Sura ya 3
Unaweza Kupata Wapi Uongozi?
NI KITU gani kinachokuzuia usiwe na furaha? Je! ni matatizo uliyo nayo? Huenda yakawa ni ya kibinafsi—yanayohusu afya, fedha, ngono, jamaa yako. Huenda yakawa yanahusu hatari ya kupatwa na uhalifu, kupungukiwa na mahitaji ya maisha, kuvurugwa na kazi unayofanya, kuchukiwa na watu bila sababu, tisho la kutokea vita. Ndiyo, watu walio wengi wana matatizo yanayowaharibia furaha.
2 Wajapokuwa wanadamu walio na elimu na ujuzi mwingi zaidi wamejitahidi sana kuyatatua matatizo hayo, yangali yapo na hata yanazidi. Yaliyoandikwa zamani za kale yamekuwa kweli: ‘Njia ya mwanadamu haimo ndani yake mwenyewe, haimo ndani ya mwanadamu ambaye hutembea kuelekeza hatua zake.’a Je! si wazi kwamba tunahitaji uongozi wa chanzo fulani chenye hekima kuliko mwanadamu ikiwa tunatumaini kupata furaha yenye kudumu? Lakini uongozi huo unapatikana wapi?
3 Watu wengi wanaamini kwamba kwa njia fulani ulimwengu mzima ni ‘kitabu cha uumbaji’ kinachotoa ushuhuda wa kuonyesha kuna Muumba. Mfalme wa kale Mwebrania alikubali jambo hilo, alipoandika hivi: “Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu.” Alisema pia kwamba Muumba amepasha watu habari katika kitabu halisi kilichoandikwa, kinachoweza ‘kumtia mjinga hekima’ na furaha.b
4 Kwa kuwa wanadamu wana uwezo wa kupashana habari—hata kupeleka ujumbe duniani wakiwa, kwenye anga za juu—je! si jambo la akili nzuri kutazamia Muumba wa mwanadamu afanye hivyo pia? Zaidi ya hilo, kwa kuwa kuna mambo mengi yanayohusu dunia, yanayoshuhudia kwamba Yeye anapendezwa na wanadamu, ni jambo wazi kwamba atataka kuwasaidia. Kufanya hivyo kungepatana mambo tunayoona katika jamaa zenye upendo: wazazi wanawapa watoto wao maarifa na uongozi. Lakini ni kwa njia gani Muumba wa mwanadamu angefanya hivyo kwa faida yetu?
5 Kwa muda mrefu kuandika kumekuwa njia bora kabisa ya kupasha watu habari kwa usahihi na kwa udumifu mwingi. Si jambo jepesi sana kumbukumbu lililoandikwa kuwa na makosa mengi kama ujumbe unaoenezwa kote kote kwa mdomo tu. Pia, kitabu kinaweza kuchapwa mara nyingi na kutafsiriwa watu wenye kutumia lugha yo yote wausome ujumbe wacho. Je! si jambo la akili nzuri kutazamia kwamba Muumba wetu ametumia njia kama hiyo kupasha watu habari?
6 Biblia imeonwa kuwa njia ya Muumba wetu ya kupashia watu habari kuliko kitabu kinginecho chote cha kidini, na kwa sababu hiyo imeenezwa kwa njia isiyo na kifani (mfano). Hilo ni jambo la maana sana. Kama Muumba wa wanadamu angetokeza kitabu chenye ujumbe wake kwa wanadamu wote, tungekitazamia kienezwe kote kote. Ndivyo ilivyo Biblia. Inaweza kusomwa kwa lugha nyingi za asilimia (%) 97 ya watu wanaoishi ulimwenguni. Hakuna kitabu kingine cha kidini kimetokezwa na kuenezwa kwa mamia mengi hivyo ya mamilioni ya nakala.
7 Kweli kweli Biblia ndicho kitabu cha kidini kinachowafaa wanadamu wote. Kwa nini? Kwa sababu kilianza kuandikwa karibu na wakati ule ustaarabu ulipokuwa katika hali ya uchanga. Ndicho kitabu kitakatifu kilicho cha pekee kueleza mwanzo wa historia y wanadamu wote. Pia, kinaeleza kusudi la Mungu kuwapa nafasi watu wa “mataifa yote ya dunia” kufurahia baraka za milele.—Mwanzo 22:18.
8 Kitabu Encyclopcedia Britannica kinaiita Biblia “mkusanyo wa vitabu ulio na uvutano mwingi zaidi katika historia ya kibinadamu.” Imepita vitabu vyote vitakatifu kwa kuwa na mavutano na matokeo yenye kuenea sana katika historia. Kwa hiyo, inafaa kusema kwamba hakuna mtu anayeweza kuonwa kuwa amepata elimu kamili ikiwa huyo hajaisoma Biblia.
9 Lakini ajabu ni kwamba watu wengine wameiepuka Biblia. Kwa nini? Mara nyingi sababu inakuwa kwamba mwenendo wa watu na mataifa yanayodhaniwa kuwa yanaifuata Biblia hauwi mwema. Katika nchi fulani-fulani inasemwa kwamba Biblia ni kitabu kinachoelekeza watu vitani, kwamba ni kitabu cha ukoloni, au ni ‘kitabu cha Wazungu.’ Lakini hayo ni maoni yenye makosa. Biblia iliandikwa katika Mashariki ya Kati. Yenyewe haivikubali vile vita vya kikoloni wala unyonyaji wenye pupa ambao umefanywa na watu wakijisingizia kuwa Wakristo. Badala yake, ukisoma Biblia utaona kwamba inakataza sana vita vya kujitafutia faida za kibinafsi tu, inakataza maisha machafu na kutumikisha wengine kwa faida yako mwenyewe. Kosa linawakalia wala pupa, wala si Biblia yenye kosa. (Yakobo 4:1-3; 5:1-6) Kwa hiyo usiache mwenendo mbaya wa watu wachoyo wenye maisha yaliyo kinyume cha mashauri ya Biblia ukuzuie kufaidika na hazina zayo.
UTAKUTA MAMBO YAKIWA NAMNA GANI?
10 Watu wengi wanashangaa wanaposoma Biblia kwa mara ya kwanza. Wanakuta kwamba hicho hasa si kitabu cha sherehe au imani za kidini tu. Wala si mkusanyo wa semi zisizo na maana au falsafa (filosofia) zisizomfaidi sana mtu asiye na maarifa mengi. Badala yake, inazungumza habari za watu halisi waliopatwa na mahangaiko na matatizo yanayofanana na yetu. Pia, inatuonyesha mambo ambayo Mungu anataka tufanye leo kwa kuonyesha namna alivyoshughulika na wanadamu zamani zilizopita. Tunakutia moyo usome kitabu cha mwanzo cha Biblia. Masimulizi yenye kupendeza yaliyomo yatakuwezesha ujue mengi juu ya kusudi la Mungu kwa wanadamu wote. Utakuta humo masomo ya kukuonyesha mambo yanayoweza kuharibia mtu furaha. Pia, utajua tabia na matendo yanayofanikisha mtu na kumpendeza Mungu.
11 Vingine kati ya vitabu 66 vya Biblia vinazungumza historia na utendaji wa kidini wa Israeli wa kale. (Kutoka, Yoshua na Kitabu cha Kwanza cha Samweli ni mifano michache ambayo pasina shaka utafurahia kusoma.) Historia hiyo iliandikwa ili sisi tuweze kufaidika nayo. (1 Wakorintho 10:11) Kwa hiyo, ijapokuwa Mungu haongozi tena taifa fulani moja tu, wala hatazamii mtu ye yote ashike sheria alizowapa Israeli wa kale tu, tunaweza kujifunza mengi kutokana na vitabu hivyo vya Biblia. Na, kama tutakavyoona baadaye mambo ambayo Mungu aliwafanyia Waisraeli (na vile vile dhabihu za wanyama walizomtolea) yana faida kwa maisha zetu.
12 Inakupasa pia usome angaa kitabu kimoja cha masimulizi ya maisha ya Yesu ili uwe na maoni yaliyosawazika juu ya Biblia. Injili fupi ya Marko ni mfano mzuri. Ukiisha kuisoma, furahia kusoma maandishi yenye kusisimua juu ya uanzishaji wa Ukristo katika Matendo ya Mitume. Kisha onja mashauri yanayofaa ambayo Biblia inawapa Wakristo, katika Barua ya Yakobo. Kuonja kidogo sehemu zote mbalimbali za Biblia kutakusaidia ufahamu kwa nini imeheshimiwa sana kwa karne nyingi.
13 Ukisumbuliwa moyoni na mambo machache unayosoma katika Biblia, subiri. Biblia ina mambo mengi ya ndani sana, na ndivyo tungekitazamia kiwe kitabu kilichotolewa na Muumba ili wanadamu wajifunze hicho muda wa karne nyingi. (2 Petro 3:15, 16) Baada ya muda fulani utaona majibu ya maulizo mengi, kwa maana masimulizi ya Biblia yanahusiana. Maulizo yanayotokea unaposoma kifungu kimoja ya tajibiwa na maandiko mengine. Unavyozidi kusoma ndivyo utakavyozidi kuona kwamba Biblia ni kitabu chenye mafaa na chenye kutosheleza. Pia, muda si muda utaona kwamba maneno ya Biblia ni tofauti sana na mafundisho na mazoea ya makanisa yaliyo mengi. Kujua hivyo kutakuchochea utake kuyasoma Maandiko yote, na huenda ukajikuta ukiyarudia-rudia mara nyingi.
BIBLIA—CHANZO CHAKE NI NINI?
14 Inaelekea unawajua watu wanaoiheshimu Biblia kuwa kitabu kizuri au kuwa kitabu chenye hekima ya kikale, lakini wenye maoni ya kwamba kimetokezwa na wanadamu tu, wala si Neno la Mungu. Lakini ukweli unaonyesha nini?
15 Unapoisoma Biblia utaona kwamba kwa kweli wanaume mbalimbali waliyaandika yaliyomo. Musa ndiye wa kwanza, na alianza kuandika mwaka wa 1513 K.W.K. Mwanamume wa mwisho kuiandika alikuwa Yohana mtume wa Yesu, naye aliiandika karibu na mwisho wa karne ya kwanza W.K. Kwa ujumla, vitabu mbalimbali vya Biblia viliandikwa na wanaume wapatao 40. Walikuwa watu wa namna gani? Walikuwa wanyenyekevu, wenye nia ya kufunua wazi makosa yao wenyewe na vilevile ya taifa lao. Tunastahili kuuangalia unyofu wao wa kusema kweli, kwa maana pia walisema kwamba waliandika mambo aliyowaagiza Mungu. Unaweza kuona mifano kwenye 2 Samwel 23:1, 2; Yeremia 1:1, 2 na Ezekieli 13:1, 2. Je! jambo hilo halipasi kutufanya tufikirie kwa uzito uhakikisho tunaopewa na Biblia kwamba “kila andiko limepewa kwa maongozi ya Mungu, na linafaa”?—2 Timotheo 3:16, ZSB; 2 Petro 1:20, 21.
16 Maandishi ya waandikaji wa Biblia ni tofauti na maandishi mengi ya kale katika mambo mengi. Kama anavyojua mwanafunzi ye yote wa historia ya kale maandishi ya Misri, Uajemi, Babeli na ya mataifa mengine ya kale yalikuwa na hadithi za uongo kisha yakaongeza chumvi mno katika kuwasifu watawala wao na shughuli walizotimiza. Lakini, Biblia imejaa kweli na usahihi. Imejaa majina yenye kutajwa wazi, na mambo yanayoweza kuthibitishwa kuwa kweli, hata kuonyesha tarehe yalipotukia. Kwa mfano, Danieli sura ya tano ni kitabu chenye habari za mtawala Mbabeli jina lake Belshaza. Kwa muda mrefu watu wenye kuchambua Biblia walisema hakukuwako mtu kama Belshaza, bali alikuwa mtu wa bandia tu ambaye habari zake ziliandikwa na Danieli. Walakini, miaka ya karibuni mabamba ya udongo yenye maandishi yamefukuliwa ardhini na kutafsiriwa yakikubaliana na maelezo yaliyo katika masimulizi ya Danieli. Kwa sababu hiyo, Profesa R. P. Dougherty (wa Chuo Kikuu cha Yale) aliandika kwamba Biblia ina usahihi mwingi kuliko maandishi mengine, naye anahakikisha kwamba kitabu cha Danieli kiliandikwa wakati ule ule unaotajwa na Biblia.—Kitabu Nabonidus and Belshazzar.
17 Ukisafiri uende Yerusalemu unaweza kupita kati ka mtaro mrefu wa maji uliopasuliwa katikati ya mwamba mgumu. Mtaro huo ulivumbuliwa na kusafishwa takataka zilizokuwamo katika muda wa karne moja tu iliyopita. Kwa nini mtaro huo ni wa maana? Ni kwa sababu unathibitisha ukweli wa yaliyoandi kwa katika Biblia miaka zaidi ya 2,000 iliyopita juu ya maji yaliyoingizwa Yerusalemu na Mfalme Hezekia —2 Wafalme 20:20; 2 Mambo ya Nyakati 32:30.
18 Hiyo ni mifano miwili tu kati ya mifano mingi inayothibitisha kwamba Biblia inatumainika kihistoria na kijiografia. Lakini usahihi tu hautoshi, kwa maana vitabu fulani vya kisasa vya historia ni sahihi. Biblia ina habari ambazo zisingaliweza kuelezwa kama ingalikuwa ni kitabu kilichotokana na wanadamu tu. Habari hizo zimewasadikisha wachunguzi wengi wenye makini kwamba Biblia imetokana na Mtu Mkubwa Kupita Wote.
19 Ingawa Biblia haikuandikwa ikiwa kama kitabu cha kujifunzia sayansi, wakati inapogusa mambo ya kisayansi inakuwa sahihi na kuonyesha maarifa ambayo wanadamu hawakuwa nayo wakati Biblia ilipoandikwa. Kwa mfano, Dakt. Arno Penzias (mshindi wa 1978 wa Zawadi ya Nobel) alisema hivi juu ya asili ya ulimwengu mzima:
“Hoja yangu ni kwamba habari bora zaidi za uhakika tunazoweza kupata zinalingana kabisa na vile mimi ningalitabiri hata kama nisingalikuwa na nyingine za kutegemea isipokuwa vile vitabu vitano vya Musa, Zaburi, Biblia kwa ujumla.”
Zaidi ya hilo, kitabu cha Mwanzo kinapanga namna uhai wa namna mbalimbali ulivyotokea ukiwa katika utaratibu ule ule ambao sasa unakubaliwa na wana sayansi wengi. (Mwanzo 1:1-27) Na ijapokuwa mataifa mengine yalifundisha hadithi za uongo kama ile kusema dunia inashikiliwa na ndovu kadha au jitu fulani nene ili isianguke, Biblia inaonyesha kwa usahihi kwamba dunia inaning’inia bila kutegemea kitu cho chote na kwamba ni ya mviringo. (Ayubu 26:7; Isaya 40:22) Waandikaji wa Biblia walijuaje mambo ambayo ‘yamevumbuliwa’ na wanasayansi majuzi tu? Pasina shaka walipata habari hizo kwenye chanzo kikubwa kuliko wao wenyewe.
20 Kuna jambo la maana hata zaidi linalosaidia kuonyesha asili ya Biblia. Jambo hilo ni unabii. Wanadamu wanaweza kukisia-kisia juu ya matukio yanayokuja, lakini hawawezi kuendelea kuutabiri wakati ujao bila kukosea. (Yakobo 4:13, 14) Lakini Biblia inautabiri. Muda mwingi kabla Babeli haijawa mamlaka ya ulimwengu na kuuharibu mji wa Yerusalemu, Mungu alimfanya nabii Isaya atabiri kwamba Babeli ingeangushwa kwa ushinde. Karne mbili hivi kabla ya hapo, Mungu alimtaja Koreshi kuwa ndiye angekuwa mshindi wa Babeli kisha akaeleza jinsi mji huo ungetekwa nyara. Isaya pia aliandika habari zilizo sahihi kabisa kuhusu kuachwa ukiwa kabisa kwa Babeli, na hali msiba huo ungekuja kutokea baada ya miaka inayozidi 1,000. (Isaya 13:17-22; 44:24-45:3) Yote aliyoandika yalitimia. Na ndivyo ulivyotimia unabii mbalimbali wa Biblia uliohusu Tiro na Ninawi. (Ezekieli 26:1-5; Sefania 2:13-15) Wewe unaweza kutembea ukaone magofu yaliyo katika Mashariki ya Kati ujionee kwa macho yako mwenyewe uthibitisho wa jambo hilo.
21 Kitabu cha Biblia cha Danieli kilitangulia mapema sana kutabiri waziwazi kabisa matukio mengine ya kimataifa. Kilisema Babeli ungeshindwa na Mamlaka ya Wamedi na Waajemi, nayo pia ingekuja kushindwa na Ugiriki. Halafu kiongozi mashuhuri wa Ugiriki (Aleksanda Mkuu) akiisha kufa, wanne kati ya wadogo wake wangeanza kuitawala milki yake. (Danieli 8:3-8, 20-22) Hiyo ni historia ya muda mrefu iliyotangulia kuandikwa mapema, na kwa kweli ilitukia kama ilivyokuwa imetabiriwa. Danieli aliijuaje? Jibu la pekee lenye kuridhisha watu linatolewa katika Biblia yenyewe: “Kila andiko limepewa kwa maongozi ya Mungu.” Jambo hilo linatuhusu sisi, kwa maana kama itakavyozungumzwa katika sura fulani ya baadaye, Biblia ina unabii mbalimbali wa mambo yaliyokwisha kutukia wakati wetu. Tena, inaeleza waziwazi sana mambo ambayo bado yatatimia wakati ujao.c
22 Biblia inatusaidia tuwezane na matatizo ya sasa zaidi ya kuutabiri wakati ujao. Inaeleza kwa nini kuna taabu nyingi sana, na inatusaidia kulifahamu kusudi la kuishi. Inatutolea uongozi wa Muumba juu ya namna tunavyoweza kushinda matatizo na kupata furaha iliyo kubwa zaidi maishani, sasa na wakati ujao. Sura za baadaye zitazungumza mengine ya matatizo ya maisha, na vilevile zitatoa maoni ya Biblia yenye mafaa juu ya namna ya kuyashinda. Walakini, kwanza inatupasa tufahamiane na Yeye ambaye ameyatoa maoni hayo.
[Maelezo ya Chini]
a Yeremia 10:23, Revised Standard Version.
c Ikiwa ungependa kujifunza mengi zaidi yakuhakikishie kwamba Biblia ni kitabu kilichotungwa na Mungu, tafadhali jipatie kitabu kinachoitwa “Is the Bible Really the Word of God?” (“La Bible est-ell, Vraiment la Parole de Dieu?”)
(Mambo ya Kuzungumziwa)
Sababu gani ni jambo linalofaa kwamba Mungu ametolea watu kitabu cha kuwaongoza? (1-5)
Kuna sababu gani za kuisoma Biblia? (6-9)
Ni habari za namna gani zilizo katika Biblia?(10-13)
Ni ushuhuda gani unaoonyesha kama Biblia imetokana au haikutokana na wanadamu tu? (14-19)
Kuna jambo gani la maana sana katika maelezo ya Biblia juu ya matukio ya wakati ujao? (20-22)
[Picha katika ukurasa wa 22]
Setilaiti za wanadamu zinaweza kupelekea watu duniani ujumbe wa namna nyingi. Je! Muumba hawezi kufanya zaidi ya hivyo?
[Picha katika ukurasa wa 23]
Je! si jambo la akili nzuri kutazamia kwamba Mungu angewapa wanadamu kitabu fulani?
[Picha katika ukurasa wa 27]
MTARO WA MAJI WA HEZEKIA
Unaweza kupita katika mtaro huu wa kale wa maji katika Yerusalemu. Unathibitisha Biblia ni sahihi.