Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 5/15 kur. 8-14
  • Wenye Kupigana na Mungu Wanashindwa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wenye Kupigana na Mungu Wanashindwa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JAMII YA KISASA YA YEREMIA
  • KUSONGA MBELE KWA JINA LA KIMUNGU
  • “Watapigana Nawe”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • “Siwezi Kunyamaza Kimya”
    Mungu Asema Nasi Kupitia Yeremia
  • Kaa Macho, Kama Yeremia Alivyofanya
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Yeremia Nabii wa Hukumu za Mungu Asiyependwa na Wengi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 5/15 kur. 8-14

Wenye Kupigana na Mungu Wanashindwa

“Nao watapigana nawe; lakini hawatakushinda; maana mimi nipo pamoja nawe, asema [Yehova], ili nikuokoe.”​—⁠Yer. 1:19.

1. Wanaoshindwa wanapigana na Mungu kwa njia gani?

WENYE kupigana na Mungu! La, hawapigani naye kwa kwenda kinyume cha sheria za uumbaji Wake, kama vile sheria ya uvutano. Bali wanapigana naye kwa kupigana na tengenezo lionekanalo la watu wake wateule na kazi anayowaamuru waifanye. Nyakati za kisasa, huenda watu wanaoziheshimu sana sheria za uumbaji zilizogunduliwa na wanasayansi wakajikuta wakipigana na Mungu wa Biblia Takatifu kwa njia hiyo. Lakini wanashindwa na kuona uchungu moyoni.​—⁠Matendo 5:39.

2. Uhakikisho unatolewaje kuonyesha kwamba Mungu amekikubali kitengenezo kinachotiliwa mashaka na kwamba hajakitupilia mbali?

2 Watu hao wenye kupigana na Mungu wanaona kwamba ni kimbelembele kwa kitengenezo kidogo duniani kujifikiria kwamba ndicho kinacholindwa sana na Mungu ili akikomboe mikononi mwa wenye kupigana naye. Lakini mambo ambayo yamelipata tengenezo hilo yanapaswa kulifanya lijijulie nini lenyewe? Kwa kuwa limeona ushuhuda wa kuongozwa na Mungu miaka 100, inalipasa likate maneno kwamba ndilo tengenezo ambalo Mungu amelichagua akalitia nguvu livumilie mashambulio yanayotoka ulimwenguni pote hata sasa. Tengenezo hilo dogo la watu walio wakf lilijulikana nyakati za kisasa kwa jina la Mungu. Ushuhuda wote unaonyesha kwamba Mungu alipendelea kutambua na kulikubali tengenezo hilo, wala hajalitupilia mbali. Muda wa miaka 100 umehakikisha kwamba ndivyo ilivyo.

3.Masihi aliyetangazwa alikuja kwa jina la nani, nao watu walimwonaje?

3 Mambo ambayo yamelipata tengenezo hilo yanalingana na yaliyotukia karne 19 zilizopita, katika nyakati za Biblia. Wakati huo katika Mashariki ya Kati mwanamume mmoja alikuwa akitangazwa kuwa ndiye Masihi aliyekuwa amengojwa muda mrefu, aliyetiwa mafuta na Mungu awe Mfalme wa serikali ambayo mwishowe ingewapa wanadamu wote utawala wenye haki. Wingi wa watu walifuata viongozi wao wa kidini na kukataa kumwamini kuwa ndiye Masihi aliyeahidiwa kutoka kwa Mungu. Lakini yeye hakuwa mdanganyifu. Yeye hakuwa Masihi wa kujibandika mwenyewe, mwenye kujitakia utukufu na mamlaka. Aliwaambia wapinzani wake hivi: “Mimi siupokei utukufu kwa wanadamu. . . . Mimi nimekuja kwa jina la Baba yangu, wala ninyi hamnipokei; mwingine akija kwa jina lake mwenyewe, mtampokea huyo.” (Yohana 5:41-43) Mwenye kuyanena maneno hayo ni Yesu, aliyekuwa mzao wa Mfalme Daudi wa Yerusalemu, kwa hiyo akawa mzao wa Ibrahimu mwaminifu pia, ambaye kupitia kwa uzao wake jamaa zote za dunia zitabarikiwa.​—⁠Mwa. 12:3; 22:18; Mt. 1:1-16.

4. Kuja kwa Yesu kwa jina la Baba yake wa mbinguni kulimaanisha nini juu yake mwenyewe?

4 Kuja kwa Yesu kwa jina la Baba yake wa mbinguni kulimaanisha kwamba hakujileta mwenyewe, bali alitumwa na Baba yake wa mbinguni. Kwa hiyo alikuwa mwana aliyepaswa kufanya mapenzi ya Baba yake duniani kwa utii. Alipaswa kujulisha watu jina la Baba yake na kuliheshimu, si kulisingizia.

5. Ingawa Yesu Masihi alikuwa nabii yeye mwenyewe, alipendezwa na unabii wa nani pia?

5 Hata leo hii Masihi Yesu amekuwa ndiye nabii mkubwa zaidi ambaye Mungu wa Biblia amepata kuwa naye duniani, hata Musa wa nyakati zilizoutangulia Ukristo akilinganishwa naye. (Kum. 18:15-19; Matendo 3:22, 23; Ufu. 22:18-20) Lakini yeye alipendezwa pia na unabii mbalimbali uliotolewa na nabii fulani aliyemtangulia, jina lake Yeremia.

6. Yeremia alikuja na kunena kwa jina la nani, nalo jambo hilo linahakikishwaje na maneno ya watu wa wakati huo?

6 Yeremia alikuwa mshiriki wa jamaa ya kikuhani iliyoishi Anathothi, ikiwa chini ya ufalme wa Yuda. Kama Yesu Kristo, Yeremia hakuja wala kunena kwa jina lake mwenyewe, ingawa alikuwa na wajibu mbalimbali wa kutimiza akiwa kuhani Mlawi. Kama ilivyokuwa kwa Yesu, upinzani ulitokea Yeremia alipotoa unabii. Wapinzani wake, waliotaka kumwua, walimwambia hivi: “Hutafanya unabii kwa jina la [ Yehova], usije ukafa kwa mkono wetu.” (Yer. 11:21) Wakati mmoja Yeremia alisema hivi akiwa amevunjika moyo: “Sitamtaja, wala sitasema tena kwa jina lake.” (Yer. 20:9) Lakini alijisikia akiwa amewaka sana neno la Mungu asiweze kuacha kulitangaza. Unabii wake ulitimia Yerusalemu ulipoharibiwa mwaka 607 K.W.K., hata hivyo Wayahudi waliookoka, waliotaka sana kufuata njia zao wenyewe, wakamwambia hivi: “Neno lile ulilotuambia kwa jina la [Yehova], sisi hatutakusikiliza.” (Yer. 44:16) Baadaye watu hao wenye kupigana na Mungu wangekiona.

7. Kulikuwa na uhitaji wa Yehova kumwambia Yeremia maneno gani yenye kumfariji hapo mwanzoni?

7 Si ajabu kwamba miaka 40 kabla ya hapo, yaani, mwaka 647 K.W.K., kulikuwa na uhitaji wa Yehova kumwambia kijana Yeremia hivi: “Ukawaambie maneno yote niliyokuamuru; usifadhaike kwa ajili yao, nisije nikakufadhaisha wewe mbele yao. Maana, tazama, nimekufanya leo kuwa mji wenye boma, na nguzo ya chuma, na kuta za shaba, juu ya nchi yote; juu ya wafalme wa Yuda, na juu ya wakuu wake, na juu ya makuhani wake, na juu ya watu wa nchi hii. Nao watapigana nawe; lakini hawatakushinda; maana mimi nipo pamoja nawe, asema [Yehova], ili nikuokoe.” ​—⁠Yer. 1:17-19.

8. Ni kwa kukumbuka nini Yeremia alipata nguvu za kuvumilia kwa muda mrefu sana, lakini sasa tunauliza ulizo gani?

8 Ufikirie upinzani ambao Yeremia alilazimika kuvumilia kwa muda unaozidi miaka 40! Alikuwa mmoja wa wanenaji wa Yehova ambao mwanafunzi Mkristo Yakobo anakaza fikira zetu juu yao, akisema: “Watwaeni manabii walionena kwa jina la Bwana, wawe mfano wa kustahimili mabaya, na wa uvumilivu.” (Yak. 5:10) Kwa kujikumbusha nyakati zote kwamba hakuwa amekuja kwa jina lake mwenyewe, bali kwamba alinena kwa jina la Yehova, Yeremia alipata nguvu za kuvumilia na kulishinda kusudi la wenye kumshambulia, ambao kwa kweli walikuwa wakipigana na Mungu. Yehova hakumfadhaisha Yeremia mbele ya washambuliaji hao, kwa maana Yeremia hakujiacha afadhaishwe na sura yao ya kutisha wala wingi wao. Hilo lilikuwa tendo bora kabisa karne 26 zilizopita, lakini je! leo tuna kifani cha jambo hilo​—⁠mfano wa kisasa? tunao!

JAMII YA KISASA YA YEREMIA

9, 10. Tunamfikiria mtu gani aliyefananishwa na Yeremia, na kwa sababu gani huu ndio wakati anaopaswa kuwapo?

9 Hatumaanishi kwamba Yeremia mwenyewe amefufuka kwa wafu. Hivyo ndivyo Waisraeli fulani wa karne ya kwanza walivyomdhania Yesu Kristo kwa sababu alikuja kwa jina la Yehova akavumilia upinzani mwingi ulioletwa na wanadini huko Israeli. (Mt. 16:13, 14) Leo tunammaanisha mtu aliyefananishwa na Yeremia wa kale. Tunammaanisha mtumishi au mtumwa ambaye Yesu Kristo alimtaja katika unabii wake unaohusu “ishara ya kuwapo [kwake, au parousia] na ya mwisho wa taratibu ya mambo.” (Mt. 24:3, NW) Leo, wanafunzi wa Biblia walio macho wanaiona “ishara” ya kuwapo, au parousia, ya Yesu aliyetukuzwa akiwa katika mamlaka ya Ufalme wa mbinguni. Kwa hiyo, mtumishi au mtumwa huyo apaswa kuwa hapa duniani sasa aikamilishe “ishara” kabisa. Katika Mathayo 24:45-47, Yesu alisema:

10 “Ni nani basi yule mtumwa mwaminifu mwenye akili, ambaye bwana wake alimweka juu ya nyumba yake, awape watu chakula kwa wakati wake? Heri mtumwa yule, ambaye bwana wake ajapo atamkuta akifanya hivyo. Amin, nawaambieni, atamweka juu ya vitu vyake vyote.”

11, 12. (a) “Mtumwa” alitokea wakati gani, na kwa njia gani? (b) Ni jambo gani lililoonyesha kwamba. “mtumwa” aliwekwa alishe “nyumba” katika wakati unaofaa?

11 “Mtumwa” aliyetabiriwa hapo hawezi kuwa ni mwanamume mmoja Mkristo, kwa maana kama ingekuwa hivyo umri wake sasa ungekuwa miaka zaidi ya 1,900. Bila shaka “mtumwa” huyo ni kundi zima la Kikristo lenye wanafunzi 144,000 ambao wamezaliwa kwa roho ya Mungu wawe warithi wenzi wa Yesu Kristo katika ufalme wake wa mbinguni. Jamii hiyo ya “mtumwa” ilitokea katika sikukuu ya Pentekoste mwaka 33 W.K. Ile sehemu ya kwanza ya jamii hiyo ya “mtumwa” ilitokea wakati Yesu Kristo aliyetukuzwa alipotumiwa kumimina roho takatifu juu ya wanafunzi (karibu 120) waliokuwa wakingoja wakiwa wamekusanyika Yerusalemu. Kuna jambo fulani lenye kuonekana waziwazi linaloonyesha kwamba jamii hiyo ya “mtumwa” iliyokuwa imeanzwa karibuni iliwekwa wakati huo iwape chakula kwa wakati wake watu wa nyumba ya Yesu Kristo aliyetukuzwa. Ni jambo gani hilo?

12 Wote waliotiwa mafuta kwa roho takatifu wakati huo walianza kusema kwa lugha za kigeni ambazo kabla ya hapo hawakuzijua, tena waliyanena “matendo makuu ya Mungu.” (Matendo 2:1-11) Muda mfupi tu baada ya hapo Wayahudi na waongofu 3,000 wenye njaa ya ile kweli walilishwa chakula cha kiroho katika wakati wake kisha wakawa Wakristo waliobatizwa, waliozaliwa kwa roho, watu wa nyumba ya Bwana Yesu Kristo.​—⁠Matendo 2:14-42; Mt. 24:45.

13. (a) “Mtumwa” huyo amefanywaje aendelee kuwa hai mpaka sasa, na kwa kutazamia nini? (b) Kwa sababu gani kipindi cha miaka 63 kilichoanza 1914 kina maana ya pekee?

13 Wakristo hao wa karne ya kwanza waliozaliwa kwa roho walikufa, lakini katika karne zilizofuata washiriki wengine wameongezwa katika kundi la “mtumwa,” na wote walikuwa wakingoja “kuwapo” kwa Bwana Yesu Kristo aliyetukuzwa katika mamlaka ya Ufalme. Tangu mwaka 1914 “ishara” imetokea ikazidi kuwa wazi nyakati zote, kuhakikisha kwamba Bwana alianza kuwapo katika mamlaka ya Ufalme mwishoni mwa Majira ya Mataifa mwaka 1914. (Luka 21:24; Dan. 4:16, 23, 25, 32) Tangu wakati huo, kipindi hicho cha miaka 63 tu kimekuwa bila kifani, kwa maana wanadamu wote wamepatwa na pigo la vita vya mataifa yote, misukosuko ya kisiasa, matetemeko mengi sana ya ardhi, magonjwa ya kipuku, upungufu wa chakula wenye kupandisha sana bei za chakula, uvunjaji mwingi wa sheria, kuonewa na kuteswa kwa jamii ya “mtumwa” wa Kristo ulimwenguni pote. Hakika kipindi hicho kilicho kati ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ya 1914 na wakati wa sasa hakijapata kuwa na kifani katika historia. Bila shaka kina maana fulani inayohusu ulimwengu mzima. Hakika kinayo! Yesu Kristo, nabii wa Mungu aliye mkubwa kuliko Musa, alieleza maana yake kwa unabii. Maana gani?

14. Kulingana na maelezo ya Yesu, kipindi hicho kina maana gani?

14 Kwamba “kuwapo” kwake, au parousia, kunaendelea sasa tangu mwaka 1914 na kwamba mwisho wa taratibu hii ya mambo unazidi kukaribia nyakati zote!

15. Kwa sababu gani leo kunapaswa kuwe na jamii ya Yeremia duniani, na ni nani waliomo katika jamii hiyo?

15 Kipindi cha “kuwapo” kwa Kristo ndio wakati wake wa kuwahukumu washiriki wa kundi la “mtumwa” aliyewekwa karne 19 zilizopita alishe watu wa nyumba yake chakula cha kiroho kwa wakati wake. (Mt. 24:45-47; 25:14-30) Kwa hiyo mabaki ya mwisho ya jamii hiyo ya “mtumwa” iliyozaliwa kwa roho wapo hapa duniani sasa wakiendelea kuhukumiwa. Uaminifu wao na hekima yao ya kiroho katika utumishi wa Bwana ndiyo inayoamua kama wanastahili kuwekwa wasimamie vitu vyote vya Bwana wao vilivyo duniani. Vilevile, kwa kuwa nyakati zetu zinalingana na siku za Yeremia nabii wa Yehova, ni sawa kuwaza kwamba jamii iliyo kama Yeremia yapaswa kuwapo leo, yenye kuja kwa jina la Yehova. Ipo! Waliomo katika jamii hiyo ni mabaki waliokubaliwa wa jamii ya “mtumwa.” Mpaka sasa wenye kupigana na Mungu hawajaiweza jamii hiyo!

16. (a) Miaka mia moja iliyopita ni kitu gani kilichokuwa kimeanza kutokea Allegheny, Pennsylvania, nacho kilikuwa na uhusiano gani na Jumuiya ya Wakristo? (b) Gazeti lenye kuhitajiwa sana lilianzaje kuchapwa wakati huo, na ni nani aliyelichapa?

16 Na tutazame nyuma miaka 101 iliyopita​—⁠mwaka 1877 W.K. Wakati huo madhehebu za kidini za Jumuiya ya Wakristo zilikuwa zimeongezeka sana. Lakini, wakati huo kulikuwa na kundi dogo la wanafunzi wa Biblia waliokuwa wakf katika Allegheny (ambayo sasa ni sehemu ya Pittsburgh), Pennsylvania, U.S.A. Kundi hilo lilikuwa limejitenga kabisa na taratibu za kidini za Jumuiya ya Wakristo, ambayo wakati huo ilikuwa ikiingiliwa na watu wenye kufuata kisio la mageuzi, kuchambua Maandiko na kutafuta vitu vya kimwili. Kundi dogo hilo lililokuwa katika Allegheny lilijifunza bila migawanyiko Neno lililoandikwa kwa uongozi wa Mungu, kisha wakataka sana kufanya kazi kwa haraka. Mzee mmoja wa kundi hilo aliona uhitaji wa kuchapa gazeti jipya ambalo lingetetea mafundisho ya msingi ya Biblia Takatifu. Aliamua kutumia utajiri wake kwa kusudi hilo. Kwa hiyo Julai mwaka 1879 alianzisha gazeti hilo lililotakiwa, yeye mwenyewe akiwa ndiye mhariri na mchapaji. Gazeti hilo lingeitatiza taratibu ya mambo ya ulimwengu, hasa Jumuiya ya Wakristo. Liliitwa “Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence” (“Mnara wa Mlinzi wa Sayuni na Mtangazaji wa Kuwapo kwa Kristo”). Mhariri na mchapaji wake alikuwa mwanafunzi wa Biblia mwenye kujitoa sana, Charles Taze Russell.

17, 18. (a) Zaidi ya linaloonyeshwa na kichwa “Zion’s Watch Tower,” wenye kuhusika na gazeti hilo walijitokeza ulimwenguni kwa jina la nani? (b) Kwa sababu gani gazeti hilo lisingeomba wala kusihi wanadamu walisaidie?

17 Mhariri huyo na wenye kumsaidia kuchapa gazeti hilo jipya, pamoja na kundi lenye kuliunga mkono, walijitokeza ulimwenguni kwa jina la Mungu wa Yeremia, aliyetumikia kama kuhani katika Sayuni wa kale. Biblia inautaja mara nyingi mji Sayuni wa wakati wa Yeremia kuwa ndiyo makao ya Mungu wa Yeremia. (Zab. 74:2; 48:1, 2) Jina la gazeti hilo, “Watch Tower,” lilihusiana na andiko lifuatalo la Biblia, lililoonyeshwa katika ukurasa wenye jina la gazeti: “Ee mlinzi, habari gani za usiku?” “Mchana unakuja.” (Isa. 21:11, 12) Hiyo ilionyesha kwamba kusudi la gazeti hilo lilihusiana na kutimizwa kwa unabii mbalimbali wa Biblia. Lakini katika ukurasa wa 2 wa toleo la pili la gazeti hilo (Volume ya 1, Namba 2), upande wa juu wa safu ya kwanza ulikuwa na kichwa hiki: “Je! Wewe Unataka ‘Zion’s Watch Tower’?” Chini ya kichwa hicho, fungu la tatu lilisema hivi:

18 “Usidhani kwamba maneno hayo yamesemwa ili kuomba pesa. Hapana. Sisi tunaamini kwamba gazeti ‘Zion’s Watch Tower’ linasaidiwa na YEHOVA, na maadamu ndivyo ilivyo gazeti hilo halitaomba wala kusihi wanadamu walisaidie. Wakati Yeye asemaye: ‘Dhahabu yote na fedha ya milimani ni mali yangu,’ atakapoacha kutoa pesa zinazohitajiwa, tutafahamu kwamba huo ndio wakati wa kuacha kulichapa.”

KUSONGA MBELE KWA JINA LA KIMUNGU

19. Ni Jambo gani linaloonyesha kama Yehova alishindwa au hakushindwa kutoa pesa za kuchapa gazeti hilo?

19 Hakuna haja ya kutokeza ubishi juu ya jambo hilo. Mchapaji wa gazeti Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence alijitokeza kati ya dini za ulimwengu kwa jina la YEHOVA, kama nabii Yeremia wa zamani zilizopita. Basi, je! Yehova aliacha kutoa pesa zilizohitajiwa ili kuendelea kulichapa gazeti hilo? Jibu li wazi kwa sababu tangu Julai 1879, gazeti hili halijapata kamwe kuacha kuchapwa wala toleo moja halijakosekana, ijapokuwa lilipigwa marufuku nyakati mbalimbali katika nchi mbalimbali!

20. Sasa gazeti hilo linachapwa nakala ngapi, nacho kichwa chake kinaelekeza fikira za watu juu ya nini?

20 Leo gazeti Watchtower (Mnara wa Mlinzi) limeongeza uchapaji kutoka nakala 6,000 kila mwezi katika lugha moja (Kiingereza) likawa na uchapaji wa nakala 9,800,000 mara mbili kwa mwezi katika lugha 80. Tangu toleo la Machi 1, 1939, gazeti hili limekuwa likiitwa “Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova.” Vilevile, leo kuna gazeti jingine linalohusiana nalo, linaloitwa “Amkeni!,” nalo linachapwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc., katika lugha 33 kwa wastani ya nakala 8,000,000.

21, 22. (a) Lengo la gazeti hilo lilifanywa liwe nini, nao wenye kulikubali liwe gazeti lao rasmi walipokea Jina gani kwa moyo sana? (b) Basi, walipata wajibu wa kufanya nini kama Yeremia?

21 Tangu toleo lake la Januari 1, 1926, gazeti Watch Tower (Mnara wa Mlinzi) lilijaribu sana kuutangazia ulimwengu mzima jina la Mungu wa Biblia, Yehova. Basi ilifaa sana miaka mitano baadaye (mwaka 1931) jina Mashahidi wa Yehova linaloitegemea Isaya 43:10 likapokewa kwa moyo sana na Wakristo hao waliokuwa wamekwisha jiweka wakf, wakabatizwa, na kulikubali gazeti hilo liwe chapisho lao rasmi. Si ajabu kwamba kuja na kunena hivyo kwa jina la Mungu wa Yeremia tangu mwaka 1879 kuliwapa wajibu fulani wachapaji na wenye kuunga mkono gazeti Watch Tower na vitabu vingine vinavyohusiana nalo. Wajibu gani? Wajibu wa kutangazia wanadamu wote mambo ambayo Yehova ametangaza katika Biblia Takatifu. Wajibu huo ulilingana na daraka ambalo Yeremia alipewa, naye aliambiwa na Mungu hivi:

22 “Haya basi, wewe jifunge viuno, ukaondoke, ukawaambie maneno yote niliyokuamuru.”​—⁠Yer. 1:17.

23. Kwa hiyo tengenezo la Mashahidi wa Yehova limeendelea kujitahidi kufanya nini, na jinsi gani?

23 Tengenezo la Kikristo la Mashahidi wa Yehova limekubali wajibu huo likaendelea kujitahidi kuutimiza. Hawachapi Biblia nzima katika tafsiri kadha tu, bali pia wanachapa na kueneza vitabu, vijitabu na vikaratasi vinavyoeleza watu Neno lote la Yehova lililoandikwa, yaani, “maneno yote niliyokuamuru.” Mpaka sasa hivi hawajaacha kufanya hivyo.

24. Ni kazi gani kubwa ambayo Yesu alitaja kwamba wanafunzi wake wangefanya?

24 Yesu Kristo, akiwa nabii mkubwa kuliko Yeremia, aliitaja kazi kubwa inayopaswa kufanywa na wanafunzi wake aliposema hivi: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote.” Vilevile: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba [Yehova] na la Mwana [Yesu Kristo] na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi. Na, tazama! mimi nipo pamoja na ninyi siku zote mpaka mwisho wa taratibu ya mambo.”​—⁠Mt. 24:14; 28:19, 20, NW.

25. Mashahidi wa Yehova wameiendeshaje kazi hiyo waliyoamriwa waifanye, lakini namna gani juu ya wenye kuipinga?

25 Kama Mwana wa Mungu Yesu Kristo alivyoamuru, kazi hiyo imepelekwa na mashahidi Wakristo wa Yehova kote kote duniani katika nchi 216 na visiwa vya bahari, katika lugha 194. Watu wanaowapinga wasifanye kazi hiyo waliyoamriwa na Mungu wanapigana na Mungu. Wanafanya hivyo bure tu maana wanashindwa. Wao wanajikaza tu wakidhani wataishinda jamii ndogo iliyotiwa mafuta ya Yeremia, pamoja na wenzi wao washikamanifu. Lakini Neno la Yehova linatuhakikishia kwamba hawatashinda kamwe!

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki