Kufaidika na Dhamiri Yako Uliyopewa na Mungu
“Sheria ya Mungu wake imo moyoni mwake. Hatua zake hazitelezi.”—Zaburi 37:31.
1, 2. Kwa sababu gani twapaswa kuhangaikia uongozi wa dhamiri zetu? (Mithali 12:15; 14:12)
INGAWA Mungu hajawapa Wakristo orodha yenye sheria nyingi, yeye ametupa sheria fulani, au amri za moja kwa moja, na kanuni nyingi za kufuata kupatana na imani na dhamiri yetu. Lakini kuwa na dhamiri ni tofauti na kufaidika nayo kikamilifu. Watu wengi wanaonelea kwamba ‘iwapo jambo fulani halisumbui dhamiri yangu, basi ni sawa.’ Je! kuwaza huko ni sahihi?
2 Biblia inaonyesha kwamba kwa sababu ya mwili wetu wenye dhambi dhamiri zetu zinaweza kutuongoza vibaya; zinaweza kuwa dhaifu, zilizopotoshwa au kuchafuliwa. Twaweza kuthamini vizuri zaidi hatari ya maoni “acha dhamiri yako ikuongoze” kwa kuchunguza wakaaji wa karne ya kwanza wa Krete, ambao juu yao ilijulikana walikuwa ‘waongo, hayawani wabaya [wenye kuumiza, NW], walafi wavivu.’—Tito 1:10-12.
3. Dhamiri ilikuwa na matokeo gani juu ya Wakrete?
3 Kama ilivyo kwa watu wote, Wakrete walikuwa wamezaliwa na dhamiri ndani yao. Lakini hawakuwa wakijifaidi nayo. Akimwandikia Tito katika Krete, mtume Paulo alisema hivi: “Vitu vyote ni safi kwa hao walio safi; lakini hakuna kilicho safi kwao walio wanajisi, wasioamini; bali akili zao zimekuwa najisi, na [dhamiri] zao pia.” (Tito 1:15; Warumi 2:14, 15) Wengi kati ya Wakrete walikuwa na dhamiri zilizokufa ganzi ambazo hazikuwa zikiwasaidia kufanya mambo ya adili au yaliyo safi. (1 Timotheo 4: 2) Kwa Wakrete wengi ‘hakuna jambo lililokuwa safi.’ Jinsi gani hivyo? Wakiwa na dhamiri zilizochafuliwa waliiona kila hali kuwa nafasi ya kufanya maovu. Huenda wakawa walisema, ‘Jambo hilo halisumbui dhamiri yangu.’ Hali ni jambo ambalo lingalipasa kuisumbua dhamiri yao! Hata hivyo, Wayahudi fulani Wakrete au waongofu walikuwa Yerusalemu kwenye Pentekoste 33 W.K. Maarifa yao ya kiroho yangewasaidia waepuke kuwa waongo, wenye kuumiza au walafi. Na wale wenye kumkubali Yesu walisaidiwa zaidi na mafundisho yake ya kuwa na dhamiri njema zenye kufanya kazi.—Matendo 2:5, 11; Tito 1:5; 2:2-5; 3:3-7.
4, 5. Twaweza kujifunza nini juu ya dhamiri kutokana na kisa cha Paulo?
4 Hata hivyo, dhamiri inaweza kumwongoza mtu vibaya hata ikiwa anafahamiana na Neno la Mungu na anataka kufanya yaliyo haki. Sauli, au Paulo, alikuwa anafahamiana na Maandiko na kwa juhudi alikuwa akiabudu kulingana na Sheria (Torati). Hata hivyo alishindwa kuambatana (kufuatana) na kutimia kwa hatua kwa hatua kwa mapenzi ya Mungu. Baada ya Masihi kufika, akahubiri na kufa kwa kutimiza unabii, Paulo aliendelea kuwa mfuasi wa Wayahudi walio Mafarisayo. Dhamiri yake haikumzuia ‘kulitesa kundi’ na “kutaka sana kuwaua wanafunzi wa Bwana.”—Wafilipi 3:4-6, NW; Matendo 9:1, 2.
5 Mifano hiyo inatuonyesha kwamba dhamiri zetu zinaweza kutuongoza vibaya. Kwa kuwa tunakabili maamuzi mengi yasiyoonyeshwa na sheria zilizo wazi za Biblia, ambayo ni mambo ya kuamuliwa na dhamiri, twahitaji kujua jinsi tunavyoweza kuzoeza dhamiri zetu na kufaidika kikamilifu kabisa kutokana nazo. Kuna sehemu tatu ambazo tutazichunguza sasa.
Neno la Mungu Linaonyesha Nini?
6, 7. Neno la Mungu linaweza kutusaidia katika njia gani moja katika mambo yanayotegemea dhamiri?
6 Neno la Mungu kamilifu lina mengi yanayoweza kutupa mwangaza wa maarifa juu ya mawazo ya Mungu, au kanuni, na kuelimisha dhamiri zetu. Kama ilivyotangulia kuonyeshwa, Yusufu hakuwa na sheria iliyoandikwa ya Mungu ya kukataza uzinzi. Lakini dhamiri ya Yusufu ilikuwa imeelimishwa inavyofaa. Bila shaka alikuwa amekwisha kuwaza uhakika wa kwamba Mungu alikuwa amekusudia mume na mke (“hao wawili”) wawe mwili mmoja, bila mzinzi mwingine aliye mtu wa tatu kujiingiza. Na hakika Yusufu alikuwa anajua kisa kilichomhusu rafiki ya Mungu, Ibrahimu, ambacho kilionyesha msimamo wa Mungu juu ya uzinzi.—Mathayo 19:5; Mwanzo 2:24; 20:1-18.
7 Sisi pia twaweza kufaidika vivyo hivyo. Kwa mfano, huenda tukakabili uamuzi juu ya kukubali mwaliko wa kula chakula au kufanya shughuli ya kikazi na mtu wa taifa tofauti, rangi au hali. Hilo ni jambo la kujifanyia uamuzi wa kibinafsi. Hata hivyo, ikiwa tumetwaa kutoka kwa Biblia maoni ya Mungu juu ya kutopendelea na kutobagua, dhamiri zetu zilizoelimishwa zitaondosha ubaguzi wo wote ambao pengine tulikuwa nao tulipokuwa tukikua. Tutatenda ipasavyo. (Matendo 10:34, 35; Yakobo 2:1-4) Kwa njia hiyo kanuni za Biblia zaweza kutusaidia sisi pia.
8. Tunapokabili uamuzi unaotegemea dhamiri, twapaswa kufanya nini?
8 Tunapohitaji kuamua jambo ili ‘tushike dhamiri njema,’ lazima tutafute yale anayosema Yehova kuhusu jambo hilo, kwa maana hilo laweza na lapasa kuwa na matokeo juu ya dhamiri zetu na uamuzi wetu. (1 Petro 3:16) Pamoja na kutafuta sheria za moja kwa moja, twapaswa kupendezwa kuona kama kuna kanuni zo zote za Biblia zinazohusiana nalo. Je! Yesu alifanya au kusema jambo lo lote linaloonyesha kuwaza kwake juu ya uamuzi huo? Twaweza kufanya uchunguzi katika vifaa vya Biblia vinavyozungumza juu ya jambo hilo. Na twaweza kutafuta mashauri kutoka kwa Wakristo wenzetu ambao huenda wakatusaidia tupate kanuni za Biblia zinazohusu. Bila shaka, hatua hiyo haipasi kuchukuliwa tukiwa na wazo kwamba watabeba daraka letu, wala hatupaswi kuuliza, ‘Kama ingekuwa wewe, ungefanya nini?’—Wagalatia 6:5.
9. Katika kuamua masuala yanayotegemea dhamiri mradi wetu ni nini?
9 Katika hali ambazo uamuzi wa kibinafsi lazima ufanywe, Wakristo wenye moyo mweupe wanapaswa kufuata mwendo utakaowaacha wakiwa na dhamiri safi na iliyotulia mbele ya Mungu. Wanapaswa kupendezwa na uwezekano wa kusema: “Ushuhuda wa dhamiri yetu . . . [ni] kwamba kwa utakatifu na weupe wa moyo utokao kwa Mungu . . . tulienenda katika dunia, na hasa kwenu ninyi.” (2 Wakorintho 1:12) Kadiri ambayo Mkristo anampenda Yehova na kanuni zake yaweza kuonyeshwa na yale anayoamua juu ya masuala ya dhamiri.
Matokeo Yatakuwa Nini juu ya Wengine
10, 11. Ulizo fulani juu ya chakula katika Korintho wa kale linaonyesha jambo gani la pili la kufikiriwa kuhusu maulizo yanayotegemea dhamiri?
10 Kwa kuwa Wakristo wanataka dhamiri zao ziwachochee wamwige Mungu, kuhangaikia wengine kwa upendo kwapasa kuwa kichocheo kikubwa katika maamuzi yanayohusu dhamiri. Jambo hilo lilitokezwa wazi wakati Paulo aliandika juu ya mambo mbalimbali yanayohusu chakula.
11 Katika kundi la Korintho hangaiko lilitokea kuhusu nyama iliyokuwa imetolewa sadaka kwa sanamu. Kwa Mkristo kula nyama ya kutolewa dhabihu wakati wa sherehe ya sanamu ingekuwa ni ibada ya sanamu. Lakini Paulo alieleza kwamba haingekuwa dhambi kula nyama iliyobaki ambayo iliuzwa mahali kama katika mikahawa yenye kuungana na hekalu au katika masoko ya nyama ya watu wote. (1 Wakorintho 8:10; 10:25; Matendo 15:29) Hata hivyo, Wakristo wengine ambao hapo kwanza walikuwa wameabudu sanamu walikuwa na dhamiri yenye kusumbuliwa (dhaifu) kuhusu nyama hiyo hata walipokuwa watu wote wakiuziwa bila kuihusianisha na mambo yo yote ya kidini. Ingawa hakuwa akiendekeza dhamiri dhaifu-dhaifu, Paulo aliwasihi wengine wawafikirie ndugu hao. Usingalikuwa upendo kufanya jambo ambalo lingaliwafanya wakwazike au kujiona huru tena kushiriki katika ibada ya sanamu.
12, 13. Kwa sababu gani maoni na dhamiri za wengine zapasa kufikiriwa? Toa mfano.
12 Paulo alionyesha nia ambayo sote twaihitaji: “Chakula [au kitu kingine] kikimkwaza ndugu yangu, hakika sitakula nyama hata milele.” Ikiwa, tunapuza dhamiri ya wengine na hivyo ‘kuwaharibu ndugu zetu ambao Kristo alikufa kwa ajili yao,’ kwa habari ya jambo linalotegemea dhamiri yetu, huenda tukapoteza msimamo wetu mzuri na Mungu. Paulo aliuliza hivi: “Kwa nini uhuru wangu uhukumiwe na dhamiri ya mtu mwingine?” (1 Wakorintho 8:3, 11-13; 10:29) Hata ingawa mtu anaonelea ni ‘jambo la kibinafsi linalotegemea dhamiri,’ ikiwa linawaharibu wengine laweza kumtokezea hukumu kali ya Yehova. Hilo linaonyesha jinsi ilivyo kujidanganya kufikiri ‘iwapo ni jambo linalotegemea dhamiri yangu, basi ni sawa.’
13 Fikiria kisa cha wenzi waliokuwa na funzo la Biblia, wakihudhuria mikutano na karibu kubatizwa. Mzee mmoja katika kundi akamwambia mwanamume yule alivyofurahia sinema fulani. Mwanamume yule akajibu, ‘Ai! Wewe unakwenda kuona sinema zinazoandikwa ni za watu wazima peke yao?’ Mzee yule akajaribu kutetea alivyotenda, na kusema kwamba baadhi ya sinema hizo (zinazotiliwa mashaka hata na ulimwengu) zina faida ikiwa sehemu zazo zisizopendeza zinapuzwa. Lakini inaonekana mwanamume yule alidhuriwa (aliumizwa). Baada ya hapo akafanya maendeleo ya polepole zaidi ya mkewe. Kama mzee yule angalitafakari juu ya maandiko kama Wakolosai 3:2-8, Waefeso 5:3-5 na Mathayo 7:12, yangalikuwa na matokeo mazuri juu ya dhamiri yake na mwenendo wake.—1 Wakorintho 9:22, 25-27.
14, 15. Dhamiri za baraza ya wazee zawezaje kuhusika katika mambo fulani ya kibinafsi?
14 Kuwafikiria wengine vilevile kunatia kutowauliza wakubali jambo lisilokubaliwa na dhamiri zao. Kwa mfano, wazee wa kundi wana daraka la kuruhusu sherehe za arusi katika Jumba la Ufalme, jinsi zitakavyoendeshwa, jinsi jumba litakavyopambwa, na kadhalika.a Wazee katika kundi moja wanaandika hivi: “Katika arusi moja wanawali wote wa bi-arusi walitembea katika kijia cha jumba wakijipungia hewa kwa vipepeo. Waliohusika katika arusi iliyokuja baada ya hiyo waliona ni lazima ishinde hiyo ya kwanza, kwa hiyo wanawali wa bi-arusi wakatembea katika kijia cha jumba wakizungusha-zungusha miavuli. Iliyofuata ilipasa kuwa kubwa zaidi na bora zaidi; walitaka wanawali wa bi-arusi ishirini na wakaribishaji ishirini. Jumba lilikuwa limeanza kutumiwa kama sarakasi.”
15 Je! hilo lilikuwa ‘jambo la kuamuliwa na dhamiri,’ la kufanyiwa uamuzi wa kibinafsi? Hapana. Hata ikiwa dhamiri za wenzi waliochumbiana zingeruhusu jambo la kupita kiasi au la kuleta aibu, dhamiri za wazee kwa ujumla hazipasi kupuzwa. Ingawa hawatakaza watu wafuate yanayowapendeza kibinafsi, wanapendezwa moyoni na amani, upatano na hali njema ya kiroho ya kundi lote. Nao wanapaswa kuwa wakisaidia watu kwa uaminifu ‘jinsi iwapasavyo kuenenda katika nyumba ya Mungu, ambayo ni nguzo na msingi wa kweli.’—1 Timotheo 3:15; 1 Wakorintho 10:31.
16. Ikiwa ni lazima uamue jambo fulani linalotegemea dhamiri yako, unapaswa kufikiria nini?
16 Kwa hiyo, tunapokabili uamuzi juu ya ‘jambo la kuamuliwa na dhamiri,’ twapaswa kufikiria (a) yanayosemwa na Neno la Mungu kulihusu, na (2) jinsi uamuzi wetu unavyoweza kuwa na matokeo juu ya wengine au kuwahusu. Hata hivyo, kuna jambo la tatu la maana.
Matokeo Yatakuwa Nini juu Yetu Sisi Wenyewe?
17. Dhamiri ilikuwa na matokeo gani juu ya ndugu mmoja katika Mji wa New York?
17 Jarida Natural History la Agosti 1981 lilikuwa na makala juu ya matarishi wa kwenda kwa baisikeli wa Mji wa New York ambao husafirisha vifurushi vinavyotakiwa haraka na barua kwa kampuni mbali-mbali katika mji huo. Kati ya watu ambao wanafanya kazi hiyo, twasoma hivi: “Donald, tarishi mwenye umri wa miaka 41, anaweza kutunza mkewe na mwana wa miaka 15 kwa mapato yake. Donald alikuwa msafishaji picha, lakini akaacha kazi yake kwa sababu, akiwa Shahidi wa Yehova, hangeweza kuendekeza sehemu aliyokuwa akifanya katika kutokeza picha za umalaya. Akiwa tarishi, si kwamba tu anahisi dhamiri yake ni safi bali pia anaweza kumaliza kazi anapoamua ili atumie wakati zaidi wa kufanya waongofu wa kidini.”
18. (a) Yaweza kuwa ndugu huyo alifikiaje uamuzi wake? (b) Unaweza kujifunza nini kutokana na hilo?
18 Mambo kadha wa kadha yanahusika katika maamuzi ya kazi za kuajiriwa (ona kisanduku katika ukurasa 17). Sawa na kisa cha Donald, huenda Mkristo akawa anafanya kazi na kampuni inayosafisha picha—picha zinazopigwa, sinema za kibinafsi, sinema za matangazo ya kibiashara na zile za kawaida. Huenda polepole kampuni hiyo ikaanza kuchukua picha za umalaya. Kufikia hatua fulani huenda dhamiri ya Mkristo ikaanza kumsumbua. Huenda akatambua kwamba yeye mwenyewe analazimishwa kuhusika na utendaji wa kutokeza vifaa vinavyohusu umalaya au utendaji mwingine haramu. Iwe ni kwa sababu ya kuwa mshiriki wa kampuni inayohusika na mambo ya umalaya au iwe na kwa sababu ya mambo anayoulizwa afanye, huenda akaona lazima ajiuzulu ili abaki ‘bila lawama,’ na hilo ni jambo la kuhangaikiwa kipekee na watu wenye mapendeleo katika kundi au wanaoyatafuta. Anapotafuta kazi nyingine, anaweza kutumainia kwa uhakika baraka za Yehova. (1 Timotheo 3:2, 8-10; Warumi 13:5) Hakika kuna Wakristo wengi ambao wameacha kazi za namna hiyo badala ya kukubali wadhoofishwe na uchafu. (Linganisha Mathayo 5:28.) Kwa hiyo, tunapokabili uamuzi unaotegemea dhamiri, twapaswa kuuliza hivi: ‘Nikifanya jambo hili au nikikataa kulifanya, litakuwa na matokeo gani juu yangu?’ Hakika hatupaswi kupuza dhamiri zetu, kuzifisha ganzi na hivyo kufanya iwe rahisi zaidi kufanya mabaya katika wakati ujao.—1 Timotheo 4:2; Yuda 10; Waefeso 4:18, 19.
19, 20. (a) Dhamiri na imani, zote mbili zaweza kuongozaje huduma yetu? (b) Tuwe matajiri au la, tamaa yetu inapasa kuwa nini?
19 Tunapotafakari juu ya uamuzi wa uaminifu aliofanya Donald, twapaswa kuangalia kwamba pamoja na kutafuta kwake uhusiano wenye kukubalika na Yehova, yeye alikuwa na tamaa ya kuitangaza imani yake zaidi. Hilo lapatana na uhusianisho wa Paulo kati ya dhamiri na imani: “Kusudi la agizo hilo ni upendo kutokana na moyo safi na kutokana na dhamiri njema na kutokana na imani bila unafiki.”—1 Timotheo 1:5, NW.
20 Ni jambo la kusifika wakati imani na tamaa ya mtu ya kuwa na dhamiri njema inamchochea afanye marekebisho ili ‘hatua zake zisiteleze’ na ili atoe wakati zaidi na fikira zaidi katika kueneza “mashauri yote ya Mungu.” (Matendo 20:26, 27, NW) Hata hivyo, twapaswa kuwaonaje wengine ambao yaelekea hali zao zinawaruhusu kuhubiri zaidi lakini hawafanyi hivyo? Huenda wakawa na mshahara mnono kutokana na kazi au biashara zao na kuonekana wamekwisha kuwa na fedha za kutosha za kuwawezesha kuwa na maisha ya starehe katika taratibu hii. Hata hivyo, badala ya kufurahia kufanya wanafunzi wakati wote wakiwa mapainia, wanaendelea kufanya kazi wapanue biashara zao, nyumba na starehe.b (Linganisha Marko 10:17-22; Luka 12:16-21.) Si juu yetu kuwahukumu wengine katika jambo kama hilo, maana “kila mtu miongoni mwetu atatoa habari zake mwenyewe mbele za Mungu.” Badala yake, imani yetu na ituchochee bila unafiki tumtumikie Mungu kikamilifu ili tufurahie dhamiri safi.—Warumi 14:1-4, 10-12.
Kuongozwa na Dhamiri Njema
21. Dhamiri zetu zaweza kuwa na matokeo gani yanayofaa juu yetu?
21 Dhamiri ya Kikristo iliyoelimishwa na ambayo haijakufa ganzi itatuongoza tufanye yaliyo mema. Ilimwongoza Paulo afanye hivyo. Yeye alikuwa anapendezwa sana na ‘ndugu zake,’ Wayahudi wenzake, hata akaandika hivi: “Dhamiri yangu inashuhudia pamoja nami katika roho takatifu, kwamba nina huzuni nyingi na maumivu yasiyokoma moyoni mwangu.” (Warumi 9:1-3, NW) Ndiyo, alifanya yote aliyoweza kushiriki habari njema za Ukristo pamoja nao.
22. Kwa sababu gani dhamiri inaweza kutuchochea hata zaidi ya amri?
22 Inapasa kuwa ivyo hivyo kwetu. Ikiwa tunathamini ubora wa dhamiri zetu tulizopewa na Mungu, hatutakuwa na maelekeo ya kufikiria-fikiria habari za amri tu. Huenda amri zikatoa matakwa au miradi ya chini zaidi inayotakiwa. Lakini dhamiri yenye kuchochewa na upendo na imani yaelekea itataka mengi zaidi kutoka kwetu, na kutusukuma tujinyime zaidi na kutokuwa na choyo. Kwa njia hiyo kwa hakika tutafaidika na dhamiri zetu. Zitatuepusha na mambo yanayoweza kutokeza kukataliwa na Mungu, na zitatusaidia kufanya mambo ambayo bila shaka anayakubali. Sana sana inakuwa hivyo dhamiri zetu zinapotuongoza tushiriki zaidi katika kutangaza habari njema. Kwaweza kuwa faida gani kubwa zaidi ya ile ambayo Paulo alimtajia Timotheo? Yeye alisema: “Jitunze nafsi yako, na mafundisho yako, Dumu katika mambo hayo; maana kwa kufanya hivyo utajiokoa nafsi yako na wale wakusikiao pia.”—1 Timotheo 4:16.
—Kutoka The Watchtower, July 15, 1982
[Maelezo ya Chini]
a Ona Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) wa Mei 1, 1974, kurasa 274-277.
b Kundi la kwenu lingefaidika kwa kuwa na mapainia zaidi. Hata hivyo, watu wengi wenye kupendezwa wenye njaa ya kiroho wako katika maeneo ambayo wachache wanaweza kuhamia kwa sababu hakuna nafasi za kazi. Ni baraka kama nini wakati Wakristo ambao wana fedha za kutosha wanaitikia miito hiyo yenye kutaka msaada!—Matendo 16:9, 10.
◻ Kwa sababu gani ni hatari kuwa na maoni ya kwamba ‘iwapo jambo fulani halisumbui dhamiri yangu, basi ni sawa?’
◻ Unapokabili ulizo ambalo uamuzi unategemea dhamiri yako, ni mambo gani matatu unayopaswa kufikiria kwa uzito?
◻ Dhamiri inapasa kuhusuje kusifu kwako Mungu waziwazi?
[Maswali ya Funzo]
[Sanduku katika ukurasa wa 17]
Mambo ya Kufikiria katika Kazi ya Kuajiriwa
Inapokuwa lazima Mkristo afanye uamuzi juu ya kazi fulani ya kuajiriwa, anapaswa kufikiria kwanza atakayokuwa akifanya hasa. Anaweza kufikiria mambo haya mawili:
Je! kazi hiyo inalaumiwa katika Biblia?
Biblia inalaani mambo kama kuiba, kuabudu sanamu na matumizi mabaya ya damu, kwa hiyo Mkristo hangeweza hata kidogo kushiriki katika kazi ambayo anaendesha mambo hayo kwa njia ya moja kwa moja.
Je! kazi hiyo ingemhusianisha mtu karibu sana na zoea linalolaaniwa hata kwamba awe ni mshiriki bila shaka?
Hata kuwa bawabu au mkaa-mlangoni kwenye jumba la kuweka akiba ya damu au kiwanda kinachotengeneza silaha za vita peke yake kunahusiana kwa njia ya moja kwa moja na kazi inayopingana na Neno la Mungu.—Mambo ya Walawi 17:3, 14; Isaya 2:2-4.
Zaidi ya yale ambayo huenda mtu akawa akifanya, mambo mengine zaidi yaweza kuhusika katika jambo hilo kwa ujumla:
Je! kazi hiyo ni utumishi wa kibinadamu ambao kulingana na Biblia si kosa?
Mchukua barua za posta hufanya utumishi wa kupeleka barua kwenye nyumba na makampuni. Je! Mkristo angelaaniwa ikiwa kati ya sehemu anazopeleka barua ni nyumba chache za wevi au kampuni inayouza sanamu za ibada?—Mathayo 5:45.
Mtu ni mwenye madaraka kadiri gani juu ya mambo yanayofanywa?
Mkristo mwenye duka hangeweka na kuuza sanamu za ibada au soseji za damu (mtura). Yeye hayuko katika hali ile ile ya mfanyi kazi katika duka la supa-maketi inayouza sigara au kitoweo cha damu pamoja na bidhaa nyingine maelfu.
Ni kwa kadiri gani mtu anahusika?
Mfanyi kazi ambaye hufanya kazi ya kuchukua fedha kutoka kwa wanunuzi na ni pindi kwa pindi tu anashughulika na sigara huenda akakata kauli kwamba hali yake si sawa na ya mfanyi kazi mwingine ambaye huzipanga kwenye rafu za kuwekea vitu karibu siku nzima.
Mshahara unatoka wapi au kazi hiyo inafanyiwa mahali gani?
Katika nchi ambayo serikali hulipa kanisa usimamizi wa shughuli zote za kijamii, huenda mtu akalipwa mshahara na shirika la kidini. Lakini kwa kweli kazi yake ya kutunza bustani za watu wote si katika shamba la kanisa. Wala namna ya kazi yenyewe si ya kidini wala haionwi kuwa ya kuendesha ibada ya uongo.
Kwa ujumla matokeo ya kufanya kazi fulani ni nini?
Je! kufanya kazi kungewakwaza wengi, na kuleta ‘laumu’? (1 Timotheo 3:2, 10) Kazi hiyo ingekuwa na matokeo gani juu ya dhamiri ya mwenye kuifanya?
[Picha katika ukurasa wa 15]
Huenda Mkristo mwenzako akakusaidia kujua ambayo Neno la Mungu linasema juu ya jambo linalotegemea dhamiri
[Picha katika ukurasa wa 16]
Fikiria jinsi maamuzi au matendo yako yanavyoweza kuwa na matokeo juu ya wengine