Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w75 10/1 kur. 435-441
  • Sauti ya Dhamiri Iliyomo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sauti ya Dhamiri Iliyomo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • DHAMIRI​—KUTOKA WAPI?
  • DHAMIRI​—KAZI YAKE NA MAZOEZI
  • Je, Dhamiri Yako Imezoezwa Vizuri?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Kuendelea Kuwa na Dhamiri Njema
    “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
  • Isikie Sauti Inayotoka Ndani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Je! Wewe Unaongozwa na Dhamiri Nyepesi ya Kikristo?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
w75 10/1 kur. 435-441

Sauti ya Dhamiri Iliyomo

“Watu wa Mataifa wasio na sheria wafanyapo kwa tabia zao yaliyo ndani ya torati, . . . hao waionyesha kazi ya torati iliyoandikwa mioyoni mwao, dhamiri yao ikiwashuhudia.”​—Rum. 2:14, 15.

1, 2. (a) Hali iko namna gani leo juu ya kanuni za adili? (b) Kwa sababu gani uongozi wa adili unahitajiwa hasa kutoka mwaka wa 1914?

LEO mambo yaliyo “haki” au “mabaya” yanabadilika-badilika nyakati zote. Dr. Emanuel Demby alisema hivi katika hotuba iliyokuwa juu ya “Adili ya Watu Wote”: “Sababu ya maana ya kuwa vigumu kuonyesha hali ya adili ilivyo hasa nyakati zetu ni kwamba hiki ni kipindi cha mabadiliko makubwa.” Kanuni zilizokubaliwa zilizokuwa zikifuatwa kila mahali miaka michache tu iliyopita zimefutwa au nafasi yazo ikachukuliwa na nyingine. Na kwa kuwa maisha yanazidi kuwa magumu sana, ni nani anayeweza kusema kanuni mpya zinafaa namna gani, au zitaendelea kwa muda gani? Mtu anao uongozi gani?

2 Hali hii inatuelekea hasa sisi tunaoishi kutoka mwaka wa 1914 C.E. Kwa sababu gani ni kuanzia wakati huo hasa? Dr. Archibald Chisholm alisema hivi: “Mabadiliko yamekuwa makubwa sana katika mawazo na maadili, hata watu wengine wanashauri kwamba tujione kama tunaishi katika mwaka [wa 61] A.B. (anno belli [mwaka wa vita]), kwa njia hiyo wakionyesha maoni yao ya kwamba muda mpya wenye matukio ya pekee ulianza ilipotokea” Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Uhakika wenyewe wa kwamba kumekuwa na mabadiliko hayo katika mawazo na maadili kutoka mwaka wa 1914 unatia mkazo juu ya uhitaji wetu wa kuwa na sauti yenye uongozi unaofaa.

3. Ni maulizo gani yanayotokea juu ya kutegemea dhamiri?

3 Watu wengi wanaoujua uhitaji huu wanatoa maoni ya kwamba mwishowe kila mtu atapaswa kutegemea dhamiri yake mwenyewe. Wanasema: “Acha dhamiri yako iwe uongozi wako.” Wanaposema “dhamiri” wanafikiri kwamba kila mtu anaelekea kuwa na “sauti” ndani yake, maono ya ndani yanayomwambia yaliyo haki na mabaya. Lakini je! ndivyo ilivyo nyakati zote? Je! wewe unajua chanzo cha dhamiri na kadiri kilivyoenea? Vile vile, maono haya ya ndani ni yenye kutegemeka kadiri gani? Hata ikiwa wengine wanaweza kutegemea dhamiri yao wenyewe, je! wewe unaweza?

DHAMIRI​—KUTOKA WAPI?

4. Kulingana na wakuu fulani wa kilimwengu, chanzo cha dhamiri ni nini?

4 Ukitegemea watu wenye akili nyingi na wanafilosofia wakueleze chanzo cha dhamiri yako, pengine utaambiwa kwamba ni kitu kilichotokea katika jamii ya watu kwa njia ya mageuzi tu. Maoni ya mwamini-mageuzi Charles Darwin yalikuwa “kwamba mnyama ye yote, aliye na tabia za asili za jamii yake, . . . bila shaka angejipatia maono ya adili au dhamiri, mara tu baada ya nguvu zake za akili kukua ziwe karibu kama zile zilizo katika mwanadamu.” Naye Sigmund Freud aliona kwamba tungeweza ‘kukataa shauri la kwamba kuna uwezo wa asili wa kutofautisha kati ya mema na mabaya.’

5. Biblia inaunga mkono maoni haya ya dhamiri ya mwanadamu?

5 Lakini je! maoni hayo yanatoa maelezo ya kweli? Maandishi yaliyo ya kale zaidi na yanayotegemeka sikuzote ya historia ya mwanadamu na matendo yake yanajibu, Sivyo! Kwanza, Biblia inasema kwa njia ya kweli mambo ambayo yamehakikishwa kwa uchunguzi wa uaminifu wa kisayansi, kwamba vyote vilivyo hai vinazaa “kwa jinsi yake.” Hivyo mwanadamu hakutokea kwa mageuzi, wala dhamiri yake haikutokea kwa mageuzi. (Mwa. 1:21-26) Tena, Biblia inaonyesha kwa njia ya kweli chanzo cha sauti hiyo iliyo ndani yako, dhamiri yako. Inaonyesha sababu gani wanadamu wanaendelea kuwa na dhamiri duniani pote ingawa wanadamu wamefanya jitihada nyingi kama vile Hitler, ambaye alijivuna akisema, “Mimi ninakomboa mwanadamu kutokana na wazo la upuzi linalojulikana kama dhamiri.” Nasi tunaweza kusaidiwa tukitumia na kufaidika kutokana na dhamiri.

6, 7. (a) Neno la Mungu linaonyesha nini juu ya mwanzo wa dhamiri? (b) Dhamiri ya Adamu ilikuwa nini?

6 Maandiko yanatuambia kwamba Muumba alimfanya mwanadamu kwa mfano Wake mwenyewe, akiwa na akili na maono ya adili, kama vile Mungu mwenyewe alivyo na mambo haya. (Mwa. 1:27) Na kutoka pale pale mwanzoni mwanadamu wa kwanza alipewa dhamiri na Mungu; hakikuwa kitu kilichokua kadiri jamii ya watu ilivyoendelea kuongezeka. Hii inaweza kuonekana katika masimulizi ya matendo na nia ya Adamu alipokwisha kuvunja amri ya Mungu juu ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya. (Mwa. 2:17) Maandishi yanasema kwamba Adamu na Hawa wakati huo “wakajificha kati ya miti ya bustani, [Yehova] Mungu asiwaone.” Na wakati Yehova aliposema, Adamu hakuitikia kwa upesi. Kwa sababu gani? Kwa sababu aliona hatia yake; ilikuwa kama kwamba kulikuwa na sauti ndani yake iliyokuwa ikimlaumu, ikimshitaki, ikishuhudia kwamba alikuwa ametenda dhambi.​—Mwa. 3:7-10.

7 Kwa hiyo, maandishi ya kale zaidi ya kihistoria yanayoweza kupatikana yanaonyesha kwamba dhamiri ya mwanadamu ilikuwako pale pale mwanzoni. Linalopendeza ni kwamba, katika karne ya kwanza C.E. mwanahistoria Myahudi Flavio Yosefu, akiandika Kigiriki, alionyesha kwamba kutotaka kwa Adamu kumwitikia Mungu kulikuwa ushuhuda wa kwamba alikuwa na “dhamiri mbaya.” Kwa neno “dhamiri” Yosefo alitumia neno la Kigiriki syneiʹdesis, ambalo kwa halisi lina maana ya “kujua jambo fulani juu yako mwenyewe.” Dhamiri ya Adamu ilitoka kwa Mungu; ilikuwa maono yake ya ndani ya adili, nayo ilihusu akili yake. Kwa kuwa aliumbwa kwa mfano wa Mungu, wakati Adamu alipotenda tofauti na sifa za Mungu au mapenzi yake yaliyoonyeshwa wazi alijisikia akiwa na vita ndani yake. Lakini hii inahusianaje na maono yetu ya moyoni na matendo yetu? Je! dhamiri ilipitishwa kwa wazao wa Adamu? Ndiyo, ushuhuda wa Biblia na usio wa Biblia pia unahakikisha ilipitishwa, hata ikatufikia kila mmoja wetu leo.

8. Ni masimulizi gani ya baadaye ya Bibiia yanayoonyesha maono ya adili yalirithiwa?

8 Angalia masimulizi ya kihistoria ya yaliyotukia kwa Yusufu zaidi ya miaka elfu mbili baada ya dhambi ya Adamu. Yusufu alikuwa mtumwa katika nyumba ya mkuu wa baraza ya Kimisri Potifa. Mke wa Potifa akajaribu kumtongoza Yusufu, pengine kwa sababu alishawishwa na uzuri wa maungo ya mwili wa Yusufu. Kwa kuwa Yusufu alikuwa mtumwa tu, angaliweza kwa vyepesi kujiona mwenye wajibu wa kumtii mwanamke huyo, pengine akitumainia kufanya cheo chake kiwe bora. Lakini, Yusufu akakataa kabisa utongozi wake wa ufisadi, akisema, “Nifanyeje ubaya huu mkubwa nikamkose Mungu?” (Mwa. 39:1-9) Ni nini kilichomwongoza Yusufu auone uzinzi kama kumtenda Mungu dhambi?

9. Kwa sababu gani Yusufu alikataa kufanya uzinzi akionyesha ni ‘kumkosa Mungu’?

9 Yeye hakuona hivyo kwa sababu ya sheria fulani ya Mungu iliyoandikwa ikikataza uzinzi, kwa maana sheria hiyo ilitokea baadaye tu katika Amri Kumi. (Kut. 20:14) Sasa Yusufu alikuwa Misri, mbali na mkazo wo wote wa jamaa au sheria za mababa wa ukoo. Kwa wazi dhamiri ya Yusufu ilihusika. Aliona uzinzi utachafua maono yake ya adili. Inaelekea angeweza ‘kujisikia’ ni vibaya kuchukua kitu kisicho chake, mke wa mwanamume mwingine. Nayo maono haya yaliweza kutiwa nguvu kwa kuwa alifikiria uhakika wa kwamba mwanamume na mke wake ni “mwili mmoja,” uhakika ambao Adamu aliufahamu sana. (Mwa. 2:24; Mt. 19:4, 5) Vile vile, inaelekea alikuwa amekwisha pata habari juu ya matendo ya Ibrahimu na Isaka, ambayo hayakuonyesha kukubaliana na uzinzi. (Mwa. 20:1-18; 26:7-11) Kwa hiyo, hata bila ya kuwa na sheria ya kukataza uzinzi dhamiri ya Yusufu ingeweza kumwongoza aukatae.

10. Kuna ushuhuda gani kwamba mataifa mengine pia yalirithi uwezo wa dhamiri?

10 Lakini ikiwa Adamu alipitisha kadiri fulani ya dhamiri kwa wazao wake, je! mke wa Potifa pia asingalipaswa kuona kwamba uzinzi ni mbaya? Ndiyo, ingawa kwa wazi aliacha nyege zimtawale. Wamisri, pamoja na watu duniani pote, walijua kwamba uzinzi ulikuwa kosa kubwa la adili. Maandiko yao yaliyo ya kale zaidi ya kidini yalishirikisha Hukumu ya Mwisho na kupima “moyo.” Naye mtu alihukumiwa juu ya nini? “Kitabu cha Wafu” cha kale cha Wamisri kinaonyesha marehemu akitangaza kutokuwa kwake na hatia, akisema, ‘Mimi sikunyang’anya. Mimi sikuua watu. Mimi sikusema uongo. Mimi sikuchafua mke wa mwanamume ye yote.’ Kwa hiyo, bila shaka dhamiri iliwaongoza kuona ubaya wa uzinzi. Akizungumza juu ya dhamiri, mwanahistoria Yosefo baadaye aliandika habari za maombi ya Yusufu kwa mke wa Potifa aepuke tamaa mbaya ambayo ingeleta huzuni kuu na masumbufu, awe mwaminifu kwa mume wake na kufurahia “dhamiri njema.”

11. Maelezo ya Biblia na yasiyo ya Biblia yanaonyeshaje namna dhamiri yenye kufanya kazi inavyokuwa?

11 Zaidi ya hayo, tunaona masimulizi ya Biblia na yasiyo ya Biblia pia yanayoonyesha dhamiri inavyofanya kazi. Wakati mmoja Mfalme Daudi wa Israeli aliagiza watu wa taifa wahesabiwe. Biblia inasimulia Daudi alivyojisikia alipojua amefanya dhambi. Ikionyesha namna dhamiri inavyofanya kazi, Biblia inasema kwamba “ndipo moyo wake Daudi ukamchoma.” (2 Sam. 1-10) Matokeo kama hayo ya dhamiri iliyochomwa yanatajwa katika ubao wa kale wenye maandishi ya Kibabeli yanayoonyesha sala ya Mbabeli aliyekuwa ametenda dhambi. Alimwomba sana mungu wake asikilize “kwa ajili ya kifua chake, ambacho kinalalama kama filimbi inayozidi kulialia.”

12. (a) Kwa hiyo, uamuzi gani unaweza kufikiwa kwa kufaa juu ya uwezo wa dhamiri, kama ilivyoonyeshwa na mtume Paulo? (b) Je! dhamiri inaonyeshwa na watu wote?

12 Haya yote yanaonyesha kwamba tunayo dhamiri kwa sababu ya kurithi akili na maono ya adili kutoka kwa Adamu. Hivyo, hata mataifa ambayo hayakujua lo lote juu ya torati ya Musa iliyopewa na Mungu, yalikataza mambo kama vile wizi, kusema uongo, zinaa ya maharimu (uasherati wa mtu na dada yake, mama yake, binti yake n. k.), uuaji na uzinzi. Ndivyo, ingawa ni “wasio na sheria,” ‘wanafanya kwa asili mambo ya sheria.’ Mtume Paulo alikazia msingi wa kanuni zao za adili, akisema, “dhamiri yao [Kigiriki syneiʹdesis] ikiwashuhudia, na mawazo yao, yenyewe kwa yenyewe yakiwashitaki au kuwatetea.” (Rum. 2:14, 15) Uwezo wa dhamiri uliopewa na Mungu unapatikana katika ulimwengu wote hata kitabu kimoja chenye maarifa ya namna zote (encyclopedia) kinasema hivi: “Hakuna utamaduni usiokubali dhamiri kama kitu cha kweli.” Na kwa habari ya watu mmoja mmoja wanaoelekea ‘kutokuwa na dhamiri,’ Dr. Geoffrey Stephenson aliandika hivi: “Ilikuwa ikionwa na ingali inaonwa na wengine kama namna ya kweli ya wazimu au hali ya kuwa na ugonjwa wa akili.”​—Linganisha Tito 1:15.

DHAMIRI​—KAZI YAKE NA MAZOEZI

13. Kwa sababu gani mengi zaidi yanahitajiwa kuliko kujua tu kwamba tunayo dhamiri?

13 Kwa hiyo, je! tunaweza ‘kufanya kwa asili tu mambo ya sheria’? Sivyo, mengi zaidi yanahitajiwa. Kufahamu tu chanzo cha kweli cha dhamiri na ilivyokuwa ndio tukawa na uwezo huo hakutuhakikishii kwamba tunafaidika kabisa kutokana nayo. Kumbuka kwamba Wamisri wa kale walikuwa na kanuni fulani za adili zilizoonyesha matokeo ya dhamiri. Lakini hayo tu yalitosha? Je! hiyo peke yake iliwalinda na kila jambo lisilofaa? Ibada yao ya kuchukiza ya wanyama, ‘kukisujudia kiumbe na kukiabudu badala ya Muumba,’ inahakikisha kwamba kuwa na kadiri fulani ya dhamiri hakukutosha. (Rum. 1:20-25) Kwa hiyo, imetupasa tujue mengi zaidi kuliko kujua tu tuna dhamiri. Inatupasa tujue namna inavyofanya kazi, namna inavyoweza kuzoezwa na mambo ambayo Mungu anasema juu ya kuitumia kwetu katika maisha yetu ya kila siku.

14. Njia moja ambavyo dhamiri yako inafanya kazi ni gani?

14 Mifano ya Biblia ambayo tumeangalia inaonyesha njia mbili ambazo katika hizo dhamiri yako inaweza na imepaswa ifanye kazi. Inaelekea kazi ya dhamiri inayofikiriwa na watu wengi zaidi ni ile ya kutazama nyuma na kuamua matendo ya mtu yaliyopita ya adili yalivyo. Tumeona namna hii ya kufanya kazi katika habari ya dhambi ya Adamu na maono ya Daudi alipokwisha kutenda isivyofaa. Dhamiri zao ziliwachoma. Je! wewe hujapata kusikia dhamiri yako ikifanya kazi kwa njia hii? Sauti ya ndani ya dhamiri inayosumbua wale ambao wamefanya mabaya inaweza kusisitiza sana hata wachukue hatua ya nguvu sana kusafisha dhamiri yao au huenda wakaumizwa na dhamiri yao kwa miaka mingi.

15. Hii inaweza kukusaidia katika njia gani ya maana?

15 Hata hivyo, matokeo ya maana zaidi ya utendaji huu wa dhamiri ni kwamba inaweza kumwongoza mtu atubu kwa njia ya kimungu. Daudi aliandika hivi: “Niliponyamaza mifupa yangu ilichakaa kwa kuugua kwangu mchana kutwa. Nalikujulisha dhambi yangu, wala sikuuficha upotovu wangu. Nalisema, Nitayakiri maasi yangu kwa [Yehova], nawe ukanisamehe upotovu wa dhambi yangu.” (Zab. 32:3, 5) Hivyo, dhamiri yako yenye kufanya kazi inaweza kukurudisha kwa Mungu, ikikusaidia uone uhitaji wa kupata msamaha wake na kufuata njia zake wakati ujao.​—Zab. 51:1-4, 9, 13-15.

16. Ni kwa njia gani nyingine dhamiri yako inavyoweza kufanya kazi na inavyopaswa kufanya kazi?

16 Ile kazi nyingine ya dhamiri ni utendaji wake wa mapema katika kuongoza na kumshauri mtu anayepaswa kufanya uchaguzi au uamuzi wa adili. Mwalimu mtoa hotuba anayeitwa Eric D’Arcy alisema hivi: “Katika maandishi ya wapagani dhamiri haikufanya kazi mpaka baada ya tendo lenyewe kufanywa, nayo kazi yake ilikuwa ya kuhukumu peke yake; lakini katika [Biblia], dhamiri inaonyeshwa kuwa yenye kufanya kazi ya kukataza mambo.” Namna hii ya dhamiri ndiyo iliyomwezesha Yusufu kuona mapema kwamba hapaswi kufanya uzinzi. Alifuata dhamiri yake kukataa mwendo uliokuwa ukipigana na maono yake ya adili. Je! dhamiri yako imepata kufanya kazi kwa njia hii? Je! inakusaidia inavyopaswa kukusaidia?

17, 18. (a) Kuna hatari gani mtu akizuia dhamiri yake? (b) Hii ingemwacha mtu katika hali gani?

17 Njia hizi mbili za kufanya kazi kwa dhamiri yetu zinahitaji kufikiriwa na kuzoezwa ikiwa itatuongoza nasi tujifaidi nayo. Inaonekana wazi kwamba njia yo yote kati ya hizi mbili haiwezi kupuzwa wala kuzuiwa kutokana na yanayotukia zinapopuzwa au kuzuiwa. Kwa kawaida, huenda dhamiri ya mtu ikamchoma kidogo au kumpa kionyo cha kwamba ni vibaya kusema uongo au kuiba kwa sababu ya kuirithi kwa Adamu. Hiki kinafanana na kionyo unachopata mkono wako unapokaribia mwali wa moto; maono yako yaliyowekwa ndani yenye kupokea vionyo yanakuamsha uone hatari nawe unaweza kuuondoa mkono wako. Lakini namna gani ikiwa ulikuwa umekwisha kuwa na makovu magumu katika sehemu hiyo ya mkono wako, au pengine mkono wako ulipata kovu baya sana kwa kuungua hapo zamani? Basi huenda maono yako ya ndani yakazuiwa; kovu lenyewe litafanya sehemu hiyo iwe isiyosikia uchungu wo wote. Ndivyo dhamiri inavyoweza kufa ganzi ikiwa inapuzwa-puzwa au kuzuiwa-zuiwa. Mtume Paulo aliandika juu ya watu “ambao dhamiri zao zimekufa sawasawa na nyama iliyounguzwa.” (1 Tim. 4:2, J. B. Pillips) Watu hao, kwa sababu ya kutokuwa na maumivu ya dhamiri, wangeweza kusema uongo, kutenda kwa unafiki au kupotosha Wakristo kwa makusudi, kama Paulo alivyosema.

18 Kwa hiyo, dhamiri iliyopuzwa au iliyozuiwa si kwamba tu inamwumiza mtu akiisha kufanya jambo baya, bali pia inakosa kutoa uongozi wenye kutegemeka mapema. Watu walio katika hali hiyo walisimuliwa katika Waefeso 4:19: “Maoni yao ya yaliyo haki na mabaya yakiisha kuwa mazito, wamejiachilia kwa uasherati nao wanafuatia kwa bidii kazi ya kila siku ya ukosefu wa adabu wa kila aina.” (Jerusalem Bible) Ni vyepesi kufahamu sababu gani Hitler alitaka kuwaingiza watu katika hali hiyo. Dhamiri yao isingewazuia hata kidogo, bali wangeweza kufanya lo lote waliloombwa, hata liwe lilikuwa la upotovu namna gani. Kwa kweli tunataka kuepuka kuwa hivyo, badala yake tuendelee kuitumia dhamiri yetu na kuifanya iwe yenye kuitikia.

19. Biblia inasaidiaje mtu awe na dhamiri yenye kufanya kazi?

19 Biblia ni msaada usiolinganika thamani yake katika jambo hili. Kwa kuwa inatoa vionyesho vikubwa zaidi ya vyote juu ya sifa na njia za Mungu, inaweza kutusaidia tujipatanishe na mfano wake. Hivyo mtunga zaburi aliimba hivi: “Unifundishe kufanya mapenzi yako, kwa maana wewe ndiwe Mungu wangu. Roho yako ni njema; na iniongoze katika nchi ya unyofu.” (Zab. 143:10, NW) Kadiri ambavyo tutazidi kujifunza na kuthamini matendo na mapenzi yake, ndivyo tutakavyozidi kutia nguvu maongozi ya dhamiri ya kimungu katika maisha zetu. (Zab. 119:1-16) Sauti ya ndani inakuwa yenye nguvu zaidi na ya wazi zaidi, sawa na vile mwimbaji peke yake anavyopata sauti nzuri zaidi na kusikiwa vizuri zaidi na kama vile mtengeneza saa anavyoona vizuri zaidi kwa kusitawisha sifa hizo na kujizoeza.

20. Kwa kuwa dhamiri inarithiwa, kwa sababu gani Biblia inazo sheria zinazokataza makosa fulani ya adili?

20 Biblia inazo sheria au amri za wazi kutoka kwa Mungu zinazokataza makosa mazito ya adili, kama vile kuiba, kusema uongo, uzinzi na uuaji. Makosa hayo yalikatazwa katika Torati aliyowapa Israeli, nayo makatazo hayo yanarudiwa katika mashauri ya Mungu kwa Wakristo. (Kut. 20:13-16; Efe. 4:28; Kol. 3:9; 1 Kor. 6:9, 10; Ufu. 21:8) Kwa hiyo, hata ikiwa dhamiri ya mtu ilikuwa imefishwa ganzi na yo yote kati ya dhambi hizi kwa malezi yake au mambo yaliyompata maishani, anaweza kwa vyepesi kuona katika Biblia kwamba ni mbaya. Kusingekuwa na msingi wa kusema, ‘Lakini mimi sikusumbuliwa na dhamiri yangu; sikudhani ilikuwa vibaya.’ Tena, sheria hizo zingeruhusu wale wanaosimamia kundi la Kikristo wachukue hatua ili kulinda washiriki wake na mtu ye yote mwenye kuzoea dhambi. Angetengwa na ushirika au kukatiliwa mbali.​—1 Kor. 5:11-13.

21. Kanuni za Biblia zina ubora gani zaidi?

21 Lakini zaidi ya sheria zinazokataza makosa mazito, Maandiko yanazo kanuni za mwenendo zinazoonyesha utu, njia na kanuni za Mungu. Hivi ni vionyesho vyenye maelezo zaidi juu ya namna tunavyoweza kuwa katika mfano wake. Ingawa mifano mingi ya kanuni za Biblia ingeweza kutajwa, angalia vionyesho vya wazi kwamba Mungu ni mwenye haki naye hapendelei. Kwanza, tunaambiwa hivyo waziwazi. (Kum. 32:4; Ayubu 34:10, 12; Matendo 10:34, 35) Nalo hili linaungwa mkono na mifano ya nyakati fulani Mungu alipoonyesha sifa hizo. Kwa mfano, wakati mfalme mtiwa mafuta wa Israeli alipotenda dhambi na kutenda wengine wa raia zake isivyo haki, Yehova alionyesha waziwazi ubaya wa mwendo wake. Na, kulingana na haki ya hukumu ya Mungu mwenyewe, hakukosa kumwadhibu hata mfalme. (2 Sam. sura 11, 12) Kwa kukaza kanuni hizo za mwenendo na vionyesho vya utu wa Mungu katika moyo na akili yetu, tunaimarisha dhamiri yetu ili itende kwa njia yenye kutegemeka. Hivyo tuasoma hivi: “Katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.”​—Mit. 3:6; Zab. 16:8.

22. Toa mfano wa kanuni ya maana ya Biblia. Hii inaweza kuhusu dhamiri ya mtu, na kumfaidi kwa njia gani?

22 Ukiisha kujua kwamba Mungu ni mwenye haki naye hapendelei, je! dhamiri yako isingekuwa yenye kuitikia zaidi juu ya kutotenda wengine isivyo haki wala kutopendelea wengine? Pengine ulilelewa ukiwa na chuki isiyo na sababu nzuri juu ya watu wenye hali fulani ya maisha, kwa hiyo uliwabagua bila kujali. Ikiwa ulikuwa ukitumikia wanunuzi dukani, pengine ulikuwa na maelekeo ya kupuza watu hao au kuwatendea bila kuwajali sana au bila kuwaonyesha fadhili sana. Lakini ndipo ukajifunza juu ya haki ya hukumu ya Mungu katika Biblia na kwamba anaomba wale wanaotaka kibali yake watende kwa njia ya haki na kutokupendelea. (Mik. 6:8; Mit. 24:23) Na ukapata kufahamu kwamba wanadamu wote wametoka kwa wazazi wale wale wa kwanza, Adamu na Hawa. (Matendo 17:26; Mwa. 3:20) Ukikabiliwa na hali kama hii ambayo katika hiyo zamani ungalitenda isivyo haki, sasa “sauti” ya dhamiri yako inakuomba utende kwa haki na kutokupendelea. Vile vile, ukifuata chuki yako ya zamani isiyo na sababu nzuri, inaelekea baadaye dhamiri yako itakusumbua. Itakuwa kama kwamba umesikia sauti iliyo ndani yako ikikulaumu kwa kufuata mwendo uliojua ni mbaya. Kwa hiyo unaweza kuona kwamba dhamiri yako imepewa mazoezi, imenolewa, imekuwa yenye kuitikia zaidi. Sasa inakupa uongozi mzuri zaidi, ikikukaribisha zaidi na mfano wa Mungu.

23. Kwa sababu gani inazidi kuwa vigumu kuamua mambo leo?

23 Kama ilivyotajwa, sisi leo tunakabiliwa na badiliko na uharibifu wa adili ulioenea pote. Hii inafanya mambo yawe magumu zaidi na zaidi kwa wale wanaotaka kushirikiana na sauti ya dhamiri yao. Vile vile, je! haielekei kwamba maisha yanazidi kuwa yenye kutatiza sikuzote? Kunaelekea kuwa na mambo mengi sana ya kufikiriwa ili kufanya uamuzi. Hakimu wa baraza ya hukumu inayoitwa U.S. Supreme Court Felix Frankfurter alisema hivi wakati mmoja: “Karibu mambo yote ni magumu kutatua mbele ya Baraza kwa kuwa yanahusu zaidi ya kanuni moja. Mtu ye yote anaweza kutoa uamuzi juu ya jambo moja ikiwa kanuni moja tu ndiyo inayohusika.”

24, 25. (a) Tunaweza kufanya nini tunapokabiliwa na uamuzi mgumu? (b) Ni kwa njia gani, basi, dhamiri yetu itakavyotusaidia?

24 Hata hivyo, kadiri tunavyojua mambo mengi zaidi juu ya kanuni za kimungu zinazopatikana katika Biblia, ndivyo tunavyoweza kupima mambo na kuamua vizuri zaidi. Tunapokabiliwa na uamuzi, tunaweza kufikiria kanuni za Biblia zinazoelekea kutumika. Ikitegemea namna ya jambo lenyewe, huenda kanuni zenyewe zikawa kama hivi: kuheshimu ukichwa (Kol. 3:18, 20); kuwa mwaminifu katika mambo yote (Ebr. 13:18); kuchukia mabaya (Zab. 97:10); kufuatia yanayoleta amani (Rum. 14:19); kutii wakuu wa serikali (Rum. 13:1; Mt. 22:21); kumtolea Mungu ibada ya pekee (Mt. 4:10); kuepuka ushirika mbaya (1 Kor. 15:33); kutokwaza wengine (Flp. 1:9, 10). Ingawa kanuni zenyewe zitatusaidia, tukiongeza ujuzi wetu juu ya kanuni na njia za Mungu na kuzithamini, sauti ya dhamiri yetu itakuwa yenye kutegemeka zaidi. Paulo alisema kwamba dhamiri yake ilikuwa ‘mshuhudiaji.’ (Rum. 9:1) Dhamiri yetu pia itakuwa mshuhudiaji. Michomo ya dhamiri yetu ambayo imezoezwa na Neno la Mungu itatusaidia kufikiria utu wa Mungu na sifa zake tunapofanya maamuzi.

25 Hivyo, sote tuna kadiri fulani ya dhamiri ya kutuongoza, tuliyopewa na Mungu. Lakini kwa kuongeza ujuzi wetu juu ya sifa na kanuni za Mungu, dhamiri yetu inaweza kuwa yenye thamani hata zaidi katika kuongoza hatua zetu na kufanya maamuzi.

[Picha katika ukurasa wa 436]

Yusufu alisikiliza sauti ya dhamiri yake akakimbia ‘asimkose Mungu’

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki