Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w80 7/1 kur. 9-15
  • Serikali ya Mungu—Tumaini Pekee La Wanadamu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Serikali ya Mungu—Tumaini Pekee La Wanadamu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • FUNDISHO KUU LA BIBLIA
  • FUNDISHO KUU TANGU MWANZO MPAKA MWISHO
  • MAARIFA KUHUSIANA NA UFALME YAONGEZEKA
  • MFALME WA SERIKALI YA MUNGU ATOKEA
  • TUMAINI LENYE KUANGAZA KATIKA GIZA
  • UTAWALA UNAOTOSHELEZA MAHITAJI YA WANADAMU
  • Serikali ya Mungu ya Amani
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Ufalme wa Mungu Watawala
    Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
  • Serikali Itakayoleta Paradiso
    Serikali Itakayoleta Paradiso
  • Namna Ufalme wa Mungu Unavyoweza Kukufaidi Wewe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
w80 7/1 kur. 9-15

Serikali ya Mungu—Tumaini Pekee La Wanadamu

1-3. (a) Matatizo yanayowapata wanadamu ni makubwa kadiri gani? (b) Wakati ujao unaweza kujulikanaje?

KIANGAZI kilichopita, katika baraza ya viongozi wa kisayansi na wa kidini katika Chuo cha Ufundi cha Masachusetts (Amerika), matatizo yanayouelekea ulimwengu yalisimuliwa kuwa ‘yakaribia sana kuwa ya maangamizi ya mwisho.’ Hakuna ‘maagizo ya kufuata ya kuokokea,’ Jerome R. Ravetz, mwalimu wa filosofia kutoka Chuo Kikuu cha Leeds katika Uingereza, akaonya. “Kadiri na ugumu wa matatizo ni kubwa sana hata kwamba akili ya mwanadamu haitayashinda.”

2 Basi, je! tutazamie nini wakati ujao? Kiongozi wa kidini wa United Church of Canada alidai hivi: “Hakuna awezaye kutabiri kwa uhakika kwamba siku nzuri inakuja. Kama ustaarabu utapotea au kama mwishowe kutakuwako jamii mpya yenye maisha tele kwa wote, liwalo lote hakuna anayefahamu kwa hakika.”

3 Lakini je! hiyo ni kweli? Hasha! Ukweli ni kwamba kuna Mtu anayefahamu wakati ujao utaleta mambo gani kwa sababu yeye yuna uwezo na hekima ya kuufanya kwa kulingana na mapenzi yake. Huyo Ndiye Muumba wetu, Yehova Mungu. Kwa sababu ya kutoweza kuliko wazi kwa wanadamu kuleta serikali nzuri, je! wewe hukubali kwamba huu ndio wakati wa kuanza kumsikiliza? Juu yake mwenyewe, Mungu anasema hivi: “Nitangazaye mwisho tangu mwanzo, na tangu zamani za kale mambo yasiyotendeka bado; nikisema, Shauri langu litasimama, nami nitatenda mapenzi yangu yote.” (Isa. 46:10) Nayo mapenzi ya Mungu ni kuwapa wanadamu serikali nzuri.

FUNDISHO KUU LA BIBLIA

4, 5. (a) Fundisho kuu la Biblia ni gani? (b) Linafahamishwaje kwa watu?

4 Ikiwa mtu angekuuliza hivi: ‘Ni nini fundisho kuu la Biblia?’ Ungesemaje? Kwa kupendeza, gazeti la kidini Modern Churchman lilisema hivi: “Msaada wa maana ambao wanafunzi wa mambo ya kidini wametoa wakati wa karne iliyopita umekuwa ni kuvumbua tena Ufalme wa Mungu kuwa fundisho kuu la Agano Jipya.’ Walakini je! wanafunzi wa mambo ya kidini na viongozi wa kidini wamekuwa wakifahamisha watu fundisho hilo la muhimu la Biblia? Ebu angalia jibu lililotolewa kujibu ulizo hilo na mwanadini wa kawaida mwenye sifa wa Presbyterian, akiandika katika gazeti Christianity and Crisis:

“Iwapo kumekuwako mabishano makali karibuni kati ya wanafunzi wa mambo ya kidini juu ya maana ya Ufalme na unavyohusu ulimwengu wetu sijapata kusikia. Na kwa habari ya mahubiri, kwa hakika imekuwa zaidi ya miaka thelathini tangu niliposikia mhubiri akijaribu kuwaeleza watu wake uhalisi wa Ufalme kwao. . . . Nikiwa mwanadini wa kawaida nawasihi wataalamu wetu wa elimu ya kidini na viongozi wetu wa kidini: Tuambieni juu ya Ufalme wa Mungu; tuelezeni ni nini na namna unavyohusiana na ulimwengu wa wakati wetu.”

5 Hata hivyo viongozi hao wa kidini hawajafanya hivyo! Wakati uchuguzi unapofanywa, ni vigumu kwa hata mwanakanisa mmoja kutambua ufalme wa Mungu ni nini, namna utakavyokuja, au utakayofanyia wanadamu. Kwa upande mwingine, gazeti hili lililo mkononi mwako limetenda kwa kulingana na kichwa chake Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova. Kwa ukawaida kurasa zake zimekazia ujumbe wa Ufalme. Kwa kweli serikali ya Mungu ndiyo fundisho kuu la Biblia.

FUNDISHO KUU TANGU MWANZO MPAKA MWISHO

6-9. (a) Ni matukio gani yaliyomfanya Yehova apange kuwe na serikali mpya? (b) Mwanzo 3:15 linatabiri juu ya nini, nao Ufunuo 12 unatusaidiaje kuufahamu utimizo wake?

6 Biblia inaanza kwa kusimulia matayarisho ya Mungu ya dunia kusudi ikaliwe na wanadamu na kuweka kwake wanadamu wawili wa kwanza katika makao ya bustani nzuri iliyoitwa Edeni. Walakini, kabla ya wenzi hao kuwa na watoto wo wote, mmojawapo wa malaika wa Mungu alitumia nyoka azungumze na mwanamke, Hawa, na kumshawishi auasi utawala wa Mungu. Naye mwanamke, akazungumza na mumewe, Adamu, na kumfanya ajiunge naye katika kuukataa uongozi wa Mungu, (Mwa. 3:1-6; Ufu. 12:9) Ilipokuwa hivyo, Yehova aliona kimbele uhitaji wa wakati ujao wa serikali mpya iliyopangwa na Mungu itawale juu ya wanadamu. Kwa hiyo, akisema na mwanzilishi wa uasi, malaika aliyejifanya mwenyewe Shetani Ibilisi, Mungu alisema hivi: “Nami nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako na uzao wake; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino.”​—Mwa. 3:15.

7 Lakini waweza kuuliza hivi: “Ni wapi katika unabii huo unapotuambia juu ya serikali mpya?” Ebu na tuuchanganue, nasi tutaona. Andiko hilo lasema kwamba kungekuwa uadui au chuki kati ya Shetani na “mwanamke,” na kati ya “uzao” wa Shetani, au watoto, na “uzao” wa mwanamke, au wazao. Kwanza kabisa, twahitaji kumtambua “mwanamke huyo.”

8 Yeye si mwanamke wa kidunia—Shetani hajapata kuwa na chuki ya kipekee kwa mwanamke ye yote wa kibinadamu. Mahali pake, huyo ni mwanamke wa mfano. Katika kitabu cha mwisho cha Biblia Ufunuo inasemwa juu yake kuwa “aliyevikwa jua, na mwezi chini ya miguu yake, na taji ya nyota kumi na mbili juu ya kichwa chake.” Ili kutusaidia kumtambua mwanamke huyo, angalia namna Ufunuo unavyoendelea kusema juu ya mtoto wake: “Kisha [mwanamke] huyo akajifungua mtoto wa kiume, ambaye atayatawala mataifa yote kwa fimbo ya chuma. Lakini mtoto huyo akanyakuliwa na kupelekwa kwa Mungu na kwenye kiti chake cha enzi.”​—Ufu. 12:1-5, HNNW.

9 “Mtoto” huyo ni nani—-huyo “mtoto” wa kiserikali—‘atakayeyatawala mataifa yote’ akiwa wakili wa Mungu? Ni ufalme wa Mungu kupitia kwa Kristo Yesu, kwa kulingana na tutakavyothibitisha baadaye. Kwa hiyo, mwanamke huyo wa kimbinguni ni tengenezo la Mungu la viumbe waaminifu wa kimalaika, ufalme wa Kimasihi ukiwa unazaliwa na tengenezo hilo. Hivyo, basi, huko nyuma wakati Adamu na Hawa walipoasi utawala wa Mungu, Yehova alichukua hatua ya kwanza na kuazimia kuwe na serikali ya Ufalme ambayo ingetumikia kama kitia nguvu na tumaini kwa wapenda haki.

MAARIFA KUHUSIANA NA UFALME YAONGEZEKA

10, 11. (a) Watumishi wa Mungu wa kale hawakutumaini falme gani, na kwa sababu gani? (b) Ni “mji” gani aliowatayarishia Mungu?

10 Yehova Mungu ametoa habari hatua kwa hatua juu ya serikali hiyo kwa watumishi wake, akiionyesha kuwa ndiyo peke yake wanadamu wanaweza kuitegemea kwa uhakika. Kwa kuwa Uwezo Wenye Nguvu Zote unahakikisha kufanikiwa kwake hakika, watumishi waaminifu wa Mungu hawakutumaini falme zilizofanywa na wanadamu. Walikiri waziwazi kwamba wao walikuwa wakingojea serikali ya Ufalme wa Mungu wa kimbinguni. Kwa mfano, mtume Paulo anaandika hivi juu ya hilo:

“Hawa wote wakafa katika imani [hawa watumishi waaminifu wa Mungu wa kabla ya Ukristo], wasijazipokea zile ahadi, bali wakaziona tokea mbali na kuzishangilia, na kukiri kwamba walikuwa wageni, na wasafiri juu ya nchi. . . . Waitamani nchi iliyo bora, yaani, ya mbinguni. Kwa hiyo Mungu haoni haya kuitwa Mungu wao; maana amewatengenezea mji.”​—Ebr. 11:13-16.

11 Ni “mji” gani huo ambao Mungu amewatayarishia watumishi wake hao wa kale? Ni ufalme wa kimbinguni wa Mungu, serikali yake. Ebu tufuatishe matayarisho yaliyofanywa kwa ajili ya kusimamishwa kwa serikali hiyo ya Ufalme. Kama ilivyotangulia kuonyeshwa katika barua ya Paulo kwa Waebrania, watumishi wa Mungu wa kale ‘hawakuzipokea zile ahadi’ zilizohusu Ufalme huo. Ahadi zipi?

12-14. Ni ahadi gani zilizotolewa kwa Ibrahimu, Isaka, Yakobo, Yuda na Daudi juu ya serikali ya Mungu?

12 Katika Mwanzo 22:18 Yehova alimwahidi Ibrahimu hivi: “Katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia.” Mtume Paulo, katika barua yake kwa Wagalatia, alimtambulisha Yesu Kristo kuwa mzao wa Ibrahimu, ambaye kupitia kwake mataifa yangejibarikia. (Gal. 3:16) Ahadi kama hizo juu ya “uzao” wenye kuja wa baraka zilitolewa kwa mwana wa Ibrahimu Isaka na mjukuu wake Yakobo. (Mwa. 26:3-5; 28:13, 14) Hivyo, kama inavyoonyeshwa na ahadi hizo, “uzao” wa mwanamke wa Mungu ulipaswa uje kupitia kwa nasaba ya Isaka na Yakobo.

13 Angalia ahadi zaidi iliyotolewa kwa mwana wa Yakobo, Yuda: “Fimbo ya enzi haitaondoka katika Yuda, wala mfanya sheria kati ya miguu yake, hata atakapokuja Yeye, mwenye milki [Shilo], ambaye mataifa watamtii.” (Mwa. 49:10) Yesu Kristo, ‘aliyetokana na Yuda,’ alipata kuwa huyo ‘Shilo’ “ambaye mataifa watamtii.” Na angalia namna jambo hilo linavyothibitishwa zaidi katika Biblia.​—Ebr. 7:14.

14 Karibu miaka 700 baada ya ahadi hiyo iliyotolewa kwa Yuda, Yehova alisema hivi kuhusiana na Daudi wa kabila la Yuda: “Nimemwona Daudi, mtumishi wangu, nimempaka mafuta yangu matakatifu. Ambaye mkono wangu utakuwa thabiti kwake, na mkono wangu utamtia nguvu. Wazao wake nao nitawadumisha milele, na kiti chake cha enzi kama siku za mbingu” (Zab. 89:20, 21, 29) Wakati Mungu anaposema “wazao” wa Daudi watadumishwa “milele,” na “kiti chake cha enzi” kikidumu “kama siku za mbingu,” anazungumza juu ya kudumu kwa serikali ya Ufalme mikononi mwa mtawala wake aliyewekwa, Yesu Kristo. Twajuaje?

MFALME WA SERIKALI YA MUNGU ATOKEA

15, 16. (a) Twajuaje kwamba Yesu Kristo ndiye “mzao” wa Daudi? (b) Sababu gani Yohana angeweza kutangaza, ‘‘Ufalme wa mbinguni umekaribia”?

15 Basi, fikiria jambo lililotokea katika karne ya kwanza ya Wakati wa Kawaida wetu. Yehova alimtuma malaika wake Gabrieli amwambie bikira Mariamu juu ya mtoto ambaye angezaliwa naye kwa njia ya mwujiza. “Jina lake utamwita Yesu,” Gabrieli akasema. “Huyo atakuwa mkuu, ataitwa Mwana wa Aliye juu, na Bwana Mungu atampa kiti cha enzi cha Daudi, baba yake. Ataimiliki nyumba ya Yakobo hata milele, na ufalme wake utakuwa hauna mwisho.” (Luka 1:31-33) Wakati wa kuzaliwa kwa Yesu ‘malaika wa Yehova’ aliwaambia wachungaji kwamba huyo alikuwa ndiye Masihi aliyeahidiwa, Mwokozi na Bwana.​—Luka 2:8-12.

16 Kwa hiyo serikali ya Mungu ilianza kuchukua maana hakika katika karne ya kwanza. Kwa wakati wake, Yohana Mbatizaji akaanza kuhubiri hivi: “Tubuni; kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia.” (Mt. 3:1, 2) Sababu gani Yohana angeweza kusema hivyo? Kwa sababu Mfalme-mkusudiwa wa serikali hiyo alikuwa katikati yao. Baada ya Yohana kumbatiza Yesu, Mungu aliimimina roho yake takatifu ili kumtia Yesu mafuta kuwa Yule ambaye angekuwa mfalme wa serikali ya kimbinguni. Kisha, wakati wa huduma ya miaka mitatu na nusu, Kristo alizionyesha sifa zake za kuwa mfalme kwa uaminifu wake kwa Mungu mpaka kufa, wakati Nyoka yule alipomjeruhi katika kisigino. (Mwa. 3:15) Tangu kufufuliwa kwake kwenye uzima mbinguni, Kristo yu katika hali ya kufikiliza mapenzi ya Babaye ‘kuvunja falme hizi zote za wanadamu vipande vipande na kuziharibu’ ili kuifungulia njia serikali inayokuja ya ulimwengu ya Mungu. Dan. 2:44; Mt. 6:9, 10.

17. Ni ufunuo gani zaidi uliotolewa juu ya washiriki wa serikali ya Mungu?

17 Ufunuo mwingine juu ya Serikali hiyo ni kwamba wengine kutoka kati ya wanadamu watakuwa na pendeleo la kutawala pamoja na Kristo kama wafalme. Kupitia kwa nabii wake Danieli, Mungu alionyesha kwamba watu wanaoitwa “watakatifu” watatawala pamoja na Mwanawe. (Dan. 7:13, 14, 27) Vilevile, Kristo alitoa ahadi kama hiyo kwa mitume wake waaminifu. (Luka 22:28-30) Mtume Paulo alieleza hivi kwa Wakristo waliotiwa mafuta, katika barua yake kwa Wagalatia: “Na kama ninyi ni wa Kristo, basi, mmekuwa uzao wa Ibrahimu.” Hivyo Paulo alionyesha kwamba, ijapokuwa kwanza kabisa Kristo ndiye mzao aliyeahidiwa, Mungu angechagua wengine washiriki naye kama “warithi wa ufalme.” (Gal. 3:16, 29; Yak. 2:5) Kwa kupatana na hilo, Paulo alimwandikia Timotheo hivi: “Tukiendelea kuvumilia, tutatawala pia pamoja naye [kama wafalme].” (2 Tim. 2:12, HNWW) Baadaye mtume Yohana aliandika juu ya wale watakaotawala kama wafalme “juu ya nchi” pamoja na Kristo Yesu, akitaja hesabu yao kuwa 144,000,—Ufu. 5:10; 14:1-3.

TUMAINI LENYE KUANGAZA KATIKA GIZA

18-20. (a) Fundi wa umeme alielezaje kwa ufupi juu ya fundisho kuu la Biblia? (b) Ni nani peke yao wanaohubiri ujumbe wa Ufalme?

18 Je! si inapendeza namna Mungu alivyofunua kusudi lake kuu la kusimamisha serikali yenye haki kwa ajili ya faida ya milele ya wale wanaompenda na kumtumaini? Hata hivyo inasikitisha kama nini namna viongozi wa kidini na wataalamu wa elimu ya kidini wasio na imani walivyoshindwa kufahamisha makundi yao kusudi hilo! Hivyo watu hao, wakiwa na akili zenye giza na pasipo maarifa ya Ufalme huo, wameweka tumaini lao katika serikali za kibinadamu moja baada ya nyingine, wakajiletea hasara na kujikatisha tamaa. Hata hivyo, je! wewe, unathamini ujumbe wa Biblia? Ungejibuje iwapo mtu angekuuliza, ‘Ni nini fundisho kuu la Biblia?’

19 Miaka michache iliyopita mmoja wa Mashahidi wa Yehova, fundi wa umeme (stimu) katika duka moja huko Dayton, Ohio (Amerika), alipata nafasi nzuri ya kutoa jibu. Aliulizwa na mhariri wa gazeti la duka hilo aandike juu ya kitabu kinachofurahisha zaidi alichosoma karibuni, Yeye aliandika hivi:

“Sitamaliza kamwe kukisoma kitabu hicho maishani mwangu mwote. Kinaanza kwa kueleza namna makao mazuri yalivyoharibiwa na uasi. Mkasa, msiba, huzuni, uuaji na kifo yafuata. Jamaa inapoongezeka, kutumbukia katika kukata tamaa na giza kwaongezeka. Karne nyingi zapita, mataifa yatokea na kutoweka, maelfu ya watu yapita maono ya wanadamu ya ndani ya kila namna kuanzia na chuki mbaya sana ya waziwazi hata upendo wa mfia imani yaonekana. Tumaini, likianza kama kaa lenye kuwaka kidogo tu, laongezeka na kuwa uhakika kamili. Serikali kamilifu itarudisha tena yale makao mazuri. Mtawala wake ni Mfalme, Kristo Yesu. Serikali hiyo, ni Ufalme wa Mungu. Jamaa hiyo, ni jamii ya kibinadamu. Kitabu hicho ni Biblia!”

20 Fundi huyo wa umeme alitoa ushuhuda mzuri kama nini juu ya ufalme wa Mungu na yale utakayofanyia wanadamu! Kweli kweli, serikali ya Mungu ndiyo tumaini pekee la kufurahia maisha kikamilifu, pamoja na furaha ya kweli! Huo ndio ujumbe ambao Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakitangaza ulimwenguni pote kwa kupatana na unabii wa Yesu: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mt. 24:14, NW) Ndiyo, karibuni serikali zote za kibinadamu zitakomeshwa—kwa kuwa zimeshindwa kutosheleza mahitaji ya watu. Hiyo itaanzisha taratibu mpya yenye haki chini ya uongozi wa Mfalme wa kimbinguni, Yesu Kristo, na watawala wenzake. O, ni heshima kama nini kuwa raia wa serikali hiyo ya Mungu! Chunguza kwa ufupi baraka ambazo Biblia inasema itawamiminia wanadamu.

UTAWALA UNAOTOSHELEZA MAHITAJI YA WANADAMU

21, 22. (a) Tofauti na jitihada za kibinadamu, Ufalme huo utafauluje katika kuondoa vita, uvunjaji wa sheria na woga? (b) Matokeo ya utawala wa Mungu juu ya wanyama yatakuwa nini?

21 Katika Zaburi 46:8, 9, NW tunaalikwa tuzichunguze kazi za Yehova: “Njoni, enyi watu, yatazameni matendo ya Yehova, jinsi alivyoweka matukio yenye kustaajabisha duniani.” Nayo baadhi ya matukio hayo yenye kustaajabisha ni yapi? “Yeye avifanya vita vikome mpaka mwisho wa dunia.” Serikali za kibinadamu zimeshindwa kwa kusikitisha kukomesha vita. Bali Mungu hatashindwa kuleta amani ya kudumu, kwa kuwa mtunga zaburi anasema hivi: “Watenda mabaya wataharibiwa, . . . asiye haki hatakuwapo.” (Zab. 37:9, 10) Jamii ya kibinadamu haitakuwa na magereza, polisi, kufuli milangoni, ndiyo, haitakuwa na woga. Hivyo, ahadi ya Mungu ni kwamba chini ya utawala wake wa Ufalme wale watakaokuwa wakiishi watafurahia maisha, “hapana mtu atakayewatia hofu.”​—Mik. 4:4.

22 Hata leo watu wenye maelekeo ya kinyama, kwa kutumia Neno la Mungu maishani mwao, wanajifunza kuishi kwa amani na wengine. Neno la Mungu linaonyesha kwamba chini ya utawala wa Ufalme, hata wanyama wataishi kwa amani. “Mbwamwitu atakaa pamoja na mwana-kondoo,” Biblia yasema, “na chui atalala pamoja na mwana-mbuzi; ndama na mwana-simba na kinono watakuwa pamoja, na mtoto mdogo atawaongoza.” Hakika hakuna serikali yo yote ya kibinadamu inayoweza hata kutumaini kutimiza jambo hilo!—Isa. 11:6.

23. Ni uwezo gani wa mtawala mpya wa dunia utakaohakikisha chakula tele kwa raia zote za Ufalme?

23 Jambo jingine linalohitajiwa katika ulimwengu ambao sote tungependa kuishi ndani yake ni kuwako kwa chakula cha kutosha wote. Serikali za kibinadamu zimeshindwa kuondoa ukosefu wa chakula na njaa, walakini utawala wa Ufalme hautashindwa. Wakati Yesu alipokuwa duniani, alionyesha kwamba, kupitia kwa roho ya Mungu, angeweza kuongoza upepo na bahari, mimea na samaki. Ebu wazia jambo hilo litamaanisha nini chini ya Ufalme! Duniani pote kutakuwa uongozi mkamilifu wa hali ya hewa, jambo ambalo litamaanisha kwamba hakutakuwa kuharibika kwa mazao. Nalo hilo, litahakikisha chakula tele kwa kila mtu. Biblia inasema: “Na uwepo wingi wa nafaka katika ardhi juu ya milima.”​—Zab. 72:16.

24-26. Ufalme utafanyia nini wagonjwa, vilema, bubu, na hata wanaozeeka?

24 Serikali za kibinadamu zimeshindwa kuweka huru jamii ya kibinadamu kutokana na magonjwa na maradhi, takwa la lazima la kufurahia maisha yenye furaha kweli kweli. Hata hivyo, alipokuwa duniani Yesu aliponya kila namna ya udhaifu, kuonyesha namna atakavyofanya duniani pote ili kutoa afya na uzima kwa raia zake zote. Chini ya utawala wa Ufalme ahadi hii ya Biblia itatimizwa kwa halisi: “Hapana mwenyeji atakayesema, mimi mgonjwa.” (Isa. 33:24) Ndiyo, hakutakuwa gharama za daktari na tabibu wa meno! Hakutakuwako tena kliniki, hospitali na gharama za hospitali!

25 Leo kuwa mzee kwaweza kuwa jambo lenye kutaabisha sana. Kama vile mwanamke mmoja alivyoandika: “Miye si wa namna ile ya kushuka moyo, lakini jambo hilo lanipata sasa nami nafahamu kwa nini hivyo, nazeeka. . . . Maumivu na uchungu wa kawaida hayanisumbui sana kama vile sura yangu. Nilikuwa mzuri sana nilipokuwa mchanga walakini si wakati huu. Nina mistari na makunyanzi ambayo hakuna upasuaji wo wote wa kuleta umbo zuri unaoweza kuyaondoa nazo nywele zangu zinakuwa na mvi. . . . Naweza kuondoaje masikitiko hayo?”—New York Post, Machi 23, 1979.

26 Ukweli ni kwamba, ufalme wa Mungu ndio suluhisho pekee la hakika la matatizo hayo. Chini ya utawala wake hali ya kuzeeka itaondolewa kwa uwezo wa Mungu, hata kwamba mwili na akili vitarudishwa upya kwenye ukamilifu! Watu watarudishwa kwenye afya kamili hata kwamba ‘nyama za mtu zitakuwa laini kuliko wakati wa ujana wake.’ (Ayubu 33:25) Hali zitakuwa kama zile zinazosimuliwa katika Isaya 35:5, 6: “Macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya vizuri yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema atarukaruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.”

27. Kuna ushuhuda gani kwamba hata kifo kitashindwa?

27 Walakini huenda mtu akasema, “Ikiwa watu wasingepatwa na magonjwa, au kuzeeka, basi wasingekufa.” Asema kweli. Hivyo ndivyo itakavyokuwa kabisa. Viongozi wa mazishi, au wazikaji, watapaswa kutafuta namna mpya za kazi, kwa sababu Mungu anaahidi hivi: “Mauti haitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Ufu. 21:4) Mtunga zaburi alisema hivi juu ya Yehova: “Waufumbua mkono wako, wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake.” (Zab. 145:16) Ebu wazia hilo linamaanisha nini! Mahitaji ya kweli na tamaa za kila mtu zitatoshelezwa, na zaidi kuliko vile ye yote wa sisi wanadamu wasiokamilika awezavyo kuwazia sasa.

28, 29. (a) Ni baraka gani nyingine ambazo zimetamaniwa kwa muda mrefu zitakazotimizwa na Ufalme? Kuna ushuhuda gani kwamba wafu watafufuliwa? (Luka 7:11-15; 8:49-56)

28 Furaha kama nini! Chini ya hali zenye haki za utawala wa Ufalme watoto watapewa nafasi ya kujifunza na kukua hata ukamilifu, bila ukosefu wa usalama wa ulimwengu huu na hatari za barabara za miji yake. Hakutakuwako tena kuogopa kuangukia utumwa wa dawa za kulevya au uvutano wa mashirika mabaya yenye kupotoa! Kila mwanadamu atakuwa na nafasi ya kusitawisha uweza na karama zake kikamilifu, na kutakuwako utendaji unaopendeza, wenye kuthawabisha kwa wote. Nabii Isaya alionyesha yale ambayo utawala wa Ufalme waweza kufanya, akisema: “Nao watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. . . . Maana kama siku za mti ndivyo zitakavyokuwa siku za watu wangu, na wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi.”​—Isa.65:17-25.

29 Hiyo ni ahadi ya heshima na kusudi kwa kila mwanamume, mwanamke na mtoto. Maisha haya ya zamani hayatakumbukwa tena. Mwanadamu atajenga, kupanda na kuvuna vitu ambavyo vitaendelea kuwa vyake mwenyewe. Watoto watalelewa katika mazingira yenye utulivu, yenye kufaa afya. Hata wafu watafufuliwa! (Yohana 5:28, 29) Akina baba na akina mama, ndugu na dada, wajomba na shangazi, rafiki na jirani kuanzia wakati wa Abeli mpaka wakati uu huu, wote wakiungana hapa duniani ili wajifunze juu ya baraka za utawala wa Ufalme! Itakuwa siku nzuri kama nini!

30. (a) Kusudi la Mungu la kwanza juu ya dunia litatimizwa kwa njia gani? (b) Tumaini la Ufalme linakuchochea wewe kufanya nini?

30 Hakuna serikali ya kibinadamu inayothubutu kuwazia kutimiza mambo hayo kwa ajili ya raia zake! Ni Mungu tu awezaye kuhakikisha kutimizwa kwa ahadi hizo! Na zaidi, chini ya utawala wa Ufalme wanadamu wote wataungana katika kumwabudu Yehova. Chini ya usimamizi wake wa kimbinguni, dunia yenyewe itabadilishwa polepole kuwa dunia iliyo paradiso, Bustani ya Edeni kuzunguka dunia yote! Wote watakaoishi watafurahia afya kamili na uzima wa milele chini ya ufalme wa Mungu. Kweli kweli ni tumaini zuri sana! Na chanzo chake ni chenye kutegemeka sana sana, Yehova Mungu mwenyewe.

[Picha katika ukurasa wa 11]

Ibrahimu aliuona ufalme huo “tokea mbali.”​—Ebr. 11:13-16

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki