Je! Wewe U Raia Mshikamanifu wa Serikali ya Mungu?
1. Unafikiri kila mtu angependa kuwe na serikali ya namna gani?
IKIWA kungekuwako taifa fulani duniani leo ambalo lingeweza kuondolea kabisa raia zake magonjwa, ambalo lingeweza kuponya kabisa viwete wote, raia zake walio vipofu kurudishiwa macho na viziwi masikio yao, makaburi yake kutoa wafu wayo kwa ufufuo wa uzima, je! serikali ya taifa hilo isingependa kujivunia matendo ya namna hiyo? Na je! kila mtu duniani asingefanya mara hiyo kila jambo awezalo ili ajipatie mahali chini ya serikali hiyo? Tungefikiri hivyo. Walakini historia yaonyesha maelekeo tofauti kwa upende wa wengi.
2, 3. Ni jambo gani lililofanya watawala Wayahudi wa karne ya kwanza, na raia zoa, wamkatae mfalme wa Mungu?
2 Ifikirie hali katika karne ya kwanza wakati Yesu Kristo, Mfalme-mkusudiwa wa serikali ya Mungu, alipokuwa akifanya matendo ya ajabu kama hayo. Watu walimpokeaje? Walivutwa kwa urahisi na watawala wao Wayahudi, wakagawanyika katika ushikamanifu wao. Kusudi kubwa la watawala hao Wayahudi lilikuwa kulinda vyeo na madaraka yao katika serikali ya kibinadamu kuliko lile la kutafuta faida bora zaidi za watu, kama inavyoonyeshwa na Biblia:
“Wakuu wa makuhani na Mafarisayo wakakusanya baraza, wakasema, Tunafanya nini? Maana mtu huyu [Yesu] afanya ishara nyingi. Tukimwacha hivi, watu wote watamwamini; na Warumi watakuja, watatuondolea mahali petu na taifa letu. Mtu mmoja miongoni mwao, Kayafa, aliyekuwa Kuhani Mkuu mwaka ule, akawaambia, Ninyi hamjui neno lo lote; wala hamfikiri ya kwamba yafaa mtu mmoja afe kwa ajili ya watu, wala lisiangamie taifa zima. . . . Basi tangu siku ile walifanya shauri la kumwua.”—Yohana 11:47-53.
3 Si kwamba tu faida za kichoyo ziliwazuia watawala Wayahudi wasitii serikali ya Mungu, bali uchoyo wao pia uliwafanya wawaongoze watu wamkatae Yesu. Biblia inasema kwamba wakati liwali Mrumi Pontio Pilato alipomtoa Yesu, akisema, “Tazama, Mfalme wenu!” watu hao walipiga kelele hivi: “Mwondoshe! [Mtundike]!” Pilato akawaambia hivi: “Je! [nimtundike] mfalme wenu! Wakuu wa makuhani wakamjibu, Sisi hatuna mfalme ila Kaisari.” Kwa hiyo ni viongozi wa kidini waliowashawishi watu wapige kura ya kumwondoa mfalme na ufalme wa Mungu.—Yohana 19:14, 15.
4. Ni uchaguzi gani unaomwelekea kila mmoja wetu leo?
4 Uwe unafahamu hivyo au hapana, unaelekeana na uchaguzi kama huo leo. Nao ndio huu: Ama kuwa raia mshikamanifu wa serikali ya Mungu, ama kuwa upande mmoja na wale wanaopinga utawala wake. Uhakika wa kwamba Yesu Kristo na watu watakaotawala pamoja naye wako mbinguni na hawaonekani hauwafanyi wasiwe watu wa kweli. Ushuhuda ni mwingi sana: Kristo alifufuliwa kutoka kwa wafu, na karibuni sasa, pamoja na watawala wenzake, atafikiliza amri ya Mungu ya kuondoa serikali za kidunia na wenye kuziunga mkono. (Dan. 2:44; 2 The. 1:6-9; Ufu. 2:26, 27) Kwa hiyo uchaguzi wako ni gani? Je! unapendelea utawala wa wanadamu au serikali ya Mungu?
MAARIFA YANAHITAJIWA ILI KUWA RAIA
5. Ni takwa gani ambalo serikali moja inawekea wageni ili waweze kupata uananchi?
5 Huwezi kuinua mkono tu na kusema: “Nataka kuwa raia wa serikali ya Mungu.” Kwa kufahamika, mambo zaidi yanahitajiwa. Kwa mfano, iwapo mgeni angetaka kuwa raia wa United States ya Amerika, atapaswa kutimiza matakwa fulani. Kitabu The World Book Encyclopedia kinaeleza hivi: “Maafisa wa Forodhani na utumishi wa Kupeana Uananchi huchunguza na kumhoji mgeni. . . . Ni lazima aonyeshe kwamba anaweza kusoma, kuandika, na kuzungumza Kiingereza cha kawaida . . . Lazima mgeni huyo aonyeshe pia anafahamu jambo fulani juu ya historia na namna ya serikali ya United States.”—chapa 1973, Kit. 14, uku. 52.
6. Twapaswa kujifunza “lugha” gani iwapo tutastahili kuwa raia za ufalme wa Mungu?
6 Ili ustahili kuwa raia wa serikali ya Mungu, unapaswa kutimiza matakwa kama hayo. Kwanza kabisa ni lazima ujifunze “lugha” ya wale watakaoishi chini ya utawala wa ufalme wa Mungu. Katika Neno lake, Biblia, Yehova anasema hivi: “Maana hapo ndipo nitakapowarudishia mataifa lugha iliyo safi, wapate kuliitia jina la [Yehova], wamtumikie kwa nia moja.” (Sef. 3:9) Hii “lugha iliyo safi” ni kweli ya Mungu kutoka katika Biblia, sana sana kuhusiana na ufalme wake ambao utaleta amani duniani. Yesu na wanafunzi wake waliizungumza hii “lugha iliyo safi” walipokuwa duniani. Walitoa ushuhuda juu ya kweli kuhusiana na Ufalme huo, wakiweka ujumbe huo mbele kabisa. Leo wale watakaokuwa raia za ufalme wa Mungu wanapaswa kufanya vivyo hivyo.—Yohana 18:36; Luka 8:1; 10:8-11.
7. Raia wa serikali ya Mungu anapaswa awe aweza kujibu maulizo gani? Je! wewe waweza kuyajibu?
7 Pamoja na hayo, ili kustahili kuwa raia wa ufalme wa Mungu, unapaswa kufahamu jambo fulani juu ya historia yake, pamoja na watawala wake. Je! unaweza kuonyesha kwamba unafahamu kwa kujibu maulizo kama: Ni wakati gani kwanza Mungu alipofanya matayarisho kwa ajili ya serikali yake ya Ufalme? Ni nani baadhi ya watumishi wa Yehova wa kabla ya Ukristo waliotazamia kuwa raia za serikali yake yenye haki? Walionyeshaje imani yao katika serikali hiyo? Ni wangapi watakaotumikia kama watawala katika serikali ya Mungu? Ni nani baadhi ya watu wanaotajwa katika Biblia walioonyesha sifa zao za kuwa watawala-wenzi na Kristo? Walifanya nini ili kuuonyesha uaminifu wao? Yesu Kristo alitimizaje sifa za kuwa mfalme? Ni hali gani zitakazokuwapo chini ya utawala wa Ufalme ambazo zitaonyesha anavyowapenda wanadamu? Kufahamu kwetu mambo hayo ni kwa maana, kwa kuwa katika sala yake kwa Babaye, Yesu alisema hivi: “Hii ndiyo maana ya uzima wa milele, wapate maarifa ya kukujua wewe, Mungu wa kweli peke yako, na ya yeye uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3, NW.
MWENENDO WA HAKI NI WA LAZIMA
8. Ni takwa gani jingine ambalo serikali moja inawekea wageni ili waweze kupata uananchi?
8 Kama vile kulivyo matakwa mengine ya kuwa raia wa serikali za kidunia, ndivyo kulivyo na mengine ya kuwa raia wa ufalme wa Mungu. Kitabu The World Book Enyclopedia kinasema hivi juu ya mtu ambaye anaweza kustahili kuwa na uananchi wa Amerika: “Ni lazima awe na adili nzuri . . . Sheria inasema kwamba mgeni hana adili nzuri ikiwa yeye ni mlevi, amekwisha fanya uzinzi, ana zaidi ya mke mmoja, anajiruzuku kwa kucheza kamari,” na mengineyo. Vivyo hivyo wale wanaostahili kuwa raia za serikali ya Mungu wanahitaji kutimiza matakwa ya adili. Yameandikwa katika Biblia.
9. Ni matakwa gani ya adili ambayo inampasa mtu kutimiza ili astahili kuwa raia wa serikali ya Mungu?
9 Kwa mfano, anayetarajia kuwa raia wa Ufalme, anapaswa kutumia maishani mwake yale ambayo Biblia inasema juu ya unyofu. Hawezi kuwa mwongo au mwivi. (Efe. 4:25, 28; Ufu. 21:8) Lazima vilevile atii katazo la Biblia la ulevi. (Efe. 5:18; 1 Pet. 4:3, 4) Na zaidi ya hayo, mazoea kama vile uasherati, uzinzi au kulalana kwa watu wa namna moja yanavunja matakwa ya Mungu, nao wanaozoea mambo hayo hawastahili uzima chini ya ufalme wa Mungu. (1 Kor. 6:18; Ebr. 13:4; Rum. 1:24-27) Walakini watu ambao wakati mmoja walikuwa wakifanya mazoea hayo, lakini wamekwisha yaacha, hawafanywi kutostahili na mwendo wao wa maisha wa uasherati wa kwanza. (1 Kor. 6:9-11) Jambo kuu ni hili: Mungu hataachilia uvunjaji wa makusudi wa sheria zake; lazima watu wajipatanishe na matakwa ya adili katika Neno lake iwapo watastahili kuwa raia za serikali yake.
10. Raia za serikali ya Mungu wanapaswa kuheshimu mpango gani wa uongozi?
10 Hii maana yake ni kwamba wale watakaoishi chini ya ufalme wa Mungu wanapaswa kujipatanisha kwa kupenda na yale ambayo Neno la Mungu linasema. Lakini kuna zaidi ya hayo yanayohitajiwa. Wanapaswa pia kuheshimu mashauri na maamuzi ya wale ambao Mungu ameweka katika vyeo vya madaraka ndani ya kundi la Kikristo. Hawawezi kuwa watu ‘wanaofanya watakalo’ bila kujali uongozi unaopokelewa kutoka kwa “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” ambaye Kristo amemwaminisha uangalizi wa faidi za Ufalme duniani. (Mt. 24:45) Mtume Petro aliandika juu ya watu waliodharau mamlaka, akiwataja kuwa “wale waufuatao mwili katika tamaa ya mambo machafu, na kudharau mamlaka.” Akiwasimulia zaidi, mtume huyo alisema hivi: “Wenye ushupavu, wenye kujikinai, hawatetemeki [wakitukana watukufu walioaminishwa uangalizi ndani ya kundi la Mungu].”—2 Pet. 2:10, 11.
11. Raia zote za Ufalme wapaswa kutii amri gani za ufalme wa Mungu? (b) Amri hizo zinafuatwaje, na sababu gani kuzitii ni jambo la muhimu sana?
11 Hata hivyo mengi zaidi yanahitajiwa kwa raia za serikali ya Mungu kuliko tu kujiepusha na njia ya maisha isiyo ya heshima, ya uasherati. Vilevile wanapaswa kuchukua hatua ya kwanza katika kutendea wengine mambo ya fadhili. Ni lazima waishi kulingana na amri ya kimungu iliyotolewa na Mfalme, Yesu Kristo: “Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo.” (Mt. 7:12) Kristo aliweka mfano katika kuwapenda wengine, hata akatoa uhai wake kwa ajili ya wanadamu. Naye akawaamuru wafuasi wake hivi: “Kama nilivyowapenda ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo.” (Yohana 13:34; 1 Yohana 3:16) Ni upendo huo wa kujinyima na kuhangaikia wengine utakaofanya kuishi kupendeze kweli kweli chini ya utawala waufalme wa Mungu. Je! mwenendo wako unakustahilisha uishi wakati huo? Je! wewe hufanya jitihada kweli kweli ufanyie wengine vitendo vya fadhili?
MUNGU ANATAKA UTEGEMEZAJI MSHIKAMANIFU
12. Ni takwa gani jingine ambalo serikali moja huwekea wageni ili waweze kupata uananchi?
12 Haipasi kushangaza kwamba Yehova Mungu anataka raia zake waunge mkono serikali yake ya Ufalme kwa ushikamanifu, kwa kuwa ndivyo serikali za kibinadamu zinavyofanya. Kitabu The World Book Encyclopedia kinaendelea kusema hivi juu ya mgeni anayetaka kuwa raia wa United States: “Anaahidi kuunga mkono na kuitetea katiba na kuchukua silaha kwa niaba ya United States.” Pamoja na hayo, yeye “anakula kiapo cha kukana vyeo vyote vya kigeni na utii kamili kwa nchi nyingine yo yote.” Lakini ni katika njia gani Mungu anataka watu waunge mkono ufalme wake kwa ushikamanifu?
13. Ni jambo gani linaloonyesha kwamba ni kosa kwa Wakristo kupigana kwa silaha za kimwili kwa ajili ya serikali ya Mungu?
13 Jambo hilo halifanywi kwa kuchukua silaha za mwili ili kupigana kwa ajili ya Ufalme huo. Yesu alimweleza liwali Mrumi Pontio Pilato hivi: “Ufalme wangu sio wa ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa wa ulimwengu huu, watumishi wangu wangenipigania, nisije nikatiwa mikononi mwa Wayahudi. Lakini ufalme wangu sio wa hapa.” (Yohana 18:36) Mapema zaidi, wakati mtume Petro alipojaribu kumkinga Bwanake, Yesu alimwambia hivi: “Rudisha upanga wako mahali pake; maana wote waushikao upanga, wataangamia kwa upanga. Ama wadhani ya kuwa mimi siwezi kumsihi Baba yangu, naye ataniletea sasa hivi zaidi ya majeshi kumi na mawili ya malaika?” (Mt. 26:52, 53) Wakristo hawatashiriki katika kuwaangamiza adui za Mungu; hiyo ni kazi ya majeshi ya Mungu ya kimbinguni. Biblia inaonyesha kwamba Wakristo hawapaswi kujiingiza katika vita vya halisi, vya kimwili.—Linganisha 2 Wakorintho 10:3-5; 2 Timotheo 2:24.
14. (a) Mungu anawataka raia za Ufalme wake wafanye kazi gani? (b) Wanapaswa kuonyeshaje kujiweka kwao wakf kwa Mungu?
14 Mahali pake, anataka raia zake wa kidunia wawe wanenaji kwa ajili ya serikali yake—mawakili wa Ufalme au watangazaji. Hivyo, ‘kwa kinywa wanafanya tangazo la waziwazi la wokovu.’ (Rum. 10:10, NW) Kwa kuongezea hayo, Mungu hutaka raia zake wajiweke wakf na kutoa utii kamili kwake. Yesu Kristo alijitoa mwenyewe ayafanye mapenzi ya Mungu, naye akabatizwa kuonyesha jambo hilo. (Mt. 3:16, 17; Ebr. 10:5-10) Wakristo wanapaswa kutenda vivyo hivyo. Baada ya kuyatwaa maarifa yaliyo ya lazima na kujipatanisha na matakwa ya Mungu ya adili, wanapaswa kuweka wakf maisha yao kwake na kuonyesha jambo hilo kwa ubatizo wa maji. Kisha wanahitaji kushiriki kwa moyo wote katika kazi kuu ya kuwajulisha watu wote ambayo Yehova anataka ifanywe.
15, 16. (a) Kazi ya kwanza kabisa ya Yesu duniani ilikuwa nini, naye alionyeshaje wanafunzi wake kwamba huo ndio ungekuwa utendaji wao mkuu pia? (b) Kufuata maagizo ya Yesu kulihitaji kwamba watu watembelewe wapi?
15 Ni mapenzi ya Yehova kwamba kila mtu afahamu ufalme wake ni nini na namna utakavyotatua matatizo ya wanadamu. Serikali hiyo ni jambo lenye thamani moyoni mwa Mungu, kwa kuwa ndiyo njia ambayo kupitia kwayo ataondolea jina lake suto lote na kuletea watu wake baraka. Hivyo Biblia inasema hivi juu ya utendaji wa kwanza kabisa wa Mwana wa Mungu hapa duniani: “Yesu alikuwa akizunguka katika miji yote na vijiji, . . . na kuihubiri habari njema ya ufalme.” (Mt. 9:35) Na katika pindi nyingine Yesu alisema hivi: “Imenipasa kuihubiri habari njema ya ufalme wa Mungu katika miji mingine pia; maana kwa sababu hiyo nalitumwa.”—Luka 4:43.
16 Yesu aliwazoeza wafuasi wake wafanye kazi iyo hiyo. Kwanza, aliwatuma mitume wake 12, akawaagiza hivi: “Katika kuenenda kwenu, hubirini, mkisema, Ufalme wa mbinguni umekaribia. . . . Na mji wo wote au kijiji cho chote mtakachoingia, tafuteni ni nani humo aliye mtu [anayestahili] mkae kwake hata mtakapotoka. Nanyi mkiingia katika nyumba isalimuni. Na nyumba ile ikistahili, amani yenu na iifikilie.” (Mt. 10:5-14) Ili kutimiza maagizo hayo, mitume walitembelea nyumba za watu, na kukaa na wenye ‘kustahili,’ wakishiriki pamoja nao ujumbe wa Ufalme. Baadaye, Yesu aliwaagiza 70 wa wanafunzi wake hivi: “Na mji wo wote mtakaouingia, wakiwakaribisha, . . . waambieni, Ufalme wa Mungu umewakaribia.” (Luka 10:1-11) Ndiyo, Yesu aliwatuma wafuasi wake wakiwa na shughuli ya Ufalme.
17. (a) Sababu gani uhodari ulihitajiwa kuuhubiri Ufalme katika karne ya kwanza? (b) Wakristo wa kwanza walionyeshaje uhodari wao katika kuhubiri?
17 Ili kushiriki katika utendaji huo uhodari mwingi ulihitajiwa. Yesu alikuwa ameuawa kwa fitina ya wapinzani wa Ufalme, na, muda si muda, wafuasi wake Stefano na mtume Yakobo waliuawa pia. (Matendo 7:54-60; 12:2) Hata hivyo wafuasi wa Yesu hawakuzuilika. Hata baada ya mitume kupigiwa mijeledi, Biblia inasema hivi, “kila siku, ndani ya hekalu na nyumbani mwao, hawakuacha kufundisha na kuhubiri habari njema za Yesu kwamba ni Kristo.” (Matendo 5:42) Miaka mingi baadaye kikundi cha watu wenye ghasia katika Thethalonike kilishitaki hivi Paulo na wenzi wake: “Hawa wote wanatenda mambo yaliyo kinyume cha amri za Kaisari, wakisema ya kwamba yupo mfalme mwingine, aitwaye Yesu.” (Matendo 17:7) Walakini mateso hayo hayakuwazuia wasihubiri. Maandiko yanaonyesha kwamba Paulo hakuacha ‘kutangaza habari njema.’ Alienda ‘akifundisha waziwazi, na nyumba kwa nyumba,’ akitoa ushuhuda kikamilifu kwa Wayahudi na wengine waliokuwa na uhitaji wa kutubu.—Matendo 20:20, 21.
WEWE UNASIMAMA WAPI?
18, 19. (a) Mapenzi ya Mungu ya kufanywa sasa ni nini? (b) Ni kwa kukumbuka mambo gani tuwezapo kusaidiwa kushiriki katika kuuhubiri Ufalme?
18 Ili kuwa wakili wa Mungu uhodari ule ule unahitajiwa. Upinzani leo unalingana kabisa na ule wa karne ya kwanza. Kwa hiyo ulizo ni hili: Unasimama wapi? Je! unaunga mkono kwa ushikamanifu ufalme wa Mungu? Mapenzi yake ni kwamba ushuhuda mkuu wa Ufalme utolewe kabla ya mwisho kuja. Je! utashiriki katika hilo?—Mt. 24:14, NW.
19 Huenda ukaona vigumu kuchukua hatua ya kwanza kuzungumza na wengine juu ya serikali ya Mungu. Lakini waweza kufanya hivyo. Kufanya hivyo kutathibitisha kwamba wampenda Yehova. (1 Yohana 5:3) Kumbuka kwamba Mungu alimpa Ibrahimu mgawo mgumu wa kumtoa mwanawe dhabihu. Ibrahimu alipotii, Mungu alimzuia asifikie hatua ya kutoa dhabihu hiyo, akamwambia hivi: “Kwa maana sasa ninajua ya kuwa unamcha Mungu.” Ndiyo, utii wa Ibrahimu ulithibitisha kwamba yeye alimtumaini Mungu kabisa. (Mwa. 22:12; Ebr. 11:17-19) Vivyo hivyo, kwa kuhubiri kwetu Ufalme kwa juhudi twamwonyesha Mungu kwamba tunaunga mkono serikali yake kwa ushikamanifu, jambo ambalo anahitaji kutoka kwa raia zake. Wakati ule ule, twaonyesha kwamba twampenda na kuhangaikia watu, kwa kuwa njia pekee wawezayo kuepuka uharibifu katika “dhiki kubwa” inayokaribia mbio-mbio ni kusikiliza ujumbe wa Ufalme na kutenda kulingana nao.—Mt. 24:21; 1 Yohana 2:17.
20. Mfano wa Musa unaweza kutusaidiaje kuchukua msimamo wenye hekima kuhusiana na matakwa ya Mungu ya adili?
20 Hata hivyo, kuunga kwetu mkono serikali ya Mungu, kunaonyeshwa vilevile kwa kushikamana kwetu na mtakwa ya Mungu ya adili. Msimamo wetu ni nini katika jambo hilo? Wengine huweka kwanza kujipendeza wenyewe, ‘kufanya watakavyo.’ Na ni kweli kwamba kunaweza kuwa furaha katika kwenda pamoja na wingi wa watu wanaojitia katika maisha ya anasa, yasiyo ya adili. Walakini furaha hiyo ni ya muda tu. Kwa hekima, Musa hakuchagua mwendo wa namna hiyo. “Kwa imani Musa, alipokuwa mtu mzima, akakataa kuitwa mwana wa binti Farao; akaona ni afadhali kupata mateso pamoja na watu wa Mungu kuliko kujifurahisha katika dhambi kwa kitambo; . . . kwa kuwa aliyatazamia hayo malipo.” (Ebr. 11:24-26) Inategemea jambo lililo la maana zaidi kwetu. Je! ni kutosheleza maelekeo yetu ya kichoyo? Au je! ni kufanya yale yanayompendeza Muumba na kutumikia faida za serikali yake ya Ufalme?
21. (a) Yesu alionyeshaje uchaguzi ambao sote tunapaswa kufanya? (b) Wewe umeazimia kufanya uchaguzi gani?
21 Hakika, kuna uchaguzi mara mbili. Kristo aliulinganisha na uchaguzi kati ya barabara mbili. Barabara moja, akasema, ni “pana.” Katika hiyo wasafiri wanapewa uhuru wa ‘kufanya watakavyo.’ Hata hivyo, barabara ile nyingine “imesonga.” Ndiyo, wale walio katika barabara hiyo wanatakiwa washikamane na uongozi wa Mungu. Yesu alitaja kwamba walio wengi, wanaichukua barabara ile pana, ni wachache tu wanaochukua ile nyembamba. Wewe utachakua barabara gani? Katika kufanya uchaguzi wako, kumbuka jambo hili: Ile barabara pana itakoma ghafula—katika uharibifu! Kwa upande mwingine, ile barabara nyembamba itaongoza mpaka kuingia katika taratibu mpya ya Mungu ambamo utaweza kuishi milele kama raia mshikamanifu wa Ufalme. (Mt. 7:13, 14) Kwa hiyo uchaguzi ni wako! Utakuwa uchaguzi gani?—Kutoka The Watchtower Jan. 15, 1980.
[Picha katika ukurasa wa 16]
Viongozi wa kidini wa siku za Yesu walikuwa na kusudi la kulinda vyeo vyao katika serikali ya kibinadamu. Kwa hiyo, walifanya shauri la kumwua
[Picha katika ukurasa wa 17]
Raia za serikali ya Mungu wapaswa kujifunza “lugha iliyo safi” ya kweli ya Biblia