wa ajabu wa Biblia? Basi, je! kitabu hicho hakistahili tukifuate sana?
[Sanduku katika ukurasa wa 3]
Biblia Takatifu
Inavuta watu wa mataifa yote
“Labda ndicho kitabu chenye kuongoza sana watu kupita vitabu vyote katika historia ya kibinadamu”
Sasa inapatikana katika lugha zaidi ya 1,600
“Ndiyo msingi imara wa vitabu vyetu vyote”
Lugha nyingi zimeweza kuandika vitabu kwa sababu ya kitabu hiki tu
Kwa sababu yake, mataifa mazima yamejua kusoma