Je! Biblia Inajipinga Yenyewe?
WAKRISTO wanaiona Biblia kama zawadi kutoka kwa Mungu. Wanaisoma kwa furaha na kwa faida. Kwa upande mwingine, watu wengine mmoja mmoja, wanabisha kwamba Maandiko haya yanajipinga yenyewe na kwa hivyo hayawezi kutegemewa.
Kwa vyo vyote, iwe kwamba watu wanaipinga Biblia au wamejaribu kuielewa na wameshindwa kupatanisha yanayoelekea kutopatana, huenda wakawa na maoni kama hayo. Huenda wakaamini kwamba kwa kweli Biblia inajipinga yenyewe. Hata hivyo, Uchunguzi wa uangalifu na wa kutumia akili unafunua nini?
JE! KUNA KUTOPATANA KWA HABARI HIZI?
Wenye kuitoa Biblia makosa wanapopata shida wanapoisoma Biblia, wanakuwa na nia ya kuwa na maoni yasiyofaa upesi, wakiamua mambo haraka-haraka. Walakini, wale wanaoithamini Biblia kama zawadi ya Mungu kwa wanadamu wanakuwa na maoni yanayofaa katika kuchunguza wapate majibu. Angalia jinsi upatano wa maandiko unavyoweza kuelezwa.
Ni nani aliyemwuza Yusufu katika Misri? Mwanzo 37:27 kinasema kwamba nduguze Yusufu ndio waliomwuza. Lakini andiko linalofuata linasema: “Wakapita wafanya biashara Wamidiani; basi [ndugu baba mzazi mmoja na Yusufu] wakamtoa Yusufu, wakampandisha kumtoa katika birika, wakamwuza Yusufu kwa Waishmaeli kwa vipande vya fedha ishirini; nao wakamchukua Yusufu mpaka Misri.” Hivyo basi, je! wafanya biashara Wamidiani ndio waliomtoa Yusufu katika birika na kumwuza Yusufu kwa Waishmaeli kwa vipande ishirini vya fedha ambao walimpeleka mpaka Misri? Sivyo, baadaye hata Yusufu mwenyewe alikubali kwamba ndugu zake wenyewe ndio waliokuwa wamemwuza, akisema: “Mimi ni Yusufu, ndugu yenu, ambaye mliniuza kwenda Misri.” (Mwa. 45:4) Kwa hiyo tufanye uamuzi gani? Kwamba ama Wamidiani hawa (ambao walikuwa na ujamaa na Waishmaeli) pia waliitwa Waishmaeli au kwamba wafanya biashara hawa Wamidiani walikuwa wakisafiri na Waishmaeli. Yusufu akauzwa na ndugu zake kwao.
Ni Waisraeli wangapi waliokufa kwa kufanya uasherati na wanawake wa Moabu na kwa kufanya ibada ya uongo kwa Baali ya Peori? Mtume Paulo alisema: “Wala tusifanye uasherati, kama wengine [Waisraeli jangwani] wao walivyofanya, wakaanguka siku moja watu ishirini na tatu elfu [23,000].” (1 Kor. 10:8) Walakini, likitaja ilo hilo Hesabu 25:9 linaripoti: “Nao waliokufa kwa pigo hilo walikuwa watu [24,000] elfu ishirini na nne hesabu yao.” Huenda ikawa kwamba hesabu ya waliouawa ilikuwa katikati ya 23,000 na 24,000, kwa hiyo, hesabu yo yote kamili ya hizi mbili ingefaa. Kwa upande mwingine, kitabu cha Hesabu sana sana kinataja uhakika wa kwamba “wakuu wote wa watu” waliojiungamanisha na Baali-peori waliuawa na waamuzi. (Hes. 25:4, 5) Huenda ikawa kulikuwa na “wakuu,” hawa 1,000 wakifanyiza hesabu ya watu 24,000 wakiongezwa kwa wale 23,000 wanaotajwa na Paulo. Mtume huyo aliandika kwa uongozi wa Mungu, na kwa hiyo, yeye hakukosea. Pia, ijapokuwa ni wazi kwamba watu 23,000 ni wale waliokufa moja kwa moja kwa sababu ya pigo lililotoka kwa Mungu, wote 24,000 kwa ujumla walipatwa na pigo la Yehova kwa kuwa wote walikufa chini ya hukumu ya Mungu.—Kum. 4:3.
Ni wakati gani Mfalme Daudi alipowaandikisha watu kwa makosa, kulikuwa na wanaume wangapi wenye kufunga silaha katika Israeli na Yuda? Kulingana na 2 Samweli 24:9, taifa la Israeli lilikuwa na watu 800,000 na Yuda lilikuwa na 500,000. Walakini, kulingana na 1 Mambo ya Nyakati 21:5, kulikuwa na watu 1,100,000 wa Israeli na watu wa Yuda walikuwa 470,000. Ni jambo lisilo la hekima kufikiri kwamba hili lilikuwa kosa la waandishi, kwa sababu habari hizi mbili huenda zikawa ziliangalia hesabu hizi katika njia zinazotofautiana. Kwa mfano, huenda ikawa kwamba washiriki wa jeshi lililokuwapo na/au wakuu wao walihesabiwa, au wakakosa kuhesabiwa. Tena, njia mbalimbali za kuhesabu huenda zikawa zilitokeza tofauti katika kuandikisha watu fulani, yaani, kama walikuwa chini ya Israeli au ya Yuda. Mambo ya Nyakati cha Kwanza 21:6 kinataja kwamba Lawi na Benjamini hawakuhesabiwa pamoja nao, lakini hakuna jambo kama hilo lililoandikwa katika Samweli wa Pili, kikionyesha pia, tofauti kama hiyo.
Daudi alilipa kiasi gani kwa ajili ya kiwanja cha kupuria nafaka alipomjengea Yehova madhabahu kama njia ya kumaliza pigo lililotokea kwa sababu Daudi aliandikisha watu. Kwa wazi, Aurana, au Ornani, ambaye ndiye aliyekuwa mwenyeji wa kiwanja hicho cha kupuria nafaka alitoa mahali hapo, pamoja na ng’ombe na vyombo vya miti kwa ajili ya sadaka, bila malipo yo yote. Lakini Daudi alisisitiza kwamba ni lazima azilipie, na 2 Samweli 24:24 linaonyesha kwamba alikinunua kiwanja hicho cha kupuria nafaka pamoja na hao ng’ombe kwa shekeli 50 za fedha. Walakini, 1 Mambo ya Nyakati 21:25 linasema kwamba Daudi alilipa shekeli 600 za dhahabu kwa ajili ya kiwanja hicho. Inaonekana kwamba mwandikaji wa Samweli wa Pili aliandika tu habari za kununuliwa kwa sehemu yalipojengwa madhabahu pamoja na vitu vya sadaka zilizotolewa wakati huo, na kwamba bei anayoitaja ilikuwa ya vitu hivi tu. Tofauti na hiyo, mwandikaji wa Mambo ya Nyakati wa Kwanza anazungumza mambo juu ya hekalu lililojengwa mahali hapo baadaye, naye anapatanisha kununuliwa huko na ujenzi huo. (1 Nya. 22:1-6; 2 Nya, 3:1) Kwa kuwa eneo lote la hekalu lilikuwa kubwa, ni wazi kwamba kiasi cha shekeli 600 za dhahabu kilitumika katika kununua anaandika juu ya njia ambayo katika hiyo ndogo iliyohitajiwa kwa kujenga madhabahu yaliyojengwa kwanza na Mfalme Daudi.
KUPATANISHA MAANDIKO KATIKA MAANDIKO YA KIKRISTO
Watu wengine mmoja mmoja wanabisha kwamba habari zilizoandikwa katika Injili juu ya Yesu Kristo na sehemu nyingine katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo hazipatani. Lakini hapo pia kutokupatana kunakodaiwa kunaweza kupatanishwa. Angalia mifano michache tu inayoonyesha kwamba maandiko mbalimbali katika Maandiko ya Kikristo yanapatana.
Pepo wabaya walioingia katika kundi kubwa la nguruwe ambalo baada ya hapo lilitelemka kwa kasi na kuzama katika Bahari ya Galilaya walikuwa wametolewa na Yesu katika watu wangapi? Mwandikaji wa Injili Mathayo anataja watu wawili. (Mt. 8:28) Lakini Marko na Luka wanataja mtu mmoja tu. (Marko 5:2; Luka 8:27) Bila shaka Marko na Luka wanaeleza habari za mtu mmoja tu wa wale wawili waliokuwa na pepo wabaya kwa sababu kisa chake kilikuwa cha kutokeza zaidi. Labda alikuwa mjeuri zaidi na labda alikuwa ametaabishwa kwa muda mrefu zaidi na pepo hawa waliokuwa wakimtawala kuliko alivyokuwa huyo mtu mwingine. Baadaye huenda ikawa kwamba mtu huyo mmoja peke yake ndiye aliyetaka kumfuata Yesu. Badala ya kukubaliana naye, Yesu alimwagiza awatangazie watu mambo ambayo Yehova alikuwa amemfanyia. (Marko 5:18-20) Katika hali ambayo karibu inafanana na hiyo, Mathayo alisema juu ya vipofu wawili ambao waliponywa na Yesu, lakini Marko na Luka wanamtaja mtu mmoja tu. (Mt. 20:29-34; Marko 10:46; Luka 18:35) Kwa kuwa ni wazi kwamba mazungumzo ya Yesu sana sana yalikuwa yanaelekezwa kwa mtu mmoja katika visa hivi viwili, Marko na Luka hawakutaja uhakika wa kwamba kulikuwako mtu mwingine aliyekuwa na pepo wabaya na mtu mwingine kipofu. Hata hivyo, habari katika Injili ya Mathayo haikosei kwa sababu ya kutoa habari hizi nyingi zaidi.
Ni nani aliyeuchukua mti wa mateso wa Yesu? Mtume Yohana alisema juu ya Yesu hivi: “Hali akijichukulia [mti wake wa mateso],” akatoka Yerusalemu. (Yohana 19:17) Lakini Mathayo, Marko na Luka wanasema kwamba ‘walipokuwa wakitoka, Simoni alishurutishwa auchukue mti wa mateso.’ (Mt. 27:32; Marko 15:21; Luka 23:26) Kwa kweli, Yesu Kristo alijichukulia mti wake wa mateso kama Yohana alivyoandika. Walakini, katika habari yake aliyoandika mambo mengi kwa ufupi, Yohana hakuongeza kwamba baadaye Simoni alishurutishwa auchukue mti wa mateso. Kwa hiyo habari za Injili zinapatana katika jambo hili.
Yuda Iskariote alikufa katika njia gani? Mathayo 27:5 anasema kwamba Yuda alijinyonga. Lakini, Matendo 1:18 linasema hivi: “Akaanguka kwa kasi akapasuka, matumbo yake yote yakatoka.” Ijapokuwa inaonekana kwamba Mathayo anaandika juu ya njia ambayo katika hiyo Yuda alijaribu kujiua, Matendo kinaeleza matokeo yake. Zinapoangaliwa zote pamoja, inaonekana kutoka habari zote mbili kwamba Yuda alijaribu kujinyonga juu ya mtelemko, lakini ama kamba au tawi lilikatika akaanguka kwa kasi na kupasuka katika miamba iliyokuwa chini. Bila shaka uwezekano kama huo unaweza kufahamika, kwa sababu ya hali ya nchi iliyoizunguka Yerusalemu.
NI NENO LA MUNGU LA KWELI
Bila shaka, baada ya kuchunguza mifano michache tu inayoonyesha kwamba Maandiko yanapatana, utakubaliana na mtunga Zaburi aliyesema kwa Mungu: “Jumla ya neno lako ni kweli.” (Zab. 119:160) Vilevile, Wakristo Wathesalonike wa karne ya kwanza walilipokea “neno la Mungu” kwa kuthamini. Mtume Paulo aliandika hivi: “Kwa sababu hiyo sisi nasi twamshukuru Mungu bila kukoma, kwa kuwa, mlipopata lile neno la ujumbe la Mungu mlilolisikia kwetu, mlilipokea si kama neno la wanadamu, bali kama neno la Mungu; na ndivyo lilivyo kweli; litendalo kazi ndani yenu ninyi mnaoamini.”—1 The. 2:13.
Vivyo hivyo leo, mashahidi Wakristo wa Yehova wanaiona Biblia yote kuwa Neno la Mungu la kweli. (2 Tim. 3:16, 17) Wanalisoma na kujifunza kwa bidii ili waweze kuzungumza juu ya Biblia, washiriki na wengine ujumbe wake unaookoa uhai. Ufahamu mzuri wa mafundindisho ya kweli ya Maandiko unampa mtu uhuru kutokana na ushirikina na dini ya uongo. (Yohana 8:32; Ufu. 18:4) Kutumia sheria na kanuni za Biblia za adili kunaleta maisha yenye furaha na uradhi sasa, pamoja na tumaini la uzima wa milele katika taratibu mpya ya Mungu aliyoiahidi. Kwa hiyo, lipate na ‘ulishike sana neno la uzima,’ kama linavyopatikana katika Biblia ujifurahishe uhusiano (urafiki) wenye thamani kubwa na Yehova Mungu, Rafiki mkubwa zaidi wa wanadamu.—Flp. 2:14-16.