“Hawatakushinda”
1, 2. Kwa sababu gani jamii ya Yeremia haina muda wa kupoteza katika huu “wakati wa mwisho”?
MWAKA 1919, ambapo Mapatano ya Amani yalifanywa Versailles baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, uliiletea mabadiliko jamii ya Yeremia iliyotiwa mafuta. Walianza kutumia Biblia kuutangaza waziwazi ujumbe wa Yehova juu ya uharibifu utakaoipata taratibu hii ya mambo wakati wa vita ya Mungu inayokaribia katika Har–Magedoni.—Ufu. 16:13-16.
2 Kwa kuwa sasa miaka zaidi ya 57 imepita tangu 1919, hakuna wakati wa kupoteza. Yeremia alikuwa na wakati mchache tu, yaani, miaka 40, kuutangaza uharibifu uliokuwa ukikaribia kuupata Yerusalemu. Wale wanaofananishwa naye nyakati za kisasa wana wakati mchache pia. Inatupasa sana tuwe macho. Baada ya miaka mingi kupita tangu Yehova alipoipa jamii ya Yeremia agizo la kutimiza, hata sasa Yeye angali macho akilikumbuka sana kusudi lake juu ya huu “wakati wa mwisho” ambamo mataifa yamo. (Dan. 12:4) Anaendelea kuwa macho akikumbuka anavyokusudia kufanya baada ya huu “wakati wa mwisho” kumalizika. Yeremia 1:11, 12 inahakikisha hilo kwa kusema:
3, 4. Yehova alimwonyeshaje Yeremia kwamba yeye mwenyewe alikuwa macho ili atimize kusudi lake, na sasa imefaa tujiulize ulizo gani?
3 “Tena neno la [Yehova] likanijia, kusema, Yeremia, waona nini? Nikasema, Naona ufito wa mlozi [shaqéd kwa Kiebrania]. Ndipo [Yehova] akaniambia, Umeona vema; kwa maana ninaliangalia neno langu [“ninaendelea kuwa macho,” NW, shaqéd],ili nitimize
4 Basi, ni nani kati yetu leo atakayethubutu kuacha kuwa macho, awe ni mmoja wa jamii ya Yeremia iliyotiwa mafuta au awe ni mmoja wa wenye kuiunga mkono jamii hiyo kwa bidii? Tutakuwa wenye hekima tukimwiga Yehova mwenyewe. Ili kuonyesha kwamba yeye mwenyewe yuko macho, alimwonyesha Yeremia “ufito wa mlozi” (au, “kitawi cha mti wa lozi,” NW) katika njozi. Yeremia alijua kwamba neno la “mlozi” (shaqéd kwa Kiebrania) linamaanisha “anayeanza kuamka.” Mti huo ndio wa kwanza kuamka kwa kuchanua maua katika masika ya mwaka. Yehova alikuwa kama “ufito wa mlozi” kwa kuwa macho na kuyajua majira ambamo mataifa na falme zilikuwa zikianza kuingia. Neno Lake la unabii linahusika katika wakati fulani uliowekwa, naye atalitimiza wakati huo ukifika. Neno Lake halitakosa kutimia kwa sababu ya yeye kukosa kuwa macho. Je! sisi tunaamini hivyo leo katikati ya mwaka huu wa 1978?
5. Yehova alionyeshaje alikuwa macho kuuona uhitaji wa kuutangaza ujumbe wake kwa haraka zaidi, nasi tutautimizaje uhitaji huo?
5 Kwa sababu Yehova ameendelea kuwa macho makumi yote hayo ya miaka ya huu “wakati wa mwisho,” ameendelea kuituma jamii ya Yeremia ikayaonye mataifa na falme. (Linganisha 2 Mambo ya Nyakati 36:15, 16, NW; Byington.) Wakati wa Yehova wa kuleta hukumu juu ya mataifa na falme uzidipo kukaribia, anazidi kuwa na haraka ya kuhakikisha kwamba onyo limetolewa ulimwenguni pote, hasa kwa faida ya watu mmoja mmoja ambao ni lazima waonyeshe msimamo wao binafsi. Wakikumbuka kwamba sasa Yehova amezidi kuwa macho sana na kwamba atakuwa tayari kwa wakati wake, inawapasa wale walio katika jamii ya Yeremia wawe macho kuuona uhitaji unaoongezeka wa kuutangaza ujumbe wao kwa haraka zaidi. Inawapasa wao wenyewe waendelee kuwa macho kwa kuutangaza ujumbe huo kote kote kwa uthabiti.
MWENYE DARAKA LA KULETA MWISHO WA TARATIBU HII
6, 7. Kutokana na mfano ambao Yehova alimpa Yeremia baada ya hapo, tunajua nini juu ya kukaribia kwa uharibifu wa taratibu hii?
6 Neno la Yehova aliloliongoza kwa roho yake linatujulisha Yule atakayeuleta uharibifu unaokaribia juu ya taratibu iliyopo ya mambo. Kwa hiyo, tunajua mahali uharibifu huo utakakotoka, na vilevile wakili atakayetumiwa kuuleta. Tunapata maelezo zaidi kuhusu uharibifu huo kutokana na mfano ambao Yehova alimpelekea Yeremia wakati wa kumwagiza awe “nabii wa mataifa”:
7 “Neno la [Yehova] likanijia mara ya pili, kusema, Waona nini? Nikasema, Naona sufuria [“lenye kupuliziwa pumzi,” NW] lenye maji yatokotayo, na mdomo wake unaelekea toka upande wa kaskazini. Ndipo [Yehova] akaniambia, Toka kaskazini mabaya yatatokea, na kuwapata watu wote wakaao katika nchi hii. Kwa kuwa, tazama, nitaziita jamaa zote na falme za kaskazini, asema [Yehova]; nao watakuja, na kuweka kila mtu kiti chake cha enzi mbele ya mahali pa kuingilia malango ya Yerusalemu, na kuzielekea kuta zake pande zote, na kuielekea miji yote ya Yuda. Nami nitatamka hukumu zangu juu yao kwa habari ya uovu wao wote; kwa kuwa wameniacha mimi, wakaifukizia uvumba miungu mingine, wakaziabudu kazi za mikono yao wenyewe.”—Yer. 1:13-16.
8. Kwa sababu gani sufuria lililoonekana katika njozi lilipuliziwa pumzi, na ni jambo gani lililoonyeshwa kwa vile liliinamishwa kutoka upande wa kaskazini?
8 Tunakumbuka kwamba Yeremia aliinuliwa mwaka 647 K.W.K. akaagizwa awe “nabii wa mataifa.” Wakati huo msiba ulikuwa ukiukaribia Yerusalemu na nchi ya Yuda. Vitu vilivyokuwa vikichemshwa katika sufuria lililoonekana katika njozi ya Yeremia havikuwa vitu vya kuufaa Yerusalemu mwasi na miji ile mingine ya Yuda. Kusudi la ‘kupulizia sufuria pumzi’ halikuwa kupoesha kilichokuwa ndani bali lilikuwa kuongeza miali ya moto iliyokuwa chini ya sufuria (au nyungu) hilo. Kwa kuwa mdomo wa sufuria ulielekea toka upande wa kaskazini, hiyo inamaanisha kwamba vitu vyenye moto vilivyokuwamo vingemiminwa juu ya kitu kilichokuwa kusini. Kitu hicho kilikuwa mji wa Yerusalemu na nchi ya Yuda. Mabaya ambayo yangeipata yasingetoka Misri kuelekea upande wa kusini wa mji huo na nchi hiyo. Kwa kupitia kaskazini, yangeelekea kusini juu ya miji hiyo iliyohukumiwa maangamizi.—Yer. 4:6, 7; 6:1, 22.
9. Ni vitu gani ambavyo Yeremia aliona vikimiminwa juu ya nchi ya Yuda kutoka lile “sufuria” la mfano?
9 Vitu vilivyokuwa ndani ya sufuria la mfano ambavyo Yehova angevimimina juu ya nchi ya Yuda vingekuwa ni “jamaa zote za falme za kaskazini.” Kwa hiyo Babeli ndiyo ingeongoza shambulio hilo juu ya nchi ya Yuda, kwa maana Milki ya Babeli ilikuwa ikiinuka wakati huo iwe Mamlaka ya Tatu ya Ulimwengu ya unabii wa Biblia. Nabii Yeremia alingoja miaka 27 kabla ya kuliona sufuria hilo la mfano likimimina vilivyokuwamo wakati nchi ya Yuda iliposhambuliwa mara ya kwanza na majeshi ya Babeli, mwaka 620 K.W.K. Miaka mitatu baadaye vilivyokuwamo katika sufuria la mfano vilimiminwa Wababeli walipoishambulia tena nchi hiyo, na mwishowe Yeremia akawa chini ya ufalme wa Sedekia aliyekuwa mtawala mdogo wa Mfalme Nebukadreza wa Babeli. Ndipo Sedekia alipoasi, halafu mwaka 609 K.W.K. sufuria la mfano likamiminwa mara ya tatu na ya mwisho wakati majeshi ya Babeli yalipoiingilia miji ya Yuda.a Katika kiangazi cha mwaka 607 K.W.K. “mabaya” yalifikia upeo wakati Yerusalemu ulipoharibiwa. Mwanzoni mwa vuli ya mwaka huo nchi yote ya Yuda iliachwa ukiwa.
10. Jamii ya Yeremia inatazamia kuona kilichofananishwa na “mabaya” hayo ya kale kikiletwa juu ya nani?
10 Wale walio katika jamii ya Yeremia leo wanatazamia kuona kilichofananishwa na “mabaya” hayo ya kale! Naam, wanatazamia kuona “mabaya” makubwa kuliko hayo yakiipata Jumuiya ya Wakristo, ambayo ndiyo mfano wa kisasa wa Yerusalemu mwasi na nchi ya Yuda.
11. Wakati Biblia inapoumulika “uovu” wa Jumuiya ya Wakristo, unaonekanaje kuwa sawa na ule wa Yerusalemu na Yuda yenye uasi?
11 Jumuiya ya Wakristo ambayo imekuwako kwa muda mrefu inao ‘uovu wote’ uliopotoa Yerusalemu wa kale na nchi ya Yuda. Wakati Biblia inapoimulika Jumuiya ya Wakristo na kuichunguza, inaonekana wazi kwamba jumuiya hiyo inaitolea dhabihu “miungu mingine” ijapokuwa inazo Amri Kumi za Yehova. Naam, inaabudu kazi za mikono ya wanadamu kwa kuziinamia. Inajidai kuwa ya Kikristo, lakini haimwigi Yesu Kristo kwa kujitenga na ulimwengu huu usiomcha Mungu. Imeenewa na utukuzo wa mataifa uliopo leo, wenye kugawanya watu na kutokeza vita. Acha uamuzi wa kitaifa ufanywe, nawe utaiona jumuiya hiyo ikiiabudu serikali ya kisiasa, kazi ya mikono ya wanadamu. Utajiri mwingi sana ambao makanisa ya Jumuiya ya Wakristo inao unaonyesha kwamba inaabudu vitu vya kimwili. Inakuwa adui ya Yehova kwa sababu ya kuwa rafiki mkubwa wa ulimwengu huu!
12. Yehova alitangulia kumwonya Yeremia juu ya nini kisha alimpa ahadi gani inayoweza kututia moyo sisi pia?
12 Yeremia wa zamani zilizopita alipaswa kuonyesha kwamba Yehova alikuwa na haki ya kumimina mabaya juu ya taifa la Waisraeli kwa sababu walivunja agano takatifu walilofanya naye. Yehova alijua kwamba mambo aliyoanza kumwamuru Yeremia katika mwaka 647 K.W.K. awaambie wakaaji wa nchi ya Yuda yangechukiza wengi wao. Kwa hiyo alitangulia kumwonya Yeremia kwa kumwambia waziwazi kwamba wafalme wa nchi, wakuu, makuhani na watu wa Yuda wangepigana naye. Angekaribia kuuawa. Kwa hiyo, ingalikuwaje kama Yehova asingalikuwa amemwahidi nabii huyo kijana kwamba adui hao wote wasingemshinda? Je! angaliendelea kujikaza kwa miaka 40 akiwa “nabii wa mataifa” wa Yehova, kisha mwishowe awaone adui zake wakali wakishindwa kabisa? Haionekani hivyo! Ahadi ambayo Yehova alimpa Yeremia wa zamani zilizopita inaihusu jamii ya Yeremia leo pamoja na wenye kuwaunga mkono!
13. “Sufuria” la mfano linaichemkia Jumuiya ya Wakristo kwa sababu ya mashtaka gani yaliyofanywa juu yake?
13 Leo “sufuria” la Yehova la mfano linauchemkia huu “wakati wa mwisho.” Kama ilivyokuwa kwa ‘vitasa saba vya dhahabu vilivyojaa ghadhabu ya Mungu’ ambavyo vilionekana katika Ufunuo 15:7, “sufuria” hilo linafananisha chombo chenye “mabaya” yote ambayo Yehova ataimiminia Jumuiya ya Wakristo. Hakika Jumuiya ya Wakristo ina ufisadi mwingi sana utakaomfanya Yehova atake imweleze kwa nini imekuwa na ufisadi huo, kwa maana inajidai kuwa katika “agano jipya” pamoja naye kupitia kwa Kristo. Jumuiya hiyo imewatesa vikali mashahidi wake Wakristo, na zaidi ya hapo sasa anaiona mikono yake ikiwa imejaa damu ya vita viwili vya ulimwengu. Basi, ni vizuri kwamba leo jamii ya Yeremia inayatumia maneno ya Yehova yaliyo katika Yeremia 2:34 (NW) kuihusu Jumuiya ya Wakristo, kwamba: “Katika marinda yako kumepatikana alama za damu ya nafsi za maskini wasio na hatia. Sikuzipata wakiwa katika tendo la kuvunja waingie [kama vile wevi wavunjavyo nyumba na kuingia ndani], bali zi juu ya [marinda] yote haya.”—Angalia The Watch Tower la Novemba 1, 1923, ukurasa wa 327, fungu la 3 (6).
14. (a) Kwa sababu gani Jumuiya ya Wakristo ndiyo sehemu yenye malawama mengi zaidi katika milki ya ulimwengu ya dini ya uongo? (b) Yehova ataimiminia nini kutoka “sufuria” lake la mfano?
14 Jumuiya ya Wakristo ingali ikiuonyesha ulimwengu mzima kwa kiburi kwamba inafuata mwendo wa kuua watu. Jumuiya hiyo ndiyo sehemu iliyo na malawama zaidi kati ya milki yote ya ulimwengu ya dini ya uongo, ,kwa maana inadai kwamba inafanya mambo kwa jina la Ukristo au kwa jina la dini ile inayokubaliwa sasa na Mungu wa Biblia. Kwa sababu ya matendo yake ya aibu, si ajabu kwamba watu wasio Wakristo hawaheshimu Ukristo! Mungu wa Biblia amesingiziwa mambo yasiyofaa kwa sababu ya Jumuiya ya Wakristo. Yeye atastahili kuiadhibu kabisa, waziwazi. Lakini kwanza ameiinua jamii ya Yeremia imwonyeshe kila mtu uasi wa imani na uzinzi wa tengenezo hilo la ulimwengu lililo kubwa kuliko matengenezo yote ya kidini. Yehova ameuinamisha ule mdomo mpana na “sufuria” lake la mfano uelekee upande wa tengenezo hilo. Saa inakaribia ambapo atalipindua kabisa sufuria hilo na kuyamimina majeshi yake ya mbinguni yenye kuua watu yaimwagikie jumuiya hiyo iliyo mfano wa kisasa wa Yerusalemu na nchi ya Yuda iliyoasi imani na kufanya uzinzi. Basi msingiziaji huyo mkuu wa jina takatifu la Yehova ataharibiwa.—Yer. 1:14-16.
15. Kwa sababu gani lazima jamii ya Yeremia ifunge mishipi viunoni na kufanya kazi kwa bidii, nayo litaendelea kufanya hivyo mpaka wakati gani?
15 Kazi ya jamii ya Yeremia haijamalizika. Lazima wale walio katika jamii hiyo waendelee kufunga mishipi katika viuno vyao na kuendelea kutia bidii mpaka kazi waliyoagizwa imalizike. Lazima “mkutano mkubwa” wote wa Wakristo wanaoisaidia sana jamii ya Yeremia waendelee kufanya kazi nao. Jamii ya Yeremia ingali inahitaji kusimama bila kutikisika kama “nguzo ya chuma” na “mji wenye boma,” wenye “kuta za shaba.” Ndivyo Yeremia wa zamani zilizopita alivyofanya. Yesu Kristo hakutofautiana kamwe na Yeremia kwa maana yeye pia aliutangaza uharibifu wa Yerusalemu uliokuwa ukikaribia siku zake, nao uharibifu wenyewe ulikuja miaka 676 baada ya Yerusalemu wa siku za Yeremia kuangamia. Kwa kuwa jamii ya Yeremia ni wafuasi wa Yesu Kristo waliotiwa mafuta, ni lazima leo wao pia wafanye ivyo hivyo, mpaka watakapouona uharibifu wa kile kinachofananishwa nyakati zetu na Yerusalemu na Yuda isiyo na uaminifu.
16. Kama Yesu, lazima jamii ya Yeremia itangaze mambo gani mawili?
16 Kama Yesu, lazima jamii ya Yeremia itangaze “siku ya kisasi cha Mungu wetu,” si “wakati uliokubalika” tu, “mwaka wa [Yehova] uliokubaliwa.”—Isa. 61:1, 2; 49:6; 2 Kor. 6:2; Yer. 11:20; 20:12; 46:10; Luka 21:22.
17. Haitupasi kufanya nini kwa sababu wafalme, wakuu, makuhani na watu wanazidi kutufanyia vita?
17 Haitupasi tujilegeze hizi “siku za mwisho” za taratibu hii ya mambo kwa sababu tu wafalme, wakuu, makuhani na watu wa Jumuiya ya Wakristo watazidi kupigana sana nasi. Jamii ya Yeremia si “mtoto” sasa kwa kuwa imefanya utumishi wa hadharani miaka zaidi ya 57 ulimwenguni pote. Tangu mwaka 1919 jamii hiyo imevumilia kwa kufanyiwa vita na wanasiasa, wanadini, na watu mashuhuri wa ulimwengu huu wa zamani.
18. Ni maneno gani ya Yehova yenye kufariji ambayo yamekwisha timia kuihusu jamii ya Yeremia, na hiyo inamaanisha nini juu ya wakati ujao?
18 Bila shaka sasa jamii ya Yeremia, ambayo imevumilia mambo hayo, imekwisha fikia utu mzima. Huenda kila mwaka ikapungua hesabu kwa sababu ya kufa kwa washiriki waaminifu wa jamii hiyo; hata hivyo inaendelea kuifanya kazi iliyopewa na Mwagizaji Mkuu, Yehova. Mpaka sasa maneno yake yenye kufariji yametimia, kwamba wafalme, wakuu, makuhani na watu wenye upinzani hawataishinda jamii hiyo. Wakati ukaribiapo wa kumimina kisasi chake kilicho katika “sufuria” (nyungu) lake la mfano, maneno Yake yatatimia ivyo hivyo katika siku zenye mikazo mingi zaidi zilizo hapa mbele yetu. Adui zetu wenye kufikiria vita tu hawatatushinda! Kwa sababu gani? Kwa sababu Bwana Mwenye Enzi Kuu, Yehova wa majeshi, atabaki pamoja nasi, ‘atuokoe’ wakati ujao kama vile ambavyo ametuokoa wakati uliopita. Kwa hiyo tutawaona adui zetu wakiuma mchanga—wakifa!
“KUJENGA NA KUPANDA”
19. Jamii ya Yeremia iliagizwa ifanye kazi gani yenye kusudi jema, nayo imeifanyaje?
19 Yeremia wa zamani zilizopita aliagizwa awe “nabii wa mataifa” ili “kujenga na kupanda,” si kung’oa, kubomoa, kuharibu na kuangamiza tu. (Yer. 1:10) Hakupaswa “kujenga” kilichobomolewa na kuharibiwa, wala “kupanda” kilichokuwa kimeng’olewa na kuangamizwa, bali alipaswa kutabiri ujenzi wa kile ambacho Yehova alikusudia kijengwe, na kupanda alichokusudia kipandwe hata kikue kabisa. Hakika sasa sehemu hiyo ya agizo ambalo Yeremia alipewa inahusiana na ufalme wa kweli wa Yehova Mungu kwa maana tangu mwaka 1914 W.K. “ufalme wa dunia umekwisha kuwa ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake.” (Ufu. 11:15) Kwa hiyo, sasa lazima maneno haya ya Kristo yatimizwe duniani pote: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote.” (Mt. 24:14, NW) Wakati zinapohubiriwa, wakati uo huo pia Ukristo wa kweli unapandwa na kujengwa katika maeneo mengi mapya yanayoanza kupewa ushuhuda na jamii ya Yeremia pamoja na wenye kuiunga mkono kwa bidii. Paradiso ya kiroho ilihitaji kujengwa.
20. Yeremia alifanyaje kazi ya kujenga na kupanda siku zake, na ni nani wanaohusika katika utimizo wa kazi hiyo leo?
20 Zamani za kale, mwaka 647-607 K.W.K., Yeremia mwenyewe alifanya kazi ya kupanda na kujenga jamii fulani ya watu wasio Waisraeli, waliopaswa kuuokoka uharibifu wa Yerusalemu mwaka 607 K.W.K. Watu hao walikuwa Warekabu, wazao wa Yonadabu, pamoja na towashi Mwethiopia jina lake Ebed-meleki. (Yer. 35:1-9; 38:1-13; 39:15-18) Rafiki hao wa Yeremia wenye kumcha Mungu waliufananisha “mkutano mkubwa” ambao leo unafanya urafiki na jamii ya Yeremia na kuwasaidia mabaki hao waliotiwa mafuta katika kazi yao.Wakiwa pamoja na jamii ya Yeremia wanapatwa na upinzani wenye kuongezeka wa wafalme, wakuu, makuhani na watu.—Angalia kurasa 62-67 za kitabu You May Survive Armageddon into God’s New World, chapa ya 1955.
21. “Mkutano mkubwa” utapewaje thawabu nyingi kwa sababu ya kushikamana na jamii ya Yeremia?
21 “Mkutano mkubwa” utapewa thawabu nyingi kwa sababu ya kuionyesha jamii ya Yeremia ushikamanifu usiovunjika. Wenye kupigana na Mungu leo hawataushinda mkutano huo. Wataiokoka “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” pamoja na jamii ya Yeremia, katika Har–Magedoni. Wao ndio watakaokuwa msingi wa “nchi mpya” wakiwa chini ya “mbingu mpya” za Yehova. (Ufu. 7:9-17; 21:1-4) Jamii ya Yeremia inafurahi sana kwa kujenga katika “mkutano mkubwa” tumaini halali la kuirithi paradiso ya duniani inayokaribia, kulingana na kusudi lenye upendo la Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova! —Kutoka The Watchtower, Dec. 15, 1977.
[Maelezo ya Chini]
a Angalia 2 Wafalme 24:1 mpaka 25:2, maelezo ya chini katika Jerusalem Bible; Kitabu cha X cha Yosefo, Antiquities of the Jews, sura ya 6; Jewish Encyclopea chini ya “Yehoyakimu”; All Scripture Is Inspired of God and Beneficial, ukurasa wa 295, chini ya mwaka 628 K.W.K. mpaka 609 K.W.K.
[Picha katika ukurasa wa 21]
“Sufuria” la Yehova lenye mabaya litamiminwa juu ya Jumuiya ya Wakristo