Kuendeleza Maoni Yaliyosawazika Juu ya Waliotengwa na Ushirika
1, 2. (a) Kwa sababu gani kundi la Kikristo linachukua hatua kwa kufaa juu ya wale wanaozoea maongozi yenye ufisadi kati yao, na ni akina nani walio na daraka la pekee katika habari hii? (b) Ni hatari gani zinazolingana zilizopo katika kushughulika na mambo hayo?
CHACHU kidogo yaweza kulichachusha donge zima la unga wa kuokea. Ndivyo na maongozi ya ufisadi yawezavyo kupenya na kuchafua kundi zima. Kwa kufaa, kundi lo lote limepaswa litake kujilinda na maongozi hayo, nao wazee wa kundi hasa wamepaswa washughulikie hili.—1 Kor. 5:6; Matendo 20:28-30.
2 Kuna hatari kubwa katika kuwa wazembe katika jambo hili, kama vile kundi la Korintho lilivyokuwa na uzembe kuelekea mtenda kosa katikati yao, wakashindwa kuchukua hatua ya kuyaondoa maongozi hayo ‘yenye kuchachusha.’ Lakini kuna hatari inayolingana na hii. Nini? Ile ya kutenda kupita kiasi upande mwingine, kutoka uzembe kuwa washupavu na wasiobadili nia.
3, 4. Ni nini maana ya maneno ya Paulo katika 2 Wakorintho 2:11?
3 Twaweza kuliangalia onyo alilolitoa mtume Paulo katika barua yake ya pili kwa Wakorintho, kwa wazi (kulingana na habari zinazozunguka) kumhusu mtenda dhambi anayesimuliwa katika barua yake ya kwanza ambaye ilikuwa imekuwa lazima ‘aondolewe miongoni mwao.’ (1 Kor. 5:1-5, 13) Katika habari hiyo mtenda kosa huyu yaelekea alikuwa ametubu. Baada ya kusema juu ya kusamehe kwa kundi mtu huyu kwa sababu ya huzuni aliyokuwa amewaletea wao kama kundi, Paulo aliendelea kusema, “Shetani asije akapata kutushinda; kwa maana hatukosi kuzijua fikira zake.” (2 Kor. 2:5-11) Mtume alikuwa na maana gani kwa kusema hivyo?
4 “Fikira” za Shetani ni kuwameza wo wote wa watumishi wa Mungu awezao, naye huzunguka-zunguka “kama simba angurumaye” atimize kusudi hilo. (1 Pet. 5:8) Mtu aliyekuwa ametengwa na ushirika Korintho alikuwa ‘ametolewa’ kwa Shetani katika maana ya kwamba alikuwa ameondolewa kundini na hivyo alitupwa nje kwenye ulimwengu unaotawaliwa na Shetani. (1 Kor. 5:5; Matendo 26:18; 1 Yohana 5:19) Kama vile “chachu kidogo” katika “donge zima” la unga wa kuokea, mtu huyu alikuwa amekuwa ndiye “mwili” kundini; na kwa kumwondoa mtu huyu mwenye zinaa kundi lenye kufikiria mambo ya kiroho lilikuwa limeuharibu “mwili” utoke katikati yao. Sasa fikira au kusudi la Shetani lingekuwa kumteka huyo mpaka afanikiwe kummeza mtu huyo kabisa, akimharibu kwa kiroho. Kama kundi lingalijihadhari kupita kiasi lisitake kumpokea tena mtenda kosa aliyetubu kweli kweli sasa na kukawiza kurudishwa kwake bila sababu, hata kwa dhamiri njema kabisa, hii ingalilitimiza kusudi la Adui. (Linganisha 2 Wakorintho 2:7.) Kwa hiyo, tafsiri nyingine za 2 Wakorintho 2:11 zasema hivi: “Kwa maana Shetani hapaswi aruhusiwe atushinde; sisi twazijua sana hila zake.” (New English Bible) “Na kwa hiyo hatutahadaliwa na Shetani—sisi twayajua makusudi yake vya kutosha [mambo anayofuatia, Goodspeed].”—Jerusalem Bible.
5, 6. (a) Kwa habari ya watu ambao wametengwa na ushirika, ni nia gani mbaya ambayo wazee wa Kikristo na washiriki wa kundi wamepaswa waiepuke? (b) Toa mfano wa hili.
5 Wazee wa kundi, na vile vile washiriki mmoja mmoja wa kundi, wanapaswa wajihadhari na kukuza nia inayolingana na ile ambayo waandishi wengine wa kidini wa Kiyahudi waliichochea juu ya Mataifa kwa kuwaona kama adui kabisa. Ni sawa kulichukia kosa lililotendwa na mtu aliyetengwa na ushirika, lakini si sawa kumchukia mtu huyo wala si sawa kumtendea huyo kikatili. Kama ilivyoangaliwa mapema, maandishi fulani ya waalimu wa kidini yalishikilia kauli ya kwamba, hata wakiwa katika hatari ya kufa, Mataifa wasipewe msaada wo wote. Basi, tuseme mshiriki wa kundi la Kikristo aliyemo katika mashua ziwani aona mashua nyingine alimo mtu aliyetengwa na ushirika ikienda mrama, na kumtupa aliyetengwa na ushirika majini huku akijitahidi kwa shida aelee majini. Je! Mkristo aweza kuipuza hatari ya huyo, apige makasia akienda zake akakosa kuwa na hatia mbele za Mungu—ati kwa sababu mtu aliyekuwa katika hatari ya kuzama ametengwa na ushirika, akionwa kama “mtu tu wa mataifa”? Hasha. Huo ungekuwa ukatili na unyama. Hatuwezi kumwazia Kristo Yesu akifanya hivyo; wala Myahudi mwingine ye yote wa karne ya kwanza aliyekuwa na maoni yaliyosawazika asingalitenda hivyo kwa Mtaifa au mtoza kodi aliye katika hatari hiyo.
6 Lakini fikiria hali isiyopita kiasi sana. Namna gani ikiwa mwanamke aliyetengwa na ushirika anahudhuria katika mkutano wa kundi na baada ya kuondoka jumbani anakuta kwamba mpira wa gurudumu la gari lake lililopangwa karibu umetoboka? Je! washiriki wa kundi walio wanaume wakatae kumsaidia wakiiona shida yake, pengine wakimwachia mlimwengu aje na kumsaidia? Huu pia ungekuwa ukatili na unyama usio na sababu. Lakini hali kama hii zimetokea, pengine kwa dhamiri njema kabisa, hata hivyo kwa sababu ya kukosa maoni yaliyosawazika.
7. Twaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Yehova Mungu mwenyewe katika habari hii?
7 Tukimwiga Baba yetu wa kimbinguni tutakumbuka kwamba yeye hata aliwaonyesha wanadamu wawili wa kwanza huruma ya kadiri fulani baada ya kutengwa kwao na ushirika katika Edeni, akawapa mavazi. (Mwa. 3:21) Hizi zilikuwa ni fadhili wasizozistahili. Kama vile Yesu alivyowakumbusha wanafunzi wake, Yehova Mungu “huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki.” (Mt. 5:45) Mtume Paulo alionyesha kwamba, ujapokuwa mwendo wa kujitegemea waliofuata mataifa yasiyo ya Kiyahudi kinyume cha njia ya Mungu, Yehova “hakujiacha pasipo ushuhuda, kwa kuwa alitenda mema, [akiwapa wao] mvua kutoka mbinguni, na nyakati za mavuno, akiwashibisha mioyo [yao] chakula na furaha.” (Matendo 14:16, 17) Kwa hiyo, ‘kutochangamana’ na mtu, au kumtendea huyo kama “mtu tu wa mataifa,” hakutuzuii tusiwe wenye adabu, wenye heshima, wenye huruma na wafadhili.
YANAYOTIWA KATIKA USHIRIKA WA KIROHO
8. (a) Usemi wa Kigiriki ‘kuchangamana na,’ uliotumiwa na mtume Paulo katika 1 Wakorintho 5:9, 11, wamaanisha nini? (b) Maana yake nini kuwa na “ushirika” na mtu mwingine? (c) Je! tukiwatia moyo watenda mabaya watubu huko ni kuwa na ushirika nao?
8 Neno la Kigiriki lililotumiwa na Paulo la ‘kuchangamana na’ ni kiarifa syn·a·na·miʹgny·mi, chenye maana ya “kuchanganya au kutia pamoja.” Kiarifa cha msingi kinachohusika (miʹgny·mi) kinatumiwa katika Mathayo 27:34 kueleza kuchanganya divai na nyongo na katika Luka 13:1 kueleza kuchanganya kwa Pilato damu na dhabihu. Kwa hiyo chahusu kuchanganya kabisa, kuunganisha vitu viwe mchanganyiko. ‘Kuchangamana’ kwetu na wengine kungemaanisha pana ushirika kati yetu. Neno la Kiswahili “ushirika” lina maana ya “urafiki; uenzi,” kuwa na “ujamii [au, kushirikiana kwa watu wote au wawili] wa mapendezi, nia, n.k.” (The World Book Dictionary) Kwa hiyo, kuwa na ushirika na mtu mwingine kwamaanisha kumkubali yule mtu mwingine kama mwenye hali inayolingana na yako mwenyewe, kupendezwa na maoni yake na kuyakubali, kuyashiriki kwa nia ya kupenda. Kwa hiyo, kuwa na ushirika wa kiroho na mtu mwingine kungekuwa na maana ya kufurahia pamoja naye mambo ya kiroho. Lakini tunapomtia mtu moyo atubu hatujiungi naye katika umoja wenye urafiki; hatushiriki naye nia yo yote isiyofaa awezayo kuwa nayo, bali twamtendea kama mtu anayehitaji kusahihishwa.
9. (a) Ni nini ambacho kingeamua Kama ingefaa kwa mzee wa kundi kusema maneno ya kutia moyo kwa mtu aliyetengwa na ushirika anayekutana naye? (b) Kwa sababu gani mzee angeweza kwa haki kumtia moyo mtu aliyekuwa ametengwa na ushirika lakini ambaye hakuwa akiufuata mwendo unaoelezwa katika 2 Yohana 7-11?
9 Namna gani basi, mzee wa kundi akikutana na mtu aliyetengwa na ushirika, pengine katika shughuli za kila siku za mzee, barabarani, kazini pake au katika shughuli kama hiyo? Je! mzee angekuwa akitenda kinyume cha tendo la kundi la kutenga na ushirika kama akisema naye, akimsihi huyo ‘ageuke’ na kutafuta kupatanishwa tena na Baba yake wa kimbinguni? Hali ndizo zitakazoamua. Bila shaka, ikiwa mwenye kutengwa na ushirika anafuata mwendo kama wale waalimu wa uongo na waeneza porojo wanaoelezwa katika 2 Yohana 7-11, akijaribu kwa makusudi kuongoza wengine wafuate imani za uongo au mazoea ya ufisadi, mzee asingetaka amfanyie huyo lo lote. Lakini si wote wanaotumbukia katika njia yenye dhambi wanaokuwa ‘wadanganyifu na wapinga Kristo.’ Kwa hiyo, ikiwa mtu huyo si wa jamii hiyo, je! mfano wa Yehova Mungu mwenyewe usingemruhusu mzee aseme maneno ya kumtia moyo aliyetengwa na ushirika arudie hali njema na Mungu? Badala ya kutenda kinyume cha kutenga na ushirika, kwa maneno yake ya kutia moyo kwa kweli mzee ataonyesha kuunga mkono kwake hatua hiyo ya kutenga na ushirika kwamba ilifaa na ilihitajiwa.
10-12. (a) Je! watu wote wanaotengwa na ushirika wanaendelea kuonyesha tabia au njia zilizowafanya wawe kama “chachu”? Toa mfano. (b) Kwa hiyo ni hali gani zinazopaswa kufikiriwa kwa uzito katika kuamua nia ifaayo juu ya wale waliotengwa na ushirika? (c) Mfano wa mwana mpotevu waonyeshaje ufahamu huu wa mambo lakini ambaye hakuwa akiufuata mwendo unaoelezwa katika 2 Yohana 7-11?
10 Pia, twaweza kuangalia kwamba katika 1 Wakorintho 5:11 mtume aonya juu ya kuchangamana na mtu ambaye “ni” mwasherati au mzoevu wa namna nyingine ya kosa zito. Walakini, namna gani yeye ambaye ametengwa na ushirika kwa sababu ya kuwa mtu wa namna hiyo lakini ambaye baada ya hapo, mapema au baadaye, anaonyesha ushuhuda wa kukomesha mazoea hayo mabaya, akiyaacha? Bila kujali alikuwa mtenda kosa wa aina gani hata ikamfanya huyo awe kama “chachu” kwa kundi je! yaweza kusemwa kwamba yeye angali “ni” mwasherati?
11 Kwa mfano, kijana aliyetengwa na ushirika kwa sababu ya uasherati huenda baadaye akaoa, akawa na jamaa na kuishi maisha yenye kuheshimika. Au mtu aliyetengwa na ushirika kwa sababu ya ulevi huenda akaacha mazoea hayo na, ikiwa anakunywa, huenda akafanya hivyo kwa kiasi. Kwa mabadiliko hayo watu hawa mmoja mmoja huenda sasa wakaheshimiwa tena na jamii ya watu. Pengine hawajaja na kujaribu kuomba warudishwe na kundi. Walakini, je! si kuna tofauti ya wazi kati ya watu hawa na wengine wanaoendelea moja kwa moja kutenda mabaya yaliyofanya watengwe na ushirika? Wale wanaoacha mazoea mabaya huenda bado wakaonyesha kuthamini kweli ya Kikristo, pengine hata wakilitetea kundi la kweli la Kikristo wakati mtu anaposema mabaya juu yake. Je! hali kama hizo hazipaswi zifikiriwe inavyofaa na kubadili nia yetu kama kundi juu ya watu hao?
12 Kwa kweli kama mwana mpotevu wa mfano angalirudi nyumbani akiwa mlevi, pengine akimkokota mmoja wa wenzi wake makahaba, baba angalitenda kwa njia tofauti. Lakini baba alikuwa na sababu ya kuamini kwamba mwana wake alikuwa akimfikia kwa nia inayofaa na, badala ya kuwa na mashaka kwamba mabaya yangefuata, baba alitumainia yaliyo bora na akaenda kumlaki mwana wake mwenye kutenda makosa.
13. (a) Ni ushuhuda gani wa toba upitao ule wa maneno, kama inavyoonyeshwa na maneno ya Yohana Mbatizaji na mtume Paulo? (b) Basi kanuni hii inatumikaje kwa habari ya mtu ambaye ametengwa na ushirika?
13 Leo, pia, imetupasa tujue kwamba mmoja wa ushuhuda ulio bora wa toba hauonyeshwi kwa maneno tu, yanayosemwa vivi hivi tu, bali unaonyeshwa kwa matendo. (Linganisha 1 Yohana 3:18.) Hivyo, wakati watu fulani walipomjia Yohana Mbatizaji (aliyekuwa akibatiza watu kwa mfano wa toba na msamaha wa dhambi), Yohana hakuyaona matendo yao ya zamani kama jambo lililo la maana zaidi au lililohitajiwa tu. Bali, aliwaambia waende ‘wakazae matunda yapasayo toba,’ akiwatajia mifano ya matunda hayo au matendo mema kama vile kuonyesha ukarimu wenye rehema, kuacha udanganyifu na unyang’anyi, kutosumbua au kutoa ushuhuda wa uongo juu ya wengine. (Mt. 3:7, 8; Luka 3:7-14) Mtume Paulo naye aliwatia moyo watu “watubu na kumwelekea Mungu, wakiyatenda matendo yanayopatana na kutubu kwao.” (Matendo 26:20) Hivyo, wakati mtu aliyetengwa na ushirika anapoacha mazoea yake mabaya yaliyolifanya kundi limwondoe kama “chachu,” huenda badiliko hili likaonwa walau kama wonyesho wa kwamba yeye ‘anageuka’ na kutubia mwendo wake wa zamani.—Matendo 3:19.
14. Ni kwa njia gani nyingine ambavyo mtu aliyetengwa na ushirika awezavyo kuonyesha ‘tunda lipasalo kutubu,’ na ni chini ya hali gani mzee aweza kuona ni vema amfikie huyo?
14 Huenda pia mtu aliyetengwa na ushirika akaonyesha ushuhuda wa ‘tunda lipatanalo na kutubu’ kwa kuja kwenye mikutano ya Kikristo iliyo wazi kwa watu wote. Tena, ikiwa yeye anakuja huko kubishana akitetea mwendo mbaya na kujaribu kuvuta wengine waamini maoni yasiyolingana na Maandiko, masimulizi yaliyomo katika 2 Yohana 7-11 yanamfaa mtu huyo. Lakini ikiwa hakuna jaribio la kufanya hivi, lisingekuwa jambo lisilopatana na shauri la Maandiko kwa mzee kumfikia huyo (pengine anapomwona huyo penye mikutano mara kadha) na kusema maneno ya kumtia moyo akitazamia kumponya kwa kiroho na kumrudisha kabisa kama mshiriki anayekubaliwa wa kundi.—Yakobo 5:19, 20.
15. Wakati mtu ambaye ametengwa na ushirika amepatwa na kizuizi kibaya sana cha kimwili juu ya kutimiza tamaa yake ya kuhudhuria mikutano, ni nini kiwezacho kufanywa kwa kufaa?
15 Nyakati nyingine huenda mtu aliyetengwa na ushirika akawa na kizuizi cha kimwili asiweze kufika penye mikutano hiyo ya Kikristo, ijapokuwa anayo tamaa ya kufanya hivyo. Huenda mahali pa mikutano pakawa mbali na huenda magari ya kusafiria yasipatikane. Au hali nyingine za kipekee au za kimwili huenda zikawa kizuizi kikubwa cha kutohudhuria mikutano. Wakati mmoja mwanamke aliyekuwa ametengwa na ushirika alitumia shilingi 56 kwa kukodi gari afike mkutanoni. Aliwaeleza wazee kwamba alitaka ahudhurie lakini asingeweza kuendelea kuja kwa sababu ya gharama hizo. Hata alionyesha ukweli wa tamaa yake Jumapili moja kwa kutembea mwendo wote. Kama washiriki wa kundi wakimwona mtu kama huyu akitembea mwendo mrefu sana kuelekea kwenye mahali pa mkutano na wana nafasi katika gari lao kumchukua, je! hilo lisingekuwa jambo la huruma kumsaidia huyo?
16. Kwa sababu gani uangalifu ni wa lazima katika mipango hiyo, na kwa hiyo ni shauri la nani limepaswa litafutwe kwa hekima?
16 Bila shaka, ikiwa hakuna ushuhuda wa “matendo yanayopatana na kutubu” naye mtu yule angali ajulikana kama anayeendelea katika mwendo wa ufisadi, hii ingebadili mambo, kwa maana kumchukua katika gari au kumsaidia kwa kawaida kwa njia kama hiyo kungeliletea kundi suto mtaani. Kwa hiyo, wakati washiriki wa kundi wanapomjua mtu aliyetengwa na ushirika anayeelekea kuhitaji na kutaka msaada aweze kuhudhuria mikutano, ingefaa watafute mashauri ya wazee wa kundi kabla hawajajipangia mipango hiyo wenyewe.—1 Pet. 2:12; 3:16.
KATI YA JAMAA
17. Ni wajibu na uhusiano gani wa Maandiko unaobaki ukiendelea katika jamaa yajapokuwa matendo ya kutenga na ushirika?
17 Kwa kuwa uhusiano wa damu na wa ndoa hauvunjwi na tendo la kutenga na ushirika la kundi, hali katika jamaa yahitaji uangalifu wa pekee. Mwanamke ambaye mume wake ametengwa na ushirika haachishwi na takwa la Maandiko la kuheshimu ukichwa wa mumewe; ni kifo tu au talaka inayolingana na Maandiko kutoka kwa mume inayomwachisha. (Warumi 7:1-3; Marko 10:11, 12) Vivyo hivyo mume haachishwi na kumpenda mke wake kama “mwili mmoja” hata ikiwa anatengwa na ushirika. (Mathayo 19:5, 6; Efe. 5:28-31) Na wazazi pia wangali wakipewa amri ya kuendelea kulea watoto wao ‘katika adabu na rekebisho la moyoni la Yehova’ hata ikiwa mwana au binti aliyebatizwa ametengwa na ushirika akiwa mdogo. (Waefeso 6:4, NW) Na wana na mabinti, bila kujali umri wao, wanabaki chini ya wajibu wa ‘kuheshimu baba yao na mama yao’ ijapokuwa huenda mmoja wa hawa au wote wawili wakawa wametengwa na ushirika. (Mt. 15:4; Efe. 6:2) Si vigumu kuelewa hivi tunapoangalia kwamba hata maafisa wa kisiasa wa ulimwengu huu wamepaswa waonyeshwe heshima ipasayo na Wakristo kulingana na Maandiko.—Rum. 13:1, 7.
18. Wazazi wanawezaje kutimiza wajibu wao kulea watoto wao katika adabu na rekebisho la moyoni la Yehova na bado waliheshimu tendo la kundi la kutenga na ushirika?
18 Washiriki wa jamaa wanaweza kutimiza wajibu wao wa Maandiko lakini wasijionyeshe wasiopatana na tendo la kundi la kumtenga mtu wa jamaa na ushirika. Wanafanya hivi kwa kutoshirikiana na huyo kwa njia ya kiroho. Lakini je!, ni kwa njia gani basi wazazi wawezavyo kutimiza amri ya kutia watoto wao adabu kupatana na Neno la Mungu wakati mmoja wa watoto wao ametengwa na ushirika? Wangali wanaweza kulitumia Neno la Mungu au vitabu vingine vinavyozungumza Biblia kuzoeza mwana au binti, lakini wanavitumia hivi kwa kusahihisha, si kana kwamba wanafurahia mambo ya kiroho na huyo kama ambavyo wangefurahia na watoto wengine. Ni juu ya wazazi kuamua namna ya kufanya hivyo. Hii haimaanishi watende kwa ukatili, lakini hawawi na uhusiano wa kiroho uliokubaliwa na mwana huyo au binti aliyetengwa na ushirika kama wanavyokuwa nao na wale wengine. Mwana au binti aliyetengwa na ushirika amepaswa atiwe moyo kuhudhuria funzo la jamaa la Biblia apate “rekebisho la moyoni la Yehova.”
19. Mkristo aliyeoa au kuolewa awezaje kusaidia kumrudisha mwenzi wake wa ndoa aliyetengwa na ushirika bila ya kukosa kupatana na tendo la kundi la kutenga na ushirika?
19 Vivyo hivyo, ikiwa mwenzi wa mtu ametengwa na ushirika, yule mwenzi mwingine, kama “mwili mmoja” na huyo, aweza kwa haki kufanya awezayo kumwelekeza huyo kwenye toba na kurudishwa kundini. Kujizuia na ushirika wa kiroho kusingekataza matumizi ya Biblia au vitabu vingine vinavyoieleza Biblia, kwa maana, kama tulivyoona, ushirika waonyesha umoja wa nia na maoni, usawa wa urafiki. Mwenzi aliye katika hali njema akilitumia Neno la Mungu au vitabu vingine vyenye msingi wake kama njia ya kumrudisha tu na kumsahihisha, hii isingemaanisha urafiki wa namna hiyo. Hivyo mume anayepanga kusoma habari fulani za Maandiko aweza kumtia mke aliyetengwa na ushirika moyo asikilize anapozisoma. Au mke ambaye mumewe ametengwa na ushirika aweza kumwuliza kama angekuwa na nia ya kusikiliza akisoma. Bila shaka, huenda mazungumzo yakatokea kwa sababu ya kusoma huko. Ikiwa ndivyo, kujizuia kutokuwa na ushirika kwa njia ya kiroho kwaendelezwa kwa kuhakikisha kwamba hakuna ushirika wa nia au maoni mabaya yaliyoonyeshwa na aliyetengwa na ushirika wala nia yo yote ya kukubali kuachilia tendo baya lililomfanya atengwe na ushirika. (Tazama kitabu Tengenezo kwa Kuhubiri Ufalme na Kufanya Wanafunzi, ukurasa 173.)
20. (a) Je! kuruhusu mwana mdogo au binti aliyetengwa na ushirika arudi nyumbani kungehitaji kwa lazima baba aondolewe katika cheo chenye daraka la kundi? Ni nini kinachohusika? (b) Ni nini ambacho kingetilia mashaka kufaa kwa kuendelea kwake katika cheo hicho chenye daraka?
20 Nyakati nyingine mwana mdogo au binti huenda akatengwa na ushirika kwa sababu ya mwendo fulani wa ufisadi na huenda akaondoka nyumbani. Baadaye, huenda huyo akafikiri tena na kuomba ruhusa ya kurudi nyumbani. Kama hili litaruhusiwa ni juu ya wazazi kuamua, hasa baba. Ikiwa mwana au binti aonyesha nia ya kuheshimu ukichwa wa wazazi, huenda baba akaamua kumruhusu arudi na kutumia nafasi hiyo kama njia ya kupata kumrudisha mwana au binti kama iwezekanavyo. Ikiwa baba ni mzee au mtumishi wa huduma hii isingehitaji kwa lazima aondolewe katika cheo hicho maadamu yeye angali anaendelea kuheshimiwa na kundi. Bila shaka, ikiwa mwana au binti anataka arudi na aendelee bado katika mazoea ya ufisadi yaliyomfanya atengwe na ushirika, kwa kweli baba asingekuwa akiziangalia faida za kiroho za jamaa yake kama angeruhusu huyo arudi na kuichafua jamaa kwa njia ya kiroho. Hii kwa kufaa ingetilia mashaka sifa zake kwa cheo cho chote cha daraka katika kundi.—1 Timotheo 3:4, 5, 12.
21. Ni nani ambaye kwa kufaa lazima aamue kadiri ya ushirika unaofanywa na watu wa jamaa waliotengwa na ushirika wanaoishi nje ya nyumba? Ni wakati gani tu ambapo wazee wa kundi wangehusika?
21 Kwa habari ya washiriki wa jamaa waliotengwa na ushirika (si wana au mabinti wadogo) wanaoishi nje ya nyumba, itaipasa kila jamaa iamue ni kwa kadiri gani watakavyokuwa na ushirika na hao. Hili si jambo ambalo wazee wa kundi wanaweza kuwaamulia. Wanaloshughulikia wazee ni kwamba “chachu” haitiwi katika kundi kupitia kwa ushirika wa kiroho na wale waliopaswa waondolewe kama “chachu” hiyo. Hivyo, mzazi aliyetengwa na ushirika akienda kumtembelea mwana au binti au kuwaona wajukuu na anaruhusiwa kuingia katika nyumba ya Kikristo, hili si shauri la wazee. Huyo ana haki ya asili kutembelea jamaa za damu na watoto wake. Vivyo hivyo, wakati wana au binti wanapomheshimu mzazi, ingawa ametengwa na ushirika, kwa kumtembelea huyu kuona hali yake ya afya yake ya kimwili au shida zake, tendo hili tu si ushirika wa kiroho.
22. Zaidi ya wana wadogo au mabinti, kwa sababu gani washiriki wengine wa jamaa waliotengwa na ushirika wanaweza kukubaliwa katika nyumba ya Kikristo wakae humo, nao uamuzi wa hili ni wa nani?
22 Nyakati nyingine mzazi aliyetengwa na ushirika anapokuwa mzee au anapokuwa na afya mbaya na ahitaji kuangaliwa, mwana au binti aweza kuona yafaa kumleta mzazi huyo nyumbani atimize wajibu ufaao wa kumpenda mzazi wake. Kwa hiyo, pia, huenda wazazi wa Kikristo wa mwana au binti aliyetengwa na ushirika ambaye si mtoto tena wakaamua kumrudisha huyo nyumbani kwa sababu ya afya mbaya sana ya huyo au kwa sababu hajiwezi kwa kupatwa na ajali au kwa sababu ya kuwa katika hali ya umaskini. Yako maamuzi ya huruma ambayo jamaa za Kikristo lazima zifanye na wazee wa kundi hawatakiwi wajitie ndani ambapo hapana ushuhuda wa kutosha wa kurudisha maongozi yenye kupotosha ndani ya kundi.
23. Ni chini ya hali gani hata washiriki wa jamaa wasingeruhusiwa kwa kufaa watembelee nyumba ya Kikristo?
23 Hata ikiwa watu wa jamaa hawahusiki, wakati mtu aliyetengwa na ushirika anapotumia vifungo vyake vya jamaa kama njia ya kuendesha utendaji kama ule unaoelezwa katika 2 Yohana 7-11, jamaa zake za Kikristo wanakataa kwa kufaa asiingie nyumbani mwao, wakimweleza huyo aliyetengwa na ushirika kwamba yeye hakaribishwi kwa maana kusudi la ziara yake ni kuendeleza imani mbaya au mwenendo mbaya.—Yuda 3, 4; linganisha Kumbukumbu la Torati 13:6-8.
24. Uhusiano wa kimwili usipohusika, imewapasa washiriki wa kundi wategemee nani kwa hekima waongoze katika kurudishwa ko kote kwa watu waliotengwa na ushirika?
24 Ikiwa uhusiano wa kimwili hauhusiki, itafaa washiriki wa kundi waufahamu ubora wa kuwaacha wazee, kama wachungaji wa kundi, wachukue daraka la kwanza la kutia moyo au kusaidia kurudisha watu waliotengwa na ushirika ambao, ingawa kwa njia fulani ‘wako mbali’ kama vile mwana mpotevu aliyekuwa akirudi, wanatoa ushuhuda wa kutaka kufuata mwendo ufaao. Nyakati nyingine huenda wazee wakaona kwamba watu fulani wangeweza kusaidia kumrudisha mtu aliyetengwa na ushirika, pengine kwa sababu ndio waliotumiwa hapo kwanza kumsaidia huyo apate maarifa ya kweli ya Biblia.
FAIDA ZA MAONI YALIYOSAWAZIKA
25. (a) Ni nini kitakachotuwezesha tuendeleze maoni yaliyosawazika juu ya waliotengwa na ushirika? (b) Ni kwa njia gani ambavyo mtu ‘anatolewa kwa Shetani, ili mwili uadhibiwe, ili na roho iokolewe,’ kama inavyotajwa katika 1 Wakorintho 5:5?
25 Kushikamana na Maandiko, kutorahisisha yanayosema wala kuongeza mambo yasiyosemwa nayo, kutatuwezesha kuendeleza maoni yaliyosawazika juu ya waliotengwa na ushirika. Sikuzote tutakumbuka sababu ya kutenga na ushirika, kuliendeleza kundi kuwa safi na lenye kukubaliwa na Mungu, bila ya maongozi yenye kuchafua. “Chachu” hiyo ingelifanya “ndonge” zima, kundi, ‘lichachuke’ kwa kiroho. Kwa hiyo kundi ‘linaharibu’ maongozi haya ya kimwili yenye dhambi yatoke katikati yake kwa kumtolea mtenda mabaya asiyetubu ulimwengu unaotawaliwa na Shetani, likifanya hivyo ili “roho,” maoni yenye nguvu na nia ya kundi ipate kuhifadhiwa, kuokolewa.—1 Kor. 5:5.
26. (a) Maoni yaliyosawazika yatawezesha washiriki wa kundi waonyeshe nini, nayo hii yawezaje kuwa na matokeo yenye faida sana na yenye kutia moyo juu ya watu wanaotamani wakubaliwe tena kundini? (b) Huenda wazee wakaona inafaa sasa kufanya nini kwa habari ya watu fulani waliotengwa na ushirika wanaoisha katika eneo linalotumikiwa na kundi?
26 Wakati ule ule maoni yaliyosawazika yatatufanya tuendelee kuonyesha kwa kupatana sifa za kimungu za Baba yetu wa kimbinguni, ambaye ni mwenye haki na mwenye rehema pia. Kwa hiyo wale ambao pengine walitengwa na ushirika na ambao mioyo yao kwa unyofu yawavuta watake kurudi hawataona sababu ya kusitasita au kuwa na mashaka juu ya kama jitihada zao za kurudi zitakubaliwa. Hawataogopa kwamba watakataliwa kwa ukatili au ubaridi. Watajua kwamba hali yao si isiyo na tumaini na kwamba wazee wa kundi watawaonyesha kwa kufaa wanavyopaswa kufanya ili warudie hali yenye kukubaliwa katika kundi la watu wa Mungu na kufurahia kabisa faida zake zote. Wazee wakiwa na sababu kamili kuamini kwamba watu fulani waliotengwa na ushirika katika eneo linalotumikiwa na kundi hawaijui mipango hii, wanaweza kuona yafaa kuwapasha habari hizo.
27. (a) Ni nini kilicho cha lazima ili mtu arudishwe kwenye hali yenye kukubaliwa katika kundi? (b) Kwa sababu gani wale wanaotaka kurudishwa imewapasa wavutwe kulionyesha sifa hii na kuchukua hatua zinazohitajiwa na kuifurua hisha jamaa yote ya Mungu mbinguni na duniani?
27 Ni kweli, ili kupata hali yenye kukubaliwa katika kundi itahitaji wonyesho wa kweli wa unyenyekevu kwa upande wa mtu aliyetengwa na ushirika. (Isa. 57:15; Yak. 4:8-10) Lakini uzima wenyewe umo hatarini, na “wakati uliokubaliwa” wa nia njema ya Mungu na uvumilivu sasa ukiendelea kufupika sana, bila shaka hawatataka kiburi kiwazuie wasimgeukie baba yao wa kimbinguni na kutafuta hali njema naye tena na ushirika kamili pamoja na watoto wake wa kiroho au wanaotazamiwa kuwa watoto katika uhusiano wao wenye furaha wa jamaa. (2 Kor. 6:1, 2) Badala yake watashukuru Mungu kwamba amefanya mipango hiyo yenye rehema kwa msamaha na kurudishwa na kutambua kwamba ‘sifa hii ya fadhili ya Mungu inajaribu kuwaelekeza kwenye toba.’—Rum. 2:4.
—Kutoka The Watchtower, Aug. 1, 1974.