Kuwa na mwenendo wa kimungu kuwaelekea wengine
‘‘Mimi ninakuandikia wewe . . . kwamba upate kujua jinsi inavyokupasa ujiendeshe mwenyewe katika jamaa ya Mungu, ambayo ndilo kundi.”—1 Tim. 3:14, 15, NW.
1, 2. Biblia inaweza kutusaidiaje katika shughuli zetu na wengine?
KATI ya faida ambazo Wakristo wanapata katika kujifunza Biblia ni kwamba wanapata kuijua njia ya kimungu ya kushughulika na wanadamu wale wengine. Hata watu wasioufahamu sana Ukristo wala Biblia wanaikubali hekima na kufaa kwa shauri kama hili: “Kama mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni vivyo hivyo.”—Luka 6:31.
2 Biblia haitoi habari za ujumla tu bila kuonyesha waziwazi mwenendo tunaopaswa kuwaonyesha wengine. Inatushauri jinsi tunavyopaswa kujiendesha kuelekea watu mmoja mmoja walio katika uhusiano fulani nasi unaotajwa waziwazi, au tunavyopaswa kujiendesha katika hali fulani fulani. Kwa mfano, inatoa mauidha (maoni) juu ya mwenendo ambao mke Mkristo anapaswa kumwonyesha mumewe asiyeamini, na mashauri juu ya mwenendo tunaopaswa kuwa nao kuwaelekea watu wa hali za chini, walio viwete na kuwaelekea wanaume au wanawake. (1 Pet. 3:1-6; Zab. 41:1; Law. 19:14; 1 Tim. 5:1, 2) Maandiko yanatoa pia mashauri mengi yenye kufaa juu ya jinsi tunavyopaswa ‘tujiendeshe wenyewe katika jamaa ya Mungu, ambayo ndilo kundi.’—1 Tim. 3:15, NW.
3. Kwa sababu gani tunahitaji uongozi wa Mungu kuhusu mwenendo wetu?
3 Ni jambo la maana sana kutumia mashauri hayo ya kimungu, kwa maana, kusema kwa ufupi, linaonyesha kwamba yeye atatuhukumu sisi kwa kutegemea jinsi tunavyojiendesha wenyewe kuwaelekea wale wengine. (Mt. 18:35; 25:40, 45; Ufu. 2:23) Kwa hiyo, badala ya kuongozwa ama na yale ambayo mwanadamu anasema tunapaswa kufanya, ama na maoni yetu ya moyoni na yale ‘tunayojisikia’ yanafaa, inatupasa tuwe na nia ya Daudi: “Ee [Yehova], unijulishe njia zako, unifundishe mapito yako, uniongoze katika kweli yako, na kunifundisha. Maana Wewe ndiwe Mungu wa wokovu wangu.”—Zab. 25:4, 5; 139:17, 21.
KUSHUGHUUKA NA WATENDA DHAMBI
4. Kwa sababu gani tunahitaji sana kujua habari za kushughulika na watenda dhambi?
4 Wakiwa ni wazao wa Adamu, wanadamu wote “wametenda dhambi na hupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Rum. 3:23, NW; 5:12) Ingawa hivyo, hali yetu haikosi kuwa na tumaini kwa maana “Kristo Yesu alikuja ulimwenguni awaokoe wenye dhambi.” Kila mtu anayelitambua jambo hilo na kuonyesha ana imani katika Kristo anaweza kupata msamaha ajapokuwa ameishi kwa kutenda dhambi siku zilizopita.—1 Tim. 1:12-16; 1 Kor. 6:9-11; Matendo 10:43; Rum. 6:12-14.
5. Ni jambo gani linalohitaji kufanywa ikiwa Mkristo ametenda dhambi nzito?
5 Lakini namna gani ikiwa, baada ya mtu kutubu, kumwamini Kristo na kuwa Mkristo aliyebatizwa, anajiacha ashindwe na udhaifu au anajikwaa na kutumbukia katika dhambi yenye kusikitisha sana? Bado anaweza kusamehewa, sawa na vile mtume Petro alivyosamehewa kwa kumkana Yesu. Wewe ukijua kwamba Mkristo mwenzako amejiacha ashindwe na dhambi yenye kusikitisha sana, ungefanya nini? Kwa sababu ya upendo wa kweli bila shaka ungetaka kumwona mtu huyo akipata msaada wa kiroho. Mara nyingi wazee wa kiroho kundini au waangalizi wenye kujitoa watumikie ndio wanaokuwa njia ya kutolea msaada huo. Wakiwa na lengo gani? Wakiwa na lengo la kumrudisha Mkristo mwenye kukosa kwenye hali yake ya kiroho.—Gal. 6:1; 1 Yohana 5:16; 2 Tim. 2:23-26; Yuda 23.
6. Ikiwa Mkristo mwenye hatia ya dhambi yenye kusikitisha sana hatubu, lazima hatua gani ichukuliwe?
6 Walakini, nyakati nyingine mtu ambaye kwa muda wa miaka fulani ametembea katika njia ya Ukristo wa kweli huiacha, anajiacha afuate mwenendo usio wa kimungu kisha anakosa kutubu wazee wajapofanya jitihada za unyofu wa moyo kumsaidia. Biblia inaonyesha kwamba jambo hilo lilitukia katika karne ya kwanza, nalo linatukia siku hizi. (2 Pet. 2:10-20) Basi ni hatua gani lazima ichukuliwe? Katika hekima yake na haki ya hukumu iliyo kamilifu, Mungu anaagiza kwamba hatua thabiti lazima ichukuliwe kuulinda usafi wa adili na wa kiroho wa kundi, na hatua hiyo huenda pia ikamshtua mkosaji mpaka arudiwe na akili. Neno la Mungu linaamuru hivi: “Ninyi mwondoeni yule mbaya miongoni mwenu.” Hiyo maana yake ni kumwondosha katika kundi la Kikristo.—1 Kor. 5:13; 1 Tim. 1:20; linganisha Kumbukumbu la Torati 17:7.
7. Ni maulizo ya namna gani yanayotokea kuhusu mtu ambaye ameondoshwa katika kundi?
7 Ni jambo la kusikitisha kwamba mwenendo wa mtu na nia yake ingefanya kuwe na uhitaji wa kuchukua hatua hiyo, lakini akiisha kuondoshwa nje, washiriki washikamanifu wa kundi wanapaswa wamwoneje na kumtendeaje? Je! inawapasa wajiendeshe kumwelekea yeye jinsi wangejiendesha kuelekea jirani ye yote, mfanya kazi mwenzao ye yote au mtu ye yote wanayeweza kukutana naye barabarani? Je! inawapasa waseme “Jambo” (Habari?) au hata waseme machache wakikutana njiani na mtu huyo aliyeondoshwa nje? Namna gani kumfanyia kazi au kumwajiri (kumwandika) kazi? Ni kufikia kipimo gani wazazi Wakristo, au watu wengine wa ukoo, wanapaswa kuongea au kushirikiana na mtu huyo? Maulizo mengi ya namna hiyo hutokea. Tunaweza kupiga asante sana kwamba Yehova Mungu hututolea uongozi katika kushughulika na mkosaji aliyeondoshwa nje.
SHAURI LA YESU JUU YA WAKOSAJI
8, 9. (a) Yesu alitoa shauri gani juu ya mtu aliyekuwa amefanya dhambi? (b) Hapa Yesu alikuwa akimaanisha dhambi ya namna gani?
8 Katika wakati ambao Mungu bado alikuwa akishughulika na Wayahudi wakiwa watu Wake, Yesu alitoa shauri fulani juu ya mtu mwenye kutenda dhambi. Wanafunzi wa Kristo, ambao wenyewe walikuwa Wayahudi, wangefahamu mauidha (maoni) aliyotoa kulingana na hali iliyokuwa katika jamii (mtaa) ya watu wa Kiyahudi. Sisi pia tunaweza kufaidika, kwa maana shauri ambalo Yesu alitoa lingetumika baadaye wakati kundi la Kikristo lilipoanzishwa na Mungu. (Mt. 21:43) Kristo alianza kwa kusema hivi: “Ikiwa ndugu yako anafanya dhambi, nenda ukafunue kosa lake kati yako wewe na yeye peke yenu. Ikiwa anakusikiliza wewe, umempata ndugu yako.”—Mt. 18:15, NW.
9 Ni wazi kwamba Yesu hakuwa akisema habari ya “dhambi” kwa kumaanisha kikosa fulani kidogo ambacho mtu ametendwa kama kile tunachosoma katika Wafilipi 4:2, 3. (Linganisha Mithali 12:18.) Bali, inaonekana kwamba alimaanisha dhambi kama kupunja (wivi wa kutumia udanganyifu) au uchongezi (kuharibu sana heshima ya mtu kwa maneno), dhambi zilizokuwa nzito kiasi cha kutosha hata zifanye mtu aondoshwe katika kundi.a Ikiwa mwenye kutendwa dhambi angeweza kulimaliza jambo hilo kwa kumwendea mkosaji faraghani, angekuwa ‘amempata ndugu yake’; wakati mtenda dhambi anapoonyesha wazi toba ya moyoni na kujaribu kulirekebisha kosa, hakuna uhitaji wa kulisogeza mbele jambo hilo.
10, 11. Kama hatua hiyo ya kwanza ingeshindwa kuwa na matokeo, hatua ya pili ingekuwa nini?
10 Namna gani kama hatua hiyo ingeshindwa? Yesu aliendelea kusema: “Lakini ikiwa yeye [mtenda dhambi] hasikilizi, chukua pamoja na wewe mtu mmoja au wawili zaidi, ili kwa kinywa cha mashahidi wawili au watatu kila shauri lipate kuthibitika.”—Mt. 18:16, NW.
11 Wenye kuchukuliwa walipaswa wawe “mashahidi,” wala si watu tu wasiopendelea upande huu wala huu wakijaribu kupatanisha mkosaji na mkosewaji. Inaelekea kwamba wangekuwa watu ‘waliolishuhudia’ (walioliona) kosa, kama vile kujua wakati mapatano ya pesa yalipokuwa yakifanywa na hivyo kuweza kutoa ushuhuda wa kama mtu amepunja au hakupunja. Au, ikiwa ushuhuda wa kosa ulikuwa mkataba (makubaliano ya kutimiza wajibu fulani) au mambo kama hayo, ndugu wenye kustahili kiroho wenye ujuzi katika hali hizo wangeweza kuitwa waje. Wangeweza kuwa mashahidi wenye kushuhudia yaliyotendeka na yaliyosemwa na mshtakiwa wakati wa mkutano huu ikiwa ilikuwa imekuwa lazima hatua ile ya mwisho ichukuliwe.
12. Hatua ya mwisho ingekuwa nini, kama Yesu alivyoeleza?
12 Yesu aliitoa hii kama hatua ya mwisho kwa habari ya mtenda dhambi: “Ikiwa yeye hawasikilizi, sema kwa kundi. Ikiwa hasikilizi hata kundi, mwache yeye awe kwako kama mtu tu wa mataifa na kama mtoza kodi.” (Mt. 18:17, NW) Naam, jitihada ya mwisho ya kumgeuza mtenda dhambi ageuke aiache njia yake ingekuwa kuwapelekea jambo hilo wanaume wazee kiroho wa kundi. Hao wangeweza kuyasikia yaliyotendeka na kupata ushuhuda wa mashahidi. Halafu wangeweza kumkaripia mkosaji kwa kulitumia Neno la Mungu. Walakini, kama angekataa kutubu, wangechukua hatua kwa ajili ya kundi wamtie adabu, wakililinda kundi na mavutano yake yenye hatari kwa kumwondosha nje.
SI KUTENDA WATU KWA UKATILI
13, 14. Tunawezaje kuwa na uhakika kwamba Yesu hakuwa akiunga mkono kuwatenda watu kwa ukatili?
13 Ili tusaidiwe kuamua tunavyopaswa kujiendesha kumwelekea mtu wa namna hiyo, tunahitaji kuyaelewa maneno haya ya Yesu: “Mwache yeye awe kwako kama mtu tu wa mataifa na kama mtoza kodi.” Katika karne za baadaye, marabi fulani wa Kiyahudi (waalimu wa kidini) walionyesha maoni ya kupita kiasi, kama yale ya kusema kwamba Myahudi hata asimsaidie mtu wa Mataifa yale mengine aliyekuwa katika hatari ya kufa. Ukatili huo wa moyo haukuonyeshwa kuwaelekea watu wa Mataifa yale mengine peke yao. Kwa mfano, katika mfano wa Yesu juu ya kuwa jirani wa kweli, Mlawi na kuhani pia walikataa kusaidia Myahudi mwenzao aliyeumia, ingawa baadaye Msamaria alimsaidia.—Luka 10:29-37.
14 Lakini katika Mathayo 18:17 Yesu hawezi kuwa alimaanisha kwamba wanafunzi wake wakatae kufanya tendo la fadhili za kibinadamu, kama wakati kunapokuwa na tukio baya lisilotazamiwa au la mtu kuwa na shida nyingi ya kuhitaji kitu fulani. Yesu aliwaonyesha fadhili hizo watu fulani wa Mataifa yale mengine. Kwa mfano, alimwonyesha fadhili hizo mwanamke Mfoinike-mshami. Ingawa Yesu, wanafunzi wake na mwanamke huyo walikubali maoni ya kwamba lilikuwa si jambo la kawaida kumfadhili mwanamke huyo kwa sababu yeye alikuwa mtu wa Mataifa naye Yesu alitumwa kwa Wayahudi, bado Kristo aliponya binti ya mwanamke huyo. (Mt. 15:21-28; Marko 7:24-30) Yesu alionyesha fadhili za kibinadamu kama hizo wakati afisi Mrumi wa kijeshi alipomsihi sana aponye mtumwa aliyepooza mwili na mwenye kutaabika. Afisa huyo alikubali maoni ya kwamba hakumtazamia Yesu, akiwa mwalimu wa Kiyahudi, aingie ndani ya nyumba yake. Na bado “wazee wa Wayahudi” walimwomba Yesu amwonyeshe rehema Mtaifa huyo mwenye kustahili, naye akafanya hivyo. (Luka 7:1-10; Mt. 8:5-13) Kwa hiyo kwa maneno aliyoyasema juu ya mtu kuwa “kama mtu tu wa mataifa na kama mtoza kodi,” Yesu hakukataza watu wasitendewe fadhili zenye rehema. Basi, yeye alimaanisha nini?
“KAMA MTOZA KODI”
15. Wayahudi waliwaonaje na waliwatendeaje watoza kodi?
15 Kwanza, Wayahudi waliwaonaje na waliwatendeaje watoza kodi?
“Watoza kodi wanaotajwa na Agano Jipya walionwa kuwa wasaliti na waasi-imani, waliochafuliwa kwa kushirikiana mara nyingi na waabudu wa miungu ya kishenzi, wakiwa kama vyombo vilivyo tayari kutumiwa na yule mwonezi. Wao walihesabiwa kuwa katika kundi moja na watenda dhambi . . . pamoja na makahaba . . . pamoja na waabudu wa miungu ya kishenzi. . . . Kwa kuwa watu wenye maisha ya adabu walijitenga nao, watoza kodi waliachwa peke yao kisha rafiki zao au wenzi wao wa pekee wakawa ni watu ambao walikuwa wamekataliwa mbali na kuepukwa kama wao wenyewe.”—Kitabu “Cyclopaedia” ya M’Clintock na Strong, Vol. VIII, uku. 769.
Naam, walioyasikia yale maneno ya Yesu walijua vizuri kwamba Wayahudi kwa ujumla waliwaepuka watoza kodi. Wayahudi walishughulika na watu hao mara chache sana walipokwenda kulipa kodi iliyotakwa na sheria, na hata nyakati chache hizo walishughulika nao bila kupenda.
16, 17. Yesu alikuwa na mwenendo gani kuelekea watoza kodi fulani?
16 ‘Lakini,’ huenda mtu akauliza, ‘Yesu hakushirikiana na watoza kodi?’ Eeh, acheni tuyachunguze mambo ya uhakika.
17 Akiwa ndiye “Mwana-kondoo wa Mungu, aichukuaye dhambi ya ulimwengu,” Yesu alikuwa nuru kwa watu wote, ingawa alikaza fikira zake juu ya Wayahudi wakati wa huduma yake ya kidunia. (Yohana 1:29; 8:12; Isa. 42:1, 6, 7; Mt. 10:5, 6; 15:24) Yeye alikuwa kama tabibu katika kuwasaidia Wayahudi wote wale waliohitaji zaidi msaada wake, kutia na watenda dhambi kama makahaba, walevi na watoza kodi, ambao mara nyingi walitumia njia za udanganyifu. Mathayo Lawi, mtoza kodi mwenye kudharauliwa, ni mmoja wa watu walioukubali ujumbe mpya wa wokovu ulioletwa na Yesu. Mathayo alimkaribisha Yesu aje nyumbani kwake kula karamu, na hivyo Mathayo na watoza kodi wengine wenye kupendezwa wakapata nafasi ya kuzisikia kweli nyingine mpya zilizokuwa nzuri sana. (Luka 5:27-32; 19:1-10) Hao ni watu waliokuwa ‘wametenda dhambi za kutokujua,’ lakini wakawa na utayari wa kuchukua hatua za ‘kufutiwa dhambi zao.’—Matendo 3:19; Ebr. 9:7.
18. Kwa sababu gani kushughulika kwa Yesu pamoja na watoza kodi fulani hakukuwa ndicho kielelezo kinachopasa kufuatwa ili kutenda kulingana na maneno yake katika Mathayo 18:17?
18 Walakini, jitihada ya Yesu ya kuwapa ushuhuda watoza kodi ambao ‘walimkaribia wamsikilize’ na ‘kumfuata’ haikuwa kielelezo chenye kuonyesha jinsi watenda dhambi wasiotubu walivyopaswa kutendewa. (Marko 2:15; Luka 15:1) Tunawezaje kuwa na uhakika wa jambo hilo? Ingawa Kristo alikula na watoza kodi hao, mtume Paulo aliagiza kwamba Wakristo ‘hata wasile pamoja na’ mtenda dhambi aliyeondolewa awe nje ya kundi. (1 Kor. 5:11) Vilevile, Yesu aliwaambia wanafunzi wake wamtendee mkosaji asiyetubu kama vile kwa kufaa wao waliwaona watoza kodi wa wakati huo. Tafsiri ya R. F. Weymouth inasema hivi: “Mchukue huyo sawasawa na vile wewe unavyomchukua Mtaifa au mkusanyaji-kodi.”—Linganisha New International Version; The New English Bible.
WATU WA MATAIFA YALE MENGINE WALIONWAJE NA WALITENDEWAJE?
19. Biblia inaonyesha uhusiano kati ya Wayahudi na watu wasio Wayahudi ulikuwa namna gani?
19 Mitume walioyasikia maneno ya Yesu yaliyoandikwa kwenye Mathayo 18:17 walikuwa Wayahudi na walijua kwamba wananchi wenzao hawakushirikiana kirafiki na watu wa Mataifa yale mengine. Torati iliwatofautisha Wayahudi na Mataifa yale mengine, nayo hiyo ikawa njia ya kutenganisha Waisraeli na mataifa yaliyowazunguka. (Kum. 7:1-4; Hes. 15:37-41; Efe. 2:11-14) Kwenye Sikukuu ya Kupitwa ya mwaka wa 33 W.K. Wayahudi walikataa kuingia katika jumba la gavana Mrumi “wasije wakanajisika” (wakachafuka). (Yohana 18:28) Nao mtengano uliokuwa kati ya Wayahudi na Wasamaria, ambao hata waliikubali Pentateuko (vitabu vitano vya kwanza vya Biblia), ulikuwa mkubwa sana hata mwanamke mmoja aliyekuwa kisimani katika Samaria akaonyesha mshangao wa kwamba Yesu alimwomba maji ‘ajapokuwa ni Myahudi.’—Yohana 4:9, NW.
20. Tunaweza kujifunza jambo gani kutokana na yaliyotendeka kati ya Petro na Kornelio ili tujue jinsi Wayahudi walivyoshughulika na watu wa mataifa.
20 Tena, katika mwaka wa 36 W.K., wakati Mungu alipokusudia kuonyesha kwamba wakati huo Mataifa wasiotahiriwa wangeweza kukubaliwa wawe warithi wa ule Ufalme, yeye alimwelekeza mtume Petro kwa yule afisa Mrumi wa kijeshi Kornelio. Lakini Petro akamwambia Kornelio: “Ninyi mnajua ya kuwa si halali mtu aliye Myahudi ashikamane na mtu aliye wa taifa lingine.” (Matendo 10:28) Maneno ya Petro yanaonyesha Wayahudi walijisikia sana kwamba hawakupaswa kuchangamana na mtu wa mataifa. Vilevile, wakati ilipojulikana kwamba Petro alikuwa amekwenda kwa Kornelio, Wakristo fulani wa Kiyahudi waliudhika sana kwa sababu Petro ‘aliingia kwa watu wasiotahiriwa akala nao.’ Naam, Wayahudi waliliona kuwa jambo la kushtua kuwa pamoja na ‘mtu wa mataifa.’—Matendo 11:1-3; linganisha Wagalatia 2:12.
21. Basi, wewe unayaelewaje maneno aliyoyasema Yesu kwamba mtenda dhambi asiyetubu awe “kama mtu tu wa mataifa na kama mtoza kodi”?
21 Kwa njia hiyo Maandiko yanatusaidia tuelewe maana ya maoni ya Yesu yanayosema tumtendee mkosaji asiyetubu aliyekataa kulisikiliza kundi “kama mtu tu wa mataifa na kama mtoza kodi.” Kutumia shauri hilo la Kristo siku hizi bila shaka kusingemaanisha kumwona mkosaji kama mtu wa kawaida tu mtaani (katika jamii ya watu), kwa maana hivyo sivyo wanafunzi wa Yesu walivyoyaelewa maneno yake. Tunaweza kulifahamu vizuri zaidi jambo hili kwa kuchunguza mashauri zaidi katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, ambayo yatatusaidia tushughulike na hali za kweli zinazotokea katika maisha ya siku hizi kuhusiana na watu walioondoshwa katika kundi la Kikristo.
[Maelezo ya Chini]
a Chini ya sheria ya Musa, dhambi fulani zenye kusikitisha sana, kama uzinzi, kulalana kwa mwanamume na mwanamume, kuua mtu bila kukusudia na uasi-imani, zisingeweza kushughulikiwa na mtu peke yake, mkosewaji akikubali masikitiko ya mkosaji na jitihada zake za kulirekebisha kosa lililofanywa. Bali, dhambi hizo zenye kusikitisha sana zilishughulikiwa kupitia wanaume wazee, waamuzi na makuhani.—Law. 20:10, 13; Hes. 5:11-31; 35:12, 19-25; Kum. 13:6-15; 17:2-9; 19:16-19; 22:22.
MANENO “KAMA MTU TU WA MATAIFA NA KAMA MTOZA KODI’’ YALIMAANISHA NINI?
Wayahudi waliwaepuka watoza kodi kwa kuwaona kuwa watu waliokataliwa mbali wasiwe kati ya jamii ya watu
Wayahudi walikataa kuingia katika jumba la gavana Mtaifa
Petro alisema haikuwa “halali” kwa Myahudi kumwendea Mtaifa
Wakristo wa Kiyahudi walishtuka kujua kwamba Petro alikula pamoja na Kornelio
[Picha katika ukurasa wa 9]
Wayahudi waliwaepuka watoza kodi, ambao walionwa kuwa watenda dhambi. Shughuli ya pekee waliyofanya nao ilikuwa wakati tu walipokwenda kuwalipa kodi iliyotakwa na sheria