Sura 15
Kuwa Raia wa Serikali ya Mungu
1, 2. Ni jambo gani linalohitajiwa iii kuwa raia wa serikali ya Mungu?
JE! WEWE unataka kuishi milele hapa duniani chini ya serikali ya Mungu? Mtu ye yote mwenye akili nzuri angejibu, Ndiyo! Baraka za ajabu zitafurahiwa. Lakini ili kuzipokea huwezi kuinua tu mkono wako na kusema hivi: ‘Mimi nataka kuwa raia wa serikali ya Mungu.’ Mengi zaidi yanahitajiwa.
2 Kwa mfano, tuseme ungetaka kuwa raia wa nchi nyingine. Ili ufanye hivyo, ingekupasa utimize matakwa yaliyowekwa na watawala wa serikali ya nchi hiyo. Lakini kabla ya kufanya hivyo, ingekupasa ujue hayo ni matakwa gani. Vivyo hivyo, inakupasa ujifunze Mungu anataka nini kwa wale wanaopenda kuwa raia za serikali yake. Kisha inakupasa utimize matakwa hayo.
MAARIFA YANAHITAJIWA
3. Ni takwa gani moja la kuwa raia wa serikali ya Mungu?
3 Takwa la maana sana la kuwa raia wa serikali ya Mungu ni kupata maarifa ya “lugha” ya serikali hiyo. Bila shaka hilo ni jambo linalolingana na kuwaza kuzuri. Serikali fulani za wanadamu zinawataka vilevile raia wapya waweze kusema lugha ya nchi yao. Hivyo basi, ni “lugha” gani ambayo wale watakaopokea uzima chini ya serikali ya Mungu lazima wajifunze?
4. Lazima watu wa Mungu wajifunze ‘lugha gani safi’?
4 Angalia anayosema Yehova juu ya hilo katika Neno lake, Biblia: “Maana hapo ndipo nitayapa mataifa lile badiliko la kuwa na lugha safi, ili wote waliitie jina la Yehova, ili wamtumikie bega kwa bega.” (Sefania 3:9, NW) Hiyo “lugha safi” ndiyo kweli ya Mungu inayopatikana katika Biblia. Hasa, ndiyo ile kweli inayohusu serikali ya Ufalme wa Mungu. Basi ili uwe raia wa serikali ya Mungu, lazima ujifunze “lugha” hiyo kwa kuyatwaa maarifa ya kumjua Yehova na mpango wake wa Ufalme.—Wakolosai 1:9, 10; Mithali 2:1-5.
5. (a) Imetupasa tujue nini juu ya serikali ya Mungu? (b) Ni maarifa gani tunayohitaji ili tupate uzima wa milele?
5 Leo serikali fulani za wanadamu zinawataka wale wanaopokea uraia wajue kwa kadiri fulani historia ya serikali yao, vilevile namna inavyotenda kazi. Hali moja na hayo, inakupasa wewe ujue mambo hayo juu ya serikali ya Mungu iwapo unataka kuwa raia wake. Maarifa hayo yanaweza kuongoza kwenye uzima wa milele. Katika sala kwa Baba yake, Yesu alisema: “Hii ndiyo maana ya uzima wa milele, wapate maarifa ya kukujua wewe, Mungu wa kweli mmoja tu, na ya yeye uliyetuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3, NW.
6. (a) Ni baadhi ya maulizo gani ambayo raia za serikali ya Mungu wamepaswa waweze kujibu? (b) Wewe unaweza kuyajibu?
6 Ikiwa umejifunza sura zilizotangulia za kitabu hiki, kwa sasa umekwisha kupokea mengi ya maarifa hayo yaliyo ya maana kabisa. Sivyo? Unaweza kuonyesha kwamba ungeyapokea kwa kujibu maulizo kama haya: Ni wakati gani Mungu alipotaja kwa mara ya kwanza kusudi lake la kuwa na serikali ya Ufalme? Ni baadhi ya watumishi gani wa Mungu waliotazamia kuwa raia za kidunia za serikali hiyo? Serikali hiyo ya Mungu itakuwa na watawala au wafalme wangapi? Wafalme hao watatawala wakiwa wapi? Ni nani waliokuwa wa kwanza kuchaguliwa kuwa wafalme katika serikali ya Mungu? Yesu alionyeshaje kwamba yeye angekuwa mfalme mzuri? Hata hivyo, ili uwe raia wa serikali ya Mungu, mengi zaidi yanatakwa kuliko kuwa na maarifa ya kuijua tu serikali hiyo.
MWENENDO WA UADILIFU UNATAKWA
7. Kwa habari ya serikali za wanadamu, matakwa ya uraia yanatofautianaje?
7 Serikali za leo zinawataka raia wapya watimize kiwango fulani cha mwenendo. Kwa mfano, huenda zikasema kwamba mwanamume anaruhusiwa kuwa na mke mmoja tu, naye mwanamke awe na mume mmoja tu. Hata hivyo serikali nyingine zina sheria tofauti. Zinaruhusu raia zao wawe na wenzi wa ndoa zaidi ya mmoja. Ni mwenendo gani ambao watu wanaotaka kuwa raia za serikali ya Mungu wanatazamiwa kuwa nao? Ni jambo gani ambalo Mungu anasema linafaa juu ya ndoa?
8. (a) Kiwango cha Mungu kwa ndoa ni nini? (b) Uzinzi ni nini, na Mungu anasema nini juu yake?
8 Mwanzoni Yehova aliweka kiwango kinachoifaa ndoa alipompa Adamu mke mmoja tu. Mungu alisema: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja.” (Mwanzo 2:21-24) Yesu alieleza kwamba hicho ndicho kiwango kinachowafaa Wakristo. (Mathayo 19:4-6) Kwa kuwa wenzi wa ndoa wamekuwa “mwili mmoja,” wanavunja heshima ya ndoa wakifanya ngono na mtu mwingine. Tendo hilo linaitwa uzinzi, naye Mungu anasema ataadhibu wazinzi.—Waebrania 13:4; Malaki 3:5.
9. (a) Maoni ya Mungu ni nini juu ya watu wanaofanya ngono na hali hawajaoana? (b) Uasherati ni nini?
9 Kwa upande mwingine, wanaume na wanawake wengi wanaishi pamoja na kufanya ngono, lakini hawaoani. Walakini, Mungu hakutaka uhusiano huo wa karibu kati ya mwanamume na mwanamke utegemee msingi wa kujaribu tu. Hivyo kuishi pamoja pasipo kufunga ndoa ni kumkosea Mungu, aliyeufanya mpango huo wa ndoa. Kufanya hivyo kunaitwa uasherati. Tendo hilo la uasherati ni kufanya ngono na mtu ye yote ambaye hukuoana naye. Nayo Biblia inasema hivi: “Haya ndiyo mapenzi ya Mungu, . . . mwepukane na uasherati.” (1 Wathesalonike 4:3-5) Hivyo, basi, ni kosa kwa mtu aliye mseja kufanya ngono na mtu ye yote.
10. Ni mazoea gani mengine ya ngono ambayo ni kinyume cha sheria za Mungu?
10 Leo wanaume na wanawake wengi wanafanya ngono pamoja na watu wa aina moja na wao, yaani, wanaume kwa wanaume na wanawake kwa wanawake. Lakini Neno la Mungu linasema kwamba wanatenda kosa, uchafu mkubwa. (Warumi 1:26, 27) Vilevile, ni kinyume cha sheria ya Mungu mtu kufanya ngono na mnyama. (Mambo ya Walawi 18:23) Ni lazima ye yote anayetaka kuishi chini ya serikali ya Mungu aache mazoea hayo machafu.
11. (a) Maoni ya Mungu ni nini juu ya matumizi ya vileo (pombe)? (b) Ni lazima wale wanaotaka kuwa raia za serikali ya Mungu waache mazoea gani yanayoharibu afya?
11 Si kinyume cha sheria ya Mungu kunywa divai, pombe au kileo fulani kwa kiasi. Kwa kweli, Biblia inaonyesha kwamba divai kidogo anaweza kufaa afya ya mtu. (Zaburi 104:15; 1 Timotheo 5:23) Lakini ni kinyume cha sheria ya Mungu kulewa, au kushiriki karamu zenye makelele mahali ambako watu wanaendesha mwenendo mchafu. (Waefeso 5:18; 1 Petro 4:3, 4) Zaidi ya kutumia vileo ili wapate kulewa, watu wengi leo wanatumia dawa mbalimbali za kulevya kwa kusudi ilo hilo. Vilevile, ili waone raha huenda wakavuta kasumba au tumbako, hali huenda wengine wakatafuna tambuu au miraa. Lakini vitu hivyo vinaichafua miili yao na kuharibu afya yao. Basi iwapo unataka kuwa raia wa serikali ya Mungu, inakupasa uache vitu hivyo vyenye kuharibu mtu.—2 Wakorintho 7:1.
12. (a) Ni baadhi ya mazoea gani yasiyo ya unyofu ambayo ni kinyume cha sheria za Mungu? (b) Mtu anayeshiriki mazoea hayo anawezaje kupata kibali ya Mungu?
12 Ni wazi kwamba serikali za wanadamu hazitaki wahalifu waingie nchini wawe raia wapya. Naye Yehova aria viwango vilivyo juu hata zaidi. Yeye anataka sisi “tujiendeshe kwa unyofu katika mambo yote.” (Waebrania 13:18, NW) Kama watu hawataki kushika sheria za Mungu, hawataruhusiwa waishi chini ya ufalme wake. Mara nyingi leo watu wanajifanya ni wanyofu, lakini wanavunja sheria nyingi. Walakini, Mungu anaweza kuona mambo yote. Hakuna mtu anayeweza kumdanganya. (Waebrania 4:13; Mithali 15:3; Wagalatia 6:7, 8) Hivyo Yehova hatawaruhusu wawe raia za serikali yake watu wanaovunja sheria zake, kama zile zinazokataza kusema uongo na kuiba. (Waefeso 4:25, 28; Ufunuo 21:8) Hata hivyo Mungu ni mvumilivu na mwenye kusamehe. Basi mkosaji akiacha mazoea yake mabaya na kuanza kufanya mema, Mungu atamkubali huyo.—Isaya 55:7.
13. Ni maoni gani ambayo watumishi wa Mungu wamepaswa wawe nayo juu ya sheria za serikali za wanadamu?
13 Lakini namna gani kushika sheria za serikali za wanadamu? Kwa muda ambao serikali za wanadamu zitaendelea kuwapo, Mungu anataka watumishi wake waitii “mamlaka iliyo kuu.” Zinapasa kulipwa kodi, hata ingawa kodi hizo ni za juu na huenda mtu asikubaliane na namna fedha za kodi zinavyotumiwa. Vilevile, sheria za serikali zinapasa zifuatwe. (Warumi 13:1, 7; Tito 3:1) Wakati mmoja tu ambao hazipasi kufuatwa ni muda zinapotaka mtu asitii sheria ya Mungu. Ikiwa hivyo, kama vile Petro na mitume wale wengine walivyosema, “Ni lazima sisi tutii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—Matendo 5:29, NW.
14. Tunaweza kuonyeshaje kwamba sisi tuna maoni yaliyo sawa na ya Mungu juu ya ubora wa uhai?
14 Mungu anauthamini sana uhai. Wale wanaotaka kuwa raia wa serikali yake lazima wafahamu hilo. Kwa wazi, uuaji wa kukusudia ni kinyume cha sheria ya Mungu. Lakini mara nyingi chuki inaongoza watu waue wenzao, na hata ikiwa mtu anaendelea kumchukia mwenzake, mchukiaji huyo hawezi kuwa raia wa serikali ya Mungu. (1 Yohana 3:15) Kwa hiyo, ni jambo la maana kabisa kufuata yanayosemwa katika Biblia katika Isaya 2:4 juu ya kutokutumia silaha ili kuua jirani zetu. Neno la Mungu linaonyesha kwamba hata uhai wa mtoto asiyezaliwa, aliye ndani ya tumbo la mama yake, ni wenye thamani (ubora) sana kwa Yehova. (Kutoka 21:22, 23; Zaburi 127:3) Na hata hivyo mamilioni ya mimba zinatolewa na kuharibiwa kila mwaka. Kuharibu uhai kwa njia hiyo ni kinyume cha sheria ya Mungu, kwa sababu binadamu aliye ndani ya tumbo la mama yake ni mtu aliye hai na hapaswi kuuawa.
15. Ni amri gani za Mfalme wa Mungu ambazo lazima raia wote wa Ufalme wazitii?
15 Hata hivyo, kwa habari ya wale wanaotaka kuwa raia za serikali ya Mungu, mengi yanatakwa zaidi ya kutotenda tu yaliyo mabaya au machafu. Lazima vilevile wajitahidi kabisa kutendea wengine mambo ya fadhili na yasiyo ya kichoyo. Lazima waishi kwa ile kanuni ya kimungu iliyotolewa na Mfalme, Yesu Kristo: “Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Kristo aliweka mfano wa kuwapenda wengine. Hata alitoa uhai wake kwa ajili ya wanadamu, akawaamuru wafuasi wake hivi: “Mpendane. Kama vile nilivyowapenda ninyi.” (Yohana 13:34; 1 Yohana 3:16) Ni upendo wa aina hiyo usio wa choyo, wa kuhangaikia wengine ndio utakaofanya maisha yafurahishe kweli kweli chini ya utawala wa ufalme wa Mungu.—Yakobo 2:8.
16, 17. (a) Kuna sababu gani nzuri za kubadili maisha yetu ili kutimiza matakwa ya Mungu? (b) Sababu gani tunaweza kuwa na hakika kwamba tunaweza kufanya mabadiliko yo yote yanayohitajiwa kabisa?
16 Biblia inaonyesha kwamba lazima watu wabadili maisha yao ili watimize matakwa ya kuwa raia za serikali ya Mungu. (Waefeso 4:20-24) Je! wewe unajitahidi kufanya mabadiliko hayo? Bila shaka kufanya hivyo kunastahili jitihada yo yote! Kwa sababu gani? Kwa sababu hutakuwa tu na maisha bora kwa miaka michache chini ya serikali fulani ya kibinadamu. Hapana, Bali utapokea uzima wa milele katika afya bora kabisa katika dunia ya paradiso chini ya serikali itakayoongozwa na Mungu!
17 Hata sasa, kwa kutimiza matakwa ya Mungu, utaweza kuwa na furaha zaidi. Lakini huenda ukahitaji kufanya mabadiliko. Kwani, watu wengi sana waliokuwa wenye kuchukiza wenzao na wenye pupa wamebadilika. Vilevile, waasherati, wazinzi, wanaume wanaofanya ngono na wanaume wenzao, na pia wanawake na wanawake wenzao, walevi, wauaji wa kukusudia, wevi, wenye kuzoea dawa za kulevya na wavutaji wa tumbako wamebadili njia yao ya maisha. Wamefanya hivyo kwa kujitahidi kweli na kwa msaada wa Mungu. (1 Wakorintho 6:9-11; Wakolosai 3:5-9) Basi ikiwa una mambo magumu unayopaswa kuyabadili ili utimize matakwa ya Mungu, usikate tamaa. Unaweza kufaulu!
USHIKAMANIFU KWA SERIKALI YA MUNGU
18. Mungu anatutazamia tuonyeshe kwa njia gani ya pekee kwamba tunaunga mkono ufalme wake kwa ushikamanifu?
18 Si ajabu kwamba Yehova Mungu angetaka raia zake waunge mkono serikali yake ya Ufalme kwa ushikamanifu. Serikali za wanadamu zinawataka raia wafanye ivyo hivyo. Lakini ni kwa njia gani ya pekee Mungu anatazamia kuungwa mkono kwa ushikamanifu? Je! ni kwa kutaka raia zake wachukue silaha wapiganie ufalme wake? Hapana. Badala yake, lazima wawe wasemaji au watangazaji washikamanifu wa ufalme wa Mungu kama Yesu Kristo na wafuasi wake wa kwanza. (Mathayo 4:17; 10:5-7; 24:14) Yehova anataka kila mtu apate kujua namna ufalme wake ulivyo na jinsi utakavyotatua matatizo ya wanadamu. Je! wewe umezungumza mambo uliyojifunza katika Neno la Mungu pamoja na watu wa ukoo wako, rafiki zako na wengine? Mungu anataka ufanye hivyo.—Warumi 10:10; 1 Petro 3:15.
19. (a) Sababu gani tunaweza kutazamia upinzani tunaposema na wengine juu ya ufalme wa Mungu? (b) Ni maulizo gani ambayo lazima wewe uyajibu?
19 Kristo na wafuasi wake wa kwanza walihitaji uhodari ili wazungumze na wengine juu ya Ufalme, kwa maana mara nyingi walipata upinzani. (Matendo 5:41, 42) Ndivyo ilivyo na leo. Ulimwengu huu unaotawalwa na Ibilisi hautaki habari njema za Ufalme zihubiriwe. Basi maulizo ndiyo haya: Wewe uko upande gani? Je! utaunga mkono ufalme wa Mungu kwa ushikamanifu? Yeye anataka ushuhuda mkubwa wa Ufalme utolewe kabla ya mwisho kuja. Je! wewe utashiriki kuutoa?
[Picha katika ukurasa wa 128]
Wale wanaokuwa raia za serikali ya Mungu lazima wapate maarifa ya kuijua
[Picha katika ukurasa wa 131]
Ni lazima raia za serikali ya Mungu waepuke vitendo vinavyolaumiwa na Mungu
[Picha katika ukurasa wa 131]
Lazima raia za serikali ya Mungu wawaambie wengine habari za serikali hiyo