“Ufalme wa Bwana Wetu na wa Kristo Wake” Waanza
1. Ni wakati gani wanafunzi wa Kristo 144,000 waliozaliwa kwa roho watakapoacha kuwa raia za kidunia za ufalme wake wa kiroho?
TUNAPENDEZWA na watawala katika serikali yetu ya ulimwenguni pote inayokuja. Baada ya muda fulani wanafunzi wote 144,000 wa Kristo waliozaliwa kwa roho watakuwa kati ya watawala hao. Wakati huo hawatakuwa tena raia za ufalme wa kiroho wa Kristo, bali watakuwa wafalme pamoja naye mbinguni. Taraja hilo linapatana na maneno ya ufunuo 5:9, 10 yanayosemwa kwa Yesu Kristo, Mwana-Kondoo wa Mungu hivi: “Ulimnunulia Mungu kwa damu yako watu wa kila kabila na lugha na jamaa na taifa, ukawafanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu; nao wanamiliki [“watatawala,” NW] juu ya nchi.”
2. Watawala katika utawala wa ulimwenguni Pote unaokuja watakuwa wa asili gani ya wanadamu.
2 Angalia, Tafadhali! Kwamba andiko hili lililoongozwa na Mungu halisemi kwamba huyu Mwana-Kondoo wa Mungu aliyetolewa dhabihu alimnunulia Mungu watu kutoka katika makabila kumi na mawili (12) ya taifa moja tu la Israeli waliosema lugha ya Kiebrania. Si watu wa taifa la Kiyahudi wasemao Kiebrania peke yao watakaokuwa sehemu ya watakaotawala katika serikali yetu ya ulimwengu wote inayokuja. Watawala wa utawala huo wa ulimwenguni pote hawatakuwa na chanzo chao katika taifa la Israeli la kiasili tu ijapokuwa Mwana-Kondoo wa Mungu, Yesu Kristo mwenyewe, alikuwa Myahudi au Mwisraeli aliyekuwa akisema Kiebrania alipokuwa mwanadamu mkamilifu duniani. Kwa kuwa sasa yuko mbinguni hatajulikana tena kulingana na jinsi ya mwili alioutoa kama dhabihu. (2 Kor. 5:16) Kupatana na haya, watu ambao atakuwa nao kama washiriki wake katika ufalme wa kimbinguni ni wale aliowanunua kutoka “kila kabila na lugha na jamaa na taifa.”
3. Kwa hiyo watawala hao watakuwa wakipendezwa sana na nani hapa duniani, na kwa sababu gani?
3 Kwa hiyo wale watakaokuwa watawala watakuwa watu wa kutoka katika mataifa yote. Kwa sababu hiyo, bila shaka watapendezwa na washiriki wote wa jamaa ya kibinadamu bila kujali rangi, ujamaa kabila, taifa wala lugha. Hii ni kama inavyopaswa kuwa, kwa sababu yule Mwana-Kondoo wa Mungu aliyechinjwa alifia jamaa nzima ya kibinadamu, wala hakufia jamaa moja wala taifa moja tu.
4. Raia za mataifa yote kwa hakika ni mali ya nani na kwa sababu gani?
4 Leo serikali nyingi za kisiasa zinaona raia zao kuwa mali ya Serikali. Katika njia hii serikali hizo zinamwondolea Mungu Muumba na Mwanawe Yesu Kristo aliyetolewa dhabihu, haki za uenyeji wa mali. Lakini, karibuni sana, katika Baraza ya Hukumu ya Kimungu mbinguni itaonyeshwa kwamba Mwana-Kondoo wa Mungu, Yesu Kristo alichinjwa hapa duniani kwa ajili ya watu wa mataifa yote. Kwa hiyo wote ni mali yake kwa haki ya ununuzi, wala si mali ya mwanadamu wala wanadamu wo wote. Wao ni mali ya Kristo, ndiyo, vilevile ni mali ya Baba yake wa kimbinguni, Yehova Mungu. Kwa hiyo, si wale 144,000 watakaokuwa wafalme pamoja na Kristo katika serikali ya kimbinguni, walionunuliwa peke yao. Inatupasa tuwe na maoni kama yale aliyokuwa nayo Yohana Mbatizaji, alipoelekeza kwa Yesu aliyebatizwa na kupaza sauti hivi: “Tazama, Mwana-Kondoo wa Mungu, aichukuaye dhambi ya ulimwengu!” Ndiyo, ya ulimwengu!—Yohana 1:29.
5. Serikali ya kifalme inayokuja itakuwa kubwa kiasi gani, na Mfalme wa Kimasihi atakuwa na nani kama raia zake?
5 Kwa kupatana sana na uhakika huu, ule utawala wa ulimwengu wote unaokuja utakuwa wa kuenea dunia yote. Unabii wa Zekaria 9:10 unasema hivi kwa habari ya Mtawala wa Kimasihi: “Naye [Mkuu wa Amani] atawahubiri mataifa yote habari za amani; na mamlaka yake yatakuwa toka bahari hata bahari, na toka Mto [Frati] hata miisho ya dunia.” Unabii wa Zaburi 72:7, 8 unatangaza hivi katika msemo unaolingana na huo: “Siku zake yeye, mtu mwenye haki atasitawi, na wingi wa amani hata mwezi utakapokoma. Na awe na enzi toka bahari hata bahari, toka Mto hata miisho ya dunia.” Unabii huu haukutimizwa katika Jumuiya ya Wakristo, ijapokuwa inajidai kuwa ufalme wa Kristo na leo inajidai kuwa na wanakanisa karibu milioni elfu moja wa madhehebu nyingi za dini kuzunguka dunia yote. Yale mataifa yanayojidai kuwa ya Kikristo ndiyo yamekuwa mataifa ya kisiasa yenye kuchafua amani kuliko yote katika uso wa dunia hii. Hayakujionyesha kuwa raia walio na umoja na Mfalme wa Amani, Kristo.—Isa. 9:6.
6.Mataifa ya Jumuiya ya Wakristo yameonyeshaje kwamba wao si raia za Mfalme wa Amani?
6 Je! si wao waliosababisha amani ya ulimwengu iharibiwe na vita ya ulimwengu miaka ya 1914 hadi 1918? Mataifa ishirini (20) au zaidi kati ya mataifa na milki 28 ambayo mwishowe yalijiingiza katika vita, yalijidai kuwa mataifa ya Kikristo. Walikwenda kupigana juu ya suala (sababu) gani? Juu ya suala la utawala wa ulimwengu. Hapana, si kupigania utawala wa ulimwengu wa Yesu Kristo, bali kupigania utawala wa ulimwengu kwa ajili ya ye yote ambaye angeshinda vita hiyo ya dunia yote. Lakini Vita ya Ulimwengu ya Kwanza haikumaliza kabisa suala hilo. Miaka 21 baadaye, walianza kupigana juu ya suala hilo kwa kadiri kubwa zaidi. Na sasa suala hilo la utawala wa ulimwengu halijamalizwa kwa kutosheka kwa mataifa ya ulimwengu baada ya miaka 32 tangu kumalizika kwa Vita ya Pili ya Ulimwengu. Hali ya ulimwengu inazidi kuwa mbaya kwa kiasi cha kutokeza vita ya tatu ya dunia yote iliyo kali sana.
7. Mataifa ya kidunia ambayo yamesimamisha enzi zao kuu wamedharau tangazo gani wanalotangaziwa na Mashahidi wa Kikristo wa Yehova?
7 Mpaka sasa mataifa ambayo yametanguliza mbele enzi yao ya kitaifa yamekataa jambo ambalo Mashahidi wa Kikristo wa Yehova wamekuwa wakiwatangazia hata katika mateso makali. Kutangaza nini? Hili: kwamba ruhusa yao ya kutawala ulimwengu bila kuingiliwa na ufalme wa Mungu ilikwisha mapema mwa kiangazi cha mwaka huo wenye vita wa 1914. Au kwa kutumia usemi wa unabii wa Yesu Kristo, “majira ya Mataifa,” “nyakati zilizowekwa za mataifa,” zilikwisha. Ndipo ulipofika wakati uliowekwa na Yehova Mungu, Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote, achukue hatua ya kusimamisha “Ufalme wa Bwana wetu na Kristo wake.” Aliusimamisha ufalme wa Kristo wake, si katika Yerusalemu wa kidunia kule Mashariki ya Kati, bali mbinguni, kwenye mkono wake mwenyewe wa kuume. (Luka 21:24, Union Version; Tafsiri ya New World) Kwa sababu jambo hili lilitukia huko mbinguni, hatukuliona likitukia. Lakini ushuhuda wake unaonekana kwetu katika mambo ambayo Yesu Kristo alitabiri kama “dalili” inayoonekana.—Mt. 24 na 25; Marko 13:3-37; Luka 21:5-36.
INGIA KATIKA “UFALME WA BWANA WETU NA WA KRISTO WAKE”
8. “Ishara” hiyo imekuwa yenye kusomeka waziwazi kuanzia wakati gani na ilionyesha ni wakati wa tangazo gani?
8 Ni wangapi kati yetu wameona “dalili” hiyo na wakajua maana yake kama vile imekuwa ikifunuliwa mbele ya macho yetu tangu mwisho wa Majira ya Mataifa mwaka 1914? Inaonyesha kwamba wakati huo ndio uliokuwa wakati wa sauti kuu katika mbingu kutangaza hivi: “Ufalme wa [ulimwengu] umekwisha kuwa ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake, naye atamiliki hata milele na milele.”—Ufu. 11:15.
9. “Ufalme” huu unalinganaje na ule unaotajwa katika Wakolosai 1:13, na ni nani anayesemwa kuwa ndiye mfalme wake?
9 Na tusikilize tangazo hilo tena tuone linavyosema. Halisemi kwamba ‘watamiliki milele hata milele,’ bali, “naye atamiliki milele hata milele.” Ni nani basi anayesemekana kwamba atatawala kama mfalme milele hata milele? Ni lazima awe yule mkuu zaidi anayesemwa katika tangazo hilo, yule ambaye ana Kristo au Mtiwa Mafuta. Ni lazima awe yule anayesemwa kuwa “Bwana wetu.” Yule anayeitwa mbinguni “Bwana wetu” Ndiye Mkuu, na “Kristo wake” ndiye wa pili, mdogo wake. Kwa hiyo, serikali inaitwa “ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake,” na ni kitu kikubwa zaidi kuliko “ufalme wa Mwana wa pendo lake,” unaotajwa katika Wakolosai 1:13, mtume Paulo alitaja ufalme kama huo miaka 35 mbele ya Yohana kuandika Ufunuo. Kwa hiyo, wakati wa kuchukuliwa kwa “ufalme wa [ulimwengu]” Yehova Mungu ndiye kwa kweli anayeanza kutawala. Yeye ndiye “Bwana wa nchi.”—Ufu. 11:4; Zek. 14:3-9.
10. Hii inaonyesha mwanzo wa jambo gani kwa Ufalme wa Milele”?
10 Yale yaliyosemwa na wale wazee 24 walipokuwa wakiabudu mbele ya kiti cha enzi cha Mungu yanaonyesha kwamba hayo ndiyo matumizi sahihi ya usemi “Bwana wetu”: “Tunakushukuru wewe, Bwana Mungu Mwenyezi, uliyeko na uliyekuwako, kwa sababu umeutwaa uweza wako ulio mkuu, na kumiliki.” (Ufu. 11:16, 17) Kwa hiyo hii inaonyesha mwanzo wa kipindi cha pekee cha utawala wa enzi kuu ya Mungu ya ulimwengu, “Mfalme wa milele.”—1 Tim. 1:17; Ufu. 15:3.
11. Mtoto mwanamume wa mfano aliyezaliwa na “mwanamke” wa Mungu ana cheo gani, lakini sana sana ni nani anayetumia mamlaka ya ufalme?
11 Ufalme wa Yehova Mungu ndio unaotukuzwa hata na yale yanayosemwa juu ya kuzaliwa kwa mtoto na “mwanamke” wa kimbinguni wa Mungu. Mtoto huyo anafananishwa na mtoto mwanamume, “atakayewachunga mataifa kwa fimbo ya chuma.” Bila shaka hiyo inamaanisha kwamba huyo mtoto mwanamume wa mfano ataponda mataifa yote ya kisiasa ya dunia vipande vipande kama kuvunja chombo cha mfinyazi. Kwa hiyo anatimiza cheo cha kiserikali. Lakini, ni nani sana sana anayetumia mamlaka ya ufalme? Tunaambiwa waziwazi katika maneno haya: “Na mtoto wake akanyakuliwa hata kwa Mungu, na kwa kiti chake cha enzi.”—Ufu. 12:5.
12. Ni nani anayemtawaza mtoto wa kiume wa mfano, na kulingana na hayo, ni nani anayesemwa baadaye kuwa anao ufalme na ni nani anayepewa mamlaka?
12 Mungu ndiye anayemtawaza huyu mtoto mwanamume wa mfano. Mungu ndiye mwenye haki yote ya utawala. Huyo mtoto mwanamume wa mfano anapewa cheo kilicho chini ya ufalme wa Mungu. Kama kitu kinachotumiwa katika serikali ya Mungu kinatajwa kama kitu kipya kabisa, kama mtoto ambaye amezaliwa hivi sasa, si kama kitu ambacho kimekuwapo tangu Pentekoste ya mwaka 33 W. K. Kulingana na hayo, wakati vita inapotokea mbinguni baada ya kuzaliwa kwa huyu mtoto mwanamume wa mfano halafu kukawa na ushindi, Shetani na mashetani wake wakiwa wamefukuzwa, sauti kuu inasikika mbinguni ikisema: “Sasa kumekuwa wokovu, na nguvu, na ufalme [wa nani?] wa Mungu wetu, na mamlaka ya Kristo wake; kwa maana ametupwa chini mshitaki wa ndugu zetu.” (Ufu. 12:7-10) Kwa mara nyingine ufalme unasemwa kuwa wa Mungu wetu. Kwa kweli Yeye ndiye anayetawala, naye Kristo wake au Mtiwa Mafuta, Yesu, anapata “mamlaka” atawale akiwa chini ya Bwana Mungu.
13. Majira ya Mataifa yalipokwisha mwaka 1914, ni suala (ulizo kuu) gani lililomwelekea Yehova, na hili lilikuwa limeonyeshwaje mapema kuelekea dunia yetu?
13 Kuna sababu nzuri ya Maandiko ya kusema mambo kwa njia hii, mkazo ukitiliwa katika ufalme wa Yehova Mungu. Wakati “ufalme wa [ulimwengu]” unapochukuliwa mwishoni mwa Majira ya Mataifa katika mwaka 1914, enzi Yake kuu ya ulimwengu wote ndiyo inayotokeza suala (jambo) linaloshindaniwa. Miaka 2,520 kabla ya hapo, Yehova alikuwa na ufalme duniani ambao ulimwakilisha katika ya mataifa yasiyo ya Kiyahudi. Huo ulikuwa ufalme wa ukoo wa Daudi katika Yerusalemu. Daudi na warithi wake wa kifalme walisemekana kwamba waliketi katika “kiti cha enzi cha [Yehova]” katika mji mkuu wa taifa hilo. (1 Nya. 29:23) Kabla tu ya kifo chake Daudi alitoa mchango kwa ukarimu kwa kumjengea Yehova hekalu na wakati huo yeye alisema hivi: “Ufalme ni wako, Ee [Yehova] nawe umetukuzwa, u mkuu juu ya vitu vyote.” (1 Nya. 29:11) Kwa hiyo ufalme wa nyumba ya kifalme ya Daudi ulikuwa wonyesho wa enzi kuu ya ulimwengu wote ya Yehova Mungu kuelekea dunia.
14. Ijapokuwa Mungu alifanya agano la ufalme wa milele na Daudi, ni kukatizwa gani kulikotokea katika kuketi katika kiti cha enzi cha ukoo wa Daudi?
14 Kupatana na agano la Mungu kwa Mfalme Daudi la utawala wa milele, nyumba ya kifalme ya Daudi iliendelea kuketi katika “kiti cha enzi cha [Yehova]” katika Yerusalemu mpaka kiangazi cha mwaka 607 K.W.K. Katika wakati huo wenye msiba majeshi ya Kibabeli yaliuteka Yerusalemu na yakauangamiza, naye Mfalme Zedekia akachukuliwa mateka mpaka Babeli. Kuachwa ukiwa kabisa kwa nchi ya Yuda kulifuata, kufikia katikati ya mwezi wa saba, Tishri, wa mwaka huo. Ingawa Wayahudi waliookoka wakiwa uhamishoni walirudishwa Yerusalemu na nchi ya Yuda miaka 70 baadaye, “kiti cha enzi cha [Yehova]” hakikusimamishwa katika Yerusalemu, kiketiwe na mtu wa ukoo wa Daudi akiwa na haki ya kifalme ya kuwa na taji na fimbo ya enzi. Kwa sababu gani?
15. Kukatizwa kwa enzi kuu ya Yehova kuelekea hapa duniani, kulifananishwaje katika ndoto ya Mfalme Nebukadreza?
15 Sababu ilikuwa kwamba, sasa, tangu nchi ya Yuda ilipoachwa ukiwa katika mwaka 607 K.W.K., Nyakati za Mataifa zilikuwa zimeanza na zingeendelea kwa muda wa miaka 2,520, au mpaka 1914 W.K. Enzi kuu ya Yehova kuelekea dunia hii ndiyo iliyokuwa kama ule mti mkubwa ulioonekana katika ndoto ya Nebukadreza. Mti huo ulikatwa ukaangushwa chini, ila kisiki cha shina lake tu ndicho kilichoachwa katika ardhi. “Nyakati saba” ziliamriwa zipite juu ya shina la kisiki hicho cha mti kabla ya ukuzi wo wote kutokea katika kisiki hicho. Kwa sababu hiyo pingu za chuma na shaba zilifungwa kukizunguka kisiki hicho cha mti, zikae mpaka “nyakati saba” zitakapomalizika. (Dan. mlango wa nne) Kulingana na ukweli wa mfano huu, mwishoni mwa “nyakati saba” za mataifa yasiyo ya Kiyahudi kutawala dunia bila kuzuiwa, enzi kuu ya Yehova ya ulimwengu wote ingejionyesha tena kuelekea dunia yetu.
16, 17. (a) Katika wakati huo uliowekwa, ni ufalme gani ambao ulipaswa kuwa mali ya Yehova na ni tangazo gani lililofaa lifanywe wakati huo? (b) Wakati wa uharibifu wa Babeli Mkuu, ni nini kitakachotangazwa kuonyesha uhakika wa kwamba Yehova amekuwa mtawala?
16 Katika wakati huo uliowekwa katika orodha ya Mungu ya mambo, ungekuwa ndio wakati wa ‘ufalme wa ulimwengu kuwa ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake.’ (Ufu. 11:15) Hiyo ingekuwa sababu inayofaa ya wale wote wanaokaa mbinguni na duniani kuwa na furaha kubwa wale waliokuwa wakimwomba Mungu aonyeshe tena enzi yake kuu kwa ukamilifu kuelekea dunia yetu, ambapo mataifa yasiyo ya Kiyahudi yalitawala kwa muda mrefu sana. Wakati huo, wala si wakati wa kumiminwa kwa roho takatifu wakati wa Pentekoste ya mwaka 33 W.K., ndio ungekuwa wakati wa kufanywa tangazo la Zaburi 97:1, 9: “[Yehova amekuwa mfalme!], nchi na ishangilie, visiwa vingi na vifurahi. Maana Wewe, [Yehova], ndiwe Uliye juu, juu sana kuliko nchi yote; umetukuka sana juu ya miungu yote.” (Pia, Zaburi 99:1.) Baadaye, kuharibiwa kwa Babeli Mkuu (milki ya ulimwengu ya dini ya uongo) kungeonyesha uhakika wa ufalme wa Yehova. Sauti zitapazwa kwa Haleluya hivi:
17 “Msifuni Yah, enyi watu, kwa sababu Yehova Mungu wetu, Mwenye Nguvu Zote, ameanza kutawala kama mfalme.”—Ufu. 19:6, NW.
18. Ni nani basi anayejichukulia uwezo wa kutawala kama mfalme, na ni thawabu (zawadi) gani anayompa Mwanawe?
18 Matangazo haya yalionyesha wazi uhakika wa kwamba Yehova, Bwana Mwenye Enzi Kuu ndiye anayechukua utawala wake tena kuelekea dunia yetu mwishoni mwa “nyakati saba” za utawala wa mataifa yasiyo ya Kiyahudi. Yeye ndiye anayeutwaa uweza wake mkuu na kuuchukua “ufalme wa [ulimwengu].” (Ufu. 11:15-17) Ndipo anapompa Mwanawe, Yesu Kristo, nafasi ashiriki katika “ufalme, wa [ulimwengu].” Kwa hiyo, “Kristo wake” anashiriki katika kitu ambacho hajapata kuwa nacho kamwe hapo kwanza, kikiwa zawadi kutoka kwa Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. Hii ndiyo zawadi aliyomwahidi. Huo ulikuwa wakati alipokuwa karibu kuangusha na kuharibu ufalme wa ukoo wa kifalme wa Daudi katika Yerusalemu. Wakati huo yeye alisema kwa mrithi wa mwisho wa Mfalme Daudi aliyekuwa akitawala hivi: “Kiondoe kilemba, ivue taji; haya hayatakuwa tena kama yalivyo. . . . Nitakipindua, nitakipindua, nitakipindua; hiki nacho hakitakuwa tena, hata atakapokuja yeye ambaye ni haki yake; nami nitampa.”—Eze. 21:25-27.
19. Kulingana na unabii wa Yesu mwenyewe katika Luka 21:24, kwa sababu gani hangepewa kile kilichopata kuwa “haki yake” hata katika Pentekoste ya mwaka 33 W.K.?
19 Yesu Kristo alijionyesha mwenyewe kuwa yeye “ambaye ni haki yake,” kwa uaminifu wake hata kufa alipokuwa na mwili hapa duniani. Yeye ndiye Mrithi wa Kudumu (wa Milele) wa Daudi. Lakini hakupewa kile ambacho “ni haki” yake katika mwaka 33 W.K., baada (nyuma) ya kwenda mbinguni. Siku 40 kabla ya kupaa mbinguni yeye alitoa unabii wake kama ulivyoandikwa katika Luka 21:5-36. Katika huo yeye alionyesha mbele uharibifu ambao ungekuja juu ya Yerusalemu uliokuwako wakati huo, na ambao uliletwa na majeshi ya Kirumi katika mwaka 70 W.K., na juu ya hili alisema hivi: “Wataanguka [Wayahudi] kwa ukali wa upanga, nao watatekwa nyara na huchukuliwa katika mataifa yote; na Yerusalemu utakanyagwa na Mataifa, hata majira ya Mataifa yatakapotimia.” (Luka 21:24) Kwa hiyo hata katika Pentekoste ya mwaka 33 W.K. yeye hangepewa kile kilichokuwa “haki” yake.
20. Kulingana na Ezekieli 21:25-27, ni kitu gani kilichopata kuwa ni “haki yake” Yesu, na ni nini ambacho Daudi angeweza kumwachia Yesu kama Mrithi wa Kudumu?
20 Kile kilichokuwa “haki” ya Yesu Kristo kilikuwa ufalme wa Daudi, ufalme wa kidunia, ambao “kilemba” na “taji” yake vilikuwa vikivaliwa na Daudi na warithi wake wa kifalme. (Eze. 21:25-27) Yesu alizaliwa katika ukoo wa kifalme wa Daudi kama mwanadamu mkamilifu (asiye na kosa), kwa hiyo bila shaka yeye alikuwa na haki ya ufalme wa Daudi. (Rum. 1:3, 4; Luka 1:32, 33) Kwa kuwa Daudi alikuwa mfalme wa kidunia, yeye hangemwachia Yesu Kristo zaidi ya kile alichokuwa nacho, ufalme wa kidunia. Malaika Gabrieli alimwambia mama ya kidunia ya Yesu, Myahudi bikira Mariamu, kwamba Mungu angempa yeye “kiti cha enzi cha Daudi, baba yake.” Je! ufalme huu ulipewa Yesu katika mwaka 33 W.K., alipopaa kurudi mbinguni akakaa katika mkono wa kuume wa Mungu? Ufalme wa Daudi ulikuwa umepinduliwa katika mwaka 607 K.W.K., uendelee bila kutenda kwa muda wa “nyakati saba” Mataifa yasiyo ya Kiyahudi yalipokuwa yakitawala dunia, au, miaka 2,520 kuanzia mwaka 607 K.W.K.—Matendo 1:6.
21. Kwa hiyo kabla Yesu hajatumia haki yake ya kutawala katika ufalme wa Daudi, alipaswa kungojea Mungu achukue tendo gani?
21 Hivyo, kabla Yesu Kristo aliyetukuzwa hajatumia haki yake katika ufalme wa Daudi wa kidunia, ilimpasa angojee katika mkono wa kuume wa Mungu mpaka Nyakati za Mataifa zimalizike katika mwaka 1914 W.K. (Ebr. 10:12, 13) Ilikuwa lazima angojee mpaka Yehova Mungu ajitwalie ‘uweza wake ulio mkuu’ akiwa kama Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote na kuzimaliza Nyakati za Mataifa na kuchukua “ufalme wa [ulimwengu].” Ndipo Mungu angemkaribisha Yesu, akiwa ndiye Mrithi wa Kudumu wa Mfalme Daudi, ashiriki pamoja naye katika “ufalme wa [ulimwengu],” ufalme juu ya wanadamu wote walioko duniani.—Ufu. 11:15
22. Hivyo basi, utawala mpya ulizaliwa wakati gani, na hii ilifananishwaje katika unabii mbalimbali wa Biblia?
22 Kwa hiyo ilikuwa mwaka 1914, wala si mwaka 33 W.K., ndipo lile “jiwe” la mfano lililoonekana katika ndoto ya Mfalme Nebukadreza lilipochongwa mlimani mkubwa uliyofananisha enzi kuu ya ulimwengu wote ya Yehova. (Dan. 2:34, 35, 44, 45) Vilevile wakati huo ndipo Yehova Mungu aliposimamisha “miguu” yake juu ya “Mlima wa Mizeituni” wa mfano ukapasuka katikati yake ukawa milima miwili, mmoja katika upande wa kaskazini na ule mwingine katika upande wa kusini. (Zek. 14:4, 9) Hii inalingana na kuzaliwa kwa mtoto mwanamume na “mwanamke” wa kimbinguni wa Mungu, kama inavyofananishwa katika Ufunuo 12:1-5. Katika njia hii “ufalme” mpya ulizaliwa, wonyesho mpya wa enzi kuu ya Mungu kuelekea dunia yetu. Wakati huo ndipo Mungu alipomtawaza Mfalme wake Aliyewekwa ili atumie “haki” yake. Zile pingu za shaba na chuma za mfano ziliondolewa kukizunguka kile “kisiki cha shina” la enzi kuu ya Mungu kuelekea dunia yetu iliyokuwa imekatizwa. Zile “nyakati saba” zilizowekwa zilikuwa zimepita juu ya hicho kisiki cha shina.—Dan. 4:23, 26.
[Picha katika ukurasa wa 11]
Kwa kuwa warithi washirika 144,000 wanachaguliwa kati ya “kila. . . . kabila” bila shaka watapendezwa na washiriki wote wa jamaa ya kibinadamu.