Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 4/1 kur. 4-7
  • Namna Mahitaji Yetu Yatakavyojazwa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Namna Mahitaji Yetu Yatakavyojazwa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Serikali ya Ulimwengu
  • Tumaini la Akili Nzuri.
  • Utawala wa Mungu na Matokeo Yake
  • Je! Wewe Utakuwako?
  • Kuwa Raia wa Serikali ya Mungu
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Namna Ufalme wa Mungu Unavyoweza Kukufaidi Wewe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Serikali ya Mungu ya Amani
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Serikali ya Mungu—Tumaini Pekee La Wanadamu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 4/1 kur. 4-7

Namna Mahitaji Yetu Yatakavyojazwa

“BAADA ya miaka 30 ya ushirikiano wa kimataifa, hesabu ya watu wenye njaa inazidi kuongezeka,” alisema mkurugenzi mkuu wa Tengenezo la Chakula na Ukulima (FAO). Alikiri kwamba “kanuni ambayo imefuatwa mpaka sasa imeshindwa kuleta mafanikio.”

Hakuna jitihada zo zote za kimataifa zinazoweza kikweli kutatua matatizo ya kuwapa wanadamu wote mahitaji yaliyo ya lazima kwa sababu nia za sasa za mataifa ni za kujifikiria yenyewe tu. Kitu kingine kinahitajiwa. Kitu gani? Watu wengi wenye kufikiri wamekata maneno wakaona kwamba kinachohitajiwa ni:

Serikali ya Ulimwengu

Lazima kuwe na serikali ya ulimwengu yenye mamlaka na uwezo wa kusimamia mali za ulimwengu na kufanya mipango mizuri ya ugawaji wa bidhaa, ili kuhakikisha kwamba hakuna mtu anayepungukiwa. Je! inawezekana kuwa na serikali ya ulimwengu ya namna hiyo? Ushirika wa mataifa na tengenezo la Umoja wa Mataifa ni majaribio mawili yaliyofanywa ili kuwe na serikali ya ulimwengu. Lakini matengenezo hayo yameshindwa kabisa kutatua matatizo yaliyosababishwa na utukuzo wa taifa wenye choyo.

Kwa hiyo ni wapi serikali ya ulimwengu yenye matokeo mazuri inapoweza kupatikana? Ni wazi kwamba lazima itoke nje ya huu mfumo wa mambo ya ulimwengu. Lakini je! kuna mamlaka kama hiyo yenye uwezo wa kutayarisha serikali ya ulimwengu? Ndiyo, kuna mamlaka moja ambayo imekuwa ikionyesha inahangaikia sana wanadamu. Mamlaka hiyo ni Mungu.

Katika hii karne ya 20 yenye utafutaji mwingi sana wa vitu vya kimwili, huenda jambo hilo likasikika kuwa la kiajabu. Je! ni jambo la akili kutumaini kwamba kutakuwa na utawala wa ulimwengu mzima wenye kuongozwa na Mungu? Je! kuna ushuhuda wo wote wa kuonyesha kwamba angalau Mungu anapendezwa na kuwa mtawala wa ulimwengu? Na kama anapendezwa, je! utawala wake ungekuwa mzuri zaidi ya utawala wa wanadamu ambao tumeuvumilia kwa muda mrefu?

Tumaini la Akili Nzuri.

Katika akili za watu wengi​—hata za wengi wanaomwamini Mungu​—mambo ya kidini yako kando kidogo na namna mambo yalivyo hasa katika ulimwengu. Kwa mfano, ni sawa kwao kusema wanaenda mbinguni wanapokufa. Lakini wana maoni ya kwamba si jambo la akili nzuri kumtazamia Mungu achukue hatua fulani hapa duniani, kwa mfano kutawala ulimwengu. Je! hayo ndiyo maoni yako?

Je! umepata kufikiria ni kwa kiasi gani tunategemea sheria za Mungu hata sasa? Hewa tunayopumua, mvua, mwangaza wa jua na kila kitu kinachowezesha kuwe na uhai kinaongozwa na zile ambazo kwa kawaida zinaitwa sheria za maumbile, sheria za Mungu. Hata watu waseme au wasiseme wanaamini Mungu, wao wanamtegemea Mungu kabisa. (Mathayo 5:45; Matendo 14:17) Je! ni ajabu ikiwa Mungu, ambaye sheria zake zinaongoza upepo, mvua na jua, aliweka pia sheria za kuongoza mambo ya wanadamu?

Zaidi ya hilo, wewe ulijua kwamba, karibu miaka 3,500 iliyopita, Yehova Mungu alichagua kundi fulani la watu, akalipanga liwe taifa na kuwapa serikali ambayo yeye ndiye aliyekuwa Mfalme wake? Taifa hilo lilikuwa Israeli, na mmoja wa manabii wao aliandika baadaye hivi: “[Yehova] ndiye mwamuzi wetu; [Yehova] ndiye mfanya sheria wetu; ndiye atakayetuokoa.”​—Isaya 33:22.

Utawala wa Mungu na Matokeo Yake

Mambo yaliwaendeaje Waisraeli? Kwa muda ambao waliishika sheria ya Mungu, walifanikiwa katika kila njia. Baada ya miaka ya kwanza 45 ya kutawalwa na Mungu, mmoja wa viongozi wao alitoa habari hizi: “Halikuanguka neno lo lote katika jambo lo lote lililokuwa ni jema ambalo [Yehova] alikuwa amelinena katika habari ya nyumba ya Israeli; yalitimia mambo yote.”​—Yoshua 21:45.

Mambo yaliyowapata Waisraeli yanaonyesha ni jambo la akili sana kusema habari za kutawalwa na Mungu. Sawa na vile alivyolitawala moja kwa moja hilo taifa dogo la Mashariki ya Kati, yeye anaweza kuitawala dunia nzima. Je! ataitawala?

Miaka elfu mbili iliyopita mtume Mkristo Yohana alisikia jambo fulani linalotupa sababu thabiti ya kutuhakikishia kwamba Mungu atachukua hatua ya kusaidia wanadamu. Yohana alipewa njozi ya mambo yatakayokuja, na katikati ya njozi hiyo alisikia kelele hii ya shangwe: “Ufalme wa dunia umekwisha kuwa ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake, naye atamiliki hata milele na milele.” Ndipo Yohana aliposikia shukrani hizi za moyoni: “Tunakushukuru wewe, Bwana Mungu Mwenyezi, . . . kwa sababu umeutwaa uweza wako ulio mkuu, na kumiliki.”​—Ufunuo 11:15, 17.

Njozi hiyo​—iliyoongozwa na Mungu mwenyewe​—ilitabiri kuchukua kwa Mungu ‘ufalme wa ulimwengu.’ Ndiyo, yeye atakuwa mtawala wa ulimwengu, na “Kristo wake,” Yesu, atakuwa ndiye msimamizi aliyewekwa naye. Hivyo tuna uhakikisho thabiti kwamba Yehova Mungu atakuwa na serikali ya ulimwengu mzima.

Hiyo serikali ya ulimwengu itakayoongozwa na Mungu ndicho kichwa kikuu cha habari za Biblia. Yesu alitufunza kuiomba katika Sala ya Bwana aliposema hivi: “Ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.” (Mathayo 6:9,10) Yehova Mungu alitumia vinywa vya manabii wengi kuelekeza watu kwenye ufalme huu kuwa ndiyo njia ya pekee ya kutatulia matatizo yenye mizizi mirefu sana ya ulimwengu huu. Je! ufalme huo utakuwa na matokeo mazuri kuliko serikali za wanadamu? Ebu fikiria hilo.

Maji ya Kunywa Yehova Mungu ndiye Muumba wa dunia. Yeye anazielewa kabisa hali zote zinazohusiana na mazingira ya dunia. Yeye alimfunulia nabii Amosi kwamba ‘anayaita maji ya bahari, na kuyamwaga juu ya uso wa nchi.’ (Amosi 9:6) Anaelewa kabisa namna maji yanavyovutwa angani na jua kisha mvua inakunya halafu kawaida iyo hiyo inazidi kurudiwa-rudiwa. Anaweza kusimamia; vizuri kabisa kawaida hiyo.

Alipokuwa akiwatawala Waisraeli kwa njia ya moja kwa moja, yeye aliahidi hivi: “Atakufunulia [Yehova] hazina yake nzuri, nayo ni mbingu, kwa kutoa mvua ya nchi yako kwa wakati wake.” (Kumbukumbu la Torati 28:12) Kwa muda ambao watu wake waliendelea kuwa waaminifu yeye aliitimiza ahadi hiyo. Sawasawa na wakati huo, yeye anaweza kutoa uhakikisho kamili kwamba atawapa maji tele wote watakaokuwa chini ya serikali yake ya ulimwengu mzima.

Chakula Wataalamu wa mambo wanasema kwamba kimoja cha vipingamizi vikubwa kuliko vyote vya kulisha wenye njaa ni utukuzo wa taifa. Serikali ya ulimwengu mzima ya Mungu ina uwezo wa kuondolea mbali vizuizi hivyo. Nabii mwenye kuongozwa na Mungu aliandika hivi “[Mungu atanyosha mambo kuhusu] mataifa wenye nguvu walio mbali; nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.”​—Mika 4:3.

Je! jambo kama hilo linawezekana? Hakika linawezekana. Kwa kweli, linatukia sasa hivi! Kuna jamii ya watu mamilioni ulimwenguni pote ambao wamekwisha kujiweka chini ya ufalme wa Mungu. Wao hawachukui tena mambo kwa njia isiyo na fikira pana, wala kwa kutukuza mataifa yao wala makabila yao, bali wanachukuana mtu na mwenzake kuwa ndugu. Wanashirikiana kwa umoja kufanya mapenzi ya Mungu. Kuwako kwa jamii ya watu hao ni uthibitisho wa kwamba serikali ya ulimwengu mzima ya Mungu ni jambo halisi, lisilo la kuwazia tu. Watu hao ni akina nani? Tunawasema Mashahidi wa Yehova.

Yehova Mungu ameahidi kwamba ataibariki dunia kisha izae vitu tele. Alimtumia mtunga zaburi kusema hivi: “Dunia yenyewe kwa uhakika itatoa mazao yake.” “Kutakuja kuwa na nafaka tele juu ya dunia; juu ya kilele cha milima kutakuwa na mfuriko.” (Zaburi 67:6; 72:16, NW) Ndiyo, chini ya utawala wa ulimwengu mzima wa ufalme wa Mungu hakutakuwa na kipingamizi cha kuzuia mahitaji hayo ya maana kabisa yasitimizwe kwa wingi.

Mavazi na Mahali pa Kukaa Yesu alionyesha kwamba Mungu anahangaikia kwa upendo masilahi ya kimwili ya watumishi wake aliposema: “Fikirini maua ya mashamba, jinsi yameavyo; hayafanyi kazi, wala hayasokoti; nami nawaambia, ya kwamba hata Sulemani katika fahari yake yote hakuvikwa vizuri kama mojawapo la hayo. Basi, ikiwa Mungu huyavika hivi majani ya kondeni, . . . je! hatazidi sana kuwavika ninyi”?​—Mathayo 6:28-30.

Ndiyo, Mungu anawatunza watumishi wake hata sasa. Mashahidi wa Yehova wanaweza kuthibitisha kwamba hiyo ni kweli. Basi, kwa uhakika wakati serikali yake ya ulimwengu mzima itakapoitawala dunia, hakutakuwa na ukosefu wa kitu cho chote tunachohitaji ili tuwe wenye furaha.

Je! Wewe Utakuwako?

Je! serikali hiyo ya ulimwengu mzima inakupendeza? Hakika mtu ye yote mwenye kufikiri vizuri angependa kuishi chini ya mfumo wa namna hiyo. Hata hivyo, ni lazima kwanza tujifunze tuone katiba ya serikali hiyo ikoje. Katiba yenyewe imekwisha kuandikwa tayari katika Biblia Takatifu. Lazima tujifunze sheria zinazopasa kutiiwa ikiwa tunataka kuishi chini ya serikali ya Mungu.

Huenda jambo hilo likatutaka tufanye mabadiliko katika maisha yetu. Hali ya mtu kujifikiria yeye binafsi inayoonekana sana katika mfumo huu wa mambo haitakwi katika mpango wa Mungu. Ni lazima raia za ufalme wa Mungu wampende yeye kwa nafsi yao yote, na pia wapende jirani yao kama wao wenyewe. Zaidi ya hilo, tukiendelea kuwa katika mazoea kama kusema uongo, kuiba, kufanya uasherati, kudanganya watu katika mambo ya pesa, kulewa na kutumia vibaya dawa za kulevya hatutastahili kuishi chini ya serikali hiyo.​—Mathayo 22:37-39; 1 Wakorintho 6:9, 10.

Je! maisha ya wakati huo yanastahili kufanyiwa jitihada? Kabisa. Yehova Mungu peke yake ndiye anayejua namna maisha yanavyoweza kufurahisha katika sayari hii yakiwa chini ya serikali ya namna inayofaa. Katika Biblia yeye ameweka vionyesho fulani. Wale ambao sasa wanatumikia Mungu kwa unyofu wa moyo wamekwisha kuanza kuona kadiri fulani ya furaha na amani ya akili itakayokuwako wakati huo.

Kulingana na ushuhuda wote uliopo, karibuni sana wale wanaokuwa raia za ufalme wa Mungu watajionea hali zote hizo na kuzifurahia. Ndiyo, matukio yanayofanyika kwa kutimiza unabii wa Biblia leo yanaonyesha kwamba ufalme wa Mungu ni karibu na muda si muda utaanza uongozi wake kwa kuziondosha serikali za ulimwengu huu zilizogawanyika na zisizokuwa na matokeo mazuri. (Luka 21:25-28, 31; Danieli 2:44) Je! wewe ungependa kuzishiriki hali zote hizo? Basi jifunze kumwamini Yehova Mungu kwa uhakika na serikali yake ya ulimwengu mzima, kwa maana hiyo pekee ndiyo suluhisho la matatizo ya siku zetu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki