“Acha Dhamiri Yako Ikuongoze”
KATIKA mambo ya uhusiano wa kibinadamu, hasa wakati watu wanapopaswa kushughulika na wenzao kwa unyofu na haki, mara nyingi wanaambiwa hivi: “Acha dhamiri yako ikuongoze.” Mtu mwenye kushauri mwenzake hivyo anafanya hivyo kwa kutikisa mabega, kwanza kwa sababu anasita-sita kumpa shauri linalofaa na pili kwa sababu anadhani mwenzake hatafuata shauri lake hata akimpa.
Usemi huo umetumiwa sana hata maana yake ikaharibika. Sasa usemi huo unakaribia kuwa sawa na kusema kwamba, ‘Fanya lo lote litakaloachiliwa na dhamiri yako.’ Huenda dhamiri ya mtu ikawa na mashaka fulani juu ya jambo fulani, lakini huenda akaipinga na kutafuta njia ya kutetea tendo lisilofaa au la udanganyifu, huku akiituliza dhamiri yake na kuipa kisababu cha kulifanya jambo hilo.
Mtu akianza kuwaza hivyo, anaweza kusitawisha dhamiri ‘iliyochomwa moto,’ nayo haiwezi kumwongoza hata kidogo. Ni kama ngozi ambayo imekuwa na kovu kwa sababu ya kuungua sana, isiyoweza kuona maumivu yo yote iweze kumwonya mwenyewe aepuke hatari. (1 Tim. 4:2) Kwa kuwa jambo hilo linaweza kutokea, haifai mtu ye yote afuate usemi uliotangulia kutajwa, bali inafaa afuate shauri hili jema: Usichafue dhamiri yako kamwe.
Watu wengi wana dhamiri inayowaonya upesi kuhusu mambo mengi ya maisha. Lakini huenda dhamiri ya mtu isimwongoze nyakati zote katika njia iliyo bora, njia inayokwenda uzimani. Hiyo ni kwa sababu huenda dhamiri yetu ikawa haitegemei kanuni zinazofaa za Mungu, ingawa ndiyo inayotuamulia mambo, kutufasiria kanuni na sheria na kutuonyesha njia tunayoamini inafaa tuzitumie kanuni na sheria hizo.
Kwa mfano, desturi ya nchi fulani ni kuoa wanawake wengi. Watu wa huko wamekuwa na mazoea hayo tu. Lakini wakiisha jua yanayosemwa na Biblia, wanaona kwamba kuoa wanawake wengi ni kinyume cha mpango ambao Mungu amewekea Wakristo. Basi wanabadili dhamiri na maisha yao.
Wako pia Wakristo fulani wenye udhaifu mbalimbali katika imani yao, yaani, hawafahamu vizuri mambo fulani yanayohusu adili na mwenendo. Wanahitaji kufundishwa wafahamu waziwazi kanuni mbalimbali na jinsi zinavyotumika, ili ‘akili zao zipate kuzoezwa kupambanua mema na mabaya.’—Ebr. 5:14.
Kwa hiyo, lazima sote tuzoeze dhamiri yetu ili ifanye maamuzi yanayotegemea sana Neno la Mungu. Inatupasa tufanye mabadiliko tupashwapo habari, wala tusiwe ‘wajinga kwa makusudi.’ (2 Pet. 3:5, Authorized Version) Kwa kufanya hivyo tu ndipo tuwezapo kusalimika kwa ‘kuacha dhamiri yetu ituongoze.’ Vilevile hatutaki kufanya dhamiri yetu wenyewe iongoze mtu mwingine. Ingawa tunaweza kutumia Biblia tusaidie mtu mwingine afahamu waziwazi mambo fulani kulingana na kanuni kuu, inatupasa tumpe uhuru ule ule tunaotaka kupewa na wengine, bila kujaribu kumwongozea dhamiri yake, maana tunaweza kumwumiza, kumzuia asiwe na dhamiri njema mbele za Mungu.—1 Kor. 8:12.