Maswali Kutoka Kwa Wasomaji
● Katika pigo la kwanza la yale mapigo kumi, Musa aligeuza maji yote ya Misri yakawa damu. Ndipo waganga wa Misri walipojitokeza wakafanya ajabu iyo hiyo. Waliyapata wapi maji waliyotumia?
Kwa habari ya pigo la kwanza, Yehova alimwambia Musa hivi: “Mwambie Haruni, Shika fimbo yako, kaunyoshe mkono wako juu ya maji ya Misri, juu ya mito yao, juu ya vijito vyao, na juu maziwa ya maji yao, na juu ya visima vyao vyote vya maji, ili yageuke kuwa damu, nako kutakuwa na damu katika nchi yote ya Misri, katika vyombo vya mti, na katika vyombo vya jiwe.” Musa na Haruni walitii, ‘na ile damu ikawa katika nchi yote ya Misri.’—Kut. 7:19-21.
Baada ya hapo masimulizi yanasema: “Lakini waganga wa Misri wakafanya mfano wa hayo kwa uganga wao.” (Kut. 7:22) Basi waganga hao walitumia maji gani?
Waelezaji fulani wamewaza wakaona kwamba pigo la kwanza halikuharibu maji yote ya Misri. (Linganisha Kutoka 9:25; 10:5.) Wamesema kwamba mtajo wa maji yaliyokuwa “katika vyombo vya mti, na katika vyombo vya jiwe” haupaswi kufahamika kuwa na maana ya kwamba maji yote yaliyokuwa katika vyombo yaligeuka yakawa damu. Ikiwa maoni yao yanafaa, basi maana ya maneno ya mwisho ya mstari wa kumi na tisa inaweza kuwa kwamba, baada ya Mto Nailo na maji yaliyokuwa katika mitaro yake yote na katika vidimbwi kugeuzwa kuwa damu, kusingepatikana maji ya kujazwa tena katika vyombo baada ya maji yaliyokuwamo kumalizika. Kwa hiyo, kulingana na wazo hilo, inawezekana kwamba waganga walifanya kiinimacho kwa kutumia maji fulani yaliyokuwa yamechotwa katika Mto Nailo kabla ya pigo hilo.
Lakini, kuna uwezekano mwingine unaolingana na mambo ya hakika. Kutoka 7:24 inasema: “Wamisri wote wakachimba-chimba kando ya mto ili wapate maji ya kunywa; maana, hawakuweza kuyanywa yale maji ya mtoni.” Basi, inaonekana kwamba maji mazuri yangeweza kuchotwa kwa kuchimba visima katika udongo wenye majimaji kando-kando ya Mto Nailo. Ikiwa Wamisri waliweza kupata maji ya kunywa katika visima hivyo, labda waganga walitumia kiasi kidogo cha maji hayo ili kuifanya ajabu yao iliyobadili nia ya Farao asiwaache Waebrania waende zao.