“Watapigana Nawe”
1. Huenda tukaonaje mwenzi wa ndoa akikosa kuwa mwaminifu?
MTU ye yote kati ya sisi tuliooa tungeonaje mwenzi wetu wa kisheria akikosa kuwa mwaminifu kwetu na kufanya uzinzi bila kujali? Kama mke tuliyeoa tangu ujana wake angevunja nadhiri zake, atuache na kutembea-tembea akijiuza kwa wanaume waasherati, je! sisi waume waaminifu tusingeona uchungu moyoni? Matumaini ya kupatana tena yakimalizika, huenda tukamtaliki aende zake. Huenda tusimtake arudi tena kwa sababu ya kuudhika!
2. Ni ukosefu gani wa uaminifu unaotajwa katika Yeremia 3:1,2 kuhusu taifa zima?
2 Karne 26 zilizopita, siku za nabii Yeremia, kisa kama hicho kilikuwa kimetokea, lakini kilitokea kuhusu taifa zima. Kisa hicho kinalingana na kingine cha kisasa, kwa hiyo kinatuhusu sisi leo. Kinastahili tukichunguze, tuone jinsi tunavyoweza kuhusika. Katika maandishi ya kisa kilichoandikwa na Yeremia, tunasoma hivi: “Watu husema, Mtu akimwacha mkewe, naye akienda zake, akawa mke wa mtu mwingine, je! mtu huyo atamrudia tena? . . . Lakini wewe umefanya mambo ya ukahaba na wapenzi wengi; nawe, je! utanirudia mimi? asema [Yehova]. Inua macho yako, ukavitazame vilele vya milima, ukaone; pa wapi mahali ambapo hawakulala nawe? Kando ya njia umeketi ili kuwangojea, kama vile Mwarabu jangwani; nawe umeitia nchi unajisi kwa ukahaba wako na uovu wako.”—Yer. 3:1, 2.
3. Yehova anamwambia mwasi anayetajwa hapa afanye nini, na kwa sababu gani?
3 Taifa la Israeli ndilo linaloambiwa maneno hayo. Kwa hiyo tunasoma hivi: “Rudi, Ee Israeli mwenye kuasi, asema [Yehova]; sitakutazama kwa hasira; maana mimi ni mwenye rehema, asema [Yehova], sitashika hasira hata milele. Ungama uovu wako tu; ya kwamba umemwasi [Yehova], Mungu wako, na njia zako zimekuwa nyingi kuwaendea wageni chini ya kila mti wenye majani mabichi, wala hamkuitii sauti yangu, asema [Yehova]. Rudini, enyi watoto wenye kuasi, asema [Yehova]; maana mimi ni mume wenu; . . . nami nitawaleta hata Sayuni.”—Yer. 3:12-14.
4. Leo ni nani aliye kama Israeli mwasi, na ni ulizo gani linalotokea juu ya kuwa mume?
4 Leo Jumuiya ya Wakristo ndiyo iliyo kama Israeli mwasi. Kuna watu zaidi ya 900,000,000 ambao bado wamefungamana na Jumuiya ya Wakristo, kwa maana majina yao yameandikwa katika madhehebu zake nyingi. Je! Yehova Mungu amepata kuwa “mume” wa Jumuiya ya Wakristo wakati wo wote? Leo jumuiya hiyo inaupunguza ubora wa jina la Yehova na kulitukuza sana jina la Yesu Mwana wa Yehova. Karne zaidi ya 18 kabla Jumuiya ya Wakristo haijatokea, Yehova alipata kuwa “mume.” Mume wa nani? Mume wa taifa la Israeli. Aliwapata wakawa wake hasa kwa kuwakomboa utumwani katika Misri ya kale na kwa kuwaingiza katika mkataba wa kisheria pamoja naye katika Mlima Sinai, ambapo nabii Musa alitumiwa kama mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu. (Kut. 19:1 mpaka 24:8) Lakini namna gani sasa juu ya Jumuiya ya Wakristo?
5. (a) Jumuiya ya Wakristo ilitokana na nini? (b) Mwaka 33 W.K., Yehova alipata kuwa mume wa nani, na jinsi gani?
5 Hili ni jambo ambalo jamii ya Yeremia iliyotiwa mafuta lazima iionyeshe Jumuiya ya Wakristo leo, nayo inafanya hivyo. Jumuiya ya Wakristo ilitokana na Ukristo wa karne ya kwanza W.K. Kundi la kweli la Kikristo lilianzwa katika sikukuu ya Pentekoste mwaka 33 wa karne hiyo. Likawa “mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki” ya Yehova Mungu. (1 Pet. 2:9) Basi uhusiano wake wa ndoa pamoja na Israeli wa asili waliotahiriwa ulifutwa. Taifa hilo lilipewa talaka! Sasa Yehova akawa “mume” wa “taifa takatifu” lililozaliwa karibuni, yaani, Israeli wa kiroho. Alikuwa amelinunua hilo “taifa takatifu” kwa damu yenye thamani nyingi ya Mwanawe Yesu Kristo, aliye Musa Mkubwa. Alilinunua “taifa” hilo akaliingiza katika “agano jipya” ambalo Yeremia alikuwa ametabiri. (Yer. 31:3134) Yesu ndiye aliyekuwa Mpatanishi wa agano jipya hilo. Katika vuli ya mwaka 36 W.K. waamini wasio Wayahudi walikubaliwa wabatizwe wawe sehemu ya Israeli wa kiroho.
6. Uasi wa kidini kati ya wenye kujidai kuwa Wakristo ya jambo gani litokee katika karne ya nne W.K.?
6 HaIafu? Baada ya kufa kwa mitume wateule wa Kristo mwishoni mwa karne ya kwanza, uasi wa kidini ulianza kutokea katika kundi la Israeli wa kiroho juu ya “mume” wake, Yehova Mungu. (Mt. 13:24-28, 36-39) Uasi huo wa imani uliongezeka kati ya wenye kujiita Wakristo, mpaka Mfalme Konstantino wa Milki ya Kirumi akapata nafsi ya kutumia hali hiyo atimize kusudi lake. Ingawa yeye hakuwa amebatizwa na bado alikuwa Askofu Mkuu wa dini ya kipagani ya Rumi, aliutangaza Ukristo wa jina tu uliokuwako siku zake kwamba ndiyo dini ya Serikali ya Rumi. Hapo ndoa ilifanyika kati ya Ukristo wenye uasi na Serikali ya kisiasa.
7. Kulingana na Yeremia 2:20, 21, lazima mashahidi Wakristo wa Yehova waionyeshe Jumuiya ya Wakristo uharibifu gani wa tabia?
7 Mashahidi Wakristo wa Yehova wana wajibu wa kusema na Jumuiya ya Wakristo ya kisasa, kama vile Yeremia alivyosema na taifa la Israeli lenye kuasi imani karne ya saba kabla ya Wakati wetu wa Kawaida. Wana maneno gani ya kuiambia kutoka kwa Yehova Mungu? Haya: “Juu ya kila kilima kirefu, na chini ya kila mti wenye majani mabichi, umejiinamisha, ukafanya mambo ya ukahaba. Nami nalikuwa nimekupanda, mzabibu mwema sana, mbegu nzuri kabisa; umegeukaje, basi, kuwa mche usiofaa wa mzabibu-mwitu machoni pangu?”—Yer. 2:20, 21.
8. Yeremia 2:2, 3 inaonyeshaje kwamba Israeli walianguka wakawa bila hali ya kiroho yenye kuheshimika?
8 Yehova aliendelea kusimulia hali ya kiroho ambayo Israeli watu wake wa agano, pamoja na ule ambao sasa unaitwa Ukristo kwa jina tu, walikuwa wameacha aliposema hivi kwa kumtumia Yeremia: “Nakukumbuka, hisani ya ujana wako, upendo wa wakati wa uposo wako; jinsi ulivyonifuata huko jangwani, katika nchi isiyopandwa mbegu. Israeli walikuwa utakatifu kwa [Yehova]; malimbuko [mazao ya kwanza] ya uzao wake.” (Yer. 2:2, 3) Israeli wa asili waliusahau utakatifu wa uhusiano huo wa agano walilofanya na Yehova Mungu, isipokuwa mabaki waaminifu, Yeremia akiwa mmoja wao. Jumuiya ya Wakristo ilikosa kwa njia iyo hiyo kuthamini kwamba Yehova Mungu alifaa kupewa ibada ya pekee. Jumuiya hiyo haikuishi kupatana na agano jipya.
9, 10. Kwa sababu gani Jumuiya ya Wakristo inauliza maulizo juu ya kama mashahidi Wakristo wa Yehova wanafaa kutenda kama Yeremia?
9 Hata hivyo, mashahidi Wakristo wa Yehova wa leo ni akina nani hata wajitwalie daraka la kufanya kama Yeremia na kuilaumu Jumuiya ya Wakristo juu ya kushindwa kutimiza matakwa ambayo Mungu amewekea Waisraeli wa kiroho walio katika agano jipya? Wao ndio akina nani hata wao wailaumu Jumuiya ya Wakristo kwamba ina hatia ya kumkosea Mungu wa agano jipya kwa kufanya uzinzi wa kiroho. (Yak. 4:4) Hayo ndiyo maoni ya Jumuiya ya Wakristo juu ya kazi ya Mashahidi wa Yehova. Jumuiya ya Wakristo imekuwako miaka zaidi ya 1,600 tangu wakati wa Konstantino Mkuu, nayo ina mamilioni ya makundi!
10 Lakini, mashahidi Wakristo wa Yehova wa leo wamekuwako muda wa karne moja tu, tangu kundi la Allegheny (Pennsylvania) la wanafunzi wa Biblia wasio na migawanyiko lilipoanzwa. Jumuiya ya Wakristo inawaona kama kikundi kichanga kilichoanza karibuni tu, kisichoweza kujisifia kuwa na masomo ya Kibiblia. Lakini, Yeremia alikuwa na umri gani wakati Yehova alipomwagiza awe nabii?
11. Kulingana na Yeremia 1:4-6, ujana wa Yeremia ulimfanya asistahili machoni pa Yehova?
11 Ujana wa Yeremia haukuwa kitu kwa Yehova. Jambo la maana kwa Yehova lilikuwa sifa za kuonyesha bidii ya kimungu na kuwa na nia ya kutumikia chini ya hali zisizopendeza. Hilo linaonekana wazi katika maandishi haya ya Biblia: “Neno [Yehova] lilinijia, kusema, Kabla sijakuumba katika tumbo nalikujua, na kabla hujatoka tumboni, nalikutakasa; nimekuweka kuwa nabii mataifa. Ndipo niliposema, Aa, Bwana MUNGU! tazama, siwezi kusema; maana mimi ni mtoto.”—Yer. 1:4-6.
NI MTOTO
12. Kwa sababu gani Yeremia hakuwa mtoto mno mwaka 647 K.W.K. asiweze kuchaguliwa na Yehova awe “nabii wa mataifa”?
12 Lakini, je! mwana huyo wa kuhani Hilkia alikuwa mchanga mno mwaka 647 K.W.K. asiweze kuchaguliwa na Yehova awe “nabii wa mataifa”? Hapana, kwa maana muda mrefu kabla Yeremia hajazaliwa, kabla mama yake hajamchukua mimba, Yehova aliona kwamba mwana fulani wa Hilkia angefaa sana kuwa katika cheo hicho—tena kwa wakati wake. Vile-vile, ikiwa Yehova aliweza kutakasa mwana huyo kabla Hilkia hajamzaa, hakika Mungu huyo Mwenye Nguvu Zote angeweza kumwingiza katika cheo kitakatifu, kama miaka 20 hivi baada ya kuzaliwa kwake, au hata miaka 25 baada ya kuzaliwa kwake, na wakati huo angestahili kuingia katika vyeo fulani vya utumishi wa kikuhani hekaluni Yerusalemu. Kwa hiyo Yeremia alizaliwa wakati ule ule uliowekwa, maana Yehova alimtaka huyo kuhani-nabii awe kijana mwanzoni mwa kazi yake.
13. Ni wakati wa utawala wa nani neno la Yehova lilimjia Yeremia, na kwa sababu gani alijiona kuwa mtoto mno asiweze kunena kama nabii?
13 Yehova alimkusudia Yeremia atumikie kama nabii muda mrefu, miaka zaidi ya 40, au mpaka awe mzee. Kwa hiyo neno la unabii la Yehova halikuanza kumjia Yeremia vivi hivi tu bila mpango, katika mwaka wa kumi na tatu wa utawala wa Mfalme Yosia wa Yerusalemu. (Yer. 1:1, 2) Lakini Yeremia mwenyewe alijiona kuwa mtoto mno asiweze kuifanya kazi ya kutoa unabii iliyomhitaji aseme na watu hadharani. Vilevile, kwa kuwa hiyo ingetia ndani kusema na wazee wa taifa hilo, watu wenye umri mkubwa, Yeremia alijiona kuwa “mtoto” tu.
14. Maoni ya Yehova juu ya ujana wa Yeremia yalitofautianaje na ya watu mashuhuri wa nchi hiyo?
14 Wafalme, wakuu, makuhani na wananchi walimdharau Yeremia wakimwona kuwa kijana, na hiyo inatukumbusha jinsi Paulo mtume Mkristo alivyomwambia Timotheo mmisionari mwenzake asiache mtu ye yote audharau ujana wake alipokuwa akitimiza maagizo aliyopewa na Paulo. (1 Tim. 4:12) Yehova hakumdharau Yeremia. Hakusema naye kwa njia ya utoto, wala hakumwongoza atoe unabii wake wa kwanza kwa njia ya utoto. Unabii huo ulisemwa kwa watu wazima kwa usemi wa heshima.
15. Muda wote Jumuiya ya Wakristo imeionaje jamii ya Yeremia, nayo jamii hiyo imekuwaje na ushujaa kama wa Daudi?
15 Muda wote taratibu za kidini zilizo za zamani zaidi, za Jumuiya ya Wakristo, zimewadharau mashahidi Wakristo wa Yehova kwa kuwaona kama “mtoto” tu wakilinganishwa na jumuiya hiyo. Ni kweli kwamba C. T. Russell alikuwa na umri wa miaka 27 tu alipoanza kuhariri gazeti Zion’s Watch Tower, lakini aliendelea kuwa mhariri miaka 37, mpaka alipokufa akiwa na umri wa miaka 64. Alitumikia kama msimamizi wa Watch Tower Bible and Tract Society karibu miaka 32 (1884-1916). Kwa kuwa Sosaiti hiyo iliandikishwa kisheria Desemba 1884, mashahidi Wakristo wa Yehova wamekuwa wakiendesha kazi kwa kushirikiana na Sosaiti hiyo karibu miaka 100 tu. Walikuwa vijana walipojitokeza kati ya dini za kisasa zenye ushindani, lakini waliingia kazini kwa ushujaa. Walikuwa kama kivulana mchungaji Daudi, wakati alipokwenda kupambana na Goliathi jitu la Kifilisti lenye silaha nyingi. (1 Sam. 17:23-54) Kama Daudi, wao walijua kwamba walikuwa wakienda kwa jina la Yehova na kwamba “vita ni vya [Yehova].”—1 Sam. 17:47.
16. Ijapokuwa Yeremia alikataa mgawo akisema “ni mtoto,” Yehova alifanya nini?
16 Yehova anaweza kuwafanya watu anaowachagua kwa ajili ya utumishi wake wafae, hata wawe wana umri gani. Yaliyompata Yeremia akiwa shahidi wa Yehova kabla ya nyakati za Ukristo yanahakikisha hivyo, ili kututia moyo sisi leo. Maandishi ambayo Yeremia ameandika juu yake mwenyewe yanasema: “[Yehova] akaniambia, Usiseme, Mimi ni mtoto; maana utakwenda kwa kila mtu nitakayekutuma kwake, nawe utasema kila neno nitakalokuamuru. Usiogope kwa sababu ya hao; maana mimi nipo pamoja nawe nikuokoe, asema [Yehova]. Ndipo [Yehova] akaunyosha mkono wake, akanigusa kinywa changu; [Yehova] akaniambia, Tazama, nimetia maneno yangu kinywani mwako; angalia, nimekuweka leo juu ya mataifa na juu ya falme, ili kung’oa, na kubomoa, na kuharibu, na kuangamiza; ili kujenga na kupanda.”—Yer. 1:7-10.
17. Agizo ambalo Yehova ameipa jamii ya Yeremia haliwapi washiriki wa jamii hiyo ruhusa ya kufanya nini?
17 Jamii ya Yeremia ya wakati wetu inalifahamu agizo ambalo imepewa na Yehova. Wanajua kwamba agizo hilo haliwapi ruhusa ya kuingia katika siasa za kilimwengu, kuendeleza au kushiriki kwa bidii katika mapinduzi ya kisiasa wala kuingia katika vyama vyenye kuchafua au kupindua serikali. Hiyo siyo njia ambayo Mungu amewakusudia ‘wang’oe, na kubomoa, na kuharibu, na kuangamiza.’ Kusudi la kuwa kwao “juu ya mataifa na juu ya falme” si kuyasimamia mataifa na falme hizo kwa nguvu, wala si kuyanyang’anya mamlaka yao ili wayatawale. Yeremia hakutimiza agizo la Mungu Aliye Juu Zaidi kwa njia hiyo, katika siku zake. Wala wale walio wa jamii ya Yeremia hawafanyi hivyo leo. Wao ni raia wenye amani na utaratibu, wenye kutii sheria za nchi za kwao.
18. Ni katika maana gani jamii ya Yeremia i juu ya mataifa na falme, na ni katika maana gani jamii hiyo inatimiza agizo ililopewa juu ya mataifa na falme hizo?
18 Basi, ni katika maana gani wako “juu ya mataifa na juu ya falme”? Wanalitimizaje agizo la kuwa juu ya mataifa walilopewa na Yehova, ambaye wametumwa kwa jina lake? Wanapewa cheo kutokana na chanzo kilicho juu kuliko mataifa na falme za kilimwengu. Kwa hiyo wana ruhusa ya kufanya matangazo ulimwenguni pote kwamba mataifa na falme hizo hazipendi kuwapa jamii ya Yeremia agizo la utangazaji bila ya kuwa na ubalozi wa kilimwengu. Wakiwa na mamlaka kutoka kwa Mungu Aliye Juu Zaidi, wanatumia usemi wa Biblia yake kutangaza tu kwamba mataifa na falme hizo zitang’olewa mahali zilipokwama, zibomolewe, ziharibiwe na kuangamizwa katika wakati wake Mungu, kwa njia aliyochagua. (Linganisha Ezekieli 43:3; Mwanzo 41:11-13.) Ni kama kwamba jamii ya Yeremia ndiyo itakayozing’oa, izibomoe, iziharibu na kuziangamiza, kwa maana Mungu atayatimiza maneno ambayo Neno Lake linaiambia jamii hiyo iyatangaze.—Yer. 18:7-10.
19. Kwa njia hiyo Yehova anajionyesha kuwa nini akilinganishwa na mataifa?
19 Kwa njia hiyo Mungu anajionyesha kuwa “mfalme wa mataifa,” kuonyesha kwamba ndiye mkuu kuliko mataifa hayo yote. Hakuna mmoja wa wafalme na watawala hao anayeweza kulingana naye,—Yer. 10:7; Ufu. 15:3; The Jerusalem Bible; The New American Bible.
20. Ili kuweza kutimiza agizo ililopewa na Mungu, jamii ya Yeremia inahitaji ushujaa kwa sababu ujumbe wao unaitikiwaje katika mataifa yote?
20 Jamii ya Yeremia inapotimiza agizo hilo inahitaji ushujaa, kwa maana ujumbe wao haupendwi na watu wengi ulimwenguni pote. Kama Yeremia, lazima watangaze kwamba mataifa yote ya kilimwengu yataharibiwa. (Yer. 25:15-30) Kwa hiyo hawawezi kushiriki katika uzalendo wa kutetea nchi zao wenyewe kama mataifa hayo yaliyohukumiwa maangamizi. Hawawezi kuifuata roho ya kutukuza mataifa iliyopo nyakati za kisasa. Wafalme na watawala wa leo wanauona ujumbe wa jamii ya Yeremia kuwa wenye kufitini serikali, kuharibu tabia ya raia zao na kudhoofisha majeshi yenye kulinda nchi zao. Kwa hiyo wanaitisha jamii hiyo yenye kutangazia ulimwengu wa kisasa unabii wa Yehova. Mara nyingi wanaongeza vitisho vyao kwa kuipa adhabu za namna mbalimbali ili wajaribu kuizuia jamii hiyo ya Yeremia. Kwa hiyo jamii hiyo inalazimika kufuata mfano wa Yeremia na kumtii Yehova kama “mfalme wa mataifa” kuliko wanadamu. Ndivyo mitume wa Kristo wa karne ya kwanza walivyofanya. —Matendo 4:19, 20; 5:29.
[Picha katika ukurasa wa 16]
Jamii changa ya Yeremia (kama ilivyochorwa katika kalenda ya zamani ya Watch Tower Society) i “juu ya mataifa” kwa kupewa na Mungu cheo na kazi ya kufanya