Je! Watu Wanaona Ni Vigumu Kufuata Shauri Lako?
“Ewe Joseph Njuguna, unajua kinachokuharibu? Wewe ni mtu wa maneno-maneno. Husikilizi kamwe. Una shingo ngumu. Mimi nakushauri ubadili nia yako. Nimekwisha kuambia hivyo nami nakuambia tena, badili nia yako! Anza kuheshimu watu! Wewe unadhani unajua yote, saa zote ni maneno-maneno tu, nawe utaingia matatani! Tena ukiingia, usije ukinililia kuniomba msaada!”
1. Kwa sababu gani mfano unaotajwa katika picha ndiyo njia isiyofaa ya kushauri watu?
HIYO ni njia moja ya kushauri mtu asikilize sana badala ya kuwa na maneno mengi. Lakini, ndiyo njia isiyofaa. Njia hiyo ni kama kushambulia mtu, nayo itamfanya mtu anayeshambuliwa atake kujitetea. Huenda shauri lenyewe likawa ni zuri, lakini halitaleta faida yo yote.
2, 3. (a) Mashirika ya kibiashara yanaonyeshaje kwamba yanataka watu washauriwe ifaavyo? (b) Paulo alimpa Timotheo mawaidha gani juu ya kutoa shauri, nalo kusudi la kushauri ni nini?
2 Mashirika yanalipa maelfu ya shilingi (au makuta) yatume wakuu wao vyuoni ili wakazoezwe jinsi ya kushauri watu na jinsi ya kufanya waambiwapo mambo magumu. Hata hivyo, njia zinazofaa sana za kufanya hivyo ziliandikwa zamani za kale katika Biblia, nazo zinajulikana bila ya mtu kutoa malipo.
3 Mtume Paulo alimwambia Timotheo kwamba, “kwa kuwapa ndugu mashauri hayo utakuwa mhudumu mzuri wa Kristo Yesu.” Hakumfundisha shauri analopaswa kuwapa tu, bali pia jinsi ya kuwapa: “Usilaumu mwanamume mzee vikali. Bali, msihi kama baba, wanaume vijana kama ndugu, wanawake wazee kama mama, wanawake vijana kama dada kwa usafi wote.” Alitumia neno kusihi, si kufanya ukorofi. Kusudi la kufanya hivyo ni kurudisha mtu, si kumfukuzia mbali.—1 Tim. 4:6, NW; 5:1, 2, NW; Yak. 5:19, 20.
4. Kwa sababu gani lazima mshauri awe mwangalifu?
4 Kutoa shauri ambalo umeombwa ni kazi inayohitaji uangalifu; kulitoa bila kuombwa kunahitaji uangalifu mwingi hata zaidi. Shauri ambalo halikuombwa linaelekea kuwa kama lawama, na hakuna mtu apendaye kulaumiwa. Subira na ujuzi wa kufundisha zinahitajiwa ili kushauri mtu bila kumwudhi, wala haitoshi kumtolea maneno mengi ya kumkemea tu. Ndiyo sababu Paulo alimwandikia Timotheo hivi: “Karipia, kemea rasmi, shauri kwa shauku nyingi, pamoja na ustahimilivu wote na ustadi wa kufundisha.”—2Tim. 4:2, NW.
NIA YA MSHAURI
5. Tukifuata mfano wa Yesu katika kutoa shauri, mwenendo wetu na nia yetu itakuwa nini?
5 Kristo Yesu, Mshauri wa Ajabu, aliweka mfano wa kushauri watu kwa upole wakati mitume walipobishania ukubwa. Aliwapa mfano na kuwaonyesha tofauti ya kwamba wafalme wa mataifa walikuwa wakipiga ubwana juu yao, lakini “kwenu ninyi sivyo.” Yesu alikuwa mwanadamu mkamilifu, nayo mashauri aliyotoa yaliongozwa na Mungu; hata hivyo alikuwa “mpole na mnyenyekevu wa moyo.” Inatufaa tufuate mfano wake. “Iweni na nia iyo hiyo ndani yenu ambayo ilikuwamo pia ndani ya Kristo Yesu.”—Luka 22:24-27; Mt. 11:29; Flp. 2:5.
6. Ni mifano gani inayoonyesha ubora wa kutumia mifano katika kushauri watu?
6 Ni vigumu kuhojiana na watu wenye hasira kali, nao mitume walikuwa wakibishana vikali wakati huo. Yesu alitumia mfano wa jinsi wafalme wenye kujiona walivyopiga ubwana juu ya wengine, basi mitume walipojiona katika hali hiyo wakatulia. Nabii Nathani pia alitumia busara wakati alipomshauri Mfalme Daudi kwa sababu ya kumchukua Bath-sheba, mkewe Uria. Alimwambia kwamba tajiri mwenye kondoo na ng’ombe wengi alimchukua mwana-kondoo wa kike aliye mmoja tu wa mtu maskini, ili alishe mgeni. Daudi alikasirika sana akaamua hivi: “Mtu huyo aliyetenda jambo hili, hakika yake astahili kufa”! Ndipo alipoelezwa kwamba yeye ndiye mtu huyo. (2 Sam. 12:1-9) Leo, mifano inaweza kutumiwa kushinda hali za moyoni za watu na kuwasaidia wawe na maoni yanayofaa.
7. Kwa sababu gani ni jambo la maana kufikiria maoni ya mshauriwa?
7 Maoni ya moyoni yanafaa yaangaliwe. Mshauri anapaswa aangalie maoni yake mwenyewe na vilevile maoni ya mshauriwa. Akitoa shauri kwa kujiona kuwa mkubwa na mwenye haki, huenda akafanya haraka isiyohitajiwa ya kutolea watu maneno mengi ya kuwakemea kwa sababu ya vikosa vidogo. (Mhu. 3:7) Mshauriwa atajua kwamba mshauri wake anajiona kuwa hivyo, kwa hiyo akionyesha nia mbaya huenda kosa likawa la mshauri, si la shauri lenyewe. Mithali 15:1 inasema: “Jawabu la upole hugeuza hasira; bali neno liumizalo huchochea ghadhabu.”
MTUME PAULO AWEKA MFANO
8. Paulo alionaje wakati alipokuwa akiwasahihisha Wakorintho kwa sababu ya kufanya kosa kubwa, nayo matokeo ya kuwasahihisha yalikuwa nini?
8 Wakati watu wanapoonyeshwa upendo na huruma ya kidugu, wanajisikia kwamba wameonyeshwa sifa hizo. Paulo alilazimika kusahihisha kosa kubwa lililofanywa na kundi katika Korintho, nalo lilimhuzunisha sana hata akalazimika kuandika maneno makali, kwa maana baadaye alisema hivi: “Katika dhiki nyingi na taabu ya moyo niliwaandikia na machozi mengi; si kwamba mhuzunishwe, bali mpate kujua upendo wangu nilio nao kwenu jinsi ulivyo mwingi.” Anaonyesha mahangaiko yake katika sura chache zinazofuata pia, anaposema hivi: “Ijapokuwa naliwahuzunisha kwa waraka ule, sijuti. . . . Maana huzuni iliyo kwa jinsi ya Mungu hufanya toba liletalo wokovu lisilo na majuto.”—2 Kor. 2:4; 7:8-10.
9. (a) Ni mifano gani ya Maandiko inayoonyesha mafaa ya kusifu watu kabla ya kuwashauri? (b) Kwa sababu gani kuna ubora wa kusifu wenye kufaidika na shauri?
9 Basi, wapunguzie watu maumivu kwa kuwaonyesha huruma wakati unapowasahihisha. Usiwavunjie heshima, uwaache waendelee kujiheshimu. Yaone mambo mema wanayofanya kisha uyathamini. Iwezekanapo wasifu kabla ya kuwashauri. (Ufu. 2:1-4, 12-14, 18-20) Paulo aliwasifu Wakorintho kwa sababu sasa walitaka sana kuona yaliyo haki yakifanywa na kujiondolea hatia kwa kulisahihisha kosa. (2 Kor. 7:11) Ndipo alipoyataja majisifu aliyomtolea Tito kwa ajili yao: “Kama nimejisifu kwake katika neno lo lote, kwa ajili yenu, sikupata haya: lakini kama tulivyosema na ninyi maneno yote kwa kweli, hivi kujisifu kwetu mbele ya Tito kulikuwa kweli.” (2 Kor. 7:14, Zaire Swahili Bible) Sisi sote tunafanya makosa na tunahitaji kusahihishwa, kwa hiyo tunapofanya jambo la haki tunasaidiwa tunaposifiwa na kuambiwa “Vema.” Tunachangamshwa roho!—Mt. 25:21, 23.
KUJIJARIBU TUONE TULIVYO
10-12. Kwa sababu gani inatupasa tushauri watu kwa fadhili na roho ya upole?
10 Katika kushauri watu tunaweza pia kulikumbuka onyo la upole linalosema “jijaribuni wenyewe kwamba mmekuwa katika imani.” (2 Kor. 13:5) Je! sisi tunaupita mtihani unaotolewa na maandiko yafuatayo?
11 Waefeso 4:32: “Iweni wafadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma.” Je! tunakuwa hivyo tunaposhauri watu?
12 Wagalatia 6:1: “Ndugu, hata ingawa mtu achukua hatua fulani ya uongo kabla ya yeye kuijua, ninyi mlio na sifa za kiroho jaribuni kumtengeneza upya mtu huyo katika roho ya upole, huku kila mtu akijiangalia mwenyewe, usije wewe pia ukashawishwa.” (NW) Je! sisi tunashauri wengine kwa upole, tukijua kwamba hata sisi wenyewe tuna udhaifu?
13, 14. Inatupasa tujue sana nini kabla ya kutoa shauri?
13 Wakolosai 4:6 (New English Bible): “Chunguzeni mwone njia bora ya kuongea na kila mtu mnayekutana naye.” Je! tunatumia wakati tumjue mtu na kuendesha maongezi yetu kwa njia itakayotimiza mahitaji yake?
14 Mithali 18:13: “Yeye ajibuye kabla hajasikia, ni upumbavu na aibu kwake.” Je! sisi tunazifahamu pande zote za jambo kabla ya kushauri mtu?
15, 16. Inatupasa tukumbuke nini juu wetu wenyewe tunaposhauri wengine?
15 Wafilipi 2:3: “Msitende neno lo lote kwa kushindana wala kwa majivuno; bali kwa unyenyekevu, kila mtu na amhesabu mwenziwe kuwa bora kuliko nafsi yake.” Tunaposhauri wengine, je! tunatambua kwamba huenda wakawa bora kuliko sisi katika njia nyingine?
16 Warumi 2:21: “Wewe umfundishaye mwingine, je! hujifundishi mwenyewe? Wewe uhubiriye kwamba mtu asiibe, waiba mwenyewe?” Je! tunaonekana kuwa wanafiki, tukiambia watu wafanye mambo tusiyoyafanya?
17, 18. Inatupasa tujizuie tusifanye nini tunaposhauri mtu, na tutafikiria nini?
17 Yohana 16:12: “[Mimi Yesu] nikali ninayo mengi ya kuwaambia, lakini hamwezi kuyastahimili hivi sasa.” Je! tunaanza kumtajia mtu makosa yake yote tunayoweza kukumbuka na kuichochea hasira yake kwa njia hiyo au kuivunja roho yake, na hali hakuna uhitaji wa kufanya hivyo wakati huo?
18 Mathayo 18:5: (NW); “Ikiwa ndugu yako anafanya dhambi, nenda ukafunue kosa lake kati yako wewe na yeye peke yenu.” Je! kwanza tunamshauri ndugu yetu faraghani, tukiyafikiria maoni yake?
19. Ni uongozi gani mwepesi wa kushauria watu, na faida zake ni nini?
19 Ufuatao ni uongozi mwepesi wa kushauri watu tunaoelekea kuusahau nyakati nyingine: “Nyakati zote watendeeni wengine kama vile ninyi mngependa wawatendee ninyi.” (Mt. 7:12, New English Bible) Sisi tunapenda kueleweka vizuri, kwa hiyo lazima tuwaelewe wengine vizuri. Sisi tunapenda kupewa nafasi ya kutoa maoni yetu wenyewe, kwa hiyo lazima tuwaache wengine watoe maoni yao. Ikiwa hatupendi kukemewa, je! sisi tunaepuka kukemea wengine? Kusikiliza kunahusika katika kushauri mtu, nasi tusikilizapo tunalifahamu tatizo lake na maoni yake, zaidi ya kuonyesha kwamba tuna kiasi. Mtu anaposhauriwa kwa njia hiyo analiona shauri kama mazungumzo wala haoni kama kwamba anakemewa.
SHAURI LAKO LINA UZURI WA KIASI GANI?
20, 21. Ni wakati gani ubora wa shauri letu unapotiliwa mashaka, nasi tunawezaje kulifanya litegemeke kabisa?
20 Nabii Yeremia alisema hivi: “Kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” Ikiwa hawezi kuelekeza hatua zake mwenyewe, anawezaje kuelekeza hatua za mtu mwingine? Baada ya hapo Yeremia alisali akasema: “Ee [Yehova], unirudi.” Tunayajua sana makosa yetu sote hivi kwamba ni vigumu kukubali tusahihishwe na ye yote kati yetu—isipokuwa kama sahihisho tunalopata ni sahihisho la Mungu! Uzuri wa shauri letu unategemea kiasi ambacho linashikamana na Neno la Mungu.—Yer. 10:23, 24.
21 “Kutokupita yale “yaliyoandikwa” ni shauri jema. (1 Kor. 4:6) Tulitoka katika taratibu zinazoongozwa na sheria za wanadamu, sheria zenye kuleta msiba. Hatutaki tena kuwekwa chini ya sheria za kibinadamu zisizotakiwa na Neno la Mungu, kwa maana hatutii ‘kwa utumwa wa macho, kama wajipendekezao kwa wanadamu, bali kwa unyofu wa moyo, tukimcha Yehova,’ tena tunalifuata shauri la Paulo: “Lo lote mfanyalo, lifanyeni kwa moyo, kama kwa [Yehova], wala si kwa wanadamu.” (Kol. 3:22, 23) Sheria za Mafarisayo zililemea watu na kulifanya Neno la Mungu liwe la bure.—Mt. 23:4; 15:3.
22, 23. Mafarisayo walikuwa na nia gani ya kujiona, lakini Paulo alionyeshaje nia tofauti?
22 Mafarisayo walipiga ubwana wakati maafisa waliotumwa wakamkamate Yesu waliporudi mikono mitupu kwa sababu ya kushangazwa na njia yake ya kufundisha. “Je! ninyi nanyi mmedanganyika?” Mafarisayo waliuliza. “Ni nani katika wakuu amwaminiye, au katika Mafarisayo? Lakini makutano hawa wasioifahamu torati wamelaaniwa.” Mafarisayo hawakutoa sababu, bali walisema kwa mkazo kwamba wenye hekima walimkataa Yesu, akasikilizwa na wapumbavu peke yao.—Yohana 7:45-49.
23 Tunaposhauri wengine inatupasa tuwape sababu na kutumia maandiko, wala haitupasi kudai wakubaliane nasi kwa sababu tuna cheo. (Flp. 4:5) Inatupasa tuwe kama Paulo, asiyetumia cheo chake cha mtume ili kukaza watu. Yeye aliwasifu kwa sababu walichunguza waone kama kufundisha kwake kuliitegemea Biblia. “Walilipokea lile neno kwa uelekevu wa moyo, wakayachunguza maandiko kila siku, waone kwamba mambo hayo ndivyo yalivyo. Basi watu wengi miongoni mwao wakaamini.”—Matendo 17:11, 12.
24, 25. (a) Njia ya Shetani ya kutumia Maandiko ilitofautianaje na ya Yesu? (b) Ni mfano gani unaoonyesha kwamba lazima habari zinazozunguka ziweke mpaka wa matumizi ya Maandiko?
24 Ibilisi alitumia Maandiko Matakatifu alipomshawishi Yesu jangwani, naye Yesu alitumia maandiko kumpinga. Wote wawili walitumia maandiko, lakini waliyatumia kwa njia zenye kutofautiana: Shetani aliyatumia vibaya, lakini Yesu akayatumia ifaavyo. (Mt. 4:1-10) Haitupasi kamwe kupinda maandiko kama Shetani ili yatumike jinsi sisi wenyewe tunavyokusudia. Na tuhakikishe kwamba Mungu anasema vile tunavyosema kwamba anasema!
25 Kwa mfano, katika Warumi sura ya 14 tunaonywa tuangalie tusikwaze walio dhaifu kwa habari ya chakula au kinywaji au kitu cho chote. Je! maana yake ni kwamba katika jamaa kubwa mshiriki mmoja akisema anakwazwa kwa sababu kahawa inaletwa mezani, hakuna kahawa inayopasa kuletwa? Au kwamba lazima mtu avae viatu vyeusi kwa sababu mtu fulani ‘anakwazwa’ na viatu vya kahawia? Je! hakuna jambo linaloweka mpaka katika matumizi ya shauri hilo? Habari zinazozunguka zinahusu mambo ya imani, siku zilizoonekana na wengine kuwa takatifu na nyama ambazo wengine walikuwa wakidhani ni najisi. Shauri hilo linahusu mambo ya dhamiri, na inatupasa tujinyime kwa njia yenye kusaidia wengine katika upande huo. Lakini hilo si agizo la kujinyima mambo yote kwa sababu ya kila wazo la kibinafsi lisilohusiana na imani.
UNAPOLIHITAJI, UNAWEZA KULIKUBALI?
26. Tunapoona ni vigumu kukubali adabu, tunapaswa kukumbuka jambo gani katika Waebrania 12:11?
26 Shauri likitolewa kwa upendo na kwa kutumia Maandiko, je! tunaweza kulikubali kwa unyenyekevu? Si vyepesi kulikubali, lakini kufanya hivyo kunaleta faida. “Kila adhabu wakati wake haionekani kuwa kitu cha furaha, bali cha huzuni; lakini baadaye huwaletea wao waliozoezwa nayo matunda ya haki yenye amani.” (Ebr. 12:11) Hapo mwanzoni tuliombwa tujichunguze tuone tunakuwa na nia gani tunapotoa shauri. Sasa acheni tujichunguze tuone kama tuna nia ya kulipokea.
27-31. Ni maandiko na maulizo gani yanayokazia uhitaji wa kusikiliza kwa utulivu tunaposhauriwa?
27 Mithali 17:27: “Azuiaye maneno yake ni mwenye maarifa; na mwenye roho ya utulivu ana busara.” Je! tunasikiliza na kuepuka kukasirika?
28 Mithali 12:15: “Njia ya mpumbavu imenyoka machoni pake mwenyewe; bali yeye aliye na hekima husikiliza shauri.” Je! tunadhani tunajua mambo yote, au tunasikiliza?
29 Mithali 29:20: “Je! umemwona mtu mwenye kuhamaki katika maneno? Afadhali kumtumaini mpumbavu kuliko yeye.” Je! tunajaribu kulipinga shauri mara linapotolewa?
30 Mhubiri 7:9: “Usifanye haraka kukasirika rohoni mwako, maana hasira hukaa kifuani mwa wapumbavu.” Je! tunakasirika upesi kupita kiasi, kuudhika upesi?
31 Yakobo 1:19, 20: “Kila mtu na awe mwepesi wa kusikia, bali si mwepesi wa kusema; wala kukasirika; kwa maana hasira ya mwanadamu haiitendi haki ya Mungu.” Je! tunaweza kusikiliza sahihisho bila kukasirika?
32. Wengine wanaoomba shauri wanaonyeshaje kwamba wanataka kujitetea tu?
32 Nyakati nyingine watu wanachagua kufuata mwendo fulani kisha wanatoka kwa mshauri huyu na huyu mpaka watakapopata mtu wa kukubaliana na wanavyotaka. Katika Israeli ya kale Mfalme Rehoboamu aliendea wazee wakamshauri, lakini akaona kwamba shauri lao halikupatana na alivyotaka. Aliwaendea vijana wakamwambia alivyotaka kuambiwa. Matokeo yakawa ni msiba: Makabila kumi yalimwasi yakajifanyia ufalme wao wenyewe! (1 Fal. 12:1-20) Mtume Paulo alisema kwamba kuna wakati ambao watu wangetafuta na kupata washauri wenye kuwaambia mambo yanayolingana kabisa na yale ambayo wangetaka kuambiwa: “Watajipatia walimu wengi kwa kuwa wana masikio ya kuwasha.”—2 Tim. 4:3, Zaire Swahili Bible.
33. Ni mifano gani inayoonyesha njia inayofaa ya kukubali shauri?
33 Walakini, inatupasa sisi tukubali shauri lenye kuungwa mkono na Neno la Mungu. Wakati Daudi alipokemewa na nabii Nathani, aliitikia kwa kusema: “Nimemfanyia [Yehova] dhambi.” (2 Sam. 12:13) Kundi katika Korintho lililikubali shauri la Paulo likajiondolea lawama. Yesu alionyesha njia fulani inayofaa kufuatwa wakati aliposimulia habari za baba aliyekuwa na wana wawili, akawaambia waende wakafanye kazi katika shamba lake la mizabibu. Mmoja alikubali kufanya hivyo, asifanye. Yule mwingine alikataa lakini baadaye akaenda, akapata kibali ingawa hapo kwanza alikawia kuitikia. (Mt. 21:28-31) Wale wanatoa shauri wanapaswa wawe na subira, wampe mkaripiwa wakati wa kulifikiria shauri.
34. Zaburi 16:7 inawatolea washauri ulizo gani wajichunguze?
34 “Nitamhimidi [Yehova] aliyenipa shauri.” (Zab. 16:7) Je! wale tunaowashauri wataweza kutuhimidi kwa sababu ya shauri letu?
35. Shauri linalotolewa hapa linatofautianaje na lililotolewa katika picha ya kwanza ya makala hii?
35 “Joseph asante kwa sababu ya kukutana nami. Sasa unafanya maendeleo mazuri kundini. Nitakutajia tena kwamba tatizo lako ni kusema kwa njia isiyo ya hekima nyakati nyingine. Bila shaka, sisi sote tuna hatia ya kufanya hivyo; kama Yakobo alivyosema, tusipoutumia ulimi vibaya sisi ni wakamilifu. Paulo aliwashauri wazee katika Efeso mchana na usiku, muda wa miaka mitatu! Kwa hiyo natumaini hutadhani nakuonea kwa kukutajia tena jambo hilo. Unafanya maendeleo, kwa hiyo endelea kujitahidi. Ningependekeza usome tena Yakobo sura ya 3. Wakati wo wote ukihitaji nikusaidie, nifikie bila kusita-sita.”—
Kutoka The Watchtower, Dec. 1, 1977.