Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • pr seh. ya 3 kur. 10-16
  • Chanzo Kisicho na Kifani cha Hekima Bora

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Chanzo Kisicho na Kifani cha Hekima Bora
  • Ni Nini Lililo Kusudi la Uhai?
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kitabu cha Kale Zaidi, Kimeenezwa kwa Wingi Zaidi ya Vyote
  • Usahihi wa Kisayansi
  • Usahihi wa Kihistoria
  • Upatano wa Ndani na Kusema Mambo Wazi
  • Sehemu Yayo Yenye Kutokeza Zaidi
  • Unabii Uliotimizwa
  • Hiyo Hutoa Jibu
  • Mafundisho ya Kweli Yanayompendeza Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Unaweza Kupata Wapi Uongozi?
    Furaha​—Namna ya Kuipata
  • Je, Kitabu Hiki Chaafikiana Na Sayansi?
    Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote
  • Je! Kweli Biblia Ilitoka kwa Mungu?
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
Pata Habari Zaidi
Ni Nini Lililo Kusudi la Uhai?
pr seh. ya 3 kur. 10-16

Sehemu ya 3

Chanzo Kisicho na Kifani cha Hekima Bora

1 Je! Biblia ni rekodi ya hekima hiyo bora? Je! hiyo yaweza kutupatia majibu ya kweli kwa maswali ya maana yanayohusu kusudi la uhai?

2 Kwa hakika Biblia yastahili kuchunguzwa nasi. Sababu moja ni kwamba hicho ni kitabu kisicho cha kawaida kilichopata kukusanywa, kilicho tofauti sana na kitabu kingine chochote. Fikiria mambo ya hakika yafuatayo.

Kitabu cha Kale Zaidi, Kimeenezwa kwa Wingi Zaidi ya Vyote

3 Biblia ni kitabu cha kale zaidi sana kilichopata kuandikwa, sehemu zayo zikiwa zimetungwa miaka ipatayo 3,500 iliyopita. Hiyo ni ya kale kwa karne nyingi kuliko kitabu kingine chochote kinachoonwa kuwa kitakatifu. Vitabu vya kwanza 66 vyayo viliandikwa karibu miaka elfu moja kabla ya Buddha na Konfusho na miaka ipatayo elfu mbili kabla ya Muḥammad.

4 Historia iliyorekodiwa katika Biblia hurudi nyuma hadi mwanzo wa familia ya kibinadamu na hueleza jinsi tulivyokuja kuwa hapa duniani. Hiyo hata huturudisha nyuma hadi wakati wa kabla ya wanadamu kuumbwa, ikitupatia mambo hakika kuhusu kufanyizwa kwa dunia.

5 Vitabu vinginevyo vya kidini, na vile visivyo vya kidini pia, vina nakala chache tu za hati za kale ambazo ziko. Nakala za Biblia karibu 11,000 zilizoandikwa kwa mkono au sehemu zazo zimo katika Kiebrania na Kigiriki, baadhi yazo zikiwa za tarehe inayokaribia ile ya maandishi ya awali. Hizo zimeokoka kujapokuwa na jitihada nyingi za majaribio ya kuangamiza Biblia.

6 Pia, kwa kulinganishwa, Biblia ndicho kitabu ambacho kimepata kuenezwa kwa mapana zaidi sana katika historia. Biblia karibu bilioni tatu au sehemu zayo zimeenezwa katika lugha zipatazo elfu mbili. Inasemekana kwamba asilimia 98 ya familia ya kibinadamu ina Biblia katika lugha yao wenyewe. Hakuna kitabu kingine kinachokaribia mwenezo huo.

7 Kwa kuongezea, hakuna kitabu kingine cha kale kinacholingana na Biblia katika kuwa sahihi. Wanasayansi, wanahistoria, waakiolojia, wanajiografia, wataalamu wa lugha, na wengineo huendelea kuhakiki masimulizi ya Biblia.

Usahihi wa Kisayansi

8 Kwa kielelezo, ingawa Biblia haikuandikwa ikiwa kitabu cha mafunzo ya sayansi, inapatana na sayansi ya kweli inaposhughulika na mambo ya kisayansi. Lakini vitabu vingine vya kale vinavyoonwa kuwa vitakatifu huwa na ngano za kisayansi, makosa, na mambo ya waziwazi yasiyo ya kweli. Ona vielelezo vinne tu kati ya vingine vya usahihi wa kisayansi wa Biblia:

9 Jinsi dunia inavyoning’inizwa angani. Katika nyakati za kale wakati Biblia ilipokuwa ikiandikwa, kulikuwa na kukisia kwingi kuhusu jinsi dunia inavyoning’inizwa angani. Watu fulani waliamini kwamba dunia ilishikiliwa na ndovu wanne waliosimama juu ya kasa mkubwa wa baharini. Aristoto, mwanafalsafa Mgiriki na mwanasayansi wa karne ya nne K.W.K., alifundisha kwamba dunia kamwe haingeweza kuning’inia katika anga tupu. Badala ya hivyo, alifundisha kwamba msingi wa maumbo ya kimbingu ulikuwa juu ya matufe magumu yenye kupenyezwa nuru, kila tufe likiwa kati ya tufe jingine. Ilidhaniwa kwamba dunia ilikuwa katika tufe la ndani zaidi, na tufe la nje kabisa lilishikilia nyota.

10 Hata hivyo, badala ya kuonyesha maoni ya kudhania tu, yasiyo ya kisayansi yaliyokuwako wakati wa kuandikwa kwayo, Biblia ilisema kisahili hivi (karibu mwaka 1473 K.W.K.): ‘Mungu anatundika ulimwengu pasipo kitu.’ (Ayubu 26:7) Katika Kiebrania cha awali, neno linalotumiwa kumaanisha “pasipo kitu” lililotumiwa hapa lamaanisha “bila kitu chochote,” na huu ndio wakati pekee linapotokea katika Biblia. Picha inayotokezwa na Biblia juu ya dunia inayozungukwa na nafasi tupu hutambuliwa na wasomi kuwa ono lenye kutokeza kwa wakati wayo. Buku Theological Wordbook of the Old Testament husema hivi: “Ayubu 26:7 huonyesha kwa njia ya kutokeza ulimwengu kama ulivyojulikana wakati huo kuwa umening’inizwa angani, kwa njia hiyo likitarajia uvumbuzi wa kisayansi wa wakati ujao.”

11 Taarifa sahihi ya Biblia ilitangulia tarehe ya Aristoto kwa miaka zaidi ya 1,100. Hata hivyo, maoni ya Aristoto yaliendelea kufundishwa yakiwa uhakika kwa yapata miaka 2,000 baada ya kifo chake! Hatimaye, katika 1687 W.K., Sir Isaac Newton alichapisha uvumbuzi wake kwamba dunia ilining’inizwa angani kuhusiana na vitu vingine vya kimbingu kwa kuvutana, yaani, nguvu ya uvutano. Lakini hiyo ilikuwa miaka karibu 3,200 baada ya Biblia ikiwa imekwisha kusema kwa usahili unaofaa kwamba dunia inaning’inia “pasipo kitu.”

12 Naam, miaka karibu 3,500 iliyopita, Biblia ilisema kwa usahihi kwamba dunia haina utegemezo unaoweza kuonekana, jambo ambalo linapatana na sheria za nguvu ya uvutano na mwendo ambazo zimeeleweka hivi karibuni. “Jinsi Ayubu alivyojua hiyo kweli,” akasema msomi mmoja, “ni swali lisilojibiwa kwa urahisi na wale wanaokana kupuliziwa kwa Maandiko Matakatifu.”

13 Umbo la dunia. The Encyclopedia Americana kilisema: “Taswira ya kale zaidi ambayo wanadamu walikuwa nayo juu ya dunia ni kwamba ilikuwa jukwaa tambarare, gumu lililo katikati ya ulimwengu wote mzima. . . . Wazo la dunia iliyo mviringo halikukubaliwa na wengi hadi wakati wa Mwerevuko.” Wasafiri-baharini fulani wa mapema hata waliogopa kwamba huenda wakaendesha meli na kuanguka kwenye ukingo wa dunia tambarare. Lakini wakati dira na vitu vinginevyo vya maendeleo vilipotumiwa, hiyo iliwezesha kuwe safari ndefu zaidi za baharini. Hizo “safari za uvumbuzi,” yaeleza ensaiklopidia nyingine, “zilionyesha kwamba ulimwengu ni mviringo, si tambarare kama vile watu wengi walivyokuwa wameamini.”

14 Hata hivyo, muda mrefu kabla ya safari hizo, karibu miaka 2,700 iliyopita, Biblia ilisema hivi: “Yeye ndiye anayeketi juu ya duara ya dunia.” (Isaya 40:22) Neno la Kiebrania lililotafsiriwa hapa “duara” laweza pia kumaanisha “mviringo,” kama vile vitabu mbalimbali vya marejezo vinavyoonyesha. Hivyo, tafsiri nyingine za Biblia husema, “tufe la dunia” (Douay Version) na, “dunia mviringo.”—Moffatt.

15 Hivyo, Biblia haikuathiriwa na maoni yasiyo ya kisayansi yaliyositawi wakati huo kuhusu utegemezo wa dunia na umbo layo. Sababu ni sahili: Mbuni wa Biblia ndiye Mbuni wa ulimwengu wote mzima. Yeye aliumba dunia, kwa hiyo yeye apaswa kujua hiyo inaning’inia juu ya nini na umbo layo ni nini. Hivyo, alipopulizia Biblia, yeye alihakikisha kwamba hakuna maoni yasiyo ya kisayansi yaliyoingizwa humo, hata iwe wengine waliyaamini kwa dhati jinsi gani wakati huo.

16 Muundo wa vitu vilivyo hai. “BWANA [Yehova, NW] Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi,” lasema Mwanzo 2:7. The World Book Encyclopedia husema hivi: “Elementi zote za kemikali zinazofanyiza vitu vilivyo hai zimo pia katika mata isiyo na uhai.” Kwa hiyo kemikali zote za msingi zinazofanyiza viumbe hai, kutia ndani mwanadamu, zinapatikana katika dunia pekee. Hili lapatana na taarifa ya Biblia inayotambulisha vitu ambavyo Mungu alitumia katika kuumba binadamu na vitu vinginevyo vilivyo hai.

17 “Kwa jinsi zao.” Biblia hutaarifu kwamba Mungu aliumba wanadamu wawili wa kwanza na kwamba kutoka kwao binadamu wengine wote walitokea. (Mwanzo 1:26-28; 3:20) Hiyo husema kwamba viumbe vingine hai, kama vile samaki, ndege, na mamalia, vilifanya ivyo hivyo, vikitokea “kwa jinsi zao.” (Mwanzo 1:11, 12, 21, 24, 25) Hivi ndivyo hasa wanasayansi wamepata katika viumbe asilia, kwamba kila kitu kilicho hai hutoka kwa mzazi wa aina yacho. Hakuna njia nyingine. Kuhusu hilo mfizikia Raymo aonelea hivi: “Uhai hufanyiza uhai; hiyo hutukia kila wakati katika kila chembe hai. Lakini kitu kisicho hai kilifanyizaje kitu hai? Ni mojapo maswali makubwa zaidi ya yote yasiyojibiwa katika biolojia, na kufikia sasa wanayoweza kutoa wanabiolojia ni makisio ya hivi-hivi tu. Kwa njia fulani mata isiyo na uhai iliweza kujipanga yenyewe kwa njia ya uhai. . . . Ingawaje, labda mtungaji Mwanzo alieleza jinsi hali ilivyo kwa usahihi.”

Usahihi wa Kihistoria

18 Biblia ina historia ya kale iliyo sahihi zaidi sana kuliko kitabu chochote kilichoko. Kitabu A Lawyer Examines the Bible chakazia usahihi wayo wa kihistoria kwa njia hii: “Ingawa masimulizi ya kimahaba, kihekaya na ushuhuda bandia huepuka kutaja tarehe na mahali pa matukio yanayosimuliwa mahali pa mbali na wakati fulani usio dhahiri, hivyo kuvunja kanuni za kwanza ambazo sisi wanasheria hujifunza juu ya kutetea vizuri kesi mahakamani, kwamba ‘ni lazima usimulizi utaje wakati na mahali,’ masimulizi ya Biblia hutupa sisi tarehe na mahali pa mambo yanayosimuliwa kwa usahihi kabisa.”

19 The New Bible Dictionary chaeleza hivi: “[Mwandikaji wa Matendo] atia usimulizi wake kwa kuambatana na historia ya wakati huo; kurasa zake zimejaa marejezo juu ya mahakimu wa majiji, magavana wa mikoa, wafalme vibaraka, na kadhalika, na marejezo hayo pindi baada ya pindi huthibitika kuwa sahihi kabisa kwa habari ya mahali na wakati unaohusika.”

20 Akiandika katika The Union Bible Companion, S. Austin Allibone asema: “Sir Isaac Newton . . . alikuwa maarufu pia akiwa mhakiki wa maandishi ya kale, na alichunguza kwa uangalifu mkubwa Maandiko Matakatifu. Kauli yake ni nini juu ya jambo hili? ‘Nakuta,’ yeye asema, ‘alama hakika zaidi za uasilia katika Agano Jipya kuliko ilivyo katika historia nyingineyo yote ya kilimwengu.’ Dakt. Johnson asema kwamba tuna uthibitisho zaidi kwamba Yesu Kristo alifia kwenye Kalvari, kama inavyoelezwa katika zile Gospeli, kuliko tulio nao kwamba Kaisari Julius alifia katika Capitol. Hakika, sisi tuna mwingi zaidi.”

21 Chanzo hiki chaongeza hivi: “Muulize yeyote anayedai kuwa anatilia shaka kweli ya historia ya Gospeli yeye ana sababu gani ya kuamini kwamba Kaisari alikufa katika Capitol, au kwamba Maliki Charlemagne alitawazwa kuwa Maliki wa Magharibi na Papa Leo 3 katika 800? . . . Unajuaje kwamba mtu kama Charles 1 [wa Uingereza] alipata kuishi, na alikatwa kichwa, na kwamba Oliver Cromwell akawa mtawala badala yake? . . . Sir Isaac Newton hupewa sifa ya kuwa alivumbua sheria ya nguvu ya uvutano . . . Tunaamini madai hayo yote yanayohusu watu hao; na hiyo ni kwa sababu tuna uthibitisho wa kihistoria wa kweli yao. . . . Ikiwa baada ya kutoa ithibati kama hiyo, wowote bado wakataa kuamini, tunawaacha wakiwa waliopotoka kipumbavu au wajinga wa mwisho.”

22 Ndipo chanzo hicho chamalizia hivi: “Tusemeje basi kuhusu wale ambao, kujapokuwa na uthibitisho mwingi ambao sasa umetokezwa na uasilia wa Maandiko Matakatifu, wajidai kuwa wasiosadikishwa? . . . Hapana shaka tuna sababu ya kutoa mkataa kwamba ni moyo wala si kichwa ambao una kasoro;—kwamba hawataki kuamini yale ambayo huwashushia fahari yao, na ambayo yatawalazimu wawe na maisha tofauti.”

Upatano wa Ndani na Kusema Mambo Wazi

23 Wazia kwamba kitabu fulani kilianza kuandikwa wakati wa Milki ya Roma, kikaendelea kuandikwa katika Enzi za Kati, na kikakamilishwa katika karne hii ya 20, huku waandikaji wengi wakishiriki kukiandika. Ungetazamia matokeo gani ikiwa waandikaji walikuwa wa kazi mbalimbali kama vile askari-jeshi, wafalme, makuhani, wavuvi, wachungaji, na madaktari? Je! ungetazamia kitabu hicho kiwe na upatani na chenye kushikamana? ‘Haiwezekani!’ huenda ukasema. Hata hivyo, Biblia iliandikwa katika hali hizo. Na bado, inapatana kuanzia mwanzo mpaka mwisho, si katika mawazo ya ujumla tu bali pia katika mambo yaliyo madogo sana.

24 Biblia ni mkusanyo wa vitabu 66 vilivyoandikwa katika kipindi cha miaka 1,600 na waandikaji tofauti wapatao 40, kuanzia katika 1513 K.W.K. na kuishia katika 98 W.K. Waandikaji hao walikuwa na njia ya maisha na kazi tofauti, na hawakuwasiliana na waandikaji wengine. Na bado, kitabu kilichotokezwa hufuata kichwa kikuu, kinachoshikamana kotekote, kama kwamba kilitokezwa na mtu mmoja. Na tofauti na itikadi ya wengine, Biblia si kitabu cha utamaduni wa Watu wa Magharibi, lakini iliandikwa na Watu wa Mashariki.

25 Ingawa wengi wa waandikaji wa kale waliripoti mafanikio yao na sifa zao bora tu, waandikaji wa Biblia walikiri waziwazi makosa yao wenyewe, kutia na makosa ya wafalme na viongozi wao. Hesabu 20:1-13 na Kumbukumbu la Torati 32:50-52 hurekodi makosa ya Musa, na yeye aliandika vitabu hivyo. Yona 1:1-3 na 4:1 huorodhesha makosa ya Yona, aliyeandika masimulizi hayo. Mathayo 17:18-20; 18:1-6; 20:20-28; na 26:56 hurekodi sifa mbaya zilizoonyeshwa na wanafunzi wa Yesu. Hivyo, kufuata haki na kusema mambo wazi kwa waandishi wa Biblia huunga mkono dai lao kuwa wamepuliziwa na Mungu.

Sehemu Yayo Yenye Kutokeza Zaidi

26 Biblia yenyewe hufunua kwa nini hiyo ni sahihi sana kisayansi, kihistoria, na katika mambo mengine na kwa nini ina upatano sana na hufuata haki. Hiyo huonyesha kwamba yule Mtu Mkuu Zaidi Sana, Mungu mweza yote, Muumba aliyebuni ulimwengu wote mzima, ndiye Mbuni wa Biblia. Yeye alitumia tu waandikaji wa Biblia wa kibinadamu kuwa waandikaji wake, akiwasukuma kwa kani yake yenye nguvu kuandika yale aliyowapulizia waandike.

27 Katika Biblia mtume Paulo husema hivi: “Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki; ili mtu wa Mungu awe kamili, amekamilishwa apate kutenda kila tendo jema.” Na mtume Paulo alisema hivi pia: “Mlipopata lile neno la ujumbe la Mungu mlilolisikia kwetu, mlilipokea si kama neno la wanadamu, bali kama neno la Mungu; na ndivyo lilivyo kweli kweli.”—2 Timotheo 3:16, 17; 1 Wathesalonike 2:13.

28 Hivyo, Biblia yatoka kwenye akili ya Mtungaji mmoja—Mungu. Na akiwa na uwezo wake mkuu, ilikuwa rahisi kwake kuhakikisha kwamba uaminifu-maadili wa yale yaliyoandikwa ulihifadhiwa hadi kufikia siku yetu. Kuhusu hilo mtaalamu mmoja wa hati za Biblia, Sir Frederic Kenyon, katika 1940, alisema: “Sasa ule msingi wa mwisho wa kuwa na shaka lo lote kwamba Maandiko yametufikia sisi kama yalivyoandikwa umeondolewa.”

29 Wanadamu wana uwezo wa kupeleka ujumbe wa redio na televisheni hadi duniani kutoka maelfu ya kilometa angani, hata kutoka kwenye mwezi. Uchunguzi wa angani umepeleka duniani vitu halisi na picha kutoka kwa sayari zilizo umbali wa mamia ya mamilioni ya kilometa. Hapana shaka Muumba wa mwanadamu, Muumba wa mawimbi ya redio, angeweza angalau kufanya vivyo hivyo. Kwa kweli, lilikuwa jambo rahisi kwake kutumia nguvu yake ya uweza-yote kupeleka maneno na picha kwenye akili za wale aliochagua waandike Biblia.

30 Isitoshe, kuna mambo mengi kuhusu dunia na uhai uliomo yanayodhihirisha kwamba Mungu anapendezwa na ainabinadamu. Kwa hiyo, inaeleweka kwamba yeye angependa kusaidia wanadamu wapate kujua yeye ni nani na kusudi lake kwao ni nini kwa kuonyesha mambo hayo wazi katika kitabu—hati ya kudumu.

31 Fikiria pia, ubora wa kitabu kilichotungwa na Mungu, kwa kulinganisha na habari inayopokezwa na binadamu kwa neno la mdomo. Neno lenye kupitishwa kwa mdomo halingetegemeka, kwa kuwa watu wangefasili ujumbe huo kwa njia tofauti, na baada ya wakati kupita, maana ya habari hiyo ingepotoshwa. Wao wangepitisha habari kwa neno la mdomo kulingana na maoni yao wenyewe. Lakini habari iliyoandikwa kwa kudumu, iliyopuliziwa na Mungu haielekei sana kuwa na makosa. Pia, kitabu chaweza kufanyizwa tena na kutafsiriwa ili kwamba watu wanaosoma lugha mbalimbali waweze kunufaika nacho. Kwa hiyo je, si ni jambo la akili kwamba Muumba wetu alitumia njia hiyo ili kuandaa habari? Kwelikweli, hilo ni jambo la akili hata zaidi, kwa kuwa Muumba asema kwamba hivyo ndivyo alivyofanya.

Unabii Uliotimizwa

32 Kwa kuongezea, Biblia ina alama ya kupuliziwa kimungu katika njia yenye kutokeza isiyo na kifani: Hiyo ni kitabu cha unabii mwingi ambao umepata kutimizwa na unaendelea kutimizwa bila kukosea.

33 Kwa kielelezo, uharibifu wa Tiro la kale, kuanguka kwa Babeli, kujengwa upya kwa Yerusalemu, na kupata umashuhuri na kuangamia kwa wafalme wa Umedi-Uajemi na Ugiriki kulitabiriwa kirefu sana katika Biblia. Unabii huo mwingi ulikuwa sahihi sana hivi kwamba wahakiki fulani walijaribu, bila kufanikiwa, kusema kwamba uliandikwa baada ya mambo hayo kutukia.—Isaya 13:17-19; 44:27–45:1; Ezekieli 26:3-6; Danieli 8:1-7, 20-22.

34 Unabii mwingi ambao Yesu alitoa kuhusu kuharibiwa kwa Yerusalemu katika 70 W.K. ulitimizwa kwa usahihi. (Luka 19:41-44; 21:20, 21) Na unabii mwingi uliotolewa na Yesu na mtume Paulo kuhusu “siku za mwisho” unatimizwa katika kila jambo dogo katika wakati huu wetu.—2 Timotheo 3:1-5, 13; Mathayo 24; Marko 13; Luka 21.

35 Hakuna akili ya kibinadamu, ambayo hata iwe yenye weledi kivipi, ingeweza kutabiri matukio ya wakati ujao kwa usahihi hivyo. Ni akili tu ya Muumba mwenye nguvu zote na mwenye hekima yote wa ulimwengu wote mzima ambayo ingeweza, kama tusomavyo kwenye 2 Petro 1:20, 21: “Maana unabii haukuletwa po pote kwa mapenzi ya mwanadamu; bali wanadamu walinena yaliyotoka kwa Mungu, wakiongozwa na Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW].”

Hiyo Hutoa Jibu

36 Hivyo, katika njia nyingi, Biblia hutoa uthibitisho wa kuwa Neno lililopuliziwa la Mtu Mkuu Zaidi Sana. Hivyo, hutuambia kwa nini wanadamu wapo duniani, kwa nini wanadamu wanateseka sana, kule tunakoelekea, na jinsi hali zitakavyobadilika na kuwa bora. Hiyo hutufunulia kwamba kuna Mungu mkuu zaidi sana aliyeumba wanadamu na dunia hii kwa kusudi fulani na kwamba kusudi lake litatimizwa. (Isaya 14:24) Biblia pia hutufunulia dini ya kweli ni nini na jinsi tunavyoweza kuipata. Hivyo, hiyo ndiyo chanzo pekee cha hekima bora ambacho chaweza kutuambia kweli kuhusu maswali ya maana juu ya uhai.—Zaburi 146:3; Mithali 3:5; Isaya 2:2-4.

37 Ingawa kuna ithibati nyingi juu ya uasilia na ukweli wa Biblia, je, wote wanaosema kwamba wanaikubali hufuata mafundisho yayo? Fikiria, kwa mfano, mataifa yanayodai kuwa hujizoeza Ukristo, yaani, Jumuiya ya Wakristo. Yamekuwa na Biblia kwa karne nyingi. Lakini je, kufikiri kwayo na matendo yayo yanaonyesha kwelikweli hekima bora ya Mungu?

[Maswali ya Funzo]

1, 2. Kwa nini twapaswa kuichunguza Biblia?

3, 4. Biblia ina umri gani?

5. Ni hati ngapi za kale za Biblia ambazo ziko, zikilinganishwa na maandishi ya kale ya kilimwengu?

6. Biblia imeenezwa kwa mapana kadiri gani?

7. Ni nini laweza kusemwa kuhusu usahihi wa Biblia?

8. Biblia ni sahihi jinsi gani katika mambo ya sayansi?

9, 10. Badala ya kuonyesha maoni yasiyo ya kisayansi ya wakati wayo, Biblia ilisema nini kuhusu utegemezo wa dunia?

11, 12. Ni wakati gani wanadamu walipokuja kuelewa kweli ya Ayubu 26:7?

13. Watu walifikiri umbo la dunia likoje karne zilizopita, lakini ni nini kilichobadili akili yao?

14. Biblia ilielezaje umbo la dunia, na lini?

15. Kwa nini Biblia haikuathiriwa na maoni yasiyo ya kisayansi kuhusu dunia?

16. Muundo wa vitu vilivyo hai hukubalianaje na taarifa ya Biblia?

17. Ni nini iliyo kweli kuhusu jinsi vitu vilivyo hai vilikuja kuwako?

18. Mwanasheria mmoja asema nini kuhusu usahihi wa kihistoria wa Biblia?

19. Chanzo kimoja kinasemaje kuhusu mambo ya kihistoria ya Biblia?

20, 21. Msomi mmoja wa Biblia asema nini kuhusu historia ya Biblia?

22. Kwa nini watu fulani hukataa kukubali uasilia wa Biblia?

23, 24. Kwa nini upatano wa ndani wa Biblia ni jambo lisilo la kawaida?

25. Kufuata haki na kusema mambo wazi kwa waandikaji wa Biblia huunga mkono dai gani lao?

26, 27. Kwa nini Biblia ni sahihi sana katika mambo ya kisayansi na mambo mengineyo?

28. Hivyo basi, Biblia yatoka wapi?

29. Uwezo wa Mungu wa kuwasiliana waweza kutolewaje kielezi?

30. Je! Mungu ataka wanadamu wajue kusudi lake ni nini kwao?

31. Kwa nini ujumbe wenye kupuliziwa ambao ukarekodiwa ni bora zaidi ya habari inayopokezwa kwa mdomo?

32-34. Biblia ina nini ambayo hakuna kitabu kingine kinayo?

35. Kwa nini unabii wa Biblia waweza kuja tu kutoka kwa Muumba?

36. Biblia hutuambia nini?

37. Ni jambo gani ambalo lazima liulizwe kuhusu Jumuiya ya Wakristo?

[Picha katika ukurasa wa 11]

Sir Isaac Newton aliamini kwamba dunia ilining’inizwa angani kuhusiana na vitu vingine vya kimbingu kwa nguvu ya uvutano

Picha inayotokezwa na Biblia juu ya dunia inayozungukwa na nafasi tupu hutambuliwa na wasomi kuwa ono lenye kutokeza kwa wakati wayo

[Picha katika ukurasa wa 12]

Wasafiri-baharini fulani wa mapema hata waliogopa kwamba huenda wakaendesha meli na kuanguka kwenye ukingo wa dunia tambarare

[Picha katika ukurasa wa 13]

Kuna uthibitisho zaidi kwamba Yesu Kristo alikuwako kuliko vile kulivyo kwamba Kaisari Julius, Maliki Charlemagne, Oliver Cromwell, au Papa Leo 3 waliishi

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kutimizwa kwa unabii mwingi ambao Yesu alitoa kuhusu kuharibiwa kwa Yerusalemu katika 70 W.K. kunathibitishwa na Tao la Tito katika Roma

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki