Je! Wewe Unaongozwa na Dhamiri Nyepesi ya Kikristo?
1. Kweli ya Biblia imebadilije watu?
WATU wengi ambao wamekuwa Wakristo wamefanya mabadiliko makubwa sana. Watu waliokuwa katika Korintho wa kale ambao wakawa Wakristo walikuwa wamekuwa waasherati, waabudu sanamu, wanaume wenye kulalana na wanaume wenzao na wanawake wenye kulala wanawake wenzao, wezi na walevi. Lakini waliposikia kweli ya Neno la Mungu na kuitumia, walibadilika ‘wakaoshwa.’ (1 Kor. 6:9-11) Je! wewe unajua watu wo wote ambao wamefanya mabadiliko kama hayo? Pengine wewe mwenyewe umefanya hivyo kwa msaada wa Mungu.
2. Neno la Mungu lina matokeo gani juu ya dhamiri ya mtu, na kwa sababu gani hii inafaidi?
2 Ni vema namna gani wakati watu wanaovutwa na ujumbe wa Kikristo wanapoacha kuwa kama wanaoelezwa katika Tito 1:15: “Hakuna kilicho safi kwao walio wanajisi, wasioamini; bali akili zao zimekuwa najisi, na [dhamiri] zao pia.” Lakini, zaidi ya kuepuka makosa mabaya sana ya adili tu, wakati mtu anapojifunza sheria na kanuni za Mungu anakuza dhamiri nyepesi zaidi. Je! dhamiri yako mwenyewe haikuwa yenye kuitikia zaidi kadiri ambavyo umeongeza maarifa na kuthamini mapenzi na utu wa Mungu? Hili ni jambo lenye kupendeza sana. Kuwa na dhamiri ya Kikristo yenye wepesi unaofaa na kuiitikia kunaweza kukusaidia upate upendeleo wa Mungu, kunaweza kufanya maisha yako yawe yenye amani zaidi, kukikuepusha na maumivu ambayo mara nyingi yanawapata wale walio na dhamiri najisi, nako kunaweza kukusaidia uishi maisha yanayoonyesha Ukristo wa kweli.—Linganisha 1 Petro 3:21.
DHAMIRI—YENYE WEPESI WA KADIRI GANI?
3. Wakristo wanataka kuepuka nini kwa habari ya dhamiri?
3 Bila shaka, sisi kama Wakristo hatutaki kuwa na dhamiri “najisi” au ‘iliyounguzwa,’ kwa maana dhamiri kama hiyo isingefaa lo lote katika kutusaidia tuonyeshe mfano wa Mungu. (Efe. 4:19) Kwa upande mwingine, dhamiri yetu haipaswi kuwa nyepesi kwa njia ya kupita kiasi au kwa njia isiyosawazika; kwa kuwa tu wanadamu wasiokamilika, hilo linaweza kutukia tusipojiangalia.
4. Dhamiri nyepesi kupita kiasi au isiyosawazika inaweza kumwongoza mtu atendeje juu ya kodi?
4 Kwa mfano, mtu anaweza kuwa anajua kwamba Yehova haungi mkono vita vya mataifa, bali kwamba yeye anaomba watu wake wajifunze njia za amani. (Isa. 2:4) Akiwa anajua kwamba mataifa kwa kawaida yanasaidia majeshi yao kwa pesa zinazotolewa kodi, je! ingekuwa sawa na ingelingana na Maandiko dhamiri yake ikimwongoza akatae kulipa kodi? Au ingekuwa sawa akilipa kodi zake bila kulipa kiasi fulani cha pesa kinacholingana na ambacho serikali inatumia katika gharama zake za kununua silaha za vita za kujilinda? Ingawa watu fulani wamefuata maoni hayo, ushuhuda wa Biblia unapinga dhamiri inayoongoza kwenye mwendo huo. Wakristo wanaambiwa waziwazi walipe kodi zao, na jambo hili liliandikwa katika Biblia ijapokuwa serikali ya Kirumi iliyokuwako wakati huo ilikuwa na jeshi kubwa sana la kulisha. (Mt. 22:17-21; Rum. 13:1, 7) Hivyo Mkristo anaweza kulipa kodi zake akiwa na dhamiri safi iliyosawazishwa na Neno la Mungu, na kuachia serikali daraka la namna pesa hizo zitakavyotumiwa.
5, 6. (a) Kwa upande mwingine, dhamiri nyepesi inavyofaa imepaswa imwongozeje mtu katika habari hii? (b) Biblia inaonyeshaje hili?
5 Kwa njia ii hii, shauri hili la Biblia limepaswa liongoze dhamiri ya mtu hata alipe kodi zake zote. Je! hivyo ndivyo dhamiri yako inavyokuongoza ufanye? Au dhamiri yako imeongozwa na maoni yaliyoenea sana ya kutolipa kodi yote kwa kutotaja mapato yote ya mtu au kutotaja bidhaa zote zinazopaswa kulipiwa kodi? Kwa mfano, ikiwa hali zako zimebadilika—pengine watoto walioa wakatoka kwako, hiyo ikiwa na maana ya kwamba utakuwa ukilipa kodi za juu zaidi—je! dhamiri yako imekuongoza ueleze mambo yalivyo na kulipa kodi yote? Ni kweli, huenda kusiwe na uwezekano mkubwa wa kuchunguzwa sana kwa risiti za kodi. Lakini kwa Mkristo mwenye dhamiri yenye wepesi unaofaa, kutaka kuepuka adhabu siyo sababu ya pekee inayomfanya atende inavyofaa; dhamiri vile vile ni sababu. Je! ndivyo wewe unavyoona kwa habari yako?
6 Katika habari hii Paulo aliandika hivi: “Kwa hiyo ni lazima kutii, si kwa sababu ya ile ghadhabu [juu ya wavunja sheria] tu, ila na kwa sababu ya dhamiri.” (Rum. 13:5) Hivyo dhamiri yako ya Kikristo yenye wepesi na iliyosawazishwa vizuri imepaswa iwe nguvu yenye kuzuia na kuongoza kwa mema. Je! ndivyo iliyo? Dhamiri yako ni yenye wepesi wa kadiri gani nayo inakusaidia kadiri gani? Na tuangalie mifano michache inayoweza kutusaidia kufanya uamuzi.
DHAMIRI NA KAZI
7. Dhamiri inaingiaje katika kazi ya mtu?
7 Kazi ni sehemu inayoleta magumu mengi yanayomhitaji Mkristo atumie dhamiri. Namna fulani za kazi, kama vile kutengeneza sanamu za ibada, kufanya kazi mahali pa kuchezea kamari au kuandikwa na tengenezo la dini ya uongo, zinapingana na Maandiko waziwazi. Kwa hiyo Wakristo wanaziepuka hizi. (1 Yohana 5:21; Kol. 3:5; Ufu. 18:2, 4, 5) Hata hivyo, si mambo yote yanayohusu kazi yanayofahamika waziwazi hivyo kuwa mabaya. Kazi fulani inaweza kuwa ngumu kufahamika kama ni mbaya au nzuri. Na nyakati nyingine mtu anaweza kuombwa mara kwa mara afanye jambo lisilofaa, ingawa kazi yake anayofanya kila siku inafaa. Kwa hiyo dhamiri inaweza kuhusika.
8, 9. (a) Toa mfano wa ugumu wa kazi unaohitaji dhamiri itumiwe? (b) Mkristo huyo alifikiria mambo gani wakati huo?
8 Kwa mfano, yako magumu ya kazi yanayohusu damu. Biblia inasema waziwazi watumishi wa Mungu wasijilishe damu. (Mwa. 9:3, 4; Matendo 15:19, 20) Kwa hiyo, mashahidi wa Yehova wa Kikristo hawali chakula chenye damu, kama vile utumbo uliochomwa wenye damu, wala hawakubali kutiwa damu mishipani. Lakini namna gani ikiwa unaombwa kazini pako upime damu au vitu vinavyotengenezwa kwa damu mara kwa mara? Je! dhamiri yako ingekuruhusu kufanya hivyo? Shahidi mmoja katika Colorado alikuwa akifanya kazi katika hospitali moja akiwa ndiye daktari mkuu mwenye kupima namna mbalimbali za chembe za mwili na majimaji yake. Kati ya mambo mengi aliyotazamiwa kupima ni namna mbali-mbali za damu. Nyakati nyingine alitakiwa kupima damu ya mgonjwa aone ana sukari au majimaji kadiri gani. Lakini nyakati nyingine alipaswa apime aone ni damu ya namna gani ili ikatiwe katika mishipa ya wagonjwa.
9 Mkristo huyu alilifikiria jambo hili kwa uangalifu. Ingeweza kuonekana kwamba isingefaa Mkristo afanye kazi yake yote katika benki ya damu, ambako kila jambo lilifanywa kwa kusudi lenye kuvunja sheria ya Mungu. Lakini sivyo ilivyokuwa kwa upande wake; yeye alipima vitu vya namna mbalimbali. Vile vile, kama ndiye angalikuwa mwenye kufanya uamuzi wa kufanya hivyo, asingeweza kuagiza mgonjwa atiwe damu mishipani, kama vile Mkristo mwenye duka asivyoweza kuagiza na kuweka bidhaa za sanamu za ibada au sigara katika duka lake. Walakini, daktari huyu alifahamu kwamba kwa habari ya damu yeye alikuwa akipima tu, kama vile ambavyo mwuguzi wa kike angaliweza kupima kuona ikoje, kama vile ambavyo mpeleka ujumbe angaliweza kuipeleka kwenye nyumba za kuichunguzia na kama vile mtu mwingine anavyoweza kumtia mtu damu mishipani au kumpa utabibu mwingine akiagizwa na daktari. Shahidi huyu aliifikiria kanuni iliyo katika Kumbukumbu la Torati 14:21. Kulingana na andiko hilo Myahudi aliyeona mzoga wa mnyama aliyekufa mwenyewe angeweza kumwondolea mbali kwa kumwuzia mgeni ambaye hakuwa chini ya vizuizi vya Torati vilivyohusu nyama ya mnyama asiyeondolewa damu yake. Kwa hiyo dhamiri ya daktari huyo ikamruhusu wakati huo kupima damu, kutia na kupima damu iliyokusudiwa kutiwa katika mishipa ya wagonjwa wasioijali sheria ya Mungu juu ya damu.
10. Tunaweza kufikiria maulizo gani juu ya namna ambavyo tungetatua ugumu huu wa kazi?
10 Je! hivyo ndivyo dhamiri yako ingaliitikia? Ikiwa sivyo, jiulize kama dhamiri yako ingekuruhusu wewe kama mfanya kazi upeleke damu ikapimwe katika nyumba za kuichunguzia. Au, tukichukua mfano mwingine usiohusiana na kutia damu mishipani, je! wewe ukiwa dereva wa gari ungepeleka kifaa cha kuipimia hospitalini? Au dhamiri yako ingekuruhusu utengeneze kioo ambacho kwacho kifaa hicho kinaweza kutengenezwa? Ni wazi kwamba si mambo yote haya yanayoweza kufikiriwa kwa akili nzuri kuwa yenye kushiriki kuvunja sheria ya Mungu juu ya damu. Lakini mtu anajuaje linalovunja na lisilovunja? Hapa ndipo dhamiri inapoingia. Ingawa ni lazima Mkristo aepuke mambo ambayo bila shaka yanapingana na sheria ya Mungu, anahitajiwa kutumia dhamiri yake kuamua mambo mengi. Je! dhamiri yako ingekufaa katika hali hizo? Je! ni nyepesi?
11. Dhamiri ilimwongozaje Mkristo uyu huyu miaka mingi baadaye?
11 Katika habari hii hasa, baada ya miaka mingi ya kupima damu, daktari huyo alianza kusumbuliwa na dhamiri yake. Haikuwa kama kwamba mtu mwingine alipaswa au angeweza kumwambia kwamba alilokuwa akifanya lilikuwa baya. Wala hakuwa akitafuta mtu mwingine amfanyie maamuzi. Lakini alianza kufikiri hivi: “Je! ni sawa kusema nampenda jirani huku nikishiriki kidogo kumfanya jirani yangu avunje sheria ya Mungu?” (Mt. 22:39; Matendo 21:25) Akifahamu wajibu wake wa Kikristo wa kuruzuku jamaa yake, akazungumza jambo hili pamoja na mke wake. (1 Tim. 5:8) Wote pamoja wakakubaliana kwamba ingekuwa afadhali kufanya badiliko ikiwa dhamiri yake ilikuwa inamsumbua. Akaacha kazi yake yenye mshahara wa shilingi 105,000 kwa mwaka akaanza kufanya kazi ya kusafisha, ingawa aliianza kwa kupata mshahara wa shilingi 25,200 tu kwa mwaka.
12. Je! hii maana yake ni kwamba uamuzi aliokuwa amefanya hapo kwanza ulikuwa mbaya, au linaloonyeshwa hasa na habari hii ni nini?
12 Na tusikose kufahamu maana ya mfano huu. Haukusimuliwa hapa kuonyesha kwamba Mkristo hawezi kuwa daktari; wako Wakristo wanaoendelea kufanya kazi kama madaktari, wauguzi wa kike, madereva wa magari, na kadhalika. Mfano huu umetolewa kuonyesha kwamba dhamiri inaweza kuhusika katika mambo ya kazi. Huenda ikawa sivyo ilivyo juu ya kazi unayofanya na mambo unayoagizwa ufanye. Lakini imewapasa Wakristo wote wafikiri kama wanaishi kupatana zaidi wanavyoweza na njia na kanuni za Mungu. Dhamiri yako iliyozoezwa na Neno la Mungu ikipatwa na maumivu kwa sababu ya mambo unayoombwa ufanye, je! utaipuza? Ni jambo la maana kadiri gani kwako kuwa na dhamiri safi mbele za Mungu na wanadamu?—1 Tim. 1:5, 19.
13. Sisi mmoja mmoja tunawezaje kufikiria kazi yetu kwa faida?
13 Bila shaka, hatuwezi kuepuka magumu yote ya kazi, kwa maana tungali tumo katika taratibu hii ya mambo. (1 Kor. 5:9, 10) Hivyo inaelekea unajua kwamba huenda usiweze kumvuta tajiri wako asitawishe dhamiri ya Kikristo. Huenda akachagua kudharau sheria fulani, huenda akauza bidhaa zake kwa bei za kupita kiasi au huenda akaweka ndani ya duka lake bidhaa fulani ambazo wewe usingeziweka ingalikuwa ni biashara yako. Au huenda wafanya kazi wenzako wakasema uongo juu ya kazi ambazo wametimiza au huenda wakakaa kilofa (bila kufanya kazi) wakati tajiri hayuko karibu. Hata hivyo, wewe unaweza na imekupasa uitikie dhamiri yako. Kwa hiyo ikiwa haikuruhusu ufanye mambo fulani au ikiwa unafanyiwa mzaha kwa sababu ya kufanya kazi kwa bidii, usijali. Mtume Petro aliandika hivi: “Ikiwa mtu, kwa sababu ya dhamiri kuelekea Mungu, anavumilia chini ya mambo yenye kuhuzunisha na kutaabishwa isivyo haki, hili ni jambo la kukubalika.”—1 Pet. 2:18, 19, NW.
DHAMIRI NYEPESI ZINATOFAUTIANA
14, 15. (a) Ni sehemu gani nyingine inayohusu dhamiri? (b) Nia ya Wakristo hasa juu ya jambo hili ni nini?
14 Sehemu nyingine inayoweza kuhusu dhamiri yako ni juu ya mamba ya kutukuza taifa, kama vile mazoezi ya kutukuza taifa hadharani. Dhamiri yako inakufanya uitikie namna gani? Hili ni ulizo linalofaa, kwa maana katika jambo hili na mambo mengine dhamiri zinatofautiana.
15 Mashahidi wa Yehova wa Kikristo wanafahamu kwamba watu wengi wanaheshimu sana matendo ya kutukuza taifa, pengine tendo linaloheshimiwa sana na watu wengi likiwa ni kusalimu bendera au kuapa mtu ni mwaminifu kwa bendera ya taifa. Kama vile kitabu Essays on Nationalism cha Carlton Hayes kinavyoonyesha: “Alama kuu ya utukuzo wa taifa inayoaminiwa na kuabudiwa sana ni bendera, na namna za ajabu za ibada zimetungwa za ‘kuisalimu’ bendera . . . ” Ingawa wanajua kabisa kwamba watu wengine wana uhuru wa kufanya mambo haya, mashahidi wa Kikristo wa Yehova wanajiepusha na matendo hayo wakiongozwa na ufahamu wao wa Biblia.—Yohana 17:16; 1 Kor. 10:14.
16. Dhamiri inaweza kuongoza Wakristo wawili wafuate miendo gani miwili?
16 Lakini dhamiri yako itakuongoza ufuate mwendo gani wakati mazoezi ya kutukuza taifa yanapofanywa? Kwa mfano, pengine wewe na watu wengine mnaosikiliza au kutazama jambo fulani mnaagizwa msimame na kusalimu bendera ya taifa. Wewe kama Mkristo bila shaka ungeepuka kufanya tendo lo lote la ibada ya sanamu. Lakini, je! dhamiri yako itakuruhusu usimame? Mkristo mmoja aliye katika hali hii huenda akafikia uamuzi wa kwamba inampasa abaki ameketi, kwa maana kwa njia hiyo yeye mwenyewe anajisikia mwenye hakika kwamba hashiriki katika sherehe hiyo. Je! hivyo ndivyo dhamiri yako wewe ingekuongoza ufanye? Mkristo mwingine aliye katika hali iyo hiyo anaweza kuamua kusimama. Yeye anajua kwamba kusimama tu hakuonyeshi mtu anashiriki kabisa. Wasikilizaji wameagizwa wasimame na kusalimu. Pengine yeye anakumbuka vile wale Waebrania watatu walivyosimama kwa kufaa mbele ya sanamu iliyosimamishwa na Nebukadreza lakini wakakataa kuiinamia. Kwa hiyo, anaweza kufanya uamuzi wa kwamba katika habari yake kushiriki kabisa kutakuwa na maana ya kusimama na kusalimu pia, kwa hiyo dhamiri yake mwenyewe inamruhusu kwa heshima tu bila kusalimu.—Dan. 3:1-18.
17. Je! hii inaonyesha kwamba jambo fulani ni baya? Sababu ya kutofautiana kwao ni nini?
17 Kama inavyoweza kuonekana, Wakristo wawili wakiwa katika hali ile ile moja, huenda dhamiri ikawaongoza kufanya maamuzi yanayotofautiana kidogo, ingawa wote wawili wanajiepusha na jambo ambalo Biblia inahakikisha halifai. (Kut. 20:4, 5; 1 Yohana 5:21) Tofauti hiyo inayoruhusiwa na kufanya kazi kwa dhamiri haionyeshi kuna mchafuko au kutopatana kati ya Wakristo. Wala hiyo haihakikishi kwamba bila shaka mmoja wa wale ndugu wawili anafanya vibaya. Bali, tofauti hiyo inaweza kuonwa kama tokeo linalotazamiwa la kupata na kutumia dhamiri ya Kikristo.
18. Tunaweza kufaidikaje kutokana na kuongozwa na udamiri ingawa kufanya hivyo huenda kukatofautiana kati ya watu mbalimbali?
18 Je! hii inakufaidi wewe? Je! kufuata dhamiri yako ni jambo kuu kuliko kufuata “sheria”? Ndiyo, nia yako ya kuzoeza dhamiri yako na kuiitikia, badala ya kufuata sheria nyingi ‘za Kifarisayo’ juu ya kila ulizo na tofauti inayoweza kutokea, inakufaidi. Inakusaidia ukumbuke sana kanuni za Biblia. Na bila shaka unakuwa mwenye uwezo zaidi wa kufikiri vizuri, akili yako inaamshwa na kutiwa nguvu. Matokeo hayo yenye kufaidi yalionyeshwa wazi katika uchunguzi uliofanywa Australia juu ya vijana wenye uwezo wa kufikiri na kutumia akili kati ya walio na umri wa miaka kumi na miwili. Habari juu ya jambo hili ilisema hivi:
“Hasa, hesabu kubwa ya watoto wenye kufikiri sana na kutumia akili walikuwa mashahidi wa Yehova. Watoto wanne kati ya hesabu yote ya watoto 394 walikuwa wa madhehebu hii, na wote wanne walionyesha wana uwezo mwingi wa kufikiri sana na kutumia akili. Kati ya wanaume na wanawake, msichana aliyepata jumla ya maksi ya juu zaidi katika mitihani iliyohusu Ziwa Torrens la Australia lenye chumvi, na msichana aliyekuwa mtoto wa pekee, kutiwa katika persenti 20 ya mitihani yote mitano, walikuwa wote wawili Mashahidi wa Yehova.”—Journal of Personality, Machi 1973.
Sababu iliyotolewa ya watoto hawa Mashahidi kuwa wenye kufikiri sana na kutumia akili ilikuwa nini? Uchunguzi ulionyesha waziwazi kwamba wao hawafanyi mazoezi ya kutukuza taifa kwa sababu tu yanafanywa shuleni. Bali, wanafikiria kanuni za Neno la Mungu na kusitawisha uwezo wa kuitikia dhamiri nyepesi ya Kikristo.
NYEPESI, LAKINI SI YENYE KUZUIA ZAIDI SIKUZOTE
19, 20. (a) Kwa sababu gani dhamiri nyepesi haizuii zaidi sikuzote? (b) Paulo alionyeshaje hili alipokuwa akizungumza juu ya nyama na sanamu za ibada?
19 Tumeona kwamba kadiri dhamiri yako inavyozoezwa na kupatanishwa zaidi na njia na mapenzi ya Mungu yaliyoonyeshwa wazi, kwa kawaida inakuwa yenye kuzuia zaidi. Haikuruhusu tena ufanye mambo fulani uliyokuwa ukifanya, kwa maana sasa unayaona kuwa yasiyopatana na kanuni za kimungu. Lakini, kuzoeza dhamiri yako kwa Neno la Mungu hakumaanishi lazima iwe yenye kukuzuia zaidi katika kila jambo. Kwa kweli huenda dhamiri yako iliyozoezwa vizuri ikaja kukuruhusu kufanya mambo fulani ambayo ulidhani yalikuwa hayafai kabla hujajua mapenzi ya Mungu.
20 Kinacholeta tofauti katika mambo hayo ni maarifa ya kweli. Hii inaonyeshwa katika maelezo ya Paulo juu ya nyama ambayo ilikuwa imetolewa sadaka kwa sanamu na kuuzwa baadaye katika soko la nyama au katika mkahawa wa namna fulani unaohusiana na hekalu la sanamu. Mtu ambaye alikuwa ameacha ibada ya kipagani karibuni akawa Mkristo angeweza kuepuka kununua nyama hiyo, akitaka kuepuka kufanya lo lote lile linalohusiana na sanamu. Lakini baadaye angeweza kuongeza maarifa na ufahamu wake. Paulo aliandika hivi: “Twajua ya kuwa sanamu si kitu . . . na ya kuwa hakuna Mungu ila mmoja tu.” (1 Kor. 8:4) Akija kufahamu jambo hili, Mkristo angeweza kufahamu kwamba nyama iliyouzwa hadharani haikuwa najisi wala haikuwa na sumu ati kwa sababu wakati mmoja ilikuwa imetolewa sadaka kwa mungu wa upuzi. Akijua hivyo dhamiri yake iliyotiwa nguvu ingeweza kumruhusu anunue nyama hiyo katika soko la nyama au katika mkahawa wa hadhara.—1 Kor. 8:10; 10:25.
21. Yawezaje kuwa namna iyo hiyo leo?
21 Yaweza kuwa namna iyo hiyo kwa dhamiri leo. Kwa mfano, kijana mmoja wa kiume katika Ohio alikua akiwa na imani ya kwamba Wakristo hawapaswi kunywa vileo. Hata alikuwa ameshika kwa kichwa maneno yenye kuonya juu ya ulevi na maelezo yanayotolewa juu ya mlevi yaliyoandikwa katika Mithali sura ya 23. Katika miaka ya baadaye alipopata kuwa mtumishi aliye wakf wa Mungu bado dhamiri yake haikumruhusu kunywa divai wala pombe yo yote. Kisha akasikia hotuba iliyoonyesha sawasawa Maandiko yanasema nini juu ya vileo na akaifikiria sana. Ilionyesha kwamba bila shaka Biblia inakataza ulevi. (Mit. 23:20, 21; Efe. 5:18; 1 Pet. 4:3) Hata hivyo Biblia haikatazi kunywa vileo kwa kiasi, kama vile Yesu alivyotengeneza divai wakati mmoja akainywa. (Mwa. 14:18; Zab. 104:15; Mhu. 9:7; Yohana 2:3-11; Luka 22:17, 18) Ingawa kijana huyo alikuwa anayajua maandiko hayo, sasa akaona uamuzi uliosawazika yaliyouonyesha. Hivyo wakati mwanamume Mwitaliano alipompa bilauri (glasi) ndogo ya divai kwa ukarimu, dhamiri ya Mkristo huyu ikamruhusu aikubali.
22. Ni jambo gani la maana sana lisiloweza kusahauliwa na mtu mwenye dhamiri iliyotiwa nguvu?
22 Je! wewe umetiwa nguvu na kusawazishiwa dhamiri yako unapozidi kupata maarifa ya Neno na njia za Mungu? Ikiwa ndivyo, inaelekea wewe vile vile unathamini ubora wa kufikiria maono ya moyoni ya mtu ambaye pengine dhamiri yake inatofautiana na yako. Hii ndiyo iliyokuwa maana ya Paulo alipokuwa akizungumza juu ya nyama iliyokuwa imetolewa sadaka kwa sanamu ambayo kwa kweli ilikuwa “si kitu.” Aliandika hivi: “Bali ujuzi huu haumo ndani ya watu wote.” (1 Kor. 8:4, 7) Kwa sababu Wakristo wengine hapo kwanza walikuwa wakiabudu sanamu, wasingeweza kula nyama kama hiyo wakiwa na dhamiri safi ingawa iliuzwa hadharani. Mkristo mwenye “ujuzi” na dhamiri yenye nguvu akila “kila kitu,” hiyo inaweza kumharibu ndugu fulani “ambaye Kristo alikufa kwa ajili yake.” Kwa hiyo Paulo alitangaza hivi: “[Nyama hiyo ikimkwaza] ndugu yangu, hakika sitakula nyama hata milele.”—1 Kor. 8:10-13; 10:27-29.
23. Ni kwa njia gani dhamiri ya wengine imepaswa ihusike katika maamuzi yetu?
23 Je! ndivyo unavyoona wewe? Kwa mfano, pengine kuna jambo linaloelekea kuruhusiwa na mapenzi ya Mungu yanayooneshwa wazi na ambalo dhamiri yako inaweza kuruhusu. Pengine ni njia fulani ya kuvalia kwako au unadhifu wako, pengine ni mapambo unayofanya nyumbani mwako au mambo unayofanya ya tafrija. Lakini namna gani ikiwa dhamiri ya watu wengine wengi walio karibu nawe inawaongoza waone kwamba mambo hayo hayamfai Mkristo? Je! Ukristo wako unakuongoza uamue kwa furaha kwamba. ‘Ikiwa hii inakwaza ndugu yangu, sitafanya hivyo kamwe, nisije nikamkwaza ndugu yangu’?
24. Tufanye nini dhamiri yetu ikipingana na dhamiri ya mtu fulani mwenye mamlaka juu yetu? Kwa sababu gani tufikirie dhamiri yake?
24 Na dhamiri za wengine zimepaswa zifikiriwe katika jambo jingine. Pengine umeanza kupenda mtindo fulani wa kisasa wa mavazi. Dhamiri yako haisumbuliwi na mtindo huo. Lakini lazima wewe kama mtoto au mwanamke aliyeolewa uombe ruhusa ya baba yako au ya mume wako. Je! wewe umefikiria dhamiri yake? Au ikiwa unataka kupata pendeleo fulani la utumishi katika kundi la Kikristo, dhamiri ya baraza ya wazee inahusika. (1 Tim. 3:9) Ni kweli, wao wanajua kwamba kuvalia kunahusu mapendezi ya kila mtu mwenyewe. Lakini wakiombwa wakupendekeze kwa utumishi wa pekee, lazima dhamiri yao isiwe na mashaka. Wao wana daraka zito linalohusu sifa njema ya Ukristo mtaani, wakifahamu kwamba wale wanaowekwa kwa ajili ya mapendeleo ya pekee wamepaswa waweke mfano mwema. (1 Tim. 3:2, 7,10) Kwa hiyo, ikiwa kitu fulani ambacho dhamiri yako inakiruhusu kinapingana na dhamiri ya wale wenye mamlaka au ukichwa juu yako, wawe ni wazazi wako, mume wako au waangalizi wa Kikristo, na uwe mwenye nia ya kufanya mabadiliko ili waweze kutoa ruhusa au kufanya pendekezo wakiwa na “dhamiri njema.”
SITAWISHA DHAMIRI NYEPESI
25. Imekupasa ufanye nini ikiwa ni “juu ya dhamiri yako” kuamua jambo?
25 Kukuza na kufuata dhamiri nyepesi inavyofaa kunahitaji kufanya hivyo sikuzote. Ni vyepesi sana kuongozwa isivyofaa na walimwengu walio karibu nasi ambao dhamiri yao inaruhusu wafanye mambo mengi kupita kiasi, au ambayo imefanywa nzito au hata ikanajisika. (Tito 1:15) Mambo mengi yatatokea ambayo lazima uyatatue kulingana na dhamiri yako mwenyewe. Ikiwa umetia bidii kusitawisha dhamiri nyepesi ya Kikristo, hiyo itakusaidia. Uwe mwenye nia ya kusikiliza kwa makini sauti ya dhamiri yako, si kujiona kwamba ikiwa ni “juu ya dhamiri yako” kuamua si kitu hata ufanye jambo gani. Ni kitu. Uamuzi utakaofanya pengine utabadili maoni yako yote juu ya maisha, sifa yako kama Mkristo, hali yako ya kiroho na, la maana zaidi, uhusiano wako na Yehova Mungu.
26, 27. (a) Mtu anaweza kusaidiwaje kwa kusema na mzee, lakini mzee hawezi kufanya nini? (b) Dhamiri nyepesi itatusaidiaje?
26 Katika shauri linalopaswa kufikiriwa kwa uzito, lakini ambalo bado ni juu ya dhamiri yako kuamua, usisitesite kusema na Wakristo waliokomaa kama vile, wazee kundini. Bila shaka, wao hawawezi kukufanyia uamuzi. (Mkristo mmoja mnyofu wa moyo aliuliza hivi alipokuwa akitaka kujua jambo fulani lililohusu jamaa: “Je! hii inapingana na dhamiri ya Kikristo?”) Sivyo, mzee hatakuambia dhamiri yako inavyopaswa kuitikia, lakini anaweza kuzungumza nawe mashauri ya Biblia yaliyosawazika ambayo unaweza kuthamini. Na ikiwa dhamiri yako imetengenezwa na njia na utu wa Yehova na inaitikia kanuni Zake, utasaidiwa kwa njia hiyo kunyosha njia yako. (Zab. 25:4, 5) Dhamiri yako nyepesi itasaidia kukuongoza.
27 Kwa kweli kuna uradhi katika kuweza kutumia uwezo wa dhamiri uliopewa na Mungu. Ni baraka. Unapoendelezwa inavyofaa kuwa mwepesi, uliosawazishwa na Neno la Mungu, unaweza kukusaidia utembee kwa hekima mbele za Mungu na wanadamu. (2 Kor. 4:2) Unaweza kuwa mshuhudiaji wa kusema kwamba unajiongoza katika njia itakayoelekea kupata kibali ya milele ya Yehova.—2 Kor. 1:12.
—Kutoka The Watchtower, April 1,1975.