Mahubiri ya Mlimani—“Heri” Tatu za Kwanza
YESU alianza Mahubiri yake ya Mlimani kwa mfuatano wa misemo tisa ambayo inasimulia watu ambao ni wenye furaha kweli kweli. Katika “heri” ya kwanza yazo, Yesu alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaoona uhitaji wao wa kiroho, kwa kuwa ufalme wa Mungu ni wao.”—Mt. 5:3, NW; An American Translation.
“Wale wanaoona uhitaji wao wa kiroho,” kulingana na Kigiriki halisi cha Mathayo, ni watu “walio maskini wa roho.” Masimulizi ya Luka yanayolingana na hayo yanamripoti Yesu akisema: “Heri ninyi mlio maskini, kwa sababu ufalme wa Mungu ni wenu.” (Luka 6:20) Yesu alionyesha kwamba sababu kubwa ya kuja kwake ilikuwa “kuwahubiri maskini habari njema.” (Luka 4:18) Hii haionyeshi kustahili ko kote kwa kipekee katika kuwa maskini wala kwamba maskini wanapata kibali ya Mungu kwa kuwa tu wao ni maskini. Walakini, kwa msingi, waliomfuata Yesu na kupewa tumaini la kuzishiriki baraka za ufalme wa Mungu walitolewa kutoka kati ya maskini au watu wa kawaida. (1 Kor. 1:26-29; Yak. 2:5) Waliokanyagiwa chini walijijua kuwa wao ni “maskini wa roho” (kiroho) pia. Mahali pa kuwa na uchungu kwa sababu ya hali zao za nje-nje, walipata ‘kuona uhitaji wao wa kiroho,’ wakifahamu zaidi tegemeo lao kwa Mungu.
Tofauti yake, Yesu alitangaza hivi: “Lakini, ole wenu ninyi mlio matajiri, maana mmekwisha pokea kituliza chenu.” (Luka 6:24, Habari Njema kwa Watu Wote) Mara nyingi mali za kimwili huzuia mtu asione uhitaji wake wa kiroho. Mfano wa hili unapatikana katika maneno ya Yesu alipokemea Wakristo fulani huko Laodikia, Asia Ndogo: “Wasema, Mimi ni tajiri, nimejitajirisha, wala sina haja ya kitu; nawe hujui [yaani, huoni kiroho] ya kuwa wewe u mnyonge, na mwenye mashaka, na maskini, na kipofu, na uchi.”—Ufu. 3:17.
Sababu ya furaha kwa wale wanaoona uhitaji wao wa kiroho ni kuwa “ufalme wa mbinguni ni wao.” Walimkubali Yesu kuwa Masihi, nalo hilo likawatolea nafasi za kutawala pamoja naye katika ufalme wa Mungu wa kimbinguni kupitia kwa Kristo. (Luka 22:30; Yohana 14:1-4) Lo! namna ilivyopendeza mioyo ya watu hao wanyenyekevu wa kawaida kufahamu kwamba wangaliweza kuupata ufalme wa Mungu, huku matajiri na wenye elimu nyingi waliotumainia mali zao na kuwaona watu wa kawaida kama kwamba “wamelaaniwa” wasiupate! (Yohana 7:49) Bila shaka matajiri wangaliweza kuonyesha waziwazi roho ile ile ya unyenyekevu na kuthamini kwa kiroho ambako kungewapa furaha vilevile.—1 Tim. 6:17-19; Yak. 1:9, 10.
N1 WATU GANI WANAOHUZUNIKA WATAFARIJIKA?
Ikiwa ndiyo “heri” ya pili, Yesu alisema: “Heri wenye huzini; maana hao watafarijika.” (Mt. 5:4) Masimulizi yanayolingana ya hayo ya Luka yanasema hivi: “Heri ninyi mliao sasa, kwa sababu mtacheka.”—Luka 6:21.
“Wenye huzuni” si watu wote wanaoonyesha majonzi. Tofauti yake, wao ni kama watu wale wale “wanaoona uhitaji wao wa kiroho” waliotajwa katika maneno ya Yesu yaliyotangulia. Huzuni yao ni “huzuni iliyo kwa jinsi ya Mungu” juu ya hali yao yenye dhambi na hali zenye taabu zilizotokezwa na dhambi ya kibinadamu. (1 Kor. 5:2; 2 Kor. 7:10) Wanalitii shauri la mwandikaji wa Biblia Yakobo: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi. Itakaseni mikono yenu, enyi wenye dhambi, na kuisafisha mioyo yenu, enyi wenye nia mbili. Huzunikeni na kuomboleza na kulia.”—Yak. 4:8, 9.
Watu hawa wanaohuzunika kwa huzuni iliyo kwa jinsi ya Mungu “watafarijika.” (Linganisha Luka 2:25.) Kati ya faraja zijazo kupitia kwa Yesu Kristo ni msamaha wa dhambi na uzima wa milele.
Wanaohuzunika waliotajwa na Yesu wanaweza kuitwa “heri” sasa na katika wakati ujao. Kwa sababu ya kumwamini Yesu, wanafurahia hali njema itokanayo na uhusiano (urafiki) wenye kibali pamoja na Yehova Mungu. (Yohana 3:36) Na kwa habari ya furaha ya wakati ujao, wanaohuzunika sasa kwa sababu ya uovu wa wanadamu wanaweza kutazamia ‘faraja wakati wa kufunuliwa kwake Bwana Yesu Kristo kutoka mbinguni pamoja na malaika wa uweza wake; katika mwali wa moto; huku akiwalipiza kisasi wao wasiomjua Mungu, na wao wasioitii Injili ya Bwana wetu Yesu.’—2 The. 1:7, 8.
Tofauti na furaha ile inayotangaziwa wanaohuzunika, Yesu alisema: “Ole wenu ninyi mnaocheka sasa, kwa kuwa mtaomboleza na kulia.” (Luka 6:25) Hii hailaumu kucheka na kujifurahisha. Kwa wazi Yesu alikuwa akizungumza juu ya watafutaji wa anasa ambao maisha yao yamewekwa wakf kwa ajili ya raha zao wenyewe. Wao hawahuzunikii ama hali yao ya dhambi waliyorithi ama kusikitikia kuteseka kwa wanadamu wenzao. Watu mmoja mmoja kama hao wanatafuta raha yao kwa mwendo wa maisha ya kujitosheleza wao binafsi kwa anasa ya muda mfupi tu inayoweza kupatikana.
Yesu alikazia kwamba kicheko chao cha upuzi ni cha “sasa” tu. Watu hao mmoja mmoja ‘wataomboleza na kulia’ wakati Mungu aletapo mwisho kwa taratibu ya mambo iliyopo ambayo imewatolea nyakati za kicheko na uchangamshi wao. (Mt. 13:42, 50; 22:13; 24:51; 25:30) Kupatana na maneno ya Yesu, Yakobo anaonya kwa upole hivi: “Kucheka kwenu na kugeuzwe kuwa kuomboleza, na furaha yenu kuwa hamu. Jidhilini mbele za [Yehova], naye atawakuza.”—Yak. 4:9, 10; 5:1-6.
FURAHA KWA “WENYE UPOLE”
Kisha, Yesu akasema: “Heri wenye upole; maana hao watairithi nchi.” (Mt. 5:5) Alizungumza juu ya watu wa namna gani?
Katika Maandiko neno linalotafsiriwa “upole,” halimaanishi woga, udhaifu au wema wa kujibandika kuelekea wale walio na cheo kidogo, upole wa kinafiki. Tofauti yake, upole ni sifa ya kindani ya upole na amani wanayoionyesha watu kwanza katika uhusiano wao na Mungu, wakitenda kulingana na mapenzi na uongozi wake. Mahali pa kuwa na uchungu kwa sababu ya uonezi na upotovu wa haki wenye kuenea pote duniani; watu mmoja mmoja wenye upole kweli kweli wanafahamu kuwa ole hizi sana sana zinatokana na kutokamilika kwa kibinadamu. Hawamwonei Mungu uchungu, bali wanaona uhitaji mwingi sana wa kumtegemea. Halafu, hali hii ya akili, inajionyesha katika mwenendo kuelekea wanadamu wengine ambao unapatana na shauri hili: “Msimlipe mtu uovu kwa uovu . . .kama yamkini, kwa upande wenu, mkae katika amani na watu wote.”—Rum. 12:17-19; Tito 3:1, 2.
“Wenye upole” hawa wanafurahi kwa sababu “watairithi nchi.” Hili linatukiaje? Yesu aliyekuwa “mpole na mnyenyekevu wa moyo” katika maana kamili, ndiye Mrithi mkuu wa nchi. (Zab. 2:8; Mt. 11:29; 28:18; Ebr. 1:2; 2:5-9) Maandiko ya Kiebrania yalitabiri kwamba “Mwana wa Adamu” atakuwa na watawala washirika katika ufalme wake wa kimbinguni. (Dan. 7:13, 14, 22, 27) Wakiwa ‘warithi pamoja na Kristo,’ wenye upole watashiriki kurithi nchi pamoja na Kristo. (Rum. 8:17) Kuongezea hayo, milki ya kidunia ya ufalme wa Yesu, watu wengine wengi wa ‘mfano wa kondoo’ wataingia katika uzima wa milele. (Mt. 25:33, 34, 46) Lo! taraja lenye furaha kweli kweli!