Mahubiri ya Mlimani—‘Iweni Wakamilifu’: Wapendeni Adui Zenu
BAADA ya kusema kwamba wasikilizaji wake hawakupaswa ‘kushindana na mtu mwovu,’ Yesu aliongeza hivi: “Mmesikia kwamba imenenwa, Umpende jirani yako, na umchukie adui yako.”—Mt. 5:39,43.
Wale waliokuwapo wakati Mahubiri ya Mlimani yalipokuwa yakitolewa walikuwa Wayahudi ambao walikuwa ‘wamesikia’ amri ya Mungu: “Usifanye kisasi, wala kuwa na kinyongo juu ya wana wa watu wako; bali umpende jirani yako kama nafsi yako.”—Law. 19:18.
Walakini, viongozi wa kidini Waisraeli walisisitiza uhakika wa kwamba “wana wa watu wako” na “jirani yako” ilihusu wayahudi peke yao. Walisisitiza vilevile kwamba amri nyingine za sheria ya Mungu ziliwahitaji Waisraeli wajitenge na yale mataifa mengine. (Kum. 7:1-4) Ijapokuwa hii ilimaanisha kujitenga kwa Israeli kama taifa kati ya jamii nyingine za mataifa, mwishowe maoni yalitokea kwamba wote wasio Wayahudi walikuwa ‘adui,’ waliopaswa kuchukiwa kama watu mmoja mmoja. Mfano wa maoni haya unaonyeshwa na maneno haya yafuatayo katika kitabu kiitwacho The Mishnah:
“Ng’ombe hawezi kuachwa mahali pa kulala watu wa mataifa kwa kuwa inashukiwa kwamba wana mazoea ya kulala na wanyama; wala mwanamke hawezi kuachwa peke yake pamoja nao kwa maana inashukiwa kwamba wao ni wafisadi; wala mwanamume hawezi kuachwa nao akiwa peke yake kwa maana inashukiwa kwamba wao ni wamwagaji wa damu. Binti Mwisraeli hawezi kumsaidia mwanamke mtaifa anapozaa kwa maana angekuwa akisaidia kuzalisha mtoto kwa ajili ya ibada ya sanamu, lakini mwanamke mtaifa anaweza kumsaidia binti Mwisraeli. Binti Mwisraeli hawezi kumnyonesha mtoto wa mwanamke mtaifa, walakini mwanamke mtaifa anaweza kumnyonyesha mtoto wa binti Mwisraeli katika makao yake huyu.”—Kijitabu Abodah Zarah (“Ibada ya Sanamu”) 2:1.
“Lakini mimi nawaambia,” akasema Yesu akitoa tofauti inayosisimua, “Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi.” (Mt. 5:44) Hapa tunaona ushuhuda zaidi wa kwamba Mwana wa Mungu alikuja, si “kutangua, bali kutimiliza” Sheria ya Mungu iliyoandikwa, kwa maana Sheria hiyo iliamuru kuwatendea wageni kwa fadhili na huruma.—Mt. 5:17; Kut. 22:31; 23:4, 5; Law. 19:33, 34; Kum. 10:19.
Walakini Yesu hakuwa na kusudi la kutoa kanuni hii iwahusu Mataifa walio adui za Israeli peke yao. Yeye alitaka wafuasi wake wawatendee kwa upendo watu wote ambao wangeonyesha uadui. Akiandika sana sana kwa ajili ya watu wasio Wayahudi, Luka anayaandika maneno ya Yesu hivi: “Lakini nawaambia ninyi mnaosikia, Wapendeni adui zenu, watendeeni mema wale ambao wawachukia ninyi, wabarikieni wale ambao wawalaani ninyi, waombeeni wale ambao wawaonea ninyi.”—Luka 6:27, 28.
Kulingana na maneno ya Yesu, wale waliokuwa ‘wakisikia,’ yaani, wale waliokuwa wakiyaweka maneno yake moyoni kweli kweli, iliwapasa waelekeane na namna tatu za chuki kwa kuonyesha namna tatu za upendo: (1) ‘Kuwatendea mema wale wanaowachukia,’ kuelekeana na uadui wa adui kwa matendo ya fadhili. (2) Chuki ikitokeza maneno ya kutusi, ‘wawabariki wale wanaowalaani. Mahali pa kulipa laana kwa laana wafuasi wa Yesu wanapaswa kusema na wapinzani wao kwa fadhili na huruma. (3) Uadui ukienda zaidi ya matusi utokeze mateso ya wafuasi wa Kristo kwa kutumia jeuri au matendo mengine ya ‘uonezi,’ inawapasa ‘wawaombee’ watesi wao kwa upendo wakimwomba Mungu kwamba wapinzani wao wabadilike moyoni na kupata kibali ya Mungu.—Linganisha Warumi 12:14-21; 1 Wakorintho 4;12; 1 Petro 3:8, 9.
Ndipo Yesu alipotoa sababu ya maana sana kwa nini inatupasa kuonyesha adui zetu upendo. “Ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni.” (Mt. 5:45a) Kwa ajili ya wasomaji wa Mataifa wasio Wayahudi, Luka anatumia maneno ‘Aliye Juu,’ mahali pa “Baba yenu aliye mbinguni.”—Luka 6:35a.
Watu wanaotii shauri la Yesu wanakuwa “wana” wa Mungu katika maana ya kwamba wanamwiga kwa kuonyesha wema wake usiobagua kuelekea rafiki na adui pia. (Linganisha Mathayo 5:9; Waefeso 4:31–5:2; 1 Yohana 3:9-12.) Mungu anaweka mfano mwema kabisa kwa maana “yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki.” (Mt. 5:45b); “Yeye ni mwema kwa wasiomshukuru na waovu.”—Luka 6:35b.
Akikazia namna lilivyo jambo la maana kwamba wasikilizaji wake ‘waendelee kuwapenda adui zao,’ Yesu aliongeza hivi: “Maana mkiwapenda wanaowapenda ninyi, mwapata thawabu gani? Hata watoza ushuru je! nao hawafanyi yayo hayo? Tena mkiwaamkia ndugu zenu tu, mnatenda tendo gani la ziada? Hata watu wa mataifa, je! nao hawafanyi kama hayo.”—Mt. 5:46, 47.
Watu wanaotaka kumwiga Mungu haiwapasi kuonyesha upendo watu wale wanaowaonyesha upendo peke yao. Hiyo haiwezi kuwastahilisha “thawabu” yo yote ya pekee au kibali ya Mungu. Hata “watoza ushuru” walikuwa na desturi ya kuwapenda wale waliokuwa wakiwapenda, ijapokuwa Wayahudi waliwaona hawa kuwa kati ya watu waliodharauliwa zaidi.—Luka 5:30; 7:34.
Salamu ya kawaida kati ya Waisraeli ilitia ndani neno shalom (“amani”), ambalo lilimtakia afya, hali njema na ufanisi mtu aliyeamkiwa. Kuamkia watu walioonwa kuwa “ndugu” peke yao kwa salamu hiyo halingekuwa “tendo la ziada,” kwa maana jambo ilo hilo lingeonekana hata kati ya “watu wa mataifa” ambao walionwa na Wayahudi kuwa hawana Mungu, wachafu na wa kuepukwa.
Luka aliyeandika Injili yake akiwafikiria watu wasio Wayahudi, anatumia usemi “wenye dhambi” ambao ni wa kawaida, mahali pa semi “watoza ushuru” na “watu wa mataifa” (ambazo kwa habari hii zingefahamika na Wayahudi peke yao). Twasoma hivi: “Maana mkiwapenda wale wawapendao ninyi, mwaonyesha fadhili gani? Kwa kuwa hata wenye dhambi huwapenda wale wawapendao. Nanyi mkiwatendea mema wale wawatendao mema, mwaonyesha fadhili gani? Hata wenye dhambi hufanya vivyo hivyo. Na mkiwakopesha watu huku mkitumaini kupata kitu kwao, mwaonyesha fadhili gani? Hata wenye dhambi huwakopesha wenye dhambi ili warudishiwe vile vile.”—Luka 6:32-34.
Yesu alimalizia sehemu hii ya Mahubiri ya Mlimani kwa usemi huu: “Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.”—Mt. 5:48.
Hii si amri kwa wanafunzi wa Yesu ya kuwataka wawe bila upungufu kimwili na kiadili, kwa kuwa katika wakati huu hilo haliwezekani kwa sababu ya dhambi iliyorithiwa. (Rum. 3:23; 5:12) Tofauti na hilo, maneno hayo yanawatia watu moyo kumwiga ‘Baba wa mbinguni,’ Yehova, wakamilishe upendo wao, waufanye ufikie kiasi kamili na kuufanya kamili kabisa kwa kuwatia ndani hata adui zao. Kupatana na hilo, masimulizi ya Luka yanayofanana na hayo yasema hivi: “Basi, iweni na huruma, kama Baba yenu alivyo na huruma.”—Luka 6:36.