Serikali Yetu ya Ulimwengu Wote Inayokuja—Ufalme wa Mungu
“Mwimbieni Mungu, naam imbeni, Mwimbieni Mfalme wetu, naam, imbeni. Maana Mungu ndiye Mfalme wa dunia yote.”—Zab. 47:6, 7.
1. Kwa sababu gani tunasema juu yake kama “serikali yetu inayokuja ya ulimwenguni pote”?
NI SERIKALI yetu sisi duniani! Serikali hii ya ulimwengu wote tunayosema, inafaa sana mahitaji yetu ya lazima. Iko karibu kuchukua mamlaka juu ya mambo yetu yote. Ndiyo sababu tunaitaja kuwa “serikali yetu ya ulimwengu wote inayokuja.”
2. Namna gani juu ya uwezo wa kutawala wa Yeye anayetoa serikali hii ya ulimwenguni pote?
2 Inatokana na chanzo kilicho juu na kikubwa kuliko sisi viumbe vinyonge vya kibinadamu, sisi tulioshindwa kabisa kuongoza mambo yetu duniani. Inatokana na Yeye anayejua jinsi ya kuongoza, si dunia yetu hii iliyo ndogo sana tu, bali vilevile ulimwengu mzima. Inatokana na Mungu Muumba wa vitu vyote. Serikali hiyo ya ulimwengu wote ni ufalme Wake ambao Yeye aliahidi zamani sana yapita miaka elfu sita. Kwa sababu ya haya yote, je! haitupasi tufurahie na tumshangilie? Inatupasa!
3. Ufalme wake ukiwa serikali ya ulimwenguni pote, Mungu atakuwa mfalme juu ya nini na juu ya nani?
3 Kwa kuwa ni serikali ya ulimwengu wote, ufalme wa Mungu hautakuwa wa taifa moja tu hapa duniani. Hapo kale, tangu masika ya mwaka 1513 kabla ya Wakati wetu wa Kawaida mpaka masika ya mwaka 33 W. K., Mungu alikuwa ndiye Mfalme wa taifa moja tu la Israeli. (Zab. 147:19, 20) Lakini sasa Yeye anatoa ahadi yake mwenyewe isiyoshindwa kwamba yeye atakuwa Mfalme juu ya dunia yote. Hii ina maana kwamba atatawala juu ya watu wa mataifa yote. Ndiyo sababu, kupitia kwa mmoja wa manabii wake mashuhuri, Isaya, yeye alisema maneno haya yenye kutia moyo mataifa yote: “Nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala kwa mataifa yote.”—Isa. 56:7.
4. Ni unabii gani wa maana kwetu sote uliotolewa na Mungu katika Edeni, na alikuwa akifikiria serikali gani?
4 Walakini, maelfu ya miaka iliyotangulia, zamani sana katika Bustani ya Edeni, Mungu alitoa unabii wenye maana kwetu sote. Wakati huo Mungu alimwambia Mshawishi mkuu wa wanadamu wote hivi: “Nami nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako na uzao wake; huo [uzao wa mwanamke] utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino.” (Mwa. 3:15) Maneno hayo ya unabii yalionyesha kwamba, kama vile wazao wote wa watu wawili wa kwanza walivyoumizwa na tendo la udanganyifu la huyo Mshawishi mkuu, ndivyo wote wangefaidika kutokana na kupondwa kichwa chake na “uzao” wenye kushinda wa “mwanamke” wa Mungu. Kwa hiyo jambo hili latupasa sisi leo, sivyo? Ndivyo! Na Mungu aliposema habari za Mponda kichwa cha yule Adui, alikuwa akisema habari za serikali ambayo angesimamisha juu ya wanadamu wote. Ilipaswa iwe serikali ya Mungu inayoongozwa na Mungu, serikali ya watu wote. Jambo hili limepaswa litufurahishe sote.
5. Wimbo ulioimbwa na Musa ukatumiwa na Paulo ulionyeshaje kwamba kusudi la wakati ujao la Mungu lilitia ndani wengi zaidi ya Israeli peke yao?
5 Serikali ya Mungu juu ya taifa la Israeli, yeye mwenyewe akiwa Mfalme wa mbinguni asiyeonakana, ilikuwa ya muda mfupi tu. Lakini kusudi lake la upendo juu ya wakati ujao lilipasa mataifa mengi zaidi ya taifa hilo dogo tu. Huko Mlima Sinai wa Manga, katika mwaka wa arobaini (40) tangu Mungu alipoanza kuwa Mfalme wa taifa la Israeli, nabii Musa aliimba wimbo wa unabii masikioni mwa Waisraeli, na katika upeo wa wimbo huo alisema hivi: “Furahini, enyi mataifa, pamoja na watu wake; kwa maana atatwaa kisasi kwa damu ya watumwa wake . . . tena atafanya kafara kwa nchi yake, na watu wake.” (Kum. 32:43) Ilipopita miaka 1,528, mwanamume aliyeongozwa na Mungu, aliyekuwa mtume wa “habari njema” kwa mataifa wasio Waisraeli alitumia maneno hayo ya Musa akayatia katika barua yake aliyoandikia waamini Wakristo wa Kirumi, akasema: “Kristo amefanyika mhudumu wa agano la kutahiriwa [Waisraeli] kwa ajili ya kweli ya Mungu, kusudi azithibitishe ahadi walizopewa baba zetu; tena ili Mataifa wamtukuze Mungu kwa ajili ya rehema zake . . . Na tena anena, Furahini, Mataifa, pamoja na watu wake.”-—Rum. 15:8-10.
6-8. (a) Paulo anaonyeshaje kwamba Mungu alifikiria mataifa yote katika kuwahesabia wanadamu haki kwa imani? (b) Kwa hiyo ni serikali ya namna gani inayokusudiwa na Mungu?
6 Mwandikaji huyo aliyetumia maneno hayo ya Musa alikuwa mtume Paulo. Wakati huo mtume huyu alikuwa mmisionari aliyekuwa na kusudi la kufika mwishowe Rumi na kupanga kwenda hata Spania. Alijua jambo ambalo Mungu alikuwa akifanya wakati huo, si kwa ajili ya Wayahudi wo wote waliozikubali “habari njema” peke yao, zaidi sana, kwa ajili ya Mataifa wasiotahiriwa, wanaoziamini “habari njema.” Alijua kwamba Mungu alikuwa akifikiria mataifa yote. Hivyo mtume Paulo akiandikia kundi katika Rumi uliokuwa na washiriki Wakristo wa Kiyahudi na wa Mataifa wasio Wayahudi, alisema hivi:
7 “Je! Mungu ni Mungu wa Wayahudi tu? Siye [Mungu] wa Mataifa pia? Naam, ni Mungu wa Mataifa pia; kama kwa kweli Mungu ni mmoja, atakayewahesabia haki wale waliotahiriwa katika imani, nao wale wasiotahiriwa atawahesabia haki kwa njia ya imani iyo hiyo.”—Rum. 3:29, 30.
8 Basi, Mungu anakusudia wakati wetu kuweko, si serikali ya taifa moja, bali serikali ya ulimwengu wote ya watu wa mataifa yote.
“UFALME WA MWANA WA PENDO LAKE”
9. Kwa sababu gani Israeli wa asili hawana dai lolote la pendeleo lililorithiwa la kusimamisha serikali ya ulimwenguni pote iliyoahidiwa?
9 Leo watu wanaoijua nia ya Mungu hawategemei taifa wala kikundi cho chote cha mataifa, wala hata Umoja wa Mataifa ulio na wanachama sasa 149, kusimamisha serikali ya ulimwengu wote inayohitajiwa sana ili izibariki jamaa zote za dunia. Wanajua kwamba Jamhuri ya Israeli haina haki zo zote ilizorithi ambazo inaweza kujidai kusimamisha serikali ya ulimwengu wote ya kubariki jamaa zote za dunia. Mambo ya hakika yaonyesha kwamba ufalme wa Mungu uliokuwa juu yao ulikoma katika karne ya kwanza W. K. Kwa furaha, wakati huo Mungu alichukua hatua kwa ajili ya serikali ya ulimwengu wote: Alisimamisha ufalme wa kiroho. Kwa vile mapendeleo ya ufalme wa Mungu yaliondolewa kwa taifa la Israeli, ufalme huo ulisimamishwa juu ya nani? Ni nani walio raia za ufalme huo wa kiroho duniani leo?
10. Katika Wakolosai 1:13, Paulo anauitaje ufalme huo nao ulianza wakati gani?
10 Ufalme huo ulianza wakati wa karne ya kwanza W. K. Mtume Paulo avuta fikira kwenye ufalme huo katika barua yake aliyoandikia kundi la Kikristo katika mji wa Kolosai, Asia Ndogo (sasa ni Uturuki), akasema hivi: “Mkimshukuru Baba, aliyewastahilisha kupokea sehemu ya urithi wa watakatifu katika nuru. Naye alituokoa katika nguvu za giza, akatuhamisha na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wa pendo lake; ambaye katika yeye tuna ukombozi, yaani, msamaha wa dhambi.” (Kol. 1:12-14) Ili waamini wapate kufurahia maono hayo mema wakati huo wa karne ya kwanza, Mungu alianza kuwastahilisha kwa kufanya mpango wa kusamehe dhambi zao ijapokuwa walikuwa watu wa kutoka kwa Mataifa.
11. Kuokolewa kwa Wakristo hao wa Kolosai na Mungu kutoka katika “nguvu za giza” kulimaanisha nini kwao?
11 Mungu alistahilisha waamini hao Wakolosai wapate kushiriki urithi wa pekee pamoja na watu watakatifu waliokuwa katika nuru. Hawa walikuwa wamekuwa chini ya “mamlaka ya giza” au chini ya mamlaka ya yote yaliyofananishwa na giza, kama vile kutokumjua Mungu au kuwa mbali naye na utawala wake. Basi, Mungu alipostahilisha waamini hao ili washiriki maisha yenye mwangaza zaidi, ‘aliwaokoa katika nguvu za giza.’ Kwa njia hiyo wakawa watu walio na nuru kuliko wote duniani, maana sasa wametiwa nuru na Mungu. Hawakuwa tena chini ya “wakuu wa giza hili, . . . majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho.” (Efe. 6:12) Mungu alikuwa ameingilia jambo hili ili “[awafumbue] macho yao, na kuwageuza waiache giza na kuielekea nuru, waziache na nguvu za Shetani na kumwelekea Mungu.”—Matendo, 26:18.
12. Paulo anasema hali ya kutiwa nuru kwa waamini wa karne wa kwanza kuliunganishwa na nini?
12 Katika njia hii waamini wa “habari njema” wa karne ya kwanza waliingizwa katika makao ya nuru. Lakini hali yao iliyotiwa nuru ilihusiana na nini? Ilihusiana na serikali. Kwa sababu, Mungu ‘alipowaokoa katika nguvu za giza,’ “[aliwaingiza pia] katika ufalme wa Mwana wa pendo lake.” (Kol. 1:13) Mwana huyu ni Yesu Kristo.
13. Wakristo Wakolosai na vilevile na maadui wao walielewa cheo rasmi cha Kristo kuwa nini wakati huo?
13 Mtume Paulo alipoandika barua yake kwa kundi la Kikristo katika Kolosai, Yesu Kristo alisemekana kuwa mfalme na kuwa amekwisha kuwa na ufalme. Hivi ndivyo kundi lililotiwa nuru katika Kolosai lilivyofahamu jambo hili. Hivi ndivyo hata adui zao walivyofahamu mambo haya. Kwa mfano, wale wafanya ghasia waliwashtaki Wakristo katika mji wa Thesalonike juu ya nini? Ili wawachochee wakuu wa mji juu ya Wakristo, wafanya ghasia hao walisema hivi: “Watu hawa [yaani, mtume Paulo na wamisionari wenzake] walioupindua ulimwengu wamefika huku nako, . . . na hawa wote wanatenda mambo yaliyo kinyume cha amri za Kaisari, wakisema na kwamba yupo mfalme mwingine, aitwaye Yesu.”—Matendo 17:6, 7.
14. Paulo alilinganishaje Makaisari wakubwa na watawala wengine wa siku zake na Yesu Kristo aliyetukuzwa?
14 Alipokuwa akionyesha tofauti kati ya Yesu Kristo aliyetukuzwa na Makaisari wanaomiliki na watawala wengine wa siasa duniani, mtume Paulo alisema habari za Mtawala asiyeweza kufa, yaani, Yesu Kristo, kuwa “Mfalme wa wafalme [wanaokufa], Bwana wa mabwana [wanaokufa]: ambaye yeye peke yake hapatikani na mauti, amekaa katika nuru isiyoweza kukaribiwa.” (1 Tim. 6:15, 16) Zaidi ya hayo, mtume Paulo anamlinganisha Mwana huyu asiyeweza kufa wa Mungu, yaani, Yesu Kristo, na Mfalme Melkizedeki wa karne ya ishirini kabla ya Wakati wetu wa Kawaida na kusema hivi: “Melkizedeki huyo, mfalme wa Salemu, kuhani wa Mungu aliye juu, aliyekutana na Ibrahimu alipokuwa akirudi katika kuwapiga hao wafalme, akambariki . . . tafsiri ya jina lake kwanza ni mfalme wa haki, tena, mfalme wa Salemu, maana yake, mfalme wa amani; . . . amefananishwa na Mwana wa Mungu; . . . Tena hayo tusemayo ni dhahiri sana zaidi, ikiwa ametokea kuhani mwingine mithili ya Melkizedeki; . . . maana ameshuhudiwa kwamba, Wewe u kuhani milele kwa mfano wa Melkizedeki.”—Ebr. 7:1-3, 15-17; Zab. 110:1-4.
15. Yesu Kristo alifanywa Mfalme-Kuhani kama Melkizedeki wakati gani?
15 Lakini ni wakati gani Mwana huyu wa Mungu, yaani, Yesu Kristo, alipofanywa kuwa Mfalme-Kuhani kwa mfano wa Melkizedeki. Ilikuwa siku arobaini alipokwisha kufufuliwa kutoka kwa wafu, alipopaa mbinguni akaonekane mbele za Mungu akiwa na thamani ya dhabihu yake kamilifu ya kibinadamu kwa ajili ya waliokombolewa watakaofanywa kuwa raia zake wakati ujao.
16. Kwa Sababu gani kufikia hapa watu wengine wanaweza kuwa na maulizo juu ya kutawala kwa Kristo?
16 Inaposemwa hivyo, huenda watu wengine wakatatizwa kidogo wakasema hivi, Mbona mimi nimefahamu kwamba Yesu Kristo amekuwa akitawala mbinguni tangu mwisho wa Nyakati za Mataifa mwaka 1914, ingeweza kuwaje kwamba amekuwa akitawala tangu mwaka ule alipopaa mbinguni, yaani, mwaka 33.W. K.? (Ebr. 9:24; 10:12, 13; Matendo 1:1-11; 2:22-36) Amekuwa Mfalme wakati wote huu kwa njia gani, tena amekuwa akitawala juu ya nani?
UFALME WA KIROHO JUU YA ISRAELI WA KIROHO
17. Ni juu ya nini Kristo hakuanza kutawala huko nyuma mwaka wa 33 W.K.?
17 Basi, Yesu Kristo aliyetukuzwa hakuanza kutawala ulimwengu wakati huo katika mwaka 33 W. K. Hakuanza wakati huo kutawala Mataifa yasiyo ya Kiyahudi, maana Majira ya Mataifa au “nyakati zilizowekwa za mataifa” hazikumalizika mpaka mwaka wa 1914 W. K.—Luka 21:24.
18. Ijapokuwa Kristo alianza kutawala wakati huo, ni kwa sababu gani haikuwa juu ya “dunia”?
18 Wakati wa Pentekoste ya mwaka 33 W. K., wakati wa kumiminwa kwa roho ya Mungu, taifa jipya lilitokea, Israeli wa kiroho. (Gal. 6:15, 16; 1 Pet. 2:9, 10) Kwa hiyo, Yesu Kristo aliyetukuzwa alianza wakati huo kutawala juu ya Israeli wa kiroho, juu ya wale ambao Mungu alikuwa ‘amewahamisha na kuwaingiza katika ufalme wa Mwana wa pendo lake.’ (Kol. 1:13) Maneno haya ya Yesu Kristo yanatumika kwa kundi hili la Israeli wa kiroho: “Wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu.” (Yohana 17:14) Tangu alipoanza kutawala juu ya wale ambao “si wa ulimwengu,” hakuwa akitawala ulimwengu wakati huo. Alikuwa akitawala juu ya kitu kilicho tofauti na ulimwengu. Raia zake walikuwa katika ulimwengu lakini “si wa ulimwengu.”
19. Kwa hiyo ni ufalme wa namna gani uliokuwa “ufalme wa Mwana wa pendo lake [Mungu],” na ni nani waliokuwa raia zake?
19 Yesu Kristo hajapata kuwa mfalme wa kidunia wa kibinadamu. Yeye ni Mfalme wa mbinguni wa kiroho. (Yohana 18:36) Kulingana na Waebrania 4:14 “yeye aliingia katika mbingu.” Na kulingana na 1 Petro 3:22 yeye “yupo mkono wa kuume wa Mungu, amekwenda zake mbinguni, malaika na enzi na nguvu zikiisha kutiishwa chini yake.” Hii inatia ndani Israeli wa kiroho duniani. Kwa hiyo tangu sikukuu ya Pentekoste ya mwaka 33 W.K. ufalme wa Kristo umekuwa ufalme wa kiroho. Makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yanayosadiki vitu vinavyoonekana, na yanayojiingiza katika siasa za ulimwengu huu, hayakuwa sehemu ya “ufalme wa Mwana wa pendo [la Mungu].” Ni rafiki za ulimwengu huu.—Yak. 4:4.
20. Kwa sababu ya uhusiano (urafiki) wa kipekee na raia zake Mungu, ufalme wa Kristo ulipaswa uwe wa namna gani?
20 Tangu mwanzo, ufalme wa Kristo ulikuwa wa aina ya kiroho kwa vile ulivyokuwa juu ya Wakristo waliojiweka wakf na kubatizwa, ambao wamezaliwa kwa roho ya Mungu wawe wana wa kiroho wa Mungu. Kama Yesu alivyomwambia mkuu wa Kiyahudi, yaani, Nikodemo: “Mtu asipozaliwa mara ya pili, hawezi kuuona ufalme wa Mungu . . . Mtu asipozaliwa kwa maji na kwa Roho, hawezi kuuingia ufalme wa Mungu. Kilichozaliwa kwa mwili ni mwili; na kilichozaliwa kwa Roho ni roho.”—Yohana 3:3, 5, 6.
21. Kwa sababu gani ufalme wa Kristo wakati huo haukuwa serikali ya ulimwenguni pote?
21 Kulingana na Yohana 1:12, 13, juu ya wale waliomkubali Yesu kama Masihi, “Aliwapa uwezo wa kufanyika watoto wa Mungu, ndio wale waliaminio jina lake; waliozaliwa, si kwa damu, wala si kwa mapenzi ya mwili, wala si kwa mapenzi ya mtu, bali kwa Mungu.” Kwa sababu hii, baada ya kumiminwa kwa roho takatifu juu ya kundi katika Yerusalemu siku ya Pentekoste ya mwaka 33 W. K., Kristo alianza kutawala juu ya jamii ya waliozaliwa kwa roho, juu ya Israeli wa kiroho. (Rum. 2:29) Haikuwa serikali ya ulimwengu wote juu ya mataifa ya kidunia.
22. Ni kulingana na tangazo gani lililofanywa wakati wa Mungu ulipofika Kristo alipaswa kushiriki katika serikali ya ulimwenguni pote?
22 Basi, je! “Mwana wa pendo lake [Mungu]” atakuwa Mfalme juu ya kundi la wanafunzi waliozaliwa kwa roho tu? Ili ulimwengu wa wanadamu uwe raia za Yesu Kristo kama Mfalme, je! itawapasa wote wawe waliozaliwa kwa roho, ‘wazaliwe mara ya pili,’ wawe wana wa kiroho wa Mungu? Je! hivyo ndivyo inavyotokea serikali ya ulimwengu wote juu ya wanadamu wote kwa ulimwengu wote kugeuzwa kuwa Wakristo kabla ya utawala wa miaka elfu wa Kristo? Sivyo! Hata hivyo, Yesu Kristo atashiriki katika serikali ya ulimwengu wote juu ya wanadamu. Unabii katika Ufunuo 11:15, unatangazwa mbinguni ufikapo wakati wa Bwana Mungu hivi: “Ufalme wa [ulimwengu] umekwisha kuwa ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake, naye atamiliki hata milele na milele.”
23. Kwa sababu gani Mungu anamtambua Yesu Kristo kuwa anastahili kushiriki katika serikali ya ulimwenguni pote?
23 Tangazo hilo linatangaza serikali ya ulimwengu! Basi, Yesu Kristo atashirikije katika serikali hiyo ya ulimwengu? Bwana Mungu anamkubali Yesu Kristo Mwana wake kuwa na haki ya ufalme huo wa ulimwengu wote. Kwa sababu gani hivyo? Kwa sababu Mungu alimtoa Mwanawe afie jamii yote ya wanadamu, naye Mwana huyu akafa kama dhabihu kamilifu ya kibinadamu na kwa njia hiyo akaikomboa jamaa nzima ya kibinadamu. Kama Waebrania 2:9 isemavyo: “Ili kwa neema ya Mungu aionje mauti kwa ajili ya kila mtu.” Tena, 1 Timotheo 2:5, 6 humwita “Mwanadamu Kristo Yesu; ambaye alijitoa mwenyewe kuwa ukombozi kwa ajili ya wote.”
24. Mungu aliweka wakati gani wa kumpa Mwanawe nafasi ya kushiriki katika serikali ya ulimwenguni pote?
24 Walakini, Mungu ameweka wakati wa kumpa Yesu Kristo Mwanawe aliyejitoa kuwa dhabihu ufalme wa ulimwengu wote. Wakati gani? Mwishoni mwa Nyakati za Mataifa. Wakati huo uliowekwa, ilipaswa imalizike ruhusa ya Mungu kwa Mataifa (kutia na wafalme wa Jumuiya ya Wakristo) kuitawala dunia nzima bila kuzuiwa na ufalme wa Mungu.—Luka 21:24; Ebr. 10:12, 13.
25. Karne zilizokuwa katikati zilimruhusu Mungu afanye jambo gani la maana linalofungamana na serikali ya ulimwengu inayokuja?
25 Karne zote za muda wa katikati zimempa Mungu nafasi ya kuendelea na jambo fulani lenye uhusiano mkubwa zaidi na serikali yetu ya ulimwengu wote inayokuja. Limekuwa jambo gani hilo? Ni kuhamishwa kwa wanafunzi zaidi waliokubaliwa wa Yesu Kristo na kuwaingiza katika “ufalme wa Mwana wa pendo lake” wa kiroho. (Kol. 1:13) Amefanya hivi kulingana na mapenzi yake mwenyewe ya kimungu kwa kuwazaa kwa roho yake. (Yak. 1:18) Kusudi lake ni kuwachukua wale 144,000 kutoka miongoni mwa wanadamu na kuwahamisha kuwaingiza katika Ufalme wa kiroho wa Mwana wake. Inawapasa hawa 144,000 wawe watu watakaoendelea kuwa waaminifu katika ufalme huo ijapokuwa majaribu yote, shida na mateso katika ulimwengu huu. Inawapasa wawe wanafunzi waliozaliwa kwa roho wanaoendelea kuwa ‘waaminifu hata kufa.’—Ufu. 2:10; 7:4-8; 14:1-3.
[Picha katika ukurasa wa 8]
Wakristo wa karne ya kwanza waliutambua ufalme wa Kristo juu yao wakiwa kama Israeli wa Kiroho.