Rehema ya Kimungu Yaonyesha Njia ya Kurudi kwa Wenye Kutenda Makosa
“Kutakuwa na furaha mbinguni kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye, kuliko kwa ajili ya wenye haki tisini na kenda ambao hawana haja ya kutubu.”—Luka 15:17.
1, 2. Ni kwa njia gani sifa za Yehova Mungu zimesawazika kwa kupatana, nayo hii yaonekanaje katika mpango wa kutenga na ushirika?
YEHOVA ni Mungu wa upendo, Mungu mwenye rehema. Mipango yake yote na maagizo ni kwa faida ya wale wapendao haki; wao hawana kusudi la kichoyo wala lenye madhara kamwe. (Kut. 34:6; 1 Yohana 4:8) Yeye pia ni Mungu wa haki na uadilifu; haachilii makosa. (Zab. 33:4, 5; 50:16-21) Hata hivyo, sifa hizi za kimungu hazikosi kupatana. Kwa kweli, upendo wa kweli unahitaji kushikamana na haki na kuisisitizia.
2 Hivyo, kati ya mipango ionekanayo katika Neno la Mungu uko ule wa kutenga na ushirika, yaani, kuondoa au kufukuza kundini watu wanaojitia katika makosa makubwa na wanaokosa kuonyesha nia ya kweli ya kutubu, ijapokuwa wanajidai kuwa Wakristo. Kuondolewa kwao ni kwa faida ya kundi ili kuuendeleza usafi wake na kulinda washiriki wake, wapendwao na Mungu, wasije wakachafuliwa na maongozi hayo ‘yenye kuchachusha’ yanayoonyeshwa na watenda makosa.
3, 4. Mtume Paulo anatoa maagizo gani juu ya kutenga na ushirika, na ni maulizo gani yanayopaswa kujibiwa?
3 Kwa hiyo, mtume Paulo aliyeongozwa kwa roho aliwaagiza Wakristo wa Korintho ‘wasichangamane na mtu aitwaye ndugu, akiwa ni mzinzi au mwenye kutamani au mwenye kuabudu sanamu au mtukanaji au mlevi au mnyang’anyi; mtu wa namna hii msikubali hata kula naye. . . . Ninyi mwondoeni yule mbaya miongoni mwenu.’—1 Kor. 5:6, 7, 11-13.
4 Walakini, je! hii inakataza kuchukua hatua yo yote ya wema baadaye kwa hao waliotengwa na ushirika, hatua ambayo ingewasaidia watubu, wageuke, warudishwe kama washiriki wanaokubaliwa walio safi wa kundi? Je! hatua zote za wema lazima ziachwe mpaka mtu yule aonyeshe toba kwa wazee wa kundi kama ilivyo kawaida, yeye mwenyewe akiomba arudishwe? Je! kumtia moyo mtu kama huyo kwa vyo vyote ‘ageuke’ na kuomba arudishwe ‘kunatuchangamanisha’ naye na kuwa na ushirika wa kiroho naye? Na tulione jibu linaloonyeshwa na Biblia.
MFANO WA MZEE MKUU
5, 6. (a) Ni uhusiano gani wa pekee ambao taifa la Israeli lilifurahia wakati mmoja na Yehova Mungu? (b) Walakini, wao walifuata mwendo gani, na kwa matokeo gani mabaya sana?
5 Ufikirie mfano wa matendo ya Yehova Mungu kwa wale waliokuwa watu wa jina lake wakati mmoja, Israeli. Wao peke yao kati ya watu wote waliokuwa duniani ndio waliokuwa katika uhusiano wa agano naye nao walikuwa wamepewa neno lake na sheria yake peke yao. (Zab. 147:19, 20; Rum. 3:1, 2) Walakini, walikosa kuwa waaminifu kwake mara kwa mara na mwishowe wakaifikia hali inayoelezwa katika sala iliyoandikwa katika Danieli 9:4-19: “Tumefanya dhambi, tumefanya ukaidi, tumetenda maovu, tumeasi, naam, hata kwa kuyaacha maagizo yako na hukumu zako; wala hatukuwasikiliza watumishi wako, manabii, ambao kwa jina lako walisema na wafalme wetu, na wakuu wetu, na baba zetu, na watu wote wa nchi.”
6 Kwa sababu ya kugeuka huku na uasi mzito, Danieli anasema kwamba Yehova ‘alimwaga laana juu yetu, na uapo ule ulioandikwa katika sheria ya Musa, mtumishi wa Mungu . . . kwa kutuletea mambo maovu makuu; maana chini ya mbingu zote halikutendeka jambo kama hili.’ Ndiyo, Mungu aliwahukumu vikali, akiyatupa makabila ya kaskazini kwanza kisha makabila ya kusini watoke nchini mwao kuingia uhamishoni, mwishowe akaliruhusu taifa zima lipinduliwe na Babeli. Kwa hiyo, Yehova ‘alilitaliki’ tengenezo la kitaifa kana kwamba lilikuwa “mke” wake na “mama” ya washiriki mmoja mmoja wa taifa.—Linganisha Isaya 50:1; 54:5, 6; Yeremia 3:8.
7. Baada ya kuwaondolea Israeli kibali yake, je! baada ya hapo Yehova aliendeleza nia ya kutowataka kabisa? Toa ushuhuda.
7 Akiisha kuwachukulia hatua hii ya hukumu, je! baada ya hapo Yehova alikataa kufanya lo lote ambalo lingeweza kuwasaidia wapate kibali yake tena? Sivyo, bali, aliwaambia maneno ya kuwakaripia, akiwatia moyo wauache mwendo mbaya uliokuwa umewaletea msiba. Mungu alisema hivi kupitia kwa nabii Yeremia, kwa wazi kwa wale waliokuwa wa ufalme wa kaskazini wa Israeli uliokataliwa: “Rudi, Ee Israeli mwenye kuasi, . . . sitashika hasira hata milele. Ungama uovu wako tu; ya kwamba umemwasi [Yehova], Mungu wako . . . Rudini, enyi watoto waasi, mimi nitaponya maasi yenu.”—Yer. 3:12, 13, 22; linganisha Maombolezo 3:31-33; Isaya 57:16-18.
8. Yehova alifunuaje nia yake juu ya wenye kukosa kupitia kwa nabii Ezekieli?
8 Usemi huu unapatana na maneno ya Yehova kupitia kwa nabii Ezekieli, ambapo anaionyesha nia yake juu ya wale ambao wangali wanaonyesha uwezekano wa kutubu: “Je! mimi ninafurahia kufa kwake mtu mwovu? . . . si afadhali kwamba aghairi, na kuiacha njia yake, akaishi? . . . Tupilieni mbali nanyi makosa yenu yote mliyoyakosa; jifanyieni moyo mpya na roho mpya; mbona mnataka kufa, enyi nyumba ya Israeli? Maana mimi sikufurahii kufa kwake afaye . . . basi ghairini, mkaishi.”—Eze. 18:23, 30-32
9. Kwa kutia moyo huko, je! Yehova Mungu alikuwa akiwa na ushirika wa kiroho na watenda mbaya?
9 Kwa kuwatia moyo wakosaji hawa kwa njia hii, je! Yehova Mungu alikuwa akishirikiana nao kwa kiroho, “kushirikiana” mambo mema ya kiroho pamoja kama vile kati ya rafiki? (Linganisha 1 Yohana 1:3, 6, 7.) Kuliko hivyo, kama vile Yehova alivyokuwa amewaambia mapema kwa kumtumia nabii Isaya, ikiwa waliutaka urafiki wake tena ingaliwapasa kugeuka. Yeye asingejishusha atembee katika njia zao mbaya na kuyakubali mawazo yao mabaya. Alisema hivi: “Mtafuteni [Yehova], . . . Mtu mbaya na aache njia yake, na mtu asiye haki aache mawazo yake; na amrudie [Yehova], naye atamrehemu; na arejee kwa Mungu wetu, naye atamsamehe kabisa. Maana mawazo yangu si mawazo yenu, wala njia zenu si njia zangu; asema [Yehova]. Kwa maana kama vile mbingu zilivyo juu sana kuliko nchi, kadhalika njia zangu zi juu sana kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu.” (Isa. 55:6-9) Ili kufurahia ushirika mtamu na Mungu tena, ingaliwapasa wayainue mawazo yao na njia zao zifikie hali zenye haki anazoshikamana nazo Mungu na ambazo Neno lake linafundisha. Hivyo wangelitii ombi lake la ‘kuja tusahihishe mambo kati yetu,’ ili dhambi zao nzito zipate kuonwa naye kama zilizofutwa.—Isa. 1:18, 19, NW.
10, 11. Ni sifa gani za Yehova zinazofananishwa na mfano wa mwana mpotevu, na kwa njia gani?
10 Mfano wa mwana mpotevu unatoa ufahamu zaidi wa nia yenye kupendeza ya Yehova ya rehema na huruma. (Luka 15:11-32) Namna baba aliyemo katika mfano alivyotenda mwana wake mpotovu aliporudi yaonyesha kwa njia yenye kupendeza sana namna Baba wa kimbinguni, Yehova, alivyo. Katika mfano, mwana alikuwa ameondoka nyumbani, akaenda zake mbali sana na kutumia wakati wake na fedha yake ovyo ovyo katika maisha ya ufisadi, kutia na kushirikiana na makahaba. Alifilisika na kuona njaa akaamua kumrudia baba yake, aliporudiwa na fahamu. Sasa, angalia mfano unavyosema: “Alipokuwa angali mbali, baba yake alimwona, akamwonea huruma, akaenda mbio akamwangukia shingoni, akambusu sana.”—Luka 15:20.
11 Hivyo, alipomwona mwanawe kwa mbali, baba hakusema: ‘Sitasogea hata kidogo wala sitasema lo lote mpaka mtenda dhambi yule anifikie miguuni pangu penyewe aombe kabisa akubaliwe tena.’ Sivyo, bali alipomwona mwanawe akimwelekea na, kwa sababu hiyo, akajua alilokuwa akifikiria mwana, baba alimlaki. Mwana aliomba msamaha kabisa baada ya baba yake kuonyesha huruma, si kabla.
12. Kwa njia gani Yehova, alivyowarudisha watenda mabaya wenye kutubu? Unabii wa Hosea waonyeshaje hili?
12 Hii yakumbusha mtajo wa mtume Paulo juu ya ‘wema wa Mungu unaojaribu kukuvuta upate kutubu.’ (Rum. 2:4) Ndiyo, Yehova Mungu anaonyesha hasira yenye haki juu ya makosa. Lakini yeye haendelei kukasirika milele makosa yakiachwa. Anajua kwamba rehema yenye uchangamfu inazo sifa za kuvuta zilizo nzuri ajabu kuwarudisha watenda makosa kwenye hatua wawezapo kuponywa.—Hos. 6:1; 14:1, 2, 4.
13. (a) Kwa sababu gani imetupasa tusitake kumwiga ndugu mkubwa katika mfano wa mwana mpotevu? (b) Imewapasa wote wale wanaotumikia kama wazee, waangalizi na wachungaji wamtegemee nani kama mfano wao katika kushughulika na wenye kutenda makosa? (c) ZaburI zaonyesha nini kwa habari ya mfano wa huyu Mzee Mkuu?
13 Kwa hiyo sisi leo hatutaki tuwe kama ndugu mkubwa wa mfano ambaye kwanza hakufurahia namna ambavyo ndugu yake mwenye kukosa alivyokubaliwa tena. (Luka 15:25-32) Bali, tutajaribu ‘kuwa wana wa Baba yetu aliye mbinguni’ kwa kuuiga mfano wa huruma wa Yehova. (Mt. 5:44-48) Yeye, kama Mungu wa umilele na “mzee wa siku,” ndiye Mzee Mkuu, Mchungaji na Mwangalizi Mkuu wa nafsi zetu. (1 Pet. 2:25) Mfano wake ndio ufaao kufuatwa sikuzote. Baadaye katika mazungumzo yetu tutaona namna mfano huo uwezavyo kutuongoza kwa njia nyingi zifaazo.—Zab. 77:7-9; 103:9, 10, 13.
KUONWA KWA MTU KAMA “MTU TU WA MATAIFA NA KAMA MTOZA KODI”
14. Ni msingi gani wa kwanza aliokuwa nao mtume Paulo kwa agizo yake juu ya kutenga na ushirika?
14 Alipokuwa akiliandika shauri lake kama mtume kwa Korintho juu ya kutenga na ushirika, Paulo alikuwa na habari zilizoongozwa kwa roho mapema kama msingi wa maagizo yake. Kristo Yesu mwenyewe alikuwa amezitoa. Mathayo 18:15-17, NW, anaandika maagizo yake ya kushughulikia dhambi walizotendwa watu mmoja mmoja (kwa wazi si makosa madogo madogo tu bali dhambi nzito kabisa). Alionyesha uwezekano wa tendo la kutenga na ushirika toba la kweli lisipoonyeshwa kwa upande wa mwenye kutenda dhambi. Baada ya kueleza jitihada moja moja za ‘kumpata’ mtu huyo kwa kumfanya alikubali kosa lake na kulitubia, Yesu alisema hivi: “Ikiwa hasikilizi hata kundi, mwache yeye awe kwako kama mtu tu wa mataifa na kama mtoza kodi.”
15. (a) Ni “kundi” gani alilokuwa Yesu akilitaja katika Mathayo 18:17, NW? (b) Kwa sababu gani, basi, twapendezwa na maneno yake kwetu katika kundi la Kikristo?
15 Wakati huu (32 C.E.) kundi la Kikristo lilikuwa halijaanzishwa bado na kwa hiyo “kundi” lililotajwa na Yesu bila shaka lilihusiana na mpango wa Kiyahudi uliokuwako wakati huo, pamoja na baraza zake za wazee, kutia na wale waliotumikia kama waamuzi na walioliwakilisha kundi katika maeneo yao katika vyeo hivyo. (Ezra 10:14; Luka 7:3) Hata hivyo, bila shaka maagizo ya Yesu yalitoa kanuni ya kuongozea ambayo ingelisaidia kundi la Kikristo la wakati ujao. Linalotupendeza hasa ni kujua kuonwa kwa mtenda dhambi asiyetubu “kama mtu tu wa mataifa na kama mtoza kodi” kulikuwa na maana gani. Ili kujua yatupasa tuone namna watu hao walivyoonwa kwa kufaa na kundi la Kiyahudi. Hii itatusaidia tuyafahamu zaidi maagizo ya mtume katika 1 Wakorintho 5:11-13 juu ya namna ambavyo imewapasa Wakristo wawaone wale waliotengwa na ushirika na kundi la Kikristo.
16. Kwa sababu gani hatuwezi kutegemea kabisa maandishi ya Kiyahudi ya waalimu wa kidini kwa habari ya nia ya Wayahudi juu ya Mataifa, nasi twapata wapi habari zinazohitajiwa?
16 Kwa kuiangalia nia ya Wayahudi juu ya watu wa mataifa, hatuwezi kuongozwa juu ya mambo yote na maandishi ya waalimu wa kidini yaliyotungwa baada ya wakati ambao Yesu alikuwa duniani. Mengine ya maandishi haya yanaonyesha chuki nyingi na dharau nyingi kupita kiasi juu ya “Mataifa.” Maandishi mengine ya waalimu wa kidini yalishikilia kauli ya kwamba haimpasi Myahudi amwokoe Mtaifa hata huyo akiwa katika hatari ya kufa. (Maimonides, Rozeach. iv, 12; McClintock and Strong’s Cyclopædia, Vol. III, uk. 789) Bali, twaweza kupata habari za kutegemeka katika Maandiko ya Mungu yaliyoongozwa kwa roho yake yatuongoze kuhakikisha nia ya Wayahudi wa karne ya kwanza ilivyokuwa.
17. Maandiko yaonyesha nia ya Wayahudi ilikuwa nini juu ya ‘watu wa mataifa’ katika karne ya kwanza, na kwa sababu gani nia hii ilikuwako?
17 Alipotumwa kwa nyumba ya Kornelio Mtaifa katika Kaisaria, mtume Petro aliwaambia hivi waliokusanyika: “Ninyi mnajua ya kuwa si halali mtu aliye Myahudi ashikamane na mtu aliye wa taifa lingine wala kumwendea, lakini Mungu amenionya, nisimwite mtu awaye yote mchafu wala najisi.” (Matendo 10:27, 28) Wakati Petro alipokwenda Yerusalemu baadaye, wenye kufuata tohara katika kundi la Kikristo walishindana naye, “wakisema, Uliingia kwa watu wasiotahiriwa ukala nao.” (Matendo 11:2, 3) Hivyo, maoni ya Wayahudi hasa yalikuwa kwamba haikuwapasa wachangamane na Mataifa, wakiwaona kama wachafu kwa kiroho. Walikuwa hivyo kwa sababu ya kuwa ‘wamefarakana na jamii ya Israeli na kuwa wageni wasio wa maagano ya ahadi ile,’ kwa hiyo hawakuwa na hali nzuri au uhusiano wenye kukubalika na Yehova Mungu. (Efe. 2:11, 12) Kuchangamana nao, kuingia katika nyumba zao na kula pamoja nao, kungewatia Wayahudi unajisi wao wa kiroho.—Linganisha Yohana 18:28; Wagalatia 2:11-14.
18. Tuna ushuhuda gani kwamba Yesu hakufuata maoni yenye kupita kiasi juu ya Mataifa yaliyoonyeshwa katika maandishi ya waalimu wa kidini?
18 Yesu Kristo alishikamana na kanuni hii ya msingi ya kutochangamana na watu wa mataifa. Naye aliwaagiza wanafunzi wake kwamba “katika njia ya Mataifa [yasiyo ya Kiyahudi] msiende, wala katika mji wo wote wa Wasamaria msiingie. Afadhali shikeni njia kuwaendea kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.” (Mt. 10:5, 6) Hata hivyo, Yesu hakukubaliana wala kupatana na maoni ya kupita kiasi yapatikanayo katika maandishi ya waalimu wa kidini yaliyowahesabu Mataifa wote kama adui wa kutendewa kwa dharau kabisa—kama vile asivyoacha maoni hayo yaongoze matendo yake kwa Wasamaria. (Yohana 4:4-40) Tofauti kabisa na hili, Yesu alilitaja Neno la unabii la Baba yake kuonyesha kwamba watu wa mataifa wangemkubali Masihi, kwamba hekalu lilipaswa liwe nyumba ya sala kwa mataifa yote, na kwamba Masihi angekuwa nuru kwa mataifa. (Mt. 12:18, 21; Marko 11:17; linganisha Luka 2:27-32; Matendo 13:47.) Wakati jemadari wa jeshi wa Mataifa, aliyekuwa amewafadhili Wayahudi sana alipomwomba Yesu amponye mtumwa mgonjwa, Yesu alifanya hivyo. (Luka 7:2-10) Kwa hiyo, ijapokuwa hakutenda kinyume cha onyo la sheria ya Musa juu ya kuchangamana na wale wasio wa kundi la Mungu (Mataifa wasio Wayahudi), Yesu hakuwa na maoni yasiyosawazika, ya kupita kiasi wala hakuwa mshupavu mno, akiwa na maoni ya uadui juu ya hawa. Kwa hekima alizitambua kanuni zilizomo katika maagizo ya Mungu naye akaongozwa nazo.
19. (a) Watoza kodi walionwaje na Wayahudi kwa ujumla? (b) Yesu alionyeshaje usawa ufaao katika matendo yake kwao?
19 Ndivyo ilivyokuwa na kwa watoza kodi, ambao kwa kawaida hawakuwa Mataifa bali Wayahudi. Kwa kuwa mara nyingi sana walikuwa wadanganyifu, watoza kodi kwa ujumla walionwa na Wayahudi wenzao kama watu wenye sifa mbaya, wa kutiwa katika fungu moja na watenda dhambi na makahaba waliojulikana. (Mt. 9:10, 11; 21:31, 32) Ijapokuwa hakuachilia njia zao mbaya, Yesu hakusita asiwasaidie watu hao walipoonyesha nia ya kuelekea kwenye haki, kama walivyofanya watoza kodi kama vile Mathayo Lawi na Zakayo. Kwa sababu aliwasaidia wafanye maendeleo ya kiroho, Yesu alishtakiwa kwa uongo kuwa “rafiki yao watoza ushuru na wenye dhambi.” Walakini, kulikuwako tofauti ya urafiki na jitihada za Yesu za kuwaponya wale waliokuwa wagonjwa kwa kiroho na kuwaelekeza kwenye toba na katika njia ya haki.—Mt. 11:19; Luka 5:27-36; 19:2-10.
20. Habari hizi juu ya maoni yafaayo ya Wayahudi juu ya ‘watu wa mataifa na watoza kodi’ yatusaidiaje kuwa na ufahamu bora wa maagizo ya mtume juu ya kutenga na ushirika, nazo zaelekeza kwenye mikataa gani?
20 Hivyo, mfano wa Yesu mwenyewe watulinda na kuwa na maoni ya kupita kiasi ya waandishi fulani wa kidini katika shauri hili la kushughulika na watu kama “mtu tu wa mataifa na kama mtoza kodi.” Twaona pia ulinganifu mkubwa kati ya walivyotendewa hawa na anavyoagiza mtume Paulo watendewe wale waliotengwa na ushirika wa kundi la Kikristo, yaani, ‘kutochangamana’ nao wala “hata kula” nao. (1 Kor. 5:11) Kwa wazi, kumtendea mtenda dhambi asiyetubu kama “mtu tu wa mataifa na kama mtoza kodi” kwamaanisha hakupaswi kuweko kuchangamana na mtu huyo. Lakini, kama vile mfano wa Yesu unavyoonyesha, hii haihitaji kumtendea huyo kama adui au kukataa kuonyesha heshima na huruma ya kawaida. Wala haikatazi kuwasaidia wale wanaotaka kusahihisha mwendo mbaya na kupata au kupata tena kibali ya Mungu.
KUELEWA MAANA YA 2 YOHANA 9-11
21. Ni maonyo gani ambayo mtume Yohana anatoa katika mstari wa 9 mpaka wa 11 wa barua yake ya pili, na hii yatokeza maulizo gani?
21 Katika barua yake ya pili, mtume Yohana anatoa onyo hili: “Kila apitaye cheo, wala asidumu katika mafundisho ya Kristo, yeye hana Mungu [yaani, hana umoja naye, hana ushirika naye; linganisha 1 Yohana 1:6]. Yeye adumuye katika mafundisho hayo, huyo ana Baba na Mwana pia. Mtu akija kwenu, naye haleti mafundisho hayo, msimkaribishe nyumbani mwenu, wala msimpe salamu. Maana yeye ampaye salamu azishiriki kazi zake mbovu.” (2 Yohana 9-11) Je! maneno ya mtume hapa yanatumika kwa lazima kwa watu wote wanaoondolewa kundini kwa kutenda makosa? Au kwa lazima yanakataza kusema maneno yo yote ya kukaripia au kutia moyo kwa mtu aliyetengwa na ushirika kwa kusudi la kumwongoza atubu, ageuke na kurudishwa kundini? Kwa kuziangalia habari zinazozunguka za maneno hayo ya mtume twaweza kupata ufahamu mzuri zaidi wa maana ya onyo lake.
22. (a) Kulingana na habari zinazozunguka, mtume alikuwa na maana ya watu wa namna gani humo? (b) Kwa sababu gani salamu kwa hao isingefaa? (c) Je! pana tofauti kati ya nia inayopendekezwa juu ya wale wanaosimuliwa na Yohana na nia inayoonyeshwa kwa kawaida na kwa kufa juu ya ‘mtu tu wa mataifa au mtoza kodi’?
22 Angalia kwamba katika mstari wa saba mtume Yohana anasema kwamba “wadanganyifu wengi wametokea duniani, wasiokiri ya kuwa Yesu Kristo yuaja katika mwili. Huyo ndiye yule mdanganyifu na mpinga Kristo.” Kisha Yohana atoa onyo kujihadhari mtu asiwakaribishe hao nyumbani mwake, kwa maana hawa ni waeneza porojo za mafundisho ya uongo, mawakili wadanganyifu wenye bidii wa mwenendo mbaya. Wasipewe nafasi hata kidogo ya kupenya ndani. Mtu hata asiwasalimu, ili aepuke kuwa mshiriki wa kazi zao mbovu. Katika habari hii, twaweza kuangalia kwamba salamu ya kawaida kati ya Wayahudi nyakati za mitume ilikuwa usemi wenye maana ya “Na uwe na amani.” Bila shaka Mkristo hawezi kumtakia mdanganyifu wala mpinga Kristo amani. Walakini, hakuna linaloonyesha kwamba Wayahudi wenye maoni yaliyosawazika na ya Maandiko walikuwa wakikataa kumsalimu “mtu tu wa mataifa” au mtoza kodi. Shauri la Yesu juu ya salamu, kwa habari ya kutia moyo kwake tumwige Mungu katika fadhili zake zisizostahili kwa “waovu na wema,” lingeelekea kukataza hali hiyo ya ushupavu,—Mt. 5:45-48.
23. Ni kwa kadiri gani au ni chini ya hali gani 2 Yohana 9-11 ingeweza kutumiwa kwa mtu aliyetengwa na ushirika?
23 Kwa hiyo, je!, wote waliotengwa na ushirika ni kama watu wanaoelezwa katika barua ya pili ya Yohana? Wakati ambapo ilikuwa lazima watengwe na ushirika kwa wazi walikuwa wakifuata mwendo unaofanana na wao au wakionyesha kidogo maelekeo yanayofanana. Kama vile kitabu Tengenezo kwa Kuhubiri Ufalme na Kufanya Wanafunzi kinavyosema katika ukurasa wa 172: “Mtu ye yote aliyebatizwa ambaye kwa kukusudia anafuatia mwendo wa ufisadi kwa kweli anakataa mafundisho ya Biblia, sawasawa na mtu anayewafundisha wengine tofauti na Maandiko yanavyosema juu ya namna Mungu alivyo, mpango wa ukombozi, ufufuo, na mengineyo. (Linganisha Tito 3:10, 11; 2 Timotheo 2:16-19.)” Na, ikiwa baada ya kutengwa na ushirika mtu anajaribu kuutetea ufisadi wake mbele ya wengine na kujaribu kupotoa wengine wafuate kuwaza kwake kulikopotoka, bila shaka yeye angefaa katika masimulizi yaliyotolewa na mtume Yohana katika barua yake ya pili.
24, 25. (a) Pana ushuhuda gani wa kwamba si wote wanaotengwa na ushirika wanaolingana na maelezo yanayotolewa katika 2 Yohana 9-11? (b) Imetupasa tutendeje kwa sababu ya hili, na ni ulizo gani la lazima tutakaloendelea kuangalia?
24 Walakini, si wote waliotengwa na ushirika wanaofuata mwendo wa hao ‘wadanganyifu na wapinga Kristo.’ Si wote wanaojitia katika kuendeleza makosa kwa bidii, wakiipinga kweli na kujaribu kudanganya wengine waufuate mwendo mbaya uliofanya watengwe na ushirika. Hii yaonyeshwa na hesabu ya wale wanaoomba warudishwe na wanaorudishwa kwa kutubu kama washiriki waliokubaliwa wa kundi. Hivyo, katika United States (ambako kuna zaidi ya mashahidi wa Kikristo wa Yehova nusu milioni sasa), wakati wa kipindi cha miaka kumi tangu 1963 mpaka 1973, ilikuwa lazima watu 36,671 watengwe na ushirika kwa sababu ya namna mbalimbali za makosa mazito. Na hali, kipindi icho hicho watu 14,508 walirudishwa, wakakubaliwa tena katika makundi kwa sababu ya toba lao la unyofu wa moyo. Hii ni karibu kiasi cha 40 kwa 100 cha jumla ya waliotengwa na ushirika. Bila shaka yatupasa sisi tuliopo duniani tufurahi pamoja na Yehova na jamaa yake ya kimbinguni kwa sababu ya jambo hili.—Luka 15:7.
25 Ikiwa jambo fulani laweza kufanywa kuwasaidia wengi hata zaidi wa wale waliotengwa na ushirika—lakini wasioufuata mwendo wa ‘wapinga Kristo’ wanaoelezwa na Yohana—warudishwe kundini, hilo ni jambo gani? Ebu na tuone namna kanuni za Maandiko zilizoangaliwa zinavyotumika kwa kufaa.
[Picha katika ukurasa wa 53]
Katika mfano wa Yesu wa mwana mpotevu, baba alimkaribisha mwana wake mpotevu mwenye kutubu kwa uchangamfu. Hii yatukumbusha rehema yenye uchangamfu ya Mungu, na kutuwekea sisi mfano