Hekima ya Kujitia Adabu
NI NANI ambaye hajaona polisi akimshika dereva wa motokaa ambaye amevunja sheria ya barabarani, kama vile kuendesha motokaa sana kupita mwendo ulioruhusiwa? Huo unaweza kuwa mfano wa dereva kushindwa kujitia adabu. Huenda alijiachilia ashindwe na jaribu la kutii sheria za barabarani, na kwa hiyo ilikuwa lazima aadibiwe.
Sheria ambazo ziko ndani ya miili yetu ambazo zinatuongoza tufanye mambo fulani zinatuadibu tusipojiadibu sisi wenyewe. Mwandikaji wa Mithali aliyeongozwa na Mungu anatwambia: “Ni nani apigaye, yowe? Ni nani aliaye, ole? . . . Ni nani aliye na jeraha zisizo na sababu? . . . Ni wale wakaao sana kwenye mvinyo; waendao kutafuta divai iliyochanganyika.” Bila shaka, mojawapo vichwa vikuu vya kitabu cha Mithali ni hekima ya kujitia adabu.—Mit. 23:29-35.
Jambo lililokuwa kweli kwa watu mmoja mmoja vilevile lilitumika kwa taifa zima la watu. Mwingereza mashuhuri (mwenye sifa) wa karne ya 18 alisema hivi: “Watu wanapewa uhuru wa kiraia kwa kadiri wanavyoweza kuzuia tamaa yao inayohusu mema na mabaya.” Alisema jambo la maana kwamba ‘jamii haiwezi kuendelea kuwako isipokuwa kuweko na nguvu yenye kuzuia nia na tamaa, watu wasipojizuia wenyewe, watazuiwa na serikali, kwa ajili ya amani na usalama.’ Kumekuwako na mifano yenye kutokeza ya jambo hili wakati watu wanaofurahia serikali ya kidemokrasi wanapokuwa wavunjaji wa sheria sana hata kunakuwa na lazima ya mtawala mwenye kutumia nguvu mwenye mamlaka peke yake achukue mamlaka. Lingekuwa jambo la hekima zaidi sana namna gani kwa watu wajizuie mahali pa kupoteza uhuru unaopendwa sana!
Kama mfano wa kisasa: Katika masika ya mwaka 1974 serikali fulani zilitisha kwamba zingechukua hatua ya kupimia watu vitu na kuweka bei ya vitu ikiwa watu na viwanda hawatajizuia katika matumizi yao.
SABABU SOTE TUNAHITAJI ADABU
Tunaposema adabu tunakuwa na maana gani? Neno la jina (noun) “adabu” linafasiriwa kama “mazoezi, sana sana ya akili na utu; . . . adhabu; mapigo.” Na namna ya kiarifa (verb) ya neno hilo inamaanisha “kuzoeza; kuleta katika hali ya utaratibu na utii; tiisha.”
Mara nyingi sana Biblia inatuonyesha sababu sisi sote tunahitaji adabu mara kwa mara. Yote yalianza huko nyuma wazazi wetu wa kwanza walipokosa kutii kwa kupenda. Hii ndiyo sababu “mawazo ya moyo wa mwanadamu ni mabaya tangu ujana wake.” (Mwa. 8:21) Vilevile ndiyo sababu Mfalme Daudi, angeweza kumsihi Yehova hivi alipofanya dhambi nzito: “Tazama, mimi naliumbwa katika hali ya uovu; mama yangu alinichukua mimba hatiani.”—Zab. 51:5.
Kwa kufaa neno la Mungu linashauri hivi: “Ujinga umefungwa ndani ya moyo wa mtoto; lakini fimbo ya adhabu itaufukuzia mbali.” “Usimnyime mtoto wako mapigo; maana ukimpiga kwa fimbo hatakufa. Utampiga kwa fimbo, na kumwokoa nafsi yake na kuzimu.”—Mit. 22:15; 23:13, 14.
Kwa sababu ya makosa yao waliyorithi, kukosa maarifa kwao pamoja na ujuzi, Wakristo wanashauriwa wawe na nia ya kukubali adabu inayotolewa kwao na Baba yao wa mbinguni: “Usiyadharau marudia ya [Yehova], wala usizimie moyo ukikemewa naye; maana yeye ambaye [Yehova] ampenda, humrudi, naye humpiga kila mwana amkubaliye. . . . Tulikuwa na baba zetu . . . walioturudi, . . . kama walivyoona vema wenyewe; bali yeye [Yehova anafanya hivyo] kwa faida yetu, ili tushiriki utakatifu wake. [Kweli,] kila adhabu wakati wake haionekani kuwa kitu cha furaha, bali cha huzuni; lakini baadaye huwaletea wao waliozoezwa nayo matunda ya haki yenye amani.”—Ebr. 12:5-11.
SABABU KUJITIA ADABU NI JAMBO LA HEKIMA
Kujitia adabu ni mwendo wa hekima kwa sababu unamwezesha mtu awe na dhamiri njema. Mtu anayejitia adabu kwa kuwa na mazoea mazuri kazini pake na kuifanya vizuri akiongozwa na dhamiri yake, ataridhika kwa kuwa na dhamiri njema. Si kitu kama anatazamwa na bwana yake ama hatazamwi—ndiyo, kwamba mtu mwingine atajua tofauti hiyo au sivyo, isipokuwa yeye mwenyewe na Mungu.—Kol. 3:23.
Vilevile hiyo ni kweli kuhusu ushirika wetu na wengine. Mtu anayeshinda jaribu la kusema hata uongo kidogo atakuwa na dhamiri njema zaidi ya yule asiyejitahidi kutosema uongo anapokuwa chini ya mkazo.—Efe. 4:25.
Kwa kweli, ayo hayo ni lazima yasemwe juu ya mwenendo unaowapasa wanaume na wanawake. Kujitia adabu ndiko kunakomwezesha mtu azuie akili zake zisifikiri juu ya mambo machafu, ajiepushe na vitabu na magazeti yanayoonyesha na kuzungumza mambo ya umalaya, apinge jaribu la maongezi ya uchumba bila nia, na kuchezea uasherati. Walakini bila shaka ni mwendo wa hekima kwa yeye awezaye kusema kama alivyosema mtume Paulo: “Mimi kwa dhamiri safi kabisa nimeishi mbele za Mungu hata leo hivi.”—Matendo. 23:1.
Yesu alipendekeza kwetu mwendo wa kujitia adabu aliposema: “Na mkono wako ukikukosesha ukate; ni afadhali kuingia katika uzima u kigutu, kuliko kuwa na mikono miwili, na kwenda zako jehanum.” “Na mguu wako ukikukosesha,” “Na jicho lako likikukosesha,” fanya vivyo hivyo na viungo hivi vya mwili wako.—Marko 9:43-48.
Kila mmoja wetu anajua ulipo udhaifu wake. Huenda wengine wasithamini uthabiti wetu katika mambo mengine, lakini sisi mmoja mmoja tunajua sehemu tunazotakiwa kujitia adabu ili kumpendeza Mungu. Mtume Paulo aliweka mfano mzuri kwetu, kwa kuwa ‘aliutesa mwili wake akautumikisha ili akiisha kuwahubiri wengine asiwe mtu wa kukataliwa.’—1 Kor. 9:27.