Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w25 Julai kur. 2-7
  • Kwa Nini Tunahitaji Kutafuta Ushauri?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwa Nini Tunahitaji Kutafuta Ushauri?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • NI LAZIMA NIWE NA SIFA GANI?
  • NI NANI ANAYEWEZA KUNIPATIA USHAURI MZURI?
  • NINAWEZAJE KUWA NA MTAZAMO UNAOFAA KUELEKEA USHAURI?
  • JE, NIWAOMBE WENGINE WANIFANYIE MAAMUZI?
  • ENDELEA KUTAFUTA USHAURI
  • Jinsi ya Kutoa Ushauri
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Maamuzi Yanayoonyesha Unamtegemea Yehova
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2023
  • Jifunze Kutokana na Maneno ya Mwisho ya Wanaume Waaminifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
  • Uwe Mwenye Kiasi Inapohusu Mambo Usiyoyajua
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
w25 Julai kur. 2-7

MAKALA YA 28

WIMBO 88 Nijulishe Njia Zako

Kwa Nini Tunahitaji Kutafuta Ushauri?

“Hekima ni ya wale wanaotafuta ushauri.”—MET. 13:10.

JAMBO KUU

Mambo ambayo ni lazima tufanye ili tunufaike kikamili kutokana na ushauri tunaopata.

1. Tunawezaje kufanya maamuzi yenye hekima na kufanikisha mipango yetu? (Methali 13:10; 15:22)

SISI sote tungependa kufanya maamuzi yenye hekima. Na sote tungependa mipango yetu ifanikiwe. Neno la Mungu linatueleza jinsi tunavyoweza kutimiza malengo hayo mawili.—Soma Methali 13:10; 15:22.

2. Yehova anaahidi kutufanyia nini?

2 Bila shaka, Yehova, Baba yetu, ndiye anayeweza kutupatia hekima na ushauri bora kabisa. Anaahidi kutusaidia, anasema hivi: “Nitakupa ushauri jicho langu likikutazama.” (Zab. 32:8) Maneno hayo yanaonyesha kwamba Yehova anafanya mengi zaidi ya kutupatia ushauri—anapendezwa nasi kibinafsi na anatusaidia kutumia ushauri wake.

3. Tutazungumzia nini katika makala hii?

3 Katika makala hii, tutatumia Neno la Mungu kujibu maswali haya manne: (1) Ni lazima niwe na sifa gani ili ninufaike kutokana na ushauri mzuri? (2) Ni nani anayeweza kunipatia ushauri mzuri? (3) Ninawezaje kuwa na mtazamo unaofaa kuelekea ushauri? (4) Kwa nini ninapaswa kuepuka kuwaomba wengine wanifanyie maamuzi?

NI LAZIMA NIWE NA SIFA GANI?

4. Ni lazima tuwe na sifa gani ili tunufaike kutokana na ushauri mzuri?

4 Ni lazima tuwe na sifa ya unyenyekevu na kiasi ili tunufaike kutokana na ushauri mzuri. Tunahitaji kutambua kwamba huenda hatuna uzoefu au ujuzi wa kutosha ili kujifanyia uamuzi wenye hekima sisi wenyewe. Ikiwa hatuna sifa ya unyenyekevu na kiasi, Yehova hataweza kutusaidia. Matokeo ni kwamba, ushauri wowote tutakaopata tunaposoma Neno la Mungu utakuwa kama maji yanayotiririka juu ya jiwe. (Mika 6:8; 1 Pet. 5:5) Hata hivyo, ikiwa sisi ni wanyenyekevu na wenye kiasi, tutakuwa tayari kukubali ushauri wa Biblia tunaosikia na kunufaishwa nao.

5. Daudi alitimiza mambo gani maishani ambayo yangeweza kumfanya awe na kiburi?

5 Fikiria jambo tunaloweza kujifunza kutokana na mfano wa Mfalme Daudi. Mambo aliyotimiza maishani yangeweza kumfanya awe na kiburi. Muda mrefu kabla ya kuwa mfalme, alijulikana kwa uwezo wake mzuri akiwa mwanamuziki. Hata aliombwa kwenda kumpigia kinubi mfalme. (1 Sam. 16:​18, 19) Baada ya Daudi kutiwa mafuta na kuwa mfalme aliyefuata, Yehova alimpatia roho Yake takatifu, iliyompa nguvu. (1 Sam. 16:​11-13) Alikuwa mashuhuri miongoni mwa watu wake kwa sababu aliwaua maadui wao, kutia ndani Goliathi, jitu la Wafilisti. (1 Sam. 17:​37, 50; 18:7) Ikiwa Daudi angekuwa na kiburi, angeweza kufikiri kwamba kwa kuwa aliweza kutimiza mambo yote hayo, basi hakuhitaji kusikiliza ushauri wa watu wengine. Lakini Daudi alikuwa mnyenyekevu.

6. Tunajuaje kwamba Daudi alikuwa tayari kupokea ushauri? (Tazama pia picha.)

6 Baada ya kuwa mfalme, Daudi alishirikiana kwa ukaribu na wanaume waliompa ushauri. (1 Nya. 27:​32-34) Hilo halishangazi kwa kuwa Daudi alikuwa na kawaida ya kusikiliza ushauri mzuri. Hakukubali tu ushauri kutoka kwa wanaume, bali pia kutoka kwa mwanamke aliyeitwa Abigaili. Mume wa Abigaili, Nabali, hakuwa na heshima, shukrani, na alikuwa mwenye majivuno. Kwa unyenyekevu, Daudi alitumia ushauri mzuri wa Abigaili, na matokeo ni kwamba aliepuka kufanya kosa kubwa.—1 Sam. 25:​2, 3, 21-25, 32-34.

Mfalme Daudi akimsikiliza kwa makini Abigaili aliyeketi chini huku akimsihi Daudi.

Kwa unyenyekevu, Mfalme Daudi alikubali na kutumia ushauri wa Abigaili (Tazama fungu la 6)


7. Tunaweza kujifunza masomo gani kutokana na kisa cha Daudi? (Mhubiri 4:13) (Tazama pia picha.)

7 Tunaweza kujifunza masomo fulani kutokana na kisa cha Daudi. Kwa mfano, huenda tuna vipawa fulani au mamlaka ya kadiri. Hata hivyo, hatupaswi kamwe kufikiri kwamba tunajua kila kitu na kwamba hatuhitaji ushauri. Na kama Daudi, tunapaswa kuwa tayari kukubali ushauri mzuri, haidhuru ni nani anayeutoa. (Soma Mhubiri 4:13.) Tukifanya hivyo, tunaweza kuepuka kufanya makosa makubwa yanayoweza kutuletea sisi na wengine huzuni.

Mkusanyo wa picha: 1. Wazee wanne wamekutana. Mzee mmoja anazungumza kwa ukali. 2. Baadaye, katika gari, mzee wa kutaniko kijana aliyekuwa katika mkutano huo anazungumza faraghani na ndugu huyo aliyezungumza kwa ukali.

Tunapaswa kuwa tayari kukubali ushauri mzuri haidhuru unatoka kwa nani (Tazama fungu la 7)c


NI NANI ANAYEWEZA KUNIPATIA USHAURI MZURI?

8. Kwa nini Yonathani alistahili kumpa Daudi ushauri?

8 Fikiria jambo lingine tunaloweza kujifunza kutokana na kisa cha Daudi. Alisikiliza ushauri aliopata kutoka kwa watu waliokuwa na uhusiano mzuri na Yehova na walioelewa vizuri changamoto aliyokuwa akipitia. Kwa mfano, alipotaka kujua ikiwa anaweza kurudisha uhusiano mzuri pamoja na Mfalme Sauli, Daudi alisikiliza ushauri kutoka kwa Yonathani, mwana wa Sauli. Kwa nini Yonathani aliweza kumpatia ushauri mzuri? Kwa sababu Yonathani alikuwa na uhusiano mzuri na Yehova na pia alimjua vizuri Sauli. (1 Sam. 20:​9-13) Tunajifunza nini?

9. Tunapaswa kuzungumza na nani tunapohitaji ushauri? Eleza. (Methali 13:20)

9 Tunapohitaji ushauri, itafaa ikiwa tutaomba ushauri huo kutoka kwa mtu aliye na uhusiano mzuri na Yehova na mwenye uzoefu inapohusu jambo tunalohitaji kusaidiwa.a (Soma Methali 13:20.) Kwa mfano, tuseme kwamba ndugu kijana anatafuta mwenzi wa ndoa anayefaa. Ni nani anayeweza kumpatia ushauri mzuri? Huenda rafiki yake ambaye ni mseja akamsaidia ikiwa atategemea kanuni za Biblia anapotoa ushauri. Lakini ndugu huyo kijana anaweza kupata ushauri hususa zaidi na unaomfaa ikiwa ataomba ushauri huo kutoka kwa wenzi wa ndoa waliokomaa kiroho, wanaomjua vizuri, na ambao wamefunga ndoa kwa muda fulani na wana furaha katika ndoa yao.

10. Tutachunguza nini sasa?

10 Tumechunguza sifa mbili ambazo ni lazima tuwe nazo na ni nani anayeweza kutupatia ushauri mzuri. Sasa, acheni tuchunguze kwa nini tunapaswa kuwa na mtazamo unaofaa kuelekea ushauri na ikiwa tunapaswa kuwaomba wengine watufanyie maamuzi.

NINAWEZAJE KUWA NA MTAZAMO UNAOFAA KUELEKEA USHAURI?

11-12. (a) Pindi fulani huenda tukafanya nini? (b) Mfalme Rehoboamu alifanya nini alipohitaji kufanya uamuzi wa muhimu?

11 Pindi fulani, huenda mtu akaonekana kwamba anatafuta ushauri, lakini ukweli ni kwamba anataka tu kuhakikisha kwamba wengine wanakubaliana na uamuzi ambao tayari amefanya. Mtu huyo kwa kweli hana mtazamo unafaa kwa kuwa anaonyesha kwamba hataki ushauri. Anapaswa kujifunza kutokana na jambo lililompata Mfalme Rehoboamu.

12 Rehoboamu alikuja kuwa mfalme wa Israeli baada ya Mfalme Sulemani. Rehoboamu alirithi taifa lililokuwa na ufanisi mwingi, lakini watu walihisi kwamba Sulemani alikuwa amedai mengi sana kutoka kwao. Watu walimfuata Rehoboamu na kumsihi apunguze mzigo wao wa kazi. Rehoboamu aliwaomba wampe muda ili atafakari kuhusu uamuzi atakaofanya. Alianza vizuri kwa kuomba ushauri kutoka kwa wanaume wazee waliokuwa wamemsaidia Sulemani. (1 Fal. 12:​2-7) Hata hivyo, alikataa ushauri aliopewa na wanaume hao wazee. Kwa nini alifanya hivyo? Je, tayari Rehoboamu alikuwa amefanya uamuzi, na je, alikuwa akitafuta tu mtu anayekubaliana na uamuzi huo? Ikiwa ndivyo, marafiki wake vijana walimpatia ushauri uliopatana na maoni yake. (1 Fal. 12:​8-14) Rehoboamu aliwajibu watu kulingana na ushauri wa rafiki zake. Matokeo ni kwamba taifa hilo liligawanyika, na kuanzia wakati huo na kuendelea alikabili matatizo.—1 Fal. 12:​16-19.

13. Tunawezaje kujua ikiwa tuna mtazamo unaofaa kuelekea ushauri?

13 Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Rehoboamu? Ni lazima tuwe na mtazamo unaofaa tunapoomba ushauri. Tunawezaje kujua ikiwa tuna mtazamo unaofaa kuelekea ushauri? Tunaweza kujiuliza hivi, ‘Je, mimi huomba ushauri, kisha ninaukataa papo hapo kwa sababu si ushauri ninaotaka kusikia?’ Fikiria mfano ufuatao.

14. Ni lazima tukumbuke nini tunapopewa ushauri? Toa mfano. (Tazama pia picha.)

14 Wazia kwamba ndugu amepata kazi yenye mshahara mnono. Kabla ya kukubali kazi hiyo, anamwomba mzee wa kutaniko ushauri. Ndugu huyo anamwambia mzee huyo kwamba kazi hiyo itamlazimu awe mbali na familia yake kwa kipindi kirefu cha wakati. Mzee anamkumbusha ndugu huyo kanuni ya Biblia inayosema kwamba jukumu lake la msingi ni kuiandalia familia yake mahitaji ya kiroho. (Efe. 6:4; 1 Tim. 5:8) Papo hapo, ndugu huyo anakataa ushauri wa mzee huyo na kuanza kuwauliza wengine kutanikoni kuhusu suala hilo mpaka anapopata mtu anayemwambia kwamba anaweza kukubali kazi hiyo. Je, kweli ndugu huyo anatafuta ushauri, au tayari amefanya uamuzi na anatafuta tu mtu wa kukubaliana naye? Ni lazima tukumbuke kwamba moyo ni wenye hila. (Yer. 17:9) Nyakati nyingine, ushauri ambao hatutaki kuusikia, ndio ushauri tunaouhitaji zaidi.

Dada akiomba ushauri kutoka kwa ndugu na dada tofauti-tofauti. Anazungumza na mmoja baada ya mwingine, huku akionyesha kutoridhika na kila ushauri anaopewa.

Je, kweli tunatafuta ushauri mzuri, au tunatafuta tu mtu wa kukubaliana nasi? (Tazama fungu la 14)


JE, NIWAOMBE WENGINE WANIFANYIE MAAMUZI?

15. Tunapaswa kuepuka kufanya nini, na kwa nini?

15 Kila mmoja wetu ana jukumu la kufanya maamuzi yake mwenyewe. (Gal. 6:​4, 5) Kama tulivyozungumzia mapema, mtu mwenye hekima atatafuta ushauri kutoka katika Neno la Mungu na kutoka kwa Wakristo wakomavu kabla ya kufanya uamuzi fulani. Hata hivyo, ni lazima tuwe waangalifu ili tusiwaombe wengine watufanyie maamuzi. Baadhi ya watu hufanya hivyo kwa kumuuliza mtu wanayemheshimu hivi: “Ikiwa ungekabili hali yangu, ungefanya nini?” Wengine huenda wakaiga uamuzi ambao mtu mwingine amefanya bila kufikiria kwa kina kuhusu uamuzi huo.

16. Ni hali gani iliyotokea Korintho kuhusiana na nyama iliyotolewa dhabihu kwa sanamu, na ni nani waliokuwa na jukumu la kuamua ikiwa watakula nyama hiyo? (1 Wakorintho 8:7; 10:​25, 26)

16 Fikiria uamuzi ambao Wakristo wa karne ya kwanza katika kutaniko la Korintho walihitaji kufanya kuhusu nyama iliyotolewa dhabihu kwa sanamu. Paulo aliwaandikia hivi Wakristo hao: “Tunajua kwamba sanamu si kitu ulimwenguni na kwamba hakuna Mungu isipokuwa mmoja.” (1 Kor. 8:4) Wakiwa na jambo hilo akilini, baadhi ya watu katika kutaniko waliamua kwamba wangeweza kula nyama ambayo huenda ilitolewa kwa sanamu na baadaye kuuzwa katika soko la nyama. Wengine waliamua kwamba hawangekula nyama hiyo kwa sababu jambo hilo lingesumbua dhamiri zao. (Soma 1 Wakorintho 8:7; 10:​25, 26.) Huo ulikuwa uamuzi wa kibinafsi. Paulo hakuwashauri kamwe Wakorintho wawafanyie wengine maamuzi au waige maamuzi ya wengine. Kila mmoja ‘angetoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.’—Rom. 14:​10-12.

17. Ni jambo gani linaloweza kutokea ikiwa tutaiga tu maamuzi ya wengine? Toa mfano. (Tazama pia picha.)

17 Hali kama hiyo inawezaje kutokea leo? Fikiria kuhusu suala la visehemu vya damu. Ni lazima kila Mkristo afanye uamuzi wake mwenyewe ili kuamua ikiwa atakubali au atakataa visehemu hivyo vya damu.b Huenda tukaona ni changamoto kuelewa habari hiyo kikamili, lakini kufanya maamuzi kama hayo ni sehemu ya mzigo ambao ni lazima kila mmoja wetu aubebe. (Rom. 14:4) Ikiwa tutaiga maamuzi ya mtu mwingine, tunaweza kudhoofisha dhamiri yetu wenyewe. Tunaweza tu kuizoeza na kuiboresha dhamiri yetu kwa kuitumia. (Ebr. 5:14) Hivyo, ni wakati gani tunapaswa kuomba ushauri kutoka kwa Mkristo mkomavu? Ikiwa bado tunahitaji msaada wa kuelewa jinsi kanuni za Biblia zinavyohusiana na hali yetu baada ya kufanya utafiti wetu wenyewe.

Mkusanyo wa picha: 1. Ndugu anatumia Biblia, somo la 39 katika kitabu cha “Furahia Maisha Milele! ”, na video yenye kichwa “Jinsi ya Kufanya Maamuzi ya Matibabu Yanayohusisha Damu” ili aweze kujaza hati ya mamlaka ya kudumu ya uwakilishi. 2. Baadaye, anamsikiliza ndugu mkomavu anayezungumza naye kwa kutumia andiko.

Tunapaswa tu kutafuta ushauri baada ya kufanya utafiti wetu wenyewe (Tazama fungu la 17)


ENDELEA KUTAFUTA USHAURI

18. Yehova ametufanyia nini?

18 Yehova ameonyesha kwamba anatutumaini sana kwa kuturuhusu tufanye maamuzi yetu wenyewe. Anatupatia Neno lake, Biblia. Na anatupatia marafiki wenye hekima wanaoweza kutusaidia kuelewa jinsi ya kutumia kanuni za Biblia. Ametimiza jukumu lake akiwa Baba yetu. (Met. 3:​21-23) Tunawezaje kumwonyesha kwamba tunamshukuru kwa msaada wake?

19. Tunawezaje kuendelea kumfurahisha Yehova?

19 Fikiria jambo hili: Wazazi wanapenda kuwaona watoto wao wakikua na kuwa watumishi wa Yehova wenye ufikirio, hekima, na wanaowasaidia wengine. Vivyo hivyo, Yehova anafurahi anapotuona tukiendelea kukomaa kiroho, kutafuta ushauri, na kufanya maamuzi yanayomletea heshima.

ILI NINUFAIKE NA USHAURI MZURI, KWA NINI NI LAZIMA . . .

  • niwe mnyenyekevu na mwenye kiasi?

  • niwe na mtazamo mzuri kuelekea ushauri?

  • nifanye maamuzi yangu mwenyewe?

WIMBO 127 Napaswa Kuwa Mtu wa Namna Gani?

a Kwa hekima, pindi fulani Wakristo wanaweza kuomba ushauri kuhusu masuala ya kifedha, kitiba, au mambo mengine kutoka kwa watu ambao si waabudu wa Yehova.

b Ili kupata habari zaidi kuhusu jambo hilo, tazama kitabu, Furahia Maisha Milele!, somo la 39, jambo kuu la 5 na sehemu ya “Chunguza Zaidi.”

c MAELEZO YA PICHA: Mzee wa kutaniko anamshauri mzee mwenzake kuhusu jinsi alivyozungumza katika mkutano waliomaliza kufanya.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki