Onyesha Uaminifu wa Kikristo Mtu wa Ukoo Anapotengwa na Ushirika
1 Uhusiano kati ya watu wa familia unaweza kuwa wenye nguvu sana. Mkristo hujaribiwa sana wakati mume au mke, mtoto, mzazi, au mtu mwingine wa jamaa anapotengwa au anapojitenga mwenyewe na kutaniko. (Mt. 10:37) Wakristo waaminifu wamtendeeje mtu huyo wa ukoo? Je, atendewe tofauti ikiwa mnaishi pamoja naye? Kwanza, na tuchunguze maoni ya Biblia juu ya jambo hili, kanuni zinazowahusu wale ambao wametengwa na ushirika na wale wanaojitenga wenyewe na ushirika.
2 Jinsi ya Kuwatendea Wale Waliotengwa na Ushirika: Neno la Mungu linawaamuru Wakristo wasishirikiane na mtu ambaye ametengwa na kutaniko: “Mkome kuchangamana katika ushirika pamoja na yeyote aitwaye ndugu ambaye ni mwasherati au mtu mwenye pupa au mwabudu-sanamu au mtukanaji au mlevi au mnyang’anyi, wala hata kula pamoja na mtu wa namna hiyo. . . . Ondoeni yule mtu mwovu miongoni mwenu wenyewe.” (1 Kor. 5:11, 13) Maneno ya Yesu katika Mathayo 18:17 pia yanahusiana na habari hiyo: “Mwache [aliyetengwa na ushirika] awe kwako kama vile mtu wa mataifa na kama mkusanya-kodi.” Wasikilizaji wa Yesu walijua vizuri kwamba Wayahudi wa wakati huo hawakuwa wakichangamana na watu wasio Wayahudi na kwamba jamii iliwatenga wakusanya-kodi. Kwa hiyo Yesu alikuwa akiwaagiza wafuasi wake wasishirikiane na watu waliotengwa na ushirika.—Ona gazeti Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 1982, ukurasa wa 10-12.
3 Hiyo yamaanisha kwamba Wakristo waaminifu hawashirikiani kiroho na mtu yeyote aliyetengwa na kutaniko. Lakini mengi zaidi yanahusika. Neno la Mungu lasema kwamba ‘hatupaswi hata kula pamoja na mtu wa namna hiyo.’ (1 Kor. 5:11) Kwa hiyo, twaepuka pia kushirikiana na mtu aliyetengwa na ushirika katika shughuli za kirafiki. Hiyo inamaanisha kwamba hatutashirikiana naye katika tafrija, sherehe, michezo, au kwenda naye madukani au kwenye majumba ya sinema au kula pamoja naye nyumbani au mkahawani.
4 Vipi kuongea na mtu aliyetengwa na ushirika? Ingawa Biblia haitaji kila hali, 2 Yohana 10 inatusaidia kuona maoni ya Yehova kuhusu jambo hilo: “Ikiwa yeyote aja kwenu na haleti ufundishaji huu, msimpokee kamwe nyumbani mwenu wala kusema salamu kwake.” Kuhusu jambo hili, gazeti Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 1982, lilisema hivi kwenye ukurasa wa 17: “Kusema neno fupi tu la ‘Jambo’ (Habari?) kunaweza kuwa ndiyo hatua ya kwanza inayopanuka na kuwa mazungumzo na hata kuwa urafiki. Je! tungetaka kuichukua hatua hiyo ya kwanza kumwelekea mtu aliyetengwa na ushirika?”
5 Kwa kweli, ni kama tu vile ambavyo toleo hilohilo la Mnara wa Mlinzi linavyosema kwenye ukurasa wa 23: “Jambo la uhakika ni kwamba wakati Mkristo anapojiacha atende dhambi kisha inakuwa lazima atengwe na ushirika, yeye anapoteza mambo mengi: msimamo wake wenye kukubaliwa na Mungu; . . . ushirika mtamu pamoja na kina ndugu, kutia na mwingi wa ushirika aliokuwa nao pamoja na watu wa ukoo wake walio Wakristo.”
6 Ikiwa Mwenye Kutengwa na Ushirika Anaishi Katika Nyumba Ileile: Je, hiyo yamaanisha kwamba Wakristo wanaoishi kwenye nyumba ileile na mtu wa familia aliyetengwa na ushirika wanapaswa kuepuka kuzungumza naye, kula naye, na kushirikiana naye katika shughuli za kila siku? Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Aprili 15, 1991, lilisema hivi katika kielezi-chini kwenye ukurasa wa 22: “Ikiwa katika nyumba ya Kikristo kuna mtu wa ukoo ambaye ametengwa na ushirika, yeye bado angekuwa sehemu ya kawaida ya shughuli na utendaji wa kinyumbani wa kila siku.” Kwa hiyo, ni juu ya familia kuamua ni kadiri gani mshiriki wa familia aliyetengwa anapaswa kuhusishwa wakati wa kula au katika shughuli nyingine za familia. Lakini haingefaa wafanye akina ndugu wanaoshirikiana nao waone kwamba hali iko kama ilivyokuwa kabla ya mtu huyo kutengwa na ushirika.
7 Hata hivyo, gazeti la Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 1982, ukurasa wa 20, lilisema hivi kuhusu mtu aliyetengwa au aliyejitenga na ushirika: “Ule uhusiano wa kiroho uliokuwapo umezuiwa kabisa. Ndivyo ilivyo hata kuhusiana na watu wa ukoo wake, kutia na wale walio ndani ya jamaa iyo hiyo ya karibu. . . . Hiyo itamaanisha wafanye mabadiliko katika ushirika wa kiroho ambao huenda ulikuwa katika jamaa hiyo. Kwa mfano, mume akitengwa na ushirika, mkewe na watoto hawatafurahia kumwacha awaongoze katika funzo la jamaa la Biblia wala katika usomaji wa Biblia na sala. Ikiwa yeye anataka kutoa sala, kama vile wakati wa kula, yeye ana haki ya kufanya hivyo katika nyumba yake mwenyewe. Lakini wao wanaweza kumtolea Mungu kwa kimya sala zao wenyewe. (Mit. 28:9; Zab. 119:145, 146) Namna gani ikiwa mtu aliyetengwa na ushirika katika nyumba hiyo anataka kuwapo wakati jamaa inaposoma Biblia pamoja au inapokuwa na funzo la Biblia? Wale wengine wanaweza kumwacha awepo asikilize ikiwa hatajaribu kuwafundisha au kuwatolea maoni yake ya kidini.”
8 Ikiwa mtoto anayeishi nyumbani ametengwa na ushirika, wazazi Wakristo bado wana daraka la kumlea. Gazeti Mnara wa Mlinzi la Novemba 15, 1988, lilisema hivi katika ukurasa wa 20: “Sawa na vile ambavyo wao wataendelea kumwandalia chakula, nguo, na makao, wao wanahitaji kumwagiza na kumtia nidhamu kupatana na Neno la Mungu. (Mithali 6:20-22; 29:17) Hivyo wazazi wenye upendo wangeweza kupanga kuwa na funzo la Biblia la kimaskani [nyumbani] pamoja naye, hata ikiwa ametengwa na ushirika. Labda atapata manufaa iliyo na usahihisho mkubwa zaidi kutokana na kujifunza kwao pamoja naye akiwa peke yake. Au wangeweza kuamua kwamba yeye anaweza kuendelea kushiriki katika mpango wa funzo la jamaa.”—Ona pia gazeti Mnara wa Mlinzi la Oktoba 1, 2001, ukurasa wa 16-17.
9 Watu wa Familia Ambao Hamuishi Nao: “Hali hii ni tofauti ikiwa yule ambaye ametengwa au amejitenga na ushirika ni mtu wa ukoo anayeishi nje ya jamaa ile ya pale pale,” lasema gazeti la Mnara wa Mlinzi la Aprili 15, 1988, ukurasa wa 28. “Labda ingewezekana kuzuia mawasiliano yote pamoja na mtu huyo wa ukoo. Hata kama kuna mambo fulani ya kijamaa yanayotaka mawasiliano, kwa uhakika yanapasa kuwekwa katika kadiri ndogo kabisa,” kupatana na ile amri ya Mungu ya ‘kuacha kuchangamana katika ushirika pamoja na yeyote’ ambaye ni mtenda dhambi asiyetubu. (1 Kor. 5:11) Wakristo waaminifu wanapaswa kuepuka ushirika usio wa lazima kabisa na mtu huyo wa familia, hata kupunguza shughuli za kibiashara pamoja.—Ona pia Mnara wa Mlinzi, Januari 1, 1982, ukurasa wa 22-23.
10 Gazeti Mnara wa Mlinzi laelezea hali nyingine ambayo huenda ikatokea: “Namna gani ikiwa mtu wa ukoo wa karibu, kama vile mwana au mzazi asiyeishi katika nyumba hiyo, ametengwa na ushirika na baada ya hapo anataka kurudi aishi pamoja nao? Jamaa hiyo inaweza kuamua jambo la kufanya kwa kutegemea ni hali gani iliyopo. Kwa mfano, huenda aliyetengwa na ushirika akawa ni mgonjwa au hawezi tena kujitunza mwenyewe kwa upande wa pesa au kimwili. Watoto Wakristo wana wajibu wa Maandiko na wa adili kumsaidia. (1 Tim. 5:8) . . . Jambo la kufanya huenda likategemea mambo kama mahitaji ya kweli ya mzazi huyo, nia yake na heshima ambayo kichwa cha jamaa kinayo kwa hali ya kiroho ya jamaa.”—Mnara wa Mlinzi, Januari 1, 1982, ukurasa wa 21-22.
11 Kuhusu mtoto, makala hiyohiyo yaendelea kusema: “Nyakati nyingine wazazi Wakristo wamemkubali arudi nyumbani kwa muda fulani mtoto aliyetengwa na ushirika ambaye amekuwa mgonjwa sana kimwili au katika mawazo yake ya moyoni. Lakini katika kila kisa wazazi wanaweza kuzipima hali za mtu huyo waone ziko namna gani. Je! mwana aliyetengwa na ushirika amekuwa akiishi kwa kujitegemea mwenyewe, na je! sasa hawezi kufanya hivyo? Au yeye anataka kurudi nyumbani kwa sababu hasa akirudi maisha yatakuwa mepesi zaidi? Nazo tabia zake na nia yake iko namna gani? Je! ataingiza ‘chachu’ nyumbani?—Gal. 5:9.”
12 Manufaa za Kuwa Mwaminifu kwa Yehova: Kuna manufaa ya kufuata mpango wa Kimaandiko wa kutenga na ushirika na kuepuka watenda makosa wasiotubu. Huhifadhi usafi wa kutaniko na kuonyesha kuwa sisi tunafuata viwango vya juu vya Biblia. (1 Pet. 1:14-16) Hutulinda na madhara. (Gal. 5:7-9) Pia humpa mkosaji fursa ya kunufaika kikamili na nidhamu aliyopata, ambayo itamsaidia atokeze “tunda lenye kufanya amani, yaani, uadilifu.”—Ebr. 12:11.
13 Baada ya kusikiliza hotuba moja kwenye kusanyiko la mzunguko, ndugu mmoja na dada yake wa kimwili waligundua kwamba wanahitaji kufanya marekebisho katika njia ambayo walimtendea mama yao aliyekuwa akiishi kwingineko na ambaye alikuwa ametengwa na ushirika kwa miaka sita. Upesi baada ya kusanyiko, ndugu huyo aliongea na mama yake, na baada ya kumhakikishia upendo wao, akamweleza kwamba hawawezi tena kuongea naye isipokuwa kuwe na mambo muhimu ya familia yaliyohitaji wawasiliane. Punde baada ya hapo, mama yake alianza kuhudhuria mikutano na baadaye akarudishwa. Pia, mume wake asiyeamini alianza kujifunza na baada ya muda fulani akabatizwa.
14 Kufuata kwa uaminifu mpango wa kutenga na ushirika ulio katika Maandiko huonyesha upendo wetu kwa Yehova na humtolea jibu yule anayemlaumu. (Mit. 27:11) Tukifanya hivyo tuna hakika tutapata baraka za Yehova. Mfalme Daudi aliandika hivi kumhusu Yehova: “Nimeshika maagizo yake yote, sikuacha kufuata masharti yake. Wewe ni mwaminifu kwa walio waaminifu.”—2 Sam. 22:23, 26, Biblia Habari Njema.
[Maswali ya Funzo]
1. Ni hali gani inayoweza kujaribu uaminifu wa Mkristo?
2. Kulingana na Biblia, Wakristo wanapaswa kuwatendeaje wale waliotengwa na kutaniko?
3, 4. Ni ushirikiano gani pamoja na watu waliotengwa na waliojitenga na ushirika unaokatazwa?
5. Mtu akitengwa na ushirika anapoteza mambo gani?
6. Je, Mkristo anapaswa kukomesha uhusiano wote na mtu wa familia aliyetengwa na ushirika ambaye wanaishi naye katika nyumba ileile? Eleza.
7. Ushirika wa kiroho nyumbani unabadilikaje mmoja wa familia anapotengwa na ushirika?
8. Wazazi Wakristo wana daraka gani kuelekea mtoto wao aliyetengwa na ushirika anayeishi nao nyumbani?
9. Mkristo anapaswa kushirikiana kwa kadiri gani na mtu wa familia aliyetengwa na ushirika ambaye haishi pamoja naye?
10, 11. Mkristo atafikiria nini kabla ya kumruhusu mtu wa familia aliyetengwa na ushirika ahamie nyumbani?
12. Taja baadhi ya manufaa za mpango wa kutenga na ushirika.
13. Familia moja ilifanya marekebisho gani, na kulikuwa na matokeo gani?
14. Kwa nini tuunge mkono kwa uaminifu mpango wa kutenga na ushirika?