MAKALA YA 29
WIMBO 87 Njooni! Mburudishwe
Jinsi ya Kutoa Ushauri
“Nitakupa ushauri jicho langu likikutazama.”—ZAB. 32:8.
JAMBO KUU
Jinsi ya kutoa ushauri kwa njia yenye matokeo.
1. Ni nani wanaohitaji kutoa ushauri? Eleza.
UNAHISIJE kuhusu kutoa ushauri? Baadhi ya watu wanapenda kutoa ushauri. Wengine husita kutoa shauri, au hawajihisi huru kufanya hivyo. Vyovyote vile, pindi kwa pindi sisi sote huhitaji kutoa ushauri. Kwa nini? Kwa sababu Yesu alisema kwamba wafuasi wake wa kweli wangetambuliwa kwa upendo ulio miongoni mwao. (Yoh. 13:35) Na njia moja tunayothibitisha kwamba tunawapenda ndugu na dada zetu ni kwa kuwapa shauri linapohitajika. Neno la Mungu linasema kwamba “urafiki mtamu” unachipuka, au unakua kwa sababu ya “shauri la unyoofu.”—Met. 27:9.
2. Wazee wa kutaniko wanapaswa kuwa na uwezo wa kufanya nini, na kwa nini? (Tazama pia sanduku “Shauri Linalotolewa Katika Mkutano wa Katikati ya Juma.”)
2 Wazee wa kutaniko wanahitaji hasa kujua jinsi ya kutoa ushauri kwa njia yenye matokeo. Yehova, kupitia Yesu, amewapatia wanaume hao mgawo wa kulichunga kutaniko. (1 Pet. 5:2, 3) Njia moja wanayofanya hivyo ni kwa kutoa ushauri unaotegemea Biblia kupitia hotuba wanazotoa kutanikoni. Ni lazima pia wamshauri kondoo mmoja-mmoja, kutia ndani kondoo waliopotea. Wazee, na sisi sote, tunawezaje kutoa ushauri mzuri?
3. (a) Unawezaje kujifunza kuwa mshauri mzuri? (Isaya 9:6; tazama pia sanduku “Mwige Yesu Unapotoa Ushauri.”) (b) Tutazungumzia nini katika makala hii?
3 Tunaweza kujifunza mambo mengi kuhusu jinsi ya kuwa mshauri mzuri kwa kuchunguza mifano ya watu katika Biblia, hasa mfano wa Yesu. Mojawapo ya vyeo ambavyo amepewa ni “Mshauri wa Ajabu.” (Soma Isaya 9:6.) Katika makala hii, tutazungumzia mambo tunayoweza kufanya tunapoombwa kutoa ushauri na mambo tunayoweza kufanya tunapohitaji kutoa ushauri bila kuombwa. Pia, tutachunguza umuhimu wa kutoa ushauri kwa wakati unaofaa na kwa njia inayofaa.
TUNAPOOMBWA KUTOA USHAURI
4-5. Mtu anapotuomba ushauri, tunapaswa kwanza kujiuliza swali gani? Toa mfano.
4 Huenda tukatendaje mtu anapotuomba ushauri? Huenda tukafurahi kwamba tunaaminiwa na tukataka kutoa ushauri bila kukawia. Lakini kwanza tunapaswa kujiuliza, ‘Je, ninastahili kutoa ushauri kuhusu jambo hilo?’ Nyakati nyingine, njia bora tunayoweza kumsaidia mtu ni kwa kutompa ushauri na badala yake kumwelekeza kwa mtu anayestahili kumpatia ushauri kuhusu jambo hilo.
5 Fikiria mfano huu. Tuseme kwamba rafiki yako wa karibu amepatwa na ugonjwa mbaya. Anakwambia kwamba ameanza kufanya utafiti kuhusu tiba zinazopatikana, kisha anaomba utoe maoni yako kuhusu tiba unayoona itamfaa. Huenda una maoni thabiti ya kibinafsi kuhusu jambo hilo, lakini wewe si daktari na huna uzoefu wa kutibu ugonjwa huo. Katika kisa hicho, jambo bora unaloweza kufanya ni kumsaidia rafiki yako kupata mtu anayestahili kumpatia tiba.
6. Kwa nini huenda tukaamua kusubiri kabla ya kutoa ushauri?
6 Hata ikiwa tunahisi kwamba tunastahili kutoa ushauri kuhusu jambo fulani hususa, huenda tukaamua kusubiri kwa muda mfupi kabla ya kumjibu mtu anayetuomba ushauri. Kwa nini? Methali 15:28 inasema kwamba “mwadilifu hutafakari kabla ya kujibu.” Namna gani ikiwa tunafikiri kwamba tunajua jibu? Huenda bado tukatumia wakati fulani kufanya utafiti, kusali, na kutafakari. Kisha tunaweza kuwa na uhakika zaidi kwamba jibu letu linapatana na maoni ya Yehova kuhusu jambo hilo. Fikiria mfano wa nabii Nathani.
7. Unajifunza nini kutokana na mfano wa nabii Nathani?
7 Mfalme Daudi alimwambia nabii Nathani kwamba alitaka kumjengea Yehova hekalu. Mara moja Nathani alimshauri afanye hivyo. Lakini Nathani alipaswa kwanza kutafuta ushauri wa Yehova. Kwa nini? Kwa sababu Yehova hakutaka Daudi ajenge hekalu. (1 Nya. 17:1-4) Kama kisa hicho kinavyoonyesha, tunapoombwa kutoa ushauri, litakuwa jambo lenye hekima ‘kutokuwa wepesi wa kusema.’—Yak. 1:19.
8. Kuna sababu gani nyingine inayofanya tufikirie kwa makini kabla ya kutoa ushauri?
8 Sababu nyingine inayotufanya tufikirie kwa makini kabla ya kutoa ushauri ni: Tunaweza kubeba sehemu ya lawama ikiwa ushauri wetu utasababisha mtu afanye uamuzi utakaokuwa na matokeo mabaya. Kwa kweli, tuna sababu nzuri ya kufikiria kwa makini kabla ya kutoa ushauri.
TUNAPOTOA USHAURI BILA KUOMBWA
9. Ni lazima wazee wawe na uhakika gani kabla ya kutoa shauri? (Wagalatia 6:1)
9 Pindi fulani, ni lazima wazee wa kutaniko wachukue hatua ya kwanza ili kumpa shauri ndugu au dada ambaye amechukua “hatua isiyofaa.” (Soma Wagalatia 6:1.) Huenda mtu akawa anafanya maamuzi yasiyo ya hekima ambayo baadaye yanaweza kumfanya atende dhambi nzito. Lengo la wazee ni kumsaidia mtu huyo abaki katika barabara inayoongoza kwenye uzima wa milele. (Yak. 5:19, 20) Hata hivyo, ili watoe ushauri kwa njia yenye matokeo, kwanza wanahitaji kuhakikisha kwamba mtu huyo kwa kweli amechukua hatua isiyofaa. Yehova anaturuhusu sisi sote tufanye maamuzi yanayotegemea dhamiri zetu wenyewe. (Rom. 14:1-4) Hata hivyo, namna gani ikiwa kwa kweli ndugu amechukua hatua isiyofaa na wazee wameamua kwamba ni lazima wachukue hatua ya kwanza ili kumpa shauri?
10-12. Wazee wanapaswa kufanya nini wanapotoa ushauri bila kuombwa? Toa mfano. (Tazama pia picha.)
10 Wazee wa kutaniko ambao ni lazima watoe ushauri bila kuombwa, wanakabili changamoto fulani hususa. Jinsi gani? Mtume Paulo alisema kwamba mtu anaweza kuchukua hatua isiyofaa kabla hajajua. Hivyo, wazee wanapaswa kwanza kumtayarisha mtu kwa ajili ya kupokea shauri.
11 Kutoa ushauri bila kuombwa ni kama kujaribu kupanda mmea katika udongo mgumu. Mkulima hulilima shamba kabla ya kuanza kupanda mbegu. Kufanya hivyo hulainisha udongo na kufanya uwe tayari kwa ajili ya kupanda. Kisha anaipanda mbegu. Mwishowe, anamwagilia maji ili kuisaidia mbegu ikue. Vivyo hivyo, kabla ya mzee kutoa ushauri bila kuombwa, kwa njia ya mfano itafaa ikiwa atatayarisha udongo. Kwa mfano, mzee atatafuta wakati unaofaa na kisha atamhakikishia ndugu kwamba anamjali na kuna jambo ambalo angependa kuzungumza naye. Ikiwa mshauri anajulikana kuwa mwenye upendo na fadhili, itakuwa rahisi zaidi kwa wengine kukubali ushauri wake.
12 Wakati wa mazungumzo hayo, mzee anaweza kuendelea kulainisha udongo kwa kukubali kwamba kila mtu hufanya makosa na huhitaji shauri pindi fulani. (Rom. 3:23) Kwa sauti ya utulivu na heshima kubwa, mzee huyo anamwonyesha waziwazi kutoka kwenye Maandiko jinsi ambavyo amechukua hatua isiyofaa. Ndugu anapokubali kwamba amefanya kosa, mzee “anapanda mbegu” kwa kumfafanulia kwa njia rahisi, mambo anayohitaji kufanya ili kurekebisha hali hiyo. Mwishowe, mzee huyo “anamwagilia maji” mbegu kwa kumpongeza kwa unyoofu ndugu huyo na kusali pamoja naye.—Yak. 5:15.
Kutoa ushauri bila kuombwa kunahitaji upendo na ustadi (Tazama fungu la 10-12)
13. Wazee wanawezaje kuhakikisha kwamba mtu ameelewa shauri alilopewa?
13 Nyakati nyingine, jambo ambalo mshauri anasema na jambo ambalo yule anayepokea shauri anasikia ni mambo mawili tofauti. Wazee wanaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba shauri wanalotoa linaeleweka kwa njia sahihi? Wanaweza kumsaidia aelewe mambo makuu kwa kumuuliza maswali kwa busara na heshima. (Mhu. 12:11) Majibu yake yatamsaidia mzee anayetoa shauri ahakikishe kwamba mtu huyo anaelewa shauri alilopewa.
KUTOA USHAURI KWA WAKATI UNAOFAA NA KWA NJIA INAYOFAA
14. Kwa nini hatupaswi kutoa ushauri tunapokuwa tumekasirika? Eleza.
14 Sisi sote si wakamilifu, hivyo tunatenda na kusema mambo ambayo yanawaudhi wengine. (Kol. 3:13) Neno la Mungu linasema kwamba nyakati nyingine mtu anaweza kutenda au kusema jambo linalotukasirisha. (Efe. 4:26) Lakini tunapaswa kuepuka kutoa ushauri tunapokuwa tumekasirika. Kwa nini? Kwa sababu “hasira ya mwanadamu haitokezi uadilifu wa Mungu.” (Yak. 1:20) Ikiwa tutatoa ushauri tukiwa tumekasirika, huenda tukafanya hali iwe mbaya zaidi. Hilo halimaanishi kwamba hatupaswi kamwe kumwambia mtu aliyetukasirisha jinsi tunavyohisi. Hata hivyo, tutakuwa na matokeo mazuri zaidi ikiwa tutazungumza na mtu huyo tukiwa na utulivu. Fikiria mfano wa Elihu, mshauri mwaminifu wa Ayubu.
15. Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Elihu? (Tazama pia picha.)
15 Kwa siku kadhaa, Elihu alimsikiliza Ayubu akijitetea dhidi ya mashtaka kutoka kwa wale wafariji wa uwongo. Elihu alimwonyesha huruma Ayubu. Hata hivyo, Elihu pia aliwaka hasira kwa sababu Ayubu hakusema ukweli kumhusu Yehova na alijikazia fikira kupita kiasi. Licha ya hilo, Elihu alisubiri mpaka wakati wake ulipofika, kisha akaanza kuzungumza kwa upole na heshima kubwa alipokuwa akimshauri Ayubu. (Ayu. 32:2; 33:1-7) Mfano wa Elihu unatufundisha ukweli huu muhimu: Njia bora ya kutoa ushauri ni kuutoa kwa wakati unaofaa na kwa njia inayofaa—kwa heshima na upendo.—Mhu. 3:1, 7.
Ingawa mapema alikuwa amewaka hasira, Elihu alitoa shauri kwa upole na heshima kubwa (Tazama fungu la 15)
ENDELEA KUTOA NA KUKUBALI USHAURI
16. Umejifunza somo gani kutoka kwenye Zaburi 32:8?
16 Andiko la msingi la makala hii linasema kwamba ‘Yehova anatupa ushauri jicho lake likitutazama.’ (Soma Zaburi 32:8.) Hilo linaonyesha kwamba ataendelea kutusaidia. Anatupatia ushauri na kutusaidia kuutumia. Huo ni mfano mzuri sana kwetu! Tunapokuwa na pendeleo la kuwashauri wengine, acheni tumwige Yehova kwa kuendelea kuwatazama na kuwategemeza kwa njia yoyote ili kuwasaidia wafanikiwe.
17. Wazee wanapotoa ushauri hususa unaotegemea Biblia, wanajithibitisha kuwa nini? Eleza. (Isaya 32:1, 2)
17 Sasa kuliko wakati mwingine wowote, tunahitaji kutoa na kupokea ushauri mzuri. (2 Tim. 3:1) Wazee ambao wanatoa ushauri hususa unaotegemea Biblia ni “kama vijito vya maji katika nchi isiyo na maji.” (Soma Isaya 32:1, 2.) Marafiki wanaojua mambo tunayotaka kusikia lakini wanatuambia mambo tunayohitaji kusikia wanatupatia zawadi yenye thamani sawa na “matofaa ya dhahabu yaliyonakshiwa kwenye vyombo vya fedha.” (Met. 25:11) Acheni sisi sote tuendelee kusitawisha hekima tunayohitaji ili kutoa na kupokea ushauri mzuri.
WIMBO 109 Pendaneni Sana Kutoka Moyoni