Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 9/1 kur. 21-23
  • Je! Imani Yako I Hai?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Imani Yako I Hai?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Habari Zinazolingana
  • Kwa Nini Mungu Aliwaamuru Waisraeli Wapigane Vita na Wakanaani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • “Imani Iliyotenganishwa na Matendo Imekufa Kama Mzoga”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Onyesha Imani Yako Katika Ahadi za Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2016
  • Jifunze Kutokana na Makosa ya Waisraeli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 9/1 kur. 21-23

Je! Imani Yako I Hai?

IMANI ni sifa ya kimungu inayohitajiwa sana. (Yohana 3:16; 2 Kor. 5:7; Ebr. 10:38) Lakini imani ni zaidi ya kuamini tu. “Wataka kujua, wewe mwanadamu usiye kitu,” auliza Yakobo mwandikaji wa Biblia, “kwamba imani pasipo matendo haizai?” (Yak. 2:20) Anaongeza hivi: “Maana kama vile mwili pasipo roho umekufa, vivyo hivyo na imani pasipo matendo imekufa.” (Yak. 2:26) Imani ya Mkristo, haiwezi kusimama mahali pamoja, lakini kama vile majani yanavyoipamba nchi na kuifanya ionekane nzuri, lazima imani iendelee kuwa hai na iendelee kukua.​—2 The. 1:3.

Tunaweza kujifunza somo la maana juu ya jambo hili kutokana na vile Israeli wa kale walivyoitikia wakati Mungu alipoahidi kuwapa nchi ya Kanaani. Mungu aliwajulisha kwamba angewapa msaada wake unaoshinda wa kibinadamu, akasema:

“Tazama, mimi namtuma malaika aende mbele yako, ili akulinde njiani na kukupeleka mpaka mahali pale nilipokutengezea. Jitunzeni mbele yake, mwisikize sauti yake, wala msimtie kasirani; maana, hatawasamehe makosa yenu; kwa kuwa jina langu limo ndani yake. Lakini ukiisikiza sauti yake kweli, na kuyatenda yote ninenayo mimi; ndipo mimi nitakuwa ni adui wa adui zako, na mtesi wa hao wakutesao.”​—Kut. 23:20-22.

Israeli walikuwa na wajibu wa kufanya kazi pamoja na Mungu katika kuwaangamiza Wakanaani. Mungu aliamuru hivi: “Nawe utawapiga; wakati huo ndipo uwaondoe kabisa; usifanye agano nao, wala kuwahurumia; wala usioane nao.”​—Kum. 7:2, 3.

Baada ya Israeli kuingia Nchi ya Ahadi na kupiga kambi katika Gilgali, mashariki mwa Yeriko, malaika, aliyejisema kuwa “amiri wa jeshi la [Yehova],” alimtokea Yoshua. Malaika huyu alimfunulia kwamba Mungu angefanya kuta za Yeriko zianguke kwa mwujiza. Na zilianguka! (Yos. 5:13​—6:27) Ulikuwa wonyesho wenye kutia imani nguvu namna gani kwamba Mungu alikuwa akijionyesha ‘kuwa adui wa adui za Israeli’!

Lakini hayakuwa hayo tu! Chini ya uongozi wa malaika amiri wa Yehova, mji baada ya mji ulianguka mbele za Yoshua na Waisraeli. (Yos. sura 6, 10, 11) Watu wa Mungu walipewa msingi imara wa kuwa na bidii katika kufuata agizo la kimungu mpaka mwisho la kujitwalia nchi kutoka kwa Wakanaani. Lakini je! walitii kiasi cha kuendeleza imani yao hai kabisa?

Hapana, kwa sababu baadaye Biblia inataja kwamba yule malaika wa Mungu alionekana tena, wakati huu akiwa na ujumbe wenye kuhuzunisha. Tunasoma hivi:

“Kisha malaika wa [Yehova] alikwea juu kutoka Gilgali kwenda Bokimu. Akasema, Mimi nimewaleta ninyi mkwee juu kutoka nchi ya Misri, nami nimewaleta hata nchi niliyowaapia baba zenu; nami nilisema, Mimi milele sitalivunja hilo agano langu nililoagana nanyi; nanyi msifanye agano lo lote na hawa wenyeji wa nchi hii; zipomosheni nchi madhabahu zao; lakini hamkuisikia sauti yangu; je! mmefanya haya kwa sababu gani? Basi kwa ajili ya hayo mimi nilisema zaidi, Mimi sitawafukuza watoke mbele zenu; lakini watakuwa kama miiba mbavuni mwenu, na miungu yao itakuwa ni tanzi kwenu.”​—Amu. 2:1-3.

Yakionyesha jinsi Israeli ‘hawakumsikia’ Mungu, Maandiko yanaeleza kwamba kabila la Yuda lilishindwa kuwafukuza wenyeji wa sehemu fulani ya upande wa kusini wa Kanaani “kwa kuwa [wenyeji hao] walikuwa na magari ya chuma.” (Amu. 1:19) Kwa wazi magari haya ya chuma yaliliogopesha kabila la Yuda. Baada ya hapo makabila ya Benjamini, Manase, Efraimu, Zebuloni, Asheri, Naftali na Dani vilevile walishindwa kuwafukuza wenyeji waliokaa miji mingi ya Kanaani. Badala yake, walikubali kukaa kati ya Wakanaani, wakawatumikisha wengine wao “kazi ya shokoa.”​—Amu. 1:21-36.

Ingawa Israeli walijidai waziwazi kuwa na imani katika Yehova na hapo mwanzoni walikuwa wamekubali kuyatenda ‘yote aliyoyasema Yehova,’ mara nyingi matendo ya kimungu yakionyesha kwamba imani yao ilikuwa hai yalikosekana. (Kut. 19:8; 24:3-7) Mwenendo wao wa kukosa imani uliwaletea huzuni badala ya kuwaletea faida. Kuhusu (juu ya) kemeo la malaika kwa Israeli katika Bokimu, Biblia inasema hivi: “Ikawa, hapo huyo malaika wa [Yehova] alipoyanena maneno haya, kuwaambia wana wa Israeli wote, ndipo hao watu wakainua sauti zao na kulia. Nao wakaliita jina la mahali pale Bokimu; [maana yake, “waliaji”]”​—Amu. 2:4, 5.

Na matokeo mabaya zaidi yalifuata. Kukaa kati ya Wakanaani wapotovu kuliwatega Israeli katika kufuata ibada ya sanamu, kuwatolea mashetani watoto wao sadaka na zaidi kumwaga damu nyingi isiyo na hatia. Kwa sababu hii, hasira ya Yehova iliwaakia.​—Zab. 106:34-42.

Wakristo leo wanaweza kujifunza nini kutokana na matukio haya ya historia ya Biblia? Ingawa hawakuamriwa wawafukuze watu halisi, Wakristo wana kazi gumu ambayo ni lazima waimalize, ambayo wanaifanya katikati ya watu wasiomwabudu Yehova. Yesu aliwaagiza wanafunzi wake wazihubiri “habari njema” za ufalme wa Mungu duniani pote, ‘waende wakafanye wanafunzi kutoka watu wa mataifa yote.’​—Mt. 24:14; 28:19, 20, NW.

Je! wewe unatii na kushiriki katika utendaji huu wa kuhubiri ufalme na kufanya wanafunzi? Maandiko yanatoa uhakika wa kwamba malaika wanasaidia katika kazi hii na kwamba itamalizwa kama anavyotaka Mungu. (Ufu. 14:6) Kama inavyoonyeshwa hapo juu, Israeli wa kale walishindwa kuonyesha imani na bidii katika kutimiza amri ya Mungu ya kuwaangamiza Wakanaani. Vivyo hivyo Wakristo wanapaswa wajiangalie wasipoe katika bidii yao katika kazi ambayo Yesu aliwaagiza wafuasi wake waifanye.

Linalolingana na amri ya Mungu kwamba Israeli ‘wasifanye agano’ na Wakanaani, Wakristo wana amri hii: “Msifungwe nira pamoja na wasioamini. . . . Tokeni kati yao, mkatengwe nao, asema [Yehova], msiguse kitu kilicho kichafu.” (2 Kor. 6:14-17) Je! wewe umeonyesha kwamba imani yako i hai kwa kujitenga na uchafu wote wa ulimwengu?

Kutokutii Mungu kwa Israeli wa kale kwa kukosa imani kuliwaletea kemeo na kilio katika Bokimu. Kukosa imani kama huko leo kunaweza kuongoza kwenye namna mbaya hata zaidi ya kilio. Namna gani hivyo?

Kutimizwa ulimwenguni pote kwa “ishara” ambayo Yesu alitoa kunaonyesha kwamba tangu mwaka 1914 tumekuwa tukiishi wakati wa ‘kuwapo kwa Kristo na wa mwisho wa taratibu [iliyopo] ya mambo.’ (Mt. 24:3—25:46, NW) Kwa hiyo Yesu alikuwa akisema juu ya kizazi hiki cha wakati huu aliposema katika mojawapo mifano yake hivi: “Hivyo ndivyo itakavyokuwa katika mwisho wa dunia [“taratibu ya mambo,” NW] ; malaika watatokea, watawatenga waovu mbali na wenye haki, na kuwatupa katika tanuru ya moto; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno.”​—Mt. 13:49, 50; 24:3, 34.

Kulingana na Maandiko, hiyo “tanuru ya moto” ni mfano wa “maangamizi ya milele” kwa waovu wakati wa kulipiza “kisasi wao wasiomjua Mungu, na wao wasiotii Injili ya Bwana wetu Yesu.” (2 The. 1:6-10) Kwa upande mwingine, kuokoka na kuingia katika taratibu mpya yenye haki ndilo tumaini lenye furaha la wale wanaozitii habari njema, watu wale ambao imani yao katika Mungu na Yesu Kristo inang’aa katika matendo wanayoyafanya siku baada ya siku, ambayo msingi wake ni Biblia. (2 Pet. 3:13; Ufu. 21:1-5) Je! imani yako i hai namna hiyo?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki