Huu Ndio Wakati wa Kumkaribisha Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote
1, 2. Danieli sura ya saba, inaonyesha “mwanadamu” akipelekwa mbele ya nani, na kama akipewa nini?
MWENYE ENZI KUU YA ULIMWENGU WOTE ndiye “Mzee wa Siku,” Yehova. “Mwana wa Adamu” Yesu Kristo aliyetukuzwa ndiye aliyemwendea, katika mwaka 1914 W.K., ili apewe nafasi ya kushiriki katika “ufalme wa [ulimwengu].”
2 Nabii Danieli alitabiri (kutoa unabii) juu ya hili, aliposema: “Tazama, mmoja aliye mfano wa mwanadamu akaja pamoja na mawingu ya mbinguni akamkaribia huyo mzee wa siku, wakamleta karibu naye. Naye akapewa mamlaka na utukufu na ufalme, ili watu na kabila zote na taifa zote na lugha zote wamtumikie. Mamlaka yake ni mamlaka ya milele, ambayo haitapita kamwe na ufalme wake ni ufalme usioweza kuangamizwa.”—Dan. 7:13, 14.
3. Kulingana na Danieli 7:27, ni nani wengine wanaoletwa kwenye ufalme huo wa milele?
3 Baadaye kidogo katika huu “wakati wa mwisho,” wale wanafunzi wa Yesu Kristo 144,000 waliozaliwa kwa roho wanaletwa katika ufalme huu. Sawasawa na Danieli 7:27 lilivyotabiri: “Na ufalme, na mamlaka, na ukuu wa ufalme, chini ya mbingu zote, watapewa watu wa watakatifu wake Aliye juu; ufalme wake ni ufalme wa milele, na wote wenye mamlaka watamtumikia na kumtii.”—Dan. 12:4; Ufu. 14:1-3; 20:4, 6.
4. “Kundi kubwa” la leo ni raia za serikali gani ya kimbinguni?
4 Kwa sababu Mzee wa Siku anamchukua Mwanawe Mtiwa Mafuta Yesu ashiriki naye katika “ufalme wa [ulimwengu],” unakuwa “ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake.” (Ufu. 11:15) Katika njia hiyo wanadamu wote wanakuwa raia za kibinadamu za kidunia za Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote Yehova na za Kristo wake. Raia hao wa kidunia sasa wanatia ndani “mkutano mkubwa” unaojulishwa kwetu katika njozi katika Ufunuo 7:9-17. Njozi hii ilieleweka mara ya kwanza katika mwaka 1935 W.K.
5. Kulingana na Ufunuo 3:21, miaka 63 baada ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. Yesu alitia moyo wanafunzi wake waliozaliwa kwa roho watazamia mbele kwenye kitu gani?
5 Leo “mkutano mkubwa” wanaelewa vizuri sana kwamba “ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake” unahusu (ni wa) watu wawili mashuhuri, yaani, Bwana Yehova na Mwanawe, Kristo Yesu; tena, kwamba serikali hii ambayo wao ni raia zake, ilianza mwaka 1914 W.K., wala si wakati wa Pentekoste ya mwaka 33 W.K. Kulingana na hili, “mkutano mkubwa” unaona kwamba, miaka 63 baada ya Pentekoste, Kristo Yesu bado alikuwa akiwatia moyo wanafunzi wake waliozaliwa kwa roho wautazamie ufalme huo, akisema: “Yeye ashindaye nitampa kuketi pamoja nami katika kiti changu cha enzi, kama mimi nilivyoshinda nikaketi pamoja na Baba yangu katika kiti chake cha enzi.” (Ufu. 3:21) Walikuwa bado hawajarithi huo ufalme wa kimbinguni uliokuwa unakuja wakiwa kama “warithi wa Mungu, warithio pamoja na Kristo.” (Rum. 8:17) Yesu Kristo ndiye Mrithi mkuu wa Mungu, nao wanafunzi wake ni warithi wadogo.—Ebr. 1:1, 2.
6. Kulingana na 2 Petro 1:10, 11 Je! wanafunzi waliozaliwa kwa roho walikuwa wamekuwa katika ufalme huo au walikuwa bado kuuingia?
6 Kwa hiyo ufalme ambao wanafunzi hawa waliozaliwa kwa roho waliokuwa duniani walikuwa “warithi pamoja na Kristo” haukuwa kitu ambacho walikuwa wameingizwa ndani yake tangu kumiminwa kwa roho takatifu katika Pentekoste ya mwaka 33 W.K. Kwa sababu hiyo, mtume Petro alipokuwa akiandika barua yake ya pili karibu na mwaka 64 W.K., au miaka 30 baada ya Pentekoste, aliwapa Wakristo wenzake onyo hili: “Maana mkitenda hayo hamtajikwaa kamwe. Maana hivi mtaruzukiwa kwa ukarimu kuingia katika ufalme wa milele wa Bwana wetu, Mwokozi wetu Yesu Kristo.”—2 Pet. 1:10, 11.
7. Ni kitu gani kinachowawezesha kuingia katika ufalme huo kinachopewa kwao, na kwa hiyo ni uhusiano (hali) gani wa muda waliokuwa nao na Yesu Kristo unaokwisha?
7 Katika wakati wake Mungu, hao warithi pamoja na Kristo 144,000 wanapewa kiingilio hicho kwenye ufalme huo wa kimbinguni kwa njia ya “ufufuo wa kwanza.” Wakati huo hawatakuwa tena raia waliozaliwa kwa roho duniani chini ya “Mwana wa pendo lake [Mungu].” Hali hiyo ya muda ya kuwa raia za kidunia za Yesu Kristo aliyetukuzwa itakuwa imekwisha kabisa. Wao watakuwa wafalme wasioweza kufa, au kuona uharibifu pamoja naye. (2 Tim. 2:11, 12; Ufu. 20:4, 6) Hii ina maana kwamba hali ya muda waliyokuwa nayo wakiwa kama raia tangu wakati wa Pentekoste ya mwaka 33 W.K. walipokuwa na mwili hapa duniani itakuwa imekwisha milele. (Kol. 1:13) Kwa kuwa waliishi maisha safi na ya uaminifu walipokuwa duniani, wanarithi “ufalme wa Kristo na Mungu.”—Efe. 5:5.
8. Je! utawala wa Kristo wa miaka elfu ulianza katika mwaka wa 1914, na “ishara” iliyotabiriwa ilionyesha nini kuhusiana (kupatana) na jambo hili?
8 Utawala wa miaka 1,000 wa Yesu Kristo pamoja na warithi wake washirika 144,000 haukuanza katika mwaka 1914 wakati wa kuanzishwa kwa “ufalme wa [ulimwengu]. . . ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake.” Kile kilichoanza wakati huo kilikuwa “kuwapo,” au parousia, kwa halali kwa Yesu Kristo kwa kifalme, ambako mitume wake walikuwa wameuliza juu yake, kulingana na Mathayo 24:3 (NW). “Kuwapo” kwake akiwa katika mamlaka ya Ufalme hakukuanza wakati Mungu alipomtumia aimimine roho takatifu katika Pentekoste ya mwaka 33 W.K. (2 The. 2:2) “Ishara” iliyotabiriwa ilianza kuonekana baada tu ya Nyakati za Mataifa kumalizika katika mwaka 1914 ikionyesha kwamba Mwana wa Mungu yupo kwa kutokuonekana akiwa na mamlaka ya Ufalme, katika “ufalme wa [ulimwengu].”
9. Kwa kutokea “ishara” hizo wanafunzi wangejua ni nini kinachokaribia, na kwa sababu gani hawangekuwa na huzuni yo yote?
9 Ufalme huu umepewa mgawo wa kuiharibu taratibu hii mbovu iliyopo ya mambo. Katika unabii wa Yesu hiyo inaanzisha mambo ambayo yanafanyiza “ishara” hiyo kubwa sana, alielekeza kwenye ufalme huo ulipokuwa karibu kutimiza kazi hii ya kuharibu, aliposema kwa mitume wake hivi: “Nanyi kadhalika, mwonapo mambo hayo yanaanza kutokea, tambueni ya kwamba ufalme wa Mungu u karibu.” (Luka 21:31) Kwa kufanya kazi hii uliyogawiwa, ufalme huu utawakomboa wanafunzi waaminifu wa Kristo wanaobaki duniani kutokana na uonezi mwingine wo wote wa mataifa yasiyo ya Kiyahudi. Hii inaonyesha sababu ya Yesu kusema kwa wanafunzi wake hivi: “Mambo hayo yaanzapo kutokea, changamkeni, mkaviinue vichwa vyenu, kwa kuwa ukombozi wenu umekaribia.”—Luka 21:28.
10. “Kuokolewa” kwa mabaki ya waliozaliwa kwa roho kutatukia wakati gani, na kunatia ndani nini?
10 Mabaki ya wanafunzi wa Kristo waliozaliwa kwa roho waliopo hapa duniani walianza kuona “mambo haya” yakianza kutokea huko nyuma katika mwaka 1914 W.K. Kukombolewa kwao kutokana na taratibu mbovu iliyopo ya mambo kunafanyika wakati “jiwe” la kifalme lililochongwa kutoka mlima wa enzi kuu ya Mungu linapogonga “sanamu” ya utawala wa kisiasa wa ulimwengu duniani na kuuharibu katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” katika Har–Magedoni. (Dan. 2:44, 45; Ufu. 16:14, 16) ‘Kukombolewa’ kwao vilevile kunatia ndani kuchukuliwa baadaye kutoka duniani na kuingizwa katika “ufalme wa milele wa Bwana wetu, Mwokozi wetu Yesu Kristo,” kupitia kwa “ufufuo wa kwanza” kutoka kwa wafu. (2 Pet. 1:11; Ufu. 20:4, 6) Hii itawawezesha watawale kama wafalme pamoja na Yesu Kristo wakati wa miaka 1,000 wakati Shetani Ibilisi na mashetani wake wanapofungwa na kuzuiliwa katika shimo refu, wasiweze tena kutawala mambo ya wanadamu bila kuonekana.—Ufu. 20:1-3.
11. Ni nani wengine watakaokombolewa. lakini ni kwa sababu ya kukataa “amri” gani Mataifa hawatashiriki wokovu huo?
11 Vilevile ukombozi unakaribia kwa “mkutano mkubwa” wa watu wenye mfano wa kondoo ambao sasa wanachukua msimamo wao katika upande wa mabaki waliozaliwa kwa roho wakiukubali “ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake.” Lakini mataifa wamekataa kutii “amri” ya Ufalme ambayo wamejulishwa, kama ilivyoandikwa katika Zaburi 2:1-9: “Mbona mataifa wanafanya ghasia, [tangu 1914 W.K.], na makabila wanatafakari ubatili? Wafalme wa dunia wanajipanga, na Wakuu wanafanya shauri moja, juu ya [Yehova], na juu ya masihi [Kristo] wake, . . . Nitaihubiri amri; [Yehova] aliniambia [mimi Kristo], ndiwe mwanangu, mimi leo nimekuzaa. Uniombe, nami nitakupa mataifa kuwa urithi wako, na miisho ya dunia kuwa milki yako. Utawaponda kwa fimbo ya chuma, na kuwavunja kama chombo cha mfinyanzi.”—Ufu 7:9, 10; 11:15.
KUTOKUWAMO KUNAKOSHIKAMANA NA KUUHUBIRI UFALME
12. Ingawa majira ya Mataifa yalikwisha mwaka Mashahidi wa Yehova wanachukua msimamo gani kuelekea siasa za ulimwengu?
12 Tangu 1914, “ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake” umekuwa na haki ya kuingilia mataifa. Je! hii ina maana kwamba sasa mashahidi wa Yehova wa Kikristo wana haki ya kujiingiza katika siasa za ulimwengu? Je! wao wanaweza kuunga mkono chama cha siasa cha upande huu au upande huu kama wanavyofanya Wakatoliki na Waprotestanti, hata kufanya mipango ya kufitini serikali za kisiasa zilizosimamishwa au kuchochea mapinduzi? Hata kidogo! Bila kukubaliana wao wamemwiga Mwana-Kondoo, Yesu Kristo, kwa kutokuwa “wa ulimwengu.” Wao wanashikamana kabisa na ufalme uliozaliwa huko mbinguni katika mwaka 1914. (Yohana 17:14, 16; Ufu. 12:1-12) Hata ingawa wanateswa vikali kwa sababu ya kutokuwamo kwao kwa Kikristo kuelekea mashindano ya ulimwengu, wao wanaendelea kutimiza unabii wa Kiongozi wao wa kimbinguni, Yesu Kristo, aliposema hivi: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mt. 24:14, NW; Marko 13:10.
13. Hivyo sababu gani mwisho wa Majira ya Mataifa, na mwanzo wa mileani (miaka elfu) ya utawala wa Kristo havikutukia wakati mmoja?
13 Ushuhuda huu wa Ufalme lazima utolewe kabla (mbele) ya taratibu hii ya mambo kwisha na kuanza kwa utawala wa Kristo wa miaka elfu. Kwa hiyo, kuanza kwa ufalme wa Mungu huko mbinguni katika mwaka 1914 hakukumaanisha mwanzo wa utawala wa miaka elfu wa Kristo. Kulingana na unabii wa Biblia, mambo mengi yangetendeka kabla ya taratibu hii ya mambo kwisha, ili kuupa nafasi utawala wa miaka elfu wa Kristo pamoja na wanafunzi wake 144,000 waliozaliwa kwa roho.—Ufu. 20:4, 6.
14. Shetani ameazimia kutimiza jambo gani kuelekea mataifa kabla ya kufungiwa shimoni refu, na kwa sababu gani?
14 Shetani Ibilisi ameazimia kwamba, kabla yeye na mashetani wake hawajatupwa katika lile shimo refu kwa miaka elfu, yeye ataangamiza mataifa yote kwa njia hiyo awazuie wasiwe raia za Kristo wakati wa utawala Wake wa miaka elfu. Kwa kusudi hilo yeye anawaongoza mataifa yote ya ulimwengu kwenye uwanja wa vita ya Har–Magedoni, ili wapigane na Yehova Mungu na Kristo wake. (Ufu. 16:13-16) Kwa hiyo Shetani Ibilisi ndiye atakayelaumiwa kwa sababu ya “ole” wa milele utakaowapata Mataifa katika Har–Magedoni, (Ufu. 12:12; 19:11-21) Tunawezaje kuepuka tusife pamoja nao katika uharibifu huo wenye ole?
15. Kwa kukataa kuenda pamoja na mataifa chini ya uongozi wa Shetani, ni mambo gani yamewapata Mashahidi wa Yehova, na kwa sababu gani?
15 Inatupasa tukatae kuambatana pamoja na Mataifa kuelekea vita vya kupigana na Yehova Mungu Mwenye Nguvu Zote katika Har–Magedoni. Mwenendo huo umeletea Mashahidi wa Kikristo wa Yehova shida kubwa. Sana sana tangu kufukuzwa kwa Shetani Ibilisi pamoja na malaika zake za kishetani kutoka mbinguni, mabaki wanaotazamia kuja kuwa warithi pamoja na Kristo ndio wamekuwa lengo la hasira ya Shetani Ibilisi. (Ufu. 12:13-17) Shabaha yake ni kuvunja ukamilifu wao kwa Mungu. Katika njia hiyo awafanye wasistahili kutawala kama wafalme pamoja na Kristo wakati wa karne kumi, wakati yeye na malaika zake za kishetani watakapofungwa katika shimo refu. Shetani Ibilisi anakusudia kumzuia Kristo asiwe na hesabu kamili ya washiriki 144,000 katika serikali yake ya ulimwengu wote ya kimbinguni. Je! Shetani Ibilisi atafaulu katika hili? Hapana!
16. Mileani (miaka elfu) isiyokuwa na mashetani itakujaje, na serikali ya Mungu ya ulimwenguni pote kupitia kwa Kristo itatawala kama wonyesho wa nini?
16 Kama vile nyungunyungu (mdudu) asivyoweza kuzuia gari la tingatinga lisimkanyage, ndivyo Shetani na mataifa yote ya kidunia ambayo yeye ndiye mtawala wao asivyoweza kufaulu kuharibu na kuzuia serikali ya Mungu ya ulimwengu wote inayokuja! Kama alivyoona uchungu wa kushindwa kwake katika vita ya kwanza mbinguni, Shetani ataona mataifa yake yaliyopotezwa yakishindwa katika Har–Magedoni. Atamwona Kristo akitumia ‘fimbo yake ya chuma’ bila kupingwa na kuyavunja-vunja mataifa yote yaliyokusanyika kana kwamba ni vyombo vya udongo vinavyofinyagwa na mfinyanzi. (Zab. 2:8, 9; Ufu. 12:5) Ndipo Shetani na mashetani wake watakapokamatwa na Kristo mshindi wafungwe minyororo na kuvurumishwa katika shimo refu la gereza. Hili litafungwa kikiki sana kwa muhuri kwa muda wa miaka elfu. Wakati wa miaka hiyo elfu isiyo na mashetani, serikali ya Mungu ya ulimwengu wote kupitia kwa Kristo itatawala kwa wonyesho wa enzi yake kuu ya ulimwengu wote.—Ufu. 20:1-6.
MKARIBISHENI “MFALME WA UTUKUFU”!
17. Ili kuonyesha imani yetu katika uhakika wa serikali ya ulimwengu wote, tunapaswa kufanya nini sasa, kwa kuiga nani?
17 Serikali ya kimungu ya ulimwengu wote ya kufariji na kubariki wanadamu wanaoonewa na kufa ni ya lazima. Je! twaamini uhakika huo? Kuamini kwetu uhakika huo wenye utukufu kwataka tufanye jambo fulani sasa! Tufanye nini? Tufanye kama “mkutano mkubwa” wa watu waliojiweka wakf na kubatizwa unavyofanya, ulioanza miaka ishirini (20) baada ya kuzaliwa kwa ufalme wa Mungu mwaka 1914. Wao wanaushangilia “ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake” kuwa tumaini peke yake la kupatia wokovu wa milele! Kulingana na unabii wa Ufunuo 7:9-17 “mkutano mkubwa” huo unasafisha maisha zao na kumtumikia Yehova Mungu katika hekalu lake la kiroho sasa! Ikiwa tunafuata mwendo uo huo, itaonyesha kwamba tuko upande wa ushindi wakati wa “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” katika Har–Magedoni. (Ufu. 16:14, 16; 19:11-21) Ndipo njia itafunguliwa mbele yetu kuingia katika paradiso ya kidunia chini ya serikali iliyo bora kuliko nyingine yo yote ambayo wanadamu wamepata kuwa nayo. Kupenda kwetu mema kwatuhimiza tuwe tumekwisha kuwa tayari ufalme huo ufikapo!
18. Sasa Mungu Bwana Mwenye Enzi Kuu analeta nini, na kwa hiyo ni nini tunachopaswa kukubali kwamba ni mali yake?
18 Tazameni, sasa, kwa macho ya imani, maandamano yenye ushindi ya Bwana Mwenye Enzi Kuu wa viumbe vyote! Aja pamoja na serikali ya ulimwengu wote kupitia kwa Kristo azibariki jamaa zote za dunia, walio hai na waliokufa. Na tuikubali enzi yake kuu ya halali tuseme, kwa maneno ya Zaburi 24:1, 2: “[Dunia] na vyote viijazavyo ni mali ya [Yehova], [nchi inayozaa] na wote wakaao ndani yake. Maana ameiweka misingi yake juu ya bahari, na juu ya mito ya maji aliithibitisha.” Hili latupa uhakikisho wa kwamba maji yaliyo chini ya nchi hayataumuka kamwe yaigharikishe dunia kama mafuriko na ya kwamba zile bahari saba zimewekewa makomeo na Muumba.
19, 20. Kulingana na Zaburi ya 24 sasa tuna sababu ya kuwa kama raia za Yerusalemu wa kale wakati wa tukio gani?
19 Sasa tuna sababu ya kuwa kama wenyeji wa Yerusalemu wa kale katika mwaka wa 1070 K.W.K. Ni wakati Mfalme Daudi alipoagiza lile sanduku la agano lipelekwe na makuhani Walawi kwenye malango ya mji. Wakati mji wenye shangwe ulipoyatazama maandamano yakikaribia yakiwa na mfano wa kuwapo kwa Mungu, walisikia kelele hii:
20 “Inueni vichwa vyenu, enyi malango, inukeni, enyi malango ya milele, Mfalme wa utukufu apate kuingia.”
21. (a) Ni kwa sababu gani malango ya zamani ya Yerusalemu walipaswa kujiinua? (b) Ni kwa sababu gani basi ilifaa kutangaza kwamba Yehova alikuwa “hodari wa vita”?
21 Ili jina la Mfalme huyu mashuhuri litangazwe pote, walinzi walio malangoni waitikia hivi: “Ni nani Mfalme wa utukufu?” Mara bila haya jibu linatoka kwa kuhani, likisema: “[Yehova] mwenye nguvu, hodari, [Yehova] hodari wa vita.” (Zab. 24:7, 8) Kumbe, si mtu tu anayetaka kuingia katika mji wa kifalme. Ni mtu aliye Mashuhuri kuliko wote katika ulimwengu wote, yaani, Yehova “Mfalme wa utukufu.” Kwa sababu hiyo malango na njia za milele au za kale za kuingilia zaonekana kuwa chini mno. Kwa hiyo zimepaswa zijiinue ili mfalme aliye mashuhuri mno apate kupita. Yeye alikuwa mashuhuri kuliko Mfalme Daudi, aliyeketi katika “kiti cha enzi cha [Yehova]” katika Yerusalemu. (1 Nya. 29:23) Labda wafalme wengine nyakati za zamani walipitia malango ya zamani ya mji huo, lakini hakuna mmoja kati yao aliyekuwa mtukufu wala hodari kama Yehova, Mungu Aliye Juu Kuliko Wote. Ndiye aliyepigana akampa Mfalme Daudi ushindi juu ya wakaaji wa kale wa kipagani wa mji huo, yaani, Wayebusi. Ndiye aliyempa Mfalme Daudi ushindi juu ya Wafilisti walipojaribu mara mbili kutaka kumwondoa Daudi katika kiti chake cha enzi katika mji mpya uliotekwa nyara wa Yerusalemu.—2 Sam. 5:4-25.
22. “[Yehova] wa majeshi” alifananishwaje wakati huo, wakati huo alikuwa akikaribia malango ya Yerusalemu akiwa katika ziara ya namna gani?
22 Kama alivyofananishwa na sanduku lake la agano, Mfalme huyu Shujaa wa Vita alikaribia Yerusalemu mwaka wa 1070 K.W.K. akiwa katika shughuli (kazi) ya amani. Tena kelele ya kuheshimu ukuu wake inazuka kutoka kwa waandamanaji wanaokuja, ikisema: “Inueni vichwa vyenu, enyi malango, naam, viinueni, enyi malango ya milele Mfalme wa utukufu apate kuingia.” Tena swali (ulizo) laulizwa hivi: “Ni nani huyu Mfalme wa utukufu?” Jibu lenye kutumainisha larudi likisema: “[Yehova] wa majeshi, yeye ndiye Mfalme wa utukufu.”—Zab. 24:9, 10.
23. (a) Ni kwa sababu gani Yehova wa majeshi amekuwa “Mfalme wa utukufu” sana sana kuanzia 1914? (b) Ni nini atakachoendeleza katika Har–Magedoni na baada ya hapo atawatendeaje wanadamu?
23 Leo, mwaka huu wa 1978 W.K., “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” katika Har–Magedoni yakaribia. Sasa, muda mrefu baada ya Nyakati za Mataifa kumalizika katika mwaka 1914, “[Yehova] wa majeshi” sana sana ndiye “Mfalme wa utukufu.” Kwa sababu gani hivyo? Kwa sababu, kama ilivyotabiri Zaburi 47:8, NW, “Mungu amekuwa mfalme juu ya mataifa,” anatenda tena kama Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote kuelekea dunia yetu. Ataonyesha ukuu wake zaidi kwa kuuendeleza “ufalme wa [ulimwengu]. . . ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake” katika Har–Magedoni. (Ufu. 11:15-18) Kristo wa Yehova, Mwanawe aliye mkuu kuliko Mfalme Daudi, ndiye Aliyemweka katika kiti chake cha enzi amwakilishe katika serikali ya ulimwengu. Kwanza, Yehova wa majeshi, akiambatana na Mwanawe Yesu Kristo na majeshi ya malaika ya mbinguni atauondolea ulimwengu wote taratibu mbovu ya mambo ya leo. Ndipo atakapowabariki wanadamu kwa utawala wenye haki kupitia kwa Mwanawe, Yesu Kristo. Taraja hili zuri sana lakaribia kutimizwa!
24. Kwa hiyo basi huyu Yehova wa majeshi anastahili kitu gani kutoka kwetu?
24 Je! huyu “Mfalme wa utukufu,” Yehova wa majeshi hastahili tumkaribishe kwa moyo wote? Bila shaka, Ndiyo! Basi, Karibu Ee Mfalme wetu mtukufu!
—Kutoka The Watchtower Mar. 1, 1978.