Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 1/1 kur. 12-18
  • Kutenga na Ushirika—Jinsi Kunavyopasa Kuonwa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutenga na Ushirika—Jinsi Kunavyopasa Kuonwa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JINSI YA KUWATENDEA WATU WALIOONDOSHWA NJE
  • WALE WANAOJITENGA WENYEWE NA USHIRIKA
  • KUWA NA USHIRIKIANO WA UMOJA PAMOJA NA KUNDI
  • JEI TUSEME NA MTU ALIYETENGWA NA USHIRIKA AU ALIYEJITENGA MWENYEWE NA USHIRIKA?
  • KUTOKUSHIRIKI KATIKA KAZI MBOVU
  • WASHIKAMANIFU KWA MAONI YA MUNGU
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Ikiwa Mtu wa Ukoo Ametengwa na Ushirika...
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Kuendeleza Maoni Yaliyosawazika Juu ya Waliotengwa na Ushirika
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Onyesha Uaminifu wa Kikristo Mtu wa Ukoo Anapotengwa na Ushirika
    Huduma Yetu ya Ufalme—2002
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 1/1 kur. 12-18

Kutenga na Ushirika​—Jinsi Kunavyopasa Kuonwa

“Ee Yehova, . . . ni nani atakayekaa katika mlima mtakatifu wako? Yeye anayetembea bila kosa na kuzoea haki.”​—Zab. 15:1, 2, NW.

1, 2. Tunajuaje kwamba Mungu anawatazamia wanaomwabudu watetee kanuni zake?

YEHOVA ni mwenye haki na mtakatifu. Ingawa yeye anawaonyesha wanadamu rehema na ufahamu (huruma), anawatazamia wale wanaomwabudu wauonyeshe utakatifu wake kwa kujaribu kuzitetea kanuni zake za haki.​—Zab. 103:8-14; Hes. 15:40.

2 Mwisraeli aliyevunja amri za Mungu kwa makusudi, kama zile zilizokataza kuasi imani, uzinzi au kuua, alipaswa akatiliwe mbali, auawe. (Hes. 15:30, 31; 35:31; Kum. 13:1-5; Law. 20:10) Uthabiti huo katika kuzitetea kanuni za Mungu zenye kiasi na haki ya hukumu uliwafaidi Waisraeli wote, kwa maana ulisaidia kuendeleza utakato (usafi) wa kundi. Tena ulisaidia kuzuia mtu ye yote asieneze uchafuzi kati ya watu wa Mungu waliokuwa wakiitwa kwa jina la Mungu.

3. Hali ya Myahudi mwenye kuondoshwa sinagogini ilikuwa nini?

3 Katika karne ya kwanza W.K. Wayahudi waliokuwa chini ya utawala wa Kirumi hawakuwa na mamlaka ya kutolea mtu adhabu ya kifo. (Yohana 18:28-31) Lakini Myahudi mwenye hatia ya kuivunja Torati angeweza kuondoshwa katika sinagogi. Matokeo ya adhabu kali hiyo yalikuwa kwamba Wayahudi wale wengine walikuwa wakimwepuka mtu huyo aliyeondoshwa. Inasemwa kwamba wengine hata walikataa kushughulika naye katika mambo ya kibiashara, wakamwuzia vitu vile tu vilivyokuwa vya lazima kwa maisha.a—Yohana 9:22; 12:42; 16:2.

4, 5. Ililipasa kundi la Kikristo lishughulikeje na mtenda dhambi asiyetubu?

4 Baada ya kundi la Kikristo kufanyizwa, lilichukua nafasi ya taifa la Kiyahudi kwa kuitwa kwa jina la Mungu. (Mt. 21:43; Matendo 15:14) Kwa hiyo, Wakristo wangeweza kutazamiwa kwa kufaa waitetee haki ya Yehova. Mtume Petro aliandika hivi: “Kama yeye aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote; kwa maana imeandikwa, Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu.” (1 Pet. 1:14-16) Yehova anawapenda watu wake na anataka kuulinda utakato wa kundi la Kikristo. Kwa hiyo yeye alitayarisha mpango wa kumkataa au kumwondosha nje mtu anayezidi kufuata mwendo unaoharibu heshima ya Mungu na kulitia kundi hatarini.

5 Mtume Paulo alishauri hivi: “Mtu aliye mzushi [“mwenye kuendeleza madhehebu” au mgawanyiko, NW], baada ya kumwonya mara ya kwanza na mara ya pili, mkatae; ukijua ya kuwa mtu kama huyo amepotoka, tena atenda dhambi, maana amejihukumu hatia yeye mwenyewe.” (Tito 3:10,11) Naam, wazee wa kiroho, kama Tito alivyokuwa mzee, wanajaribu kwanza kumsaidia mkosaji kwa upendo. Ikiwa yeye anakataa msaada wao na kuzidi kufuata mwendo wa ‘kutenda dhambi,’ wao wana mamlaka ya kuita halmashauri ya wazee ‘waamue washiriki wa ule ushirika.’ (1 Kor. 5:12, Today’s English Version) Kumpenda Mungu na kupenda utakato wa watu wake kunawahitaji wale walio katika “ushirika,” lile kundi, wamkatae mtu huyo.

6. Kwa sababu gani ilikuwa haki na ilifaa kuwaondosha nje watenda dhambi wasiotubu?

6 Katika karne ya kwanza wengine wa wakosaji hao walitokea. Himenayo na Iskanda walikuwa watu wa namna hiyo, wanaume waliokuwa ‘wameangamia kwa habari ya Imani.’ Paulo alisema: “Nimempa Shetani watu hao, ili wafundishwe wasimtukane Mungu.” (1 Tim. 1:19, 20) Kuwaondosha nje wanaume wawili hao kulikuwa njia kali ya kuwatiisha, au kuwatia adabu, kuwapa adhabu ambayo ingeweza kuwafundisha wasimwonyeshe madharau Mungu mtakatifu aliye hai. (Linganisha Luka 23:16, mahali neno la msingi la Kigiriki ambalo mara nyingi hutafsiriwa ‘kutia adabu’ limetumiwa.) Lilikuwa jambo lenye kufaa watu hao wenye kuonyesha madharau kwa mambo ya kimungu wageuziwe mamlaka ya Shetani, watupwe ndani ya giza la ulimwengu ulio chini ya mavutano ya Shetani.​—2 Kor. 4:4; Efe. 4:17-19; 1 Yohana 5:19; linganisha Matendo 26:18.

JINSI YA KUWATENDEA WATU WALIOONDOSHWA NJE

7, 8. Tunaweza kuamuaje mwenendo tunaopaswa kuwa nao kumwelekea mtu aliyeondoshwa kundini?

7 Walakini, huenda maulizo fulani yakatokea juu ya jinsi tunavyopaswa kumtendea mtu aliyekuwa mshiriki ambaye sasa ameondoshwa nje. Jambo la kupigia asante ni kwamba Mungu ameweka katika Neno lake majibu na maelekezo ambayo tunaweza kuwa na uhakika ni makamilifu, yenye haki ya adili na haki ya hukumu.​—Yer. 17:10; Kum. 32:4.

8 Wakati mmoja mwanamume mmoja katika kundi la Korintho alikuwa akizoea uasherati na kwa wazi hakutaka kutubu. Paulo aliandika kwamba mwanamume huyo ‘aondolewe miongoni mwao,’ kwa maana alikuwa kama chachu ndogo ambayo ingeweza kuchachisha, au kuchafua, donge zima. (1 Kor. 5:1, 2, 6) Lakini, akiisha kuondoshwa nje, je! mtu huyo angetendewa kama kwamba alikuwa mtu wa kawaida tu wa ulimwengu ambaye Wakristo wangeweza kukutana naye katika ujirani wao au katika maisha ya kila siku? Angalia aliyoyasema Paulo.

9. Shauri la Paulo lilikuwa nini juu ya kushughulika na watu wasio haki kwa ujumla?

9 “Naliwaandikia katika waraka wangu, kwamba msichangamane na wazinzi. Sisemi msichangamane kabisa na wazinzi wa dunia hii, au na wenye kutamani, au na wanyang’anyi, au na wenye kuabudu sanamu; maana hapo ingewalazimu kutoka katika dunia.” (1 Kor. 5:9, 10) Katika maneno hayo Paulo alikubali waziwazi kwamba watu wengi tunaokutana nao katika shughuli zetu za kila siku hawajapata kamwe kuijua njia ya Mungu wala kuifuata. Huenda wakawa ni waasherati, wanyang’anyi au waabudu sanamu, na kwa hiyo si watu ambao Wakristo wanachagua wawe washiriki wao wa kawaida, wa karibu. Hata hivyo, tunaishi juu ya sayari hii kati ya wanadamu na huenda tukalazimika kuwa karibu na watu hao na kusema nao kazini, shuleni na katika ujirani.

10, 11. Kwa sababu gani inawapasa Wakristo wamtendee kwa njia tofauti mtenda dhambi ambaye ameondoshwa kundini?

10 Katika mstari unaofuata Paulo anatofautisha hali hii na jinsi Wakristo wanavyopaswa wajiendeshe kuelekea mtu aliyekuwa amekuwa “ndugu” wa Kikristo lakini akaondoshwa kundini kwa sababu ya kufanya kosa: “Naliwaandikia [“sasa mimi ninawaandikia,” NW] msichangamane [acheni kuchangamana katika ushirika, NW] na mtu aitwaye ndugu, akiwa ni mzinzi au mwenye kutamaini [mwenye pupa, NW] au mwenye kuabudu sanamu au mtukanaji au mlevi au mnyang’anyi; mtu wa namna hii msikubali hata kula naye.”​—1 Kor. 5:11.

11 Mtu huyo aliyeondoshwa kundini si mtu wa kawaida tu wa ulimwengu ambaye hajapata kamwe kumjua Mungu wala si mtu ambaye hajapata kamwe kuifuatia njia ya kimungu ya maisha. Bali, yeye amepata kuijua njia ya kweli na haki, lakini akaiacha njia hiyo na kufuatia dhambi bila kutubu kufikia hatua iliyofanya iwe lazima kumwondosha nje. Kwa hiyo anapaswa atendewe kwa njia tofauti.b Petro alieleza jinsi watu hao waliokuwa Wakristo hapo kwanza wanavyotofautiana na ‘mtu wa kawaida tu anayetembea barabarani.’ Mtume alisema hivi: “Kwa maana wale waliokwisha kuyakimbia machafu ya dunia kwa kumjua Bwana na Mwokozi Yesu Kristo, kama wakinaswa tena na kushindwa, hali yao ya mwisho imekuwa mbaya kuliko ile ya kwanza. . . . Lakini imetukia kwao sawasawa na ile mithali ya kweli, Mbwa ameyarudia matapiko yake mwenyewe, na nguruwe aliyeoshwa amerudi kugaa-gaa matopeni.”​—2 Pet. 2:20-22; 1 Kor. 6:11.

12. (a) Kwa sababu gani maneno “kutenga na ushirika” yanafaa? (b) Historia inaonyesha wenye kujiita Wakristo waliwatendeaje watenda dhambi katika nyakati za mwanzo-mwanzo?

12 Naam, Biblia inawaamuru Wakristo wasishirikiane na mtu ambaye ameondoshwa kundini. Hivyo “kutenga na ushirika” ndiyo maneno yanayotumiwa kwa kufaa na Mashahidi wa Yehova wanapotaja kuondoshwa na kuepukwa sana kwa mkosaji wa namna hiyo asiyetubu. Wanapokataa kushirikiana kwa njia yo yote ya kiroho au ya kirafiki na mtu aliyeondoshwa wanaonyesha ushikamanifu kwa kanuni za Mungu na utii kwa amri yake iliyo kwenye 1 Wakorintho 5:11, 13. Kufanya hivyo kunapatana na maoni ya Yesu kwamba mtu wa namna hiyo aonwe kwa njia ile ile ambayo ‘mtu wa mataifa’ alionwa na Wayahudi wa wakati huo. Kwa muda fulani baada ya mitume kufa, ni wazi kwamba wale wenye kusema walikuwa Wakristo waliufuata utaratibu huo wa Biblia.c Lakini ni makanisa mangapi siku hizi yanayoyafuata maelekezo ya Mungu yaliyo wazi katika habari hii?

WALE WANAOJITENGA WENYEWE NA USHIRIKA

13. Ni jambo gani linalopasa lifanywe katika kisa cha mtu anayekuwa dhaifu na kuwa asiyetenda?

13 Huenda Mkristo akawa dhaifu kiroho, labda kwa sababu hajifunzi Neno la Mungu kwa ukawaida, kwa sababu ya kuwa na matatizo ya kibinafsi au kupatwa na mateso. (1 Kor. 11:30; Rum. 14:1) Huenda akaacha kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Sasa iwe namna gani? Kumbuka kwamba mitume walimkimbia Yesu usiku wa kukamatwa kwake. Hata hivyo Kristo alikuwa amekwisha kumhimiza Petro kwa kusema, “Mara ukiisha kurudi, tia nguvu ndugu zako [ambao pia walimkimbia Yesu].” (Luka 22:32, NW) Kwa hiyo, kwa sababu ya upendo wazee wa Kikristo na wengine wanaweza kumtembelea na kumsaidia mtu ambaye amekuwa dhaifu akawa asiyetenda. (1 The. 5:14; Rum. 15:1; Ebr. 12:12, 13) Ingawa hivyo, mambo yanakuwa tofauti wakati mtu anaposema wazi kabisa hataki kuwa Mkristo kisha anajitenga mwenyewe na ushirika.

14. Mtu anaweza kujitenga mwenyewe na ushirika kwa njia gani?

14 Huenda mtu ambaye amekuwa Mkristo wa kweli akaikana njia ya ile kweli, akisema kwamba hajioni tena kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova au hataki kuitwa mmoja wao. Jambo hilo lisilotukia mara nyingi litukiapo, mtu huyo anakuwa akikana msimamo wake kama Mkristo, akijitenga mwenyewe na ushirika wa kundi kwa makusudi. Mtume Yohana aliandika hivi: “Walitoka kwetu, lakini hawakuwa wa kwetu. Maana kama wangalikuwa wa kwetu, wangalikaa pamoja nasi.”​—1 Yohana 2:19.

15, 16. (a) Ni kwa njia gani nyingine mtu anaweza kujitenga mwenyewe na ushirika? (b) Inawapasa Wakristo wawaoneje na wawatendeeje watu waliojitenga na ushirika?

15 Au, huenda mtu akapakataa mahali pake katika kundi la Kikristo kwa matendo yake, kama vile kuwa sehemu ya tengenezo lenye lengo lisilopatana na Biblia na, kwa sababu hiyo, tengenezo hilo likiwa chini ya hukumu ya Yehova Mungu. (Linganisha Ufunuo 19:17-21; Isaya 2:4.) Kwa hiyo mtu aliyekuwa Mkristo akichagua kujiunga na wale wanaokataliwa na Mungu, ingefaa kundi litoe tangazo fupi kusema kwamba alijitenga mwenyewe na ushirika wala si mmoja tena wa Mashahidi wa Yehova.

16 Watu wanaojifanya wawe ‘si wa kwetu’ kwa kuikataa makusudi imani na mambo ambayo Mashahidi wa Yehova wanaamini wanafaa waonwe na kutendwa kama wale ambao wamekwisha kutengwa na ushirika kwa sababu ya kufanya kosa.

KUWA NA USHIRIKIANO WA UMOJA PAMOJA NA KUNDI

17, 18. Ni mambo gani yanayohusika katika kukubaliana kwetu na kundi kwa habari ya kutenga na ushirika?

17 Ingawa Wakristo wanafurahia ushirika wa kiroho wanapozungumza au kujifunza Biblia na ndugu zao au watu wanaopendezwa, wasingetaka kuwa na ushirika huo pamoja na mtenda dhambi aliyeondoshwa nje (au mtu ambaye ameikataa imani na mambo ambayo Mashahidi wa Yehova wanaamini, kwa njia hiyo akijitenga mwenyewe na ushirika). Mtu aliyeondoshwa nje ‘amekataliwa,’ “amejihukumu hatia yeye mwenyewe” kwa sababu ya ‘kutenda dhambi,’ na wale walio katika kundi wanaikubali hukumu ya Mungu na kuitetea pia. Walakini, kutenga na ushirika hakumaanishi kuacha kuwa na ushirika wa kiroho tu.​—Tito 3:10, 11.

18 Paulo aliandika hivi: “Acheni kuchangamana katika ushirika . . . , wala hata kula pamoja na mwanamume kama huyo.” (1 Kor. 5:11, NW) Wakati wa kula chakula ni wakati wa kustarehe na kushirikiana kirafiki. Kwa hiyo, hapa Biblia inakataza ushirika wa kirafiki pia, kama kujiunga na mtu aliyeondoshwa kundini katika pikniki (pique-nique) au kwenye chai iliyoandaliwa, kwenye mchezo, safari ya kwenda kwenye ufuo wa bahari au kwenda kwenye jumba la maonyesho, au kuketi pamoja naye ili kula.d (Matatizo ya pekee yanayohusu mtu wa ukoo ambaye ametengwa na ushirika yanazungumzwa katika makala inayofuata.)

19. Kwa sababu gani huenda nyakati nyingine ikaelekea kuwa vigumu kuiunga mkono hatua ya kutenga na ushirika, lakini kwa sababu gani ni jambo la maana tuiunge mkono?

19 Nyakati nyingine huenda Mkristo akajisikia akikazwa sana sana ayapuze maoni hayo ya Biblia. Huenda maoni yake mwenyewe ya moyoni yakaleta mkazo huo, au huenda ukaletwa juu yake na watu wanaomfahamu. Kwa mfano, ndugu mmoja alikazwa awe ndiye afisi mwenye kuandikisha kisheria ndoa ya watu wawili waliotengwa na ushirika. Je! kuwapa utumishi huo kungeweza kusemwa ni jambo dogo la kuwaonyesha fadhili tu? Huenda mtu akawa na maoni hayo. Lakini kwa nini walitaka utumishi wa ndugu huyo, badala ya kutumikiwa na wakili wa serikali mwenye kuandikisha ndoa za watu? Je! sababu haikuwa kwamba yeye alikuwa na msimamo wa kuwa mhudumu wa Mungu na alikuwa na uwezo wa kutoa mashauri ya ndoa kutokana na Neno la Mungu? Kujiacha ashindwe na mkazo huo kungemtia ndani ya ushirika wa watu hao wawili, ambao walikuwa wameondoshwa kundini kwa sababu ya njia yao isiyo ya kimungu.​—1 Kor. 5:13.

20. Imetupasa tutendeje ikiwa mtu tunayeshirikiana naye katika kazi ametengwa na ushirika?

20 Matatizo mengine hutokea kuhusiana na biashara au kazi. Namna gani kama wewe ungekuwa umeandikwa kazi na mtu ambaye baadaye anakuja kutengwa na ushirika, au wewe uliandika mtu kazi ambaye baadaye alikuja kutengwa na ushirika? Sasa iweje? Ikiwa hali ya mkataba (mapatano) mliofanya au hali ya pesa inakulazimisha uendelee kuwa na uhusiano wa kibiashara naye kwa wakati uliopo, bila shaka sasa ungeonyesha nia tofauti kumwelekea mtu huyo aliyetengwa na ushirika. Huenda kuzungumza naye mambo ya kibiashara au kuonana naye kazini kukawa jambo la lazima, lakini utayaacha mazungumzo ya kiroho na ushirika wa kirafiki pamoja naye. Kwa njia hiyo ungeweza kuonyesha unamtii Mungu na kujipatia kinga (ulinzi). Vilevile, huenda kufanya hivyo kukamwonyesha kwa njia yenye mkazo dhambi yake imemletea hasara kubwa katika njia mbalimbali.​—2 Kor. 6:14, 17.

JEI TUSEME NA MTU ALIYETENGWA NA USHIRIKA AU ALIYEJITENGA MWENYEWE NA USHIRIKA?

21, 22. Maandiko yanatoa maoni gani juu ya kusema na mtu aliyetengwa na ushirika?

21 Je! kutetea haki ya Mungu na mpango wake wa kutenga watu na ushirika kunamaanisha kwamba Mkristo hapaswi kusema hata kidogo na mtu aliyeondoshwa kundini, hata kusema “Jambo” (Habari?)? Watu fulani wameshindwa kujua jibu la ulizo hilo, kwa sababu ya maoni ambayo Yesu alitoa tupende adui zetu na ‘kutokusalimu ndugu zetu tu.’​—Mt. 5:43-47, NW.

22 Kusema kweli, katika hekima yake Mungu hakujaribu kuzungumza kila hali inayoweza kuwako. Tunalohitaji ni kuielewa maana ya mambo ambayo Yehova anasema juu ya jinsi ya kumtendea mtu aliyetengwa na ushirika, kwa maana ndipo tunapoweza kujitahidi tuyatetee maoni Yake. Kwa kumtumia mtume Yohana, Mungu anaeleza hivi:

“Kila apitaye cheo, wala asidumu katika mafundisho ya Kristo, yeye hana Mungu. . . .Mtu akija kwenu, naye haleti mafundisho hayo, msimkaribishe nyumbani mwenu, wala msimpe salamu. Maana yeye ampaye salamu azishiriki kazi zake mbovu.”​—2 Yohana 9-11.

23, 24. Kwa sababu gani ni jambo la hekima kuepuka kusema na watu walioondoshwa kundini?

23 Mtume aliyetoa onyo hilo lenye hekima alikuwa rafiki wa karibu wa Yesu na alijua vizuri vile Kristo alivyokuwa amesema juu ya kusalimu watu. Alijua pia kwamba salamu iliyokuwa kawaida ya wakati huo ilikuwa “Amani.” Ikiwa mtu aliyetengwa na ushirika au aliyejitenga mwenyewe na ushirika anajaribu kuwatia wengine moyo wafuate njia yake ya kuasi imani au waitetee, au ikiwa anaendelea kuufuata mwenendo wake usio wa kimungu, kwa uhakika huyo hastahili kutakiwa “Amani” kwa maana yeye ni tofauti na “adui” fulani wa mtu au mtu wa kiulimwengu mwenye kuwapinga Wakristo. (1 Tim. 2:1, 2) Nasi sote tunajua kutokana na mambo tuliyojionea wenyewe muda wa miaka iliyopita kwamba kusema neno fupi tu la “Jambo” (Habari?) kunaweza kuwa ndiyo hatua ya kwanza inayopanuka na kuwa mazungumzo na hata kuwa urafiki. Je! tungetaka kuichukua hatua hiyo ya kwanza kumwelekea mtu aliyetengwa na ushirika?

24 Huenda mtu akataka kujua, ‘Itakuwaje ikiwa huyo anaelekea kuwa na toba na anahitaji kutiwa moyo?’ Kuna mpango wa kushughulikia hali kama hizo. Waangalizi walio kundini wanatumikia kama wachungaji na walinzi wa kiroho wa lile kundi. (Ebr. 13:17; 1 Pet. 5:2) Mtu aliyetengwa au aliyejitenga mwenyewe na ushirika akipeleka maombi, au akionyesha ushuhuda wa kutaka kurudia upendeleo wa Mungu, wazee wanaweza kusema naye. Watamweleza kwa fadhili mambo anayohitajiwa kufanya na wanaweza kumpa maonyo fulani ya upole yanayomfaa. Wanaweza kushughulika naye kwa kutegemea mambo ya uhakika yanayohusu dhambi aliyofanya wakati uliopita na kwa kutegemea nia yake. Wale wengine kundini hawajui habari hizo. Kwa hiyo mtu fulani akifikiri kwamba yule aliyetengwa au aliyejitenga mwenyewe na ushirika ‘ana hali ya kutubu,’ je! inaweza kuwa kwamba uamuzi huo unategemea maoni yake mwenyewe badala ya kutegemea habari zilizo za kweli? Kama waangalizi wangesadiki kwamba mtu huyo ametubu na anaendelea kuzaa matunda ya toba,e angerudishwa ndani ya kundi. Baada ya kurudishwa kwake, wale wengine wote kundini wanaweza kumkaribisha mikutanoni kwa uchangamfu, wamwonyeshe msamaha, wamfariji na kumhakikishia wanampenda, kama vile Paulo alivyowahimiza Wakorintho wamfanyie mwanamume aliyerudishwa kundini huko Korintho.​—2 Kor. 2:5-8.

KUTOKUSHIRIKI KATIKA KAZI MBOVU

25, 26. Mungu anashauri nini juu ya kuwa ‘mshiriki’ pamoja na mtu aliyetengwa na ushirika?

25 Wakristo wote walio waaminifu wanahitaji kuithamini sana kweli isiyo ya kuchezewa ambayo Mungu alimwongoza Yohana aandike: “Yewe ampaye salamu [mtenda dhambi aliyeondoshwa kundini mwenye kuwatia watu moyo wafuate fundisho lenye makosa au kuendelea na mwenendo usio wa kimungu] azishiriki kazi zake mbovu.”​—2 Yohana 11.

26 Waelezaji wengi wa Jumuiya ya Wakristo wanaepuka kuyaeleza maneno ya 2 Yohana 11. Wanadai kwamba maneno hayo ni ‘shauri lisilo la Kikristo, linalotofautiana na roho ya Bwana wetu,’ au kwamba yanawatia watu moyo wasiwavumilie wenzao. Lakini maoni hayo yanatokana na matengenezo ya kidini yasiyoitumia amri ya Mungu inayosema “mwondoeni yule mbaya miongoni mwenu,” ambayo ni mara chache kabisa yanapowaondosha wakosaji wenye sifa mbaya sana katika makanisa yao, na hata inaweza kuwa kwamba hayawaondoshi kamwe. (1 Kor. 5:13) “Kuvumilia” kwao hakupatani na Maandiko, wala si kwa Kikristo.​—Mt. 7:21-23; 25:24-30; Yohana 8:44.

27. Ni kwa njia gani Mkristo anavyoweza kuwa ‘mshiriki’ wa namna hiyo, na matokeo yanaweza kuwa nini?

27 Lakini si kosa kuwa washikamanifu kwa Mungu wa Biblia aliye mwenye haki ya adili na haki ya hukumu. Yeye anatuambia kwamba atawakubali ‘katika mlima mtakatifu wake’ wale peke yao wanaotembea bila kosa, wanaozoea haki ya hukumu na kusema kweli. (Zab. 15:1-5) Ingawa hivyo kama Mkristo angekubaliana na mkosaji ambaye amekataliwa na Mungu na kutengwa na ushirika, au ambaye amejitenga mwenyewe na ushirika, tendo hilo lingekuwa sawa na kusema ‘Mimi sitaki hata kuwekewa mahali katika mlima mtakatifu wa Mungu.’ Kama wazee wangemwona akielekea upande huo kwa kushirikiana kwa ukawaida na mtu aliyetengwa na ushirika, wangetumia upendo na subira wajaribu kumsaidia aanze tena kuwa na maoni ya Mungu. (Mt. 18:18; Gal. 6:1) Wangemwonya kwa upole na, kukiwa na uhitaji mkubwa, ‘wamkaripie kwa ukali.’ Wao wanataka kumsaidia abaki ‘katika mlima mtakatifu wa Mungu.’ Lakini ikiwa yeye hataacha kushirikiana na mtu yule aliyeondoshwa kundini, kwa njia hiyo amejifanya awe ‘mshiriki (mwenye kuunga mkono au kushiriki) katika kazi hizo mbovu’ na lazima aondolewe kundini, aondoshwe nje.​—Tito 1:13; Yuda 22, 23; linganisha Hesabu 16:26.

WASHIKAMANIFU KWA MAONI YA MUNGU

28. Tunaweza kuonyeshaje ushikamanifu wetu kwa maoni ya Yehova?

28 Ushikamanifu kwa Yehova Mungu na mipango yake unaleta furaha, kwa maana njia zake zote ni za haki ya adili, haki ya hukumu na ni njema. Ndivyo ilivyo, pia, kuhusu mpango wake wa kutenga na ushirika wakosaji wasiotubu. Tunapokubaliana na mpango huo, tunaweza kuyatumaini maneno ya Daudi: “Ujue kwamba Yehova kwa uhakika atamtofautisha mshikamanifu wake.” (Zab. 4:3, NW) Naam, Mungu huwaweka kando, huwatukuza na kuwaongoza wale walio washikamanifu kwake na kwa njia zake. Kati ya baraka nyingi tunazopokea kutokana na ushikamanifu huo ni furaha ya kuwa kati ya wale ambao Mungu anawakubali wawe ‘katika mlima mtakatifu wake.’​—Zab. 84:10, 11.

WEWE UNAYAKUMBUKA MAMBO HAYA?

Wakati Wayahudi walipoondoshwa sinagogini, walitendewaje?

Paulo alionyesha tofauti gani katika kuwatendea

(1) waasherati katika ulimwengu?

(2) waasherati waliotengwa na ushirika wa kundi?

Inawapasa Wakristo wamwoneje mtu anayejitenga mwenyewe na ushirika wa kundi?

“Kutenga na ushirika” kunamaanisha kukomesha namna gani za ushirika?

Kwa sababu gani Wakristo hawawasalimu wala hawasemi na watu waliotengwa na ushirika?

Kwa habari ya kutenga na ushirika, sisi tunahitaji kufanya nini ili tubaki ‘katika mlima mtakatifu wa Mungu’?

[Maelezo ya Chini]

a Kuanzia wakati huo alionwa kuwa kama mtu aliyekufa. Hakuruhusiwa kujifunza pamoja na wengine, wala hakukupaswa kuwa na uhusiano [wa kirafiki] pamoja naye, hata hakupaswa kuonyeshwa mahali njia ilipo. Ni kweli angeweza kununua vitu alivyovihitaji kwa maisha, lakini ilikatazwa kula au kunywa pamoja na mtu huyo.”​—Kitabu cha Kiingereza kiitwacho The Life and Times of Jesus the Messiah (Maisha na Nyakati Ambazo Yesu Masihi Aliishi), cha A. Edersheim, Vol. II, uku. 184.

b Kupatana na fundisho hili la Biblia, Adam Clarke anaikazia tofauti, akisema: “Msifanye mashauriano pamoja na [mtenda dhambi aliyeondoshwa nje] katika mambo matakatifu wala ya kiraia. Mnaweza kuendesha shughuli zenu za kilimwengu pamoja na mtu asiyemjua Mungu, asiyesema ni Mkristo, hata awe ana tabia ya adili ya namna gani; lakini, haiwapasi kamwe mfikie kiasi hicho cha kutambua mtu mwenye kusema ni Mkristo, anayefuata mwenendo wenye kuleta aibu. Mwacheni huyo atiwe alama hii ya ziada ya kuchukia kwenu dhambi ya namna zote kiasi cha kutapika.’’

c Joseph Bingham mwanahistoria wa kidini aandika hivi juu ya karne za kwanza-kwanza: “Adhabu iliyotolewa na kanisa ilikuwa na uwezo wa kuwanyima watu faida zote na mapendeleo yote yanayotokana na ubatizo, kwa kuwaondoa katika jamii ya kanisa na ushirika walo, . . . na kila mtu aliwaepuka katika mazungumzo yale ya kawaida, kwa upande mmoja akiwa na kusudi la kuwathibitishia mambo ambayo kanisa halikutaka wapate na hatua zilizochukuliwa juu yao, na kwa upande mwingine akiwa na kusudi la kuwaaibisha, na kwa upande mwingine kujipatia usalama kusiwe na hatari ya kuambukizwa na mtu huyo hali yake yenye makosa.” “... hakuna mtu aliyepaswa kuwapokea katika nyumba yake watu waliotengwa na ushirika, wala kula kwenye meza moja pamoja nao; watu hawakupaswa kuzungumza nao kama watu wanaofahamiana, wakiwa wangali hai; wala hawakupaswa kuwafanyia sherehe za maziko, wakati walipokufa, . . . Maagizo hayo yalitolewa kwa kufuatisha kielelezo cha sheria za mitume, zilizowakataza Wakristo wasiwaunge mkono kwa njia yo yote wakosaji wenye sifa mbaya sana.”​—Kitabu The Antiquities of the Christian Church (Desturi za Kale za Kanisa la Kikristo), kur. 880, 891.

d Toleo letu la Desemba 15, 1981, lilizungumza 2 Wathesalonike 3:14, 15 (NW) ambapo Biblia inasema kwamba huenda kukawa na uhitaji mkubwa wa ‘kumtia alama’ Mkristo anayejikaza azidi kufuata mwenendo wa kukosa utaratibu. Bado yeye ni ndugu ua anapaswa aonywe kwa upole kama ndugu, lakini Wakristo wale wengine wanapaswa ‘waache kushirikiana na yeye’. Ikiwa wanapaswa kuepuka ushirika wa kirafiki pamoja na huyo, kunapasa kuwe na mtengano mkubwa zaidi katika visa vya wakosaji waliotengwa au waliojitenga wenyewe na ushirika.

e Ili upate mazungumzo yanayohusu toba, angalia Mnara wa Mlinzi wa Desemba 15, 1981.

[Picha katika ukurasa wa 15]

“Msikubali hata kula’’ na mtu aliyetengwa na ushirika

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki