Maswali Kutoka kwa Wasomaji
● Mithali hii inamaanisha nini inaposema: “Mpige mwenye mzaha, na mjinga atapata busara; mwonye mwenye ufahamu, atatambua maarifa”?
Mithali hii inapatikana katika Mithali 19:25, nayo inavuta fikira zetu kwenye njia mbili za kufundisha. Wazazi wanapaswa kujua njia hizi mbili.
Kama vile mithali inavyotangulia kusema, ili mtu asiye na ujuzi au mjinga ajifunze uhitaji wa kuepuka kufanya makosa, huenda akalazimika kuona mkosaji mwenye shingo ngumu na mwenye dhihaka (mzaha) akiadhibiwa. Tendo hilo lenye nguvu linamfundisha huyo asiye na ujuzi. Huenda kwake kikawa kizuizi chenye nguvu. Walakini, mwenye ufahamu, hahitaji somo la onyo lenye nguvu namna hiyo. Mara nyingi inatosha kusikia tu maneno yenye kukaripia; anakubali shauri upesi na kulitumia.
Wazazi wengi wameona ukweli wa maneno haya, nao wengine huenda wakafanya hivyo wakati ujao na kufaidika kwa kutumia mithali hii. Ili ajifunze kuepuka mwendo wenye makosa, mara nyingi mtoto anahitaji kuonana na adhabu yenye nguvu, kama vile mapigo (ama kuiona akipewa mwingine, au yeye mwenyewe). Ijapokuwa adhabu ya namna hiyo huenda isipendeze mwanzoni kwa wote wawili mtoto na wazazi, matokeo yanaweza kuonyesha kwamba ilistahili kutolewa. (Ebr. 12:11) Mtoto anaweza kuletwa katika hali inayoelezwa mwishoni mwa Mithali 19:25.
Mara nyingi mtoto anaposahihishwa na kuongozwa kwa uthabiti na wazazi wake, anafanya maendeleo kufikia wakati ambapo anaweza kujifunza kutokana na maneno ya makaripio au ya mashauri ya wazazi wake. Lo! somo jema namna gani la kujifunza tunapokuwa wachanga!